Kama kuna jambo ambalo limewaacha wananchi wengi katika mfadhaiko mkubwa ni habari kwamba nchi za Kenya na India zimeipita Tanzania kwa mbali kwa kusafirisha na kuuza katika soko la dunia, madini ya Tanzanite ambayo yanapatikana hapa nchini pekee. Ni habari za kushtusha ambazo ni vigumu kuingia akilini, kwamba Taifa la Tanzania liko katika usingizi wa pono, huku madini yetu ya Tanzanite yakizinufaisha nchi ambazo hazijawahi kuwa na migodi ya madini hayo.
Kamishna wa Madini katika Wizara ya Nishati na Madini, Mhandisi Paul Masanja alisema juzi kuwa, mwaka jana Tanzania haikufikia hata nusu ya Kenya kwa mauzo ya madini hayo ya vito na kwamba nchi hiyo ilisafirisha na kuuza nje Tanzanite yenye thamani ya Sh173 bilioni tofauti na Sh45.5 bilioni iliyouzwa na Tanzania. Alisema kwamba katika kipindi hicho, India iliuza Tanzanite yenye thamani ya zaidi ya Sh509 bilioni, kiasi cha baadhi ya wanunuzi wakubwa wa madini hayo, hasa kutoka Marekani kujiuliza iwapo madini hayo yanachimbwa India.
Hizi ni habari mbaya zinazodhihirisha kwamba Tanzania ni kichekesho cha dunia, kwani nchi nyingine duniani hulinda rasilimali zake kwa udi na uvumba pasipo kutoa mianya kwa mataifa ya nje kuzidhalilisha na kuzinyonya kiuchumi kama inavyofanyika kwa Tanzania. Ni aibu na janga kubwa kwa nchi yetu kukubali kugeuzwa shamba la bibi na nchi za kigeni zinazopora rasilimali zetu kama vile Tanzania haina mwenyewe. Tunashuhudia Serikali ikitazama upande wa pili, huku wanyamapori na rasilimali nyingine nyingi kama madini na misitu zikiporwa na wageni kwa kiwango na kasi ya kutisha.
Ni Tanzania pekee ambayo inaweza kuruhusu na kuvumilia hali hiyo ya kuporwa rasilimali zake mchana kweupe na asilimia kubwa ya wananchi wake wakiishi maisha ya udhalilishaji na umaskini uliopitiliza. Ni matokeo ya viongozi wengi kukosa uzalendo kiasi cha kutokuwa na uchungu na rasilimali za Taifa. Matokeo yake ni kuwapo rushwa na ufisadi uliokubuhu unaochochewa na mikataba mibovu inayosainiwa na viongozi wetu kwa kisingizio cha kuwavutia wawekezaji. Tumebakia kulewa sifa kutoka mataifa ya nje kwamba Watanzania wana utamaduni wa upole, amani na utulivu. Hatujiulizi kama sifa hizo zinatusaidia kujitambua ama zinatupumbaza zaidi kiasi cha kuwaachia wageni na washirika wao hapa nchini wapore rasilimali zetu.
Itakuwa ndoto kwetu kujikwamua kama viongozi wetu hawatabuni mifumo rasmi ya kibiashara badala ya kulalamika. Kamishna wa Madini anasema asilimia 80 ya Tanzanite inayopatikana Mirerani, mkoani Manyara huuzwa kwa njia za panya nje ya nchi. Hata hivyo, Serikali haionyeshi kutambua kwamba watoroshaji wakubwa wa madini ni wachimbaji wadogowadogo, wengi wao wakiwa ni matajiri wakubwa hapa nchini, lakini hawalipi kodi. Tunaambiwa Serikali inakusudia kuwasilisha muswada bungeni kurekebisha Sheria Namba 6 ili kumpa madaraka Kamishna wa Madini kutaifisha madini yanayomilikiwa kinyume cha sheria, ingawa bado ina safari ndefu kama hakutakuwapo utashi wa kisiasa.
Tunaambiwa pia kwamba kikosi kazi kitakachojumuisha askari kutoka vyombo vya ulinzi na usalama kukabiliana na utoroshaji madini nje ya nchi kitaundwa. Sisi tunadhani kwamba juhudi zote hizo hazitazaa matunda yoyote kama viongozi na wananchi kwa jumla hawataonyesha uzalendo na kuwa na uchungu kwa nchi yetu na rasilimali zake.