Kikosi bora cha Ligi Kuu Bara msimu wa 2014/15
Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2014/15 imemalizika juzi huku Yanga ikitwaa ubingwa na Polisi Moro pamoja na Ruvu Shooting zikishuka daraja.
Ligi Kuu msimu huu ilikuwa na 14 ambazo ni Yanga, Azam, Simba, Mtibwa, Mbeya City, Kagera Sugar, JKT Ruvu, Coastal Union, Ruvu Shooting, Tanzania Prisons, Ndanda FC, Mgambo JKT, Stand United na Polisi Moro.
Baada ya kuangalia mechi zote za Ligi Kuu Bara msimu huu, Spoti Mikiki inawaletea kikosi bora cha msimu wa 2014/15 kilichotokana na maoni ya makocha wengi wa Ligi hiyo na maoni ya wachezaji wengi wa ligi hiyo waliowapendekeza kutokana na ubora wao msimu huu.
1.Ali Mustapha ‘Barthez' (Yanga)
Kati ya makipa wavumilivu kwenye Ligi Kuu Bara, ‘Barthez' anaweza kuwa namba moja, kwani tangu akiidakia Simba alivumilia benchi mpaka akaondoka na kujiunga na Yanga, pia aliendelea kuvumilia kukaa benchi. Hata hivyo alipata nafasi ya kukaa golini akichukua nafasi ya aliyekuwa kipa namba moja, Deogratius Munishi ‘Dida'. Amedaka vizuri msimu huu huku akikosa kucheza mechi chache.
2.Juma Abdul (Yanga)
Kati ya mabeki wa pembeni waliofanya vizuri msimu huu hasa beki ya kulia huwezi kuacha kumtaja Juma Abdul. Alikaa benchi katika mechi za mwanzoni mwa msimu na nafasi yake kuchukuliwa na Mbuyu Twite, lakini baadaye alirejeshwa katika nafasi yake na hakutoka tena katika kikosi cha kwanza. Sifa yake kubwa ni kupandisha mashambulizi ya timu na kurudi kukaba kwa haraka.
3.Mohamed Hussein ‘Tshabalala' (Simba)
Timu nyingi kwenye Ligi Kuu Bara zinakabiliwa na uhaba wa mabeki wa kushoto, lakini msimu uliopita Simba ilipata bahati kumpata beki akitokea Kagera Sugar.
Aliitendea haki nafasi yake katika msimu huu kwani alipandisha mashambulizi na kukaba kwa ufasaha.
4.Kelvin Yondani (Yanga)
Ni beki mkongwe. Utulivu wake na umakini uliisaidia sana Yanga kutofungwa mabao mengi msimu huu na kuwa timu iliyoruhusu mabao machache. Ukabaji wake wa umakini na wakati mwingine ubabe kidogo kwa washambuliaji ulizifanya timu nyingi kupata wakati mgumu kuipenya ngome ya Yanga.
5.Serge Pascal Wawa (Azam)
Ni beki mtulivu sana na anayecheza kwa akili mno akiwa uwanjani na kupiga pasi ndefu. Ni raia wa Ivory Coast ambaye ni mara ya kwanza kucheza Ligi Kuu Bara msimu huu. Wawa ameonyesha kiwango kikubwa na wadau wengi wa soka wamekikubali.
6.Jabir Aziz (JKT Ruvu)
Mchezaji huyu amewahi kuichezea Simba miaka ya nyuma, lakini aliondoka na kujiunga na Azam na kucheza msimu mmoja tu na mkataba wake ulipomalizika alijiunga na JKT Ruvu. Aziz ameichezea timu hiyo karibu mechi zote msimu huu na ameonyesha kiwango kikubwa katika kukaba na kuanzisha mashambulizi.
7.Simon Msuva (Yanga)
Msuva anaweza kuwa mchezaji bora wa Ligi Kuu msimu kwa jinsi alivyocheza kwa kiwango cha juu. Kwanza ameisaidia timu yake kuwa bingwa na pia ameibuka mfungaji bora wa ligi akiwa amefunga mabao 17. Alikuwa bora msimu huu licha ya mara kwa mara kuzomewa na mashabiki wa klabu yake alipokosa mabao. Hata hivyo hakukata tamaa na kila mara aliwaonyesha ana thamani ndani ya klabu hiyo kwa kuwafungia mabao katika mechi muhimu.
8.Salum Telela (Yanga)
Ni mmoja ya viungo mahiri na wavumilivu kwenye Ligi Kuu Bara kwani licha ya misimu iliyopita kuandamwa na majeraha ameweza kupambana bila ya kukata tamaa. Telela alirejea kwa nguvu msimu huu na kuwa roho ya Yanga katikati ya uwanja akipangwa kiungo wa chini au kiungo wa juu. Alicheza kwa ufasaha na kuiunganisha timu yake kwa kukokota mpira vizuri, kupiga pasi nzuri na kufunga mabao anapopata nafasi. Amechangia kwa kiasi kikubwa Yanga kutwaa ubingwa msimu huu.
9.Amisssi Tambwe (Yanga)
Ukitaka mashabiki wa Simba wakuchukie litaje jina la Tambwe mbele yao kwani wanaijua shughuli yake na wamekuwa kila mara wakiulaumu uongozi wa timu yao kwa kumuacha mchezaji huyo mzuri. Tambwe alijiunga na Yanga wakati wa dirisha dogo akitokea Simba walikomuacha kwa madai ameshuka kiwango, lakini alikuja kuonyesha wote waliombeza kuwa bado yuko juu na ndio maana ameshika nafasi ya pili kwa ufungaji msimu huu akiwa na mabao 14 licha ya kucheza mechi chache akiwa katika klabu ya Yanga.
10.Emmanuel Okwi (Simba)
Nyota huyu ni mzee wa kubadili matokeo wakati wowote. Okwi anajiamini na ndiyo mchezaji ambaye amechangia kwa kiasi kikubwa Simba kumaliza ligi katika nafasi iliyopo kwa ajinsi anavyocheza kwa kujituma uwanjani.
Okwi amekuwa akiipatia ushindi timu yake hata pale inapokuwa katika wakati mgumu. Katika msimu huu alikuwa akikosekana Okwi timu ya Simba ilikuwa inayumba katika safu ya ushambuliaji.
11.Haruna Niyonzima (Yanga)
Inasemekena ndiye kiungo aliyetoa pasi nyingi za mabao katika timu ya Yanga msimu huu. Kocha wake Hans Pluijm alikuwa akimchezesha kama winga wa kushoto na mara nyingine kiungo. Hata hivyo alimudu kucheza nafasi yake mpya ya winga na kushirikiana vizuri na wenzake jambo lililoisaidia sana timu hiyo kuweza kutoa vipigo kila mara katika michezo yake.
Wachezaji wa Akiba
Aishi Manula (Azam)
Hassan Kessy (Simba)
Himid Mao (Azam)
Mbuyu Twite (Yanga)
Mudathir Yahaya (Azam)
Jonas Mkude (Simba)
Mrisho Ngassa (Yanga)
Steven Mazanda (Mbeya City)
Didier Kavumbagu (Azam)
Rashid Mandawa (Kagera Sugar)
Ibrahim Ajibu (Simba)
Kocha: Hans van Pluijm
Fomesheni: 4-4-2