Kitabu: Maisha ya Malcom X

Kitabu: Maisha ya Malcom X

Sura ya 17
MECCA
Hija ya Mecca ni takwa la kidini ambalo kila Muislamu, iwapo anaweza, anatakiwa alitimize walau mara moja katika maisha yake.
Quran Takatifu inasema kuwa “Hija ya Kaaba ni jukumu ambao binadamu anadaiwa na Mungu; wale wanaoweza wafanye safari.”
Allah anasema: “Natangaza hija kwa watu; watakuja kwako kwa miguu, juu ya ngamia, watakuja kutoka mabonde yote marefu.”
Kwenye vyuo kadhaa, ilitokea baada ya hotuba na tukiwa tumekusanyika kwa maongezi, nilifuatwa na watu kadhaa weupe weupe hivi. Walijitambulisha kuwa wao ni Waarabu na Waislamu kutoka Mashariki ya Kati au Afrika Kaskazini, na wapo Marekani kwa matembezi, kwa masomo au wanaishi hapa. Walisema kuwa, ukiachana na kauli zangu za kuwashutumu wazungu, walihisi kwamba nilikuwa muaminifu katika kujiita kwangu Muislamu, na walihisi kuwa iwapo nitaujua waliouita “Uislamu wa kweli.” “Nitauelewa na kuukubali.” Nikiwa kama mfuasi wa Elijah Muhammad, nilikasirika kila niliposikia hayo.

Lakini nilipokuwa nikitafakari nikiwa mwenyewe baada ya mambo yote yale kutokea, nilianza kujiuliza: kama mtu alikuwa ni mfuasi mzuri wa hiyo dini, kwa nini ajizuie kupata maarifa zaidi kuhusu dini hiyo?

Siku moja katika maongezi niligusia hili kwa Wallace Muhammad, mtoto wa Elijah Muhammad. Alisema ndiyo, hakuna shaka kuwa Muislamu anatakiwa kujifunza Uislamu kadri ya uwezo wake. Siku zote niliyaheshimu sana maoni ya Wallace Muhammad.

Wale Waislamu halisi niliokutana nao, kila mmoja wao alinihimiza kuonana na kuongea na Dr. Mahmoud Youssef Shawarbi. Niliambiwa kuwa ni msomi mkubwa wa dini ya Kiislamu. Mhitimu wa Chuo Kikuu cha Cairo, akipata shahada yake ya uzamivu kutoka Chuo Kikuu cha London., mhadhiri wa Kiislamu, mshauri wa Umoja wa Mataifa na muandishi wa vitabu vingi. Alikuwa ni profesa kamili katika Chuo kikuu cha Cairo, na atakuja likizo New York na kuwa kama mkurugenzi wa Shirikisho la Taasisi za Kiislamu katika Marekani na Kanada(F.I.A). mara kadhaa nilipokuwa nikiendesha maeneo ambayo kulikuwa na makao makuu ya F.I.A, nilizuia shauku ya kutaka kuingia kwenye jengo lao, lakini siku moja muuza magazeti Fulani alinitambulisha kwa Dr. Shawarbi.

Alikuwa mwenye urafiki sana. Alisema kuwa huwa ananifuatilia kwenye vyombo vya habari. Nilimjulisha kuwa niliambiwa kumhusu na watu mbalimbali. Basi tukazungumza kwa kama dakika kumi na tano hadi ishirini hivi. Sote tulikuwa na mihadi ya kwenda sehemu Fulani.
Kabla ya kuachana aliniambia jambo fulani ambalo halijawahi kunitoka kichwani. Alisema, “Hakuna mwenye imani kamili mpaka pale atakapotamani yampate ndugu yake yale anayotamani yampate yeye mwenyewe.”
Turudi kwa dada yangu Ella. Sikuweza kutoa akilini mwangu kile alichonifanyia. Nimekwisha sema alikuwa ni mwanamke mweusi shupavu kutoka Georgia. Msimamo wake na ukichwa ngumu wake vilisababisha atengwe kutoka Msikiti Namba Kumi na Moja wa Boston; walimrudisha lakini baadaye akaondoka mwenyewe. Akaanza kujifunza na Waislamu asilia, kisha akaanzisha shule ambayo ilifundisha na Kiarabu! Yeye mwenyewe hakuweza kukiongea, aliajiri waalimu wa kukifundisha. Huyo ndiye Ella! Alikuwa anafanya biashara ya majengo na alikuwa akitunza pesa kwa ajili ya hija. Karibu kila siku usiku tulikaa na kuzungumza; aliniambia kuwa suala hilo halina mjadala. Ni muhimu sana nikienda mimi hija. Wakati wote wa kurudi New York nilikuwa nikimfikiria Ella. Mwanamke shupavu sana. Amevunja ushupavu wa wanaume watatu, akiwa mshupavu kuliko wote watatu wakiwekwa pamoja. Alikuwa na nafasi muhimu sana maishani mwangu. Zaidi yake hakukuwa na mwanamke mwenye nguvu za kutosha kuniongoza; mimi ndiye niliongoza wanawake. Nilimvuta Ella kwenye Uislamu, na sasa alikuwa akigharamia safari yangu ya Mecca.

Sikuzote ukiwa pamoja na Allah, basi naye atakupa ishara kuwa yupo pamoja nawe.

Nilipoenda kuomba visa kwenye ubalozi wa Saudi Arabia, balozi wa Saudi Arabia aliniambia kuwa hakuna Muislamu aliyesilimu akiwa Marekani anayeweza kupata visa ya hija bila ya kupata saini ya kukubaliwa na Dr. Mahmoud Shawarbi. Huo ulikuwa ni mwanzo tu wa ishara kutoka kwa Allah. Nilipompigia simu Dr. Shawarbi, alishangaa sana. “Nilikuwa ndiyo najiandaa kukutafuta,” alisema, “Karibu uje.”

Nilipofika ofisini kwake, Dr. Shawarbi alinipatia barua iliyosainiwa ya kunikubalia kwenda hija, na kisha akanipatia nakala ya kitabu. Kilikuwa ni kitabu kilichoitwa The Eternal Message of Muhammad kilichoandikwa na Abd-Al-Rahman Azzam.

Dr. Shawarbi alisema kuwa mwandishi alikuwa ametuma nakala hiyo kwa ajili yangu. Aliendelea kunieleza kuwa mwandishi ni raia wa Saudi Arabia aliyezaliwa Misri, mwanadiplomasia mashuhuri na mmoja wa washauri wa karibu wa Mwanamfalme Faisal, mtawala wa Saudi Arabia. “Amekufuatilia sana kupitia vyombo vya habari.” Iliniwia vigumu sana kuamini.

Dr. Shawarbi alinipa namba ya mwanaye aliyeitwa Muhammad Shawarbi, alikuwa ni mwanafunzi huko Cairo, akanipatia na namba ya mwandishi wa kitabu kile, Omar Azzam ambaye aliishi huko Jedda, “Jitahidi uwapigie wote ukifika kituo cha mwisho kabla ya Mecca.”

Niliondoka New York kimyakimya(Sikujua kabisa kuwa kurudi kwangu kutakuwa kwa makelele sana). Ni watu wachache tu waliambiwa kuwa ninasafari. Sikutaka watu wa usalama au wengine wowote waniwekee vizuizi dakika za mwisho. Waliokuja kuniaga uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kennedy walikuwa ni mke wangu Betty, mabinti zangu watatu na watu wangu wa karibu wachache. Ndege ya shirika la Lufthansa ilipoacha ardhi, nilisalimiana na majirani niliokaa nao. Ishara nyingine! Wote walikuwa Waislamu. Mmoja alielekea Cairo kama mimi, na mwingine alielekea Jedda ambako ningefika baada ya siku chache. Tuliongea na majirani zangu wale kwa safari nzima hadi Frankfurt, Ujerumani. Tulipokuwa hatuzungumzi nilisoma kitabu nilichopewa. Tulipofika Frankfurt, ndugu aliyeelekea Jedda alituaga sisi tulioelekea Cairo. Tulikuwa na saa kadhaa kabla ya kuruka kuelekea Cairo hivyo nikaamua kutembeatembea kidogo kuiona Frankfurt.

Nilipokuwa maliwatoni pale uwanja wa ndege, nilikutana na Mmarekani wa kwanza aliyenitambua, alikuwa ni mwanafunzi wa kizungu kutoka Rhode Island. Aliniangalia kwa muda kisha akanifuata, “Wewe ni X?” Nilicheka na kumwambia ndiyo, sijawahi kusikia nikiitwa hivyo. “Haiwezekani!” alisema kwa mshangao. Hakuna mtu atakayeniamini nikimwambia hili!” Alisema kuwa alikuwa anasoma huko Ufaransa.

Mimi na yule ndugu yangu Muislamu tulishangazwa sana na urafiki wa watu wa Frankfurt. Tulitembelea maduka mengi, tuliingia kwenye duka na kupokelewa kwa bashasha sana. Ndani ya Marekani unaweza ingia dukani na kutumia dola mia moja na kuondoka na bado ukawa mpita njia tu.
Wote, wewe na muuzaji mnakuwa kama kila mmoja anamfanyia mwenzake hisani. Watu wa Ulaya wanaubinadamu zaidi. Ndugu yangu Muislamu ambaye aliweza kuzungumza Kijerumani kwa kiasi, aliwaeleza kuwa tulikuwa Waislamu, hapo niliona kitu kile kile pale watu waliponichukulia kama Muislamu na si mtu mweusi. Watu wakikuchukulia kama Muislamu wanakuchukulia kama binadamu, na wanakutendea kwa njia tofauti sana.

Tulirudi uwanja wa ndege na kuchukua ndege ya shirika la ndege la United Arab kuelekea Cairo. Watu wengi—bila shaka Waislamu waliokuwa wanaelekea hija, walikuwa wakikumbatiana na kusalimiana kwa bashasha. Walikuwa watu wa rangi na jamii mbalimbali, yalikuwa mazingira ya kirafiki sana. Niliingiwa na hisia kuwa hakukuwa na tatizo la rangi mahali hapa. Nilihisi kama vile mtu aliyetoka tu kutoka gerezani.

Nilimwambia ndugu yangu yule kuwa nilitaka kutalii jiji la Cairo kwa siku kadhaa kabla ya kuelekea Jedda. Alinipa namba yake na kuniambia nimpigie sababu alitaka kuniunganisha na rafiki zake ambao waliweza kuongea Kiingereza na walikuwa wakielekea hija, na kuwa watafurahi kuniongoza.

Basi nilitumia siku mbili za furaha kutalii jiji la Cairo. Nilipendezwa sana na shule za kisasa, nyumba za makazi za umma, barabara kubwa na maendeleo ya viwanda niliyoyaona. Nilikuwa nimesoma na kusikia kuwa Rais Nasser alikuwa amejenga moja ya nchi iliyoendelea zaidi kiviwanda katika Afrika. Jambo lililonishangaza zaidi nikuwa magari na mabasi yalikuwa yakitengenezwa pale pale Cairo.

Nilikuwa na wakati mzuri nilipokutana na mtoto wa Dr. Shawarbi, Muhammad Shawarbi, alikuwa ni kijana wa miaka kumi na tisa, alikuwa akisomea uchumi na sayansi ya siasa katika Chuo Kikuu cha Cairo. Aliniambia kuwa ndoto ya baba yake ni kujenga Chuo Kikuu cha Kiislamu ndani ya Marekani.

Watu wengi wenye urafiki niliokutana nao walishangaa sana kusikia kuwa nilikuwa Muislamu kutoka Marekani! Moja ya watu hao alikuwa mwanasayansi mmoja wa Misri pamoja na mkewe—nao wakiwa safarini kwenda hija Mecca. Bwana huyo alinisisitiza kwenda pamoja nao kwenye mgahawa uliokuwa eneo moja la Cairo lililoitwa Heliopolis. Walikuwa wenzi wenye akili na maarifa sana. Ukuaji wa kiviwanda wa Misri ilikuwa ndiyo moja ya sababu iliyofanya mataifa ya magharibi yaichukie sana. Mwanasayansi yule aliniambia kwa sababu ilikuwa ikizionyesha nchi zingine za kiafrika yale zinayozipasa kufanya. Mke wake aliniuliza, “Kwa nini watu duniani wanakabiliwa na njaa wakati Marekani inachakula kingi sana cha ziada? Wanakifanyia nini, wanakitupa baharini?” Nilimjibu “Ndiyo, lakini vingine wanaweka kwenye maghala na vyumba vya kutunza baridi na kuviacha huko, kukiwa na watu wa kuvitunza mpaka pale vitakapokuwa havifai tena kuliwa. Kisha watu wengine watakuja na kuvitoa ili kupata nafasi kwa ajili ya vipya.” Aliniangalia akiwa haamini kabisa. Pengine alihisi natania. Lakini walipa kodi wa Marekani wanafahamu kuwa ni kweli.

Lakini sikumwambia kuwa hata Marekani kwenyewe kuna watu wanateseka na njaa.

Nilimpigia simu yule rafiki yangu Muislamu kama alivyoniagiza, kisha nikaonana na rafiki zake waliokuwa wanakwenda hija. Jumla na mimi tulikuwa watu nane, kati yetu walikuwemo jaji na afisa kutoka wizara ya elimu. Waliongea Kiingereza kizuri na walinikubali kama ndugu yao. Niliichukulia hiyo kama ishara nyingine kutoka kwa Allah, kila nilikoenda kulikuwa na mtu aliye tayari kunisaidia na kuniongoza.

***

Maana halisi ya Hajj katika Kiarabu ni kuchukua hatua katika kufanya jambo fulani. Kwenye sheria za Kiislamu, inamaanisha kwenda Kaaba, Nyumba Takatifu, na kutimiza takwa la hija. Uwanja wa ndege wa Cairo ndipo palikuwa mahali ambapo vikundi kadhaa vya Mahujaji vinakuwa Muhrim yaani kuingia katika hali ya Ihram(Kunuia na kujiweka tayari kwa hija na kujitenga na mambo ya dunia). Baada ya kupokea ushauri, niliamua kuacha mizigo yangu yote pale Cairo, ikiwa pamoja na kamera zangu nne, moja ikiwa ya video. Pale Cairo nilinunua mkoba mdogo wa kutosha suti moja, shati, nguo za ndani na jozi za viatu. Kwenye safari ya kwenda airport nilikuwa na wasiwasi sana, nilifahamu kuwa kuanzia hapo itanipaswa kuwaangalia watu wanaofahamu wanachokifanya na kujaribu kuwaiga.

Katika kuingia hali ya Ihram, tulivua nguo zetu na kujifunga mataulo mawili meupe. Moja linaloitwa Izar, lilikuwa la kujifunga kiunoni. Jingine, Rida lilizungushwa shingoni na mabegani na kuacha bega na mkono wa kushoto wazi. Pia kulikuwa na’l , makubadhi ambayo yaliacha kifundo cha mguu wazi. Juu ya fundo la kiunoni la Izar kulikuwa na mkanda wenye mfuko wa pesa, na kwa ajili ya kubebea passport na nyaraka zingine muhimu, kama ile barua niliyopata kutoka kwa Dr. Shawarbi.

Kila mmoja kati ya maelfu ya watu waliokuwepo uwanjani pale wakijianda kwenda Jedda, alivalia namna hii. Unaweza kuwa mfalme au mkulima masikini na mtu yeyote asijue. Baadhi ya watu wakubwa ambao nilionyeshwa kwa siri walikuwa wamevalia kama mimi tu. Mara tu baada ya kuvalia hivi, wote tulianza kuita kwa kupokezana “Labbayka! Labbayka!” (Nakuja kwako Ee Mungu!) Uwanja wa ndege ulijaa sauti kubwa za Muhrim wakitaja nia yao ya kufanya Hija.

Ndege zilizojaa mahujaji zilikuwa zikipaa kila dakika, lakini bado uwanja ukawa umejaa wengine wengi pamoja na ndugu na rafiki zao waliokuja kuwaaga. Wale ambao walikuwa hawaendi walikuwa wakiwaomba wengine wasali wa niaba yao huko Mecca. Tulikuwa tayari ndani ya ndege ndipo nilipotambua kwa mara ya kwanza kuwa hakukuwa na nafasi yangu lakini walikuwa wamefanya mipango na mtu fulani alishushwa sababu hawakutaka kumuangusha Muislamu kutoka Marekani. Nilipatwa na hisia mchanganyiko, dhamira ikinisuta kuwa nilisababisha mtu mwingine ashushwe kwa ajili yangu, na pia nilijihisi mnyenyekevu na mwenye shukrani sana kwamba niliheshimiwa kiasi kile.
Ndani ya ndege kulijaa watu weupe, wa kahawia, wekundu na wamanjano, wenye macho ya bluu, nywele za rangi ya dhahabu na mimi mwenye nywele nyekundu zilizojikunjakunja, wote kama ndugu! Wote tukimtukuza Mungu mmoja, Allah, wote tukiheshimiana.

Kutoka kwa mtu fulani wa kwenye kundi letu, habari zilianza kusambaa kiti hadi kiti kuwa nilikuwa Muislamu kutoka Marekani. Watu walinigeukia na kunisalimu kwa tabasamu. Chakula cha mchana kilipitishwa, tulipokuwa tunakula, habari zilifika chumba cha marubani kuwa ndani ya ndege kulikuwa na Muislamu kutoka Marekani.

Rubani wa ndege alikuja kunisalimu. Alikuwa ni Mmisri, alikuwa na weusi wa ngozi kuliko hata mimi; angeweza kutembea katika mitaa ya Harlem bila mtu hata mmoja kumshangaa. Alifurahi sana kukutana na Muislamu kutoka Marekani. Aliponialika kutembelea chumba cha rubani nilikubali mara moja.

Rubani msaidizi alikuwa ni mweusi kuliko hata yeye. Siwezi kukuelezea jinsi nilivyohisi. Sijawahi kuona mtu mweusi akirusha jeti. Ile paneli iliyojaa vitufe: hakuna mtu anayeweza kuelewa vilimaanisha nini. Marubani wote walijawa na tabasamu, wakinitendea kwa heshima kama nilivyotendewa tokea nitoke Marekani. Nilisimama ndani mle nikiangalia anga juu yetu. Katika Marekani nilipanda ndege mara nyingi pengine kuliko mtu mweusi mwingine yeyote
yule, lakini sijawahi karibishwa kwenye chumba cha marubani. Lakini tazama hapa nimekaa na Waislamu wenzangu wawili, mmoja kutoka Misri na mwingine kutoka Arabia, sote tukielekea Mecca, na mimi nikiwa kule kwenye chumba cha marubani. Ndugu! Nilijua kuwa Allah yuko pamoja nami.

Nilirudi kitini kwangu. Kwa safari nzima ya kama saa moja, mahujaji tulikuwa tukipiga kelele, “Labbayka! Labbayka!” Ndege ikatua uwanja wa ndege wa Jedda, ni mji wa bandari katika bahari ya Shamu. Ni sehemu ambayo mahujaji wote wanaoenda na kurudi kutoka Mecca hupita. Mji wa Mecca upo umbali wa maili arobaini mashariki ya Jedda.
Uwanja wa ndege wa Jedda ulionekana kujaa watu kuliko hata ule wa Cairo. Kikundi chetu kikawa moja tu ya vikundi vingi vya watu kutoka mataifa mbalimbali vilivyokuwa vikipishana pale uwanjani. Kila kikundi kilikuwa kinaelekea kupanga mstari mrefu kwenye ofisi za uhamiaji. Kabla ya kufika ofisi za uhamiaji, kila kikundi cha mahujaji kilipewa mtu aliyeitwa Mutawaf, huyu jukumu lake lilikuwa ni kusafirisha kikundi hicho kwenda Mecca. Baadhi ya mahujaji walikuwa wakipaza sauti wakisema “Labbayka!” wengine, baadhi yao wakiwa vikundi vikubwa, walikuwa wakisema sala kwa pamoja, nitaitafsiri sala hiyo, “Sijisalimishi kwa mwingine yoyote ila wewe. Ee Allah, sijisalimishi kwa mwingine ila wewe. Najisalimisha kwako kwa sababu huna mshirika. Sifa na Baraka zote zinatoka kwako. Nawe upo peke yako katika ufalme wako.” Dhumuni kubwa la sala hiyo ni kukiri Mungu mmoja.

Ni maafisa tu ndiyo hawakuvaa mavazi ya ki-Ihram au kofia nyeupe, kanzu nyeupe na makubadhi waliyovaa Mutawaf, yaani wale waliowaongoza mahujaji. Katika kiarabu neno Mutawaf linamaanisha “Yule anayeongoza” mahujaji kwenda “Tawaf” ambacho ni kitendo cha kuizunguka Kaaba.

Nikiwa katikati ya kikundi chetu, niilisonga kwenye mstari wa kusubiria passport zetu zikaguliwe, nilijawa na wasiwasi. Siamini kuwa nipo kwenye chimbuko la Uislamu, nawapatia passport ya Marekani ambayo inawakilisha kitu tofauti kabisa na kile ambacho Uislamu unakisimamia.

Jaji aliyekuwa kwenye kundi letu alihisi wasiwasi wangu, alinishika begani kunituliza. Upendo, unyenyekevu na undugu wa kweli ulionekana kila nilikogeuka. Mwishowe kundi letu likamfikia karani aliyechunguza passport na mikoba ya mahujaji kwa makini kabla ya kuwaruhusu kusonga mbele.
Nilikuwa na wasiwasi sana kiasi kwamba nilipofungua mkoba wangu kwa ufungua na ukagoma kufunguka, niliufungua kwa nguvu, nikiogopa kuwa wasije hisi kwenye mkoba wangu nina vitu nisivyotakiwa kuwa navyo. Karani akaona kuwa nina passport ya Marekani, aliishika huku akiniangalia, kisha akasema jambo fulani kwa kiarabu. Rafiki zangu niliokuwa nao wakaanza kuongea kwa ajili yangu haraka haraka kwa kiarabu. Jaji, kwa Kiingereza akaniuliza kuhusu barua kutoka kwa Dr. Shawarbi, aliichukua na

kuiweka mezani pa karani. Karani aliisoma na kuirudisha huku akisema kuwa nilitakiwa kusema mapema. Ubishi kunihusu ukaendelea, nilijihisi kama mpumbavu, sikuweza kusema chochote wala kuelewa kilichokuwa kikisemwa.Mwishowe, kwa unyonge, jaji alinigeukia na kusema kuwa nilitakiwa kupitia Mahgama Sharia. Ilikuwa ni mahakama kuu ya Kiislamu. Ilichunguza Waislamu wasio wa kweli waliojaribu kuingia Mecca. Ilikuwa wazi kuwa ni marufuku kabisa kwa asiye Muislamu kuingia Mecca.
Iliwabidi rafiki zangu wandelee kwenda Mecca bila ya mimi. Walionekana kujaa wasiwasi juu yangu. Nami nilijawa na wasiwasi lakini nilipata maneno ya kuwafariji, niliwaambia, “Nitakuwa sawa. Allah ananiongoza.” Walisema kuwa watasali kila saa kwa ajili yangu. Mutawaf woa aliwahimiza kuendelea mbele ili kuondoa msongamano pale uwanja wa ndege. Tulipungiana mkono, nikiwaangalia wakienda zao.
Wakati huo ilikuwa ni kama saa tatu asubuhi, siku ya Ijumaa. Sijawahi kuwa kwenye msongamano wa watu mkubwa kama ule, lakini sijawahi kujihisi mpweke na mnyonge tokea nilipokuwa mtoto. Mbaya zaidi ni kuwa, siku ya Ijumaa kwenye ulimwengu wa Kiislamu ni kama Jumapili kwenye ulimwengu wa Kikristo. Siku ya Ijumaa Waislamu wote hukusanyika kwa ajili ya kusali pamoja. Tukio hilo huitwa yawn al-Jumu’a “siku ya kukusanyika.” Ilimaanisha kuwa hakuna mahakama iliyofanya kazi siku ya Ijumaa. Itanibidi kusubiri hadi Jumamosi.

Afisa mmoja alimwita msaidizi wa Mutawaf. Kwa kiingereza kibovu afisa yule alinielekeza kuwa nitapelekwa eneo ambalo lilikuwepo palepale uwanja wa ndege. Passport yangu ilibaki ofisi za uhamiaji, nilitaka kupinga kwa sababu sheria ya kwanza ya msafiri ni kutoachana na passport yake, lakini sikufanya hivyo. Nikiwa kwenye mataulo na makubadhi, nilimfuata muongozaji yule aliyekuwa amevaa kofia nyeupe, kanzu nyeupe na makubadhi. Nafikiri ilivutia kututazama. Watu tuliopishana nao waliongea kila aina ya lugha. Sikuweza kuongea lugha yoyote nyingine. Nilikuwa kwenye hali mbaya sana.

Nje tu ya uwanja wa ndege kulikuwa na msikiti, na sehemu ya juu ya uwanja wa ndege kulikuwa na jengo kubwa lililokuwa kama bweni. Wakati huo ilikuwa karibu na mapambazuko, ndege zilikuwa bado zinaruka na kutua—taa zao za mkiani zikimulika-mulika anga. Mahujaji kutoka Ghana, Japan, Indonesia, Urusi na kwingineko, walikuwa wakiingia na kutoka kwenye jengo lile la bweni nilikokuwa napelekwa. Sidhani kama kuna kamera ya video imewahi chukua picha ya binadamu wenye pilika pilika kama niliyochukua kwa macho yangu. Tulifika kwenye jengo na kuanza kupanda hadi ghorofa ya nne, ghorofa ya juu kabisa. Njiani tulikutana na watu wa kila aina duniani. Wachina, Waindonesia, waafghanistani. Wengi wao wakiwa bado hawajavaa nguo za ki-Ihram, bado wamevalia mavazi ya kitamaduni ya nchi zao. Ilikuwa kama kuangalia kurasa za jarida la National Geographic.

Tulipofika ghorofa ya nne, muongozaji wangu alinielekeza kwenye chumba changu ambacho kilikuwa na watu wengine kama kumi na tano. Wengi wao wakiwa wamelala kwenye mazulia yao. Niliweza kuona kuwa wengine walikuwa ni wanawake, wakiwa wamejifunika kutoka usoni hadi miguuni. Kulikuwa na Muislamu mmoja mzee na mke wake ambao walikuwa macho. Walinishangaa kistaarabu. Waislamu wawili kutoka Misri na mwingine wa kutoka Iran waliamka wakati wakati muongozaji wangu aliponiingiza ndani. Kwa ishara, alisema kuwa atanionyesha njia sahihi ya kukaa wakati wa kusali. Fikiria kuwa Imam wa Kiislamu, kiongozi katika Taifa la Kiislamu la Elijah Muhammad lakini ukawa hujui taratibu za sala!

Nilijaribu kufanya alivyofanya, nilijua kuwa sikuwa nafanya sahihi. Niliweza kuona macho ya Waislamu wengine yakinitazama. Vifundo vya miguu vya mtu wa Magharibi haviwezi kufanya kile ambacho vifundo vya Muislamu vimekuwa vinafanya maisha yake yote. Watu wa Asia huchuchumaa wanapoketi, watu wa magharibi huketi wima vitini. Muongozaji wangu alipokuwa ameinama, nilijitahidi kila niwezavyo kufanya kama alivyofanya lakini sikuweza. Baada ya kama saa moja muongozaji wangu aliondoka na kuashiria kuwa atarudi baada ya saa moja.
Hata sikuweza kulala. Niliendelea kufanyia mazoezi mkao wa kusali. Nilijizuia kufikiria jinsi nilivyoonekana kituko mbele yao. Baada ya muda kidogo nikawa nimejifunza mbinu ya kuniwezesha kuinama hadi sakafuni, lakini baada ya siku mbili au tatu kifundo changu cha mguu kilikuja kuvimba.

Kulipokucha Waislamu waliamka na walitambua uwepo wangu mara moja, tuliendelea kushangaana huku wakiendelea na shughuli zao. Nilianza kuona jinsi ambavyo zulia ni muhimu sana katika maisha ya Waislamu. Kila mtu alikuwa na zulia dogo, na kila mtu na mkewe au na kundi kubwa, walikuwa na zulia kubwa. Waislamu hawa walisali kwenye mazulia yao mulemule chumbani. Baada ya hapo waliweka kitambaa cha mezani juu ya zulia na kuanza kula, hivyo zulia likawa chumba cha chakula. Baada ya kutoa vyombo na kitambaa cha mezani, waliketi zuliani, likawa sebule. Wanapolilalia linakuwa chumba cha kulala. Kabla ya kuondoka, ikanijia akilini na kuelewa kwa nini mtu yule aliyenunua vitu vya wizi nilipokuwa jambazi kule Boston alilipia pesa nyingi sana kwa ajili ya mazulia ya mashariki. Ni kwa sababu mazulia kutoka nchi ambazo mazulia ni muhimu sana yalishonwa kwa ustadi sana. Baadaye nilipokuwa Mecca, nilijionea umuhimu mwingine wa mazulia. Iwapo mzozo wowote ulitokea, mtu aliyeheshimiwa sana na ambaye hakuhusika na mzozo aliketi kwenye zulia huku wale wanaozozana wakimzunguka, na hilo lilifanya zulia kuwa mahakama. Nyakati nyingine lilikuwa darasa.

Mmoja wa Waislamu kutoka Misri alikuwa akiniangalia sana kwa jicho la wizi. Nilimuangalia na kutabasamu. Aliinuka na kunifuata. “Hel-lo-” alisema, alisikika kama wakati Lincoln anatoa hotuba kwenye makaburi ya Gettysburg. Nilimjibu, “Hello!” Nilimuuliza jina lake, lakini hakuelewa vizuri kiingereza. Nafikiri alikuwa na maneno ishirini tu ya kiingereza. Nilikuwa nasema chochote kilichonijia kichwani. Mwishowe nilisema, “Muhammad Ali Clay-”Waislamu wote waliokuwa wakisikiliza walinga’aa kwa shangwe kama mti wa Krismasi. “Ni wewe? Ni wewe?” alisema rafiki yangu akinionyeshea kidole. Nilitingisha kichwa na kusema, “Hapana, hapana, Muhammad Ali ni rafiki yangu!” Baadhi walielewa kiasi, wengine hawakuelewa kabisa na hivyo ndivyo ilivyoanza kusambaa kuwa nilikuwa Cassius Clay, bingwa wa ndondi wa uzito wa juu duniani. Baadaye nilikuja kufahamu kuwa karibu kila mwanaume, mwanamke na mtoto wa Kiislamu alikuwa amesikia jinsi ambavyo Sonny Liston(Mtu ambaye kwa Waislamu alikuwa kama zimwi mla watu) alipigwa na Cassius Clay kama vile Daudi alivyompiga Goliati, Cassius ambaye baadaye aliutangazia ulimwengu kuwa jina lake ni Muhammad Ali na dini yake ni Uislamu na Allah ndiye aliyempa ushindi.

Kuanza kuwasiliana kulisaidia sana. Kuwa kwangu Muislamu kutoka Marekani, kulibadili mtazamo wao, kutoka kuniangalia tu hadi kutaka kunisaidia. Sasa wengi wakaanza kutabasamu. Walikuja karibu na, walinitazama juu hadi chini-kistaarabu. Nilikuwa kama mtu kutoka sayari ya Mirihi.

Yule msaidizi wa Mutawaf alirudi na kuonyesha ishara kuwa nimfuate. Alionyeshea Msikiti ulikokuwa na nikafahamu kuwa alikuja kunichukua kwa ajili ya sala ya alfajiri, El Sobh iliyofanyika kabla ya jua kuchomoza.

Nilimfuata na njiani tulikutana na maelfu ya mahujaji, wakiongea lugha mbalimbali isipokuwa Kiingereza. Nilijichukia kwa kutojifunza taratibu halisi za sala kabla ya kuondoka Marekani. Kwenye Taifa la Kiislamu la Elijah Muhammad hatukuwahi kusali kwa Kiarabu. Miaka kadhaa nyuma, nilipokuwa gerezani, Muislamu mmoja asilia kutoka Boston aliyeitwa Abdul Hameed, alinitembelea na baadaye akanitumia sala zikiwa katika kiarabu. Wakati huo nilijifunza sala zile. Lakini sikuwahi kuzitumia tena.

Niliamua akilini kuwa nitamuacha muongozaji wangu afanye kila kitu kwanza nami nitamuangalia. Haikuwa kazi ngumu kumfanya aanze kufanya kwanza, alikuwa na shauku ya kunionyesha. Nje ya msikiti kulikuwa na mabomba yamejipanga. Udhu ulifanyika kabla ya sala. Hilo nililifahamu. Lakini hata baada ya kumuangalia sikuweza kufanya kwa usahihi. Kulikuwa na njia sahihi ya kujiosha, na kufanya kwa njia sahihi ilikuwa muhimu sana.

Nilimfuata kuelekea msikitini, nyuma yake nikimuangalia kwa makini. Aliinama, kichwa chake kikagusa chini. Nami nikafanya hivyo. “Bi-smi-llahi-r-Rahmain-r-Rahim-” (“Kwa jina la Allah, mwenye kuruzuku na mwenye rehema”) sala zote za Waislamu huanza hivyo. Baada ya hapo nadhani nilikuwa nasema vitu visivyo sahihi, lakini niliendelea kusema.

Si nia yangu jambo hili lionekane kama mzaha. Kwangu haukuwa mzaha hata kidogo. Hakuna ambaye alikuwa karibu ambaye angeweza kusema kuwa nilikuwa sisemi yale waliyokuwa wanasema wengine.

***

Baada ya sala hiyo, muongozaji wangu alinipeleka hadi kwenye makazi yangu. Kwa ishara, aliniambia kuwa atarudi baada ya saa tatu, kisha akaondoka.

Sehemu tuliyokuwa ilituwezesha kuona eneo la uwanja wa ndege vizuri sana. Nilisimama kwenye kibaraza nikiangalia. Ndege zilikuwa zinaruka na kutua bila kupumzika. Maelfu elfu ya watu kutoka kote duniani walipita huku na kule. Niliona vikundi vilivyokuwa vinaelekea Mecca kwa mabasi na magari madogo. Niliona wengine walioamua kutembea maili zile arobaini. Nilitamani name ningeanza kutembea. Walau hilo nilijua jinsi ya kulifanya.

Nilikuwa naogopa hata kufikiri yatakayotokea. Je nitakataliwa kuingia Mecca kuhiji? Niliwaza maswali ya kunipima yatakuwaje na muda gani nitafika mbele ya Mahakama Kuu ya Kiislamu.

Yule Muislamu kutoka Iran alinifuata. Alinisalimu kwa kusita kidogo, “Mmare . . . Mmarekani?” alionyesha ishara kuwa anataka niende kujumuika naye na mkewe kwenye kupata kifungua kinywa, kwenye zulia lao. Nilifahamu kuwa ni ukarimu mkubwa sana alikuwa akinifanyia. Haunywi chai na Muislamu pamoja na mkewe kirahisirahisi. Sidhani kama Muiran yule alinielewa nilipotingisha kichwa na kutabasamu, nikimaanisha “Hapana, ahsante.” Hata hivyo aliniletea chai na biskuti. Mpaka wakati ule nilikuwa sina kabisa wazo la kula.

Wengine walifika na kunisalimu kwa ishara ya kichwa huku wakitabasamu. Rafiki yangu wa kwanza, yule aliyeongea kiingereza kidogo alikuwa amekwishaondoka. Nilikuwa sifahamu kinachoendelea, lakini alikuwa amesambaza taarifa kuwa kwenye ghorofa ya nne kulikuwa na Muislamu kutoka Marekani. Msongamano wa watu ukaanza kupita kuelekea kwenye makazi yetu. Waislamu wakiwa wamevalia mavazi ya ki-Ihram, na wengine wakiwa bado wamevaa mavazi yao ya kitamaduni, walinipita polepole huku wakitabasamu. Jambo hilo liliendelea kwa muda mrefu niliokuwepo eneo lile. Lakini sikufahamu kuwa mimi ndiye nilikuwa kivutio.

Siku zote nimekuwa mtu asiye na utulivu na mwenye wasiwasi. Maidizi wa Mutawaf hakurudi baada ya saa tatu kama alivyokuwa amesema na hilo lilinifanya niingiwe na wasiwasi. Niliogopa kuwa atakuwa ameamua kuachana na mimi kwa kuona kuwa siwezi kusaidika. Na wakati huo njaa nayo ilianza kunibana. Waislamu wote katika chumba chetu walikuwa wamenikaribisha chakula nami nilikataa. Naomba nikiri kuwa tatizo ni sikudhani kama nitaendana na namna yao ya ulaji. Kila kitu kiliwekwa kwenye poti moja juu ya zulia lililokuwa chumba cha chakula, na niliona wote wakila humo kwa kutumia mikono yao.

Niliendelea kusimama kibarazani pale nikiangalia uwanja wa ndege kule chini, mwishowe nikaamua nitembee-tembee kidogo. Nilishuka chini mpaka kwenye ua, nilionelea kuwa nisiende mbali, mtu anaweza kuja kunitafuta. Basi nikarudi chumbani kwetu. Baada ya kama dakika arobaini na tano nikashuka tena chini, safari hii nilienda, mbali kidogo. Niliona mgahawa mdogo uliokuwa karibu na ua. Niliingia ndani moja kwa moja. Ulikuwa umejaa huku lugha mbalimbali zikisikika. Kwa kutumia ishara, nilinunua kuku mzima wa kukaanga na chips nene za viazi. Nilirudi uani na kumchanchana kuku yule, nikitumia mikono yangu. Waislamu wote walionizunguka walikuwa wanafanya hivyo hivyo. Niliona wanaume wa walau miaka sabini wakikaa kwa kukunja miguu mpaka wakawa wanaonekana kama wamejifunga hivi. Wakila kwa furaha na kuridhika kama vile wapo ndani ya mgahawa mzuri, wakiwa wamezungukwa na wahudumu. Wote walikula pamoja na kulala pamoja. Kila kitu kuhusu mazingira ya hija, kilionyesha umoja wa binadamu chini ya Mungu mmoja.

Siku ile nilifanya safari kadhaa kati ya chumbani kwetu na kwenye ua wa jengo, kila wakati nikienda kutembea mbali kidogo. Nilikutana na wanaume wawili weusi na nikawasalimia kwa kichwa. Ilikuwa karibu nipige kelele kwa shangwe baada ya mmoja wao kunisalimu kwa Kiingereza chenye lafudhi ya Uingereza. Hatimaye nilikutana na Waislamu wawili waliozungumza kiingereza, bahati mbaya ndiyo walikuwa wanaondoka. Kabla ya kikundi chao kuondoka kuelekea Mecca, tulizungumza kidogo. Nikajitambulisha kuwa ni Mmarekani na wao wakaniambia ni Waethiopia. Waethiopia wale walikuwa wamepata elimu yao katika jiji la Cairo na sasa walikuwa wakiishi na kufanya kazi katika jiji la Riyadh, mji mkuu wa Saudi Arabia. Baadaye nilishangaa sana baada ya kufahamu kuwa kati ya raia milioni kumi na nane wa Ethiopia, milioni kumi walikuwa ni Waislamu. Watu wengi hudhani kuwa Ethiopia ina Wakristo wengi. Lakini ni serikali yake tu ndiyo ina Wakristo wengi. Siku zote nchi za magharibi zimeisaidia serikali ya Kikristo kubaki madarakani.

Nilikuwa nimeishasali sala yangu ya jioni, El Maghrib; nikawa nimelala kitandani kwangu kwenye chumba chetu. Nikijihisi mpweke na mnyonge ndipo ghafla ukaja mwanga!

Lilikuwa ni wazo la ghafla. Katika safari zangu za kwenda kwenye ua wa jengo lile, mahali palipokuwa pamejaa watu, nilikuwa nimewaona maafisa wanne waliokuwa wamekaa karibu na simu. Nikakumbuka namba alizonipatia Dr. Shawarbi kule New York, namba ya mtoto wa mwandishi wa kile kitabu alichonipatia, ambacho tayari nilikuwa nimekimaliza kukisoma. “Baba yangu atafurahi sana kuonana nawe,” alisema Dr. Azzam.

Nilimuuliza maswali kuhusu baba yake. Abd-Al-Rahman Azzam alijulikana zaidi kama Azzam Pasha, au Bwana Azzam mpaka wakati wa mapinduzi ya Misri pale Rais Nasser alipofuta vyeo vyote vya “kibwana.” “Nadhani atakuwepo nyumbani kwangu tukifika huko,” alisema Dr. Azzam. “Anatumia muda mwingi New York kwenye kazi yake ya Umoja wa Mataifa, amekufuatilia kwa ukaribu sana.”
Nilibaki mdomo wazi.

Ilikuwa ni alfajiri tulipofika kwenye nyumba ya Dr. Azzam. Baba yake alikuwepo pale. Pia walikuwepo kaka wa baba yake, ambaye alikuwa ni mkemia na rafiki yao mwingine, wote wakiwa macho mapema ile wakitusubiri. Kila mmoja alinikaribisha kwa bashasha kama vile nilikuwa mwana wao niliyepotea kwa muda mrefu. Sikuwahi kuwaona watu hao maishani lakini walinitendea kwa ukarimu sana! Nikuambie tu kuwa sijawahi heshimishwa namna ile maishani mwangu wala kuona ukarimu wa kweli kiasi kile.

Mhudumu alituletea chai na kahawa, kisha akaondoka. Niliambiwa nijisikie nipo nyumbani. Hakuna mwanamke aliyeonekana. Ukiwa Arabia unaweza dhani nchi haina wanawake.

Dr. Abd-Al-Rahman azzam ndiye aliyeongoza mazungumzo. Kwa nini sikupiga simu mapema? Hawakuelewa kwa nini sikufanya hivyo. Walionekana kufedheheka kuwa nilikaa uwanja wa ndege; na kwamba nilicheleweshwa kuingia Mecca. Nilijitahidi kuwaaminisha kuwa nilikuwa sawa na hakuna shida yoyote hawakukubali. “Unatakiwa kupumzika,” alisema Dr. Azzam, kisha akaenda kupiga simu.

Sikujua mtu huyu muungwana alikuwa anafanya nini. Nilipoambiwa nitarudishwa baadaye kwa ajili ya chakula cha jioni, na kuwa wakati huo nirudi garini, sikujua kabisa kuwa nilikuwa naenda kupokea ukarimu mkubwa kabisa wa Kiislamu.

Abd-Al-Rahman Azzam anapokuwa nyumbani Saudi Arabia huwa anaishi kwenye hoteli ya Jedda Palace. Kwa sababu niliwatembelea nikiwa na barua kutoka kwa rafiki yao, yeye aliamua kuishi nyumbani kwa mwanawe na kuniacha mimi nitumie makazi yake ya hotelini mpaka nitakapokwenda Mecca.

Nilipokuja kufahamu jambo hilo nilikuwa nimeishachelewa na sikuweza tena kupinga; tayari nilikuwa ndani ya makazi yale na Dr Azzam mdogo akawa ameishaondoka. Hakukuwa na wakumbishia. Makazi yake ya hotelini yalikuwa na vyumba vitatu vikubwa vya kulala. Kulikuwa na bafu kubwa kama mara mbili ya yale ya hoteli ya Hilton ya New York. Yalikuwa makazi namba 214. Na hata kulikuwa na kibaraza nje yake na hivyo kukuwezesha kuona vizuri mji ule wa pwani ya bahari ya Shamu.

Hapo kabla hisia zangu hazijawahi guswa kusali kama siku ile-na nikafanya hivyo. Nikasali kwenye zulia lililokuwako sebuleni.

Katika maisha yangu ya aina mbili niliyoishi kama mtu mweusi wa Marekani, hakuna hata moja iliyonipa mtazamo wa kiitikadi. Siku zote akili yangu ilichunguza sababu la lengo la mtu yeyote liyenitendea jambo ambalo sikustahili. Na siku zote, kama mtu huyo ni mzungu niliweza kuona lengo lake la kibinafsi.

Lakini siku ile hotelini pale ilikuwa ni moja ya mara chache sana ambazo nilipigwa na butwaa kiasi cha kushindwa kupinga. Mzungu yule—walau kwa Marekani angechukuliwa kuwa ni mzungu, alikuwa na undugu na mtawala wa Saudi Arabia ambaye alikuwa ni mshauri wake, mtu mkubwa kimataifa ambaye hana lolote la kupata kwa kunikarimu aliniachia makazi yake ya hotelini! Hakuwa na uhitaji wowote na mimi. Alikuwa na kila kitu. Ukweli ni kuwa alikuwa na vingi vya kupoteza kuliko kupata. Alikuwa amenifuatilia kwenye vyombo vya habari vya Marekani. Na kama alifanya hivyo, alifahamu vyema kuwa sikuwa na chochote zaidi ya kupewa sifa mbaya na kunyanyapaliwa. Nilikuwa dubwana lenye mapembe. Nilikuwa “mbaguzi wa rangi.” Nilikuwa “Mchukia wazungu” na yeye kwa muonekano alikuwa mzungu. Nilitwa mhalifu; na si hilo tu, bali kila mtu alikuwa akinishutumu kutumia dini yake ya Uislamu kama kichaka cha falsafa zangu na matendo yangu ya kihalifu. Na hata kama alikuwa na lengo la kunitumia, alifahamu vyema kuwa nilitengana na Elijah Muhammad na Taifa la Kiislamu, “nguzo zilizonipa nguvu,” kama vilivyodai vyombo vya habari vya Marekani. Taasisi pekee niliyokuwa nayo ilikuwa na majuma machache tu tokea ianzishwe. Sikuwa na kazi. Sikuwa na pesa. Na hata kufika pale nilikuwa nimekopa pesa kutoka kwa dada yangu.

Asubuhi ile ndipo nilipoanza kumtafakari “mzungu” tena. Ndipo nilipoanza kuchukulia kuwa neno “mzungu”, kama ambavyo limezoeleka kutumika, halimaanishi kutokana na rangi yake hasa, bali hasa linamaanisha tabia na matendo yake. Ndani ya marekani “mzungu” linamaanisha tabia na matendo fulani kuelekea mtu mweusi na watu wengine wote wasio weupe. Lakini kwenye ulimwengu wa Kiislamu, niliona watu wenye rangi nyeupe wakiwa na upendo wa kweli kuliko niliowahi kuuona kutoka kwa yeyote yule.

Asubuhi ile ndipo ndipo mtazamo wangu mzima juu ya “mzungu” ulipobadilika.

Ngoja ninukuu kutoka kwenye kijitabu changu. Niliandika haya mchana ule nilipokuwepo hotelini: “Siwezi kuelezea shangwe niliyonayo nikiwa nimekaa hapa nikisubiri kwenda mbele ya Kamati ya Hajj. Dirisha langu linaangalia upande wa Magharibi, iliko bahari. Mitaa imejaa mahujaji kutoka kote duniani. Sala zinatolewa kwa Allah na aya za Quran zipo kwenye midomo ya kila mmoja. Sijawahi ona jambo zuri kama hili, wala kushuhudia, wala kulihisi.

Ninajihisi salama, maelfu ya maili kutoka kwenye maisha tofauti kabisa niliyoishi. Piga picha kuwa saa ishirini na nne zilizopita nilikuwa kwenye chumba kilichokuwa katika ghorofa ya nne pale uwanja wa ndege, nikiwa nimezungukwa na watu ambao siwezi kuwasiliana nao, nikiwa sijui kabisa mustakabali wangu utakuwaje na kujihisi mpweke sana, lakini simu moja tu kama Dr. Shawarbi alivyonielekeza, imefanya nikutane na mmoja ya watu wenye nguvu sana katika Ulimwengu wa Kiislamu. Muda si mrefu nitalala kitandani pake ndani ya hoteli ya Jedda Palace. Natambua vyema kuwa nimezungukwa na rafiki ambao hawana unafiki na ni watu ninaoweza kuhisi nguvu ya imani yao. Inanipasa kusali tena kumshukuru Allah kwa Baraka hii, inanipasa kusali kwa ajili ya mke wangu na watoto wangu waliopo Marekani ili nao wapokee Baraka siku zote kutokana na kujitoa kwao.”

Nilisali sala mbili zaidi kama nilivyoandika kwenye kijitabu changu. Baada ya hapo nikalala kwa saa nne mpaka pale simu ilipoita. Alikuw ani Dr. Azzam mdogo. Alisema kuwa baada ya saa moja atakuja kunichukua kwa ajili ya kwenda kupata chakula cha jioni. Nilijiumauma wakati wa kujaribu kutafuta maneno ya shukrani. Alinikatisha kwa kusema, “Ma sha’a-llah” neno linalomaanisha, “Mungu ndiye aliyepanga.”

Wakati wa kumsubiri Dr. Azzam, nilikimbia mara moja kwenda ukumbi wa mapokezi ya hoteli. Nilipokuwa natoka nilionana koridoni na mtu mmoja aliyevalia kiramsi huku akiwa amezungukwa na wahudumu. Ilionekana wazi kuwa anaishi pale. Naye alikuwa anashuka chini. Nilifuatana nao walipokuwa wanashuka hadi kupita ukumbi wa mapokezi. Nje kulikuwa na msafara mdogo wa magari ukiwasubiri. Jirani yangu yule alipotokea mlango wa mbele wa hoteli, watu walimkimbilia na kumbusu mkono. Nilikuja kutambua kuwa alikuwa ni Mufti Mkuu wa Jerusalem. Baadaye hotelini pale nilipata wasaa wa kuongea naye kwa kama nusu saa. Alikuwa mtu mwenye urafiki na mwenye kujiendesha kwa heshima sana. Alifahamu vyema mambo ya dunia, na hata matukio yaliyokuwa yanaendelea Marekani.

Sitakuja kusahau ule mlo wa jioni nyumbani kwa Azzam. Nitanukuu daftari langu tena: ‘Akilini mwangu sikuweza kujiambia kuwa watu hawa ni ‘wazungu.’ Kwa nini, kwa sababu walinitendea kama vile ni ndugu yao, Dr. Azzam mkubwa kama baba yangu. Maneno yake ya kibaba na kiuanazuoni yalinifanya nimhisi kama baba yangu. Haikuwa kazi ngumu kugundua kuwa alikuwa mwanadiplomasia mbobezi, mtu mwenye maarifa mengi. Alifahamu mambo yanayoendelea duniani kama mtu anavyofahamu yanayoendelea sebuleni kwake.

‘Kadri tulivyozungumza, ndivyo maarifa yake juu ya mambo mbalimbali yalivyoonekana hayana kikomo. Aliongelea jamii ya vizazi vya Mtume Muhammad, na alionyesha jinsi ambavyo walikuwepo weupe na weusi. Alionyesha pia jinsi ambavyo tatizo la ubaguzi wa rangi kwenye ulimwengu wa Kiislamu lipo kwenye maeneo yale tu yaliyoathiriwa na nchi za magharibi. Alisema kuwa kiasi cha ubaguzi wa rangi anachokutana nacho mtu sehemu fulani kinaashiria kiasi cha ushawishi wa magharibi katika eneo hilo.’

Wakati wa chakula nilifahamishwa kuwa nilipokuwa hotelini, Kamati ya Hajj ilijulishwa kuhusu suala langu, na kwamba asubuhi natakiwa kufika huko. Nilifanya hivyo.

Jaji alikuwa ni Sheikh Muhammad Harkon. Mahakamani hakukuwa na watu isipokuwa mimi na dada mmoja kutoka India ambaye zamani alikuwa ni mprotestanti na sasa amesilimu, na kama mimi tu, naye alikuwa anajaribu kufanya hija. Alikuwa na rangi ya kahawia na sura ndogo ambayo ilikuwa imezibwa kwa sehemu kubwa. Jaji Harkon alikuwa mtu mpole na thabiti, tuliongea na aliniuliza maswali kadhaa, akijaribu kuona kama nimeamini kweli. Nilimjibu kwa ukweli wangu wote. Si tu kuwa alinitambua kama Muislamu wa kweli, bali pia alinipatia vitabu viwili. Kimoja kimeandikwa kwa Kiingereza na kingine kwa Kiarabu. Aliandika jina langu kwenye orodha takatifu ya Waislamu wa kweli na tukawa tumemaliza. Aliniambia, “Natumaini utakuwa mhubiri mkubwa wa Uislamu katika Marekani.” Nilimwambia kuwa nami nina matumaini hayo na nitajaribu kuyatimiza.

Familia ya Azzam ilifurahi sana kusikia kuwa nimekubaliwa kwenda Mecca. Nilipata chakula cha mchana kwenye hoteli ya Jedda Palace kisha nikalala tena kwa saa saba, simu ndiyo iliyoniamsha.

Alikuwa ni Muhammad Abdul Azziz Maged, makamu mkuu wa protokali wa Mwanamfalme Faisal. “Gari maalumu itakusubiri kwenda Mecca mara tu baada ya chakula cha jioni,” aliniambia. Aliniambia nile vya kutosha sababu taratibu za Hajj zinahitaji nguvu nyingi. Mpaka wakati huo sikuwa nashangaa tena.

Waarabu wawili vijana waliambatana nami kwenda Mecca. Barabara kubwa ya kulipia iliyokuwa na mwanga wa kutosha ilifanya safari iwe rahisi sana. Walinzi wa njiani walitizama ndani ya gari mara moja na dereva aliwaonyeshea ishara na tukaruhusiwa kupita, bila hata ya kupunguza mwendo. Kwa wakati huohuo mmoja, nilikuwa mtu niliye muhimu na mnyenyekevu na mwenye shukrani.

Mji wa Mecca ulionekana kama mji wa kale sana. Gari letu lilipita kwenye barabara za mitaa zilizojipindapinda, zikiwa
zimejaa maduka pembeni yake. Mabasi, magari na makumi elfu ya mahujaji kutoka duniani kote walifurika mitaani.
Gari ilisimama mahali ambapo Mutawaf alikuwa akinisubiria. Alivalia kofia nyeupe na kanzu nyeupe, kama wale wa uwanja wa ndege. Alikuwa mwarabu mmoja mfupi na mweusimweusi hivi, jina lake aliitwa Muhammad. Hakuongea kiingereza hata kidogo.

Tulipaki karibu na Msikiti Mkuu wa Mecca. Tulifanya udhu na kuingia. Ndani kulijaa mahujaji waliosongamana. Wengine wakiwa wamelala, wengine wamekaa, wanaotembea na wengine wakisali.

Sina maneno ya kuuelezea msikiti mpya uliokuwa unajengwa kuzunguka Kaaba. Nilifurahi kufahamu kuwa ulikuwa ni moja ya miradi mikubwa ya ujenzi kati ya ile iliyosimamiwa na Dr. Azzam mdogo, mtu aliyekuwa mwenyeji wangu. Msikiti Mkuu wa Mecca utakapokamilika, utalipita jengo la Taj Mahal la India kwa uzuri.

Nilimfuata Mutawaf nikiwa nimebeba makubadhi yangu. Kisha nikaiona Kaaba. Jengo kubwa katikati ya Msikiti Mkuu. Lilikuwa linazungukwa na maelfu-elfu ya mahujaji wanaosali, watu wa jinsia zote, rangi, maumbo na kila aina kutoka pande zote duniani. Niliifahamu sala iliyopaswa kutolewa mara tu mahujaji anapoiona Kaaba. Tafsiri yake inasema, “Ee Mungu, wewe ni amani na amani inatoka kwako. Tunaomba Ee Mungu utukaribishe kwa amani.” Baada ya kuingia ndani ya Msikiti Mkuu, mahujaji anatakiwa kuibusu Kaaba iwapo anaweza, lakini kama umati unamzuia kuifikia, anapaswa kuishika. Na kama umati unamzuia kufanya hivyo, anatakiwa kuinua mkono juu na kupaza sauti, “Takbir!” (“Mungu ni Mkubwa”). Sikuweza kufika karibu. “Takbir!”

Hisia zangu mahali pale katika Nyumba ya Mungu zilikuwa kama nimepigwa ganzi. Mutawaf wangu aliniongoza hadi kwenye umati wa mahujaji waliokuwa wakitoa sala huku wakiizunguka Kaaba mara saba. Wengine walikuwa wamepinda na ngozi zao kujikunja sababu ya uzee; ilikuwa taswira ambayo si rahisi kukutoka kichwani. Niliona mahujaji walemavu wakiwa wamebebwa. Sura zao ziking’aa kwa furaha. Kwenye mzunguko wa saba, nilisali Rak’a mbili, nikiinama hadi kichwa kugusa chini. Nilianza kwa kusali aya ya Quran “Sema yeye ni Mungu, Mungu pekee”, sala ya pili: “Sema ee nyinyi msioamini, siabudu kile mnachoabudu ”

Nilipokuwa nikisali, Mutawaf wangu aliwazuia mahujaji wengine wasije kunikanyaga-kanyaga.

Kisha mimi na Mutawaf wangu tukanywa maji kutoka kisima cha Zamzam. Baada ya hapo tukakimbia kati ya vilima viwili, Safa na Marwa, mahali ambapo Hagari alitangatanga akitafuta maji kwa ajili ya mwanawe Ishmaeli.

Baada ya hayo, nilitembelea Msikiti Mkuu mara tatu na kuizunguka Kaaba. Asubuhi iliyofuata tulienda kwenye mlima Arafat, tulikuwa maelfu ya watu, tukipaza sauti kwa pamoja, “Labbayka! Labbayka!” na “Allah Akbar!” Mecca imezungukwa na milima ya kutisha ambayo sijawahi kuona mahali pengine; ni kama vile ilitengenezwa kwa uji wa chuma kutoka kwenye tanuri. Hakuna kitu chochote kilichoota juu yake. Tulipofika ilikuwa tayari mchana, tulisali mpaka jua lilipozama, tulifanya huko sala maalumu za mchana na jioni.

Mwishowe tuliinua mikono yetu na kutoa sala na shukrani, tukirudia maneno ya Allah: “Hakuna Mungu isipokuwa Allah. Hana mshiriki. Yeye ni mwenye mamlaka na sifa. Mema yanatoka kwake naye ni mwenye nguvu juu ya vitu vyote.”

Kusimama juu ya mlima Arafat ndiyo jambo la mwisho kwa mahujaji wa Mecca kutimiza. Hakuna mtu anayeweza kujiita mahujaji iwapo hajatimiza hilo.

Ihram ikawa imeisha. Tulimtupia shetani mawe saba. Wengine walikata nywele na ndevu zao. Niliamua kuwa nitaziacha ndevu zangu. Nilijiuliza mke wangu Betty na binti zangu wadogo watasema nini baada ya kuniona na ndevu nitakaporudi New York. New York ilionekana kama ipo umbali wa maili milioni moja. Sikuona gazeti lolote ninaloweza kusoma toka nitoke New York. Sikujua chochote juu ya yanayoendelea huko. Chama cha watu weusi waliomiliki bunduki ambacho kilikuwepo Harlem kwa miaka mingi kilikuwa “Kimegunduliwa” na polisi; ilikuwa inatangazwa kuwa nilikuwa nyuma ya suala hilo. Taifa la Kiislamu la Elijah Muhammad lilikuwa limenifungulia kesi, wakitaka kunitoa mimi na familia yangu kwenye nyumba tuliyoishi huko Long Island.

Magazeti makubwa, vituo vya redio na televisheni vya marekani vilikuwa na wawakilishi jijini Cairo waliokuwa wakijaribu kuniwinda kila sehemu, kujua niko wapi ili wanihoji juu ya mambo yanayoendelea huko New York, mambo niliyoshutumiwa kusababisha wakati sikujua chochote kuyahusu.

Kitu pekee nilichofahamu ni yale niliyoyaacha nilipoondoka Marekani, mambo ambayo ni kinyume kabisa na niliyoyakuta kwenye ulimwengu wa Kiislamu. Waislamu kama ishirini hivi tuliokuwa tumemaliza Hajj tulikuwa tumekaa kwenye hema kubwa lililokuwepo kwenye mlima Arafat. Nikiwa kama Muislamu kutoka Marekani, macho mengi yalinielekea. Waliniuliza ni kitu gani katika Hajj kilichonipendeza sana. Mmoja ya walioweza kuzungumza Kiingereza aliuliza na kisha kuwatafsiria wengine majibu yangu. Jibu langu kwa swali hilo halikuwa lile walilotegemea, lakini walielewa vyema nilichomaanisha.

Nilisema “Undugu! Kitendo cha watu wa kila aina na rangi, kutoka kote duniani kuja pamoja kama kitu kimoja! Kimenithibitishia nguvu za Mungu Mmoja.”

Pengine hapakuwa mahala pake, lakini hilo lilinipa nafasi ya kuwahubiria kidogo kuhusu ubaguzi wa rangi uliopo Marekani na madhira yake.

Niliweza kuona jinsi hilo lilivyowagusa. Walikuwa wanafahamu madhira waliyokutana nayo watu weusi wa Marekani, lakini hawakujua kama walitendewa kama wanyama, kwamba kilichofanyika kilikuwa sawa na kuhasiwa kisaikolojia. Watu hawa kutoka maeneo mbalimbali ya dunia walishangazwa sana. Wakiwa kama Waislamu, walikuwa na mioyo ya huruma sana kwa wale waliokuwa wanapitia taabu, na watu waliguswa sana haki na kweli. Walielewa vyema mtazamo wangu wa mambo—kwamba kwangu mimi uovu mkubwa sana duniani ni ubaguzi wa rangi, na viumbe wa Mungu kushindwa kuishi kama kitu kimoja katika ulimwengu wa Magharibi.

***
 
Sura ya 17 inaendelea.​

Niliketi na kuandika barua iliyofunua mambo yaliyokuwa yanapita akilini mwangu.

Upofu wa kutoona rangi uliopo katika jamii ya kidini ya Waislamu. Na upofu wa rangi uliopo kati ya jamii ya binadamu wa Kiislamu.
Barua ya kwanza ilikuwa ni kwenda kwa mke wangu Betty. Sikuwa na shaka kuwa baada ya kushangazwa mwanzoni, ataungana na namna yangu ya kufikiri. Nilikuwa na uhakika mara elfu kuwa imani ya Betty juu yangu ilikuwa ni kamili
kabisa.Nilifahamukuwa ataona
nilichoona—kwamba​
kwenyenchi yaMuhammad na
Abraham, nilikuwa​
nimebarikiwa na Allah kwa kupewa mtazamo mpya juu ya dini ya kweli ya Kiislamu, na uelewa mzuri juu ya tatizo la rangi la Marekani.

Baada ya kuandika barua kwa mke wangu, niliandika nyingine ya namna ile ile kwa dada yangu Ella. Nilijua Ella amesimama upande gani. Yeye mwenyewe alikuwa akitunza pesa kwa ajili ya kwenda hija Mecca.

Nilimuandikia Dr. Shawarbi ambaye imani yake juu yangu ilifanya niweze kupata passport ya Mecca.

Usiku mzima nilikuwa ninanakili barua ile kwenda kwa watu wangu wa karibu. Mmoja wao alikuwa ni kijana wa Elijah Muhammad, Wallace Muhammad ambaye alikuwa amekiri kwangu kuwa njia pekee kwa Taifa la Kiislamu kusonga mbele ni kuukubali na kuutenda Uislamu wa asili.

Pia niliwaandikia wasaidizi wangu waaminifu kwenye taasisi yetu mpya ya Muslim Mosque, Inc huko Harlem. Niliambatanisha na ujumbe kuwa barua yangu itolewe nakala na zisambazwe kwenye vyombo vya habari.
Nilifahamu kuwa mara tu barua yangu itakapochapwa magazetini, wengi watashangazwa sana-wapendwa wangu, rafiki na adui pia. Na mamilioni wengine ambao sikuwafahamu wangeshangazwa pia-watu ambao kwa miaka kumi na mbili niliyokuwa na Elijah Muhammad walikuwa wanataswira ya “chuki” juu ya Malcom X.

Hata mimi mwenyewe nilishangazwa. Lakini barua hii haikuwa bahati mbaya. Maisha yangu yote yamekuwa ya kubadilikabadilika.

Hiki ndicho nilichoandika . . .kutoka moyoni kabisa: ‘Kamwe sijawahi kushuhudia ukarimu wa kweli na undugu wa kweli kati ya watu wa kila rangi kama nilioshuhudia hapa kwenye nchi takatifu, nyumbani kwa Abraham, Muhammad na manabii wengine watakatifu walioandikwa katika Maandiko Matakatifu. Katika juma lililopiata, nimepigwa na butwaa na kushindwa kuongea kutokana na ukarimu nilioonyeshwa na watu walionizunguka, watu wa kila rangi.

‘Nimebarikiwa kuweza kutembelea Mji Mtakatifu wa Mecca. Nimeizunguka Kaaba mara saba, nikiongozwa na Mutawaf kijana aitwaye Muhammad. Nimekunywa maji kutoka kisima cha Zamzam. Nimekimbia mara saba kati ya vilima vya Al-Safa na Al-Marwah. Nimesali kwenye mji wa kale wa Mina, na nimesali kwenye mlima Arafat.

‘Kulikuwa na makumi elfu ya mahujaji kutoka duniani kote. Watu wa kila rangi, kutoka wenye macho ya bluu na nywele za rangi ya dhahabu hadi waafrika wenye ngozi nyeusi. Wote tulifuata taratibu zilezile, tukionyesha roho ya umoja na undugu, vitu ambavyo kuishi kwangu Marekani kuliniaminisha kuwa haviwezekani kutokea kati ya mzungu na mtu asiye mzungu.

‘Marekani inatakiwa kuuelewa Uislamu kwa sababu hii ndiyo dini pekee inayofuta tatizo la ubaguzi wa rangi kwenye jamii. Katika kutembea kwangu kote kwenye ulimwengu wa Kiislamu, nimekutana, nimeongea na hata kula na watu ambao Marekani wangechukuliwa kuwa ni ‘wazungu’ lakini dini ya Kiislamu imeondoa mtazamo wao wa ‘kizungu’ katika akili zao. Kamwe sijawahi ona undugu wa kweli ukifanywa na watu wa kila rangi, bila kujali rangi zao.

‘Unaweza kushangazwa kusikia maneno hayo yakitoka kwangu. Lakini katika hija hii, yale niliyojionea na kuyaishi, yamesababisha kubadili sehemu kubwa ya mtazamo wangu niliokuwa nao hapo kabla, na kuachana na baadhi ya mambo niliyoamini hapo kabla. Hili halikuwa jambo gumu kwangu. Pamoja ya kuwa mimi ni mtu thabiti katika misimamo, lakini siku zote nimekuwa mtu ninayejitahidi kukubaliana na ukweli na hali halisi ya maisha kadri mambo na maarifa mapya yanavyojifunua. Siku zote nimekuwa na akili huru, kitu ambacho ni muhimu ili kuendana na mabadiliko yanayoambatana na kutafuta ukweli.

‘Katika siku kumi na moja zilizopita nilizoishi hapa katika ulimwengu wa Kiislamu, nimekula kutoka kwenye sahani moja, na kunywa kutoka kwenye glasi ileile, na kulala katika kitanda kimoja(Au kwenye zulia moja)-nikisali kwa Mungu yuleyule na Waislamu wenzangu, watu ambao macho yao yalikuwa ya bluu hasa, na nywele zao za dhahabu hasa, na ngozi zao nyeupe hasa. Niliona maneno na matendo yasiyo na unafiki kutoka kwa Waislamu weupe kama tu niliyoona kutoka kwa Waislamu weusi wa Afrika kutoka Nigeria, Sudan na Ghana.

‘Sote tulikuwa sawa(Ndugu)-sababu imani yao katika Mungu mmoja iliondoa ‘weupe’ katika akili zao, ‘weupe’ kutoka katika tabia zao, na ‘weupe’ kutoka kwenye mitazamo yao.

‘Katika hilo niliona kuwa, pengine wazungu wa Marekani wakikubali Mungu mmoja, pengine pia nao watakubali ukweli kuwa binadamu wote ni wamoja-na kuacha kuwapima, kuwadhuru na kuwakwamisha wengine kutokana na rangi ya ngozi zao.

‘Ugonjwa wa ubaguzi wa rangi ukiwa umeiandama Marekani kama kansa. Mioyo ya wakristo wa Marekani inatakiwa kukubaliana na suluhisho lililothibitika kutibu ugonjwa huo mbaya. Pengine haitakuwa kuchelewa kuiokoa Marekani kutoka kwenye janga linaloikabili-janga la maangamizi kama lile lililoikuta Ujerumani sababu ya ubaguzi, janga ambalo mwishowe liliwaangamiza Wajerumani wenyewe.

‘Kila saa inayopita katika hii Nchii Takatifu, inanifanya nielewe vyema kiroho hali ya mambo yanayoendelea Marekani kati ya wazungu na watu weusi. Kamwe mtu mweusi wa Marekani hawezi kulaumiwa kuwa ni mbaguzi wa rangi-anachofanya ni matokeo ya ubaguzi wa rangi aliokabili waziwazi kwa miaka mia nne.

‘Lakini kadri ambavyo ubaguzi wa rangi unaipeleka Marekani kwenye kujiangamiza, nina imani kuwa kizazi cha vijana wa Marekani, kutokana na uzoefu niliopata kwa kukaa nao-vijana walioko vyuoni wataona maandishi ukutani na wengi wao watageukia njia ya kweli ya kiroho-njia pekee kwa Marekani kuepuka janga ambalo litaletwa na ubaguzi wa rangi.

‘Kamwe sijawahi heshimiwa namna hii. Wala sijawahi nyenyekezwa na kufanywa nihisi sistahili. Nani ataamini Baraka zilizojazwa kwa mtu mweusi wa Marekani? Siku chache zilizopita, mtu ambaye Marekani angeitwa ‘mzungu’,mwanadiplomasia wa Umoja wa Mataifa, balozi, mwambata wa Wafalme-alinipatia makazi yake ya hotelini, kitanda chake. Kupitia mtu huyu, Mtukufu Mwanamfalme Faisal, mtawala na nchi hii Takatifu, alijulishwa uwepo wangu katika mji wa Jedda. Asubuhi iliyofuata, mwana wa Mwanamfalme Faisal mwenyewe, alinijulisha kuwa kwa mapenzi ya baba yake, nitakuwa mgeni wa kitaifa.

‘Makamu mkuu wa protokali, alinichukua yeye mwenyewe kwenda mahakama ya Hajj. Mtukufu Sheikh Muhammad Harkon mwenyewe ndiye aliyeniruhusu kwenda Mecca na kunipatia vitabu viwili vya Kiislamu, vikiwa na muhuri wake binafsi na sahihi yake, na kuniambia kuwa anasali ili niwe mhubiri wa Uislamu mwenye mafanikio katika Marekani. Nimepewa gari, dereva na muongozaji na hivyo kuniwezesha kusafiri katika nchi hii Takatifu nipendavyo. Serikali imenipatia makazi yeye kiyoyozi na wahudumu katika kila mji niliotembelea. Kamwe sijawahi ota kuwa nitakuja pokea heshima kubwa namna hii-heshima ambayo Marekani hutolewa kwa Wafalme, si kwa mtu mweusi.

‘Sifa zote zimuendee Allah, Bwana wa Ulimwengu wote. “Wako Muaminifu,” El-Hajj Malik El-Shabazz “(Malcom

X)”

Mwisho wa sura ya 17​
 
Sura ya 18
El-HAJJ MALIK EL-SHABAZZ
Mwanamfalme Faisal, mtawala wa Arabia alinifanya kuwa mgeni wa kitaifa. Hadhi hii iliambatana na huduma nyingi, moja ambayo niliifurahia na kuitumia bila kujivunga ilikuwa ni usafiri wa gari, gari ilinitembeza maeneo mbalimbali ya mji wa Mecca huku muongozaji akinionyesha maeneo mbalimbali ya muhimu. Baadhi ya maeneo ya Mji Mtakatifu yalionekana kuwa ni ya kale sana na mengine yalikuwa ya kisasa kama vile upo vitongoji vya Miami. Siwezi kuelezea hisia nilizopata pale nilipoweka mkono wangu kwenye ardhi ambayo manabii wakubwa waliikanyaga miaka elfu nne iliyopita.

Jina “Muislamu kutoka Marekani” lilizua udadisi wa watu kote nilikoenda. Mara kadhaa nilidhaniwa kuwa ni Cassius Clay. Gazeti moja lilichapisha picha yangu na Cassius Clay tukiwa Umoja wa Mataifa. Kupitia kwa dereva-muongozaji na mtafsiri wangu, niliulizwa maswali mengi kuhusu Cassius. Kwenye ulimwengu wa Kiislamu hata watoto walimfahamu na kumpenda. Cinema kotekote Afrika na Asia zilikuwa zimeonyesha pambano lake. Katika siku hizo za mwanzo za kazi yake, Cassius alikuwa ameteka nyoyo za dunia yote ya watu wasio weupe.

Gari ilinichukua kwenda kushiriki maombi maalumu kwenye mlima Arafat na Mina. Barabarani kulikuwa na vurugu ambazo sijawahi ona, msongamano wa kutisha, breki na matairi yakipiga kelele na honi zikilia (Naamini uendeshaji magari wote katika Mji Mtakatifu unafanyika kwa jina la Allah.) Nilikuwa nimeishaanza kujifunza sala kwa kiarabu, lakini jambo lililokuwa gumu kwangu ni mikao ya sala. Mikao ile ambayo sikuizoea ilisababisha kidole gumba changu cha mguu kivimbe na kuuma.

Lakini mila za ulimwengu wa Kiislamu nilikuwa nimeishazizoea. Mkono wangu ulikuwa upo tayari kuchota chakula kutoka kwenye chombo ambacho tulishirikiana na ndugu wengine wa Kiislamu; nilikunywa kutoka kwenye kikombe tulichoshirikiana na wengine bila kusita; nilinawa kutoka kwenye jagi moja; na kulala zuliani kwenye sehemu ya wazi na watu wengine nane hadi kumi. Nakumbuka usiku mmoja huko Muzdalifa, nilijilaza nikitazama anga katikati ya ndugu wa Kiislamu waliokuwa wamelala usingizi, nilitambua kuwa mahujaji wa rangi, vyeo, hadhi na kazi tofauti wote walikoroma kwa lugha moja.

Ninadhani kuwa kwenye baadhi maeneo ya Nchi Takatifu niliyotembelea, mamilioni ya chupa za vinywaji yalinywewa- na sigara milioni kumi zitakuwa zilivutwa. Waislamu, hasa Waarabu, walivuta sigara karibu muda wote, hata wanapokuwa kwenye hija ya Hajj. Jambo ovu la uvutaji wa sigara halikuwepo enzi za Mtume Muhammad-kama lingekuwepo ninaamini kuwa angelipiga marufuku.

Baadaye nilikuja kuambiwa kuwa Hajj ya mwaka ule ilikuwa ndiyo kubwa kuliko zote katika historia. Kasem Gulek kutoka bunge la Uturuki, kwa majivuno, aliniambia kuwa Uturuki peke yake kulitoka mabasi zaidi ya mia sita na zaidi ya mahujaji elfu hamsini walifanya hija. Nilimwambia kuwa ninaota siku ambayo meli na ndege zilizojaa Waislamu wa Marekani zikija Mecca kwa ajili ya Hajj.
Kulikuwa na watu wa kila rangi kwenye umati. Mara tu nilipoliona hilo, nilianza kulichunguza kwa umakini zaidi. Kuwa kwangu Mmarekani kulifanya niwe mtu wa kutilia maanani sana rangi za watu. Niliona kuwa watu waliofanana walitembea pamoja. Hili lilifanyika kwa hiari yao wenyewe; hakukuwa na sababu nyingine nyuma yake. Waafrika walikuwa na Waafrika wenzao, Wapakistani na wapakistani wenzao nk. Niliweka akilini kuwa nitakaporudi nyumbani, nitawaambia Wamarekani juu ya jambo hili; kuwa mahali ambapo kuna undugu wa kweli kati ya watu wa rangi zote, ambapo hakuna anayehisi kubaguliwa, mahali ambapo hakuna anayejiona bora wala anayejiona duni-hapo ndipo watu wanaofanana huja pamoja kwa hiari yao wenyewe, huvutwa na kule kufanana kwao.
Nia yangu ni kuwa kwenye hija inayofuata niwe tayari nafahamu lugha ya Kiarabu kwa kiasi. Katika ujinga wangu wote nilikuwa na bahati ya kupata marafiki wavumilivu walioniruhusu niongee kupitia mtafsiri. Kamwe maishani mwangu sijawahi kujihisi kiziwi na mjinga kama wakati ambao hakukuwa na mtafsiri wa kuniambia kinachoongelewa na Waislamu wengine kabla hawajafahamu kuwa “Muislamu kutoka Marekani” anafahamu sala chache tu kwa Kiarabu, zaidi ya hapo alitikisa kichwa na kutabasamu tu.

Lakini nyuma ya tabasamu langu na kutikisa kichwa nilikuwa natafakari. Niliona kuwa usilimuji wa watu unaweza kuongezeka mara mbili hadi mara tatu iwapo undugu unaokuwepo wakati wa hija ungetangazwa na kujulishwa kwa watu wa nje. Niliona kuwa Waarabu si wazuri katika kutambua saikolojia ya watu wasio Waarabu, na umuhimu wa mahusiano na umma. Waarabu walisema “insha Allah”(“Mungu akipenda”) na kisha wakaaa kusubiria watu wasilimu. Lakini hata kwa njia hii bado Uislamu ulikuwa unakua kwa kasi, lakini nilifahamu kuwa kwa kuboresha mahusiano ya umma, watu wapya wanaosilimu wangeweza kufikia mamilioni.

Kila nilikokwenda, muda wote nilikuwa nikiulizwa maswali juu ya ubaguzi wa rangi unaoendelea Marekani. Pamoja na historia ya maisha yangu, lakini nilishangazwa sana kuwa sifa kuu ya Marekani ilikuwa ni ubaguzi wa rangi.
Kwenye mamia ya mazungumzo niliyofanya na Waislamu kwenye nchi Takatifu, wenye vyeo na wadogo, na kutoka kote duniani-na baadaye nilivyokwenda nchi za Waafrika weusi, sikujivunga hata mara moja au kuacha nafasi ipite hata mara moja bila ya kueleza ukweli kuhusu uhalifu, uovu na udhalilishaji unaowakumba watu weusi wa Marekani. Kupitia mtafsiri wangu-sikupoteza hata nafasi moja madhira halisi yanayowakabili watu weusi wa Marekani. Nilihubiri hilo kwenye mlima Arafat, nililihubiri kwenye ukumbi wa mapokezi wa hoteli ya Jedda Palace. Niliwanyooshea vidole mmoja baada ya mwingine ili wanielewe vizuri; “Wewe . . . wewe . . . sababu ya rangi yako yenye weusi, ungekuwa Marekani nawe pia ungeitwa ‘Negro.’ Ungeweza pigwa mabomu, pigwa risasi, au kupigwa na maji yenye presha na kupigwa ngumi na mateke sababu tu ya rangi yako.”

Kama ambavyo mahujaji masikini walivyonisikia, ndivyo mahujaji ambao ni watu wakubwa walivyonisikia. Niliongea kwa kirefu na Hussein Amini, Mufti Mkuu wa Jerusalem-mtu mwenye macho ya bluu na nywele za rangi ya dhahabu. Tulitambulishwa na mbunge kutoka uturuki, Kasem Gulick, tulipokuwa kwenye mlima Arafat. Wote walikuwa ni watu wenye elimu; wote walisoma vizuri mambo yahusuyo Marekani. Kasem Gulick aliniuliza kwa nini nimetengana na Elijah Muhammad. Nilimwambia kuwa nilipendelea kutoelezea tofauti zetu ili kuendelea kulinda umoja wa watu weusi wa Marekani. Wote walielewa na kukubaliana na hilo.

Nilizungumza na Meya wa Mecca, Sheikh Abdullah Eraif, mtu ambaye wakati alipokuwa muandishi wa habari alikuwa ameshutumu uendeshwaji wa Manispaa ya Mecca. Mwanamfalme Faisal alimfanya kuwa Meya ili kuona kama anaweza kufanya vizuri zaidi. Watu wengi walikubali kuwa Sheikh Eraif alikuwa akifanya kazi nzuri. Kipindi cha televisheni kilichoitwa “Muislamu kutoka Marekani” kilitengenezwa na Ahmed Horyallah na mwenzake Essid Muhammad wa kutoka kituo cha televisheni cha Tunis.

Wakati fulani huko Chicago, Ahmed Horyallah alimfanyia Elijah Muhammad mahojiano.
Ukumbi wa mapokezi wa hoteli ya Jedda Palace iliniwezesha kuongea na watu wengi mashuhuri kutoka nchi mbalimbali waliokuwa na hamu ya kumsikia “Muislamu wa Marekani.” Nilikutana na Waafrika wengi ambao wamewahi kuishi Marekani au kusikia ushuhuda kutoka kwa Waafrika wenzao juu ya jinsi ambavyo Marekani ilikuwa ikiwatendea watu weusi. Nakumbuka wakati fulani waziri mmoja kutoka nchi za Waafrika weusi(alifahamu mambo yanayoendelea duniani kuliko mtu mwingine yeyote niliyewahi kukutana naye) alinisimulia juu ya safari zake za mara kwa mara za kwenda Marekani, kote, Marekani kusini na kaskazini, na kwa makusudi kabisa akiacha kuvaa mavazi ya kitamaduni ya nchini kwake. Kukumbuka tu udhalilishaji aliokutana nao kama mtu mweusi kulionekana kuamsha hisia kali kwa afisa huyu mkubwa. Macho yake yalikuwa mekundu kwa hasira, mkono wake ukipiga hewani. “Kwa nini mtu mweusi wa Marekani anaridhika na kukandamizwa? Kwa nini mtu mweusi wa Marekani hapiganii haki yake ya kuwa binadamu?”

Afisa mmoja wa ngazi za juu kutoka Sudan alinikumbatia na kusema, “Wewe ni shujaa wa watu weusi!” afisa mmoja kutoka India alilia kwa uchungu akisema, “Kwa ajili ya ndugu zangu katika nchi yenu.” Mara nyingi sana nimetafakari jinsi ambavyo mtu mweusi wa Marekani alivyochotwa akili kabisa ili asione wala kujifikiria mwenyewe kwa namna inayotakiwa, yaani kama mmoja wa watu wa duniani wasio wazungu. Mtu mweusi wa Marekani hafahamu juu ya mamia ya mamilioni ya watu wengine wasio wazungu wanavyomjali: hafahamu juu ya hisia zao za kindugu walizonazo juu yake.

Ilikuwa ni kule kwenye Nchi Takatifu na baadaye katika Afrika ndiko nilikofikia hitimisho ambalo naliamini hadi leo- kwamba takwa la kwanza kwa kiongozi yeyote wa watu weusi ndani ya Marekani linatakiwa kuwa kusafiri vya kutosha kwenda kwenye nchi za wasio wazungu, na safari hizo zinatakiwa kuhusisha vikao vingi na watu wakubwa wa nchi hizo. Nina hakika kuwa kiongozi yeyote wa kweli wa watu weusi na aliye tayari kujifunza atarudi nyumbani akiwa na fikra bora zaidi juu ya njia za kutatua tatizo linalomkabili mtu mweusi wa Marekani. Na zaidi ya yote, viongozi hao watagundua kuwa viongozi wengi wakubwa wa huko, hasa wa kutoka Afrika watawaambia-kwa faragha kuwa watapenda kutoa msaada wao kusaidia harakati za mtu mweusi huko Umoja wa Mataifa na kwa njia nyingine pia. Lakini viongozi hawa wanafahamu vyema kuwa mtu mweusi wa Marekani hajielewi na amegawanyika kiasi kwamba yeye mwenyewe hafahamu harakati zake zinahusu nini. Ni Waafrika ndiyo walioniambia kuwa hakuna anayetaka kuabika kwa kumsaidia ndugu ambaye haonyeshi kama anataka msaada huo-na ambaye anaonekana kukataa kutoa ushirikiano kwa jambo lenye maslahi kwake mwenyewe.
Tatizo kubwa la “viongozi” wa watu weusi wa Marekani ni kukosa maono! Namna yake ya kufikiri na mbinu zake(kama anazo) zimeishia pale aliposhauriwa au aliporuhusiwa na mzungu. Na kitu cha kwanza ambacho utawala wa Marekani hautaki ni kwa mtu mweusi kuanza kufikiri kimataifa.

Nafikiri kosa baya kabisa lililofanywa na taasisi za watu weusi wa Marekani na viongozi wao ni kushindwa kujenga mahusiano ya kindugu kati ya watu weusi wa Marekani na nchi huru za Afrika. Inatakiwa kila siku viongozi wa mataifa ya weusi ya Afrika wawe wanapokea taarifa ya yale yanayoendelea kwenye harakati za mtu mweusi wa Marekani-badala yake, Idara ya Taifa ya Marekani ndiyo inawapatia Waafrika taarifa, taarifa ambazo zinaonyesha kuwa matatizo yanayowakumba watu weusi wa Marekani yameshapatiwa ufumbuzi.

Waandishi wawili wa kimarekani ambao vitabu vyao vimeuza sana katika Nchi Takatifu wamesaidia sana kujulisha watu juu ya hali ya mtu mweusi wa Marekani. Kitabu cha James Baldwin kilichotafsiriwa kimekuwa na matokeo makubwa sana, kama tu kiitabu Black Like Me chake John Grin. Kama hukifahamu kitabu hicho-kinaelezea kisa cha Grin, mzungu, alivyojidai mtu mweusi na kusafiri sehemu mbalimbali za Marekani kama mtu mweusi kwa muda wa miezi miwili; baada ya safari hizo akaandika kuhusu mambo yaliyompata. “Mambo ya kuogofya kabisa!” nilisikia mara nyingi watu waliosoma kitabu hicho maarufu wakisema kule kwenye Nchi Takatifu. Lakini kila niliposikia hilo, nilijaribu kufunua fikra zao zaidi, “Kama yalikuwa mambo ya kuogofya kwake aliyejidai mtu mweusi kwa muda wa siku sitini tu, hebu fikiria waliyopitia watu weusi halisi wa Marekani kwa muda wa miaka mia nne.”
Jambo moja la heshima ambalo nilikuwa nimesali linikute lilikuwa ni kualikwa kuonana ana kwa ana na Mtukufu Mwanamfalme Faisal.

Sitasahau fikra nilizokuwa nazo wakati nilipokuwa ninaingia ofisini kwake, kwamba mbele yangu alikuwepo mmoja wa watu muhimu zaidi duniani, lakini pamoja na heshima yote aliyokuwa nayo, mtu aliweza kuona unyenyekevu wake wa kweli. Nilipoingia, Mwanamfalme Faisal, mrefu na nadhifu, aliinuka kunikaribisha. Alinielekeza kuketi kwenye kiti kilichoangaliana na chake. Mtafsiri wetu alikuwa ni makamu mkuu wa protokali, Muhammad Abdul Azziz Maged, Mwarabu mzaliwa wa Misri ambaye kwa muonekano alikuwa kama mnegro wa Harlem.

Mwanamfalme Faisal alinikatisha mara moja pale nilipoanza kujiumauma nikijaribu kutoa shukrani zangu kwa kunifanya kuwa mgeni wa kitaifa. Alisema kuwa ulikuwa ni ukarimu tu ambao Muislamu mmoja alimfanyie mwingine, na kuwa mimi kuwa Muislamu kutoka Marekani halikuwa jambo la kawaida. Aliniomba nielewe kuwa yote aliyofanya ni kwa sababu alipenda kufanya, hakukuwa na lengo lingine.

Mwanamfalme Faisal alipokuwa anaongea, mhudumu alituandalia aina mbili ya chai maalumu. Mwana wake, Muhammad Faisal alikuwa ameniona kwenye vituo vya televisheni vya Marekani alipokuwa akisoma chuo kikuu cha Northern California. Mwanamfalme Faisal alikuwa amesoma magazeti ya Misri kuhusu “Waislamu wa Marekani.” Kama wanachosema waandishi hao ni kweli, basi Waislamu weusi wa Marekani wana Uislamu usio sahihi,” alisema. Nilieleza nafasi yangu katika kuratibu na kujenga Taifa la Kiislamu kwa miaka kumi na mbili iliyopita. Nilisema kuwa lengo langu la kufanya Hija lilikuwa ni kuuelewa Uislamu wa kweli.

“Hilo ni jambo zuri,” alisema Mwanamfalme Faisal na kueleza kuwa kulikuwa kuna machapisho mengi yanayoelezea Uislamu katika lugha ya Kiingereza-hivyo hakukuwa na sababu ya msingi ya kutoufahamu, na hakuna sababu kwa watu wanaotaka wanaotaka kujua kweli kupotoshwa.

***

Mwezi wa nne mwaka jana, 1964, nilisafiri kwenda Beirut, mji mkuu wenye bandari wa Lebanon. Kuna sehemu yangu nilikuwa nimeiacha kwenye Mji Mtakatifu wa Mecca, na kwa kufanya hivyo nikawa nimeondoka na sehemu fulani ya Mecca.
Nilikuwa safarini kwenda Ghana na Nigeria. Lakini rafiki fulani niliokutana nao kwenye Nchi Takatifu walikuwa wamenisisitiza nipite sehemu kadhaa nami nikakubali. Kwa mfano, ilipangwa kuwa kituo cha kwanza nipitie na kuhutubia wahadhiri na wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Beirut. Kwenye hoteli ya Beirut Palm Beach nililala mustarehe kwa mara ya kwanza toka nitoke Marekani. Kisha nikatoka kwenda matembezini. Nikiwa tu nimetoka Nchi Takatifu- mara moja tabia na mavazi ya wanawake wa Lebanon​

yalishtua akili yangu. Kwenye Nchi Takatifu kulikuwa na wanawake wa kiarabu waliovalia kwa staha sana-lakini hapa ghafla kuna wanawake; nusu Wafaransa na nusu Waarabu wa Lebanon ambao kwa mavazi yao walionyesha mtazamo wao wa kuwa huru na kujiamini zaidi katika kujiamulia mambo. Niliona wazi athari za Ulaya kwenye utamaduni wa Lebanon. Ilinionyesha jinsi ambavyo maadili ya nchi yanaweza kupimwa kwa haraka kwa kuangalia tabia na mavazi ya wanawake wao wanapokuwa nje, hasa wanawake vijana. Sehemu yoyote ambayo thamani ya mambo ya kiroho imeshushwa kama siyo kutoweka kwa kupenda mambo ya kimwili, mara zote hilo hujionyesha kwa wanawake. Angalia wanawake wa Marekani-wakubwa kwa wadogo-mahali ambapo hakuna maadili yoyote yaliyobakia. Inaonekana nchi zingine nazo ziko zimeegemeo upande mmoja au mwingine. Ukweli ni kuwa tunaweza kuwa na paradiso iwapo mambo ya kimwili nay a kiroho yatafanywa kwa uwiano mzuri.

Niliongea kwenye Chuo Kikuu cha Beirut kuhusu hali halisi ya mtu mweusi wa Marekani. Huko nyuma nilisema kuwa mzungumzaji mwenye uzoefu anaweza kuhisi muitikio wa wasikilizaji wake. Nilipokuwa ninaongea, niliweza kuhisi kujitetea kutoka kwa wanafunzi wazungu wa Kimarekani waliohudhuria-lakini upinzani wao ulipungua polepole kadri nilivyoendelea kumwaga ukweli ulio wazi. Siwezi kuelezea wala kusahau jinsi wanafunzi kutoka Afrika walivyoonyesha hisia zao.

Baadaye, kwa mshangao nilisikia kuwa magazeti ya Marekani yalikuwa yameandika kuwa hotuba yangu ya Beirut ilikuwa imesababisha “vurugu.” Vurugu gani? Sifahamu ni jinsi gani mwandishi wa habari mwenye dhamira njema anaweza kutuma taarifa kama hiyo. Gazeti la Beirut, Daily Star liliandika kuhusu hotuba yangu kwenye kurasa ya mbele, lakini halikuandika habari yoyote kuhusu vurugu-sababu hazikutokea. Nilipomaliza hotuba yangu, wanafunzi karibu wote kutoka Afrika walinizingira wakitaka saini yangu; kuna baadhi walinikumbatia. Hata wasikilizaji weusi wa Marekani hawajawahi kunikubali kama Waafrika wale wanyenyekevu na wenye kuonyesha hisia zao waziwazi.
Kutoka Beirut nilipanda ndege hadi Cairo, huko nilipanda treni hadi Alexandria. Nilipiga picha kwa kamera yangu kila kituo. Nilipofika nikachukua ndege kwenda Nigeria.

Kwenye safari hiyo ya saa sita, nilipokuwa sizungumzi na rubani(ambaye alikuwa muogeleaji kwenye mashindano ya olimpiki ya mwaka 1960), niliketi na mwanasiasa mmoja wa Afrika. Alikuwa karibu kupiga kelele kwa hamasa “watu wanapokuwa katika hali ya mkwamo na wanatolewa wanatolewa, kunakuwa hakuna muda wa kupiga kura.” Wazo lake ni kuwa hakuna nchi mpya ya Kiafrika inayotaka kuondoa athari za ukoloni kisha ikaweka mfumo wa kisiasa unaoruhusu migawanyiko na mabishano. “Watu hawajui kura zinamaanisha nini! Ni jukumu la viongozi walioelimika kuwatoa watu wao kutoka kwenye ujinga.”

Nilipofika Lagos, nilipokelewa na Profesa Essien-Udom kutoka Chuo Kikuu cha Ibadan. Sote tulifurahi sana kuonana. Tulikuwa tumekutana kwa mara ya kwanza nchini Marekani alipokuwa akifanya utafiti wa kitabu chake, Black Nationalism. Jioni hiyo mlo wa jioni uliandaliwa kwa heshima yangu, ulihudhuriwa na maprofesa na wataalamu wengine. Tulipokuwa tunakula, daktari mmoja kijana aliniuliza iwapo ninafahamu kuwa magazeti ya New York yalichukizwa sana kwa mauji ya mwanamke wa kizungu yaliyotokea huko Harlem hivi karibuni, na kulingana na magazeti hayo, watu wengi walikuwa wananilaumu mimi kwa namna fulani. Wanandoa fulani wazee wa kizungu walikuwa wameshambuliwa na vijana kadhaa weusi, na mwanamke alikuwa amechomwa visu hadi kufa. Baadhi ya vijana hao walikamatwa na polisi, na katika kuhojiwa walisema kuwa wao ni washiriki wa taasisi iitwayo “Blood Brothers.”(Ndugu wa damu) Vijana hao walisema, au waligusia kuwa wanauhusiano na “Waislamu Weusi” ambao walijitenga na Taifa la Kiislamu na kuungana nami.

Nilimwambia wageni kuwa ndiyo mara ya kwanza kusikia kisa hicho, lakini kuwa sikushangazwa kwa kwa matendo ya ukatili kutokea kwenye eneo lolote la maghetto ndani ya Marekani, mahali ambako watu weusi waliishi kama wanyama au watu wenye ukoma. Nilisema kuwa shutuma dhidi yangu ni mbinu ya kawaida ya mzungu kutafuta mbuzi wa kafara-kwamba kila mara kwenye maeneo ya watu weusi kinapotokea kitu ambacho wazungu hawakipendi, basi macho ya wazungu hayakuelekezwa kwenye kiini cha tatizo bali kwa mbuzi wa kafara.
Na kuhusu “Ndugu wa damu,” nilisema kuwa niliwachukulia watu weusi wote kuwa ndugu zangu wa damu. Nilisema kuwa jitihada za mzungu kuchafua jina langu zimefanikiwa kwa kufanya mamilioni ya watu weusi kunichukulia kama Joe Louis.

Kwenye hotuba yangu ndani ya ukumbi wa Trenchard, katika Chuo Kikuu cha Ibadan, nilisema kuwa nchi huru za Afrika zinatakiwa kuona umuhimu wa kusaidia kupeleka suala la watu weusi wa Marekani mbele ya Umoja wa Mataifa. Nilisema kama tu ambavyo Wayahudi wa Marekani wanavyoshirikiana kisiasa, kiuchumi na kitamaduni na Wayahudi wengine duniani, ninaamini sasa ni wakati wa watu weusi wa Marekani kuungana na umoja wa watu wenye asili ya Afrika duniani. Nilisema kuwa kimwili, Wamarekani weusi tutabaki Marekani tukipigania haki zetu za kikatiba, lakini kifalsafa na kitamaduni, Wamarekani weusi tunahitaji sana “kurudi” Afrika, na kuunda kitu kimoja juu ya nguzo ya umoja wa watu wenye asili ya Afrika.

Vijana wa Kiafrika waliniuliza maswali ya kisiasa yenye akili kuliko mtu anayoweza kuyasikia kutoka kwa watu wazima wa Marekani. Kisha likatokea jambo la kushangaza baada ya mzee mmoja mwenye asili ya visiwa vya Karibeani kusimama na kuanza kunishutumu kuwa nilikuwa nikiishambulia Marekani. “Kaa kimya! Kaa Kimya!” wanafunzi walipiga kulele huku wakizomea. Mtu yule alijaribu kubishana nao, lakini ghafla kundi la wanafunzi lilimrukia na kuanza kumkimbiza. Aliponea chupuchupu. Sijawahi ona kitu kama kile. Walimpigia kelele na kumtoa nje ya eneo la chuo. (Baadaye nilikuja kufahamu kuwa mtu yule alikuwa ameoa mwanamke wa kizungu, na alikuwa akijaribu kupata kazi kutoka shirika fulani la wazungu na ndilo lililompa kazi ya kunipinga. Hapo nikawa nimeelewa tatizo lake.)
Hii haikuwa mara yangu ya mwisho kushuhudia Waafrika wakionyesha unazi wa kisiasa.

Baadaye kwenye mkutano na umoja wa wanafunzi, niliulizwa maswali mengi na kufanywa kuwa mwanachama wa heshima wa chama cha Wanafunzi wa Kiislamu wa Nigeria. Ninayo kadi ya uwanachama hapa kwenye pochi yangu: “Alhadji Malcom X. Namba ya usajili M-138.” Baada ya kuwa mwanachama nilipewa na jina jipya: “Omowale.” Kwa lugha ya Kiyoruba linamaanisha, “Mwana aliyerejea nyumbani.” Sikudanganya nilipowaambiwa kuwa sijawahi pokea heshima yeye thamani kama ile.

Nigeria kulikuwa na washiriki wa Peace Corps mia sita, nilikuja kufahamu kuwa baadhi ya wana-peace corps wazungu nilioongea nao walijisikia aibu kwa yale yanayofanywa na wazungu wenzao ndani ya Marekani. Kati ya wana-peace corps ishirini weusi nilioongea nao, aliyenivutia zaidi alikuwa ni Larry Jackson, mhitimu wa chuo cha Morgan. Alikuwa mwenyeji wa Fort Lauderdale, Florida. Alijiunga na Peace Corps mwaka 1962.

Nilitembelea vituo vya radio na televisheni vya Nigeria. Ninapokumbuka kuona watu weusi wakiendesha vyombo vyao vya habari wao wenyewe najawa na hisia kali. Mmoja ya waandishi wa habari walionihoji alikuwa ni Mmarekani mmoja mweusi kutoka jarida la Newsweek-jina lake lilikuwa William. Alikuwa anasafiri sehemu mbalimbali za Afrika, hivi karibuni alikuwa amemhoji Waziri mkuu wa Ghana, Kwameh Nkrumah.

Tulipokuwa faragha, kikundi fulani cha maafisa wa Nigeria kiliniambia jinsi ambavyo idara ya habari ya Marekani ilikuwa ikijitahidi kuwasambazia Waafrika habari kuwa watu weusi wa Marekani walikuwa wanapiga hatua vizuri sana, na kuwa tatizo la ubaguzi wa rangi litatatuliwa hivi karibuni. Afisa mmoja mkubwa aliniambia, “Viongozi wetu na watu wengine wengi wanaelewa kuwa mambo ni kinyume chake.” Aliongeza kuwa wanadiplomasia wa Afrika katika Umoja wa Mataifa walielewa kuwa mzungu alikuwa amepanga hila za kuwatenganisha watu wenye asili ya Afrika.

“Nchini kwako ni watu wangapi wanafahamu kuwa Amerika ya Kaskazini, Kati na Kusini ina watu milioni themanini wenye asili ya Afrika?” aliniuliza.
“Hakuna shaka kuwa dunia itabadilika siku ambayo watu wenye asili ya Afrika watakuja pamoja kama ndugu!”
Sikuwahi kusikia mtazamo huo wa kumfikiria mtu mweusi kidunia kutoka kwa Mmarekani mweusi yeyote.
Kutoka Lagos, Nigeria, nilipanda ndege hadi Accra, Ghana.

Nadhani katika bara la Afrika hakuna nchi tajiri na yenye watu wenye uzuri wa asili kama Ghana, nchi ambayo inajivuna kuwa kisima cha Umoja wa Waafrika.

Nilishuka kwenye ndege na kupokelewa na mshtuko. Kuna mzungu wa Marekani alikuwa amenitambua; alikuwa na ujasiri wa kunifuata na kuniambia kuwa alitokea Alabama, na kunialika nyumbani kwake kwa chakula cha jioni!
Kwenye chumba cha chakula cha hoteli niliyofikia kulijaa wazungu waliokuwa wakiongelea utajiri wa Afrika ambao haujatumiwa bado, kama vile wale wahudumu Wakiafrika walikuwa hawana masikio. Hilo karibu liniharibie mlo wangu-kufikiri jinsi ambavyo katika Marekani waliwafungulia mbwa wa polisi wawashambulie watu weusi, na kurusha mabomu kwenye makanisa ya watu weusi huku wakifunga milango ya makanisa yao ili watu weusi wasiingie- na sasa kwa mara nyingine mzungu huyohuyo yupo nchi ambayo babu zake waliwaiba watu weusi na kuwafanya watumwa.

Palepale kwenye kifungua kinywa niliazimia kichwani mwangu kuwa, katika siku nitakazokuwepo Afrika, nitahakikisha nafanya maisha ya mzungu yule anayekenua na kutaka kuinyonya Afrika kwa mara nyingine kuwa magumu sana-mara ya kwanza alinyonya utajiri wake wa watu, sasa anataka utajiri wake wa madini.

Nilifahamu vyema kuwa mtazamo wangu haukupingana na ule wa kindugu nilioupata kwenye Nchi Takatifu. Waislamu wenye muonekano wa “kizungu” ambao walibadili mtazamo wangu walikuwa ni watu walionionyesha kuwa walikuwa na undugu wa kweli. Na nilifahamu vyema kuwa ni vigumu sana kumpata mzungu wa Marekani mwenye undugu wa kweli na watu weusi, haijalishi anakenua namna gani.

Muandishi Julian Mayfield alionekana kuwa ndiye kiongozi wa kikundi kidogo cha Wamarekani weusi walioishi Ghana. Nilimpigia simu Mayfield, kufumba na kufumbua nikawa nimekaa nyumbani kwake nikiwa nimezungukwa na Wamarekani weusi kama arobaini hivi; walikuwa wakisubiri ujio wangu. Kulikuwa na wafanyabiashara na watu wenye taaluma mbalimbali, kama wanandoa na wanaharakati kutoka Brookyln, Dr Roberts E. Lee na mkewe, wote wakiwa ni madaktari wa meno ambao wamekana uraia wao wa Marekani. Wengine walikuwa Alice Windom, Maya Angelou Make, Victoria Garvin na Leslie Lacy-walikuwa wameunda “Kamati ya Malcom X” ambayo kazi yake ilikuwa kuniongoza kwenye ratiba waliyonipangia.

Hapa kwenye mkoba wangu kuna baadhi ya habari zilizoandikwa kwenye magazeti ya Afrika baada ya kufahamu kuwa nilikuwa natembelea nchi za Afrika.

“Jina la Malcom X ni maarufu kwa watu wa Ghana kama ilivyo kwa mbwa, maji yenye presha, fimbo na sura zenye chuki za wazungu wa kusini ya Marekani. . . .” “Uamuzi wa Malcom X kuingia kwenye harakati za watu wote unatoa ishara mpya ya matumaini kwenye mapambano ya amani ambayo ni ya kinyonge na yanayosuasua ”

“Jambo la muhimu kabisa ni kuwa Malcom X ni kiongozi wa kwanza wa Wamarekani weusi anayejulikana kitaifa kufanya ziara ya Afrika tokea Dr. Du Bois alipokuja Ghana. Pengine huu ni mwanzo mpya wa harakati zetu. Acha tusidharau jambo hili kama ambavyo serikali inafanya.”

Na jambo jingine: “Malcom X ni mmoja ya viongozi wetu muhimu sana ambao tuko nao katika mapambano. Jitihada zitafanyika ili kumchafua na kufanya aonekane hana maana. . . .”

Sikuamini hata kidogo aina hii ya mapokezi niliyopata maili elfu tano kutoka Marekani! Maafisa kutoka vyombo vya habari walifanya mipango ya kulipia gharama zangu za hoteli, na hawakutaka kusikia hata kidogo nikipinga hilo. Maafisa hao walitia ndani T. D. Baffoe, mhariri mkuu wa gazeti la Ghananian Times; G. T. Anim, mkurugenzi mkuu wa Idara ya habari ya Ghana; Kofi Batsa, mhariri wa Spark na katibu mkuu wa chama cha waandishi wa habari wa Kiafrika; bwana Cameron Duodu; na wengineo. Sikuwa na kingine zaidi ya kuwashukuru. Wakati wa mlo mzuri ulioandaliwa na Ana Livia, mke mrembo mwenye asili ya Puerto Rica wa bwana Julian Mayfield(Ana Livia alikuwa ndiye msimamizi wa mpango wa afya wa wilaya ya Accra)-niliulizwa maswali mengi na watu weusi wale wenye shauku, watu waliotoka Marekani na kurudi kwenye bara lao la asili.

Natamani kila Mmarekani angeshiriki kuona, kusikia na kuhisi pamoja nami yale yaliyonitokea kule Ghana. Na lengo la kusema hivyo si kuzungumzia mapokezi niliyopokea nikiwa kama mtu ambaye tayari walikuwa wameisha msikia, bali mapokezi niliyopata nikiwa kama alama ya wanaharakati weusi wa Marekani.

Kwenye mkutano uliojaa niliofanya na klabu ya waandishi wa habari, nakumbuka swali la kwanza kuulizwa lilikuwa ni kwa nini nilitengana na Elijah Muhammad na Taifa la Kiislamu. Waafrika walikuwa wamesikia tetesi kuwa Elijah Muhammad alikuwa amejijengea jumba la anasa huko Arizona. Nilirekebisha uzushi huo na kuepuka kutoa shutuma zozote. Nilisema kuwa kutokubaliana kwetu kulikuwa juu ya muelekeo wetu wa kisiasa na ushiriki wetu kwenye harakati za kupigania haki za binadamu nje ya dini. Nilisema kuwa nililiheshimu Taifa la Kiislamu likiwa kama chanzo cha mabadiliko ya kisaikolojia, kimaadili na kijamii, na kuwa ushawishi wa Elijah Muhammad kwa mtu mweusi wa Marekani ulikuwa ni wenye manufaa.

Nilivisisitiza vyombo vya habari juu ya umuhimu wa uwepo wa mawasiliano na kusaidiana kati ya Waafrika na Wamarekani wenye asili ya Afrika, watu ambao mapambano yao yanafanana. Nakumbuka kuwa kwenye mkutano huo nilitumia neno “Negro,” na nikasahihishwa mara moja. “Hilo neno halikubaliki hapa bwana Malcom X. Jina Wamarekani wenye asili ya Afrika ni la heshima na lenye maana zaidi.” Niliomba radhi mara moja. Sidhani kama nilitamka neno “Negro” tena kwa muda wote niliokuwepo Afrika. Nilisema kuwa Wamarekani wenye asili ya Afrika milioni ishirini na mbili wanaweza kuwa na mchango mkubwa kwa Afrika-wakati huo huo mataifa ya Kiafrika yanaweza na yanatakiwa kutoa mchango wao katika kupambana na ubaguzi wa rangi unaoendelea Marekani. Nilisema kuwa ‘Afrika yote imeungana kupinga ubaguzi wa rangi unaofanyika huko Afrika Kusini na kwenye makoloni ya Ureno. Lakini mnapoteza muda wenu kama hamtatambua kuwa Verwoerd, Salazar, Uingereza na Ufaransa hawawezi kudumu hata siku moja bila ya msaada wa Marekani. Kwa hiyo basi, mpaka pale mtakapomuumbua mtu wa Washington, D.C., hamtakuwa mmefanya chochote kile.’

Nilifahamu kuwa G. Mennen Williams, kutoka Idara ya Taifa alikuwa anatembelea Afrika wakati huo kwa ziara rasmi. Nilisema, “Aminini maneno yangu, kuweni makini na hawa maafisa wa Marekani wanaokuja Afrika wakiwakenulia wakati kule nyumbani hawatukenulii.” Niliwaambia kuwa baba yangu mzazi aliuawa na wazungu kwenye jimbo la Michigan, jimbo ambalo wakati fulani G. Mennen Williams amewahi kuwa Gavana wake.

Kwenye klabu ya waandishi wa habari niliheshimishwa zaidi na wawakilishi mbalimbali wa vyombo vya habari. Nilikuwa mgeni nyumbani kwa binti wa Richard Wright, mwandishi Mmarekani mwenye asili ya Afrika ambaye sasa ni marehemu. Binti huyo aliitwa Julia na mumewe wa Kifaransa alikuwa akichapisha gazeti moja pale Ghana. Siku za baadaye nilipokuwa Paris, nilipata nafasi ya kuonana na Hellen, mjane wa Wright, na Rachel, binti yao mdogo.

Nilienda kwenye balozi mbalimbali na kuzungumza na mabalozi. Balozi wa Algeria alinivutia sana kwa sababu alikuwa amejitoa kabisa kwenye mapambano ya kijeshi na mapinduzi duniani, kama njia ya watu wanaokandamizwa duniani kujikomboa. Maono yake hayakuishi tu kwa Waalgeria, bali yalihusisha watu weusi wa Marekani na wengine wote-popote walipokandamizwa. Balozi wa China, Bwana Huang Ha, mtu mwenye maono sana na mwanaharakati hasa, alikazia juu ya jitihada za nchi za magharibi kuwatenganisha Waafrika na watu wenye asili ya Afrika duniani kote. Balozi wa Nigeria aliguswa sana na madhira yanayowapata watu weusi wa Marekani. Alijua vema matatizo yao kwa sababu aliwahi kusoma na kuishi jijini Washington, D.C. Mtu mwingine aliyeguswa namna hiyo alikuwa balozi wa Mali, aliwahifika New York kwenye Umoja wa Mataifa. Nilipata kifungua kinywa na Dr. Makonnen wa British Guiana. Tulizungumza juu ya umuhimu wa kuwa na umoja wa Waafrika ambao utahusisha Wamarekani wenye asili ya Afrika. Pia nilizungumza kwa kirefu na waziri wa utamaduni wa Ghana, Nana Nketsia, juu ya matatizo ya wamarekani wenye asili ya afrika.

Niliporudi hotelini nilikutana na simu kutoka New York ikinisubiria, ilikuwa inatoka kwa Mai Goode, wa shirika la utangazaji la Marekani. Mai Goode aliniuliza maswali nami niliyajibu naye aliyarekodi. Aliniuliza kuhusu “Ndugu wa damu” wa Harlem. Chama cha wamiliki wa bunduki weusi na mambo mengine niliyohusishwa nayo na vyombo vya habari vya Marekani.

Kwenye ukumbi mkubwa wa Chuo Kikuu cha Ghana nilihutubia umati mkubwa kuliko yote niliyohutubia katika Afrika. Wengi wao walikuwa ni Waafrika na baadhi wazungu. Mbele ya umati huu nilijitahidi kila niwezavyo kuondoa uzushi juu ya mahusiano ya watu wa rangi mbalimbali huko Marekani, uzushi niliofahamu kuwa ulikuwa ukienezwa na idara ya habari ya Marekani. Nilijaribu kuwajengea picha halisi ya madhira wanayokutana nao watu weusi wa Marekani katika mikono ya wazungu. Niliwapa ukweli wao wazungu wale waliokuwa kwenye hadhara.

“Sijawahi kuona wazungu wengi wakiwa wema kwa watu weusi kama nilivyoona hapa Afrika. Huko Marekani watu wenye asili ya Afrika wanapambania uchangamano. Wanatakiwa kuja hapa Afrika na kuona jinsi mnavyowakenulia Waafrika. Hakika hapa kuna uchangamano. Lakini mnaweza kuwaambia Waafrika kuwa huko Marekani mnawakenulia watu weusi? Hapana hamuwezi! Na kusema ukweli si kwamba mnawapenda Waafrika hawa zaidi, bali mnachopenda ni madini ambayo yamo ndani ya ardhi ya Afrika . . .”

Wazungu wale walibadilika rangi na kuwa wekundu. Walifahamu kuwa nilikuwa ninaongea ukweli. “Siichukii Marekani na sijaja hapa kuishutumu Marekani-nataka kuweka hilo wazi!” Niliwaambia. “Nimekuja hapa kuongea ukweli, na kama ukweli unaishutumu Marekani basi inastahili kushutumiwa!”

Jioni moja nilikutana na maafisa wengi wa Ghana-wengi wao tayari tulikuwa tumeishazungumza hapo kabla, na tuliongea zaidi katika tafrija niliyoandaliwa na mheshimiwa Kofi Baako, waziri wa ulinzi wa Ghana na kiongozi wa bunge. Niliambiwa kuwa hiyo ni mara ya kwanza kwa mgeni kuheshimishwa namna hiyo tokea Dr. W. E. B. Du Bois alipofika Ghana. Kulikuwa na muziki, dansi na vyakula vitamu vya kighana. Watu kadhaa kwenye tafrija ile walikuwa wakicheka, wakisema kuwa kwenye tafrija ya mapema siku ile, balozi wa Marekani, bwana Mahomey, alionekana kituko wakati akijaribu kuwa mkarimu na mcheshi kupita kiasi. Wengine walisema kuwa alikuwa anafanya jitihada kupinga ukweli kuhusu Marekani, ukweli niliokuwa nauweka wazi kila nipatapo nafasi.

Kisha nikapata mualiko ambao sijawahi hata kuota. Sikuwahi wazia kabisa kuwa nitakuja kupata nafasi ya kuhutubia wabunge wa Ghana!

Nilitoa hotuba yangu kwa ufupi lakini nilihakikisha ni yenye nguvu: “Mnawezaje kuilaani Ureno na Afrika Kusini wakati watu weusi wa Marekani wanaumwa na mbwa na kupigwa kwa marungu?” nilisema kuwa nilihisi sababu pekee kwa ndugu zetu wa Afrika kukaa kimya juu ya yale yanayoendelea Marekani ni kwa sababu wamelishwa uongo na propaganda na serikali ya Marekani.

Mwisho wa hotuba yangu nilisikia, “Ndiyo! Tunawaunga mkono Wamarekani wenye asili ya Afrika . . .kimaadili, kimwili, na hata kwa mali ikibidi!”

Huko Ghana au niseme katika Afrika nzima, heshima kubwa niliyopewa ilikua ni kukutana na Osagyefo(mwokozi)Dr. Kwame Nkrumah.

Kabla ya kukutana naye nilipekuliwa vya kutosha. Naheshimu ulinzi ambao waghana wanampa kiongozi wao. Ilinifanya niwaheshimu zaidi watu weusi walio huru. Nilipoingia ofisi ya Dr. Nkrumah, aliinuka kutoka kitini. Dr. Nkrumah huvalia mavazi ya kawaida tu, alinyoosha mkono kunisalimia huku akitabasamu. Tulikaa kwenye kochi na kuzungumza. Nilifahamu kuwa alikuwa na taarifa za kutosha juu ya madhira ya Wamarekani wenye asili ya Afrika maana ameishi na kusoma Marekani kwa miaka mingi. Tulizungumza juu ya umoja wa Waafrika na watu wenye asili ya Afrika. Tulikubaliana kuwa umoja ndiyo msingi kutatua tatizo la watu wenye asili ya Afrika. Niliweza kuona ucheshi na unyenyekevu wa Dr. Nkrumah. Nilihisi kama muda wangu pamoja naye uliisha haraka sana. Niliahidi kuwa nitakaporudi Marekani, nitawapelekea Wamarekani wenye asili ya Afrika salamu zake.

Mchana wa siku ile, maili thelathini na tisa huko Winneba, nilihutubia kwenye taasisi ya itikadi ya Dr. Kwame Nkrumah- mahali ambapo wanafunzi mia mbili walikuwa wanafundishwa ili kuendeleza mapinduzi ya kifikra ya Ghana, hapa pia nilishuhudia unazi wa kisiasa wa vijana wa Kiafrika.

Wakati wa kipindi cha maswali na majibu baada ya kuhutubia, kijana wa kimarekani mwenye asili ya Afrika alisimama, “Mimi ni Mmarekani mweusi,” alijitambulisha. Kwa namna fulani akaanza kumtetea mzungu wa Marekani. Wanafunzi wakiafrika walianza kumzomea na kumzonga. Mara tu baada ya mkutano kuisha, walimbana na kuanza kumshambulia kwa maneno, “Wewe ni wakala wa wakina-Rockfeller?” . . . “Acha kupotosha watoto wetu!” (Ilikuja kufahamika kuwa kijana yule ni mwalimu wa shule ya sekondari ya karibu, akiwekwa kwenye kazi hiyo na Wamarekani) . . . “C. I. A” . . . “Shushushu wa Marekani!”

Balozi wa China, bwana Huang Ha na mkewe waliandaa mlo wa kitaifa kwa ajili yangu. Kati ya wageni walikuwepo mabalozi wa Cuba na Algeria, pia ni kwenye karamu hii ndipo nilikutana na bibi W. E. B. Du Bois. Baada ya mlo mzuri, filamu tatu zilionyeshwa, filamu moja ya rangi ilihusu sherehe ya maadhimisho ya miaka kumi na nne ya kuanzishwa kwa Jamuhuri ya watu wa China. Mtu ambaye alijitokeza mara kwa mara kwenye filamu hii alikuwa ni mwanaharakati aliyeitwa Robert Williams, alikuwa ni Mmarekani mweusi kutoka Carolina ya Kaskazini, alikuwa amekimbilia Cuba baada ya kusema kuwa watu weusi wa Marekani wanatakiwa kubeba silaha ili kujilinda. Filamu ya pili ilikazia jinsi watu wa China wanavyounga mkono harakati za watu weusi wa Marekani. Mwenyekiti Mao Tse-tung alionyeshwa akitoa tamko juu ya uungwaji mkono huo. Ndani ya filamu kulikuwa na vipande vya kutisha vikionyesha ukatili mbaya wa polisi na raia wa kizungu dhidi ya Wamarekani wenye asili ya Afrika waliokuwa wakiandamana kwenye majiji mbalimbali ya Marekani, wakidai haki za kiraia. Filamu ya mwisho ilihusu mapinduzi ya Algeria.

“Kamati ya Malcom X” ilinikimbiza haraka kutoka kwenye tafrija ya Ubalozi wa China hadi mahali ambapo klabu ya waandishi wa habari ilikuwa imeandaa tafrija kwa ajili yangu, tafrija yenyewe tayari ilikuwa imeishaanza. Ilikuwa ni mara yangu ya kwanza kuona Waghana wakicheza dansi. Kila mtu alikuwa na wakati mzuri sana. Nilisisitizwa kutoa hotuba fupi. Kwa mara nyingine nilisisitiza umuhimu wa umoja kati ya Waafrika na Wamarekani wenye asili ya Afrika. Nilisema kutoka moyoni, ‘Kwa sasa cheza dansi na imba! Lakini unapofanya hivyo mkumbuke Mandela, mkumbuke Sobokwe! Mkumbuke Lumumba akiwa ndani ya kaburi lake! Wakumbuke Waafrika Kusini walio gerezani!’
Nilisema, ‘Mnajiuliza kwa nini sichezi dansi? Kwa sababu nataka muwakumbuke Wamarekani weusi milioni ishirini na mbili waliopo Marekani!”

Lakini ukweli nilitamani sana kucheza dansi. Waghana wanacheza dansi kama vile wameshikwa na pepo. Binti mmoja mrembo Wakiafrika aliimba “Blue Moon” kama Sarah Vaughan. Wakati mwingine bendi ilipiga kama Milt Jackson, na wakati mwingine kama Charlie Parker.

Asubuhi iliyofuata, Jumamosi, nikapata habari kuwa Cassius Clay na watu wake waliwasili. Kulikuwa na mapokezi makubwa uwanja wa ndege. Niliwaza kuwa iwapo mimi na Cassius tutaonana, litakuwa jambo la kufedhehesha sana kwake, maana alikuwa amechagua kubaki na Uislamu wa Elijah Muhammad. Binafsi nisingefedheheka lakini nilifahamu kuwa Cassius alipigwa marufuku kujihusisha nami. Nilifahamu vyema kuwa Cassius alijua nilikuwa pamoja naye, kwa ajili yake na nilikuwa na imani naye wakati ambao wale ambao baadaye walikuwa karibu naye walipomuona kuwa hawezi kufika popote. Niliamua kumuepuka Cassius ili nisimuweke katika nafasi mbaya.
Mlo wa mchana wa siku ile niliandaliwa na balozi wa Nigeria, mheshimiwa Alhadji Isa Wali, mtu mmoja mfupi, aliyevaa miwani, mcheshi na mwenye urafiki sana. Aliwahi kuishi Washington D.C. kwa miaka miwili. Baada ya mlo, alizungumza na wageni wake jinsi alivyokutana na ubaguzi alipokuwa Marekani, na urafiki aliofanya na Wamarekani wenye asili ya Afrika na kukazia undugu uliopo kati ya Waafrika na Wamarekani wenye asili ya Afrika.

Kabla ya mlo, mheshimiwa alikuwa amewapatia wageni jarida la Kimarekani liitwalo horizon. Lilikuwa limefunguliwa sehemu ambayo kuliandikwa makala kuhusu Taifa la Kiislamu iliyoandikwa na Dr. Morroe Berger kutoka Chuo Kikuu cha Princeton. Kurasa moja nzima ilikuwa na picha yangu; kurasa nzima upande wa pili kulikuwa na mchoro wa Muislamu mweusi aliyeishi Nigeria, miaka mia moja iliyopita. “Nilipoangalia picha hizi, nilijua watu hawa ni wamoja,” alisema mheshimiwa. ‘Tofauti pekee ni kwenye nguo walizovaa-na mmoja alizaliwa Marekani na mwingine Afrika.​

“Kwa hiyo basi, ili kumfanya kila mtu aamini kwamba sisi ni ndugu, nitampatia Alhadji Malcom X vazi kama lile lililovaliwa na mnaigeria wa kwenye picha.”

Niliachwa mdomo wazi kwa uzuri wa vazi lile la bluu na kitambaa cha rangi ya machungwa ambacho mheshimiwa yule alinipatia. Alikuwa ni mfupi, hivyo niliinama ili aweze kunivisha kilemba. Kisha mheshimiwa Alhadji Isa Wali alinipatia matoleo mawili ya tafsiri ya Quran Takatifu. Baada ya mlo huu wa mchana usiosahaulika, bibi Shirley Graham Du Bois aliniendesha mpaka nyumbani kwake ili kwenda kuona na kupiga picha nyumba ambayo mume wake na mtu mashuhuri, Dr. W. E. B. Du Bois aliishi katika siku za mwisho za maisha yake. Bi Du Bois alikuwa ni mwandishi na mkurungenzi wa kituo cha televisheni cha Ghana, kituo ambacho lengo lake kuu lilikuwa kutoa elimu. Aliniambia kuwa Dr. Du Bois alipofika Ghana, Dr. Nkrumah alimpokea mwanaharakati na mwanazuoni yule mzee kutoka Marekani kama mfalme, akimpatia Du Bois kila kitu alichohitaji. Bi Du Bois aliniambia kuwa afya ya Dr. Dubois ilipoanza kukungoroka kwa kasi, Dr. Nkrumah alimtembelea na wawili hao waliongea maneno ya kwaheri, wote wakifahamu kuwa kifo cha mmoja wao kilikaribia-na kuwa Dr. Nkrumah aliondoka huku machozi yakimtoka.
Tukio langu la mwisho la kijamii pale Ghana ilikuwa ni kwenye tafrija iliyoandaliwa kwa heshima yangu na mheshimiwa Armando Entralgo Gonzalez, balozi wa Cuba nchini Ghana. Siku iliyofuata ilikuwa ni Jumapili-“Kamati ya Malcom X” ilikuwa inanisubiri nje ya hoteli kunisindikiza uwanja wa ndege. Tulipokuwa tunaondoka hotelini, tulikutana na Cassius Clay na baadhi ya watu wake wakitoka matembezi ya asubuhi. Kwa sekunde kadhaa Cassius alikuwa kama ameshikwa na kigugumizi, kisha akaongea kitu, nadhani alisema “Habari yako?” taswira ya jinsi tulivyokuwa karibu kabla ya pambano lililobadili maisha yake ilinijia kichwani. Nilimjibu kuwa nzuri au kitu kama hicho, na kuwa ni matumaini yangu kuwa naye ni mzima pia-na hilo lilitoka moyoni. Baadaye nilimtumia Cassius ujumbe nikimwambia kuwa natumaini anatambua jinsi anavyopendwa na Waislamu kokote waliko; na kwamba hataruhusu mtu yeyote amtumie na kumpotosha kusema mambo ambayo yatachafua taswira yake.

Tulikuwa uwanja wa ndege nikiagana na “Kamati ya Malcom X” na ghafla msafara mdogo wa mabalozi matano ulifika kuniaga. Mpaka hapo nilikuwa nimeishiwa maneno ya kusema.

Nikiwa kwenye ndege kuelekea Monrovia, Liberia ambako ningetumia siku moja, niliwaza kuwa baada ya mambo yaliyonipata kwenye Nchi Takatifu, jambo jingine nitakaloenda nalo Marekani ni jinsi ambavyo Waafrika wanavyojitambua, utajiri wake na nguvu zake na nafasi yake katika dunia.
Kutoka Monrovia, nilipanda ndege mpaka Dakar, Senegali. Wasenegali waliokuwepo uwanja wa ndege baada ya kusikia kuhusu Muilsmu kutoka Marekani, walisimama kwa mstari ili kunisalimu kwa mkono, na niliandika saini nyingi. “Watu wetu hawazungumzi Kiarabu, lakini Uislamu upo mioyoni mwetu,” alisema Msenegali mmoja. Nikasema kuwa iko hivyo pia kwa Waislamu wenzao Wamarekani wenye asili ya Afrika.

Kutoka Dakar nilipanda ndege hadi Morocco ambako nilitumia siku moja kutembea hapa na pale. Nilitembelea Casbah, eneo la maghetto ambalo lilitokea baada ya wakoloni wa Kifaransa kuwakataza wazawa wasio wazungu kuishi maeneo fulani ya Casablanca. Maelfu kwa maelfu ya wazawa waliokandamizwa waliishi kwa kusongamana kwenye maghetto, kama tu ambavyo Harlem, New York ilivyokuja kuwa Casbah ya Marekani.

Nilipowasili Algiers ilikuwa ni Jumanne, tarehe 19 ya mwezi wa tano, mwaka 1964, siku yangu ya kuzaliwa. Mambo mengi yamepita tokea ziku zile. Kwa namna fulani nilikuwa na uzoefu kuliko dazani ya watu. Dereva wa taxi aliyenichukua kwenda hoteli ya Aletti, alinielezea ukatili uliofanywa na Wafaransa na hatua alizochukua yeye binafsi ili kulipa kisasi. Nilitembea katika jiji la Algiers nikisikia maneno ya chuki dhidi ya Marekani kwa kitendo chake cha kuunga mkono ukandamizaji wa Waalgeria. Walikuwa ni wanamapinduzi hasa, hawakuogopa kifo. Kwa muda mrefu sana wamekabiliana na kifo.

***​
 
Sura ya 18 inaendelea.

Nilipanda ndege ya shirika la Pan American kurudi nyumbani. Tulitua uwanja wa ndege wa Kennedy, New York. Ilikuwa saa kumi na dakika ishirini na tano jioni, tarehe 21 mwezi wa tano. Abiria tulitoka kwenye ndege kwa mstari kuelekea ofisi za uhamiaji. Nilipoona umati wa waandishi wa habari na wapiga picha kama hamsini au sitini hivi, nilijiuliza ni mtu gani maarufu nilikuwa naye kwenye ndege.

Lakini kumbe nilikuwa ndiye “Mtu mbaya” waliyekuja kwa ajili yake.

Kule Harlem, na kwenye majiji mengine ya Marekani, mlipuko wa vurugu uliotarajiwa kwenye majira ya joto ya mwaka 1964 ulikuwa umeanza. Makala juu ya makala kwenye magazeti ya mzungu yalikuwa yameniweka mimi kama alama-kama siyo msababishi kabisa wa “machafuko” na “Vurugu” za watu weusi, haijalishi zilitokea wapi.

Kwenye mkutano mkubwa kabisa na waandishi wa habari kuliko yote niliyowahi kufanya, taa za kamera zilimulika na waandishi walinishambulia kwa maswali.

“Bwana Malcom X, vipi kuhusu wale ‘Ndugu wa Damu’ waliotajwa kuwa wanauhusiano na taasisi yako, wanasemwa kuwa wamefundishwa kufanya vurugu, watu ambao wameua wazungu wasio na hatia?” . . . “Bwana Malcom X, vipi kuhusu maoni yako kuwa watu weusi wanatakiwa kuunda vyama vya wamiliki wa bunduki? . . .”

Nilijibu maswali yao. Nilijua kuwa nimeisharudi Marekani baada ya kusikia maswali ya mtego na ya kutafuta mbuzi wa kafara kutoka kwa wazungu. Vijana wa kizungu wa jiji la New York walikuwa wakiua watu, hilo lilikuwa tatizo la “Kijamii.” Lakini vijana weusi walipoua mtu, serikali ilitafuta kumnyonga. Pale ambapo watu weusi walipouawa na umati au kwa namna nyingine bila huruma, ilisemwa kuwa, “Mambo yatakuwa mazuri huko mbeleni.” Wazungu wanapokuwa na bunduki, ni katiba imewapa haki ya kulinda nyumba zao na wao wenyewe. Lakini watu weusi hata wanapoongelea tu kumiliki bunduki majumbani mwao, inakuwa nongwa kubwa.”

Niliwaambia waandishi wa habari wale kitu fulani ambacho hawakutegemea kabisa. Niliwaambia kuwa watu weusi wa Marekani wanatakiwa kuacha kufikiri kwa namna waliyofundishwa na mzungu-kwamba mtu mweusi hana njia mbadala zaidi ya kuomba zile zinazoitwa “Haki za kiraia.” Nilisema kuwa mtu mweusi anatakiwa kutambua kuwa ana kesi ya msingi na yenye nguvu sana mbele ya Umoja wa Mataifa dhidi ya Marekani. Kesi ya kunyimwa “Haki za binadamu”-na kuwa, kama Angola na Afrika Kusini walistahili kuwa na kesi kama hiyo, basi hakukuwa na njia kwa Marekani kuepuka kesi, hapa hapa kwenye ardhi yake.
Kama ambavyo nilifahamu, vyombo vya habari vilitaka niachane na hoja hiyo. Niliulizwa kuhusu “Barua Yangu Kutoka Mecca”-nilikuwa nimeandaa kabisa hotuba kwa ajili ya jambo hilo:
‘Ni matumaini yangu kuwa Hija yangu kwenye Mji Mtakatifu wa Mecca imeifanya taasisi yetu ya Msikiti wa Kiislamu, Inc ikubalike na Waislamu wengine wa kweli milioni 750 duniani kote. Na ninafahamu kwa uhakika kabisa kuwa Waafrika wanawachukulia Wamarekani weusi milioni
22 kama ndugu zao waliopotezana nao kwa muda mrefu!

Wanatupenda! Wanafuatilia mapambano yetu ya uhuru. Walifurahi sana kusikia kuwa tulikuwa tunaamka kutoka katika usingizi wetu wa muda mrefu-baada ya wale wanaoitwa wazungu ‘Wakristo’ wa Marekani kutufundisha kuwa tunatakiwa kuwaonea aibu ndugu zetu wa Kiafrika na bara la asili yetu!
‘Ndiyo-niliandika barua hiyo kutoka Mecca. Mnaniuliza, ‘Je, haukusema kuwa sasa unawakubali wazungu kama ndugu?’ jibu langu ni kuwa, katika dunia ya Kiislamu niliona, nilihisi na kuandika barua nikielezea jinsi ambavyo fikra zangu zilikuwa zimetanuka! Kama tu nilivyoandika, nilishiriki undugu wa kweli na Waislamu wengi wenye muonekano wa kizungu ambao hata siku moja hawakuwahi kuwazia habari za rangi, au muonekano wa Muislamu mwenzake.

‘Hija yangu ilikuwa imetanua uelewa wangu. Imenibariki kwa kunipatia mtazamo mpya. Kwa wiki mbili nilizokaa katika Nchi Takatifu, nimeshuhudia mambo ambayo sijayashuhudia ndani ya Marekani kwa miaka thelathini na tisa niliyoishi. Niliona watu wa jamii na rangi zote, kutoka wazungu wenye macho ya bluu na nywele za rangi ya dhahabu hadi Waafrika weusi, wote wakiwa katika undugu wa kweli! Katika umoja! Wakiishi kama kitu kimoja! Wakiabudu kama kitu kimoja! Hakuna wabaguzi wala waliberali; hata hawangejua maneno hayo yana maana gani.

‘Ni kweli kuwa huko nyuma niliwashutumu wazungu wote vikali. Sitafanya hivyo tena kwa sababu sasa naelewa kuwa baadhi ya wazungu ni watu wema, kwamba wanaweza kuwa ndugu wa kweli na mtu mweusi. Uislamu wa kweli umenifundisha kuwa si sawa kuwahukumu wazungu wote kama tu ambavyo wazungu wanavyowahukumu watu weusi wote.
‘Ni kweli nimeshawishiwa kuamini kuwa baadhi ya wazungu wa Marekani wanataka kusaidia kutibu tatizo la ubaguzi wa rangi, tatizo ambalo likiendelea litaiangamiza nchi yetu!

‘Ni kwenye Ulimwengu mtakatifu ndiko mtazamo wangu ulibadilika kutokana na niliyotendewa na niliyoyashuhudia huko kuhusu undugu-si tu undugu kunielekea, bali undugu kati ya watu wote, wa mataifa na rangi zote waliokuwepo kule. Sasa nimerudi Marekani, mtazamo wangu kuelekea wazungu mahali hapa unatakiwa kuongozwa na kile ambacho mimi na ndugu zangu weusi wengine wanachopitia na kushuhudia kuhusiana na swala la undugu. Tatizo la hapa Marekani ni kuwa tunakutana na wazungu ‘Wema’ wachache sana. Hapa Marekani, ukiachana na wazungu ‘Wema’ wachache, kuna wazungu wengine milioni 150 ambao watu weusi milioni 22 wanakabiliana nao.

‘Kwa nini hapa Marekani mizizi ya ubaguzi wa rangi imejikita sana ndani ya wazungu wengi. Imani yao kwamba kwa namna fulani wao ni ‘Bora’ zaidi imekita mizizi sana ndani yao, mambo haya yapo kichwani mwao. Wazungu wengi hata hawatambua kwamba ni wabaguzi wa rangi mpaka pale wanapokabiliana na aina fulani ya mtihani, hapo ndipo ubaguzi wao wa rangi unapojitokeza kwa namna moja ama nyingine.
‘Sikilizeni! Ubaguzi ambao mzungu anamfanyia mtu mweusi hapa Marekani ndiyo unaomuingiza matatizoni na watu wasio wazungu duniani kote. Mzungu hawezi kujitenga na unyanyapaa anaohisi kuelekea wengine, haijalishi ni nani, ilmradi tu siyo wa rangi yake. Na watu wasio wazungu duniani wamechoshwa na kudharauliwa na wazungu! Hiyo ndiyo sababu unaona matatizo yote haya sehemu kama Vietnam. Au huku huku magharibi ya dunia ambako watu wenye asili ya Afrika kama milioni 100 wamegawanyika wenyewe kwa wenyewe, wakifundishwa na mzungu kuchukiana na kutoaminiana. Huko kwenye visiwa vya Karibeani, Cuba, Brazil, Venezuela, Amerika Kusini na ya Kati yote! Maeneo yote hayo yamejaa watu wenye asili ya Afrika. Hata barani Afrika mzungu amefanikiwa kuwafarakanisha Waafrika weusi na Waarabu wa wa kahawia, kuwagawa kati ya ‘Waafrika Waislamu’ na ‘Waafrika Wakristo.’ Unaweza kuwazia nini kitatokea iwapo watu wote hawa wenye asili ya Afrika wakitambua kuwa wao ni damu moja, wakitambua kuwa lengo lao ni moja na kuungana?’

Waandishi wa habari walishukuru kuachana nami siku ile. Naamini kuwa ndugu weusi niliowaacha Afrika watakuwa walihisi kuwa nimeitendea haki mada ile. Karibu usiku wote simu yangu ya nyumbani ilikuwa inaita. Ndugu na dada zangu weusi kutoka New York na majiji mengine walikuwa wananipigia simu kunipongeza kwa kile walichosikia redioni na kuona kwenye televisheni, na watu wengi, hasa wazungu walikuwa wanataka kufahamu iwapo nitahutubia na wapi nitahutubia.

Siku iliyofuata nilikuwa nikiendesha gari yangu, niliposimama kwenye taa nyekundu, gari nyingine ikawa imesimama pembeni yangu. Mwanamke mzungu alikuwa anaendesha na kwa pembeni yake alikaa mwanaume mzungu. “Malcom X” aliita kwa sauti. Nilipogeuka alitoa mkono wake nje ya gari huku akikenua. “Kuna tatizo ukipeana mkono na mzungu?” Piga picha jambo hilo! Wakati huo taa za kijani nazo zikawa ndiyo zinawaka, nilimwambia, “Sina tatizo kupeana mikono na binadamu. Wewe ni binadamu?”
 
Sura ya 19
1965
Lazima niwe mkweli. Wamarekani weusi hawakuonyesha nia yoyote ya kukimbilia Umoja wa Mataifa kudai haki zao ndani ya Marekani. Na ukweli nilikuwa nimefahamu toka mapema kuwa wasingefanya hivyo. Mzungu wa Marekani amemchota mtu mweusi akili kabisa kiasi kwamba mtu mweusi anajiona kuwa tatizo lake ni tatizo la haki za kiraia za ndani ya Marekani pekee. Pengine itachukua zaidi ya muda nitakayoishi kwa mtu mweusi kuona kuwa mapambano ya mtu mweusi wa Marekani ni ya kimataifa.

Na pia nilifahamu kuwa watu weusi hawangeharakisha kunifuata kwenye Uislamu asilia, Uislamu ulionipa mwanga wa kufahamu kuwa mtu mweusi na mzungu wanaweza kuwa ndugu. Watu weusi wa Marekani, hasa wazee-wamezama sana kwenye kwenye Ukristo wenye mtazamo wa undumakuwili pale linapokuja suala la ukandamizaji wa watu. Basi kwenye mikutano “niliyokaribishwa na umma” ambayo nilianza kuihutubia kila jumapili mchana au jioni kwenye ukumbi wa Audubon, mahali ambako niliwahubiria watu ambao wengi wao hawakuwa Waislamu-sikukazia sana suala la dini ya Kiislamu bali kwa ajili ya wote walioketi mbele yangu:

“Si Waislamu, si Wakristo, si Wakatoliki, si Waprotestanti . . .Wabaptisti au Wamethodisti, Wademokrati au Warepublikani, Wamasoni—namaanisha watu weusi wa Marekani na duniani kote. Watu weusi wote kwa ujumla wetu, si tu tumenyimwa haki za kiraia, bali pia haki za binadamu, haki ya kuishi kama binadamu ”
Baada ya hotuba yangu, watu wengi mtaani walionipa mkono na kutaka nisaini vitabu vyao, lakini kwenye sura zao niliona mtazamo wa kukaa na kusubiri litakalotokea . Nilielewa mtanziko wao juu ya mahali niliposimama. Tokea “uhuru” uliopatikana baada ya vita ya wenyewe kwa wenyewe ya Marekani, mtu mweusi amepita njia nyingi bila matunda yoyote. Iko wazi kuwa viongozi wake wamemuangusha. Dini ya Ukristo imemuangusha. Mtu mweusi alikuwa ameishaumizwa hivyo alikuwa makini sana.

Sasa naelewa vizuri kuliko hapo mwanzo. Kwenye Ulimwengu Mtakatifu, mbali na Marekani kwenye ubaguzi wa rangi, ilikuwa ndiyo mahali pekee nilikoweza kutafakari kwa kina juu ya mgawanyiko wa wazungu wa Marekani na jinsi ambavyo mtazamo na malengo ya vimemuathiri mtu mweusi. Kwa miaka yangu thelathini na tisa duniani hapa, kwenye Mji Mtakatifu wa Mecca ndiyo ilikuwa mara yangu ya kwanza kusimama mbele ya Muumba Vyote na kujihisi kama binadamu.

Kwenye amani ile ndani ya Nchi Takatifu-usiku ule niliosema nililala nje kwenye uwazi kati ya mahujaji wanaokoroma, akili yangu ilinichukua na kunipeleka kwenye kumbukumbu za maisha yangu . . .ilinichukuaa nyuma kabisa hadi nilipokuwa kijana mdogo wa miaka nane au tisa hivi. Nikiwa nyuma ya nyumba yetu, huko vijijini karibu na Lansing Michigan. Kulikuwa na kilima kimoja tulichokiita kilima cha Hector. Nilipokuwa kwenye Nchi Takatifu nilikumbuka jinsi nilivyokuwa nikilala kwenye kilima cha Hector na kutazama angani, nikitazama mawingu yakipita na kuota ndoto za mchana za kila aina. Nakumbuka miaka mingi baadaye nilipokuwa gerezani, nilizoea kulala kwenye kitanda changu, hasa wakati nilipokuwa natumikia kifungo cha kutengwa-nilikuwa napiga picha nahutubia umati mkubwa. Sikujua kwa nini maono hayo yalikuwa yakinijia, lakini yalinijia. Kumhadithia mtu yeyote wakati ule ningeonekana kichaa. Mimi mwenyewe sikuwa nayatilia maanani . . . .

Pia nilipokuwa Mecca, kumbukumbu za miaka kumi na mbili niliyokuwa na Elijah Muhammad ilinijia kama vile filamu. Nadhani haikuwezekana kwa mtu mwingine yeyote kuelewa ukubwa wa imani yangu kwa Elijah Muhammad. Nilimuamini si kama tu kiongozi wa kibinadamu lakini pia kama kiongozi mwenye uwezo wa kimungu. Niliamini kuwa hakuwa na udhaifu wala kasoro za kibinadamu hivyo hawezi kukosea hata kwa bahati mbaya. Kule juu ya kilima katika Nchi Takatifu, nilitambua jinsi ilivyo hatari kwa watu kumchukulia binadamu yoyote namna hiyo, hasa kumfikiria mtu kuwa anaongozwa na kulindwa na Mungu.

Fikra zangu zilifunguliwa kabisa nilipokuwa Mecca. Kwenye barua ile ndefu niliyowaandikia rafiki zangu, nilijaribu kuwaelezea mtazamo wangu mpya juu ya matatizo na harakati za watu weusi wa Marekani na pia juu ya ukweli na haki.

“Nimechoshwa na propaganda kutoka kwa watu,” niliwaandikia rafiki zangu hao. “Ninasimama kwenye ukweli, haijalishi anayeusema ni nani. Ninasimamia haki, haijalishi ni kwa ajili au ni dhidi ya nani. Kabla ya mengine yote mimi ni binadamu kwanza na kutokana na hilo, mimi nakuwa kile ambacho kipo kwa maslahi ya binadamu wote.

Kwa sehemu kubwa vyombo vya habari vya wazungu viligoma kueleza kuwa nilikuwa najaribu kuwafundisha watu weusi mtazamo mpya. Vurugu za majira ya joto ya mwaka 1964 zilizokuwa bado zinaendelea hapa na pale. Vurugu hizo zilifanya nishutumiwe mara kwa mara kuwa nilikuwa nawachochea watu weusi. Kila mara nilipokuwa mbele ya kinasa sauti, redioni au kwenye televisheni na nikaulizwa kuhusu “Kuwachochea watu weusi” au “Kuchochea vurugu,” nilipandwa na hasira kali.

“Bomu la kisaikolojia linalotokana na kukosa ajira, makazi duni, elimu duni lililopo kwenye maeneo ya maghetto halihitaji mtu yeyote kulichochea ili lilipuke. Mazingira haya ya kihalifu yamekuwepo kwa muda mrefu sana hivyo hayahitaji kulipuliwa, yanalipuka yenyewe; yanajichocheza kutoka ndani yake yenyewe.”
Waliniita mtu mweusi mwenye hasira zaidi katika Marekani.” Sikukataa shutuma hizo. Niliongea vile nilivyohisi. “Nakubaliana na hasira. Biblia inasema kuwa kuna wakati wa hasira.” Waliniita mwalimu na mchochezi wa vurugu. Hilo nilijibu bila kumung’unya maneno, ‘huo ni uongo, sipendelei vurugu, lengo langu ni haki. Naamini iwapo wazungu wangekuwa wanashambuliwa na watu weusi-na iwapo vyombo vya dola vingeonekana haviwezi au havitaki kuwalinda wazungu hao kutoka kwa watu weusi-basi wazungu hao wanapaswa kujilinda dhidi ya weusi wanaowashambulia, kwa kutumia silaha pale inapobidi. Na naona kuwa pale vyombo vya dola vinaposhindwa kumlinda mtu mweusi dhidi ya mashambulizi kutoka kwa wazungu, basi watu weusi hao wanatakiwa kutumia silaha pale inapobidi ili kujilinda.’

“Malcom X anashauri watu weusi wabebe silaha!” Hilo lina ubaya gani” nitakwambia shida iko wapi. Nilikuwa mtu mweusi niliyekuwa naongelea kujilinda dhidi ya mzungu. Wazungu wanaweza kuwaua, kuwachoma na kuwapiga mabomu watu weusi-hakuna tatizo: “Kuweni na subira” . . . “Mambo haya yamekuwepo kwa muda mrefu hayawezi kuondoka siku moja . . . ‘Lakini mambo yanazidi kuwa mazuri.’ Nafikiri ni uhalifu kwa mtu anayekandamizwa kuendelea kuvumilia ukandamizwaji huo bila ya kufanya jambo lolote kujitetea. Kama hivyo ndivyo falsafa ya “Kikristo” inavyotafsiriwa, kama hivyo ndivyo falsafa ya Gandhi inavyofundisha, basi nitaziita falsafa za kihalifu.

Kwenye kila hotuba yangu nilijitahidi kuelezea mtazamo wangu mpya kuelekea wazungu-“Sina jambo lolote dhidi ya wazungu wema. Nimejifunza kuwa wazungu wa namna hiyo wapo. Nimejifunza kwamba si wazungu wote ni wabaguzi wa rangi. Naongea dhidi ya wabaguzi wa rangi, na mapambano yangu ni dhidi ya wabaguzi wa rangi wa kizungu. Ninaamini kuwa watu weusi wana haki ya kupambana dhidi ya wabaguzi hawa, kwa njia yoyote ile.” Lakini waandishi wa habari wa kizungu bado walitaka kunihusianisha na “vurugu.” Sidhani kama kulikuwa na mahojiano ambayo sikutupiwa shutuma hizo.

“Ninaunga mkono vurugu iwapo kutokuwa na vurugu kunamaanisha kuacha matatizo ya mtu mweusi wa Marekani yaendelee ili tu kuepuka vurugu. Siungi mkono njia zisizo za vurugu iwapo zinamaanisha kucheleweshwa kwa utatuzi wa tatizo la mtu mweusi wa Marekani. Kwangu mimi kuchelewesha utatuzi ni kutotatua kabisa. Au niseme kwa njia nyingine; kama vurugu ndizo zinahitajika ili kumpatia mtu mweusi haki zake katika nchi hii, basi naunga mkono vurugu kama ambavyo unafahamu kuwa Wairish, Wapoland na Wayahudi wangefanya iwapo wangekuwa wanabaguliwa. Mimi niko tu kama wao iwapo wangekuwa kwenye nafasi yangu, na wangeunga mkono vurugu bila kujali matokeo wala ambaye angeumizwa na vurugu hizo.”

Jamii ya wazungu inachukia sana kusikia-hasa kutoka kwa mtu mweusi juu ya uhalifu ambao mzungu amemfanyia mtu mweusi. Siku zote nilielewa kwa nini niliitwa “mwanamapinduzi.” Ilikuwa kama vile nimefanya uhalifu fulani! Na mtu mweusi wa Marekani hahitaji kujiingiza kwenye mapinduzi ya kweli. Neno “Mapinduzi” kwa

Kijerumani ni Umwalzung. Linamaanisha mabadiliko kabisa kabisa. Kupinduliwa kwa Mfalme Farouk wa Misri na kuingia kwa Rais Nasser madarakani ni mfano mmojawapo wa mapinduzi ya kweli. Kunamaanisha kuharibu kabisa mfumo wa kale na kuweka mfumo mpya mahala pake. Mfano mwingine ni mapinduzi ya Algeria yaliyoongozwa na Ben Bella; waliwapindua Wafaransa waliowatawala kwa miaka zaidi ya 100. Sasa mtu mwenye akili zake anawezaje kusema kuwa mtu mweusi wa Marekani anataka kufanya mapinduzi? Ni kweli kuwa anaulaani mfumo uliopo, lakini hataki kuubadili wala kuuondoa. Ule unaoitwa uasi wa watu weusi ni harakati tu za kutaka kukubaliwa kwenye mfumo uliopo! Uasi wa kweli wa watu weusi utahusisha kupigania majimbo huru ya watu weusi ndani ya nchi hii-jambo ambalo watu na vikundi vingi vimelipigania miaka mingi kabla ya Elijah Muhammad.

Ni wazi kuwa mzungu alipofika katika nchi hii kwa mara ya kwanza hakuonyesha mtazamo wowote wa “kutokuwa mtu wa vurugu.” Na ukweli ni kuwa mtu yuleyule ambaye jina lake leo hii ni ishara ya kutokuwa na vurugu alisema:

“Nchi yetu ilizaliwa kutoka kwenye mauaji ya halaiki pale ilipokubaliana na sera kuwa Mhindi wa Amerika ni mtu duni. Hata kabla hakujawa na watu weusi wengi katika nchi hii, tayari makovu ya chuki zitokanazo na ubaguzi wa rangi yalikuwa yameathiri jamii ya kikoloni. Kutoka karne ya kumi na sita na kuendelea, damu ilimwagika kwenye vita juu ya ukuu wa watu wa rangi fulani. Pengine sisi ndilo taifa pekee ambalo tulikuwa na sera za taifa zilizojaribu kuwaangamiza wenyeji wa nchi. Na zaidi ni kuwa tulilifanya jambo hilo baya kuwa jambo la kishujaa. Na hata leo hii bado hatujakubali kulilaani au kuhisi hatia juu ya jambo hilo la aibu. Vitabu vyetu, filamu, maigizo na hekaya zinalitukuza jambo hilo. Watoto wetu bado wanafundishwa kutukuza ukatili uliowafanya watu wekundu waliokuwepo hapa toka kale kuwa vikundi vya watu wachache tu wanaosagwa kwenda kwenye maeneo waliyotengewa.”

“Kukaa pamoja kwa amani!” hilo ni jambo lingine ambalo mzungu amekuwa mwepesi kulipigia kelele. Sawa! Lakini ni yapi yamekuwa matendo ya mzungu? Katika historia yote amekuwa akipeperusha bendera ya Ukristo . . . huku kwenye mkono mwingine akiwa ameshika upanga na bunduki.

Unaweza kurudi nyuma hadi wakati wa kuanzishwa kwa Ukristo. Ukatoliki, mwanzo wa ukristo tunaoujua leo ulianzishwa Afrika na wale ambao kanisa linawaita “Mapadri wa Jangwani.” Kanisa la Kikristo liliingiliwa na ubaguzi wa rangi lilipofika Ulaya. Kanisa hilo lilirudi Afrika likiwa linapeperusha bendera ya uvamizi, mauaji, unyonyaji, ubakaji, uonevu, kupiga na kufundisha ukuu wa mzungu. Hivi ndivyo mzungu alivyoweza kujiweka kwenye uongozi wa dunia-kwa kutumia mabavu, hakuwa kiroho kabisa. Historia ya binadamu inaonyesha kuwa sifa ya kweli ya kuwa kiongozi ni sifa ya kiroho. Watu wanavutiwa na sifa za kiroho. Kwa mabavu watu huwa wanalazimishwa tu. Upendo unatengenezwa na roho. Mabavu huzalisha hofu.

Ninakubaliana kwa asilimia mia moja na wabaguzi wa rangi wanaosema kuwa hakuna sheria ya serikali inayoweza kuwalazimisha watu waishi kama ndugu. Suluhisho pekee la matatizo yanayoikumba dunia leo hii ni serikali zinazoongozwa na dini ya kweli. Hapa Marekani-nchi iliyogawanyika sababu ya ubaguzi wa rangi, naamini kuwa dini ya Kiislamu inahitajika haraka, hasa kwa mtu mweusi wa Marekani. Mtu mweusi wa Marekani anatakiwa kutafakari kuwa amekuwa Mkristo muaminifu zaidi katika Marekani-na hilo limemfikisha wapi? Ukristo katika mikono ya mzungu, na kama ulivyotafsiriwa na mzungu-umeifikisha watu dunia? Umeifanya theluthi mbili ya watu wa dunia ambao siyo wazungu waasi. Theluthi mbili ya watu duniani leo wanaiambia theluthi moja-wazungu wachache, “Toka!” Na mzungu anatoka kwao. Na anapoondoka tunaona watu wasio wazungu wakirudia dini zao za asili kwa kasi, dini zilizoitwa za “kipagani.” Ni dini moja tu-Uislamu ndiyo yenye nguvu ya kuweza kupambana na Ukristo wa mzungu kwa miaka elfu! Ni Uislamu pekee ndiyo unaoweza kuudhibiti Ukristo wa mzungu.

Waafrika wanaurudia Uislamu na dini zingine za asili.
Waasia wanarudi kuwa Wahindu, Wabuddha na Waislamu.
Kama ambavyo vita vitakatifu vya Ukristo vilivyoelekea mashariki, vita vitakatifu vya Uislamu vinaelekea magharibi. Asia Mashariki ikiwa imezuia Ukristo, Afrika ikisilimu kwa kasi, na Ulaya ikienda mbali na Ukristo kwa kasi kubwa- inakubalika duniani kote kuwa ustaarabu wa “Kikristo” wa Marekani-ambao unamuinuamzungu duniani kote-ndiyo ngome pekee ya Ukristo iliyobakia.

Basi kama hivyo ndivyo ilivyo-kama huo unaoitwa “Ukristo” unaofanyika Marekani ndiyo Ukristo bora uliobakia duniani-basi hakuna mtu mwenye akili timamu atakayehitaji ushahidi zaidi kujua kuwa mwisho wa Ukristo upo karibu sana.

Unafahamu kuwa baadhi ya wanatheolojia wakiprotestanti katika maandiko yao wanatumia neno “zama za baada ya Ukristo” na wanamaanisha zama hizo ni sasa?

Na ni sababu gani moja kubwa kwa kanisa la Kikristo kushindwa vibaya namna hii? Ni kwa sababu ya kushindwa kwake kupambana na ubaguzi wa rangi. Ni matokeo ya ile habari ya zamani isemayo, “Utavuna ulichopanda.” Kanisa la Kikristo lilipanda ubaguzi wa rangi-tena kwa kufuru; sasa unavuna ubaguzi wa rangi.
Piga picha asubuhi moja ya Jumapili ya mwaka huu wa 1965- waumini Wakikristo wakilindwa na mashemasi mlangoni ili kuzuia waumini weusi wasiingie, wakiwaambia, “Hamuwezi kuingia katika hii nyumba ya Mungu!”
Niambie iwapo kuna jambo la kusikitisha kama ambavyo kwenye mji wa St. Augustine, Florida. Mji wenye jina la mtakatifu ambaye alikuwa ni mtu mweusi aliyeuokoa Ukatoliki dhidi ya uzushi, lakini hivi karibuni palikuwa mahali palipotokea machafuko ya ubaguzi wa rangi na umwagaji damu.

Naamini kuwa kipindi hiki Mungu anaipa jamii ya “Wakristo wa kizungu” nafasi ya mwisho kutubu na kulipa kwa uhalifu wao wa kunyonya na kufanya watumwa watu wa dunia wasio wazungu. Ni kama tu Mungu alivyompa Farao nafasi ya kutubu. Lakini Farao aliendelea kukaidi kuwapa haki zao wale aliowakandamiza. Na tunafahamu kuwa mwisho wake Mungu alimuangamiza Farao.

Je wazungu wa Amerika wanajuta kikweli kwa uovu wao dhidi ya watu weusi wa Marekani? Je mzungu wa Marekani anao moyo wa kuweza kutubu? Je wengi wao wanauwezo wa kutubu na kulipia, au hata theluthi ya wazungu wa Marekani?

Watu wengi weusi wangependa kusamehe na kusahau uovu waliotendewa. Lakini wazungu wengi hawaonyeshi kuwa wanataka kutubu kikweli.

Tuseme ukweli, jamii ya wazungu inawezaje kulipa kwa kufanya watumwa, kubaka, na kuwafanyia ukatili mamilioni ya binadamu kwa mamia ya miaka? Ni malipo gani Mungu wa haki atakubali kwa kupora watu weusi nguvu kazi yao, maisha yao, utamaduni wao, historia yao na hata ubinadamu wao?

Kutumia kikombe cha kahawa kwa pamoja, ukumbi, vyoo vya umma-na matendo yote ya kuonyesha “uchangamano” wa kinafiki si malipo.

Baada ya kukaa kidogo Marekani, nilisafiri tena. Safari hii nilitumia wiki kumi na nane huko Mashariki ya Kati na Afrika. Viongozi wa kitaifa ambao nilizungumza nao kwa faragha wakati huu walikuwa ni pamoja na Rais Gamal Abdel Nasser wa Misri; Rais Julius K. Nyerere wa Tanzania; Rais Nnamdi Azikiwe wa Nigeria; Osagyefo Dr. Kwame Nkrumah wa Ghana; Rais Sekou Toure wa Guinea; Rais Jomo Kenyatta wa Kenya; na Dr. Milton Obote, Waziri Mkuu wa Uganda.

Pia nilikutana na viongozi wa kidini, Waarabu, Waafrika, Waasia, Waislamu na wasio Waislamu. Na katika nchi zote hizi nilizungumza na Wamarekani wenye asili ya Afrika na wazungu waliokuwa wana taaluma mbalimbali.

Balozi mmoja wa Marekani katika nchi fulani ya Afrika alikuwa ndiye balozi wa Marekani aliyeheshimika zaidi katika Afrika. Niliambiwa hayo kiongozi mmoja mkubwa katika Afrika. Tulizungumza mchana wote. Kutokana na niliyosikia kumhusu, niliamini pale aliponiambia kuwa anapokuwa Afrika hafikiri watu kulingana na rangi zao. Kwamba anashughulika na binadamu na si rangi zao. Alisema kuwa alitilia sana maanani tofauti ya lugha kuliko ya rangi.

Nilimwambia, “Unachoniambia ni kuwa si mzungu wa Marekani ambaye ni mbaguzi bali mazingira ya Marekani ya kisiasa, kiuchumi na kijamii ndiyo yanayomuathiri mzungu kisaikolojia na kumfanya kuwa mbaguzi wa rangi.” Alikubaliana na hilo.

Sote tulikubali kuwa jamii ya Marekani inafanya isiwezekane kwa binadamu kukutana ndani ya Marekani na wasitilie maanani tofauti za rangi zao. Na pia tulikubaliana kuwa iwapo ubaguzi wa rangi ungekoma ndani ya Marekani, basi kungekuwa na jamii ambayo matajiri na masikini wanaishi pamoja kama binadamu.

Mazungumzo na balozi yalinipa mtazamo mpya-mtazamo nilioupenda: Kwamba mzungu si muovu kwa asili, bali jamii ya kibaguzi ya Marekani inamlazimisha kutenda kiovu. Jamii imetengeneza na kuendeleza saikolijia inayofanya binadamu kuwa wa ovyo kabisa.

Nilikuwa na mazungumzo tofauti kabisa na mzungu fulani mwingine niliyekutana naye Afrika-mtu huyu aliwakilisha kitu kilekile ambacho nilijadiliana na balozi. Katika safari yangu yote nilikuwa natambua kuwa nilikuwa nachunguzwa muda wote. Shushushu huyu alitambulika mara moja, na alikuwa mwenye kuudhi. Sina hakika alitoka idara gani, naye hakusema. Basi mwishowe nilishindwa kumvumilia baada ya kuona kuwa siwezi kula chakula hotelini kwa amani bila ya kumuona akinifuatilia. Ungeweza dhani nilikuwa John Dillinger au mtu wa namna hiyo.

Asubuhi moja wakati wa kifungua kinywa nilisimama na kumfuata. Nikamwambia kuwa ninafahamu kuwa ananifuatilia, na kama kuna kitu anataka kukifahamu kwa nini asiniulize. Alianza kuniletea zile za kujidai yeye hawezi kujishusha kwa kuanza kunifuatilia. Pale pale nikamwambia wazi kuwa alikuwa ni mpumbavu na hakunijua au kujua kile ninachosimamia, na kwamba ni mmoja wa wale watu ambao huacha wengine wafikiri kwa niaba yao; na kwamba haijalishi mtu anafanya kazi gani, walau basi awe na uwezo wa kufikiri mwenyewe. Hilo lilimgusa na hakuwa na la kujibu.

Nilimsikiliza akinishutumu kuwa mchukia Marekani, mhaini na labda mkomunisti. Nilimwambia kuwa anayoongea yanaonyesha wazi ni jinsi gani anaufahamu mdogo kunihusu. Nilimwambia kuwa kitu pekee ambacho F.B.I, C.I.A au taasisi yoyote ile inachoweza kunikuta nina hatia nacho ni kuwa muelewa. Nilimwambia kuwa mimi natafuta kweli, na najaribu kupima mambo bila ya kuegemea upande wowote. Nilisema kuwa nilichopinga ni kufikiri kwa kujifunga na jamii iliyojifunga. Nilimwambia kuwa naheshimu haki ya kila mtu kuamini kile ambacho akili yake inamwambia ni sahihi, na natarajia kila mtu kuheshimu haki yangu ya kuamini namna hiyo.

Basi shushushu huyu mkubwa akaleta habari za imani za kidini za “Waislamu weusi.” Nilimuuliza iwapo makao makuu hawajamdokeza kuwa imani na mtazamo wangu umebadilika? Nilimwambia kuwa Uislamu ambao ninauamini sasa ni Uislamu unaofundishwa Mecca-kwamba hakuna Mungu ila Allah, na kuwa Muhammad ibn Abdullah ambaye aliishi Mecca miaka elfu moja na mia nne iliyopita alikuwa ndiye mtume wa mwisho wa Allah.

Tokea mwanzo nilikuwa nimehisi kitu fulani, niligusia na kumshtua kabisa shushushu yule. Kutokana na maongezi na maswali yake ya kuegemea upande fulani, nilitambua kitu fulani kumhusu na nikamwambia,“Unajua, nahisi kuwa wewe ni Myahudi mwenye jina la Kiingereza.” Muitikio wake ulinionyesha kuwa nimepiga penyewe. Aliniuliza nimejuaje. Nilimwambia kuwa ninauozoefu na jinsi ya kuwatambua Wayahudi kwa jinsi walivyonishambulia. Nilimwambia tatizo langu pekee na Wayahudi ni unafiki wao wa kujifanya rafiki wa watu weusi wa Marekani, na kuwa inanikera kuitwa “mchukia Wayahudi” pale ninapoongea mambo ninayofahamu kuwa kweli kabisa kuhusu Wayahudi. Nilimwambia kuwa ninawasifu Wayahudi kwa kuwa kati ya watu weupe wachakarikaji, wenye sauti, na wanaojitolea kifedha kwenye harakati za mtu mweusi wa Marekani. Lakini nilimwambia kuwa Wayahudi wanafanya yote hayo kwa sababu maalumu: Kadri ambavyo ubaguzi na unyanyapaa unavyoelekezwa kwa mtu mweusi wa Marekani, ndivyo ambavyo unyanyapaa wa mzungu unavyopungua kwa Wayahudi. Nilisema kuwa kwangu mimi, uhusikaji wa Wayahudi kwenye harakati za mtu mweusi kudai haki ulikuwa ni wa kinafiki maana huko kaskazini ni Wayahudi wenyewe ndiyo wa kwanza kufanya ubaguzi wa kutenga watu kulingana na rangi. Tazama kwenye karibu kila kitu ambacho mtu mweusi anajaribu kuleta “uchangamano,” utaona kuwa kama Wayahudi si wamiliki, basi wanakiendesha au wana hisa kubwa na wako kwenye nafasi ya maamuzi. Je wanatumia nafasi zao kupinga ubaguzi? Hapana.

Na kumpa ushahidi wa wazi kabisa wa jinsi Wayahudi wanavyowachukulia watu weusi nilimwambia juu ya kile kinachotokea watu weusi wanapohamia kwenye maeneo ya watu weupe ambao wengi wao ni Wayahudi. Ni nani ambaye siku zote huongoza watu weupe kuhama? Wayahudi! Wakati mwingine baadhi ya watu weupe hubaki kwenye maeneo haya. Utawaona Wairish, Wakatoliki, Waitaliano; lakin ni ngumu kuwakuta Wayahudi. Na cha kuchekesha ni kuwa Wayahudi wenyewe wanapata wakati mgumu sana “kukubalika.”

Najua kwa kusema haya nitasikia tena kelele za “mchukia Wayahudi” kutoka kila kona. Lakini ukweli utabaki kuwa ukweli.

Safari hii nilipokuwa ng’ambo siasa ndizo zilikuwa zimetawala Marekani. Nilipokuwa Cairo na tena Accra, vyombo vya habari vya Marekani vilinitafuta kwa simu, wakiniuliza namuunga mkono nani kati ya Johnson na Goldwater?

Nilisema kuwa kulingana na hali ya mtu mweusi wa Marekani, wote wako sawa tu. Nilihisi kuwa kwa mtu mweusi ilikuwa ni suala na Johson—mbweha mjanja au Goldwater— mbwa mwitu mwenye kunyafua.
“Uhafidhina” wa Marekani unamaanisha, “Tuwadhibiti watu weusi waendelee kuwa walivyo.” “Uliberali” unamaanisha, “Acha tuwadhibiti watu weusi kwenye nafasi yao lakini tuwaambie kuwa tutawatendea vyema kidogo; tuwadanganye tena kwa ahadi zaidi.” Kwa machaguo haya mawili, nahisi mtu mweusi anatakiwa kuchagua aliwe na nani, mbweha “mliberali” au mbwa mwitu “mhafidhina” maana ukweli ni kuwa wote watamla.

Sikumuunga mkono Goldwater kama ambavyo sikumuunga mkono Johnson, lakini walau kwenye pango la mbwa mwitu nitakuwa na tahadhari zaidi. Nitamuangalia mbwa mwitu hatari kwa ukaribu zaidi kuliko mbweha mwenye hila. Kuunguruma tu kwa mbwa mwitu kutanifanya niwe chonjo na kunifanya nipambane naye ili kuishi, lakini mbweha anaweza kunidanganya kwa hila. Nitakupa mfano mmoja wa mbweha. Mauaji wa Rais kule Dallas yalipomfanya Johnson kuwa Rais, ni nani alimpigia simu yake ya kwanza? Alikuwa ni rafiki yake kipenzi, “Dicky”-Richard Russell wa Georgia. Harakati za haki za kiraia ni suala la “kimaadili” Johnson alimwambia kila mtu huku rafiki yake kipenzi ni mbaguzi wa rangi kutoka kusini aliyeongoza mapambano dhidi ya haki za kiraia. Angechukuliwaje polisi ambaye anatangaza waziwazi kuwa anapinga uporaji kwenye mabenki na wakati huo huo rafiki yake kipenzi ni Jesse James?

Nilimheshimu Goldwater kwa kuongea mtazamo wake waziwazi-kitu ambacho ni adimu sana kwenye siasa za siku hizi. Hakuwa ananon’gona na wabaguzi wa rangi huku akitabasamu mbele za wanaohubiri uchangamano. Niliona kuwa Goldwater alipaswa kusema waziwazi mtazamo wake ili kukubalika, aliwaambia watu weusi waziwazi kuwa hayuko pamoja nao, na kuna jambo la kuangalia kutoka kwenye hilo: siku zote watu weusi wamepiga hatua pale walipoona kuwa wanatakiwa kusimama na kupambana dhidi ya mfumo ambao waliona wazi kuwa upo dhidi yao. Chini ya nyimbo tamu za mbweha waliberali, mtu mweusi wa Kaskazini amefanywa kuwa ombaomba. Lakini mtu mweusi wa kusini anayekabiliana na mzungu anayebweka. Amesimama na kupambana na mzungu huyo kwa ajili ya uhuru wake-miaka mingi kabla mapambano kama hayo hayajatokea kaskazini.

Vyovyote vile, sikuhisi yoyote kati ya Johnson au Goldwater atakuwa bora kwa watu weusi. Sikuwepo Marekani wakati wa uchaguzi, lakini hata ningekuwepo nisingempigia kura yeyote kati yao kuwa Rais, wala nisingemshawishi mtu mweusi yeyote kufanya hivyo. Matokeo ya kura yameonyesha Johnson ndiye mshindi-na kura za watu weusi zilikuwa sababu kubwa ya ushindi wake. Kama Goldwater ndiye angeshinda, ninasema kuwa walau watu weusi wangefahamu kuwa wanapambana na mbwa mwitu anayenguruma badala ya mbweha na kujikuta wameshaliwa nusu kabla hawajajua nini kinaendelea.

Nilipata kila aina ya matatizo nilipokuwa najaribu kuunda Taasisi ya Umoja wa watu weusi. Kwa nini umoja wa watu weusi? kwenye mazingira ya ushindani ya Marekani, kunawezekanaje kuwa na umoja kati ya wazungu na watu weusi kabla ya kuwepo umoja kati ya watu weusi wenyewe? Kama unakumbuka, utotoni mwangu nilisikia mafundisho ya umpoja wa watu weusi yake Marcu Garvey-mafundisho niliyoambiwa yalipelekea kuuawa kwa baba yangu. Hata nilipokuwa mfuasi wa Elijah Muhammad, nilifahamu vyema jinsi ambavyo umoja wa watu weusi kiuchumi, kisiasa na kijamii unavyoweza kumfanya mtu mweusi ajivunie rangi yake, kujiheshimu na kujiamini ambako watu weusi wa leo waliopiga magoti wanakuhitaji sana ili kusimama.

Moja ya tatizo kubwa nililokabiliana nao katika jitihada zangu za kuunda taasisi niliyoitaka-taasisi ya watu weusi wote ambayo lengo lake kuu litakuwa ni kuunda jamii ambayo kuna undugu wa kweli kati ya watu weusi na wazungu- lilikuwa ni picha yangu ya awali ambayo umma ulikuwa nayo, picha yangu ya “Muislamu Mweusi” iliendelea kuwa kikwazo kwangu. Polepole nilijaribu kubadili picha hiyo. Nilijaribu kuwapatia watu picha mpya, hasa watu weusi. Si kwamba sikuwa na hasira kama zamani, lakini undugu wa kweli nilioshuhudia kwenye Ulimwengu Mtakatifu ulinifanya nione kuwa hasira zinaweza kumpofusha mtu.
Kila fursa niliyopata, niliongea na watu mashuhuri wa Harlem, na nilitoa hotuba nikisema kuwa: ‘Uislamu wa kweli umenifundisha kuwa jamii na familia kamili ya binadamu inaundwa na mambo yote, ya kidini, kiuchumi, kisisas, kisaikolojia na kitamaduni.’

“Toka nimejifunza kweli katika jiji la Mecca, nimepata rafiki wa dhati kutoka kwa watu wa kila aina-Wakristo, Wayahudi, Wabudha, Wahindu na hata wasioamini Mungu! Nina rafiki wanaoitwa Mabepari, Wajamaa na Wakomunisti! Baadhi ya rafiki zangu ni wenye msimamo wa wastani, wahafidhina, wenye misimamo mikali na hata baadhi ni vibaraka! Rafiki zangu leo ni weupe, weusi, wa kahawia, wekundu na wamanjano!”
Niliuambia umati kwenye mitaa ya Harlem kuwa ni pale tu binadamu watakapo jiweka chini ya Mungu mmoja muumba vyote, ni hapo tu ndipo binadamu ataikaribia “amani” ambayo inazungumzwa sana . . . amani ambayo ni jitihada kidogo sana zinafanywa kuifikia.

Nilisema kuwa mahali ambapo tatizo la ubaguzi wa rangi lilipofikia katika Marekani, tunatakiwa kulikabili tatizo la mzungu kumbagua mtu mweusi kama tatizo la kibinadamu, kwamba tunatakiwa kuachana na unafiki wa kisiasa na propaganda. Nilisema kuwa watu wa rangi zote-kama binadamku wanawajibu wa kutatua tatizo la kibinadamu lililopo ndani ya Marekani. Nilisema kuwa wazungu wenye nia njema wanatakiwa kupambana vikali na ubaguzi uliopo ndani ya wazungu wengine. Na kuwa watu weusi wanatakiwa kutambua kuwa uwepo wa haki sawa unakuja sambamba na wajibu sawa.

Nilifahamu vyema kuliko watu weusi wengi jinsi ambavyo wazungu wengi wanataka tatizo la ubaguzi wa rangi ndani ya Marekani litatuliwe. Nilifahamu kuwa wazungu wengi walitatizika kama tu watu weusi. Nadhani kuwa kuna baadhi ya siku nilipokea barua hadi hamsini kutoka kwa wazungu. Baada ya hotuba zangu kuna wazungu walinizonga na kuniuliza, “Mzungu mwenye nia njema anaweza kufanya nini?”

Ninaposema jambo hili sasa kumbukumbu zangu zinarudi kwa yule mwanafunzi wa ualimu niliyekusimulia. Yule aliyepanda ndege kutoka chuoni kwake New England hadi New York, na kunifuata Harlem kwenye mgahawa wa Taifa la Kiislamu na nikamwambia kuwa “hakuna” kitu anaweza kufanya. Ninajuta kuwa nilimjibu namna ile. Leo natamani ningefahamu jina lake au namna ya kumpigia simu au kumuandikia barua na kumwambia yale ninayowaambia wazungu wenye nianjema leo wanaponifuata na kuniuliza kitu kilelekile alichoniuliza.

Kitu cha kwanza ninachowaambia ni kuwa taasisi yangu ni taasisi ya wamarekani wenye asili ya Afrika hivyo hawataweza kujiunga. Nimekuwa na mtazamo kuwa wazungu wanaojiunga na taasisi za watu weusi, hufanya hivyo ili tukusafisha dhamira zao. Kwa kuonekana pamoja nasi wanakuwa wanaonyesha kuwa wako “pamoja nasi.” Lakini ukweli mchungu ni kuwa hilo halisaidii katika kutatua tatizo la ubaguzi wa rangi ndani ya Marekani. Si watu weusi wanaofanya ubaguzi wa rangi. Sehemu ambayo wazungu wenye nia njema wanatakiwa kujithibitisha si kati ya wahanga weusi bali kule ambako mapambano dhidi ya ubaguzi wa rangi wa Marekani yapo, kwenye jamii zao wenyewe; ubaguzi wa rangi ndani ya Marekani upo kwa wazungu wenzao. Huko ndiko wazungu wenye nia njema na wanaotaka kutimiza kitu cha maana wanatakiwa kwenda.

Mbali na hilo, sina jambo jingine lolote dhidi ya wazungu wenye nia njema pale ninaposema kuwa uwepo wa wazungu kwenye taasisi ya watu weusi unaifanya taasisi hiyo isifanye kazi yake vyema. Hata wazungu wema kabisa watawafanya watu weusi washindwe kutambua nini wanatakiwa kufanya, na hasa ni nini wanaweza kujifanyia wao wenyewe wanapofanya mambo yao wenyewe-kwenye jamii zao.

Sina nia kabisa ya kuumiza hisia za mtu yeyote, lakini ukweli ni kuwa sijawahi waamini wazungu ambao wanatamani sana kujumuika na watu weusi au kwenye maeneo ya watu weusi. Siamini wazungu wanaopenda watu weusi wawe karibu yao muda wote. Sijui hisia hizi zilikotoka- labda ni kutoka kipindi kile nilipokuwa mpambanaji kwenye mitaa ya Harlem, na wale wazungu waliokuwa wamelewa kwenye clubs zinazokesha ambao walikuwa wakimshika mtu mweusi na kuanza kusema, “Nataka utambue kuwa wewe ni bora kama mimi tu-” kisha wakaingia kwenye magari na kurudi mjini-kati wanakoishi na kufanya kazi, mahali ambako watu weusi hawatakiwi isipokuwa vijakazi wao. Mbali na hilo, nafahamu vyema kuwa pale wazungu wanapojiunga kwenye taasisi ya watu weusi, haichukui muda mrefu watu weusi wanaanza kuwategemea wazungu hao kuigharamia taasisi hiyo, na kufumba na kufumbua mtu mweusi anakuwa tu sura ya taasisi lakini wazungu sababu ya pesa zao wanakuwa hasa ndiyo wenye sauti.

Huwa ninawaambia wazungu wenye nia njema, “Fanyeni kazi sambamba nasi-kila mmoja akifanya kwenye jamii yake.” Wazungu wenye nia njema wawatafute wenzao wenye mtazamo kama wao na waunde taasisi yao ya wazungu tu, na hiyo ifanye kazi ya kuwageuza wazungu wengine wenye mawazo na matendo ya kibaguzi. Wazungu wenye nia njema wakawafundishe wazungu wengine kutotumia vurugu!
Tutawaheshimu kabisa wazungu wanaofanya kazi moja nasi. Watahitaji sifa zote nasi tutawapa sifa zote. Lakini wakati huo huo sisi tutakuwa tunafanya kazi kati ya watu wetu, kwenye jamii zetu za watu weusi-tukiwafundisha na kuwaelekeza watu weusi kwa namna ambayo ni mtu mweusi pekee anaweza kufundisha-kwamba mtu mweusi anatakiwa kujisaidia yeye mwenyewe. Pamoja na kila mtu kufanya kazi na watu wake, wazungu na watu weusi wenye nia njema watakuwa wanafanya kazi moja.

Kwa pamoja bila unafiki tunaweza kuionyesha jamii ya Marekani njia ya wokovu. Na inaweza kuokolewa pale tu haki na heshimu ya kibinadamu vitakapowafikia watu weusi. Ni matendo hayo tu yanayoongozwa na ubinadamu na maadili ndiyo yanaweza kugusa kiini kinachosababisha tatizo la ubaguzi wa rangi ndani ya Marekani. Kinyume na hapo, tatizo la ubaguzi wa rangi ndani ya Marekani litazidi kukua. Na ukweli ni kuwa hakuna chochote kitakachotatuliwa kwa kuendelea kunilaumu mimi na watu weusi wanaoitwa “wenye msimamo mkali” na “demagogues” kwa ubaguzi wa rangi unaoendelea ndani ya Marekani.

Siku nyingine huwa hata naota-naota kuwa siku moja historia itasema kuwa sauti yangu, sauti iliyochachafya majivuno na majidai ya mzungu-ni sauti iliyosaidia kuiokoa Marekani kutoka kaburini.
Siku zote lengo limekuwa lile lile lakini njia za kulifikia zimekuwa tofauti sana, kama ilivyo kwa njia yangu na ya Dr. Martin Luther King na maandamano yake ya amani yasiyo na vurugu, maandamano ambayo huonyesha ukatili wa wazungu dhidi ya watu weusi wasio na ulinzi wowote. Na kwa jinsi mazingira ya ubaguzi yalivyo nchini hapa leo hii, mtu anaweza kuona ni njia gani ya kutatua tatizo la mtu mweusi wa Marekani itakomeshwa haraka, njia ya “amani” ya Dr King au ile yangu inayoitwa ya “vurugu.”

*******
 
Tafsiri ya kitabu The Autobiography of Malcom X. Unaweza kukisoma ndani ya Maktaba app.
View attachment 2728790

Muandishi: Malcom X(Alex Haley), 1965.

Mtafsiri: Pictus Publishers ltd

Email: pictuspublishers@gmail.com.

Whatsapp: 0715278384

©Pictus Publishers Ltd2023.

Sura ya kwanza
JINAMIZI​
Mama yangu alinisimulia kuwa alipokuwa na mimba yangu, usiku mmoja kundi la wabaguzi wa rangi la Ku Klux Klan lilifika kwa farasi nyumbani kwetu huko Omaha, Nebraska. Waliizingira nyumba yetu huku wakionyesha bunduki zao, walipiga kelele wakimtaka baba yangu atoke nje. Mama yangu alienda mlangoni na kufungua.

Akisimama sehemu ambayo waliweza kuona hali yake ya ujauzito, aliwaambia kuwa alikuwa peke yake na wanawe watatu wadogo, na kuwa baba yangu alikuwa amesafiri, ameenda kuhubiri huko Milwaukee. Watu wale walitoa vitisho na onyo wakisema ni vyema tukahama mji haraka kwa sababu “Wakristo wema wa Kizungu” hawatavumilia kuona baba yangu “akifanya uchochezi” kati ya Manegro “wema” wa Omaha kwa kutumia mahubiri ya “kurudi Africa” ya Marcus Garvey.

Baba yangu, mchungaji Earl Little alikuwa ni mchungaji wa kanisa la Baptist, mfuasi mtiifu wa chama cha Marcus Aurelius Garvey, U.N.I.A(Universal Negro Improvement Association(Chama cha Kuwainua Watu Weusi Duniani)). Kwa msaada wa mitume kama baba yangu, Garvey kutoka katika makao yake makuu huko Harlem, New York-alikuwa akitoa mwito juu ya ubora wa watu weusi na akiuhimiza umma wa watu weusi kurudi Afrika, nyumbani kwa mababu zao-kampeni iliyomfanya Marcus Garvey kuwa mtu mweusi mtata zaidi dunaini.

Huku wakiendelea kutoa vitisho, wabaguzi wale waliamrisha farasi wao kukimbia kuizunguka nyumba huku wao wakivunja vioo vyote vya madirishani kwa vitako vya bunduki. Kisha wakaenda zao, mioto yao iking’aa gizani kama walivyokuja.

Baba yangu aliporudi alikasirika sana. Aliamua kusubiri mpaka nitakapozaliwa-na wakati ulikuwa karibu, kisha ahamishe familia yake. Sijajua kwa nini alifanya uamuzi huu maana hakuwa Mnegro muoga kama ambavyo wengi walikuwa nyakati hizo, na bado wengi wako hivyo hadi hii leo.

Baba yangu alikuwa na mwili mkubwa, urefu wa futi sita na nchi nne na mweusi ti. Alikuwa na jicho moja tu zima. Mpaka leo sijajua nini kililipata lile lingine. Alikuwa ni mzaliwa wa Reynolds, Georgia ambako aliacha shule baada ya darasa la tatu au la nne. Aliamini-kama alivyoamini Marcus Garvey, kuwa mtu mweusi hawezi kupata uhuru, kujitegemea na kujiheshimu ndani ya Marekani, hivyo inampasa mtu mweusi kumuachia mtu mweupe Marekani na yeye kurudi Afrika alikotokea. Moja ya sababu iliyofanya baba yangu kutumia muda wake na kuhatarisha maisha yake kusambaza falsafa hii kati ya watu wake ni kuwa alikuwa ameshuhudia kaka zake wanne kati ya sita wakiuawa kikatili. Watatu kati yao wakiuawa na wazungu, akiwemo mmoja kwa kuuliwa na umati. Kitu ambacho baba yangu hakujua wakati ule ni kuwa, kati ya watatu waliobaki, yeye akiwemo, ni mmoja tu-mjomba Jim ndiye atakufa kifo cha kawaida kitandani.

Baadaye, polisi wa kizungu wa kaskazini ya Marekani walimpiga risasi mjomba wangu Oscar. Na mwishowe baba yangu mwenyewe alikufa kwa mikono ya wazungu.

Siku zote imekuwa ni imani yangu kuwa mimi pia nitakufa kikatili. Nimefanya kila niwezalo kujiandaa.

Nilikuwa mtoto wa saba kwa baba yangu. Alikuwa na watoto wengine watatu kutoka kwenye ndoa yake ya kwanza, Ella, Earl na Mary walioishi Boston.

Alikutana na kumuoa mama yangu huko Philadelphia, na huko ndiko mtoto wao wa kwanza, kaka yangu mkubwa Wilfred alizaliwa. Walihama kutoka Philadelphia kwenda Omaha ambako Hilda na Philbert walizaliwa.

Kisha nikafuata. Mama yangu alikuwa na miaka ishirini na nane nilipozaliwa tarehe 19/5/1925, kwenye hospitali huko Omaha. Kisha tukahamia Milwaukee ambako Reginald alizaliwa.

Toka uchanga wake amekuwa na aina fulani ya ugonjwa wa ngiri ambao ulimsumbua maisha yake yote.

Mama yangu, Louise Little alizaliwa huko Grenada, British West Indies. Mama yangu alionekana kama mwanamke wa kizungu. Baba yake alikuwa ni mzungu.

Alikuwa na nywele ndefu nyeusi, na ongea yake haikuwa kama ya mtu mweusi. Sijui chochote juu ya baba yake mzungu zaidi ya kuwa alijisikia aibu kuzaliwa naye. Nakumbuka kumsikia akisema kwamba hajawahi kumuona. Na ni kwa sababu yake ndiyo maana nina rangi hii ya ngozi na nywele.

Nilikuwa ndiye mtoto mweupe zaidi katika familia yetu(Baadaye maishani nilipokuwa huko Boston na New York, nilikuwa kati ya mamilioni ya watu weusi ambao walikuwa wehu hadi kufikiri kuwa ilikuwa ni aina fulani ya hadhi kuwa na weupe-na kuwa mtu alikuwa na bahati kuzaliwa hivyo. Lakini badaye zaidi nilikuja kuchukia kila tone la damu ya mzungu yule mbakaji ndani yangu).

Familia yetu haikukaa sana huko Milwaukee maana baba yangu alitaka kuishi sehemu ambayo tungepanda vyakula vyetu wenyewe na ambako angeweza kuanzisha biashara, na kuishi kulingana na mafundisho ya Marcus Garvey ya kutotegemea wazungu. Kwa sababu fulani, tulienda Lansing, Michigan.

Baba yangu alinunua nyumba, na ndani ya muda mfupi, kama kawaida yake, akaanza kujitolea kuhubiri kwenye makanisa ya kibapstisti ya watu weusi yaliyokuwepo eneo letu, na siku za juma alikuwa akizunguka akitangaza maneno ya Marcus Garvey.

Alikuwa ameanza kutunza pesa kwa ajili ya duka ambalo siku zote alikuwa ametamani kumiliki, kisha, kama kawaida, watu weusi fulani wapumbavu wa jamii ya Uncle Tom(Vibaraka) wakaanza kupeleka maneno kwa wazungu juu ya muelekeo wake wa kimapinduzi. Safari hii kitisho cha kutakiwa kuhama mji kilitoka kwa kikundi cha wabaguzi kilichoitwa the Black Legion, hawa walivaa kanzu nyeusi badala ya nyeupe. Haikuchukua muda ikawa kila mahali ambako baba yangu alikwenda, wanachama wa Black Legion walikuwa wakimfuata ili kumuumbua kama mnegro “mwenye kujifanya” kwa sababu ya kutaka kwake kufungua duka, kwa kuishi nje ya eneo la Lansing lililotengwa kwa ajili ya watu weusi na kwa kuchochea vurugu na uasi kati ya watu “weusi wema.”

Kama ilivyokuwa Omaha, wakati huu mama yangu alikuwa mjamzito tena, wakati huu ilikuwa mimba ya dada yangu mdogo. Muda mfupi baada ya Yvonne kuzaliwa, ulifika usiku wa kutisha wa mwaka 1929, kumbukumbu yangu ya kwanza ambayo bado ipo. Nakumbuka ghafla kubebwa juu juu katikati ya vurugu za milio ya bastola, kelele, moshi na moto. Baba yangu alikuwa akifoka na kupiga risasi kuelekea wazungu wawili waliokuwa wamewasha moto na sasa wakikimbia. Nyumba yetu ilikuwa ikiungua.

Tulikuwa tukikanyagana na kugongana tukijaribu kujiokoa. Nusura nyumba imuangukie mama yangu akiwa na mtoto mkononi, alikimbia kupitia mlango wa uani huku nyuma yake nyumba ikianguka na kurusha cheche huku na kule. Nakumbuka tukiwa nje usiku tukiwa na nguo zetu za ndani, tukilia na kupiga kelele. Polisi na askari wa zimamoto wa kizungu walifika na kusimama wakiangalia nyumba ikiteketea hadi chini.

Marafiki kadhaa walimsaidia baba yangu kutupa hifadhi na nguo kwa muda; kisha akatuhamishia kwenye nyumba fulani pembezoni mwa Mashariki ya Lansing. Wakati huo watu weusi hawakuruhusiwa kuwepo katikati ya Lansing Mashariki baada ya giza kuingia.

Huko ndiko ambako chuo kikuu cha Jimbo la Michigan kilikuwepo: nilisimulia haya yote nilipozungumza na wanafunzi wa chuo hicho mwezi wa kwanza mwaka 1963(Na nilikutana na mdogo wangu Robert baada ya kipindi kirefu cha kutoonana, alikuwa pale akichukua masomo ya juu ya saikolojia).

Niliwaeleza jinsi ambavyo Lansing Mashariki ilitunyanyasa hadi tukalazimika kuhama tena, wakati huu tukienda maili mbili nje ya mji. Huko ndiko ambako baba yetu kwa mikono yake mwenyewe alitujengea nyumba ya vyumba vinne.

Huko ndiko nilikoanza kukumbuka mambo, hiyo ndiyo nyumba niliyokulia.

Nakumbuka baada ya tukio la moto, baba yangu aliitwa na kuhojiwa juu ya kibali cha bastola ambayo alifyatulia wazungu wawili waliowasha moto.

Nakumbuka mara nyingi polisi walikuwa wakifika nyumbani kwetu na kurusha vitu huku na kule, wakitafuta bastola. Bastola waliyokuwa wakiitafuta, ambayo hawakuwahi kuipata, na ambayo hawangeweza kumpa baba yangu kibali cha kuimiliki-ilikuwa imeshonewa ndani ya mto.

Lakini bunduki ya baba yangu na gobole lake vilikuwa peupe tu; kila mtu alikuwa navyo kwa ajili ya kuwindia ndege, sungura na wanyama wengine.

Baada ya hapo, kumbukumbu zangu ni juu ya mizozo kati ya baba na mama yangu.

Ilionekana kama walizozana muda wote. Wakati mwingine baba yangu alimpiga mama. Pengine ilitokana na kuwa mama yangu alikuwa na elimu nzuri.

Sijui alikoipata, lakini nafikiri mwanamke mwenye elimu hawezi zuia kishawishi cha kumsahihisha mwanaume asiye na elimu. Mara moja moja alikuwa akimsahihisha naye baba hakusita kumkunja.

Baba yangu alikuwa pia mkali sana kwa watoto wake wote isipokuwa mimi. Ndugu zangu wakubwa walipigwa kikatili kila walipovunja sheria zake-na alikuwa na sheria nyingi hivyo haikuwa rahisi kuzifahamu zote.

Karibu vipigo vyangu vyote vilitoka kwa mama yangu. Nimejiuliza sana kwa nini? Naamini kabisa kuwa, pamoja na kuwa baba yangu alikuwa mpinga wazungu, lakini kwenye akili yake alikuwa ameathirika na mtazamo wa wazungu kiasi kwamba alipendelea watoto weupe, na kati ya watoto wake mimi ndiye niliyekuwa mweupe zaidi.

Wazazi wengi weusi wa wakati huo walikuwa wakiwatendea watoto weupe kwa upendeleo kuliko wale weusi. Hii ilitoka moja kwa moja wenye utamaduni wa wakati wa utumwa kuwa “chotara” kwa sababu alikuwa anafanana na mtu mweupe kwa karibu, basi alikuwa bora.

Kumbukumbu zangu nyingine mbili juu ya baba yangu ni nje ya nyumbani. Moja ni juu ya kazi yake kama mhubiri wa Kibapstisti. Hakuwahi kuwa mchungaji mwenye kanisa lake mwenyewe; siku zote alikuwa ni “mhubiri mualikwa” nakumbuka mahubiri yake maarufu aliyopendelea sana, “treni ndogo nyeusi inakuja. . . na ni vyema ukaweka mambo yako yote sawa!” Nadhani kuwa hili lilihusiana na kampeni ya Marcus Garvey ya kurudi Afrika, ikiwa na kaulimbiu, “Treni nyeusi kuelekea nyumbani.” Philbert, kaka yangu ambaye alikuwa amenipita umri kidogo tu, alipenda sana habari za kanisa, lakini mimi zilinichanganya na kunishangaza.

Nilikuwa nikikaa nimemtumbulia macho baba yangu akiruka na kufoka alipokuwa akihubiri huku kanisa zima likiruka na kupiga kelele nyuma yake, likiwa limejitoa roho na mwili kwenye kuimba na kusali.

Hata katika umri huo mdogo, sikuweza kuamini dhana ya Wakristo kuwa Yesu ana uungu. Na hakuna mtu yeyote wa kidini, hadi nilipokuwa mtu mzima wa miaka ishirini-na baadaye nikiwa gerezani, aliyeweza kunieleza chochote.

Niliwaheshimu kidogo sana watu waliowakilisha dini.

Ni kupitia kazi yake hii ya uhubiri ndipo baba yangu aliweza kukutana na watu wengi weusi walioishi Lansing.

Niamini ninapokuambia kuwa Manegro wale walikuwa na hali mbaya sana wakati huo. Bado hata sasa wana hali mbaya-japo ni kwa namna nyingine. Kwa kusema hivyo, namaanisha kuwa sijawahi kuona mji ambayo una asilimia kubwa zaidi ya watu weusi wanaoitwa wa “daraja la kati” walioridhika na waliopotoshwa –watu weusi watafuta hadhi na kuchangamana.

Hivi karibuni nilikuwa nimesimama kwenye sehemu ya mapokezi ya Umoja wa Mataifa nikiongea na balozi kutoka nchi ya Afrika na Mke wake. Mtu mweusi mmoja alinifuata na kusema, “Unanifahamu?”

nillifedheheka kidogo sababu nilifikiri labda ni mtu ninayepaswa kumfahamu. Kumbe ni mmoja wa wale Manegro wa “daraja la kati” wanaojisifu na kuridhika kutoka Lansing. Sikujisikia vizuri.

Alikuwa ni aina ya mtu mweusi ambaye kamwe hangeweza kujihusisha na Afrika hadi pale kitendo cha kuwa na rafiki wa kiafrika kilipokuwa kama fasheni kati ya watu weusi wa “daraja la kati.”

Zamani nilipokuwa nakua, watu weusi wa Lansing waliokuwa na “mafanikio” walikuwa ni wahudumu na wang’arisha viatu.

Kuwa mfanya usafi kwenye duka fulani mjini ilifanya mtu aheshimike sana. Watu wa “maana,” “wakuu,” “wasemaji wa watu weusi,” walikuwa ni wahudumu wa Lansing Country Club na wang’arisha viatu kwenye makao makuu ya jimbo.

Watu weusi pekee waliokuwa na pesa kiukweli walikuwa ni wachezesha kamari au ambao kwa namna fulani waliishi kwa kunyonya masikini zaidi, na masikini walikuwa wengi sana. Wakati ule hakuna mtu mweusi aliyeajiriwa na kiwanda cha magari cha Lansing au kiwanda cha Reo. (Unakumbuka magari ya Reo? Yalitengenezwa Lansing na R. E. Olds, mtu ambaye yaliitwa jina lake, aliishi Lansing. Vita ilipoingia, waliajiri wafanya usafi kadhaa weusi.) Sehemu kubwa ya watu weusi ilitegemea msaada wa serikali, au W.P.A(Works Projects Adminstration)., au iliteseka kwa njaa.

Siku ilifika ambayo familia yetu ilikuwa masikini hadi tulikula tundu la donati; lakini wakati huo tulikuwa na hali nzuri kidogo kulinganisha na watu weusi wengine. Sababu kubwa ni kuwa tulizalisha sehemu kubwa ya chakula chetu wenyewe huko nje ya mji tulikokuwa.

Tulikuwa na afadhali kuliko watu weusi wa mjini ambao walipiga kelele, kama baba yangu alivyosema kwenye mahubiri yake, juu ya keki angani na mbingu yao baadaye wakati mzungu anayo yake hapahapa duniani.

Nilifahamu kuwa michango ambayo baba yangu alipata kwenye kazi yake ya kuhubiri ndiyo hasa ilitulisha na kutuvisha, na pia alifanya kazi zingine za ajabu, lakini picha yake inayofanya nijivunie zaidi ni harakati na upambanaji wake juu ya maneno ya Marcus Garvey.

Pamoja na udogo wangu niliokuwa nao, nilifahamu kutokana na niliyosikia kwamba baba yangu alikuwa akiongea mambo yaliyomfanya awe “shupavu.” Nakumbuka mwanamke mzee mmoja akitabasamu na kumwambia baba yangu, ‘Unawaogopesha wazungu, wako karibu kufa.’

Moja ya sababu zinazofanya nihisi kuwa baba yangu alikuwa akinipendelea ni kuwa, kulingana na kumbukumbu zangu, ilikuwa ni mimi tu ndiye aliyenichukua kwenda naye kwenye mikutano ya chama cha Garvey, U. N. I. A ambayo aliifanya kwa siri kwenye nyumba za watu tofautitofauti. Mikutano hiyo haikuwa na watu wengi, hawakuzidi ishirini.

Lakini hao walikuwa ni wengi sana kwenye sebule ya mtu. Nilitambua walivyokuwa tofauti wakati wa mikutano hii japo ni watu walewale waliokuwa wakiruka na kupiga kelele kanisani. Kwenye mikutano hii, wote-kutia ndani baba yangu, walikuwa makini sana, wenye akili zaidi na wanyenyekevu. Hili lilinifanya nami nijihisi namna hiyohiyo.

Nakumbuka kusikia, “Adam alifukuzwa kwenye bustani ya Eden kwenda kwenye mapango ya Ulaya,” “Afrika kwa waafrika,” ‘Waethiopia amkeni!” Kisha baba yangu angeongea kwamba haitachukua muda mrefu Afrika yote itaongozwa na mtu mweusi. Alipendelea kutumia neno “mtu mweusi” badala ya Negro.

“Hakuna anayejua wakati ambao saa ya ukombozi wa afrika itafika. Ipo kwenye upepo inakuja. Siku moja, kama tufani itafika.”

Nakumbuka kuona picha kubwa za kung’aa za Marcus Garvey zikipitishwa kwa kupasiana mikononi. Baba alikuwa na bahasha kubwa ya kuzihifadhi ambayo mara zote aliibeba kwenye mikutano hii. Kwenye picha zile, niliona kama mamilioni ya watu weusi wakiwa wamesongamana nyuma ya Marcus Garvey aliyekuwa amepanda gari zuri sana.

Mtu mweusi mkubwa akiwa amevalia sare nadhifu iliyokuwa na mapambo ya dhahabu, na pia alivalia kofia nzuri ikiwa na manyoya marefu. Nakumbuka nilisikia kuwa ana wafuasi weusi si tu katika Marekani bali duniani kote, na nakumbuka jinsi mikutano ilivyoisha mara nyingi kwa baba yangu kusema, huku watu wakimfuatisha; “Simama ewe mtu mkuu, utatimiza unachotaka!”

Sijawahi elewa kwanini baada ya kusikia mambo haya, kwa namna fulani, wakati huo; sikufikiria juu ya watu weusi wa Afrika. Picha yangu juu ya Afrika wakati huo ilikuwa ni washenzi walio uchi, wala watu, nyani, simba na misitu yenye joto.

Kwenye ziara zake baba yangu alitumia gari yake kuukuu iliyokuwa na rangi nyeusi, wakati mwingine alinichukua na tukaenda wote kwenye maeneo mbalimbali yaliyozunguka Lansing. Nakumbuka mkutano mmoja wa mchana(Mikutano mingi ilifanyika usiku) kwenye mji wa Owosso, umbali wa maili arobaini kutoka Lansing, mji ambao watu weusi waliuita “Mji mweupe” (Jambo kubwa ambalo Owosso ilijivunia ni kuwa mji wa Thomas. E. Dewey).

Kama ilivyokuwa East Lansing, watu weusi hawakuruhusiwa kutembea usiku, ndiyo sababu ya kufanya mkutano mchana. Na ukweli ni kuwa, miji mingi ya Michigan ilikuwa hivyo wakati huo. Kila mji ulikuwa na watu weusi wachache walioishi hapo. Wakati mwingine ilikuwa ni familia moja tu, kama ilivyokuwa kwenye makao makuu ya county, Mason. Huko kulikuwa na familia moja tu ya watu weusi, familia ya Lyon. Bwana Lyon alikuwa ni mcheza mpira maarufu wa shule ya sekondari ya Mason, aliheshimika sana huko Mason. Sa sasa alikuwa akiishi mjini humo akifanya vibarua vya hapa na pale.

Wakati huo mama yangu alionekana kama vile muda wote alikuwa akifanya kazi, akipika, akifua, akipiga pasi, akisafisha nyumba na kupigishana kelele na sisi watoto wake nane, na kawaida alikuwa akibishana au amenuniana na baba yangu. Moja ya chanzo cha mizozo yao ilikuwa ni mama yangu kuwa na msimamo mkali juu ya vitu ambavyo hataki kula, na wala hataki sisi tule, mfano nguruwe na sungura, vitu ambavyo baba yangu alivipenda sana.

Alikuwa ni mtu mweusi kutoka Georgia na aliamini katika kula vya kutosha chakula ambacho hapa Harlem tunaita “Chakula cha roho.”

Nimesema kuwa mama yangu ndiye aliyekuwa akinichapa-Lakini ilimbidi kufanya hivyo wakati ambao angeepuka aibu kutoka kwa majirani ambao wangeweza dhani kuwa alikuwa akitaka kuniua.

Kila alipojaribu kuinua mkono kunichapa, nilifungua mdomo na kupiga kelele za kufanya dunia yote ijue. Kama kuna mtu alikuwa anapita barabarani, basi angehairisha au angenichapa fimbo chache tu.

Nikiwaza kuhusu hilo leo, nahisi kuwa, kama ambavyo baba yangu alinipendelea kwa kuwa mweupe kuzidi wengine, mama yangu aliniadhibu vikali kwa sababu hiyohiyo.

Yeye mwenyewe alikuwa mweupe lakini aliwapendelea watoto waliokuwa weusi zaidi. Nafahamu kuwa kipenzi chake alikuwa ni Wilfred.

Nakumbuka alikuwa akiniambia nitoke ndani na “Acha miale ya jua ikupige ili upate rangi kidogo.”

Bidii yake katika kunifanya nisijihisi bora kutokana na rangi yangu ilivuka mipaka. Nina hakika alinitendea hivi kutokana na jinsi yeye mwenyewe alivyopata kuwa mweupe.

Nilijifunza mapema maishani kuwa kupiga kelele kunaweza kusaidia. Kaka zangu wakubwa na dada yangu walikuwa wameanza shule, wakati mwingine walikuwa wakirudi toka shule na kuomba biskuti zenye siagi au kitu fulani, kwa mkato mama yangu aliwajibu hapana. Lakini mimi nikikataliwa nililia na kufanya fujo mpaka nipate ninachotaka. Nakumbuka vizuri mama yangu akiniuliza kwa nini siwi mtoto mwema kama Wilfred; lakini nilijiambia mwenyewe, Wilfred kwa kuwa mwema na mkimya kulimfanya ashinde njaa mara nyingi. Hivyo basi, ingali bado mdogo sana nilijifunza kuwa kama unataka kitu fulani ni vyema ukapiga kelele.

Hatukuwa tu na bustani kubwa, bali pia tulifuga kuku. Baba yangu alinunua vifaranga na mama alivilea. Sote tulipenda kuku. Hicho ndicho chakula pekee ambacho hakukuwa na ubishani kati ya mama na baba. Kitu kimoja ambacho kinanifanya nimshukuru mama yangu ni hiki, siku moja nilimfuata na kumuomba niwe na bustani yangu na akaniruhusu kuwa na kitalu changu mwenyewe.

Nilikipenda na nilikihudumia vizuri sana. Nilipenda zaidi kupanda njegere. Nilijivuna sana tulipozila mezani petu. Niling’oa magugu kwenye bustani yangu kwa mikono mara tu yalipochomoza.

Nilikagua matuta nikiwa nimepiga magoti kuangalia minyoo na wadudu. Niliwaua na kuwazika. Wakati mwingine ambapo kila kitu kilikuwa safi na sina cha kupanda, nililala katikati ya matuta na kuangalia anga la bluu na mawingu yanayosafiri huku nikiwaza mambo mbalimbali.

Baada ya kufikisha miaka mitano nami pia nikaanza shule, nikiondoka nyumbani asubuhi pamoja na Wilfred, Hilda na Philbert. Shule yetu ilianzia chekechea hadi darasa la nane.

Ilikuwa umbali wa maili mbili kutoka mjini, nafikiri hakukuwa na shida sisi kusoma pale kwa sababu tulikuwa ndiyo watu weusi pekee kwenye eneo lile.

Kipindi hicho wazungu wa kaskazini walikuwa na kawaida ya”kuasili” watu weusi wachache kwenye jamii yao; hawakuwaona kama kitisho. Watoto wa kizungu hawakutufanyia ubaguzi mkubwa. Walituita “nigger” “weusi” na “Rastus” mara nyingi kiasi kwamba tulidhani hayo ndiyo majina yetu ya asili. Lakini hawakusema hivyo wakiwa na lengo la kututusi, ni namna tu waliyofikiria kutuhusu.
***​
MWANAUME!
Kudos mtoa mada!
 
Sura ya 19 inaendelea.

Leo hii kila jambo ninalolifanya ninalichukulia kuwa ni la dharura. Hakuna mtu anayepewa muda mwingi zaidi ya ule wa kukamilisha kile ambacho ni lengo lake maishani. Kamwe maisha yangu hayajakuwa ya aina moja kwa muda mrefu. Umejionea jinsi ambavyo maisha yangu yamebadilika badilika.

Nafahamu ukweli kuwa naweza kufa muda wowote ule. Hili limekuwa wazi zaidi tokea nifanye ziara ile nje ya Marekani. Nimeona jinsi mambo yalivyo na nimesikia mambo kutoka kwenye vyanzo vya kuaminika.

Fikra za kwamba nitakufa hazinisumbui kama ambavyo zinawasumbua watu wengine. Sikuwahi waza kuwa nitaishi hadi kuwa mzee. Hata kabla ya kuwa Muislamu-nilipokuwa mpambanaji kwenye maeneo ya maghetto, na baadaye kuwa mfungwa gerezani, siku zote nilijua kichwani mwangu kuwa nitakufa kifo cha kuuawa. Ukweli ni kuwa jambo hilo lipo kwenye familia yetu. Baba yangu na sehemu kubwa ya ndugu zake walikufa vifo vya kuuawa-baba yangu sababu ya kile alichoamini. Kwa hiyo nikiangalia mambo ninayoamini na nikiongeza suala la hasira zangu, jumlisha ujitoaji wangu wa asilimia mia moja kwa kitu chochote ninachoamini-naona mambo hayo yanafanya isiwezekane kabisa kwangu kufa kifo cha uzee.
***

Nimekipa kitabu hiki muda wangu mwingi sababu ninahisi kabisa kuwa kama nikisimulia maisha yangu, na kikisomwa kwa nia njema, basi nafikiri msomaji anayetafuta ukweli ataona kuwa kwenye jamii niliyoishi kama kijana mweusi hapa Marekani, suala la kwenda gerezani lilikuwa haliepukiki. Hilo linatokea kwa maelfu elfu ya vijana weusi.

Nafikiri msomaji anayetafuta ukweli ataona jinsi gani niliposikia kuwa “mzungu ni shetani” na kutafakari yaliyonipitia maishani-ilikuwa haikwepeki kwangu kukubaliana na hilo na kisha kutumia miaka kumi na mbili iliyofuata nikifanya bidii kufundisha watu weusi jambo hilo.

Ninafikiri na ninatumaini kuwa msomaji anayetafuta ukweli baada ya kufuatilia simulizi ya maisha yangu, atapata picha nzuri zaidi juu ya maeneo ya maghetto ya watu weusi, na jinsi yanavyoathiri maisha na kufikiri kwa watu weusi milioni 22 wa Marekani kuliko ile aliyokuwa nayo hapo kabla.

Kila mwaka maghetto hayo yanajaa vijana kama nilivyokuwa mimi-wakiiga mifano ya watu wasiofaa na kushawishiwa kufuata mambo yasiyofaa. Sisemi kuwa wote watakuwa mtu wa ovyo kama nilivyokuwa. Bahati nzuri wengi sana hawatakuwa hivyo. Lakini wale wachache wanaogeukia utukutu wanazidi kuongeza idadi ya wahalifu vijana. Muda si mrefu F.B.I wametoa taarifa inayoonyesha kuwa tokea mwisho wa Vita ya Pili ya Dunia kumekuwa na ungezeko kubwa la uhalifu, ongezeko la asilimia kumi hadi kumi na mbili kila mwaka. Taarifa hiyo haikueleza zaidi lakini nasema kuwa sehemu kubwa ya ongezeko la uhalifu huo linatoka kwenye maeneo ya maghetto ya watu weusi ambayo jamii ya kibaguzi ya Marekani imeacha yaendelee kuwepo. Kwenye vurugu za majira ya joto ya mwaka 1964, katika majiji makubwa mbalimbali ya Marekani, vijana weusi waliotengwa na jamii ndiyo walikuwa mstari wa mbele.

Katika mwaka huu wa 1965, nina hakika vurugu nyingi na mbaya zaidi zitalipuka kwenye majiji mengi zaidi, licha ya kupitishwa kwa muswada wa haki za kiraia. Sababu ya vurugu hizi ni kuwa kansa ya ubaguzi wa rangi ndani ya Marekani imeachwa kwa muda mrefu bila ya kushughulikiwa.

Naamini kuwa inaweza kuwa ni vigumu kumpata mtu mweusi ndani ya Marekani aliyeishi kwenye matope ya kijamii kuliko mimi; au mtu mweusi aliye mjinga zaidi ya nilivyokuwa; au mtu mweusi aliyepitia maisha ya taabu kuliko mimi. Lakini ni baada ya mateso makali ndipo furaha kuu hutokea; ni baada ya utumwa na kufungwa gerezani ndipo utamu wa uhuru unaweza kuonwa.

Ninaamini kuwa nimepambana kwa uwezo wangu wote juu ya uhuru wa ndugu na dada zangu weusi milioni 22 wa hapa Marekani. Pamoja na madhaifu yangu yote, na nafahamu kuwa nina madhaifu mengi.

Nadhani udhaifu wangu mkubwa ni kuwa sijapata elimu ya namna ile ya kunifanya labda kuwa mwanasheria. Bado naamini kuwa ningekuwa mwanasheria mzuri sana. Siku zote nimependa vita ya maneno. Niamini nikuambiapo kuwa iwapo ningekuwa na muda, nisingeona aibu kwenda kujiandikisha shule hapa New York na kuendelea pale nilipoishia na kuendelea hadi kupata shahada. Sababu ni kuwa sina uwezo wa kielimu wa kufuatilia mambo mengi ambayo ningependa kufuatilia. Kwa mfano, ninapendelea lugha, ninatamani ningekuwa nguli wa lugha. Sifahamu jambo jingine linalotatiza kama kuwa kati ya watu wanaoongea lugha ambayo huielewi kabisa. Hasa iwapo ni watu wenye muonekano kama wako. Afrika nilizisikia lugha za asili kama Kihausa na Kiswahili zikiongelewa nami nilikuwa nimesimama pale kama mvulana mdogo nikisubiri mtu anitafsirie kilichokuwa kinaongelewa; sitasahau jinsi nilivyojihisi mjinga.
Mbali na lugha za msingi za Afrika, nitajitahidi kujifunza Kichina, maana inaonekana kuwa huko baadaye Kichina kitakuwa lugha yenye nguvu sana kisiasa duniani. Tayari nimeishaanza kujifunza Kiarabu ambacho nafikiri kitakuwa lugha muhimu zaidi ya kiroho huko mbeleni.

Ningependelea tu kuzidi kujifunza mambo mbalimbali sababu nina akili yenye njaa ya maarifa. Ninavutiwa na mada yoyote unayoweza kuitaja. Nafikiri hii ndiyo sababu nimekuja kuwapenda sana baadhi ya waendeshaji wa mijadala ya kwenye redio na televisheni niliyowahi kuhudhuria, na pia naheshimu akili zao-sababu hata kama walipingana kabisa na mimi kuhusiana na suala la ubaguzi wa rangi, lakini walikuwa na mtazamo wa wazi juu ya ukweli wa mambo yanayoendelea duniani. Watu kama Irv Kupcinet wa Chicago, Barry Farber, Barry Gray na Mike Wallce na wengineo. Pia walinionyesha kuwa wanaheshimu akili yangu kwa namna hata wao wenyewe hawakufahamu. Nilifahamu hivyo kwa sababu siku zote walinialika kutoa maoni kwenye mambo yasiyohusiana na ubaguzi wa rangi. Na wakati mwingine baada ya vipindi tulikaa na kuzungumza mambo mbalimbali kwa saa kadhaa, matukio ya karibuni na mambo mengine mengi. Utaona kuwa wazungu wengi, hata kama wanakubali kuwa mtu fulani mweusi ni muelewa, lakini wanahisi kuwa mtu mweusi anachoweza kuzungumza ni masuala ya ubaguzi wa rangi tu; wazungu wengi hawadhani kuwa watu weusi wanaweza kuchangia chochote kwenye mada nyinginezo. Utaona kuwa ni mara chache sana kumsikia mzungu akimuuliza mtu mweusi maoni yake juu suala la afya duniani. Au habari za kukimbizana kuwa nchi ya kwanza kupeleka mtu mwezini.

***
Kila siku asubuhi ninavyoamka naichukulia siku hiyo kama siku ya mkopo. Kwenye jiji lolote ninaloenda kutoa hotuba, kufanya vikao vya taasisi yangu au kwa ajili ya shughuli zingine, kuna watu weusi wanaofuatilia nyendo zangu zote, wakisubiria fursa ya kuniua. Nimesema hadharani mara nyingi kuwa nafahamu wamepewa maelekezo hayo. Yeyote ambaye haamini ninachosema basi hawajui Waislamu wa Taifa la Kiislamu.

Lakini pia nimebarikiwa kuwa na wafuasi waaminifu ambao ninaamini ni waaminifu kwangu kama nilivyokuwa muaminifu kwa bwana Elijah Muhammad. Wale wanaowinda wenzao wakumbuke kuwa msituni kuna wanaowinda wawindaji.

Nafahamu pia kuwa ninaweza kuuawa ghafla na wabaguzi wa rangi wa kizungu. Au kuuawa na mtu mweusi aliyeajiriwa na mzungu. Au anaweza kuwa mtu fulani mweusi aliyechotwa akili akiamini kuwa kwa kuniua atakuwa anamsaidia mzungu, sababu ya jinsi ninavyomuongelea mzungu.

Kwa hiyo, kila siku naishi kama tayari nimeishakufa na nitakwambia kile nitakachopenda ufanye. Nitakapokufa- nasema hivyo kwa sababu kwa mambo ninayoyafahamu sitarajii kuishi hadi kusoma kitabu hiki kikiwa kimekamilika- nataka uangalie kama kile ninachosema ni kweli; kwamba mzungu, kwenye vyombo vyake vya habari atanihusianisha na “chuki.”

Atanitumia nitakapokufa kama alivyonitumia nilipokuwa hai, kwamba ni alama ya “chuki”-na hilo litamsaidia kuepuka kukabiliana na ukweli kuwa kitu pekee nilichokuwa nafanya ni kushika kioo tu kuonyesha historia ya uovu usiosemeka ambao jamii yao umeifanyia jamii yangu.

Utaona, nitasemwa kuwa nilikuwa mtu mweusi “nisiyejali” au “nisiyemakini” zaidi. Siku zote nimehisi jambo hili, “viongozi” wa watu weusi ambao mzungu anasema kuwa wako “makini” ni wale ambao hawaleti matokeo yoyote. Utaleta matokeo kama mtu mweusi pale tu utapochukuliwa na wazungu kama “usiyemakini.” Jambo hili nilijifunza nikiwa bado mvulana mdogo tu. Na toka nimekuwa kama “kiongozi’ wa watu weusi kwenye hii jamii ya kibaguzi ya Marekani, nimethibitishiwa mara kwa mara kuwa mzungu anaponipinga au anaponishambulia kwa nguvu huwa anazidi kuniaminisha kuwa ninafanya kitu sahihi kwa ajili ya maslahi ya watu weusi wa Marekani. Upinzani kutoka kwa wabaguzi wa kizungu unanifanya nifahamu moja kwa moja kuwa ninawafanyia watu weusi jambo la maana.

Ndiyo, nimekubaliana na kazi yangu ya “U-demagogue.” Nafahamu kuwa mara nyingi jamii zimewaua watu waliosaidia kuzibadili. Na kama nikifa nikiwa nimefanikiwa kuleta mwanga fulani, nimeweka wazi ukweli fulani wa maana ambao utasaidia kuiangamiza kansa ya ubaguzi wa rangi ambayo ipo ndani ya mwili wa Marekani-basi sifa zote ni kwa Allah. Ni makosa tu ndiyo yalikuwa yangu.

Mwisho wa Sura ya 19 na Maelezo ya Malcom X​
 

HITIMISHO—NA ALEX HALEY​

Mnamo mwaka elfu moja mia tisa hamsini na tisa, wakati ambao umma ulianza kufahamu uwepo wa Waislamu baada ya kipindi cha televisheni “Chuki inayozalishwa na chuki” kurushwa. Nilikuwa huko San Francisco, nikiwa karibu kustaafu baada ya kufanya kazi kwenye jeshi la Walinzi wa Pwani wa Marekani kwa miaka ishirini. Rafiki yangu mmoja aliyekuwa ametoka kutembelea huko kwao Detroit ndiye aliyeniambia kuhusu dini tata ya watu weusi, ‘Taifa la Kiislamu’ ambayo alishangaa kukuta familia yake yote inaabudu huko. Nilisikiliza nikiwa siamini jinsi ambavyo “mwanasayansi kichaa, bwana Yakub” alivyomtengeneza mzungu kijenetiki kutoka kwa watu weusi wa asili. Kiongozi wa dini hiyo alijulikana kama “Mtukufu Elijah Muhammad” na mkurugenzi wake mkuu alikuwa ni “Imam Malcom X”

Nilipoaanza maisha ya kiraia kama muandishi katika jiji la New York, nilikusanya maandiko juu ya mambo yenye utata huko Harlem kisha nikawasilisha muswada wa kuandika makala kuhusu kikundi-tata kwenye jarida la Reader’s Digest. Nilitembelea mgahawa wa Waislamu huko Harlem na kuuliza jinsi ninavyoweza kuonana na Imam Malcom X, nilionyeshwa aliko-alikuwa anaongea na simu kwenye kibanda kilichokuwa
nyuma yangu. Haikuchukua muda mrefu akawa ametoka, mtu mmoja mrefu mwenye rangi ya kahawia inayoenda kwenye wekundu. Alinitazama kutoka kwenye miwani yake. Wakati huo alikuwa na miaka thelathini na tano. Nilipomueleza lengo langu alisema, “Wewe ni mmoja wa vibaraka wa wazungu uliyetumwa kuja kupeleleza!” Alinishutumu bila kuuma maneno, Nilisema kuwa nilikuwa nimepewa kazi rasmi ya kuandika na kumuonyesha barua kutoka kwenye jarida ikionyesha kuwa makala isiyoegemea upande wowote ilihitajika, makala itakayoonyesha kile ambacho Waislamu wanasema kujihusu na kile kinachosemwa na wanaowashambulia. Malcom X alibeza na kusema kuwa ahadi za mzungu za kwenye makaratasi si kitu; alihitaji muda kuamua iwapo atoe ushirikiano au la. Lakini alitoa pendekezo kuwa nihudhurie baadhi ya mikutano ya Hekalu namba 7 la Harlem(Sasa mahekalu yanaitwa misikiti”) ambalo watu weusi wasio Waislamu waliruhusiwa.

Pale mgahawani nilionana na baadhi ya watu waliosilimu, wote wakiwa wamevalia nadhifu na wakarimu kupitiliza. Tabia na mienendo yao vilionyesha nidhamu ya kijeshi ambayo taasisi yao ilisisitiza, na hakuna aliyeongea chochote zaidi ya maneno yaliyozoeleka ndani ya Taifa la Kiislamu. Hata hali nzuri ya hewa ilichukuliwa kuwa ni Baraka kutoka kwa Allah wakifuatia na sifa kwenda kwa “Mtukufu Elijah Muhammad.”
Baadaye Imam Malcom X aliniambia kuwa hataamua yeye mwenyewe, na kwamba ninatakiwa kuongea na bwana Elijah Muhammad mwenyewe kuhusiana na makala yangu. Nilikubali, mipango ikafanywa nami nikapanda ndege kuelekea Chicago. Nilikutana na bwana Muhammad, alikuwa mtu mwenye umbo dogo, mwenye aibu na sauti ya upole, alinialika kupata chakula pamoja na familia yake kwenye jumba lake. Nilifahamu vyema kuwa nilikuwa nilikuwa nachunguzwa kwa umakini pale alipoanza kuongea jinsi ambavyo F.B.I na mamlaka ya kodi za ndani zinavyochunguza taasisi yake kwa ukaribu mkubwa, na tetesi za ujio wa uchunguzi utakaoendeshwa na bunge. “Lakini siwaogopi hata kidogo. Ninacho kile ninachohitaji-kweli,” alisema bwana Muhammad. Suala langu la kutaka kuandika makala halikugusiwa, lakini niliporudi New York, Malcom X alionyesha ushirikiano zaidi ya pale mwanzo.

Alikuwa akiketi nami kwenye meza moja ndani ya mgahawa wa Waislamu na kujibu kila swali. Mara kwa mara mazungumzo yetu yalikatishwa na simu zilizopigwa kutoka vyombo vya habari vya New York. Nilipomuuliza kama naweza kuona shughuli za Waislamu kwenye majiji mengine, alifanya mipango na Maimam wengine ili nihudhurie mikutano kwenye mahekalu ya Detroit, Washington na Philadelphia.
Makala yangu yenye kichwa “Bwana Muhammad anaongea” ilichapishwa mwanzoni mwa mwaka 1960, na ilikuwa ni makala ya kwanza kwenye majarida kuhusu suala hilo. Muda si mrefu nikapokea barua kutoka kwa bwana Muhammad akinipongeza kuwa makala yangu ilikuwa kama nilivyoahidi. Malcom X naye alinipigia simu na kunipongeza. Ni wakati huu ndipo kitabu cha Dr. Eric Lincoln, Waislamu weusi wa Marekani kilipochapishwa na hivyo watu wengi wakaanza kuwafuatilia Waislamu weusi. Mnamo mwaka 1961 na 1962, gazeti la Saturday evening post liliniambatanisha na muandishi mzungu aliyeitwa Al Balk kuandika makala; kisha nikafanya mahojiano na Malcom X kwa ajili ya jarida la Playboy ambalo liliahidi kuchapisha majibu yake kama yalivyo. Kwenye mahojiano hayo ambayo yalichukua siku kadhaa, mara kwa mara Malcom X alisema baada ya kushutumu vikali Ukristo au wazungu, “Unafahamu vyema kuwa shetani hata chapisha hilo!” Alistaajabu sana baada ya jarida la Playboy kutimiza ahadi yao.

Malcom X akaanza kunichangamkia polepole. Alikuwa ametambua umuhimu wa vyombo vya habari vya kitaifa, na akawa amenichukulia kama njia ya kuvifikia, japo hakuniamini kwa asilimia zote. Mara kwa mara alianza kunipigia simu na kunijulisha kuhusu mahojiano ya redioni, televisheni au hotuba alizokuwa amepanga kufanya, na alinialika kuhudhuria baadhi ya matukio yaliyofanywa na Waislamu weusi.

Uhusiano wetu ukawa umefika hapo na Malcom X ambaye mara nyingi alipokuwa akijielezea kwenye redio na televisheni alisema kuwa yeye ni mtu mweusi mwenye “hasira zaidi katika Marekani” Mwanzoni mwa mwaka 1963 wakala wangu alinikutanisha na kampuni ya uchapaji ambayo makala yangu kwenye jarida la Playboy iliipa wazo la kuchapisha kitabu juu ya simulizi ya maisha ya Malcom X. Niliulizwa iwapo ninaweza kumfanya akubali kusimulia maisha yake kwa kina. Nilisema sifahamu ila nitamuuliza. Mhariri aliniuliza iwapo ninaweza kuandaa muundo wa kitabu hicho, nilipoanza kumuelezea nilifahamu jinsi ambavyo nilimfahamu Malcom X kidogo sana licha ya kufanya naye mahojiano mengi. Swali lile lilinionyesha jinsi ambavyo Malcom X amekuwa muangalifu sana, akijishusha na kumkweza kiongozi wake, Elijah Muhammad.

Nilisema kuwa kitu nilichofahamu ni Malcom X kugusia kuhusu kupitia maisha ya uhalifu na kufungwa gerezani kabla hajawa Muislamu mweusi; mara nyingi akiniambia: “hutaamini nikikuambia maisha niliyopitia,” na niliwasikia baadhi ya watu wakiniambia kuwa kuna kipindi aliuza madawa ya kulevya, wanawake na kufanya ujambazi wa kutumia silaha.

Nilifahamu kuwa Malcom X alikuwa ni mtu anayejali muda kupitiliza. “Katika watu wote, siwezi kabisa kumvumilia mtu asiyevaa saa. Mtu wa hivyo, mtu huyo hajali muda,” aliniambia wakati fulani. “Katika mambo yetu yote, kuthamini na kuheshimu muda kunaamua kufaulu au kushindwa mambo hayo.” Nilifahamu jinsi ambavyo ilidaiwa kuwa wanachama wa Waislamu weusi waliongezeka kila sehemu ambayo Malcom X alifundisha, na nilifahamu kuwa alijivuna jinsi Watu weusi wengi walio magerezani walivyokuwa wanaifahamu dini ya Kiislamu kama ambavyo yeye aliifahamu alipokuwa mfungwa. Nafahamu kuwa alikiri kuwa anakula kile tu ambacho Muislamu mweusi(Hasa mke wake Betty) amepika na jinsi alivyokunywa vikombe visivyo na idadi vya kahawa aliyochanganya na maziwa, akisema kwa utani, “Kahawa ndiyo kitu pekee ninachopenda kiwe kimechangamana.” Nilimwabia mhariri jinsi ambavyo Malcom X alivyoweza kuwafadhaisha wale wasio Waislamu, mfano mmoja ni siku niliyopanda gari yake, nilianza kuwasha sigara naye aliniambia bila kuuma maneno, “Hilo litakufanya wewe kuwa mtu pekee kuwahi kuvuta sigara kwenye gari hii.”
*****​
 
Hitimisho la kitabu hiki ambalo linazungumzia kuuawa kwa Malcom X ni refu sana. Kama pages 100. Kwa hapa JF tutaishia hapa. Unaweza kumalizia kusoma ndani ya app ya Maktaba Sauti, ipo playstore. Kusoma humo ni bure. Kuna vitabu zaidi ya 100 vingine.
 
Back
Top Bottom