Simba ni klabu kubwa na yenye heshima kubwa nchini na Afrika kwa ujumla, ni timu yenye historia iliyosheheni mambo mema katika nyanja ya burudani.
Lakini mbali ya ukubwa huo wa jina, bado Simba iko na itaendelea kufanya kazi chini ya Shirikisho la Soka nchini TFF kama mlezi na mwendeshaji wa shughuli zote za soka nchini.
Mgogoro kati ya mchezaji Morrison ulianza miezi kadhaa iliyopita na ulibaki Kama mgogoro binafsi unaozihusu Yanga na Morrison huku TFF akibaki mwamuzi asiye na upande. Ghafla Morrison akagoma kucheza Yanga akisema mkataba wake umeisha kwani ulikuwa wa miezi 6 pekee, lakini Yanga wakamshtaki Morrison TFF kupitia Kamati husika inayojihusisha na haki za wachezaji.
Yanga wakaambiwa wapeleke vielelezo vya mkataba wa miaka miwili (ambao ulishasajiliwa na TFF na CAF), na baada ya TFF kupokea nakala halisi (Original Copy) ya mkataba huo Wakamuita Morrison lakini akaukana.
Hivyo TFF wakalazimika kuhusisha vyombo vya uchunguzi wa kijinai (Polisi) ili isaidie kupata ukweli wa suala hili kama saini iliyoko kwenye mkataba ni ya Morrison kweli (genuine) au ni ya kughushi (forged).
Kabla majibu ya uchunguzi huo hayajatolewa hadharani na mamlaka mhusika (TFF), Jana likaibuka suala ambalo klabu yoyote makini isingeweza kulifanya. Akaonekana Morrison akisainishwa mkataba mpya na Klabu ya Simba, akavalia Uzi wa Simba na akaunti ya klabu ikaliweka tukio hilo kuonesha kuwa ni official event.
Hapa ndipo ninapolazimika kuwaambia Simba mmewaingiza TFF kwenye mtego ambao huenda ukawapa maumivu makali na wasieleweke kwa yeyote hata wakijitetea.
Nani ataamini TFF endapo watakuja na majibu kwamba mkataba ule ni feki kwa vile saini imeghushiwa iwapo tayari wapinzani wa mlalamikaji mnaonekana mnajua hukumu ya kesi kabla ya kusomwa rasmi? Watu wakisema (na wana haki ya kusema) kwamba TFF wamewapa kilichoko kwenye hukumu (wamevujisha) mtakataa? Kwa nini hata kama mlitaka kufanya, msingefanya jambo hili kimya kimya ili likija kinyume mnachana mkataba au likiwa upande wenu mnaibuka kwa shangwe?
Mmewezaje kufunga ndoa na mwanamke ambaye anadai talaka mahakamani na kesi inaendelea? Nani mwenye akili fupi kiasi hiki huko hadi anafyanya mambo ambayo yanatakiwa kufanywa na Lufinyo FC ya Madibila?