Waziri wa Ujenzi, Innocent Bashungwa @innocentbash ameuagiza Wakala wa Majengo (TBA) kuhakikisha wanakuja na mikakati itakayosaidia kujenga nyumba za bei nafuu hasa kwa Vijana wanaoajiriwa katika utumishi wa umma hususani Dodoma ili kuweza kumudu gharama za maisha.
“Kuna Vijana ambao wanaingia kwenye kada ya utumishi wa umma na bado hawajawa na uwezo wa kujijengea nyumba, kupitia TBA mnaweza kujenga nyumba za bei rahisi kwa ajili ya Vijana hao ili kuwarahisishia gharama za maisha”
Bashungwa pia ameutaka Wakala huo kuwa na utaratibu wa kuwajengea uwezo Watalaamu walionao ili kuenda sambamba na kasi ya mabadiliko ya teknolojia hasa katika suala la ujenzi na uendelezaji wa majengo mbalimbali.
Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa TBA, Arch. Daud Kondoro, amesema kuwa Wakala huo utahakikisha unatafuta ufumbuzi wa changamoto zilizopo na kumuahidi Waziri Bashungwa kuandaa mikakati mizuri itakayosaidia Wakala huo kutoa huduma bora kwa Wananchi.
Awali, Arch. Kondoro ameeleza kuwa hadi sasa TBA inaendelea kutekeleza mradi wa ujenzi wa nyumba 3500 za watumishi wa umma eneo la Nzuguni Dodoma ambapo awamu ya kwanza ya nyumba 150 utekelezaji umefikia asilimia 95 na awamu ya pili ya ujenzi wa nyumba 150 utekelezaji wake umefikia asilimia 10, miradi mingine ni ujenzi wa nyumba 20 za Viongozi Jijini Dodoma ambazo zililenga kukabiliana na uhaba wa nyumba za Viongozi baada ya Serikali kuhamia Dodoma ambapo mradi huo umekamilika kwa asilimia 100 na nyumba zimeanza kutumiwa na Viongozi.