Makapuku Forum

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk Hussein Ali Mwinyi leo Jumanne Septemba 12, 2023 ametengua uteuzi wa aliyekuwa Kamishna wa Idara ya Bajeti, Ofisi ya Rais, Fedha na Mipango, Saumu Khatibu Ally pia ametengua uteuzi wa Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Barabara Zanzibar (Zanroads), Makame Ali Makame.

Taarifa ya utenguzi hiyo imetolewa na Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi, Mhandisi Zena Said.
 
Idadi ya waliofariki tetemeko la ardhi Morocco wamefikia 2,800.

Madaktari na waokoaji wanaendelea kupambana huku matumaini yakififia kupata watu wakiwa hai ambao wanadhaniwa kufukiwa chini ya vifusi kutokana na miundombinu.

Umoja wa Mataifa umesema kwamba takriban watoto 100,000 wameathiriwa na tetemeko hilo.

Waokoaji kutoka nchi za Qatar, Uhispania, Falme za Kiarabu na Uingereza wamejitolea katika shughuli za utafutaji na uokoaji unaendelea nchini humo.

 
Zaidi ya wananchi 23,000 waishio katika Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe mkoani Kagera na maeneo jirani wataondokana na adha ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma za upasuaji, baada ya hospitali ya halmashauri hiyo kuanza kutoa huduma hiyo hii leo.

Hospitali hiyo iliyoanza kujengwa mwaka 2019 na kukamilika mwaka 2020, imejengwa kwa gharama ya Sh3.4 bilioni huku ikiwa na majengo 14 na watumishi 45.

Zawadi Jackson ambaye amekuwa mwananchi wa kwanza kupata huduma hiyo hospitalini hapo leo Septemba 12, 2023 ameishukuru Serikali inayoongozwa na Rais Samia suluhu Hassan kwa kuwezesha kupatikana kwa huduma hiyo.

“Kwanza nashukuru nimehudumiwa vizuri na mimi pamoja na mwanangu tunaendelea vizuri. Napenda kuishuru sana Serikali kwa kutuletea hii huduma hapa kwetu. Sisi kina mama tulikuwa tunatembea umbali mrefu kufuata hii huduma Bukoba mjini na sehemu nyingine. Tunaomba tuzidi kuletewa huduma nyingine zaidi,” amesema.

Upasuaji huo wa kwanza hospitalini hapo umefanywa na na madaktari Dk Karimu Abdalah, Dk Mugisha Laurian wakishirikiana manesi Irene Mlekio, Lydia Kanyinginya mtaalamu wa usingizi, alikuwa ni Oscar Kilengule.
 
Uhaba wa Dola nchini umeendelea kuumiza makundi ya watu wakiwemo wakulima wa tumbaku ambao wengi wao mpaka sasa wana mashaka na maandalizi ya msimu ujao wa zao hilo.

Mwananchi Digital imepokea malalamiko ya wakulima kutoka maeneo mengi ya nchi ikiwemo mikoa ya Shinyanga, Mbeya (Wilaya ya Chunya), Tabora na kwingineko kunakolimwa zao hilo.

Diwani wa Kata ya Ulowa inayoongoza kwa kulima tumbaku ndani ya Halmashauri ya Ushetu, Pascal Meyengo alisema wakulima wengi hususani waliouza kwa kampuni ya Mkwawa hali yao ni mbaya, huku akisema kuna wasiwasi msimu ujao ukaenda vibaya kwa kuwa wengi hawajapata pesa za maandalizi.

"Ukipita hata maeneo ya biashara kwa walima tumbaku yamepoa sio migahawa wala baa hamna watu, katika kilimo cha zao hilo huwa tunatumia wasaidizi ambao mikataba yao ni kuwalipa mwishoni mwa Juni, msimu huu hawajalipwa na hali hiyo imesababisha migogoro mikubwa," alisema.

Mkulima wa tumbaku, Makwaya Samweli alisema kila mara amekuwa akipewa ahadi ya uongo lakini amesikia kuwa kuna vyama viwili wameanza kulipwa hivyo matumaini yake ni kuwa na yeye atafikiwa.

Akilizungumzia hilo, Naibu Mkurugenzi wa Kampuni ya Mkwawa, Richard Sinamtwa alisema kuwa wakulima wanaodai fedha zao watatabasamu wiki hii kwani mipango ya kuwalipa wote imeiva huku akisema suala la uhaba wa Dola ndilo lililosababisha wachelewe kulipwa.

"Licha ya uchanga wetu sokoni lakini sisi ndio wanunuzi wakubwa, hapa katikati tuliiomba wizara tulipe kwa Shilingi lakini baadaye wenyewe tukaona tukilipa kwa fedha hiyo mkulima hatapata thamani halisi," alisema.

Sinamtwa ambaye alisema thamani ya manunuzi yao kwa mwaka huu ni takribani Dola 100 milioni (Sh250 bilioni).

 
Vigogo kumiliki ardhi na watumishi wa ardhi kuwa na maslahi katika upimaji, ni miongoni mwa mambo magumu yatakayomkabili Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Jerry Silaa.

Kwa mujibu wa wabunge, ugumu wa wizara hiyo unakuja pale ambapo maeneo nyeti nchini yanamilikiwa na wale waliowaita vigogo, hivyo inahitaji moyo wa chuma kuwashughulikia.

Kauli za wabunge kuhusu ugumu huo, zinakuja wiki moja tangu mbunge huyo wa Ukonga jijini Dar es Salaam, aapishwe kushika wadhifa huo ambao awali ulikuwa chini ya Dk Angeline Mabula aliyekuwa akikabiliwa na rundo la migogoro ya ardhi. Kwa mujibu wa bajeti ya wizara hiyo kwa mwaka 2023/24 iliyowasilishwa na mtanguzi wake, Mabula inaonyesha hadi kufikia Mei 15 mwaka huu migogoro 2,684 ilikuwa imeshughulikiwa kiutawala.

Jijini Dodoma, migogoro 815 ilipokelewa ambapo 429 sawa na asilimia 52.6 ilipatiwa ufumbuzi na 386 inaendelea kushughulikiwa huku Mkoa wa Dar es Salaam, migogoro 386 ilipokelewa, 201 sawa na asilimia 52 ilipatiwa ufumbuzi na 186 iliyosalia inaendelea kupatiwa ufumbuzi.

Tangu alipoapishwa, Silaa ameonekana mara kadhaa kuzungumza na menejimenti ya wizara hiyo na msisitizo wake ni kuomba ushirikiano na kuwataka watumishi wake kumaliza migogoro ya ardhi ndani ya siku 100 na kula sahani moja na wazembe.

Pamoja na mwanzo wa ahadi na msisitizo wa utendaji, inamhitaji moyo wa chuma kwa kuwa nafasi yake hiyo ya kushughulika na ardhi si jambo lelemama, kama anavyoelezwa na wabunge wenzake walipozungumza na gazeti hili.

Mbunge wa Tarime Vijijini (CCM), Mwita Waitara alisema inahitaji moyo kuwasaidia wananchi wa ngazi ya chini, ilhali maeneo nyeti ya ardhi yanamilikiwa na vigogo.

 
Mahakama Kuu Kanda ya Shinyanga imeitisha jalada la shauri la madai ya mahari lililotolewa hukumu na Mahakama ya Wilaya ya Meatu Machi 14 mwaka huu, kwa ajili ya kulipitia upya.

Mahakama hiyo ya Meatu, Mkoa wa Simiyu iliamuru nyumba ya mkazi wa Kijiji cha Nkoma mkoani humo, Selemani Mussa (65) kuuzwa ili kulipa deni la Sh1.1 milioni analodaiwa ili kukamilisha mahari ya kijana wake.

Uuzwaji wa nyumba hiyo ni kufikia Sh2.2 milioni walizokubaliana kabla ya ndoa ya kimila kufungwa mwaka 2019 ikiwa ni makubaliano ya ng'ombe 15 kwa thamani ya Sh150,000 kwa kila ng'ombe mmoja.

Julai 28 mwaka huu, Mwananchi Digital iliripoti habari hiyo na kuibua mjadala kwenye maeneo mbalimbali juu ya suala hilo.

Mwishoni mwa wiki Saidi Kisamba anayemuwakilisha mdaiwa Seleman Mussa alisema Mahakama imeliagiza jalada kutoka Mahakama ya wilaya ili kulifanyia kazi, hivyo baada ya kulipitia wanaweza wakatoa maelekezo mengine.

Hukumu ya shauri la madai namba 81 ya mwaka 2020 ilitolewa na hakimu F. F. Madungu ikiamuru kukamata nyumba namba 27 B ya Seleman Mussa iliyopo kijiji cha Nkoma wilayani Meatu mkoani Simiyu kufidia deni la mahari la Sh1.1 milioni kati ya Sh2.2 milioni walizokubaliana.

Akizungumza na Mwananchi Digital Kisamba alisema “Mahakama Kuu ina mamlaka ya kuita jalada la kesi kufanyia mapitio, baada ya hapo litarudishwa mahakama ya wilaya kwa ajili ya utekelezaji kwa amri itakayokuwa imetolewa na jaji.

Alisema alipigiwa simu kutoka Mahakama Kuu akiarifiwa hatua hiyo kwa ajili ya kumtaarifu mteja wake na kwa sasa wanasubiri uamuzi wa Mahakama.

Mwananchi Digital ilizungumza na Seleman Mussa ambaye ni mdaiwa katika shauri hilo alisema Septemba 4, mwaka huu alipokea taarifa kwa njia ya simu akiambiwa shauri lake lipo Mahakama Kuu.

"Niliambiwa kesi yangu imefika kule kwa hiyo nisubiri maamuzi yatakayotolewa na jaji," alisema Seleman.

 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…