Mambo muhimu ya kufanya unapohitaji msaidizi wa kukulelea mtoto

Mambo muhimu ya kufanya unapohitaji msaidizi wa kukulelea mtoto

Joined
Oct 5, 2018
Posts
33
Reaction score
58
Kutokana na sababu zilizo nje ya uwezo wa wazazi/walezi kuna kipindi katika maisha yao hulazimika kutafuta wasaidizi wa kuwalelea watoto wao. Wazazi/walezi wengi katika juhudi za kuyafikia mahitaji yao na ya watoto wao hujikuta wanakosa kabisa muda wa kuwapa uangalizi wa kutosha watoto wao hivyo kulazimika kutafuta wasaidizi.

Kumekuwa na changamoto nyingi zinazowakuta wazazi/walezi na watoto pia kutokana na wazazi/walezi kutozingatia baadhi ya mambo pindi wanapotafuta wasaidizi: changamoto kama vile watoto kufanyiwa matendo ya kikatili, wazazi/walezi kuibiwa, watoto kufundishwa mambo mabaya na mengine mengi. Katika makala hii naenda kueleza mambo ya kuyazingatiwa na mzazi/mlezi anapoamua kutafuta mtu wa kumsaidia kulea mtoto.

FANYA MAHOJIANO NA MSAIDIZI KABLA YA KUMPOKEA. Andaa maswali mbalimbali ili kuukagua uwezo, imani na uzoefu wake. Uliza maswali ya msingi yatakayoweza kuweka bayana imani na mtizamo wake juu ya watoto, familia na malezi, maswali kama endapo mtoto akikosea na kukuchukiza, utachukua hatua gani au umelea mtoto mara ya mwisho kwa muda mrefu kiasi gani? Hii itakusaidia kujua kama mzaidizi huyo anakidhi vigezo na mahitaji yako.

ENDESHA MAFUNZO KWA MSAIDIZI ILI KUMJENGEA UWEZO ZAIDI. Mafunzo lazima yalenge kumuandaa msaidizi kuyafikia mategemeo yako juu ya malezi; kwa mfano unaweza kumfundisha namna ya kumfanya mtoto atii amri zake kirahisi, namna ya kumuandalia mtoto chakula au kumsafisha. Msaidizi akikosea jambo mwelekeze kwa njia nzuri bila hasira, hakikisha kila penye kosa unamwonyesha njia bora ya kufanya jambo hilo husika. Hii itasaidia kuyaondosha mapungufu ya msaidizi na kumuandaa na kumjengea uwezo zaidi, hali itakayofanya aweze kumudu vyema kazi yake.

FUATILIA MAISHA YAKE ILI KUJUA HISTORIA YAKE. Uliza katoka wapi kabla ya kwako, kwanini kaja kwako na kaacha huko alikokuwa mwanzoni, muombe akukutanishe na watu aliowahi kuwapa huduma hiyo hapo awali. Hii itakusaidia kuepuka kumpa jukumu mtu ambaye anaweza kuwa sio mzuri au salama kwenye malezi ya mtoto. Wazazi/walezi wengi wamejikuta katika matatizo kwa kuwachukua wasaidizi ambao hawaijui kabisa historia yao.

AWE NA UMRI WA MIAKA 18 NA KUENDELEA. Mtu mwenye umri chini ya miaka 18 huyo ni mtoto asipewe jukumu la kulea mtoto, ni ngumu sana mtu mwenye umri chini ya miaka 18 kujua anachokifanya kwa ukamilifu pale anapolea mtoto. Kwa kumpa jukumu hili mtu mzima, mzazi/mlezi utajihakikishia kuwa mtoto wako yupo salama kwa asilimia kubwa hata bila ya uwepo wako. Tumeshuhudia watoto wanaopewa jukumu la kulea watoto wakileta madhara makubwa sana kwa watoto wanaowalea.

MALIPO YA MSAIDIZI YASIWE MADOGO SANA. Malipo ya wasaidizi wa kulea watoto mara nyingi ni madogo sana hali inayopelekea wasifanye kazi yao kwa hamasa kubwa. Ni lazima mzazi/mlezi uhakikisha unamlipa msaidizi malipo ambayo angalau ataridhika na ataweza kumudu mahitaji yake ya kila siku. Hii itasaidia sana msaidizi kuwa na hamasa ya kulea mtoto vizuri.

JENGA MAHUSIANO MAZURI NA MSAIDIZI. Jenga mahusiano ya kirafiki ili awe huru na wewe kwenye mambo mbalimbali yahusianayo na mtoto. Mfanye kama mtu wa muhimu anayekusaidia kulea mtoto na sio kijakazi wako. Ukijenga naye mahusiano mazuri utamfanya ampende na kumthamini mtoto wako kama wake. Ni ngumu sana msaidizi kumlea mtoto wako kwa upendo kama hautoishi naye kwa upendo pia.

FANYA UCHUNGUZI JUU YA NAMNA MSAIDIZI ANALEA MTOTO PINDI USIPOKUWEPO. Wasaidizi wengi huwafanyia vitendo vya kikatili sana kwa watoto pindi wazazi/walezi wao hawapo. Tumeshuhudia wasaidizi wakiwapiga watoto kupitiliza. Uchunguzi huu sio kwa ajili ya hila au hofu juu ya msaidizi bali kwa ajili ya usalama wa mtoto.

WEKA WAZI MAJUKUMU YOTE ANAYOPASWA KUYATIMIZA MSAIDIZI. Majukumu yote anayopaswa kuyatimiza msaidizi wako ni lazima yawekwe wazi na endapo kutakuwa na mabadiliko basi msaidizi aelezwe na namna atakavyofidiwa katika malipo au muda wake. Hii itamfanya msaidizi kujua mipaka na mahitaji ya kazi yake kila siku, hali ambayo itaongeza ufanisi katika kazi na kupunguza migogoro isiyo ya lazima kati yake na wewe.

ZINGATIA ELIMU/UFAHAMU WA MSAIDIZI. Msaidizi wako ana nafasi kubwa sana katika kumuendeleza mtoto wako kisaikolojia, kiimani, kijamii, kitaalama au kitamaduni, hivyo chagua msaidizi atakayekua na elimu angalau kidogo ya kuweza kusaidia ukuaji wa mtoto katika njanja mbalimbali angalau kidogo.
Mwisho nimalizie kwa kusema kwamba ni muhimu sana mzazi/mlezi ukiyazingatia mambo haya kwa ajili ya kuyahakikisha maendeleo na ukuaji bora na salama wa mtoto wako.

Mwisho nimalizie kwa kusema kwamba ni muhimu sana mzazi/mlezi ukiyazingatia mambo haya kwa ajili ya maendeleo na ukuaji bora na salama wa mtoto wako. Wasaidizi wa melezi ni walezi wa pili wa mtoto wako hivyo ni muhimu ukijihakikishia kuwa wanaweza kuifanya kazi hiyo kama ambavyo wewe pia ungeifanya.

IMEANDIKWA NA:
EDUCATOR, AUTHOR, PARENTING CONSULTANT
MWANGA MPYA EDUCATIONAL SERVICES AND PRODUCTS

EMAIL: justinekakoko@gmail.com. KARIBU SANA!
 
Huu uzi umefanya nimeongeza kitu kipya juu ya hawa wasaidizi wetu kwa siku ya leo. Thanks.
 
JENGA MAHUSIANO MAZURI NA MSAIDIZI - Nakikazia kipengele hiki kwani kwa upande wangu huwa kinasababisha nikiwa na safari za dharura za kuniweka mbali na familia kwa siku kadhaa niwe ni mwenye kuwa na amani ya moyo kwa kuwa nimeacha watoto katika mikono salama.

Na hata nirudipo watoto huwa hawana habari na mimi utadhani nilikuwepo na hii yote inatokana na mahusiano mazuri yaliyopo baina yangu na msaidizi.
 
malipo ni kidogo ndiyo maana ni adimu! Tuongezeni dau tuone kama hawatoongezeka!
Na walio wengi kazi pia huwa zinawazidia. Yaani hawapangiwi na wala kujua majukumu yao ni yapi mana waeza kuta hata yale ya kufanya mwenye nyumba bado yanakuwa ya msaidizi.

Kwa hali hii ni lazima wawe adimu sababu akishaondoka aezi rudi na hata kama ana mtu wa karibu aezi mshawishi kujaribu kufanya hiyo kazi.
 
Kwa kweli hivyo ni vitu/vigezo muhimu sana vya kuzingatia ila kwa bahati mbaya tulipofikia kama jamii kwa sasa na kwa uhalisia wa maisha haya yanaonekana kama”masharti magumu sana” kutekelezeka, miaka ijayo watoto wengi sana watalelewa “day care” kama ilivyo nchi zilizoendelea.
 
Kwa kweli hivyo ni vitu/vigezo muhimu sana vya kuzingatia ila kwa bahati mbaya tulipofikia kama jamii kwa sasa na kwa uhalisia wa maisha haya yanaonekana kama”masharti magumu sana” kutekelezeka, miaka ijayo watoto wengi sana watalelewa “day care” kama ilivyo nchi zilizoendelea.
Daycare ni suluhu nzuri pia. Kikubwa tu iwe nzuri na inayojali watoto na sio pesa tu.
 
we mama unapoajiri msichana wa miaka 18 na kuendelea ujue uwezekano wa kuajili mke mwenzio ni mkubwa sana maana wasichana hao hufanya kazi zote kuliko hata wewe mama mwenye nyumba
 
Back
Top Bottom