Dar es Salaam, Tanzania. Rais John Magufuli amemwagiza Waziri wa
Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Kikanda na Mambo ya Jumuiya ya
Afrika Mashariki, Balozi Dk Augustine Mahiga kuanza kushughulikia
mgogoro wa Burundi na ametaka kazi hiyo afanye kwa kushirikiana na
waziri wengine kutoka Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
Huu utakuwa mtihani wake wa kwanza kwa Balozi Mahiga ambaye
aliapishwa hivi karibuni kwenye wadhifa huo baada ya kuteuliwa na
Rais kuwa mbunge. Balozi Mahiga aliliambia gazeti moja akisema
kuwa, ameagizwa kushughulikia kiini cha mzozo huo na tayari wakati
wowote alitarajiwa kuwasili Bujumbura kuanza mazungumzo.
Hata hivyo, alitarajiwa kuwasili kwanza mjini Arusha kwa ajili ya
majadiliano na Katibu Mkuu wa EAC, Dk Richard Sezibera na baadaye
kuweka mikakati ya pamoja ya namna ya kushughulikia mzozo huo.
Tanzania ndiye mwenyekiti wa EAC.
Wakati hali ya wasiwasi ikiendelea kujitokeza Burundi, ripoti zinasema
kuwa zaidi ya raia 1O0,000 wamewasili nchini kwa ajili ya kuomba
hifadhi tangu mzozo huo ulipoanza Aprili mwaka huu.
Wakati Tanzania ikianzisha juhudi mpya kuhusiana na mzozo huo,
kuna ripoti kuwa Umoja wa Afrika (AU) umeanza kujadili uwezekano
wa kutumwa jeshi la Afrika Mashariki nchini humo kwa lengo la
kuzima ghasia na machafuko yanayotishia kuitumbukiza nchi hiyo
kwenye vita vya ndani.
Baraza la Usalama na Amani la Umoja wa Afrika limesema hali ya
Burundi ni mbaya na kwamba hatua za dharura zinahitaji kuchukuliwa
ili kuepusha nchi hiyo kutumbukia kwenye vita vya wenyewe kwa
wenyewe.
Kamishna Mkuu wa baraza hilo, Ismail Chergui ameandika kwenye
ukurasa wake wa Twitter akisema kuwa mauaji nchini Burundi ni
lazima yakomeshwe. Baraza hilo la AU limefanya kikao cha dharura
kujadili kadhia ya Burundi na pendekezo la kutumiwa kikosi maalumu
kinachojulikana kama East Africa Standby Force kwa ajili ya kudhibiti
hali ya mambo katika nchi hiyo limetolewa. Kikosi hicho kiliundwa
mwaka 2003 na kinajumuisha nchi za Kenya, Burundi, Comoros,
Djibouti, Ethiopia, Rwanda, Ushelisheli, Somalia, Sudan na Uganda.
Huku hayo yakijiri, Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja
wa Mataifa amewalaumu viongozi wa Burundi kwa kuchochea ghasia
na machafuko nchini humo na kulitaka Baraza la Usalama la umoja
huo kuwawekea vikwazo vya usafiri viongozi kama njia moja ya
kuwashinikiza wakomeshe ghasia hizo.
CHANZO: Gazeti La Mwananchi
NOTE:
SAWA! ILA ZANZIBAR MBONA UMEWAPA KISOGO? AU YAMEKUSHINDA MH.???