54.
hicho nilibahatika kufahamu kuwa asili yangu ni Tanzania, si Uganda wala Kenya kama nilivyoelezwa awali. Toka hapa niliongeza jitihada kubwa za upelelezi hata nikayabaini yote yaliyonihusu, baba aliyenisusa, mama aliyeuawa na pacha mwenzangu ambaye tulitenganishwa toka tungali wachanga. Nikaongeza juhudi. Niliwasiliana na vituo vyote vya kulelea watoto yatima Afrika Mashariki, ofisi zote za Ustawi wa Jamii, shule na vyuo mbalimbali. Juhudi zangu zililipa takribani mwaka mmoja baadaye, nilipoletewa picha ya msichana aliyesimama katika mojawapo ya mitaa ya Dar es Salaam, ambaye ningeweza kuapa kuwa alikuwa mimi. Tulifanana reale kwa ya pili. Nilitetemeka mwili mzima huku nikiangua kilio, hasa baada ya kupewa historia ya msichana huyo kuwa aliitwa Mona Lisa; alilelewa na Wamisionari wa dhehebu la Katoliki, akaelimishwa katika vyuo vyao na baadaye kwenda nchini Uingereza ambako alipata shahada yake ya pili majuzi tu. Kwamba, alikuwa amesomea fani ya uandishi wa habari za kubuni na mengine mengi.”
Joram alihisi akianza kupata mwanga zaidi. Alimkumbuka Mona Lisa na mswada wake wa ‘Ubongo wa Mwalimu Nyerere.’ Alikumbuka msichana huyu alivyomjia na kumtaka ushauri. Akaukumbuka ule mswada mzuri, ambao ungeweza kuwa kitabu cha kusisimua sana kama kile kifo cha kusikitisha kisingemkuta, tena juu ya kitanda chake. Hasira zikampanda na kumfanya amkazie Margareth macho makali yaliyojaa maswali.
Maswali ambayo Margareth aliendela kuyatolea ufafanuzi katika simulizi yake.
“Kiumbe huyu ambaye alianza kama baba kisha akawa mume na baadaye kuondokea kuwa adui yangu mkubwa, siku zote alikuwa na ndoto juu ya nchi hii ya Tanzania. Kila mara aliita, ‘Nchi yangu.’ Wakati mwingine alizungumza hata akiwa usingizini, akiitaja Tanzania. Siku moja alinivuta faragha na kuniambia, “Unafahamu kuwa tutaitawala dunia kutokea Tanzania?” bado sikuweza kumwelewa. Wakati huo tulikuwa tukifanya ziara nyingi za siri humu nchini na kufungua miradi mingi chini ya mwamvuli wa uwekezaji.”
“Wakati hayo yanatokea tayari nilikwishapewa mafunzo
makubwa ya ujasusi, upelelezi na matumizi ya silaha anuwai. Nilipelekwa Israel, Lebanon, Marekani na Pakistan ambako nilikutanishwa na Osama bin Laden ambaye alinipenda ghafla na kujaribu kunirubuni. Nikamwacha, lakini si kabla ya kuchota mengi toka kwake kitaaluma.”
“Taaluma hiyo iliniwezesha kujua na kutumia vitendea kazi vya aina mbalimbali, kimojawapo ikiwa ile pete ya mawasiliano ambayo nilifanya hila hata marehemu akaipokea na kukubali kuivaa akiamini kuwa ni zawadi toka kwa mtu mwingine kabisa, pete ambayo, nikiwa umbali usiozidi kilomita moja niliweza kusikiliza maongezi yake yote bila ya yeye kujua. Kadhalika, iliniwezesha kujua mahala alipo muda wote.”
Margareth alisita tena, kama anayesikiliza maumivu ya hadithi yake mwenyewe. “Lazima nikiri kuwa niliishi kwa taabu sana katika kipindi hicho, Joram,” aliendelea. “Fikiria, ndugu yako wa damu, hujapata kuzungumza naye kwa miaka, toka mlipokuwa mkigombea titi la mama, halafu unamwona, unamsikiliza. Lakini huwezi kujitokeza na kujitambulisha kwake.”
“Kwa nini hukujitokeza?” Joram aliuliza.
Margareth alimtazama Joram kwa mshangao, akamwambia taratibu, “Wewe si mtu wa kuuliza swali kama hilo Joram.”
Ni kweli, Joram aliwaza. Kujitambulisha kwa Mona Lisa lilikuwa ni jambo ambalo Magreth asingeweza kulifanya kwa sababu nyingi sana. Kwanza, alikuwa akiishi katika dunia ile ambayo Wamarekani huiita ‘Underground World’ dunia ya kujificha mchana na kutembea usiku. Kama angejitokeza ingekuwa sawa na Osama bin Laden kuitangazia dunia amejichimbia wapi. Kwa upande mwingine, Joram alifahamu kuwa Margareth alisita kufanya hivyo kwa kuchelea kuhatarisha maisha ya ndugu yake huyo wa pekee duniani. Mwajiri au mfadhili wake alikuwa mtu hatari ambaye asingesita kumuua msichana huyo asiye na hatia kwa ajili ya kulinda maslahi yake. Angemuua kwa kukusudia, si kwa bahati mbaya kama alivyofanya. Lakini, vilevile maisha yao tayari yalikuwa na tofauti kubwa sana. Wakati Mona alikuwa kama malaika, Magreth alijiona kama shetani asiye na lolote la kuzungumza naye.
“Mshenzi yule,” Margareth aliendelea. “Alikuwa ananiamini sana. Lakini pamoja na hayo alikuwa akinificha baadhi ya mikakati yake nyeti. Ni majuzi tu, akiwa amejawa na furaha, aliponiita na kuniambia, ‘Tayari. Hakuna tena kitakachotuzuia kuitawala dunia. Tutaanza na Tanzania. Baada ya muda mfupi tutaichukua Afrika na muda si mrefu dunia nzima itakuwa chini ya himaya yetu.’ Sikumwelewa. Ni kweli kuwa alikuwa na hela, tena nyingi sana na zilizochimbiwa sehemu mbalimbali duniani. Ni kweli pia kuwa alikuwa na mtandano mkubwa; viongozi mbalimbali wa kisiasa na kijeshi, wasomi na watu wa kada nyinginezo wakipokea maelekezo toka kwake. Sikuwa na shaka kuwa angeweza kuandaa na hata kuangusha utawala wa nchi yoyote duniani, hasa zile nchi dhaifu kiuchumi. Lakini kuitawala dunia…”
“Alibaini kuwa nilikuwa sijamwelewa. Ndipo aliponifungulia kompyuta yake na kunionyesha hicho nilichokionyesha, ambacho alikitaja kama silaha yake pekee ya kuitawala dunia, silaha ya maangamizi ya kutisha ambayo mimi niliichukulia kama mtambo wa mauti. Niliogopa, nikatetemeka sana na kumwambia waziwazi kuwa siafikiani naye. Kwa hulka yake nilijua kuwa kauli yangu ilikuwa hukumu ya kifo changu mwenyewe, lakini sikujali. Kifo changu kilikuwa kheri mara elfu moja kuliko kuiacha dunia nzima iteketezwe kwa ajili ya ndoto za mwendawazimu mmoja.”
Ndipo nikaelewa kwa nini alifanya kila njia kuhakikisha naajiriwa katika Jeshi la Polisi la Tanzania na baada ya kuhakikisha kupitia kwangu amepata kile alichotaka akanitoa kwa kubuni ule mpango wa ajali ambao ulisababisha kupoteza maisha ya watu wasio na hatia.
“Nikiwa ndani ya polisi ndipo nilipoanzisha ule utani wa kujiita ‘Mona Lisa’ kama njia pekee ya kuwa karibu na ndugu yangu, jina ambalo kwa ajili ya maumbile yangu lilikubalika mara moja na kudumu hadi kilipotokea ‘kifo changu’.
Baada ya kusita kwa muda, Margareth akaendelea, “Nililazimika kutumia busara juu ya mkakati wake wa kishetani. Nilijitia kumsikiliza wakati akijitahidi kunishawishi na kunipamba kwa joho la ‘Umalkia wa Dunia.’ Usiku huohuo nilinakili toka katika kompyuta yake mpango wake
huo na kutoroka. Ndipo ulipoanza ule mchezo wa paka na panya. Alifungulia majeshi yake yote na kuniwinda kwa udi na uvumba. Pale kitandani kwako, pamoja na mzaha wangu wa kawaida kwa hayati ndugu yangu niliitumia fursa ile kwa masuala mawili. Moja ilikuwa kujificha. Lakini pili, nilikuwa nikitafuta nafasi nzuri zaidi ya kukufahamu na kuona kama ungeweza kukidhibiti kichaa changu. Lazima nikiri kuwa sikujua kama alikuwa na mtandao mpana kiasi kile nchini. Nadhani ni kwa ajili ya kufanana kwangu na Mona Lisa ndiyo sababu walinifikia haraka kiasi kile na kuishia kumuua yeye badala yangu.”
Margareth alisita tena, machozi yakianza tena kumtoka. Alitetemeka mwili mzima, jasho jembamba likimtoka. Kwa mara nyingine tena, alimwangukia Joram kifuani na kunong’ona, “Samahani sana. Mimi ni mwanamke mbaya sana, muuaji na katili mkubwa. Mona Lisa hakustahili kuwa ndugu yangu. Nadhani hata wewe sistahili kukukumbatia, Joram. Lakini bado nitaua! Kwa mara ya mwisho! Baada ya hapo nitakuwa radhi kufa!”
W 11 X
WAKATI watu mbalimbali wakitaabika usiku huo, mtu mmoja alikuwa akichekelea. Kwa jina aliitwa Christopher Marlone, ingawa kwa sasa hakujulikana kwa jina hilo.
Marlone alikuwa na kila sababu ya kuchekelea. Aliamini kabisa kuwa usiku huu ulikuwa mwisho wa ndoto yake kuitawala dunia na mwanzo wa ndoto hiyo kutimia. Kesho ingekuwa siku nyingine kabisa katika historia ya maisha yake, historia ya Tanzania na historia ya dunia. Kesho atakuwa Ikulu, akitoa maagizo ambayo nchi nzima itayatekeleza. Mwaka kesho Afrika nzima ingemtii na muda mfupi baadaye dunia nzima ingetekeleza matakwa yake. Zimebakia saa tu! Aliwaza.
Safari ya kuifikia tamati ya ndoto yake haikuwa fupi. Kwa ujumla, ilikuwa ndefu, ngumu na iliyohitaji uvumilivu mkubwa. Tangu pale mikakati yake ilipoharibika kwa bahati mbaya, mwaka 1995, kufuatia ajali mbaya ya gari jijini London, Uingereza na kumfanya King Halfan ambaye angekuwa mtu wake pale Ikulu achoropoke toka mikononi mwake. Marlone, hakuipoteza ndoto yake. Badala yake ndio kwanza aliivalia njuga na kuzama katika mbinu na mikakati mbalimbali ya kujiandaa kuichukua nchi yake na baadaye dunia nzima.
Matarajio yake hayo yalipata nguvu zaidi pale mmoja wa ‘watoto’ wake, ambaye alimfadhili katika masomo ya sayansi
alipoibuka na ugunduzi wa kuumba upya na kisha kuviumbua virusi vya UKIMWI. Kwa kutumia maabara ya siri aliyomjengea msichana huyu yatima, ambaye wazazi wake wote walipoteza maisha kutokana na tatizo hilo, alifanikiwa kuumba kirusi ambacho kilifanya kazi ya kuteketeza chembechembe nyeupe katika damu kwa kasi ya kutisha, chembechembe ambazo pia alikuwa na uwezo wa kuziteketeza kwa kasi ileile kwa kuziagiza vinginevyo.
Msichana yule, ambaye alikuwa amefanya kazi katika maabarambalimbalizinazojihusishanavirusinakuwashangaza mabingwa wa taaluma hiyo duniani, aliufanya ugunduzi huo kwa nia njema kabisa. Alitarajia ufumbuzi wake uwe mwisho wa zahama ya UKIMWI ambayo inatishia kuiangamiza dunia. Lakini mfadhili au ‘baba’ yake alikuwa na mawazo tofauti, “Usimwambie mtu yeyote juu ya hili. Tutaitumia hii kuitawala dunia. Wewe na mimi. Wewe utakuwa malkia, mimi nikiwa mfalme!” alisema.
Msichana hakuelewa. Lakini alipomwagiwa fedha nyingi na vifaa mbalimbali vya uzalishaji wa virusi hivyo viliponunuliwa, huku maabara kubwa zikijengwa kwa siri katika nchi mbalimbali za dunia na mitandao ya kuzisafirisha na kuzisambaza kuundwa ndipo alipoelewa. Ndio kwanza akaelewa kuwa mfadhili wake huyo alikuwa mwendawazimu. Alijaribu kuiharibu fomula yake lakini akawa tayari amechelewa. Marlone alikuwa tayari ameinakili na kumfundisha mmoja wa wasaidizi wake mwenye ‘kifua’ zaidi ya msichana huyo.
Jaribio la awali kwa binadamu dhidi ya virusi hivyo lilikuwa lile la kupenyeza nyama zilizosagwa katika tafrija ya harusi moja kubwa jijini Dar es Salaam. Kila aliyekula nyama hiyo alipoteza maisha katika saa ishirini na nne zilizofuata. Jambo ambalo lilimsisimua sana Marlone na kumthibitishia kuwa alikuwa amepata silaha pekee aliyohitaji.
Majaribio ya virusi hivyo yalipoanza kufanyika kwa watu wasio na hatia, na kufanya madaktari bingwa duniani washindwe kuamini kile wanachokiona binti wa watu alifanya kitu pekee alichokuwa na uwezo nacho. Alijiua kwa kutumia virusi alivyovibuni mwenyewe.
Marlone hakujali. Aliendelea na maandalizi yake ya
kuidhoofisha na kisha kuitawala dunia.
Fedha haikuwa tatizo. Biashara zake halali kwa haramu pamoja na hujuma mbalimbali alizopata kufanya maishani mwake zilikuwa zimemwingizia mamilioni kwa mamilioni, ambayo aliyachimbia katika benki mbalimbali katika nchi mbalimbali duniani.
Hapa nchini, sura yake ya hadharani ilimchora kama mwekezaji mashuhuri anayejihusisha na uchimbaji wa madini, uingizaji na usafirishaji wa mafuta, umiliki wa viwanda vya chakula; na kadhalika. Kwa majina ya bandia alimiliki benki, kampuni ya bima na maduka kadhaa ya kubadili fedha. Kwa siri sana, alikuwa msafirishaji mkubwa wa dawa za kulevya mara nyingi akitumia ndege zake binafsi ambazo ziliandikishwa kwa majina bandia vilevile.
Katika daftari lake la siri la mishahara, Marlone alikuwa na orodha ndefu sana ya waheshimiwa sana katika kila pembe ya dunia. Wako marais ambao bila msaada wake ama kiuchumi ama kijeshi wasingeweza kuiona Ikulu. Wako majemedari, madaktari, wahandisi, wanasiasa na wengineo ambao waliishi kwa fadhila zake. Wengi kati ya hawa ama hawakumfahamu kabisa au walimfahamu kijuujuu katika sura na jina alilotaka yeye, kulingana na mazingira.
Wakati akikamilisha mtandao wake wa kusambaza virusi hivyo duniani, kupitia katika maji na chakula, ndipo lilipozuka tatizo la yule msichana wake kujiua, kwa maana ya kupingana na harakati zake, tatizo ambalo halikumsumbua sana kwani tayari alikuwa amelipatia ufumbuzi kitambo kirefu. Na baada ya hilo likafuata lile la Margareth…
Kwake Margareth alikuwa zaidi ya kila mtu. Alimtegemea kwa kila hali, kuliko yeye mwenyewe alivyofahamu. Uzuri wake usio wa kawaida ulikuwa chombo kilichomsaidia sana kunasa marafiki au maadui zake. Ujasiri wake katika matumizi ya mwili wake, akili zake na silaha yoyote anayoitia mkononi, ulikuwa msaada usio kifani kwake. Hata ile hatua ya kumwingiza katika jeshi la polisi la Tanzania, na baadaye kumtoa kwa kisingizio kuwa alikufa katika ajali ya gari, ilikuwa moja ya harakati zake za kuujenga vizuri zaidi mtandao wake katika jeshi hilo.
Hivyo, Margareth naye alipooneka kupingana na mkakati wake na baadaye kutoweka na siri zake lilikuwa pigo kubwa kwake, pigo ambalo hakulitegemea kamwe. Hata ile kauli yake ya kuamuru Margareth auawe aliitoa shingo upande, kinyume kabisa na tabia yake ya kuhukumu mtu kifo kwa urahisi kama anayeamrisha kuku achinjwe.
Akiwa anafahamu fika Margareth alivyofundwa akafundika katika taaluma ya ujasusi, Marlone alisita kuutumia mtandao wake wa kawaida katika kazi hiyo. Badala yake akamkodi mtu wa nje ambaye mara nyingi alitumiwa kwa mauaji. Ikamshangaza kuona muda mfupi baadaye mtu huyo akidaiwa kuikamilisha kazi aliyopewa. Hakuamini ingawa alikubali kummalizia malipo yake.
Hivyo, hakushangaa zilipoibuka taarifa za Margareth, aliyetarajiwa kuwa marehemu, kuonekana tena mitaani katika hali ya kuchanganyikiwa. Marlone alipoletewa picha ya marehemu alishangaa kuona kuwa ilikuwa ya Margareth yuleyule aliyemjua, jambo ambalo lilichanganya sana akili yake. Ndipo akachukua uamuzi wa kufanya lile jambo la hatari, kuuiba mwili wa marehemu toka jengo la maiti la Muhimbili na kuupeleka katika misitu ya Pugu ambako alikwenda kuukagua, kazi ambayo ilikamilika kwa kuhakikisha yule mlevi, Super D, anauawa kwanza na maiti yake kuchukua nafasi ya marehemu.
Marehemu alikuwa Margareth! Marlone hakuyaamini macho yake. Ni pale tu, kupitia mtandao wake aliouamini, alipofahamishwa juu ya ‘Margareth’ mwingine aliyeishi hoteli ya New Africa kwa siku kadhaa ndipo alipobaini kuwa walikuwa pacha. Ilimwuma kuona kuwa aliishi gizani kwa muda mrefu bila kujua kuwa Margareth alikuwa na ndugu, mzuri kama yeye, aliyekuwa akiitwa Mona Lisa.
Aliamuru mwili wa marehemu uzikwe humo msituni na
kaburi lake kufichwa vilivyo.
Mkasa huo wa kifo kisichokusudiwa ungeweza kabisa kuvuruga mikakati yake ambayo hadi hapo ilikuwa ikienda kwa mujibu wa mpangilio. Hivyo, alitoa amri nyingine, ya kuhakikisha Margareth anauawa haraka, mahala popote na wakati wowote, amri ambayo aliitoa kwa watu kadhaa bila
wao kufahamiana, miongoni mwao wakiwemo wale waliokuwa na jukumu la kufuta ushahidi kwa kumuua muuji kabla hajafungua mdomo wake.
Kitu kingine kilichomsisimua Marlone ni taarifa kuwa mtu aliyeachwa hai pale kitandani, baada ya aliyedhaniwa kuwa Margareth kuuawa, alikuwa Joram Kiango! Kiango, kijana hatari na machachari, ambaye amekuwa akivuruga harakati nyingi za hujuma hapa nchini na nje ya nchi, Joram ambaye alisababisha makaburu wa Afrika Kusini wabadili siasa zao na kumruhusu Nelson Mandela, mtu mweusi, aichukue nchi, baada ya harakati zao kubwa kutibuliwa, Joram mwenye roho ya paka! Joram anayeweza kuponyoka hata katika mikono ya nunda au kuchoropoka katika dimbwi la damu! La, hakuwa mtu wa kuishi. Amri ya kifo cha Margareth iliambatana na ile ya kumuua pia Joram Kiango mahala popote na wakati wowote.
Haikuwa kazi rahisi. Joram Kiango alitoweka, Margareth Johnson aligeuka mbogo. Badala ya kuuawa ni yeye aliyeua, sirini na hadharani. Hali iliyopelekea Marlone aanze kuingiwa na hofu. Hakuna uwezekano wowote wa kuendelea na program yake huku Margareth akipumua, Joram akimvizia.
Faraja na matumaini vilimrejea alipoarifiwa juu ya Joram Kiango na Margareth Johnson kuonekana wakipanda gari moja na kuondoka katika Uwanja wa Ndege wa Dar es Salaam kwa gari moja na baadaye kuripotiwa kuingia katika vyumba vyake, huko Bunju. Taarifa za polisi wa kiraia na wenye sare kuizingira nyumba hiyo pia zilimfikia. Mmoja wao, akiwa mtu wake, alimletea taarifa zote, hatua kwa hatua.
Haikuwepo namna yoyote ya Marlone kuipoteza nafasi hii adimu, Marlone aliamua. Akatoa amri ya kwanza kwa mtu wake mzito katika Jeshi la Wananchi wa Tanzania, nyumba ya Joram Kiango ilipuliwe, Joram, Margareth na kila kilichomo ndani ya nyumba hiyo kiteketezwe kabisa, amri ambayo ilitekelezwa mara moja.
Margareth alikuwa marehemu! Joram Kiango amekuwa historia! Hakuna tena ambacho kingesimama kati yake na azma yake ya muda mrefu.
Ni hayo ambayo yalimfanya achekelee, tabasamu likichanua
mara kwa mara katika uso wake. Sasa alikuwa na muda mfupi tu wa kusubiri kabla hajatoa amri nyingine. Baada ya hapo atatoa amri zote akiwa ndani ya Ikulu ya Dar es Salaam, akiwa juu ya kiti cha enzi.
Mara kwa mara Marlone aliitazama saa yake. Aliiona kama inayochelewa. Alikuwa akiwasubiri wajumbe wa kikao cha Ikulu watimie, Rais achukue nafasi ili aitoe amri yake hiyo, ya mwisho akiwa uraiani.
“Bado watatu Chifu,” aliendelea kupokea taarifa katika simu yake.
“Bado wawili.”
Na baadaye kidogo, “Bado mmoja!” Kisha, “Sasa anasubiriwa Rais tu!”
Marlone lishusha pumzi kwa nguvu. Akaitazama tena saa yake. “Dakika kumi tu baadaye,” alinong’ona akilazimisha tabasamu ambalo aliliona likianza kutoka kwa shida kuliko awali.
“Rais anaingia, Chifu!”
***
Kilikuwa kimoja kati ya vile vikao adimu sana, kikao cha watu wazito ambao dhamana ya uhai na usalama wa Taifa uko mikononi mwao. Alikuwapo mkuu wa Majeshi ya Ulinzi; alikuwapo Mkuu wa Kitengo cha Usalama wa Taifa; alikuwapo Mkuu wa Jeshi la Polisi, Mawaziri wa Baraza zima walialikwa pia.
Ukiwa mkutano wa dharura ulioitishwa ghafla kufuatia tukio la dharura, kila mmoja kati yao alikurupuka na kuja kikaoni. Wako waliotokea kwenye hafla mbalimbali, ambao suti na tai zao zilikuwa bado zinaning’inia katika shingo zao. Wako waliotokea kitandani, ambao walijitupia vazi lolote lililokuwa karibu. Wako ambao walitokea kazini, ambao hawakupata hata muda wa kubadili sare zao zilizolowa jasho na kuchakaa kwa vumbi. Miongoni mwao alikuwamo Inpsekta Haroub Kambambaya.
Si kwamba yeye alichakaa mwili na mavazi tu, bali pia alikuwa amechakaa kwa uchovu, njaa na ukosefu wa usingizi. Alikuwa hajapata mapumziko wala fursa ya kutia
chochote mdomoni kwa takribani saa ishirini na nne sasa. Akiwa Bunju, macho yake yakishuhudia nyumba ya raia na chochote kilichomo kikiteketezwa mbele yake, wito wa kuja Ikulu aliutelekeza bila kupitia nyumbani wala ofisini. Alikuwa mmoja kati ya waliotangulia kuingia ukumbini hapo na kusubiri kimya juu ya kiti chake. Akiwa mmoja kati ya viongozi wakuu wa operesheni ile, kila mmoja alijaribu kumdodosa juu ya tukio hilo, “Ni kweli haya tunayosikia? Ilikuwaje?”
“Hicho ulichosikia kizidishe mara nne ndipo utaupata ukweli wa tukio zima,” Kambambaya limjibu mmoja wao, akimwonyesha dalili kuwa hataki mazungumzo zaidi.
Minong’ono ilizimika ghafla mlango wa Ofisi ya Rais
ulipofunguka naye kuingia taratibu.