Si ajabu basi kumsikia Paulo anakakamia kwa hasira isiyofichikana akisema:
Lakini nifanyalo nitalifanya, ili niwapinge hao watafutao nafasi wasipate nafasi; ili kwamba katika neno hilo wajisifialo waonekane kuwa kama sisi. Maana watu kama hao ni mitume wa uwongo, watendao kazi kwa hila, wanaojigeuza wawe mfano wa mitume wa Kristo. Wala si ajabu. Maana Shetani mwenyewe hujigeuza awe mfano wa malaika wa nuru. Basi si neno kubwa watumishi wake hao wakajigeuza wawe mfano wa watumishi wa haki, ambao mwisho wao utakuwa sawasawa na kazi zao.
2 Wakorintho 11.12-15
Ni dhaahiri kuwa Paulo anakusudia kwa matusi yake haya kuwatukana wale wanafunzi wa Yesu, ambao Yesu mwenyewe aliwateua, ambao wakiongozwa katika kutimiliza ujumbe wa Yesu na watu kama Yakobo, ambaye anaambiwa kuwa ni nduguye Yesu.
Je, sisi tutendeje tunapokabiliwa na maoni mbali mbali yanayogongana miongoni mwa watu ambao wote wanadai kuwa ni wanafunzi wa Yesu, ijapokuwa huyu mmoja Paulo, hata hakumwona Yesu, na huo ushahidi wa kuwa kamwona katika njozi ni wake yeye tu, tena unagongana na kupingana wenyewe kwa wenyewe?
Tutendeje?
Liliopo ni tuyaendee mafunzo yake mwenyewe Yesu, ambayo ijapokuwa yametatanishwa na maongezo na mapunguzo, lakini hayaachi kuwepo ya kutosha kwa jumla kutufahamisha nini khasa mafunzo yake.
Ikiwa kweli tunatafuta hakika ya mambo na ukweli wake basi tutayachukua yale yalio wazi, dhaahiri, katika maneno yake mwenyewe Yesu, na tusiyabali yale ambayo ni maneno ya wasimulizi.
Kadhaalika yasitushughulishe yale ya mafumbo yanayotatanisha tukajaribu kuleta tafsiri na maelezo tuyapendayo nafsi zetu. Ikiwa ni kufasiri basi tufasiri fumbo kwa kauli ya Yesu ilio wazi. Wapotoshaji hufanya kinyume cha hayo.
Mafundisho yaliyotulia kabisa ya Yesu ni yale aliyohubiri juu ya Mlima wa Zaituni.
Na maoni yake yaliyo wazi na kauli ya kukata juu ya sharia na matendo, ni yaliyomo katika sura 5 ya Mathayo. Akizungumzia juu ya wale wanaodai kuwa wao ni wafuasi wake, na kuwa ati wanafunza mafunzo yake, na huku kumbe wanayapotoa yale aliyoyafunza, Yesu anaambiwa kasema:
Si kila mtu aniambaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni. Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi? Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu. Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba. Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa.
Mathayo 7.21-27
Hayo ni maneno aliyokhitimishia Yesu mawaidha yake juu ya Mlima wa Zaituni.
Ni maneno yaliyokaa sawa, yawazi, hayana ubabaishi.
Ni nani hao "watendao maovu", hao wapumbavu, wasiofuata mafunzo ya Yesu wakayatenda, mafunzo ambayo msingi wake ni kutimiliza sharia na manabii, na kutenda mapenzi ya Mungu?
Ni nani hao wanaodai kufanya miujiza na kuponyesha watu kwa jina la Yesu, na kudai kuwa ni mitume wa Kristo, na huku wanapinga mafunzo yake, na kuwaambia watu kuwa wataokoka kwa imani tu kwamba Yesu kafa msalabini kwa ajili yao, bila ya haja ya vitendo?
Ni nani hao wanaolitumia jina la Yesu naye mwenyewe atawakataa?
Kama tuna akili basi yafaa tuitumie.
Tusiwe kama mtu mpumbavu ajengaye nyumba yake juu ya fungu la mchanga.
Tutaanguka, na anguko letu litakuwa kubwa.