Zanzibar yatangaza bajeti
na Saada Said
SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) jana ilitangaza bajeti yake ya mwaka 2008/09, iliyoipa jina la Bajeti ya Maendeleo, ambayo kama ilivyo ile ya Muungano, imeongeza kodi na ushuru katika bia, vinywaji vikali na sigara.
Akisoma bajeti hiyo katika Baraza la Wawakilishi jana, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais anayeshughulikia Fedha na Uchumi, Dk. Mwinyihaji Makame Mwadini, alisema lengo la kuifanya bajeti hiyo kuwa ya maendeleo, haliishii kwenye maneno matupu.
Alisema ili kuakisi lengo hilo, serikali imeamua kwa dhati mwaka huu, kutenga fedha nyingi kwa ajili ya miradi ya maendeleo tofauti na miaka iliyotangulia.
"Ni bajeti ya maendeleo, kwa maana kwamba sehemu kubwa ya bajeti imeelekezwa kwenye matumizi ya maendeleo kuliko matumizi ya kawaida kama ilivyokuwa katika bajeti zilizopita," alisema waziri huyo wakati akiwasilisha bajeti hiyo jana jioni.
Akitoa takwimu, Makame alisema katika mwaka ujao wa fedha, fedha zilizotengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo ni sh bilioni 42.8, ambazo ni sawa na asilimia 28.7 ya bajeti yote.
Alisema mipango hiyo inatokana na kukua kwa pato la taifa na kutolea mfano sekta ya viwanda ambayo mchango wake katika pato la taifa ulipanda kutoka asilimia 14.8 mwaka 2006 hadi kufikia asilimia 15.4 mwaka 2007.
Alisema kwa sehemu kubwa, ongezeko katika sekta hiyo lipo katika ukuaji wa sekta ya ujenzi, ambayo mchango wa pato lake umeongezeka kutoka asilimia 7.5 mwaka 2006 hadi asilimia 8.8 mwaka 2007.
Alisema kulikuwa na angezeko la asilimia 34.5 katika thamani ya shughuli za ujenzi visiwani hapa, kutoka sh bilioni 38.3 mwaka 2006 hadi sh bilioni 51.5 mwaka 2007.
Waziri huyo alisema kwa kuzingatia ukuaji wa uchumi na malengo ya mpango wa bajeti ya mwaka 2008/2009, serikali imelenga kukusanya mapato ya ndani yenye jumla ya sh bilioni 134.550.
Katika mapato hayo, sh bilioni 124.709 zitatokana na kodi na sh bilioni 9.841 zitatokana na mapato yasiyokuwa ya kodi.
Kwa upande wa matumizi, alisema kwa mwaka wa fedha 2008/09, serikali imepanga kutumia jumla ya sh bilioni 341.709 kwa kazi za kawaida na miradi ya maendeleo kulingana na ukusanyaji wa mapato.
Hata hivyo, alisema kwenye mipango ya makusanyo na matumizi, inajitokeza nakisi ya bajeti ya sh bilioni 207.159.
Akifafanua kuhusu mapato, alisema kuwa serikali inatarajia kupata sh bilioni 23.407 kama misaada ya kibajeti na sh bilioni 8 kutokana na fedha za misamaha ya madeni, na hivyo kupunguza nakisi ya bajeti hadi sh bilioni 175.752, ambazo zitazibwa kwa mikopo na ruzuku.
Alisema Serikali ya Mapinduzi Zanzibar inatarajia kupokea mikopo yenye thamani ya jumla ya sh bilioni 72.427 na mikopo ya fungate ya sh bilioni mbili pamoja na ruzuku ya miradi ya sh bilioni 101.325.
Kwa upande mwingine, serikali imeamua kuitumia bajeti hiyo, kutimiza malengo yake ya kuzuia matumizi ya kilevi kupita kiasi.
Utekelezaji wa azima hiyo unajionyesha katika viwango vya kodi zilizopangwa kwa vileo. Dk. Mwadini alisema kuwa serikali imedhamiria kuweka viwango vipya vya kodi ya sh 400 kwa lita ya bia na vinywaji vikali na kodi ya sh 500 kwa kila sigara 1,000 zinazoingizwa Zanzibar.
Dk. Mwadini alisema serikali imechukua hatua hizo kama njia ya kudhibiti matumizi yanayoongezeka ya vinywaji vikali na sigara, kutokana na vinywaji hivyo kuathiri afya za wananchi.
"Kutokana na athari za kiafya kwa matumizi ya bidhaa hizi, serikali imekusudia kuchukua hatua za kupunguza matumizi yake na Sheria ya biashara itapitiwa kwa lengo la kupunguza matumizi yake pia," alifafanua Dk. Mwadini.
Akizungumzia hali ya uchumi, waziri huyo aliliambia Baraza la Wawakilishi kuwa uchumi wa Zanzibar umekua kwa asilimia 6.5, hatua ambayo imetokana na kukua kwa pato la taifa.
Akifafanua, alisema kuwa pato la taifa limekua hadi kufikia sh bilioni 588.5 mwaka 2007. Mwaka 2006, ukuaji wa uchumi ulifikia asilimia 6.1.
Kwa upande wa pato la mtu binafsi, nalo limeonekana kukua hadi kufikia wastani wa sh 518,000 kwa mwaka 2007, ikilinganishwa na sh 459,000 mwaka wa 2006.
"Ni matarajio yetu kwamba kwa mwelekeo huu, kasi ya ukuaji wa uchumi itakuwa kubwa zaidi kwa mwaka ujao na hivyo hali za maisha za wananchi zitakuwa bora zaidi," alisema.
Dk. Mwadini alisema sekta nyingine iliyochangia kwa kiasi kikubwa kuimarika kwa uchumi wa Zanzibar ni utalii. Alisema kuwa kulikuwa na ongezeko la idadi ya watalii walioingia visiwani humo.
Akitoa takwimu, alisema kuwa mwaka juzi, waliingia watalii 137,111, lakini idadi hiyo iliongezeka kwa asilimia 4.5 mwaka jana kutokana na watalii 143,265 walioingia.
Kwa mujibu wa bajeti hiyo, sekta ya huduma za jamii ndiyo inayoongoza kwa mchango katika pato la taifa, na Dk. Mwadini alisema kuwa, mchango wa sekta hiyo katika pato la taifa umeongezeka na kufikia asilimia 43.9 mwaka 2007, kutoka asilimia 43.5 za mwaka 2006.
Lakini mchango wa sekta ya kilimo umeyumba. Dk. Mwadini alisema kuwa mchango wa sekta hiyo umeshuka kutoka asilimia 30 kwa mwaka 2006 kufikia asilimia 27 mwaka 2007.
Hata hivyo, alisema hali hiyo ilijitokeza baada ya sekta hiyo kuonyesha ukuaji mkubwa katika miaka kadhaa iliyopita ambapo ulifikia kiwango cha asilimia 19 mwaka 2005.
Akifafanua sababu zilizochangia mchango wa sekta hiyo kushuka, alisema kulikuwa na sababu kadhaa, lakini nyingi zilisababishwa na wawekezaji.
"Kumejitokeza tabia kwa baadhi ya wawekezaji wa kigeni kuhodhi maeneo ya ardhi kwa muda mrefu bila ya kuyaendeleza, tabia hiyo inazuia fursa kwa maeneo hayo kutumiwa na wawekezaji wengine walio makini. Hivyo katika mwaka wa fedha wa 2008/09 serikali imekusudia kukamilisha mapitio ya ada za ukodishaji wa ardhi kwa kuweka viwango," alisema.
Kwa upande mwingine, Dk. Mwadini alisema katika mwaka ujao wa fedha, serikali imedhamiria kwa kiasi kikubwa kutekeleza hatua mbali mbali zilizopitishwa kwa kufanyiwa kazi kwa mwaka wa 2007/08, na kuanzisha hatua chache mpya.
Alizitaja baadhi ya hatua zilizopitishwa mwaka jana na ambazo zitatekelezwa mwaka huu, kuwa ni pamoja na ukusanyaji wa ada ya usalama wa anga, ushuru wa kuongeza ujuzi, kukamilika kwa mapitio na kuanza rasmi kutoza viwango vipya vya ukodishaji wa ardhi, utoaji wa ada maalumu ya biashara kwa vinywaji vikali, bia na sigara.
Alizitaja baadhi ya hatua mpya zitakazotekelezwa kuwa ni pamoja na kupitia sheria ya usajili wa majina ya biashara na kuanza rasmi utozaji wa kodi kwenye majengo.