Naitwa Analyse, na hii ndio safari yangu ya maisha...

Naitwa Analyse, na hii ndio safari yangu ya maisha...

.... Fursa nyingi mwanzoni huwa na changamoto, lakini fursa ya hazina ya mjerumani ina zaidi ya changamoto. Tulifika hadi Nyasa. Ulizia sana alipo huyo mzee, maana huyu jamaa sio kusema kwamba alikuwa anajua pakumpata, na yeye alisikia tu habari zake. Tulizunguka sana kwenye vijiji vya kule, mwisho wa siku tukafanikiwa kuelekezwa hadi nyumbani kwake kabisa. Tulipokelewa vizuri, tukaeleza shida yetu, wakatuelewa. Wakatwambia hizo habari mnazoziongea kuhusu mzee ni za kweli, ila zinaendelea kuenezwa kila siku japokuwa mhusika mwenyewe (yule mzee) ameshafariki yapata mwaka sasa. NIKACHOKA.

Ikabidi tuondoke, tukiwa njiani kuna mzee mwingine akatudaka. Akasema kama shida yenu ni hiyo naweza kuwasaidia. Ikabidi tumskilize. Tukafika kwake, nae akatupa maelezo ya kina. Kisha akatwambia, kama kweli mmezamilia kuzitafuta hizi hazina, basi kuna vitu muhimu inabidi muwe navyo. Cha kwanza inabidi muwe na vichaa/matahira wawili, hawa watawasaidia kuwakinga kipindi mnaingia kufukua hazina, alaf kitu cha pili inabidi muwe na Mjerumani au Muisrael kwa ajili ya kutafsiri baadhi ya mambo.

Kwangu masharti yote mawili niliyaona magumu, tena sana. Namtoa wapi mjerumani au muisrael? Pia hao vichaa, sawa hata tukiwapata, ni vipi tutaweza kuwadhibiti tukiwa nao (maana vichaa wanajulikana mambo yao),mnaweza mkaona hazina, yeye ghafla akatimua mbio, sasa kama wao ndio kinga, hapo tufate hazina au tuwakimbize? Na bora angekuwa mmoja, wapo wawili. Vipi kila mmoja akikimbia na njia yake?

Nadhani yule mzee aliona wasiwasi wangu, akasema msiwe na shaka vijana, nitawasaidia hayo mambo yote mawili, cha msingi muwe na kiasi cha pesa hata kidogo. Nikasema sawa mzee, pesa kidogo ipo. Vizuri, basi leo pumzikeni kwavile mmetembea umbali mrefu sana hadi kufika hapa, tusubirie kesho asubuhi tuanze mchakato wenu uliowaleta. Alitufanyia mpango wa msosi, tukala. Mzee pamoja na umri kwenda ila alikuwa anaishi peke yake, kibachela. Hakuwa na kitu cha thamani zaidi ya dhana za kilimo.


Kesho yake tulichelewa sana kuamka, sijui ni sababu ya uchovu au vipi. Nakumbuka tuliamka kwenye mida kama ya saa nne hivi. Pako kimya kabisa, wanaskika ndege tu. Katika safari yetu, mimi nilikuwa na begi la mgongoni, jamaa yangu nae hivyo hivyo, sema lake lilikuwa dogo kidogo. Ila cha ajabu asubuhi hiyo tulikuta mabegi yote yapo wazi, vitu vimetupwa tupwa ovyo. Kuangalia vizuri, hela hakuna na mzee hayupo. Baharia wa nchi kavu nimelizwa. Aisee nilitamani kulia. Kilichonisaidia, huwa nikiwa ugenini hela zangu siweki zote sehemu moja. Nakumbuka kuna baadhi zilikuwa kwenye begi, zingine kwenye mfuko wa suruali, na nyingine niliweka kwenye viatu (nilitoa kapeti la ndani ya kiatu, nikaweka mtonyo alafu nikalirudisha). Nilifanya hivyo kwenye viatu vyote viwili.

Yule Mzee mpaka leo naamini ujana wake aliulia Dar es salaam. Maana hela za kwenye begi aliziona, za kwenye suruali aliziona na za kwenye viatu aliziona. Sema za kwenye viatu alichukua kwenye kiatu kimoja, nahisi baada ya kukuta hela kwenye kimoja hakufikiria kama ningeweza kuweka na kwenye kingine. Jamaa yangu yeye alipigwa zoote.

Ikabidi tutoke nje tunaita, ila hamna kitu. Ikabidi tuchukue vitu vyetu tusepe. Njiani ni mashamba tu, bahati nzuri mbele tukakuta familia inalima. Tukajaribu kuwaelezea mkasa wetu. Tulivyowaelekeza nyumba tuliyokuwa pamoja na yule mzee alivyo, bahati nzuri wakamjua. Wakatwambia ile ni nyumba ambayo hutumiwa kipindi cha mavuno au wakati wa kulima, ila haikaliwi na mtu. Wakatuelekeza anapokaa. Tukamfata.


Fika mpaka kwake, tukamuulizia, wakatuelekeza yupo kilabuni, tukaelekezwa tukaenda. Pale kilabuni mzee tulimkuta yupo chakali, ashalewa pombe zao za kienyeji zile. Anatuuliza mnasemaje? Nilikuwa nimefura kwa hasira, nikamwambia Mzee tunasafari ndefu, tupe hela zetu tusepe. Kwa sauti ya kilevi mzee anasema hela ameshalipia madeni, iliyobaki ndio ile ameinunulia pombe, hana kitu labda na sisi tukae tunywe.

Nilimwangaliaa yule mzee wee, ila nkakosa cha kumfanya. Mzee ikabidi atuchane ukweli, robo ya ujana wake ameipotezea kwenye kusaka hazina ya mjerumani, na mpaka anazeeka hajawahi hata kuiona picha ya hiyo pasi ya Mjerumani. Mwishoni akatwambia "Nimepoteza hela nyingi sana vijana wangu kwenye kusaka hizo hazina, nimedhurumiwa mara nyingi sana, tena nyie mnabahati walau niliwapa hata chakula, mwenzenu hata maji nilikuwa sipewi na hela inaenda, hii hela fanyeni kama mmelipia twisheni tu ya maisha, nyie vijana bado mnanguvu mtapata zingine"

Hasira tuliyokuwa nayo sijui niielezee vipi, Mzee nae anatuangalia kilevi, hana hata chembe ya wasi wasi. Ikabidi tusepe tu, hakuna namna.

*** *** *** *** *** *** ***

Kufika town jamaa ananiuliza tunafanya nini kutokea hapa? Nikamwambia sina cha kufanya na wewe, we endelea tu na harakati zako (Hasira za kupoteza hela nyingi kwa wakati mmoja zilikuwa bado zipo kichwani).

Nikarudi kwenye kufanya vibarua vyangu huku natafakari kitu cha kufanya. Kuna siku likanijia lile wazo " Kama mnataka mali, mtazipata shambani". Nikaamua kujikita kwenye kilimo. Amini na kwambia "KAMA UNATAKA STRESS, BASI UTAZIPATA SHAMBANI" maana kama hujaparalaizi basi unaweza ukafa kabisa.


Maisha ni safari,kuna mnaosafiri kwa ndege,wengine kwa miguu,ila wote tunaelekea sehemu moja. Usitishwe na umbali wa unakoenda,tiwa nguvu na ulikotoka,nia ndio kila kitu


Sikiliza kilichonikuta Baharia wa nchi kavu.....



........
Words kwa paragraph ya mwisho hapo
 
... Nilipata mzuka wa kuingia kwenye kilimo baada ya kufanya kazi kwenye shamba la matikiti la mzee mmoja hivi. Mavuno aliyoyapata ndio yalinishawishi na mimi kujikita huko.

Kutokana na ka akiba ambako nilikuwa nimekusanya mpaka muda huo, nikatafuta shamba kule kule Songea. Nilibahatika kupata eneo la kukodi sehemu fulani inaitwa Mpitimbi, heka 1. Kuna dogo nilikuwa nimezoeana nae kutokana na mishe za vibarua, huyo ndio nikawa napiga nae. Niliandaa shamba vizuri (robo 3 heka),weka samadi ya kuku, mwagilia kwa muda wa wiki kama mbili alafu ndio nikapanda mbegu zangu. Siku chache baadae zikaanza kuchipua. Ila walitokea wadudu wakaanza kushambulia yale majani mawili ya mwanzo kabisa. Nikajitahidi kupiga sana dawa, hatimaye nikafanikiwa kudhibiti. Hapo ile robo heka iliyobaki wazi,nikaweka maharage ya njano,lengo ni kujaribu kuona mwelekeo wake pia.


Miezi ikakata, tikiti zikatoka vizuri japo sio kwa wingi na ukubwa niliotarajia. Utata ukaja kwenye soko. Nakumbuka mnunuzi alikuja hadi shambani kwangu. Wakati mm gharama toka mwanzo mpaka yanakomaa nilitumia kwenye kama laki 7 mpaka 8, ila hesabu za kuyauza yote hela iliyokuja ni kama laki 3 na 40. Tulizozana sana na yule mnunuzi, ila mwisho wa siku ikawa ndio hivyo. Mpaka leo ile karatasi ya mahesabu na yule mnunuzi ninayo (Badae naweza nikaiweka hapa).

Kule ikabidi nitoke baada ya kuvuna na yale maharage pia ambapo nilipata kilo kama 60 (mimi nilipanda kilo 15), nikatafuta eneo jingine la kulima. Kuna sehemu inaitwa mshangano, kuna bonde la umwagiliaji, nikapata nusu heka. Nikaamua kulima tena tikiti, maana kila nikifikiria yule mzee wa kwanza alivuna fresh tu kwanini mm ishindikane?

Mwanzo mambo yalienda vizuri tu. Dawa nilikuwa napiga kila baada ya wiki au wiki mbili kutegemeana na aina ya dawa. Nakumbuka yalikuwa yamebakiza kama wiki 3 yatimize miezi mitatu, nilienda kwa ajili ya ukaguzi wa kawaida tu na kupiga dawa. Kama sikuzimia siku ile basi sizimii tena. Nafika shambani, kila tikiti unaloshika linabonyea, kugeuza chini limeanza kuoza. Nilisizi kwa dakika kadhaa, nikakaa na chini kabisa.

Badala ya kuuzia watu, niliishia kumuuzia mfuga nguruwe, kiufupi yakageuka chakula cha mifugo.


Ile kilo 60 ya maharage ambayo nilikuwa nafikiria pengine nije kuyafanya kama mbegu upya maana mwelekeo wa kilimo chake niliuona kidogo mzuri,nilikuwa nayatunza gheto. Nilipoyavuna na kuweka kwenye kiroba,sikuyapiga dawa,siku nakuja kuyacheki nakuta matobo matobo tu,wadudu washapita.


Kutokea hapo nikafulia upya. Nikaanza tena kufanya vibarua. Kuna jamaa akanishawishi sana tulime mahindi maana yanalipa ila sikumuelewa, nikaendelea na vibarua. Kuna siku nikapata tenda ya kuvuna na kupakia tangawizi kwenye lori, maana kuna mteja alinunua sasa anahitaji huo msaada. Nikaenda kupiga kazi, hiyo sehemu inaitwa Madaba. Tunalima na kujaza kwenye maroba, kila ukijaza kiroba kimoja unapewa 5000. Baada ya kama siku 5 kazi ikaisha tukarudi na lori hadi town Magingo kwa mbele kidogo kuna soko la tangawizi . Kufika pale baada ya ukaguzi, nikapata kibarua cha kupakia kwenye lori la mteja. Kazi imeisha, naenda kupokea ujila wangu, nakuta bosi ni faza, yani baba angu kabisa. Kumbuka hapo tokea nilipoondokaga home sikiwahi kurudi wala kuwa na mawasiliano nao. Na toka tunazaliwa,baba alikuwa anajishughulisha na biashara za kununua na kuuza mazao,japo kipindi naondoka nyumbani alikuwa shughuli zake zilikuwa ndani ya mkoa wetu tu,kati ya vijijini na mijini. Na ndio biashara iliyotukuza,kumuona pale maana yake biashara zake zimepanuka.

Tuliangaliana kwa dakika kadhaa, natamani kama nimkumbatie, maana kiukweli baharia nilikuwa nimeshapigika sana. Atleast hata ningekutana na mama katika mazingira yale walau ningepata faraja kidogo, mshua kauzu ananiangalia tu bila kusema chochote.

Nikamwamkia akaitikia vizuri. Ikabidi nimuombe msamaha. Badala ya kuitikia, ananiuliza hapa umekuja kuniomba msamaha au kufata ujira wako? Nikamwambia lengo ilikuwa ujira mzee, ila baada ya kukuona sina budi kuomba msamaha. Mshua ananiambia kama ungetaka kuniomba msamaha ilibidi urudi unifate nyumbani, yani tunakutana tu kwa bahati mbaya ndio unaomba msamaha, tusingekutana je?

Nikawa mpole kidogo. Ila nikamwambia natamani kurudi ila nauli ndio ilikuwa tatizo, lasivyo ningesharudi kitambo. Mshua akasema utarudi nyumbani kama ulivyoondoka, yani nikupe nauli ili tu uje kuniomba msamaha? Kama kweli unania basi tafuta nauli urudi, we si mwanaume? Nikamwambia lakini nauli ya kunitoa nyumbani ulinipa wewe, kwanini usinipe na ya kurudi, maana sina kitu kweli.

Nikimwangalia mshua naona kabisa kuwa ananionea huruma, ila kwa nje ameamua kuleta ule ukauzu wa kiume. Acheni mama aitwe mama tu, pale angekuwa yeye nadhani yale maongezi tungekuwa tunayafanya huku tumekaa sehemu tunakula. Faza alikuwa mkavu usoni hadi na mimi nikaanza kupata wasi wasi kama ule wa kwake wa kipindi kile, kuwa mimi ni mwanae kweli? Ila nilivyokumbuka ile kauli ya mama alafu nikaangalia pua ya baba, nikaona bila shaka huyu ni baba angu.

Baada ya kuniangalia sana, sasa sijui kama na yy alikuwa anawaza kama kweli me mwanae, au alikuwa anaangalia pua ili kuthibitisha kauli ya mama, sijui. Ila alimuita Mfanyabiashara mwenzie aliyekuja nae, wakazungumza pembeni alafu nikaona kapewa hela.

Alirudi kwangu akanikabidhi laki 3 na 50. Akaniambia "Ujue kama ungekubali kuendelea na shule, basi ile hela niliyokupa mara ya kwanza isingetosha, awamu ya pili ilibidi nikupe tena. Sasa hii hela ninayokupa kuna posho yako ya kazi ya leo pamoja na ya mahitaji yako ya shule kipindi kile kama ungesoma. Hata siku moja usijekusema hukusomeshwa.

Nikapokea ile hela, nikashukuru sana. Mshua yeye ananiangalia tu. Nikamuomba tena msamaha. Ila msimamo wake ukawa ule ule, ukitaka kuniomba msamaha rudi nyumbani,maana hujui hata mama yako yupo na hali gani miaka yote umeondoka na hakuna anayejua upo wapi. Kwa mara ya kwanza nikakumbuka kuulizia hali za ndugu zangu kule nyumbani, hasa mdogo wangu wa mwisho na Mama. "Ukitaka kujua hali zao, fanya matumizi mazuri ya hiyo hela, sina haja ya kukwambia hali zao, rudi nyumbani ujionee" ilo ndio jibu alilonipa.


Tukaachana, nikarudi zangu kwenye ghetto langu kule moonlinght. Pamoja na maongezi yote yale na Mzee, ila sikumuomba namba ya simu, sio kwamba sikukumbuka, ila nilikuwa nasubiria walau aniulize kama nina simu. Na yeye hakuniuliza wala kuomba namba yangu. Sio kwamba hakufikiria ilo, nilikuja kujua baadae kuwa nae ilo swala alilifikiria ila hakujishughulisha nalo.

Huwa tunarithi vitu na tabia toka kwa wazazi wote wawili, ila nahisi wanaume tunarithi vingi sana toka kwa baba zetu kuliko toka kwa mama. Ukiona huna tabia unazofanana na mzee wako,muulize mama vizuri pengine huyo baba ni mlezi tu


*** *** *** *** *** *** ***


Kesho yake wakati naendelea kutafakari namna ya kurudi nyumbani, jioni nilienda kwenye kijiwe cha draft sehemu moja inaitwa Bombambili. Story za hapa na pale, kuna jamaa akaanza kuongea kuhusiana kilimo cha mbaazi jinsi kilivyo na hela na soko la uhakika. Baadae nikapiga stori kwa kirefu na yule mdau, tukabadilishana namba.

Niliporudi ghetto, baada ya kutafakari sana nikajiambia inabidi nisubirie msimu wa kilimo ufike nilime mbaazi hata msimu mmoja, nipige hela alafu ndio niende nyumbani.

Nikaghairi kurudi nyumbani kwa wakati ule, nikaanza ushanta ili nipate hela ya kujazia kwenye mtaji. Hutakiwi kujikita kwenye kilimo ikiwa unapresha. Kilichoenda kunikuta sitakaa nisahau kamwe. NILILIMA MBAAZI KIPINDI CHA MAGU.

Analyse #Baharia wa nchi kavu.

........
Hahaha....mzee baba alikuwa kauzu zaidi ya dagaa
 
Aisee the same to me.
Kilichonikuta mwaka huu n balaaa
Nimekodi nimekodi sehemu kubwa sana ya kulima mpunga kwa pesa nyingi jumlisha walimaji wapandaji daaaa kilichonikuta,
Jua limepiga mpunga ote kwisha yan sijavuna hata gunia moja aisee.
Kilimo sikia tu mwenzio amelima amepiga gunia 50.
Mbona masanja anasema amekuwa tajiri kupitia kilimo Cha mpunga?
 
Mkuu umepoteza sana nguvu sijui kwa nini hukuwaza hata kuuza mitumba viatu au nguo ambavyo haviozi? kuliko kilimo? Baba yako ile laki 3.5 ulikuwa mtaji kabisa.

Kumbe juzi tu kipindi cha magu?

Nyumbani ulitoka mwaka gani?
Sio kipind cha magu hapo kanogesha tu story

We hukusoma kiswahili kwani ?!

Teh .....

[emoji28][emoji28][emoji28]
 
Somehow ulikosea kukataa school,ungeenda halafu ukifika unabadil combination juu kwa juu huko shuleni.
Kuna mjomba wangu mmoja alifaulu kwenda form one miaka ya 90,akaanza form one akisomeshwa kwa tabu na bibi,alipofika form 3 akaanza kugoma shule,huku akidanganya kudaiwa hela kibao shuleni ,bibi kwa tabu akawa anampatia anaenda kula Bata na marafiki zake pamoja na mademu zao.Walipofika form 4 wakasimamishwa shule yeye na group lake lote,wakaambiwa waje kufanya mtihan wa mwisho tu.Ulipofika muda wa mitihan akawa anapelekwa shule na tax na dada yake,ila dada yake akawa anamwambia fulan utakuja juta kwa hili.Akamaliza lakin alifel,leo hii yapata miaka 16,amepigika anajuta hana hamu.Kutwa kutupiga mizinga wajomba na kulalamiki hatumsaidii.
 
Hizi ni picha mbili zinaonesha mahesabiano kati yangu na yule jamaa mnunuzi wa matikiti. Picha ya kwanza palipozungushiwa na bluu hiyo ni bei alafu kushuka chini ni idadi. Mfano matikiti ya yeye kuyanunua kwa elfu mbili yalikuwa manne tu.

Picha ya pili palipozungushiwa na kijani ni hela ambayo aliyotakiwa anipe kulingana na mahesabu. Ilikuwa 318400 (haikufika hata laki 3 na 40)

Screenshot_20190616-133812.jpeg
IMG-20190616-WA0002.jpeg
 
Back
Top Bottom