Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,872
- 34,363
Hussein Semdoe na Burhani Yakub, Handeni
WANAJESHI wawili ambao ni marubani wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) wa Kambi ya Ngerengere mkoani hapa, wamekufa baada ya ndege waliyokuwa wakisafiria kuligonga gari la watalii na kupinduka.Ndege hiyo ya Jeshi ambayo inatumika katika mafunzo ya kijeshi, jana ilitua barabarani na kusababisha ajali iliyoua marubani wawili wa Jeshi la Wananchi (JWTZ) baada ya kugongana na lori lililokuwa limebeba watalii.
Ndege hiyo ndogo yenye namba F59119 iligongana na gari hilo eneo maarufu kwa jina la Zimbabwe lililo Kijiji cha Manga, Kata ya Mkata wilayani Handeni.
Baadhi ya watu walioshuhudia ajali hiyo ya nadra sana kutokea walieleza kuwa waliiona ndege hiyo ikishuka kabla ya kutua katikati ya barabara na baadaye kujaribu kuruka tena, kitu kinachoonyesha kuwa rubani alikuwa katika harakati za kuinusuru.
Walisema, hata hivyo, ndege hiyo ilishindwa kuruka juu na kuserereka barabarani.
Walisema wakati ikiyumba, ndege hiyo nusura iligonge basi la kampuni ya Simba Mtoto lililokuwa likitokea jijini Tanga kuelekea Dodoma.
Kaimu kamanda wa polisi mkoani Tanga, Jafari Mohammedi ambaye alikuwa kwenye eneo la tukio hilo, aliwataja waliokufa kuwa ni rubani wa ndege hiyo Meja Kathbet Leguna (41) na mwanafunzi wake Luteni Andrew Yohana Kijangwa (31).
Mmoja wa wafanyakazi wa gari hiyo iliyogongana na ndege hiyo Solomon Talalai alisema ndani walikuwepo watu 24 ambao 19 kati yao ni raia kutoka Uholanzi, wanne kutoka Kenya na mmoja Mtanzania.
Alisema ajali hiyo ilitokea kwa gari hilo kugongana uso kwa uso na ndege barabarani.
Kamanda Mohammed alisema kuwa maiti hao walipelekwa hospitali ya Magunga iliyopo wilayani Korogwe, huku taarifa nyingine zikieleza kuwa maiti hao walisafirishwa jana kwenda kuhifadhiwa Hospitali Kuu ya Jeshi Lugalo, Jijini Dar es Salaam.
Habari zaidi zinasema kuwa marubani hao walikuwa katika mazoezi ya kawaida katika anga ya eneo hilo.
Lakini wakati ikiwa angani, inaelezewa kwamba ilipata hitilafu ndipo rubani akaamua atue barabarani ili kuokoa maisha yao, lakini kwa bahati mbaya gari hiyo ikiwa kwenye mwendo mkali iliigonga.
Viongozi waliofika kwenye eneo la tukio ni mkuu wa mkoa wa Tanga, Meja Jenerali Saidi Kalembo, mkuu wa wilaya hiyo, Kapteni Seifu Mpembenwe na viongozi mbalimbali wa kisiasa.
Mpaka jana jioni, JWTZ ilikuwa halijatoa taarifa kuhusu chanzo cha ajali hiyo na polisi walikuwa wanaendelea na uchunguzi.
Mmoja wa askari wa JWTZ aliyezungumza na gazeti hili kwa sharti la kutotajwa jina alisema kwa kawaida marubani wamefundishwa kuwa pale wanapoona ndege imepata hitilafu na hakuna kiwanja cha ndege karibu, inabidi watue barabarani.
Taarifa zaidi kutoka JWTZ zilieleza kwamba Meja Leguna alikuwa ni mwalimu wa mafunzo
ya ndege za kivita katika kikosi hicho cha Ngerengere na alikuwa anamfundisha urubani Luteni Kijanga.
Walikuwa katika mafunzo ya kawaida ya urushaji wa ndege za kivita. Walitokea kikosini Ngerengere na walikuwa katika mizunguko ya kawaida na ilikuwa warejee kikosini, ndipo wakapata ajali hiyo," alisema mwanajeshi huyo.
Muda mfupi baada ya ajali hiyo eneo hilo lilizingirwa na askari wa JWTZ ambao hawakutaka mtu yeyote kukaribia.
Chanzo Ndege ya jeshi yagonga gari, yaua
Waliofariki Mungu awalaze pema peopni tumepoteza Marubani wetu wawili inasikitisha sana hii ajali.