Stephano Mgendanyi
JF-Expert Member
- May 16, 2020
- 2,833
- 1,301
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika Kongamano la Kwanza la Kiswahili la Kimataifa litakalofanyika jijini Havana, nchini Cuba, kuanzia Novemba 7 hadi 10, 2024.
Kongamano hilo linatarajiwa kuhudhuriwa na washiriki takriban 600 kutoka nchi mbalimbali duniani. Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Damas Ndumbaro, ameeleza hayo leo Oktoba 30, 2024, katika mkutano wake na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.
Amesema kuwa kongamano hilo litahudhuriwa pia na Rais wa Cuba, Miguel Diaz-Canel.
Dkt. Ndumbaro ameongeza kuwa kutakuwa na semina mbalimbali pamoja na uzinduzi wa Kamusi ya Kiswahili na Kispaniola iliyotayarishwa na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
"Lugha ya Kiswahili imefanikiwa kutambuliwa na UNESCO kama lugha ya saba ya kimataifa, ikiwa na wazungumzaji zaidi ya milioni 500 duniani, hivyo ni wakati wa kukipeleka katika mataifa mbalimbali kwa ajili ya kukibidhaisha," amesema Dkt. Ndumbaro.
Amefafanua kuwa uamuzi wa kufanyia kongamano hilo nchini Cuba unatokana na umuhimu wa Kiswahili kufikia hadhira ya wazungumzaji wa Kispaniola, hatua ambayo itaendeleza Kiswahili katika mataifa mengine. Amesema washiriki 600 wa kongamano hilo wanatarajiwa kutoka taasisi binafsi, vyuo vikuu, na vyama vya Kiswahili, huku vikundi mbalimbali vya burudani vikitarajia kupamba kongamano hilo.