mpasta
JF-Expert Member
- Jan 17, 2011
- 919
- 2,004
- Thread starter
-
- #21
HUJUMA NZITO-PART 09
"Halafu mmepata taarifa ya kustusha kijijini Kwembe, kule kaburini kwa Dr.Pius Chilembwa feki?" aliuliza mmoja wapo wa wana kikundi kile mle kwenye chumba cha mkutano wao. "Wewe ndio wa kutujuza maana shughuli za mazishi yote yalikuwa ni jukumu lako, kuanzia usafiri, mazishi, chakula mpaka ulinzi..!" alichangia mmoja wapo, huku kila mmoja akipatwa na wahaka wa moyo wa kutaka kufahamu kumetokea nini huko maziarani.
"Taaarifa niliyoipata ni kuwa mlinzi wa kaburi la marehemu Dr.Pius niliyemuweka amekutwa asubuhi akiwa ameleweshwa madawa ya kulevya amelala fo fo fo hajitambui. Lakini kaburini kuna dalili kama lilitobolewa ingawa limeonekana limezibwa tena, na mwili upo kama tulivyouzika," alitoa ripoti hiyo iliyowapa jambamoto na wahaka mkubwa wana mkutano wote kwenye ukumbi ule.
Maana walijua fika kama siri yao ya kuidanganya mamlaka ya nchi kuwa Dr.Pius Chilembwa ni marehemu hali ya kuwa ni mzima wa afya, ikigundulika patachimbika.
Dr.Pius marehemu kanyaboya ndio huyo wanayemuita kwenye kikao chao kwa jina la Mkubwa, alikuwa anakula zake maisha nchini Afrika ya Kusini na kuja Tanzania kwa mficho akitumia hati feki ya kusafiria. Pindi akiwa nchini inabidi mdogo wake, pacha wake Alex awe mafichoni kwa muda ili watu wasitambue kama huyu ni Dr.Pius ambaye ni marehemu.
"Mie ushauri wangu ni kuwa wala tusipigwe na taharuki mpaka tukashindwa kupanga mipango ya kumdhibiti huyu mpumbavu Kachero Manuel. Siwezi kuamini sisi na akili zetu mtu mmoja tu atusumbue, mpaka atunyime usingizi..!" alizungumza mmoja wa wajumbe wa mkutano ule wa siri.
"Kama atakuwa ni yeye huyo basi atakuwa ni mzuka maana mie nilihudhuria mazishini ulinzi ulikuwa mkali sana na yeye alikuwa ni muwindwa namba moja. Mawakala wetu wote tuliwapa picha ya Kachero Manu. Na maagizo yetu kwao yalikuwa wazi wakimuona mtu hata anayefanana na yeye ni kumtandika risasi kwanza kisha ndio uhakika wa kuwa ni yeye au sio ufanyike. Hivyo kuniambia kuwa huyu mjuba alikuwepo msibani na ameshafanya yake mimi nakula yamini kuwa hakuwepo labda ni mzuka wake" mjumbe mwingine aliongea kwa kujiamini, kuelezea namna hali ya ulinzi alivyoiona msibani.
"Mie nakubaliana na wewe kuwa ulinzi ulikuwa madhubuti na kama mlikuwa hamjui nilichukua mamluki wa Kizulu toka nchini Afrika ya kusini ambao hata lugha ya kiswahili kwao ni shida ili kama wakimkamata iwe ni utekelezaji wa vitendo na sio wa maneno mengi ya mahojiano" alizungumza kwa kujigamba Chew Master huku akiwa amevua miwani yako na kuiweka juu ya meza, anaongea kwa kutumia mikono yake kuonyesha msisitizo wa kile anachokiongea.
"Sasa kwa tahadhari tu, tutawapa taarifa watu wetu wote waliopo kwenye taasisi za upimaji wa DNA za hapa Afrika Mashariki ili kama kuna chochote amenyofoa kaburini anataka kufanya vipimo vyake aangukie pua.
Pia sasa tutazidi kuimarisha ulinzi wa mipaka yetu yetu ya nchi kavu, baharini na njia ya anga kuona kama anataka kutoka nje ya nchi kumsaka Dr.Pius maana hatujui kwenye mpambano wake na mwanajeshi wetu Luteni Koba huenda ameropoka mambo yoyote sisi hatujui.
Hivyo lazima tuwe na tahadhari maili 100 mbele yake kimtazamo" alifunga kikao muwakilishi wa Dr.Pius katika kikao kile kabambe cha siri kilichofanyika usiku wa manane kwa lengo la kuandaa mikakati ya kumziba mdomo Kachero Manu, ambaye shughuli yake pevu ilikuwa inawanyima usingizi wadau wa harakati za kuisimamisha Dola ya Nyasa.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
[emoji3586]Paka anampenda panya kwa mapenzi ya maki[emoji3586]
Nathanieli Banda au wana mtandao wenzake wa "Nyasa Empire Supporter" (NES) wakimfahamu sana kwa jina mpachiko la kimombo "Masterminder". Alikuwa ametinga suti yake nadhifu ya kahawia na viatu vyake vya rangi nyeusi ngozi halisi, ametulia ndani ya mgahawa uliopo kwenye Hoteli ya Hyatt Regency iliyopo barabara ya Kivukoni.
Ilikuwa ni Hoteli ya kifahari yenye mandhari tulivu sana inayokuwezesha kuburudisha mboni za macho yako kwa kuiangalia mubashara Bahari ya Hindi mpaka mwisho wa upeo wa macho yako.
Ama kwa hakika siku hiyo Nathanieli alikuwa amependeza sana kimuonekano, vijana wa mjini wanasema "aliamua kuvunja kabati".
Alikuwa ana muonekano mithili ya Bwana harusi anayesubiria saa na wakati tu akakabidhiwe jiko mbele ya Baba mchungaji. Alikuwa ni kijana wa makamo mwenye kila aina ya mafanikio ambayo kila barobaro wa kileo anayaota awe nayo maishani mwake.
Kwa upande wa elimu alikuwa ametabahari vya kutosha, kwa shahada zake mbili za Uzamili. Moja ikiwa ni ya uchambuzi wa mifumo ya kompyuta aliyoipata nchini Afrika ya Kusini "Cape Town University" na ingine ni ya usimamizi wa fedha aliyoipata hapa hapa nchini, Chuo Kikuu Mzumbe, Morogoro.
Ukija kwenye kibarua cha kumuingizia mkate wa siku, alikuwa ni Afisa Mwandamizi katika Benki Kuu ya Tanzania (BKT) Makao Makuu, Jijini Dar es Salaam. Ajira ambayo ilikuwa inampa mshahara mnono na marupurupu kochokocho kwa mwezi. Pesa ambayo ilimfanya ayaendeshe maisha yake anavyotaka yeye yasonge na sio kuendeshwa na maisha yatakavyo.
Vidosho wenye kupenda kuwapapatikia wanaume tabaka a'ali, walikuwa wamejaribu kumtega Nathanieli kwa kila aina ya mitego na tashwishi lakini wapi, walishindwa kufua dafu. Mahusiano yake ya kimapenzi alikuwa anayaweka sirini sana, kiasi kwamba ilikuwa ni ngumu kumng'amua mpenzi wake. Habari kauzwa na Vidinga popo walipata uwanja wa kumchafua kwa kusambaza habari za uwongo za kimahusiano ya Nathanieli.
Wapo waliosema "anaye mchumba mrembo wa shani lakini anaishi Bondeni kwa Mzee Madiba, nchini Afrika ya Kusini". Walipata kani ya kuropoka hivyo kutokana na safari zake za huko zisizokauka. Chambilecho "akutukanae hakuchagulii tusi", wapo walioamua kupitiliza kumchafua kabisa wakavumisha kuwa "jogoo lake halipandi mtungi ndio maana anajitia hana mpango na warembo walioumbwa wakaumbika".
Maneno yote hayo ya lolololo Nathanieli aliyapuuza, hakuwa na muda mchafu wa kujiosha mbele yao wazandiki wa mambo. Ulevi wake mkubwa Nathanieli uliokuwa unajulikana na watu wengi ni upenzi wake kupitiliza wa motokaa za kileo. Alikuwa anabadilisha magari ya kisasa ya kutembelea kama vile mtu anavyobadilisha libasi zake.
Lakini kama ujuavyo hamna mkate mgumu mbele ya chai ya mkandaa, na ugumu wa siagi kiboko yake kisu, Nathanieli majivuno na nyodo zake zote za kuwadharau wanawake wa Kitanzania ziliyeyuka mbele ya mrembo Yasmine. Tokea siku ya kwanza tu kuripoti kwake kazini kwa Kachero Yasmine pale Benki Kuu na kutambulishwa mbele ya watumishi wenzake, Nathanieli tayari alishashikwa na gagaziko la moyo juu ya huba la Yasmine.
Bila kuchelewa kwa kuhofia ngoja ngoja huumiza matumbo akaanza kumfukuzia kwa kutega nyavu na kurusha ndoano zake zenye chambo cha udaga kwa Yasmine. Lakini kinyume na matarajio yake, hakuwa kisura wa mahonyo mwenye kubabaikia wenye nazo. Baada ya kupigwa kalenda kwa zaidi ya miezi miwili leo ndio alikubaliwa na Yasmine mualiko wake wa mlo wa usiku katika hoteli hiyo ya kifahari.
Yasmine kukubali kwake kukutana faragha na Nathanieli hakukuwa kibubusa tu. Bali kutokana na speksheni zake za muda mfupi tu pale ofisini kwake BKT alinusa harufu na kuona kuna dalili za uhusika wa Nathanieli kwa kiasi kikubwa kwenye ushiriki wake wa ukwapuaji wa mabilioni ya pesa zilizopotea.
Nathanieli furaha aliyokuwa nayo siku hiyo ilikuwa haisemeki baada ya kukubaliwa ombi lake na Kachero Yasmine. Ndio maana siku hiyo aliamua kuvunja kabati kabisa kwa kuvalia libasi za kutungua toka Ughaibuni na kujipulizia marashi ya ukwasi pia toka nchi za ng'ambo ili mradi tu awe nadhifu mbele ya mahabuba wa moyo wake. Ilipofika majira ya magharibi Nathanieli alikuwa tayari ameshawasili eneo la miadi kwa kutumia moja ya gari zake za kifahari aina ya "Range Rover Spot" rangi ya kijivu.
Lakini tokea awasili eneo la miadi, muda ulikuwa unazidi kuyoyoma Yasmine alikuwa bado hajang'aza uso wake. Kila wakati macho yake Nathanieli yalikuwa hayabanduki mlangoni ili amuone anapowasili.
Na pia macho yake yalikuwa hayabanduki kwenye saa yake ya mkononi kuangalia namna mishale yake ya saa hiyo inavyoshinda kusukuma muda mbele. Kadri saa zilivyoenda matiti, moyo wake ukaanza kupigapiga kwa haraka akianza kupatwa na wasiwasi wa kuachiwa manyoya na Yasmine kwenye majilisi hiyo aghali hapa Jijini.
"Huyu Binti mjanja mjanja kama sungura asije akawa ameamua kuniacha solemba. Muache aruke aruke mimi ndio "Masterminder" kama hanifahamu, lazima nimuingize kwenye mtego wangu" mkondo wa mawazo hasi ulikuwa unatiririka katika ubongo wake. Kila anapojaribu kumtafuta hewani kwenye simu yake, anajibiwa namba anayopiga haipatikani.
Ilipofika majira ya saa 2:00 usiku, Nathanieli tayari ameshaanza kukata tamaa juu ya hudhuri ya Yasmine, ghafla bin vuu...bila kutarajia, mlango mkubwa wa kuingilia alionekana msichana mmoja mrembo sana akiwa anatembea kwa madahiro. Alionekana anaingia huku anaangaza macho yake yasari na yamini kama vile kuna mtu anamsaka ila bado hajamtia machoni mwake.
Kimuonekano alikuwa ni hirimu, ana sura ya mvuto, macho yake legevu ya ukubwa wa wastani yaliyorembuliwa kama vile amekula kungumanga. Kifua chake cha wastani kilibarikiwa chuchu za kusimama zinazotaka kutoboa sidiria yake mithili ya ncha ya mkuki. Umbo lake lilikuwa limejengeka vyema na kuunda namba nane hasa kutokana na kiuno chake kubonyea katikati kama mdudu nyigu.
Alivutia mno kumtazama msichana huyo si kwa nywele zake laini na ndefu za Kisomali alizokuwa amezifunga kwa nyuma kwa mtindo wa mchicha, bali hata kwa ngozi yake ang'avu yenye kumesamesa kama taa ya aladini nyikani kwenye kiza kinene cha usiku. Kwa mwendo wake wa maringo tu aliwaacha midomo wazi watu wote waliomuangalia akitembea mle mgahawani.
Hatua zake alikuwa anaziachia sakafuni mithili ya mshindani wa mashindano ya ulimbwende. Wapenzi watazamaji wa mrembo yule wengine waliokuwa wanajipatia maakuli yao ya usiku, wengine walijikuta wanakosea badala ya kupeleka chakula kwenye mdomo ili kishuke tumboni, wakajikuta wanapeleka puani na wengine shavuni hali iliyopelekea kujimwagia ovyo chakula kama watoto wadogo. Ili mradi macho yao yalishikwa na mshawasha wa umbea.
Nathanieli alijikuta nae anapigwa na bumbuwazi, maruweruwe na mapigo ya moyo wake kusimama kwa sekunde mbili na nusu akiwa haamini kama yule ndio kweli Yasmine aliyemuweka doria karibia saa mbili ametokea.
Kisha akajikuta anapatwa na nguvu za ajabu akajikaza kisabuni na kujizoazoa kitini, akasimama na kujikuta anachanganya miguu yake kwa kujilazimisha mithili ya mtoto mdogo anayejifunza kutembea kwenda kumlaki.
"Ooooh...Waaaooh..! Yasmine Mpenzi wangu..karibu sana majilisi, siamini kama umetimiza miadi yako....!" alijikuta tu anaropoka Nathanieli kama mwehu mwenye kupandisha wazimu wakati wa mwezi mchanga. Wakati huo huo anamsaidia kutoa pochi yake ya rangi ya pinki kwapani ili aibebe yeye.
Bila hiana wala kinyongo Yasmine akamuachia pochi ile huku akiwa ameachia tabasamu pana lililoacha wazi sehemu ya meno yake ang'avu yaliyopangika kiufundi mkubwa na kuachia mwanya mdogo na kusababisha mbonyeo kwenye mashavu yake. Kisha kwa sauti yake laini ya kubembeleza usiku ule tulivu akaongea, "Samahani sana Mpenzi kwa kuchelewa....unajua hili Jijini lenu foleni sana, tofauti na kwetu Visiwani".
"Usijali naelewa cha muhimu ni kuwa umefika basi" alijibaraguza Nathanieli kujibu kwa lugha ya kinyenyekevu kuwa hamna tatizo lolote huku anachekacheka ovyo kama majinuni. Wakawa wameshafika kwenye meza maalumu aliyoichagua Nathanieli wakaketi vitini.
Yasmine alikuwa amevalia kisketi kifupi cha kubana cha dangirizi chenye rangi ya bahari buluu kilichoyaacha sehemu kubwa ya mapaja yake meupe wazi.
Kwa juu alivalia brauzi nyeupe nyepesi iliyombana vyema. "Umenisubiri sana? aliuliza Yasmine kwa sauti ya kudeka huku akiwa anachezea ufunguo wake wa gari kwa mkono wake wa kushoto.
"Nakuuliza wewe ujue, kwamba je umenisubiria sana..?" Nathanieli macho yake na mawazo yake yalikuwa yanashangaa mapaja mororo ya Yasmine, akiwa haamini kama huyu kweli ameumbwa na Jalali au amejiumba mwenyewe kutokana na kutokuwa na kasoro yoyote ya kimwili labda ya kitabia.
"Aaaah..! Samahani nilikuwa mbali sana mawazo yangu, ndiyo nimekusubiri sana muda mrefu yani mpaka nilibaki kidogo tu kukata tamaa, tahamaki ukatokea alizungumza Nathanieli kwa sauti ya kitetemeshi kama mtu aliyekurupushwa usingizini.
"Basi mie ngoja niondoke kumbe upo na mimi hapa kimwili tu lakini kifikra haupo nami unawaza michepuko yako mingine hukoooo....!" akatikisa kiberiti Yasmine huku akijitia kunyanyuka na kuchukua kibegi chake na kutaka kuanza kunyanyua hatua zake.
Weeeeh...! Nathanieli alikuwa mdogo kama piritoni anaona kabisa tonge linamponyoka mbele yake wakati tayari limeshafika kinywani. Alishapagawa anatetemeka huku anaweweseka kama mgonjwa degedege.
"Tafadhali....! Nisamehe sana, nimekosa sana nipe nafasi ya pili...! Tulia basi nikuambie ukweli nini nilichokuwa nakiwaza, nadhani utastaaajabishwa na maelezo tafadhali nipe nafasi ya kunisikiliza..!" alibembeleza Nathanieli huku amepiga magoti na Yasmine alishasimama tayari. Akajitia amemsamehe na kurudi kuketi tena kwenye nafasi yake. "Siku nyingine usijaribu kunifanyia hivyo, mie sipendi dharau hata kidogo" aljifanya amekuwa mkali kama pilipili kichaa.
"Hivi kwanini Yasmine unautesa moyo wangu kiasi hicho? hivi nizungumzie lugha gani nyepesi na rahisi upate kunielewa kuwa sina hali juu yako nipo mahamumu, ukipenda unifunge tu kwenye gereza la chumba cha chini kabisa katika sakafu ya moyo wako. Nimekufa juu ya penzi lako unanichelewesha tu mwenyewe kunizika moyoni mwako. Mimi ni mateka wako wa vita ya huba, nimesalimu amri nipo tayari kukukabidhi kila kitu changu, unifanye nitakavyo" akasita kuzungumza kwa muda akameza mate.
"Tafadhali sana Yasmine usiendelee kunipa mateso ya moyo, maisha yangu bila wewe ni sawa na kula chakula kisicho na chumvi, sipo tayari kuona nakukosa maishani mwangu. Mungu alipomuumba baba yetu Adamu alipomuona ni mpweke hana furaha kule bustanini Edeni, akamletea mwenza wake wa kumliwaza ambaye ni Hawa. Na mimi kipindi chote cha maisha yangu sikuona mwanamke anayeweza kuniondolea upweke na kunipa furaha maishani, mpaka nikajiona sina bahati duniani ya kubahatika kupata mwenza.
Lakini pindi ulivyojitokeza wewe pale kazini sasa naona kama nimeshapata mahabuba muafaka kwangu. Tangu ujio wako pale ofisini kwetu naona ni kama nyota jaha inayonifanyia upendeleo wa makusudi kwangu kuangaza mchana wa jua kali kwa kusaidiana na jua....!!" Nathanieli Banda alikuwa anajimaliza tu kwa kushusha mashairi matamu matamu ya kubembeleza, kudekeza akilimendea penzi la Kachero Yasmine Abeid lakini wapi kilikuwa hakieleweki kitu.
Binti wa Kipemba aliyelowea Zanzibari alikuwa mgumu kama chuma cha pua, na sio maharage ya Mbeya maji mara moja umekula. Alimkazia haswa kuwa hayupo tayari kuwa mpenzi wake, yupo pale kikazi tu na sio mambo mengine.
Hayo mashairi ya leo yalikuwa ni muendelezo tu, simu ya Yasmine ilikuwa imejaza meseji za mahaba toka kwa Nathanieli, mfanyakazi mwenzake katika kitengo kimoja cha kudhibiti fedha za nje na ndani. Kitengo ambacho Bosi wake alikuwa marehemu Dr.Pius Chilembwa, akisaidiwa kwa karibu na Nathanieli Banda na mwanamke mwingine akiitwa Flora Tarimo, na Makatibu Muhtasi wao wawili.
Kwa ujumla kitengo hicho nyeti kilikuwa na watu watano tu. Hivyo kifo cha Dr.Pius kikafanya idara hiyo iwe na watu wanne huku Kachero Yasmine Abeid akihamishiwa kitengo hicho akitokea Zanzibari. Nafasi ya Dr.Pius Chilembwa ilikuwa ikikaimiwa na Nathanieli Banda, hivyo alikuwa ni Bosi wa Yasmine kwa muda.
Baada ya mazungumzo ya hapa na pale wakanyanyuka kwa pamoja kwenda kuchota chakula wakaanza kupata chakula cha chajio kwa pamoja kwa kuwa usiku ulikuwa umeshafika. Sasa wakawa wanaendelea na mazungumzo yao huku sasa Nathanieli akiitumia fursa hiyo vilivyo kwa kuendelea kubembeleza penzi la mfanyakazi mwenzake.
"Hivi mimi na wewe tukiwa wapenzi, wafanyakazi wenzetu watatuchukuliaje kwa mfano! Si italeta taswira mbaya kwa taasisi yetu yenye heshima ya kutukuka itaonekana ni kama danguro. Mie naomba niendelee kukuheshimu kama kaka yangu tu na si vinginevyo, tusivuke zaidi ya hapo, samahani sana kama jibu langu kwako litakuwa limekukera na kuleta gharika ya moyo" Kachero Yasmine alijibu ombi la kuwa wapenzi toka kwa Nathanieli akiwa tayari ameshamaliza kula huku akijifanya anakwepesha macho anamuonea aibu. Anatafuna moja ya kucha zake katika kidole kidogo cha mkono wa kulia.
Jibu ambalo liliupasua na kuuchanachana vipande vipande moyo wa Nathanieli. Hakutegemea kupewa jibu kama hilo na kisura Yasmine. Nathanieli alijua tayari ameshamaliza kazi, ni kama anamsukuma mlevi kwenye mlima, sasa anaona binti anambadilikia kama kinyonga.
"Kwanza kinachonishangaza sana kaka Nathanieli ni kuwa kama uzuri basi Flora ni mzuri maradufu yangu mimi na katu sijaona kasoro yake katika tabia anachukuliana na kila mtu, kwanini unitongoze mimi na sio Flora ambaye mpo pamoja kitambo kirefu idarani?" Kachero Yasmine alizidi kumdodosa ili ajianike kila kitu kwa kutumia nguvu ya mapenzi tu.
"Swali zuri, Flora alikuwa chakula ya Bosi sasa siwezi kula sahani moja na Bosi sio adabu asilani" alijtetea Nathanieli kwa mafumbo, kiasi kwamba Kachero Yasmine alikuwa anataka mambo yawekwe hadharani na sio kufungwa fungwa kwenye bahasha.
"Unajua sijakuelewa bado unavyosema kuhusu Flora, kuwa ni chakula ya Bosi niweke sawa..!". Aliuliza Kachero Yasmine akiwa na tashiwishi ya kufahamu ukweli kinagaubaga.
"Ninamaanisha ya kuwa nisingeweza kutoka kimapenzi na Flora kwa sababu alikuwa ni mpenzi wa siri wa Bosi wetu wa idarani marehemu Dr.Pius Chilembwa, kuanzia Ijumaa kila wiki alikuwa hawaonekani kazini na Bosi wanakula bata ndefu tu, kifo cha Bosi ni pigo sana kwa Flora, hivyo namheshimu kama mjane wa Bosi wangu" aliweka wazi dhahiri shahiri ufafanuzi wa maelezo yake Bwana Nathanieli.
"Oooh.... masikini ya Mungu pole yake, nilikuwa siyajui hayo sasa naanza kuelewa, ndio maana mara nyingi siku ya Ijumaa hafiki kazini mpaka nikawa najiuliza kulikoni ana matatizo gani? Nadhani kwa sababu alishajizoesha toka zamani kuifanya kuwa sio siku ya kazi kwa upande wake. Pia kuna wakati anaonekana kama ni mtu mnyonge ana mawazo mengi sana" alinogesha mazungumzo hayo Kachero Yasmine kwa kukoleza umbea.
"Kunikataa mimi unachezea bahati kubwa sana Yasmine, mimi ni Gavana mtarajiwa wa Benki Kuu, ni suala la muda tu, sasa unadhani mie nikiwa mumeo halafu Gavana unatarajia nini...!" Nathanieli alichepusha mazungumzo na kumrudisha Yasmine kwenye lengo la kumpa mualiko ule, hata akajikuta kwa nguvu ya penzi anaropoka siri za ndani za NES hata zisizotakiwa kuzungumza mbele za watu ili mradi tu amuingize kwenye reli. Sasa aliamua kubadilisha gia angani kwa kumtega kwa kutumia nyadhifa ya cheo chake tarajaji.
Yasmine akajifanya ameshikwa na taharuki kupata taarifa hiyo mpya ya Ugavana akajifanya kama amejigonga kweli kweli na kukipapatikia hiko cheo cha kindotondoto anachokiota Nathanieli cha Ugavana.
"Oooh! Kweli jamani mpenzi wangu..au kamba tu za paukwa pakawa!!, unataka kupewa cheo cha Ugavana? nitajidaije mie nitakapoutangazia umma call me Mrs. Gavana, ha.. ha... ha.... ha...Hongera sana..!" alijitia kustaajabishwa kwelikweli na cheo hicho huku sasa akiwa amemuinamia Nathanieli kifuani kwake huku mkono wake wa kushoto unazichezea ndevu za Nathanieli.
"Eeeeh...ndio hivyo mubashara hamna chenga, mimi sio mtu mdogo kwenye hiyo serikali ijayo, ila siri yako usimwambie mtu mpenzi wangu. Kuna mgombea Urais ambaye ana nguvu kubwa ya zaidi ya asilimia 100% kushinda uchaguzi mkuu ujao wa mwakani. Kaniahidi kwa maandishi kabisa hiyo ni uhakika kabisa haina longolongo mbele ya mwanasheria wangu Ila narudia tena ni siri yako usimwambie mtu yoyote yaani wewe ndio wa kwanza kukupa siri hii hata mama yangu mzazi, kipenzi changu Bi Marieta wa kule Mbamba Bay sijawahi kumwambia habari hii abadaan katan" alijikuta Nathanieli anajikaanga kwa mafuta yake mbele ya adui yake bila kufahamu.
Yasmine moyoni mwake alikuwa na furaha maradufu isiyopimika katika mizania za kupimia furaha ya mwanadamu. Hasa kutokana na jambo lililomleta BKT kuchunguza linaanza kufungua wenyewe bila papara wala kokoro. "Simwambii mtu mpenzi.....kuwa na amani kabisa" aliongea alijiapiza kuifanya siri ahadi ya Ugavana aliyopewa kuwa ataificha.
"Mtakunywa vinywaji vyovyote tafadhali?" walitibuliwa mazungumzo yao na mhudumu wa mkahawa baada ya kuwaona wamekaa muda mrefu baada ya kumaliza kula bila kupata vinywaji. Hivyo hisia zake zikamtuma ajiongeze tu kwa kuwafuata na kuwauliza.
"OK...ahsante bila samahani hamna shida, tena umetufaa mie naomba "Grand Reserve ya Wine list" nichague kwanza kabla sijakuagiza" alizungumza Nathanieli huku akinyoosha mkono wake wa kulia kupokea karatasi ya orodha ya vinywaji aliyoiomba toka kwa yule mhudumu. "Nipatie glasi ya mvinyo wa "Bovlei Cape classic dry red" tafadhali" alimpa oda mhudumu huku nae Yasmine akiwa ameikamatia ile karatasi aliyoichukua toka kwa Nathanieli nae akawa anaperuzi kwa haraka haraka orodha ya vinywaji ili achague.
"Nipatie "Pearly Bay Sparkling" niijaribishe sijawahi kuinywa hiyo" alitoa oda yake Kachero Yasmine. "Aaah..bora ungeagiza "Swartland Bay Sparkling" nayo pia haileweshi ni katika kundi moja la vinywaji visivyo na kilevi, vinywaji vyenu watoto wa Masheikh lakini mie naona ndio ina ladha tamu kuliko uliyoiagiza, lakini ni ushauri wangu tu... ..! " aliingilia kati Nathanieli uchaguzi wa kinywaji wa Kachero Yasmine huku wakiangua kicheko kutokana na utani huo.
"Wewe ondoa hofu mie leo naenda kulala kwako leo laazizi, Baba mdogo amesafiri kikazi toka juzi anarudi kesho, maana naona unavyohangaika kutaka kunichagulia vilevi vikali vikali, ili niangushe gari hapa hapa mkahawani ujiokotee embe dodo chini ya mwarobaini..!" alijibu Yasmine, jibu ambalo lilisababisha wote wafe kwa kicheko kwa mara ya pili huku Nathanieli akiwa haamini kama kweli mambo yamekuwa mepesi kuliko alivyotegemea.
Akawa anavuta taswira Yasmine ndio kashafika nyumbani kwake wako wawili tu, jinsi nyasi za uwanja wa fundi seremala zitakavyowaka moto, kwenye pambano la patashika nguo kuchanika hakuna kulala hiyo mpaka lyamba. Kuna kipindi wakati vinywaji vyao vimeshaletwa, Nathanieli akajiroga kwenda msalani, Kachero Yasmine hakupoteza fursa aliyokuwa anaisotea kwa muda mrefu.
Akachomoa kichupa kidogo toka kwenye mkoba wake, akanyunyizia dawa za kulevya kidogo tu kwenye kinywaji cha Nathanieli, na kukirudisha haraka haraka kichupa chake kwenye mkoba wake. Dawa hizo alizonyunyiza zilikuwa zinatenza nguvu taratibu na kukufanya uwe unaonekana umelewa maradufu bila kukuchosha. Baada ya kuburudika kwa vinywaji kwa muda fulani tokea arudi msalani, Nathanieli taratibu bila kujielewa akaanza kujiskia vibaya.
Hiyo ilikuwa ni ishara ya kuzidiwa na mtindi alioutwika kichwani, akajikuta anaanza kulalama. "Aiseeh...Mpenzi tuondoke haraka tukalale, ila gari yangu utaendesha wewe najiskia vibaya sana, pombe zimenielemea vibaya leo kuliko kawaida yangu mpaka najishangaa.. !".
Yasmine akachangamkia fursa haraka kwa kulipa bili za gharama ya huduma ya vinywaji na chakula walivyokula na kunywa. Kisha Yasmine akachukua funguo za gari za Nathanieli zilizokuwa zipo mezani kwa ajili ya kuondoka. Akafanya maamuzi ya kuiacha gari yake pale pale Hotelini kwa minajiri ya kuwa atalifuata kwa muda wake.
Sasa alikuwa anajua anakwenda nyumbani kwa Nathanieli kufanya taftishi ya chochote kitakachomsaidia kwenye upelelezi wake kwa raha mustarehe bila usumbufu. Kwa mihadarati aliyomchanganyia, alijua fika muda sio mrefu atalala fe fe fe, aweze kujimwayamwaya anavyotaka yeye.
"Toka lini paka na panya wakapendana kwa mapenzi ya maki! Huo ni ujuha, imekula kwake" aliwaza Kachero Yasmine kwa furaha ya ushindi huku akiwa anaendesha gari kwa ustadi mkubwa kuelekea nyumbani kwa Nathanieli.
ITAENDELEA
"Halafu mmepata taarifa ya kustusha kijijini Kwembe, kule kaburini kwa Dr.Pius Chilembwa feki?" aliuliza mmoja wapo wa wana kikundi kile mle kwenye chumba cha mkutano wao. "Wewe ndio wa kutujuza maana shughuli za mazishi yote yalikuwa ni jukumu lako, kuanzia usafiri, mazishi, chakula mpaka ulinzi..!" alichangia mmoja wapo, huku kila mmoja akipatwa na wahaka wa moyo wa kutaka kufahamu kumetokea nini huko maziarani.
"Taaarifa niliyoipata ni kuwa mlinzi wa kaburi la marehemu Dr.Pius niliyemuweka amekutwa asubuhi akiwa ameleweshwa madawa ya kulevya amelala fo fo fo hajitambui. Lakini kaburini kuna dalili kama lilitobolewa ingawa limeonekana limezibwa tena, na mwili upo kama tulivyouzika," alitoa ripoti hiyo iliyowapa jambamoto na wahaka mkubwa wana mkutano wote kwenye ukumbi ule.
Maana walijua fika kama siri yao ya kuidanganya mamlaka ya nchi kuwa Dr.Pius Chilembwa ni marehemu hali ya kuwa ni mzima wa afya, ikigundulika patachimbika.
Dr.Pius marehemu kanyaboya ndio huyo wanayemuita kwenye kikao chao kwa jina la Mkubwa, alikuwa anakula zake maisha nchini Afrika ya Kusini na kuja Tanzania kwa mficho akitumia hati feki ya kusafiria. Pindi akiwa nchini inabidi mdogo wake, pacha wake Alex awe mafichoni kwa muda ili watu wasitambue kama huyu ni Dr.Pius ambaye ni marehemu.
"Mie ushauri wangu ni kuwa wala tusipigwe na taharuki mpaka tukashindwa kupanga mipango ya kumdhibiti huyu mpumbavu Kachero Manuel. Siwezi kuamini sisi na akili zetu mtu mmoja tu atusumbue, mpaka atunyime usingizi..!" alizungumza mmoja wa wajumbe wa mkutano ule wa siri.
"Kama atakuwa ni yeye huyo basi atakuwa ni mzuka maana mie nilihudhuria mazishini ulinzi ulikuwa mkali sana na yeye alikuwa ni muwindwa namba moja. Mawakala wetu wote tuliwapa picha ya Kachero Manu. Na maagizo yetu kwao yalikuwa wazi wakimuona mtu hata anayefanana na yeye ni kumtandika risasi kwanza kisha ndio uhakika wa kuwa ni yeye au sio ufanyike. Hivyo kuniambia kuwa huyu mjuba alikuwepo msibani na ameshafanya yake mimi nakula yamini kuwa hakuwepo labda ni mzuka wake" mjumbe mwingine aliongea kwa kujiamini, kuelezea namna hali ya ulinzi alivyoiona msibani.
"Mie nakubaliana na wewe kuwa ulinzi ulikuwa madhubuti na kama mlikuwa hamjui nilichukua mamluki wa Kizulu toka nchini Afrika ya kusini ambao hata lugha ya kiswahili kwao ni shida ili kama wakimkamata iwe ni utekelezaji wa vitendo na sio wa maneno mengi ya mahojiano" alizungumza kwa kujigamba Chew Master huku akiwa amevua miwani yako na kuiweka juu ya meza, anaongea kwa kutumia mikono yake kuonyesha msisitizo wa kile anachokiongea.
"Sasa kwa tahadhari tu, tutawapa taarifa watu wetu wote waliopo kwenye taasisi za upimaji wa DNA za hapa Afrika Mashariki ili kama kuna chochote amenyofoa kaburini anataka kufanya vipimo vyake aangukie pua.
Pia sasa tutazidi kuimarisha ulinzi wa mipaka yetu yetu ya nchi kavu, baharini na njia ya anga kuona kama anataka kutoka nje ya nchi kumsaka Dr.Pius maana hatujui kwenye mpambano wake na mwanajeshi wetu Luteni Koba huenda ameropoka mambo yoyote sisi hatujui.
Hivyo lazima tuwe na tahadhari maili 100 mbele yake kimtazamo" alifunga kikao muwakilishi wa Dr.Pius katika kikao kile kabambe cha siri kilichofanyika usiku wa manane kwa lengo la kuandaa mikakati ya kumziba mdomo Kachero Manu, ambaye shughuli yake pevu ilikuwa inawanyima usingizi wadau wa harakati za kuisimamisha Dola ya Nyasa.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
[emoji3586]Paka anampenda panya kwa mapenzi ya maki[emoji3586]
Nathanieli Banda au wana mtandao wenzake wa "Nyasa Empire Supporter" (NES) wakimfahamu sana kwa jina mpachiko la kimombo "Masterminder". Alikuwa ametinga suti yake nadhifu ya kahawia na viatu vyake vya rangi nyeusi ngozi halisi, ametulia ndani ya mgahawa uliopo kwenye Hoteli ya Hyatt Regency iliyopo barabara ya Kivukoni.
Ilikuwa ni Hoteli ya kifahari yenye mandhari tulivu sana inayokuwezesha kuburudisha mboni za macho yako kwa kuiangalia mubashara Bahari ya Hindi mpaka mwisho wa upeo wa macho yako.
Ama kwa hakika siku hiyo Nathanieli alikuwa amependeza sana kimuonekano, vijana wa mjini wanasema "aliamua kuvunja kabati".
Alikuwa ana muonekano mithili ya Bwana harusi anayesubiria saa na wakati tu akakabidhiwe jiko mbele ya Baba mchungaji. Alikuwa ni kijana wa makamo mwenye kila aina ya mafanikio ambayo kila barobaro wa kileo anayaota awe nayo maishani mwake.
Kwa upande wa elimu alikuwa ametabahari vya kutosha, kwa shahada zake mbili za Uzamili. Moja ikiwa ni ya uchambuzi wa mifumo ya kompyuta aliyoipata nchini Afrika ya Kusini "Cape Town University" na ingine ni ya usimamizi wa fedha aliyoipata hapa hapa nchini, Chuo Kikuu Mzumbe, Morogoro.
Ukija kwenye kibarua cha kumuingizia mkate wa siku, alikuwa ni Afisa Mwandamizi katika Benki Kuu ya Tanzania (BKT) Makao Makuu, Jijini Dar es Salaam. Ajira ambayo ilikuwa inampa mshahara mnono na marupurupu kochokocho kwa mwezi. Pesa ambayo ilimfanya ayaendeshe maisha yake anavyotaka yeye yasonge na sio kuendeshwa na maisha yatakavyo.
Vidosho wenye kupenda kuwapapatikia wanaume tabaka a'ali, walikuwa wamejaribu kumtega Nathanieli kwa kila aina ya mitego na tashwishi lakini wapi, walishindwa kufua dafu. Mahusiano yake ya kimapenzi alikuwa anayaweka sirini sana, kiasi kwamba ilikuwa ni ngumu kumng'amua mpenzi wake. Habari kauzwa na Vidinga popo walipata uwanja wa kumchafua kwa kusambaza habari za uwongo za kimahusiano ya Nathanieli.
Wapo waliosema "anaye mchumba mrembo wa shani lakini anaishi Bondeni kwa Mzee Madiba, nchini Afrika ya Kusini". Walipata kani ya kuropoka hivyo kutokana na safari zake za huko zisizokauka. Chambilecho "akutukanae hakuchagulii tusi", wapo walioamua kupitiliza kumchafua kabisa wakavumisha kuwa "jogoo lake halipandi mtungi ndio maana anajitia hana mpango na warembo walioumbwa wakaumbika".
Maneno yote hayo ya lolololo Nathanieli aliyapuuza, hakuwa na muda mchafu wa kujiosha mbele yao wazandiki wa mambo. Ulevi wake mkubwa Nathanieli uliokuwa unajulikana na watu wengi ni upenzi wake kupitiliza wa motokaa za kileo. Alikuwa anabadilisha magari ya kisasa ya kutembelea kama vile mtu anavyobadilisha libasi zake.
Lakini kama ujuavyo hamna mkate mgumu mbele ya chai ya mkandaa, na ugumu wa siagi kiboko yake kisu, Nathanieli majivuno na nyodo zake zote za kuwadharau wanawake wa Kitanzania ziliyeyuka mbele ya mrembo Yasmine. Tokea siku ya kwanza tu kuripoti kwake kazini kwa Kachero Yasmine pale Benki Kuu na kutambulishwa mbele ya watumishi wenzake, Nathanieli tayari alishashikwa na gagaziko la moyo juu ya huba la Yasmine.
Bila kuchelewa kwa kuhofia ngoja ngoja huumiza matumbo akaanza kumfukuzia kwa kutega nyavu na kurusha ndoano zake zenye chambo cha udaga kwa Yasmine. Lakini kinyume na matarajio yake, hakuwa kisura wa mahonyo mwenye kubabaikia wenye nazo. Baada ya kupigwa kalenda kwa zaidi ya miezi miwili leo ndio alikubaliwa na Yasmine mualiko wake wa mlo wa usiku katika hoteli hiyo ya kifahari.
Yasmine kukubali kwake kukutana faragha na Nathanieli hakukuwa kibubusa tu. Bali kutokana na speksheni zake za muda mfupi tu pale ofisini kwake BKT alinusa harufu na kuona kuna dalili za uhusika wa Nathanieli kwa kiasi kikubwa kwenye ushiriki wake wa ukwapuaji wa mabilioni ya pesa zilizopotea.
Nathanieli furaha aliyokuwa nayo siku hiyo ilikuwa haisemeki baada ya kukubaliwa ombi lake na Kachero Yasmine. Ndio maana siku hiyo aliamua kuvunja kabati kabisa kwa kuvalia libasi za kutungua toka Ughaibuni na kujipulizia marashi ya ukwasi pia toka nchi za ng'ambo ili mradi tu awe nadhifu mbele ya mahabuba wa moyo wake. Ilipofika majira ya magharibi Nathanieli alikuwa tayari ameshawasili eneo la miadi kwa kutumia moja ya gari zake za kifahari aina ya "Range Rover Spot" rangi ya kijivu.
Lakini tokea awasili eneo la miadi, muda ulikuwa unazidi kuyoyoma Yasmine alikuwa bado hajang'aza uso wake. Kila wakati macho yake Nathanieli yalikuwa hayabanduki mlangoni ili amuone anapowasili.
Na pia macho yake yalikuwa hayabanduki kwenye saa yake ya mkononi kuangalia namna mishale yake ya saa hiyo inavyoshinda kusukuma muda mbele. Kadri saa zilivyoenda matiti, moyo wake ukaanza kupigapiga kwa haraka akianza kupatwa na wasiwasi wa kuachiwa manyoya na Yasmine kwenye majilisi hiyo aghali hapa Jijini.
"Huyu Binti mjanja mjanja kama sungura asije akawa ameamua kuniacha solemba. Muache aruke aruke mimi ndio "Masterminder" kama hanifahamu, lazima nimuingize kwenye mtego wangu" mkondo wa mawazo hasi ulikuwa unatiririka katika ubongo wake. Kila anapojaribu kumtafuta hewani kwenye simu yake, anajibiwa namba anayopiga haipatikani.
Ilipofika majira ya saa 2:00 usiku, Nathanieli tayari ameshaanza kukata tamaa juu ya hudhuri ya Yasmine, ghafla bin vuu...bila kutarajia, mlango mkubwa wa kuingilia alionekana msichana mmoja mrembo sana akiwa anatembea kwa madahiro. Alionekana anaingia huku anaangaza macho yake yasari na yamini kama vile kuna mtu anamsaka ila bado hajamtia machoni mwake.
Kimuonekano alikuwa ni hirimu, ana sura ya mvuto, macho yake legevu ya ukubwa wa wastani yaliyorembuliwa kama vile amekula kungumanga. Kifua chake cha wastani kilibarikiwa chuchu za kusimama zinazotaka kutoboa sidiria yake mithili ya ncha ya mkuki. Umbo lake lilikuwa limejengeka vyema na kuunda namba nane hasa kutokana na kiuno chake kubonyea katikati kama mdudu nyigu.
Alivutia mno kumtazama msichana huyo si kwa nywele zake laini na ndefu za Kisomali alizokuwa amezifunga kwa nyuma kwa mtindo wa mchicha, bali hata kwa ngozi yake ang'avu yenye kumesamesa kama taa ya aladini nyikani kwenye kiza kinene cha usiku. Kwa mwendo wake wa maringo tu aliwaacha midomo wazi watu wote waliomuangalia akitembea mle mgahawani.
Hatua zake alikuwa anaziachia sakafuni mithili ya mshindani wa mashindano ya ulimbwende. Wapenzi watazamaji wa mrembo yule wengine waliokuwa wanajipatia maakuli yao ya usiku, wengine walijikuta wanakosea badala ya kupeleka chakula kwenye mdomo ili kishuke tumboni, wakajikuta wanapeleka puani na wengine shavuni hali iliyopelekea kujimwagia ovyo chakula kama watoto wadogo. Ili mradi macho yao yalishikwa na mshawasha wa umbea.
Nathanieli alijikuta nae anapigwa na bumbuwazi, maruweruwe na mapigo ya moyo wake kusimama kwa sekunde mbili na nusu akiwa haamini kama yule ndio kweli Yasmine aliyemuweka doria karibia saa mbili ametokea.
Kisha akajikuta anapatwa na nguvu za ajabu akajikaza kisabuni na kujizoazoa kitini, akasimama na kujikuta anachanganya miguu yake kwa kujilazimisha mithili ya mtoto mdogo anayejifunza kutembea kwenda kumlaki.
"Ooooh...Waaaooh..! Yasmine Mpenzi wangu..karibu sana majilisi, siamini kama umetimiza miadi yako....!" alijikuta tu anaropoka Nathanieli kama mwehu mwenye kupandisha wazimu wakati wa mwezi mchanga. Wakati huo huo anamsaidia kutoa pochi yake ya rangi ya pinki kwapani ili aibebe yeye.
Bila hiana wala kinyongo Yasmine akamuachia pochi ile huku akiwa ameachia tabasamu pana lililoacha wazi sehemu ya meno yake ang'avu yaliyopangika kiufundi mkubwa na kuachia mwanya mdogo na kusababisha mbonyeo kwenye mashavu yake. Kisha kwa sauti yake laini ya kubembeleza usiku ule tulivu akaongea, "Samahani sana Mpenzi kwa kuchelewa....unajua hili Jijini lenu foleni sana, tofauti na kwetu Visiwani".
"Usijali naelewa cha muhimu ni kuwa umefika basi" alijibaraguza Nathanieli kujibu kwa lugha ya kinyenyekevu kuwa hamna tatizo lolote huku anachekacheka ovyo kama majinuni. Wakawa wameshafika kwenye meza maalumu aliyoichagua Nathanieli wakaketi vitini.
Yasmine alikuwa amevalia kisketi kifupi cha kubana cha dangirizi chenye rangi ya bahari buluu kilichoyaacha sehemu kubwa ya mapaja yake meupe wazi.
Kwa juu alivalia brauzi nyeupe nyepesi iliyombana vyema. "Umenisubiri sana? aliuliza Yasmine kwa sauti ya kudeka huku akiwa anachezea ufunguo wake wa gari kwa mkono wake wa kushoto.
"Nakuuliza wewe ujue, kwamba je umenisubiria sana..?" Nathanieli macho yake na mawazo yake yalikuwa yanashangaa mapaja mororo ya Yasmine, akiwa haamini kama huyu kweli ameumbwa na Jalali au amejiumba mwenyewe kutokana na kutokuwa na kasoro yoyote ya kimwili labda ya kitabia.
"Aaaah..! Samahani nilikuwa mbali sana mawazo yangu, ndiyo nimekusubiri sana muda mrefu yani mpaka nilibaki kidogo tu kukata tamaa, tahamaki ukatokea alizungumza Nathanieli kwa sauti ya kitetemeshi kama mtu aliyekurupushwa usingizini.
"Basi mie ngoja niondoke kumbe upo na mimi hapa kimwili tu lakini kifikra haupo nami unawaza michepuko yako mingine hukoooo....!" akatikisa kiberiti Yasmine huku akijitia kunyanyuka na kuchukua kibegi chake na kutaka kuanza kunyanyua hatua zake.
Weeeeh...! Nathanieli alikuwa mdogo kama piritoni anaona kabisa tonge linamponyoka mbele yake wakati tayari limeshafika kinywani. Alishapagawa anatetemeka huku anaweweseka kama mgonjwa degedege.
"Tafadhali....! Nisamehe sana, nimekosa sana nipe nafasi ya pili...! Tulia basi nikuambie ukweli nini nilichokuwa nakiwaza, nadhani utastaaajabishwa na maelezo tafadhali nipe nafasi ya kunisikiliza..!" alibembeleza Nathanieli huku amepiga magoti na Yasmine alishasimama tayari. Akajitia amemsamehe na kurudi kuketi tena kwenye nafasi yake. "Siku nyingine usijaribu kunifanyia hivyo, mie sipendi dharau hata kidogo" aljifanya amekuwa mkali kama pilipili kichaa.
"Hivi kwanini Yasmine unautesa moyo wangu kiasi hicho? hivi nizungumzie lugha gani nyepesi na rahisi upate kunielewa kuwa sina hali juu yako nipo mahamumu, ukipenda unifunge tu kwenye gereza la chumba cha chini kabisa katika sakafu ya moyo wako. Nimekufa juu ya penzi lako unanichelewesha tu mwenyewe kunizika moyoni mwako. Mimi ni mateka wako wa vita ya huba, nimesalimu amri nipo tayari kukukabidhi kila kitu changu, unifanye nitakavyo" akasita kuzungumza kwa muda akameza mate.
"Tafadhali sana Yasmine usiendelee kunipa mateso ya moyo, maisha yangu bila wewe ni sawa na kula chakula kisicho na chumvi, sipo tayari kuona nakukosa maishani mwangu. Mungu alipomuumba baba yetu Adamu alipomuona ni mpweke hana furaha kule bustanini Edeni, akamletea mwenza wake wa kumliwaza ambaye ni Hawa. Na mimi kipindi chote cha maisha yangu sikuona mwanamke anayeweza kuniondolea upweke na kunipa furaha maishani, mpaka nikajiona sina bahati duniani ya kubahatika kupata mwenza.
Lakini pindi ulivyojitokeza wewe pale kazini sasa naona kama nimeshapata mahabuba muafaka kwangu. Tangu ujio wako pale ofisini kwetu naona ni kama nyota jaha inayonifanyia upendeleo wa makusudi kwangu kuangaza mchana wa jua kali kwa kusaidiana na jua....!!" Nathanieli Banda alikuwa anajimaliza tu kwa kushusha mashairi matamu matamu ya kubembeleza, kudekeza akilimendea penzi la Kachero Yasmine Abeid lakini wapi kilikuwa hakieleweki kitu.
Binti wa Kipemba aliyelowea Zanzibari alikuwa mgumu kama chuma cha pua, na sio maharage ya Mbeya maji mara moja umekula. Alimkazia haswa kuwa hayupo tayari kuwa mpenzi wake, yupo pale kikazi tu na sio mambo mengine.
Hayo mashairi ya leo yalikuwa ni muendelezo tu, simu ya Yasmine ilikuwa imejaza meseji za mahaba toka kwa Nathanieli, mfanyakazi mwenzake katika kitengo kimoja cha kudhibiti fedha za nje na ndani. Kitengo ambacho Bosi wake alikuwa marehemu Dr.Pius Chilembwa, akisaidiwa kwa karibu na Nathanieli Banda na mwanamke mwingine akiitwa Flora Tarimo, na Makatibu Muhtasi wao wawili.
Kwa ujumla kitengo hicho nyeti kilikuwa na watu watano tu. Hivyo kifo cha Dr.Pius kikafanya idara hiyo iwe na watu wanne huku Kachero Yasmine Abeid akihamishiwa kitengo hicho akitokea Zanzibari. Nafasi ya Dr.Pius Chilembwa ilikuwa ikikaimiwa na Nathanieli Banda, hivyo alikuwa ni Bosi wa Yasmine kwa muda.
Baada ya mazungumzo ya hapa na pale wakanyanyuka kwa pamoja kwenda kuchota chakula wakaanza kupata chakula cha chajio kwa pamoja kwa kuwa usiku ulikuwa umeshafika. Sasa wakawa wanaendelea na mazungumzo yao huku sasa Nathanieli akiitumia fursa hiyo vilivyo kwa kuendelea kubembeleza penzi la mfanyakazi mwenzake.
"Hivi mimi na wewe tukiwa wapenzi, wafanyakazi wenzetu watatuchukuliaje kwa mfano! Si italeta taswira mbaya kwa taasisi yetu yenye heshima ya kutukuka itaonekana ni kama danguro. Mie naomba niendelee kukuheshimu kama kaka yangu tu na si vinginevyo, tusivuke zaidi ya hapo, samahani sana kama jibu langu kwako litakuwa limekukera na kuleta gharika ya moyo" Kachero Yasmine alijibu ombi la kuwa wapenzi toka kwa Nathanieli akiwa tayari ameshamaliza kula huku akijifanya anakwepesha macho anamuonea aibu. Anatafuna moja ya kucha zake katika kidole kidogo cha mkono wa kulia.
Jibu ambalo liliupasua na kuuchanachana vipande vipande moyo wa Nathanieli. Hakutegemea kupewa jibu kama hilo na kisura Yasmine. Nathanieli alijua tayari ameshamaliza kazi, ni kama anamsukuma mlevi kwenye mlima, sasa anaona binti anambadilikia kama kinyonga.
"Kwanza kinachonishangaza sana kaka Nathanieli ni kuwa kama uzuri basi Flora ni mzuri maradufu yangu mimi na katu sijaona kasoro yake katika tabia anachukuliana na kila mtu, kwanini unitongoze mimi na sio Flora ambaye mpo pamoja kitambo kirefu idarani?" Kachero Yasmine alizidi kumdodosa ili ajianike kila kitu kwa kutumia nguvu ya mapenzi tu.
"Swali zuri, Flora alikuwa chakula ya Bosi sasa siwezi kula sahani moja na Bosi sio adabu asilani" alijtetea Nathanieli kwa mafumbo, kiasi kwamba Kachero Yasmine alikuwa anataka mambo yawekwe hadharani na sio kufungwa fungwa kwenye bahasha.
"Unajua sijakuelewa bado unavyosema kuhusu Flora, kuwa ni chakula ya Bosi niweke sawa..!". Aliuliza Kachero Yasmine akiwa na tashiwishi ya kufahamu ukweli kinagaubaga.
"Ninamaanisha ya kuwa nisingeweza kutoka kimapenzi na Flora kwa sababu alikuwa ni mpenzi wa siri wa Bosi wetu wa idarani marehemu Dr.Pius Chilembwa, kuanzia Ijumaa kila wiki alikuwa hawaonekani kazini na Bosi wanakula bata ndefu tu, kifo cha Bosi ni pigo sana kwa Flora, hivyo namheshimu kama mjane wa Bosi wangu" aliweka wazi dhahiri shahiri ufafanuzi wa maelezo yake Bwana Nathanieli.
"Oooh.... masikini ya Mungu pole yake, nilikuwa siyajui hayo sasa naanza kuelewa, ndio maana mara nyingi siku ya Ijumaa hafiki kazini mpaka nikawa najiuliza kulikoni ana matatizo gani? Nadhani kwa sababu alishajizoesha toka zamani kuifanya kuwa sio siku ya kazi kwa upande wake. Pia kuna wakati anaonekana kama ni mtu mnyonge ana mawazo mengi sana" alinogesha mazungumzo hayo Kachero Yasmine kwa kukoleza umbea.
"Kunikataa mimi unachezea bahati kubwa sana Yasmine, mimi ni Gavana mtarajiwa wa Benki Kuu, ni suala la muda tu, sasa unadhani mie nikiwa mumeo halafu Gavana unatarajia nini...!" Nathanieli alichepusha mazungumzo na kumrudisha Yasmine kwenye lengo la kumpa mualiko ule, hata akajikuta kwa nguvu ya penzi anaropoka siri za ndani za NES hata zisizotakiwa kuzungumza mbele za watu ili mradi tu amuingize kwenye reli. Sasa aliamua kubadilisha gia angani kwa kumtega kwa kutumia nyadhifa ya cheo chake tarajaji.
Yasmine akajifanya ameshikwa na taharuki kupata taarifa hiyo mpya ya Ugavana akajifanya kama amejigonga kweli kweli na kukipapatikia hiko cheo cha kindotondoto anachokiota Nathanieli cha Ugavana.
"Oooh! Kweli jamani mpenzi wangu..au kamba tu za paukwa pakawa!!, unataka kupewa cheo cha Ugavana? nitajidaije mie nitakapoutangazia umma call me Mrs. Gavana, ha.. ha... ha.... ha...Hongera sana..!" alijitia kustaajabishwa kwelikweli na cheo hicho huku sasa akiwa amemuinamia Nathanieli kifuani kwake huku mkono wake wa kushoto unazichezea ndevu za Nathanieli.
"Eeeeh...ndio hivyo mubashara hamna chenga, mimi sio mtu mdogo kwenye hiyo serikali ijayo, ila siri yako usimwambie mtu mpenzi wangu. Kuna mgombea Urais ambaye ana nguvu kubwa ya zaidi ya asilimia 100% kushinda uchaguzi mkuu ujao wa mwakani. Kaniahidi kwa maandishi kabisa hiyo ni uhakika kabisa haina longolongo mbele ya mwanasheria wangu Ila narudia tena ni siri yako usimwambie mtu yoyote yaani wewe ndio wa kwanza kukupa siri hii hata mama yangu mzazi, kipenzi changu Bi Marieta wa kule Mbamba Bay sijawahi kumwambia habari hii abadaan katan" alijikuta Nathanieli anajikaanga kwa mafuta yake mbele ya adui yake bila kufahamu.
Yasmine moyoni mwake alikuwa na furaha maradufu isiyopimika katika mizania za kupimia furaha ya mwanadamu. Hasa kutokana na jambo lililomleta BKT kuchunguza linaanza kufungua wenyewe bila papara wala kokoro. "Simwambii mtu mpenzi.....kuwa na amani kabisa" aliongea alijiapiza kuifanya siri ahadi ya Ugavana aliyopewa kuwa ataificha.
"Mtakunywa vinywaji vyovyote tafadhali?" walitibuliwa mazungumzo yao na mhudumu wa mkahawa baada ya kuwaona wamekaa muda mrefu baada ya kumaliza kula bila kupata vinywaji. Hivyo hisia zake zikamtuma ajiongeze tu kwa kuwafuata na kuwauliza.
"OK...ahsante bila samahani hamna shida, tena umetufaa mie naomba "Grand Reserve ya Wine list" nichague kwanza kabla sijakuagiza" alizungumza Nathanieli huku akinyoosha mkono wake wa kulia kupokea karatasi ya orodha ya vinywaji aliyoiomba toka kwa yule mhudumu. "Nipatie glasi ya mvinyo wa "Bovlei Cape classic dry red" tafadhali" alimpa oda mhudumu huku nae Yasmine akiwa ameikamatia ile karatasi aliyoichukua toka kwa Nathanieli nae akawa anaperuzi kwa haraka haraka orodha ya vinywaji ili achague.
"Nipatie "Pearly Bay Sparkling" niijaribishe sijawahi kuinywa hiyo" alitoa oda yake Kachero Yasmine. "Aaah..bora ungeagiza "Swartland Bay Sparkling" nayo pia haileweshi ni katika kundi moja la vinywaji visivyo na kilevi, vinywaji vyenu watoto wa Masheikh lakini mie naona ndio ina ladha tamu kuliko uliyoiagiza, lakini ni ushauri wangu tu... ..! " aliingilia kati Nathanieli uchaguzi wa kinywaji wa Kachero Yasmine huku wakiangua kicheko kutokana na utani huo.
"Wewe ondoa hofu mie leo naenda kulala kwako leo laazizi, Baba mdogo amesafiri kikazi toka juzi anarudi kesho, maana naona unavyohangaika kutaka kunichagulia vilevi vikali vikali, ili niangushe gari hapa hapa mkahawani ujiokotee embe dodo chini ya mwarobaini..!" alijibu Yasmine, jibu ambalo lilisababisha wote wafe kwa kicheko kwa mara ya pili huku Nathanieli akiwa haamini kama kweli mambo yamekuwa mepesi kuliko alivyotegemea.
Akawa anavuta taswira Yasmine ndio kashafika nyumbani kwake wako wawili tu, jinsi nyasi za uwanja wa fundi seremala zitakavyowaka moto, kwenye pambano la patashika nguo kuchanika hakuna kulala hiyo mpaka lyamba. Kuna kipindi wakati vinywaji vyao vimeshaletwa, Nathanieli akajiroga kwenda msalani, Kachero Yasmine hakupoteza fursa aliyokuwa anaisotea kwa muda mrefu.
Akachomoa kichupa kidogo toka kwenye mkoba wake, akanyunyizia dawa za kulevya kidogo tu kwenye kinywaji cha Nathanieli, na kukirudisha haraka haraka kichupa chake kwenye mkoba wake. Dawa hizo alizonyunyiza zilikuwa zinatenza nguvu taratibu na kukufanya uwe unaonekana umelewa maradufu bila kukuchosha. Baada ya kuburudika kwa vinywaji kwa muda fulani tokea arudi msalani, Nathanieli taratibu bila kujielewa akaanza kujiskia vibaya.
Hiyo ilikuwa ni ishara ya kuzidiwa na mtindi alioutwika kichwani, akajikuta anaanza kulalama. "Aiseeh...Mpenzi tuondoke haraka tukalale, ila gari yangu utaendesha wewe najiskia vibaya sana, pombe zimenielemea vibaya leo kuliko kawaida yangu mpaka najishangaa.. !".
Yasmine akachangamkia fursa haraka kwa kulipa bili za gharama ya huduma ya vinywaji na chakula walivyokula na kunywa. Kisha Yasmine akachukua funguo za gari za Nathanieli zilizokuwa zipo mezani kwa ajili ya kuondoka. Akafanya maamuzi ya kuiacha gari yake pale pale Hotelini kwa minajiri ya kuwa atalifuata kwa muda wake.
Sasa alikuwa anajua anakwenda nyumbani kwa Nathanieli kufanya taftishi ya chochote kitakachomsaidia kwenye upelelezi wake kwa raha mustarehe bila usumbufu. Kwa mihadarati aliyomchanganyia, alijua fika muda sio mrefu atalala fe fe fe, aweze kujimwayamwaya anavyotaka yeye.
"Toka lini paka na panya wakapendana kwa mapenzi ya maki! Huo ni ujuha, imekula kwake" aliwaza Kachero Yasmine kwa furaha ya ushindi huku akiwa anaendesha gari kwa ustadi mkubwa kuelekea nyumbani kwa Nathanieli.
ITAENDELEA