Riwaya: "Hujuma Nzito"

Riwaya: "Hujuma Nzito"

Mpasta umepotelea wapi? au na wewe unaleta hujuma nzito kwetu wasomaji?
 
RIWAYA-HUJUMA NZITO-PART 20


SURA YA KUMI

"Mtume weeeeeeh.....!! Mtume weeeeeeh..!! Dada unaniua dada nimekoma dadaaaah....Weeh dadaaaah.... Sirudii tenaaaaa...Mama weeeeeh Mama weeeeh...Ooooh Oooh...Nakufaaaaa... Nakufaaaa...!! " yalikuwa ni sehemu tu maneno yaliyoambatana na kilio cha mayowe chenye majonzi na maumivu makali sana yasiyoelezeka.

Alikuwa ni Mohammed Mtoni huyo akipokea mateso ya kuzimu wakati bado yupo hai duniani. Mateso yote hayo muasisi wake ni Kachero Yasmine. Alikuwa amemvua nguo zake, kisha amemtundika kwenye bomba lenye umbo la mstatili kama goli la uwanja wa mpira. Alimfunga kwa kamba kichwa chini miguu juu, huku mikono yote imefungwa pingu, hafurukuti.


Kisha akamchanja na wembe mgongo wake wote, baada ya hapo akampaka pilipili na chumvi. Kisha akaanza kumchapa mgongoni na mkia wa samaki taa, mkia ambao ulikuwa na sifa ya kupasua ngozi vilivyo.


Kachero Yasmine masikioni alikuwa anasikiliza muziki kwa kutumia vifaa maalumu hivyo hakuwa anasikia vilio vya mateso ya "Muddy Comp". Alimpa kila aina ya mateso kwa muda wa saa tatu mfululizo mpaka akawa hatamaniki.

Baada ya hapo akamfungua kamba zote na kumuacha chini anatwetwa kama mbwa koko aliyefukuzwa maili nyingi. "Sasa upo tayari kujibu yale maswali yangu uliyonijibu kifedhuli mwanzoni au nirudie tena dozi?" alikuwa anazungumza Yasmine huku anatabasamu utsema hana mfuko wa uzazi kwa jinsi alivyokosa huruma.

"Dadaa nitasema kila kitu sitaki matatizo mimi tena. Kwanza Shikamoo watu wa usalama popote mlipo..!!" alikuwa ameshachanganyikiwa hataki matatizo tena. Alishajua huyu mwanamke ni hatari sana sura yake na matendo yake ni mbingu na ardhi.

"Eeh...ulikuwa unapewa kazi gani na Nathanieli wa Benki Kuu mpaka unalipwa pesa sufufu namna ile kupitia kwenye kwenye akaunti ya "JUAKALI GENERAL SUPPLIES"?" aliuliza swali la kwanza na Kachero Yasmine huku amejiandaa kumrekodi majibu atakayopewa kwa kutumia simu yake ya mkononi.

"Kazi ilikuwa ni kufoji saini ya Gavana kuidhinisha pesa zinapelekwa nje ya nchi nchini Afrika ya Kusini kupitia nyaraka mbalimbali anazoniletea" alijibu kiufasaha bila kupindisha maneno wala kuleta usani wowote.

"Mlikuwa mnakutania wapi kupeana hizo kazi?" alichomekewa swali la pili. "Alikuwa ananichukua kutoka kijiweni Mkwepu kisha napelekwa kwenye Hoteli za kifahari tofauti tofauti kuifanya hiyo kazi kwa utulivu".

Aliendelea kujieleza huku sasa ameanza kuwa na amani anajua usalama wake umepatikana."Unalo lolote la ziada ungependa serikali yako ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania walijue kwenye sakata hili? " aliuliza swali la mwisho kwa siku hiyo Kachero Yasmine.

"Ninalo dadaa ninaloo...kuna mwenzangu mmoja anakaa Sinza sipakumbuki vilivyo aliponitajia, yeye pia anatengeneza ATM-kadi za kuchukulia pesa, sasa kuna siku tulikuwa Hotelini wote, yeye anafyatua ATM kadi mimi nipo kwenye kazi yangu ya saini" aliongea huku analia kwa uchungu akitaka na huyo mwenzake asakwe pia nae apitie suluba kama alizopitia yeye.

"Huyo unayemtaja nafahamu hadithi yake na habari yake usiku huu inaishia usihofu, sasa wewe utapumzishwa jela maalumu kwa ajili ya usalama wako na pia una kesi ya kujibu ya uhujumu uchumi na kula njama za kutaka kuiangusha serikali iliyopo madarakani.

Subiri wenzako mkamilike utaenda kujitetea mbele ya Pilato mimi sina mamlaka ya kukuachia huru au kukutia hatiani" alipomaliza maelezo hayo Kachero Yasmine akaanza kupiga simu kitengo maalumu waje kumchukua Mohammed Mtoni, akaunganishwe na wenzake waliokamatwa asubuhi wale wa "JUAKALI GENERAL SUPPLIES".

"Muddy Comp" alishaanza kuishiwa nguvu alikuwa amelala tu chini, mwili umevimba utasema mwanamasumbi aliyeshindwa kufua dafu ulingoni anasubiri machela tu impeleke hospitalini. Haukupita muda mrefu sana gari maalumu likaja kumbeba ili limkimbize hospitali kisha akipata nafuu akahifadhiwe sehemu salama mpaka kesi yake itakapopelekwa mahakamani.

Kachero Yasmine alipanga alasiri yake aelekee nyumba Namba 29-Sinza-Mori akashughulike na hayawani mwingine, mshirika mkuu wa "Nyasa Empire Supporters" (NES), Bwana Newton Temba.
,[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]
Ilikuwa ni majira ya Alasiri tulivu, adhana ya Allahu-Akbar Allahu-Akbar ikitolewa msikitini, ile inayowataka waislamu swalihina waende kuabudu Mola wao. Kachero Yasmine alasiri hiyo ilimkuta yupo mitaa ya Sinza, saluni ya kike ya kutengeneza nywele. Saluni hiyo ilikuwa katika moja ya jengo refu la roshani moja la kibiashara, lililokatwa fremu nyingi za biashara mbalimbali.

"Hivi kwanini mwenye kiwanja cha mbele yenu asingetafuta mwekezaji amtolee matoleo kama ghorofa hili apige pesa ndefu, hiyo nyumba haivutii kwa kweli" alichokonoa mazungumzo Kachero Yasmine na dada aliyekuwa anamsuka nywele zake. Kama ujuavyo saluni ndio vijiwe vya umbea kwa akina mama. Ukitaka habari motomoto za Mjini nenda kwenye saluni.

Kachero Yasmine alikuwa anaitazama nyumba ambayo anahisi ni namba 29 hapo maeneo ya Sinza Mori. Lakini cha kustaajabisha nyumba hiyo ilikuwa haina kibao chochote ila ya mbele yake ikisoma namba 30 na ya nyuma yake inasoma namba 28, hivyo hiyo kwa vyovyote hisia zilimtuma itakuwa ni namba 29.

Pia nyumba hiyo kimtazamo wa nje haikufanania na hadhi ya huyo mtu anayemtafuta. Mmoja wa watuhumiwa wakuu wa kundi la "Nyasa Empire Supporters" (NES) kama Man-Temba asingeweza kuwa maskani yake ni hapo, ndio maana akaamua aingie hapo saluni huenda akaibuka na umbea wa kuhusu hiyo nyumba.

Mawazoni kabla hajawasili eneo hilo la tukio, alitegemea kuona kumeshushwa mjengo wa adabu, ofisi zenye kupulizwa na viyoyozi na vikorombwezo kedekede vya kustarehesha, tofauti na nyumba mbavu za mbwa aliyoikuta.

"Babu mwenye nyumba anaishi Kibada huko kashaisusa. Madaraka yote kamuachia kichaa mmoja muokota makopo anaitwa Temba na hii ndio mida yake ya kurejea, utamuona hivi punde, anapita kulaanika juani mchana kutwa kuokota makopo" aliongea yule msusi huku akiwa analainisha nywele za Kachero Yasmine kwa mafuta ya nazi na kuanza kupasua njia katikati ya nywele kwa kutumia chanuo la mti wa mpingo.

"Sista Anita usidanganyike mjini shule yule wala sio kichaa ana akili zake timamu wala hazijadaathari, anajifanyisha uzumbwani tu" alidakia mazungumzo mmoja wa wahudumu wa ile saluni ambaye alikuwa anamfumua mteja mwingine rasta. Wajihi wake yule dada ukionyesha kabisa kukerwa na tabia za Man-Temba.

"Kuna siku alikuja dada wa Baba Aika, huyo Mzee Mwakibete wa hilo duka la nguo, alikuja kuosha nywele hapa, kipindi unamuuguza mama yako Muhimbili, mhhh aliongea mambo mengi ya huyu mwehu wetu Temba" akasimamisha mazungumzo wakati anahangaikia kuwasha mashine ya kukaushia nywele aliyoenda kuichomeka ukutani kwenye swichi.

Kachero Yasmine alitulia kimya kama zuzu hata kutikisika hataki, anasikiliza kwa umakini maelezo.
"Basi dada yake mama Aika akasema huyu Temba anamjua fika, kwanza alishtuka kumuona yupo Jijini Dar es Salaam, huko Mbeya wanajua amekufa. Akatusimulia ya kuwa ameshawahi kukamatwa kesi ya wizi wa pesa za kigeni enzi zile iliyovuma sana ya Kasusura.

Alituambia inasemekana huyu ndio alichora ramani yote ya wizi ule uliotikisa nchi ila Mahakama haikumkumkuta na hatia ikamuachia huru. Akazidi kutupasha kuwa utapeli wake alijifunza Naijeria alikokaa miaka mingi sana huko. Mtu mwenyewe huyooo anarudi ha.. ha... ha.. hatari kweli!" wamama wote wa mule saluni wakageuza shingo zao kama feni.

Walikodoka kumuangalia Man-Temba akiwa na mabuti yake ya mvua huku juu amevalia koti la mvua, nywele vuruvuru, amechafuka mavumbi mwili mzima utasema kichaa kwelikweli. Akaanza kuvua shati lake lenye viraka kochokocho na kulitupia pembeni na kukiacha wazi kidari chake kilichojengeka mithili ya mataruma ya reli.

"Ila naweza kuanza kuamini kwa mbali lisemwalo lipo. Anachonishangaza kila siku utamkuta na majarida na magazeti ya lugha ya Kiingereza. Pia kuna siku alikisahau kidaftari chake hapo barazani tukakuta amerekodi bei za manunuzi ya fedha za kigeni kwa kila siku kwenye mabenki mbalimbali, sasa huyo kichaa gani kweli anapenda kujua mambo hayo ya Maafisa..!" Anita alionyesha kukubaliana na dhana ya msaidizi wake kuhusiana na Man-Temba.

Baada ya muda mle saluni, mada ikabadilika sasa zikarudi zile mada zao pendwa za umbea na upashikuna.
Sifa za umbea hakuzipenda, akabaki yupo nao kimwili lakini rohoni anapanga mipango ya mbinu mbalimbali za kumvamia Man-Temba kwenye nyumba yake ya madongo poromoka.

Akili yake ilikuwa haikubali kuwa Babu mmiliki wa nyumba hiyo iliyopo ndani ya kitongoji cha Sinza, Jijini Dar es Salaam akubali tu kiubwete ubwete kichaa akae tu bila malipo yoyote. "Lazima atakuwa analipwa pesa ndefu sana na wahalifu wanaojificha hapo" aliwaza Kachero Yasmine.
ITAENDELEA

Sent from my TECNO CC6 using JamiiForums mobile app
 
RIWAYA-HUJUMA NZITO-PART 21


Ilipofika majira ya magharibi akiwa tayari kashamaliza kusukwa nywele zake na msusi, akalipia pesa na kuagana nao kwa bashasha. Akarejea kwa miguu hadi kwenye kituo cha mafuta cha Big-Bon alipoomba kuegesha gari yake.


Akalichukua na kuelekea maeneo ya Afrikasana, Hongera Bar kupata nyama choma safi maana tumbo lake lilikuwa linadai haki yake ya kupata maakuli.
Hapo palikuwa ni moja ya maeneo ya kula bata kwa wakazi wengi wa Sinza na vitongoji vya jirani.

Palikuwa usiku huo mbichi pameshaanza kuchangamka kwa wateja kuanza kujazana eneo hilo. Kwa bahati alipoegesha tu gari akaanza kugombaniwa kama mpira wa kona na wahudumu zaidi ya watatu kila mmoja akimtaka ampe huduma kutoka kwenye jiko analolisimamia.

Kachero Yasmine hakuwajali akawa anatabasamu tu huku anatembea kusaka meza huru, kwa bahati akaketi alipopachagua. Mhudumu mmoja wapo akasogelea na kuchukua oda yake aliyoiagiza. Macho yake yalikuwa yanaangalia usalama wa gari yake na alikuwa anashuhudia mubashara magari yanavyotembea kama kinyonga eneo hilo lenye msongamano wa magari hasa kuanzia magharibi na kuendelea.


Ghafla bin vuu wakati analetewa nyama choma yake aliyoiagiza kwa ugali, akamuona hasimu wake Man Temba anakuja kwa kasi anakimbia kuelekea yalipoegeshwa magari. Kisha alipofika kwenye gari la Kachero Yasmine akasimama kidogo na kuanza kulichunguza kwa umakini sana. Akaanza kulizunguka kama askari wa barabarani anavyolikagua gari lenye makosa.


Kachero Yasmine akawa ameganda bado hajaanza kula chakula chake anajishauri kama atoke pale alipo na kumfuata au asubirie aone mwisho wake ni nini haswa. Man Temba Akachomoa kidaftari chake na kuanza kuandika pleti namba za gari kisha alipomaliza akaitia mfukoni na kuelekea moja kwa moja kwa kasi jikoni wanapouza vyakula.


"Dada yangu asikutie presha ni mwehu yule, ndio kawaida kufanya vibweka kila leo!" mhudumu alimtoa hofu Yasmine baada ya kumuona mteja wake aliyemuandalia maakuli amesusa kula kabisa anaangalia gari lake linavyochezewa shere na Man-Temba.

"OK..kama hivyo sawa maana nikijua ni mkora anataka kuchomoa kifaa kwenye gari ila anaigiza uchizi tu..!" alimjibu huku mkono wa kulia wa Yasmine ukianza na Bismillahi kwenye sahani ile ya kuku kwa kunyofoa kipande cha firigisi ya kuku.

"Yule tumemzoea sana hapa, ndio muda wake huu, hapo nae ataagiza kuku wa kienyeji mzima, akitoka hapo ataingia kaunta ya vinywaji atainuka na chupa yake ya Hennessy, huyooo anatimua zake" akazidi kumtoa mashaka Yasmine, mhudumu yule.

"Oooh..Waaooh.. sasa nina amani ya moyo, anapata wapi hizo pesa zote za kunywa pombe ya bei aghali kama Hennessy?" Yasmine akajifanya ni buda akichokoza mjadala ule ili azidi kuvuna taarifa zaidi za hasimu wake Man-Temba.

"Hilo hata sisi linatufikirisha sana, maana hata wale madadapoa wanaojiuza miili yao, huwa siku akiwafuata hapa, wanapigana kumgombania na uchafu wake vilevile alivyo. Wenyewe wanamuita gari la mishahara limekuja wanasema anawalipa vizuri sana kwa huduma wanayotoa kwake.

Changudoa mmoja anasema kuna siku wakati yupo nae mfukoni mwake zilidondoka ATM kadi kama 10 za benki tofauti tofauti. Pia Kuna mteja wetu mmoja ni mfanyakazi wa benki anakuja sana hapa kula, anasema huyu ana rafiki zake wapo nchini Afrika ya Kusini huenda ndio wanaomuwezesha kipesa. Hivyo hapa mjini kila mtu anaishi kwa mtindo wake" akamalizia mazungumzo yule dada huku akiomba udhuru wa kujitoa na maongezi yale akahudumie wateja wengine waliokuwa sasa wameshajazana furifuri kwenye eneo hilo.


Ndani ya robo saa tu kuku mzima wa kienyeji na posheni ya ugali ikawa imeshasambaratisha pale mezani kwa Kachero Yasmine. "Dada yangu hongera sana, Mungu akuzidishie hamu ya kula unajua siku amini kama utamaliza kuku yule" alijisemesha mhudumu yule mbele ya Kachero Yasmine, wakati anaondosha vyombo mezani, akiwa hayaamini macho baada ya kuona sahani imepambwa na mifupa tupu.

"Ha ha ha... Hivyo ulijua utaambulia kitu muwauzie wateja wengine eeh..leo nimekukomesha. Maana sehemu zingine nyie wahudumu Mungu awasamehe tu, maana unaagiza kuku mzima, lakini unaletewa kuku kwenye sahani ana shingo tatu, mpaka unajiuliza huyu jogoo alikuwa na vichwa vitatu nini" alijibu mapigo ya utani ule Kachero Yasmine wote wakajikuta wanakufa kicheko.

"Ni ukweli uyasemayo dada yangu watu hatufanani, wanachofanya ukiagiza kuku mzima kama akikuona umelewa anachomoa shingo anaficha kwenye mfuko wa nguo yake. Akija mteja mwingine anakwapua bawa. Hivyo hivyo wanakwapua mpaka na yeye anakuwa ana kuku mzima yupo mfukoni mwake. Sasa akija mteja wa kuku mzima haendi jikoni tena anauza yule wa vipande vipande alivyokwapua kwa wateja.

Sasa akijichanganya ndio hapo anapokuletea jogoo wa vichwa vitatu ha ha ha ha" alisema huku anapokea pesa yake yenye bahashishi ya huduma nzuri ndani yake kisha Kachero Yasmine akaondoka zake eneo lile na kuelekea maeneo ya "Mlimani City Mall" kutulizana kwanza.


Alitaka afanye uvamizi eneo lile analoishi Man-Temba manane ya usiku. Lakini pia alitaka aombe ofisini kwao atumiwe kwa haraka kesi ya Kasusura ambayo inasemekana Man-Temba ndio alikuwa fundi mkuu wa tukio zima. Alishtushwa sana kuona mtu hatari kama Man Temba yupo uraiani anashiriki kuhujumu uchumi wa nchi kwa mara ya pili mfululizo.

Alipofika "Mlimani City Mall" na kuegesha gari yake hakutoka nje ya gari. Alichofanya ni kuchomeka kifaa aina ya modemu kwenye kompyuta mpakato yake ili kuunganisha mtandao. Alipofanikiwa kupata mtandao haraka haraka akatuma ujumbe ofisini kwao kwa Katibu Muhtasi wao Kokunawa. Kwa bahati nzuri Kokunawa muda huo wa saa 3:15 usiku mbichi alikuwa bado yupo, ofisini hivyo akaahidi kumtumia faili aliloliomba ndani ya nusu saa.

Wakati analisubiria faili hilo litumwe akashuka chini ya gari lake akafungua droo ya upande wa siti ya abiria, akachomoa paketi la sigara. Lilikuwa paketi la sigara aina ya 'Vogue', moja ya sigara ambazo ni gharama ya juu duniani. Kampuni hii ya sigara ilikuwa pia inatengeneza sigara maalumu kwa ajili ya watumiaji wanawake, kama 'Vogue Superslims' na 'Vogue Superslims Menthol'.


Kachero Yasmine alikuwa ni mvutaji wa mara moja moja sana, kwa muda wa miezi mitatu anaweza kuvuta kwa mkupuo sigara hata kumi kutuliza alosto yake. Mara nyingi sana akiwa kichwani kuna jambo linamsumbua na hajaweza kulikamilisha bado ndipo anapopatwa na alosto ya matumizi ya sigara zake pendwa za Vogue.

Akachomoa sigara za kutosha toka kwenye paketi lake, na kurudisha bunda lililobaki kwenye droo, kisha akaibusha moto. Akaanza bandika bandua ya kulichafua anga kwa moshi wa sigara akipingana na mkataba wa Kyoto wa mwaka 1997 unaokataza uchafuzi wa mazingira, huku anazunguka kwenye bustani ya pale "Mlimani City Mall". Tahamaki akajikuta kashateketeza fegi miche kama minane.


Akachomoa peremende kadhaa kutoka kwenye mfuko wa suruali ya dangirizi yake na kuanza kuzimung'unya ili kuupa mdomo wake riha ya kuvutia. Baada ya hapo akarejea kwenye gari na kuwasha tena kompyuta yake kuangalia kwenye barua pepe yake nyaraka aliyoiomba kwa Katibu Muhtasi wao.

Kwa bahati nzuri nyaraka hiyo ilikuwa imeshatumwa punde kama dakika 5 zilizopita. Akalifungua faili hilo na kuanza kulisoma. Ilikuwa ni taarifa ndefu iliyoandaliwa kiustadi mkubwa na mwandishi wao wa habari wa Idara ya Usalama wa Taifa.

Baada ya kumaliza kusoma ripoti hiyo ndefu isiyochosha kutokana na kuandaliwa kwa ufundi mkubwa, akashusha pumzi ndefu kuonyesha ngoma ni nzito sana. Fikra zake zikawa zinatembea kwenye mafaili mawili aliyoyaona kwa Nathanieli akashindwa kuyafungua.

Faili la kwanza ni MAN-TEMBA [emoji654]FILE️S/N: 532- 'THREE IN ONE-SOWETO-HOUSE NO. 29, SINZA-MORI [emoji654]️ATM-ISSUES', na faili la pili la 'MAN-TEMBA, FILE S/N: 189- SANDTON CITY CODING SYSTEM'. Akili yake ilikuwa inamtuma ya kuwa lazima akienda pale anapojiegesha Man-Temba atapata majibu yake hayo mafaili yana kitu gani haswa.

ITAENDELEA

Sent from my TECNO CC6 using JamiiForums mobile app
 
RIWAYA-HUJUMA NZITO-PART 22


Faili la kwanza ni MAN-TEMBA [emoji654]FILE️S/N: 532- 'THREE IN ONE-SOWETO-HOUSE NO. 29, SINZA-MORI [emoji654]️ATM-ISSUES', na faili la pili la 'MAN-TEMBA, FILE S/N: 189- SANDTON CITY CODING SYSTEM'. Akili yake ilikuwa inamtuma ya kuwa lazima akienda pale anapojiegesha Man-Temba atapata majibu yake hayo mafaili yana kitu gani haswa.

Akazima kompyuta yake na kuirudisha sehemu yake salama anapoihifadhi kwenye gari, kisha akawasha gari lake kuelekea tena Sinza Mori. Alishaghailisha mipango yake. Badala ya kuvamia usiku wa manane, aliamua aende sasa hivi. Aliamua hivyo kwa kigezo cha kuwa Man Temba yupo mitaani, hivyo nyumba ipo huru.

Alipoangalia saa yake ya mkononi wakati anaegesha gari yake mbele ya saluni aliyotoka kusukwa nywele zake, ilikuwa inasoma saa sita usiku kasoro dakika tano na sekunde kadhaa. Maduka yote yaliyopo eneo hilo yalikuwa yamefungwa. Aliposhuka tu akasalimiana kwa bashasha na mlinzi wa eneo lile na kumuachia majukumu ya ulinzi wa gari lake kwa muda.

Mlinzi yule alifurahi mno maana alijua atakapokuja kulichukua gari lake hatomuacha hivi hivi lazima atamtoa kwa chauchau ya kupunguza ukali wa maisha. Kachero Yasmine akavuka barabara na kuzuga kama analipita pagale analoishi Man-Temba halafu ghafla akavamia kuingia ndani huku tayari mkononi amekamata pisto yake pendwa aina ya Glock-G yenye kiwambo cha kuzuia sauti tayari kwa kazi.

Uzuri kulikuwa hamna mlango wa mbele pako wazi tu, pamesitiriwa na pazia kadimu lililojaa mavumbi. Mboni za macho yake zilikaribishwa na giza totoro lisilo na mfano wake.
Akaanza kutembea kwa tahadhari ndani ya nyumba huku miguu yake inakanyaga ardhini kwa unyenyekevu. Miguu hiyo ikamjulisha kuwa sakafu ya nyumba hiyo chini ilikuwa imepondeka pondeka na kutengeneza makorongo, nyufa na mashimo yasiyo rasmi.

Hakutaka kuwasha kurunzi yake akihofia huenda akashtukiwa kama ndani yake kuna mtu. Alikuwa anatembea kwa mwendo wa pole kwa kupapasa kiambaza huku kadri anavyokwenda mbele anasikia sauti za popo kujigonga ukutani na kuanguka chini, wakichagizwa na upepo mwanana unaovuma nje kupitia madirishani.

Akasita kwenda mbele kwa muda baada ya kukumbuka jambo. Alitanabahi kumbe ana kifaa cha kumsaidia kuona gizani halafu anajitaabisha bure. Akachomoa toka kwenye mfuko wa mbele wa dangirizi yake miwani maalumu yenye uwezo wa kumlinda macho yake na kumsaidia kuona kirahisi akiwa gizani. Alipoivaa akatabasamu kwa furaha na kuanza kutembea bila hofu yoyote, kwani alikuwa anaona kila kitu kiufasaha.

Kwa taftishi yake ya haraka haraka aliyoifanya, ilikuwa ni nyumba ndogo ya vyumba vitatu, vyumba viwili vya kwanza vilikuwa vipo wazi huku cha tatu kikiwa kina mlango wa bati chakavu uliofungwa na kufuli linaloning'inia mlangoni.
Hisia zikamtuma achungulie kwenye hivyo vyumba viwili, macho yake yakakaribishwa na mafurushi ya mizigo isiyo na faida yoyote. Akavikacha vyumba hivyo kisha moja kwa moja akaelekea kwenye kile chumba cha tatu chenye kufuli.

Ile kugusa tu kufuli ili afungue kwa funguo zake malaya, wakatokea mapaka wa rangi nyeusi tii kama watatu, macho yao yanang'ara kama taa ya Aladini. Paka hao wakaanza kumfokea kwa makelele kana kwamba wanamtishia Kachero Yasmine asiguse kabisa ule mlango.

Kachero Yasmine akaanza kurudi nyuma nyuma kwa tahadhari kubwa mpaka alipofika ukutani akajiegemeza huku anatwetwa kwa kuogofya viroja vile mbele yake.
Jasho jekejeke likaanza kumtirika mwilini, hakutegemea kukutana na jeshi la Ibilisi usiku ule. Walikuwa sio paka wa kawaida, ukubwa wao ulikuwa unataka kukaribiana na kitoto cha mbuzi.

Halafu ghafla, ukasikika msonyo wa sauti kubwa ya mtu asiyeonekana kisha wale paka watu wakatimua zao kuelekea kusikojulikana. Kachero Yasmine akashusha pumzi ndefu ya ahueni kutokana na vibweka hivyo vya kimazingara vilivyotoweka.

Kwa ujumla alipwaya kama mtu aliyetoka ugonjwani. Alitanabahi kuwa kazi aliyopewa sio rahisi kama kuhesabu moja, mbili, tatu, ni kazi ngumu na ya hatari anaweza kupoteza uhai akiingia kichwa kichwa na kujifanya pofu kama jongoo. Akakumbukia tukio hilo na ugumu walioupata wakati wanamsaka gaidi wa Amboni kijana Maso Maso kutokana na mambo ya mashetani wa mapangoni.
Akiwa anapanga na kupangua kichwani mwake kitu cha kufanya pindi walipotoweka wale paka, ghafla alipoangaza mbele yake akaanza kuona maji kama ya bahari yamefunika eneo lote la upeo wa macho yake.

Kwa ufupi kila chumba kikawa kimetoweka kwenye uoni wake wa macho. Alinyamaza shuuu huku akiwa amejibanza ukutani, amejinyoosha kama maiti anawaza kitu cha kufanya.
Kwa kuwa Kachero Yasmine pia amekomazwa sio mnemba, alishajua hapo hapaingiliki tena, dawa ya moto ni moto. Himahima akageuka na kutoka nduki nje ya ile nyumba haraka sana kuelekea kwenye gari yake. Mbwa wa nyumba za jirani kumuona anatoka na mbio zile wakaanza kubweka wooh wooh...! lakini Yasmine hakujihangaisha nao. Akakimbia mpaka lilipo gari lake.

Akafungua mlango wa gari lake akaingia na kuufunga, huku amefumba macho yake anatweta kwa uoga. "Vipi dada ndio unatimka sio, basi ganji hata ya soda kidogo..!" alizinduliwa Kachero Yasmine na sauti ya yule mlinzi wa nyumba iliyokuwa mkabala na nyumba ya Man Temba akimpiga kirungu cha kuomba pesa.

Bila kumjibu kitu akachomoa noti ya shilingi elfu kumi kutoka kwenye pochi yake na kumpatia huku akipandisha kioo cha gari yake baada ya kumkabidhi pesa hiyo kuonyesha hataki usumbufu. Yule mlinzi aliganda kwa dakika kadhaa akiwa haamini kama amepewa yote hiyo au ameambiwa arudishe chenji.

Alipoona kimya haambiwi kitu chochote, taratibu akaanza kuondoka mlinzi yule akihofia msamaria mwema wake asije kubadilisha mawazo ikala kwake. Kwa mshahara wake wa kilo na nusu anaoupokea kila tarehe 40, na wakati mwingine mpaka tarehe 50, shilingi elfu kumi kwake ilikuwa ni mshahara wake wa siku mbili kamili.

Kachero Yasmine alikuwa bado na fikra pacha, moja inamuambia aondoke ameshachemsha hamuwezi Man Temba ni bahari kuu, yeye kweli ni “Three In One. Kwa maana ya kuwa ni mtabe wa fani ya mawasiliano 'IT', pia yupo vizuri kwenye Juju za Kinaijeria mpaka amemtumia paka watu pia ni mtaalamu wa kupanga matukio ya kiuhalifu wa wizi wa fedha kinyang'anyi na kiteknolojia.

Sifa zote tatu zilijikusanya kwa Man-Temba, jeshi la mtu mmoja. Huku fikra ingine ikimuambia serikali haiamini uchawi hivi akiondoka zake akarudi ofisini ataenda kumueleza nini Bosi wake Mzee Omega Mtanika, ambaye tayari ameshampachika jina la Singeli, mvivu wa kazi.

Ataenda kuelezea simulizi za Ablakadabra kuwa ameona mauzauza nyumbani kwa Man-Temba?. Nani atamuamini na hadithi hiyo ya kufikirika isiyo na kichwa wala miguu. Hivyo huu upelelezi ulikuwa ni muhimu kwake kujijengea heshima hasa ukichukulia anapambana peke yake akiwa nchini bila kubebwa na kivuli cha Kachero Manu.

"Lazima nipambane kwa juhudi na maarifa siwezi kuweka silaha chini, lazima tuwaonyeshe Watanzania kuwa wanawake tukipewa nafasi tunaweza, hatubebwi tu ili mradi kuleta usawa, kama wanavyotushutumu waumini wa mfume dume..!" alijiapiza huku anapiga mikono juu ya usukani wa gari kwa hamasa.

Ghafla bin vuu akatulizana tuli kana kwamba kuna kitu amekikumbuka. Akaunda tabasamu pana la ushindi usoni mwake. Akashuka haraka chini ya gari na kwenda kufungua buti la gari kisha akashusha chini moja ya begi lake la safari. Begi ambalo lilikuwa na nguo na vifaa vya kazi vya akiba, kiasi kwamba akikurupushwa hata usiku wa manane kuhusiana na safari ya pande yoyote ya dunia anasafiri bila tatizo lolote.
ITAENDELEA

Sent from my TECNO CC6 using JamiiForums mobile app
 
HARDCOPY UKIHITAJI
NICHEKI 0625920847
IMG_20210115_075113_392.jpg


Sent from my TECNO CC6 using JamiiForums mobile app
 
Hii Movie kiboko.Kwa wale wenye bundle unaweza watch:
 
RIWAYA- HUJUMA NZITO-PART 23


Ghafla bin vuu akatulizana tuli kana kwamba kuna kitu amekikumbuka. Akaunda tabasamu pana la ushindi usoni mwake. Akashuka haraka chini ya gari na kwenda kufungua buti la gari kisha akashusha chini moja ya begi lake la safari. Begi ambalo lilikuwa na nguo na vifaa vya kazi vya akiba, kiasi kwamba akikurupushwa hata usiku wa manane kuhusiana na safari ya pande yoyote ya dunia anasafiri bila tatizo lolote.

Alifungua na kuanza kupekenyua ndani ya begi lake. Alikuwa anakitafuta kijitabu chake kidogo alichopewa na marehemu Babu yake mzaa mama siku alipompa taarifa za kuajiriwa kwake kama Afisa Usalama.

"Mjukuu wangu, nakukabidhi kitabu hiki kinaitwa Yasini Mubin ni kidogo lakini penda sana kukisoma kitakupa kinga dhidi ya wabaya wako, hata uchawi na mazingaombwe havitaweza kukudhuru ukikitumia ipasavyo. Mjukuu wangu kazi yako hiyo nzito lazima ujikomaze vilivyo kwa kuwa karibu na Allah Subhanahu Wata'ala" Yasmine alikuwa anayakumbukia maongezi yake na Babu yake siku alipokuwa anamkabidhi kitabu hicho alichokihifadhi ndani ya begi lake.

Bahati nzuri akafanikiwa kukifukunyua kitabu hicho mahali kilipojibanza. Sasa alikuwa tayari ameshakishika mkononi mwake kijitabu hicho, ambacho kimtazamo kilikuwa kimeanza kupoteza nuru kwenye kurasa zake kwa uchakavu wake uliokithiri.

Akafunga begi lake hilo na kulirudisha ndani ya buti na kurudi ndani ya gari yake. Kwa msaada wa mwanga wa ndani ya gari akaanza kuzitafuna nuni na jiimu za kwenye kitabu hicho maktubu kwa lugha ya kiarabu bulbu, kisicho na hata nukta ya kosa la kisarufi.

Ilimchukua kama nusu saa kukimaliza chote. Lakini maajabu kadri alivyokuwa anakisoma kijitabu kile kuna vitu mwilini mwake vilikuwa vinafunguka na mwili wake unaanza kuwa mwepesi na kurudia hali yake ya kawaida na uoga wote umemvuka. Akagundua kumbe alishaanza kufungwa na marogo ya kwenye nyumba ile.

Ghafla mvua nzito ile ya kidindia ikaanza kunyesha kwenye anga ile ya Sinza Mori huku sauti za radi zinalipuka angani mtindo mmoja mithili ya mabomu kwenye uwanja wa vita. Kachero Yasmine hakuwa na muda wa kupoteza ikabidi achomoe koti lake la kujikinga na mvua kutoka siti ya nyuma ya gari na kujivika mwilini. Baada ya hapo akateremka nje ya gari na kuvuka barabara kuelekea kiamboni kwa Man-Temba kwa mara ingine akiwa anatimua mbio.

Safari hii alipoingia tu ndani ya nyumba hiyo akawasha kurunzi yake, akamulika waa nyumba nzima na bastola yake ipo mkononi mwake. Nyumba nzima ilikuwa inavuja utasema imeezekwa na chujio mbovu. Alipoukaribia ule mlango wa bati, ghafla wakajitokeza tena paka wale wale watatu wanaanza kumcheza shere Kachero Yasmine Kama mwanzoni. Safari hii hakutana utani nao tena, akamlenga mmoja wao kwa bastola yake na kumfyatulia risasi moja iliyotua sawia kichwani mwa paka huyo.

Pale pale kiumbe kile kikadondoka chini na kuanza kupwiripwita kwa huruma mpaka kikata roho. Wale paka wengine kuona mwenzao anavuja damu wakatoka nduki huku nyayo zao zinalia pukutu pukutu kutokana na kuzidiwa kwa uzito wa miili yao.

Yasmine alipoumulika kwa kurunzi ule mzoga wa paka akakuta shingoni umefungwa bonge la hirizi nyekundu. Hapo hapo ule mzoga ukaanza kunuka fee fee harufu ya uozo. Hiyo ikazidi kuthibitisha kuwa yule hakuwa paka wa kawaida. Akaachana nao ule mzoga na kuendelea na kilichomleta kwenye nyumba ile.

Akalikorokochoa kufuli lile kwa funguo malaya mpaka likafunguka na kumuwezesha kuingia kwenye chumba kile. Alipokimulika mwangaza vizuri akakuta kuna tandiko moja tu, jembamba mithili ya ulimi wa ng'ombe. Hakukuwa na kitu kingine chochote kile cha thamani, jambo ambalo lilimstaajabisha sana Kachero Yasmine. Tandiko hilo lilikuwa limewekwa juu ya zulia chakavu lililoenea chumba kizima.

Kijasho chembamba cha juu ya pua zake kikaanza kumvuja bila kupenda. Alijiona kama vile Amechezewa kanya boya ya hatari, kuliko mategemeo yake. Fikrani mwake alihisi huenda kitakuwa ni chumba ambacho kimesheheni vifaa vizito vya kazi kama ishara ya meseji alizokuta nyumbani kwa Nathanieli zilivyoashiria.

Akakifanyia speksheni chumba kizima kwa umakini mkubwa, mpaka sehemu za ukutani labda atakuta unafunguka popote, akatoka patupu. Baada ya taftishi ya zaidi ya nusu saa akaamua atimke zake ndani ya chumba kile hamna chochote cha maana anapoteza muda wake tu.

Alipoufikia mlango wa kuingilia anataka sasa ausukumize mlango ule wa bati atoke nje akasita kidogo. Akageuka nyuma na kumulika kurunzi pale kwenye tandiko kwa sekunde kadhaa kama mtu aliyegundua kitu. Akaamua arudi tena mahali ambapo limewekwa godoro. Alipofika akalipiga teke kwa kutumia viatu vyake vya raba vya ngozi, likasogea pembeni lile godoro. Akaanza kumulika kwa umakini mkubwa eneo lote pale sakafuni lililokuwa limezibwa na godoro lile.

Kuna kitu akakigundua katika taftishi yake hiyo. Aliona kuna mkato wa duara juu ya lile zulia katikati ya pale palipozibwa na godoro. Mkato huo ulionekana kuungwa kiustadi mkubwa na sehemu nyingine ya zulia hilo. Akafanya maamuzi ya kuvuta kwa nguvu sehemu hiyo ya zulia kwa bahati ikanyofoka na kuacha eneo wazi la sakafuni lililozibwa na mfuniko wa shaba.

Akajibidiisha kuuvuta huo mfuniko kwa nguvu zake zote, lakini akaukuta umeng'ang'ania ng'ang'anu hauchomoki kirahisi. Akaendelea kujibidiisha mtoto wa kike kwa nguvu zote kuuvuta mfuniko huo bila kukata tamaa mpaka ukakubali kufunguka. Ukalia mlio wa sauti buuuh..! mfuniko ule baada ya kukubali kuachia.

Sasa usoni mwake furaha yake ilikuwa sheshe isiyo na kifani, huku kijasho chembamba cha juhudi kikimtiririka mashavuni mwake. Alipoangalia saa yake ilikuwa inasoma saa nane na robo ya usiku wa manane. Pia huko nje, mvua ilishakata kunyesha kabisa kitambo kirefu.
Alipopiga chabo ndani ya shimo, kulikuwa na kiza totoro kiasi kwamba kurunzi ilikuwa haitoshi mwangaza wake. Akapiga moyo konde na kuanza kuteremka kuelekea chini ya shimo lile huku akiurudishia vizuri mfuniko ule juu, akijipa moyo wa liwalo na liwe. Muda wote alikuwa anawaza huyu mkazi wake hii nyumba, Man-Temba yupo wapi mpaka sasa.

Akaanza kuteremka ngazi moja baada ya ingine kuelekea chini ya shimo. Kadri anavyoshuka chini ndio hali ya hewa inazidi kumchefua chefu chefu, lakini akazidi kupiga moyo konde aendelee na msafara wake bila kusalimu amri.
Alishuka kama mwendo wa dakika 10 hivi ndipo akakiona mbele yake chumba kimoja kizuri ila kidogo sana chenye uwezo wa kuingiza watu wasiozidi watatu tu.

Kwa bahati mlango wake chumba hicho ulikuwa umebugazwa tu. Akausukuma na kuingia ndani mzima mzima. Ndani ya kichumba Kulikuwa na meza ndogo juu yake kuna kompyuta mpakato ndogo na mzinga mkubwa wa konyagi.
Alipomulika zaidi kwenye chumba kile akaona swichi ya umeme na kiyoyozi mle kwenye kijichumba. Akaelekea ukutani na kuwasha batani hizo, kufumba na kufumbua nuru ikaenea chumba kizima na kiyoyozi kikaanza kuleta hewa nzuri ya kuvutia ndani ya chumba kile na kulifukuza kwa kasi joto lililokuwa limeshitadi ndani ya chumba kile.

Akavuta kiti kisha akaketi juu yake na bila kupepesa macho akaanza kuhangaika kuiwasha kompyuta hiyo. Wakati Kompyuta inajiweka sawa kwa ajili ya kuanza kupiga kazi, akavuta droo ndogo ya upande wa kushoto wa meza hiyo, akashtuka kidogo.

Alikutana na lundo la ATM-kadi za benki tofauti tofauti za ndani na nje ya Tanzania na mishumaa isiyopungua mitano. Kadi hizo zilikuwa ni mali za benki mbalimbali za Congo, Gambia, Afrika ya Kusini na nchi nyinginezo. Akakumbuka wameshawahi kupewa mafunzo namna pesa zinavyoibwa kwenye mashine za benki, enzi ATM-Mashine zimeanza kutumika nchini Tanzania kwa mara ya kwanza.

Aina hii ya kuiba pesa kwa kutumia nta ya mshumaa, hii ni mbinu ya kizamani kidogo lakini bado kwa nchi zinazochechemea kiteknolojia ilikuwa inaweza kufanya kazi kwa asilimia kadhaa. Akaachana na kadi hizo huku akiweka umakini kwenye kompyuta aliyoiwasha punde ili kujitafutia kilichomleta ndani ya chumba hicho cha maajabu..

Kompyuta sasa ikawa imefunguka, akaanza kuyaperuzi mafaili ndani yake kadri atakavyo. Mafaili yote yaliyohifadhiwa ambayo aliyaona yana manufaa kwake alikuwa anayafowadi kwa Kachero Manu kwenye baruapepe yake na kuyahifadhi pia kwenye flashi yake. Alipanga akayasome vizuri nyumbani kwake atakaporejea maana tayari kichwa kilishachoka.

Ghafla wakati anajiandaa kuifunga ile kompyuta ikaja meseji kwenye mesenja yake Man-Temba, anaulizwa swali, "Pesa zinakaribia kusafirishwa wiki ijayo, tunasubiria mtu toka Tanzania atakayesindikiza magari hayo kutoka nchini Afrika ya Kusini kama ulivyoahidi". Ujumbe uliandikwa kuwa umetoka kwa Professor "Potchefstroom". Kachero Yasmine akashtuka na kubaki ameduwaa mdomo wazi kwa sekunde kadhaa kama zuzu hajui atoe jibu gani pale.

"Mbona hutoi jibu haraka, tukichelewa pesa zitagandishwa tushindwe kuzitoa kwa wakati, tekeleza makubaliano yetu kwa kumtuma mtu makini kama ulivyoahidi, hatuna muda wa kupoteza..!" ujumbe mwingine ulitumwa papo kwa papo kwa mtindo wa bandika bandua.

Yasmine akili yake ikachakata mambo kwa haraka sana, ikabidi ajiongeze tu kwa kujibu kwa kubahatisha tu."Sawa ameshafika mtu wetu, mpe mawasiliano namna atakavyokupata.!". Kimya kirefu kikatawala bila majibu yoyote toka upande wa pili mpaka akaanza kuingiwa na wasiwasi Kachero Yasmine kuwa huenda ameshtukiwa kuwa ni mdukuzi.

Mara akaona yule mtu anayejiita Professor Potchefstroom anachapa maneno ya kujibu. Uso wa Yasmine ukarudiwa tena na bashasha mpwitompwito na uchangamfu wake ulioanza kupotea. "OK... atapokewa na Mr. Okworonko, Sandton Gautrain Station kesho saa 6:00 mchana. Akifika ampigie kwa namba +27 83 347 21143. Tusiwasiliane tena kuanzia sasa mpaka siku mzigo wa kwanza unatua Dar es Salaam, Bye..Tchaooo..!!" jamaa akatoka kwenye mtandao.

Kachero Yasmine bila kufanya ajizi akatuma taarifa zote kwenye barua pepe ya Kachero Manu ikiwa na maelezo ya kina ya kumtaka ajifanye yeye ndio wakala aliyetumwa na Man-Temba nchini Afrika ya Kusini kufuatilia fedha. Alipotaka kuifunga kompyuta hiyo hakutaka kuiacha salama. Akairushia moja ya virusi wabaya wanaotafuna mafaili yote yaliyohifadhiwa.

Kirusi hicho kibaya ni Kachero Yasmine pekee ndio angeweza kuyarudisha mafaili hayo pindi akiyahitaji. Baada ya kufanikisha lengo lake hilo akajikuta anaunda tabasamu la ushindi, huku alijiapiza kiwa siku za wanaokula njama za uhaini kukamatwa zinahesabika kwa vidole.

Wakati anajiandaa kuondoka kwenye chumba kile akiwa tayari ameshasimama wima, akahisi kitu kama ubaridi usio wa kawaida juu ya sikio lake la kushoto. Alipogeuka tu akakutana na mdomo wa bastola unamsalimia. "Mrembo karibu kiamboni kwetu, jiskie huru..!" alikaribishwa na sauti nzito, yenye mikwaruzo ya mtu aliyekuwa amejifunika sura yake na kuachia macho yake tu huku akiwa tayari ameitwaa silaha ya Kachero Yasmine iliyokuwa pembeni ya meza yenye kompyuta.

Kachero Yasmine alipigwa na butwaa asijue la kufanya huku akijilaumu kwa uzembe wake wa kupitiliza uliomfanya afumaniwe kiwepesi sana. Nafsini kwake alikubali kabisa kuwa hakuchukua tahadhari ya kutosha. Uso wa Kachero Yasmine ulipigwa na taharuki, fedheha na soni isiyomithilika, akiwa ameishiwa mipango
ITAENDELEA
HAYA KACHERO YASMINE, KASHAINGIA KWENYE 18 ZA MAN-TEMBA
[emoji1787][emoji1787][emoji1787][emoji1732][emoji1732][emoji1732][emoji91][emoji91][emoji91]

Sent from my TECNO CC6 using JamiiForums mobile app
 
Back
Top Bottom