Riwaya: "Hujuma Nzito"

Riwaya: "Hujuma Nzito"

Hongera mpasta
kipindi hiki cha majonzi mngetupia humu threads za kutosha ili watu waweze kujifariji.Nina uhakika wengine humu wamejiweka Lockdown bila shuruti!
 
RIWAYA-HUJUMA NZITO-PART 24


Wakati anajiandaa kuondoka kwenye chumba kile akiwa tayari ameshasimama wima, akahisi kitu kama ubaridi usio wa kawaida juu ya sikio lake la kushoto. Alipogeuka tu akakutana na mdomo wa bastola unamsalimia. "Mrembo karibu kiamboni kwetu, jiskie huru..!" alikaribishwa na sauti nzito, yenye mikwaruzo ya mtu aliyekuwa amejifunika sura yake na kuachia macho yake tu huku akiwa tayari ameitwaa silaha ya Kachero Yasmine iliyokuwa pembeni ya meza yenye kompyuta.

Kachero Yasmine alipigwa na butwaa asijue la kufanya huku akijilaumu kwa uzembe wake wa kupitiliza uliomfanya afumaniwe kiwepesi sana. Nafsini kwake alikubali kabisa kuwa hakuchukua tahadhari ya kutosha. Uso wa Kachero Yasmine ulipigwa na taharuki, fedheha na soni isiyomithilika, akiwa ameishiwa mipango.

Akili yake ilikuwa inamchombeza "pambana wewe mpaka tone lako la mwisho la damu usikubali kushindwa kibwege" lakini alikuwa anasitasita kuanzisha varangati kwa sababu alikuwa hajui ukubwa wa nguvu za adui yake, kama yupo peke yake au na wenzake.

Akajipa moyo kuwa subira yavuta heri, na daima haraka haraka haina baraka, ngoja aone mwisho wake itakuwaje. Huku akijiapiza kuwa kosa lolote ambalo maadui zake watalifanya dhidi yake atalitumia vizuri ipasavyo kuweza kuwageuzia kibao.

Yule jamaa akaipandisha barakoa yake kichwani kwa juu kidogo na kuachia mdomo wake wazi, kisha akasogeza mdomo wake ampige denda Yasmine. Mdomo ambao meno yote yalikuwa ya njano kutokana na uvivu wa kupiga mswaki, unywaji wa pombe na uvutaji wa bangi na sigara wa kupitiliza huku ukitoa riha mbaya yenye kuchukiza kwenye pua.

Yasmine akili zake zilishafanya kazi yake ipasavyo akaligundua lengo la yule jamaa kuacha mdomo wazi. Akakwepesha mdomo wake usikutane na mdomo wa mjuba yule kwa kukaza misuli ya shingo yake na kufumba mdomo wake.

"Sasa mbona huna ushirikiano Bibie? Ulivyofanya maamuzi ya kuja kwenye gheto la mwanaume wa shoka ulitegemea nini? Pumbavu sana wewe" alizungumza kwa ukali jamaa yule na matusi lukuki huku akimshindilia vibao vya nguvu kwenye uso wa Yasmine. Kisha akapiga mluzi kuelekea juu ya shimo kule juu.

Punde si punde akashuka kijeba cha mtu, mweusi ti ti ti, ana mapengo mdomo mzima amevalia pensi nyeusi ya dangirizi. Chini alikuwa amevaa viatu aina ya buti. Alifika ndani ya kile chumba, wakawa sasa wamembana vilivyo Kachero Yasmine hawezi kabisa kufurukuta wala kujimwayamwaya mbele yao.

Yule kibushuti ukimtazama umbile lake alikuwa anatisha kimuonekano, uso wake wote umepambwa kwa makovu ya suluba mbalimbali alizowahi kukutana nazo kwenye shughuli zake za uhalifu.
Alikuwa akicheka kama analia vile. "Vipi mbona unacheka nae...huyu ni mtu hatari sana, mpaka kafanikiwa kufika hapa ujue amefukunyua mambo yetu mengi sana..!!" aliongea kwa sauti yenye kukwaruza isiyo na chembe ya masikhara yule mtu mfupi.

"Huyu Inabidi tuondoke nae tukambinye taarifa gani alikuwa anazidukua na amezituma wapi. Tatizo Man-Temba amelewa sana, yupo chakari tumsubirie asubuhi atakapokuwa na fahamu ndio ataweza kugundua taarifa gani zimedukuliwa" alijibu yule mjuba aliyejisitiri uso wake.

"Basi kama ni hivyo sasa tukamgeuze kuwa Bibi yetu mpaka asubuhi, hakikisha umebeba kondomu za kutosha maana Binti ni mbichi huyu kabisa chuchu zimemsimama haswa" alichagiza yule kibushuti huku sasa akimkamata kwa nguvu Kachero Yasmine na kuanza kumpapasa kimahaba, akionekana nae pia ni mbovu wa ngono.

Akawa anajaribu kujipapatua bila mafanikio toka mwilini kwa kibushuti yule ambaye alishapandisha ashki ya ngono. Kachero Yasmine hakukubali kirahisi kuliwa denda kibudu bila idhini ya Walii wake na hotuba ya Sheikh, akamng'ata meno shingoni kibushuti yule ambaye alishaanza kulegea kimahaba.

"Aaaaaah...!" Aligugumia kwa maumivu makali wakati Yasmine kanyofoa kipande cha nyama shingoni mwake. Yule kibushuti akajipachua mwenyewe mwilini mwa Kachero Yasmine bila kupenda. Yule mjuba mwingine kuona hivyo akamvaa wanguwangu Yasmine ili amuadabishe.
Kumbe alimuona vizuri anavyokuja, akajipinda kidogo, yule jamaa akapita mzima mzima na kwenda kuiparamia kompyuta pale mezani na kwenda kujigonga ukutani.

Yule kibushuti kumbe alishajipanga zamani, akawahi kudaka kiti cha chuma kilichomo chumbani mule.
Kachero Yasmine alipogeuka, tayari alikuwa ameshachelewa kukipangua kiti hicho kilitua sawia kichwani mwake maeneo ya kichogoni. Hamadi! lilikuwa ni pigo takatifu lililomfanya ahisi kizunguzungu na kuanza kuyumba na kujikuta anaanguka sakafuni kwenye zulia na kupoteza fahamu.

Alisikia kwa mbali sana kauli za wale mahasimu wake wakishauriana watoke nae haraka asije akawafia mle ndani kutokana na upotevu mkubwa wa damu mwilini mwake. Akaanza kuona nyota nyingi usoni mwake. Nyota ambazo wataalamu wa elimu ya anga hawawezi kuzieleza kazi yake. Akajiona anaanza kushuka kwenye shimo lefu lenye kiza kinene lisilo na mwisho, mpaka akapoteza fahamu.

SURA YA KUMI NA MOJA

Professor Potchefstroom..
"Sandton Gautrain Station" ni kituo cha treni cha kisasa kilichopo nchini Afrika ya Kusini, kilichojengwa katika makutano ya barabara za Rivonia na West Streets. Ni kituo kilichojengwa kwa ajili ya kupitisha treni za chini kwa chini zinazoelekea katika Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa 'OR TAMBO AIRPORT', huku juu yake kukijengwa platifomu mbili za juu, nazo zenye kufanya safari zake sehemu mbalimbali.

Kulikuwa na njia za mabasi ya kisasa yanayowatoa abiria na kuwaleta kituoni hapo, yenye kwenda na kurudi maeneo yasiyo pungua sita. Nazo njia hizo ni,Wendywood (S2), Rivonia (S3), Randburg (S4), Fourways (S5), Rosebank (S6) na Sandton CBD loop (S1). Hicho kituo kilizinduliwa rasmi mwaka 2010 kutokana na umuhimu wa kiuchumi wa eneo hili la Sandton City lililopo ndani ya Jiji la Johanesburg.

Huu Mji mdogo wa Sandton ulikuwa ndio chemchem ya uchumi wa Afrika ya Kusini kwa upande wa biashara. Majengo makubwa ya kibiashara "Malls" yalikuwa yanapatikana ndani ya Mji huo. Kampuni kubwa zote duniani unazozijua wewe zilikuwa na maduka yao ya kuuzia bidhaa halisi ndani ya eneo hilo.

Kuanzia kampuni ya mikoba ya mikononi kama Louis Vuitton, mpaka wauza bidhaa za mapochi, na mikanda, kampuni ya Gucci nao wapo hapo. Bila kusahau kampuni kama za Prada, Patek Phillipe, Dolce & Gabbana hao wote walipiga kambi kwenye eneo hilo dogo lenye ukwasi wa kupindukia.

Kwa ujumla Sandton ni eneo la kifahari sana pale Johanesburg, kuna nyumba za gharama kubwa mno, mahoteli ya kifahari mno, magari ya anasa, yaani kila kitu unachokiona hapo ni cha kifahari. Inasemekana Sandton ndio mtaa wa kitajiri zaidi barani Afrika. Eneo hilo peke yake linakadiriwa kuwa na mabilionea wanane (8), na mamilionea (USD) si chini ya mia moja ishirini na saba (127).

Kiufupi kuishi katika Mji huo inakubidi uwe vizuri zaidi ya sana kiuchumi. Kila mtu unayekutana nae mtaani ana dalili zote za kuwa ni Mlalaheri na sio Mlalahoi, haswa kutokana na gari yake anayoiendesha, nyumba anayoishi, kazi anayofanya na mengineyo.

Kachero Manu kwa upande safari ya kurejea Tanzania ilishakufa tayari kutokana na maelekezo aliyopewa na Kachero Yasmine kuwa aonane na Mr.Okworonko kwa ajili ya kushughulikia pesa zilizotoroshwa Tanzania na kuja kufichwa nchini Afrika ya Kusini namna zitakavyorudishwa kinyemela nchini Tanzania zifanye lengo lililokusudiwa. Alijifanya ndio ametoka Tanzania kuja kwa kazi hiyo aliyoagizwa na Man Temba, kumbe hata kufahamiana hawafahamiani.

Roho yake ilikuwa inamdunda hasa kuogopea kushtukiwa na maadui zake hasa ukichukulia wameanza kuisaka roho yake tokea siku ya kwanza tu anakanyaga nchini Afrika ya Kusini. Alijibadilisha kidogo muonekano wake kwa kunyoa upara na ndevu zake zote, akawa anaonekana ni kijana haswa hasa kutokana na umbo lake la kimazoezi.

Alipowasili tu pale stesheni ya Sandton Gautrain akapiga namba simu aliyopewa na Kachero Yasmine. Bahati nzuri akajibiwa kuwa Mr.Okworonko yupo njiani anakuja. Alipojibiwa hivyo akatafua mgahawa hapo hapo stesheni ili apate kifungua kinywa maana alikurupuka nyumbani bila hata kuuchoma utumbo wake kwa chai.

Ile anamalizia tu staftahi yake akasikia simu yake inaita, bila kufanya ajizi akaipokea. "Hellow....Yap...Al-right..haina noma naja" alijibu Kachero Manu simu ya upande wa pili kisha akakata simu. Alipigwa na bumbuwazi kwa muda akishangazwa na Kiswahili fasaha kinachocharazwa na Mr.Okworonko. Akafanya haraka kwenda kumuwahi kwenye eneo la maegesho ya magari pale stesheni kumlaki.

"Ooh...Nice to meet you, I'm Mr.Okworonko, if you wish call me Mr.OK...that is my nickname, and you?? akatupiwa swali Kachero Manu akiwa ameshapanda kwenye gari, swali ambalo hakujiandaa nalo kulijibu kwa haraka haraka. Hakujipanga kabisa na swali hilo.
"I'm...I'm....call me Ken-D my nickname..!" alipatwa na kigugumizi cha ghafla Kachero Manu. "Ooh..Sorry Be free to speak Swahili najua nyie Wabongo wengi Kiingereza ni tatizo kwenu... teh... teh.. teh..!" alimtoa hofu Kachero Manu, kisha wote kwa pamoja wakaangua kicheko.

Wakaelekea nyumbani kwa Mr.Okworonko.
Kumbe angejua kuwa Kachero Manu, kimombo ndio kimelala kwake utasema kazaliwa nyumbani kwa Malkia wa Uingereza, wakati ni Mmwera tu wa Mahiwa, Lindi. Alipofika nyumbani kwa Mr.Okworonko bila kuchelewa mafunzo yakaanza mara moja, ya namna ya kuendesha mifumo mbalimbali ya utapeli wa kwenye mabenki.
ITAENDELEA

Sent from my TECNO CC6 using JamiiForums mobile app
 
RIWAYA- HUJUMA NZITO-PART 25


Moja ya lengo la Nyasa Empire Supporters (NES) lilikuwa ni kuweka kituo cha utapeli huo kwa ajili eneo la Afrika Mashariki na Kati. Jukumu la kwanza lilikuwa ni kuhakikisha pesa zilizoibwa na kutoroshwa kwenda kufichwa kwenye Mabenki katika Mji wa Sandton City zinarudi Tanzania kinyemela na kufanya lengo husika lililokusudiwa. Lengo la pesa hizo lilikuwa ni kutumika kwenye Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani kwa kuhakikisha wapiga kura wanahongwa ili wakichague na kukiingiza madarakani kwa kishindo chama cha upinzani cha National Movement Party (NMP) kinachoongozwa na Dr Patrick Ndomba.


Kwa muda wa siku tatu tu Kachero Manu alizoishi katika Mji huo akagundua kitu kimoja, kwamba kuna asilimia kubwa sana ya vijana wadogo kiumri wanaishi hapo Sandton City, na wengi walikuwa ni watu wenye asili ya Afrika Magharibi kuanzia Naijeria, Cameroon na Ghana.
Walikuwa na maisha mazuri mno, wengi wao wakionekana maeneo ya kula bata wakiwa na magari ya thamani sana na kufanya vitu vya anasa. Cha kushangaza hawa vijana hawakuwa na kazi wala biashara yoyote ya maana, hawakuwa na michongo yoyote ya kueleweka hadharani. Lakini waliweza kumudu maisha ya Sandton na anasa za hali ya juu.

Mfano mwenyeji wake Mr.Okworonko alikuwa anamkodishia Kachero Manu kila siku gari la kifahari aina ya 'Rolls-Royce Phantom' kwa gharama ya R4000 kwa ajili ya kumzungusha kwenye mizunguko yake ya mjini kila siku na kumrudisha mahali alipofikia.
Ilipofika siku ya tano, akiwa tayari ameshaanza kuiva na kufundwa mbinu mbalimbali za ukwapuaji wa pesa kwenye Mabenki, siku moja usiku wa majira ya saa 4:00 Kachero Manu akaitwa na Mr.Okworonko sebuleni kwake, wakaketi kwa ajili ya mazungumzo yao ya faraghani yaliyohitaji utulivu mkubwa baina yao.

"Kesho Asubuhi ndio nakupeleka kwa Professor Potchefstroom..!!" alifungua maongezi yake Mr.Okworonko kisha akaweka kituo akawa anajimiminia maji kwenye glasi yake na kuanza kuyagida mfululizo, kisha akaendelea. "Mimi nilichoagizwa nikufundishe nimeshamaliza kazi, Yeye ndio ataenda kukupa mbinu za mwisho namna pesa zitakavyotoka hapa na kurejea kwenu Tanzania.

Onyo ninalokupa ni kuwa Professor Potchefstroom hataki ubabaishaji, usaliti wowote dhidi yake ujue kifo kinakuita. Ana mtandao mpana Afrika nzima mpaka katika bara la Amerika. Una bahati sana kuonana na yeye, mimi nipo hapa nchini Afrika ya Kusini mwaka wa 10 sasa sijabahatika kumuona uso kwa uso zaidi ya kupokea maagizo toka kwa wakubwa zangu waliopo nchini Naijeria ambao nao Bosi wao ni Professor Potchefstroom.

Nikutakie kila la kheri kwenye safari yako ya kurejea nyumbani kwenu Tanzania". Yalikuwa ni mazungumzo mafupi yenye kutoa zaidi maelekezo ya upande mmoja badala kufungua mjadala.
Kachero Manu alikuwa anasikiliza tu kwa umakini mkubwa huku moyoni akifurahia kwenda kukutana na mzizi wa tatizo. Mtu ambaye ndiye aliyehandisi uhaini na ukwapuaji huo mkubwa wa pesa katika mabenki Tanzania, uliotikisa nchi nzima.

Wakatakiana usiku mwema huku kila mmoja akielekea kwenye khurfa yake kulala, tayari kwa Kachero Manu kujiandaa na safari ya kesho yake kuelekea kwa Professor Potchefstroom.
[emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586][emoji3586]

Mama Catherine alikuwa tayari ameshawasili katika viunga vya shule ya sekondari ya wasichana-Kilakala iliyopo takribani kilometa 5 kutoka stendi kuu ya Mabasi ya Msamvu, ndani ya Mji kasoro Bahari, Morogoro.

Ujio wake pale shuleni ulitokana na barua ya wito toka shuleni ukimtaka afike mara moja bila kukosa tarehe 30/07/1970 saa 4:00 asubuhi. Ni barua ambayo ilizua taharuki kubwa katika mioyo ya wazazi wake Catherine Mushi, mwanafunzi wa Kilakala. Kwani binti yao alikuwa hajamaliza hata wiki tatu tokea aripoti shuleni hapo kwa ajili ya kuanza durusu za kidato cha 5.

Catherine alikuwa ni binti yao wa pekee katika ndoa yao ya zaidi ya miaka 20. Alichaguliwa kujiunga na shule ya wasichana Kilakala akitokea sekondari ya Korogwe Girls baada ya kuongoza kitaifa kwa upande wa wasichana katika matokeo ya mtihani wa kidato cha 4 kwa mwaka 1969. Alipata alama 'A' kwenye kila somo alilofanya mtihani wake, likiwemo mpaka somo la ufahamu wa maarifa ya Biblia.
Hivyo mtoto wao huyo wa pekee walimuona kama ni nyota ya baadae kwa Taifa la Tanzania hasa ukichukulia kipaji chake pekee cha kiakili alichojaaliwa na Mwenyezi Mungu na maadili ya hofu ya Mungu waliyomlea.

Mama Catherine alikuwa amekaa pamoja na wazazi wenzake watatu chini ya turubai maalumu lililowatenganisha wao na watoto wao likiwa nje ya ofisi kuu ya walimu. Ndani ya ofisi hiyo kulikuwa na kikao cha bodi ya shule inarindima huku vigogo wote wa bodi na uongozi wa Mkoa wa Morogoro ukiwa ndani ya kikao hicho. Mabinti hao walikuwa wanaitwa mmoja mmoja ndani ya kikao hicho kuhojiwa.

Wazazi wote walikuwa kama wamechanganyikiwa hawajui maswahibu gani ya kinidhamu yamewakuta watoto wao, hasa baada ya kuona kila binti akitoka kwenye mahojiano hayo anaangusha kilio kama amepewa taarifa za msiba.

Majira ya alasiri wazazi wote wakaitwa ndani ya kikao cha bodi hiyo kupewa nia na madhumuni ya wito wao. Walikabidhiwa rasmi barua za kuwajulisha kuwa watoto wao wamefukuzwa kwa kosa la kinidhamu la kukutwa na mimba.
Katika utaratibu wa kawaida wa shule wa kuwapima wasichana pindi wanaporudi toka likizo, ndio ukawanasa Mabinti hao wanne kuwa na mimba pamoja na Catherine nae akiwemo. Walitulizwa kwa kupewa ushauri nasaha wa kuishi nao kiustaarabu bila kuwanyanyapaa kuogopea wasije Mabinti hao wakachukua maamuzi magumu ya hata kujiua.

Baba Catherine, Meja Mushi alivyopata habari hiyo alicharuka kama mbogo aliyekoswakoswa risasi na jangili. Alitaka hata kumpiga risasi binti yake kwa aibu hiyo aliyoileta kwenye familia. Lakini ndugu, jamaa na marafiki wakafanya kazi kubwa ya kumshusha wahaka wake.
Mama Catherine bado nae akawa haamini anatafakari mwanawe kaipatia wapi mimba hasa ikichukuliwa maadili mufti aliyomkuza nayo bintiye. Jibu la mhusika wa mzigo huo likawa ni gumu kulipata wakabaki na giza zito kwenye mioyo yao.

Siku hazigandi hatimaye muda wa kujifungua ukatimu, akazaliwa mtoto dume. Mjukuu ambaye furaha yake ya kuzaliwa ikawasahaulisha aibu iliyoletwa na Catherine. Mjukuu akaleta neema ya upendo na umoja upya katika familia.
Babu yake akampa jina la 'Asante-Rabbi', akimaanisha Ahsante Mungu kwa zawadi ya mjukuu. Asante-Rabbi huyu Mziwanda wa Catherine ndio huyu Professor Potchefstroom kigogo mzito wa Nyasa Empire Supporters (NES) ya leo inayowatoa jasho na kamasi akina Kachero Manu na Kachero Yasmine na kuutikisa uchumi wa nchi.

Ndio huyo anayeheshimiwa na matapeli wote wa wizi wa mtandao kutoka nchi zote za Afrika Magharibi. Asante-Rabbi huyu alilelewa na kukuzwa kwa upendo na mahaba mazito na familia nzima, walikuwa wanamtunza kama mboni ya jicho. Kwa ujumla alikuwa mtoto wa Bibi na Babu.

Alipofikisha umri wa miaka 7, mwaka 1977 akaandikishwa darasa la kwanza. Kwa jina la Asante-Rabbi Mushi, babu yake hakutaka hata kulisikia jina la baba wa mtoto likitajwa. Alikuwa akitajwa mhusika jina lake anajisikia kichefuchefu.
Mhusika alikuwa ni Shamba-Boi wao aliyekuwa akijulikana kwa jina moja tu la Ngwenyama. Ambaye baada ya kupata penyenye kuwa Catherine kafukuzwa shule kwa sababu ya ujauzito, alilala mitini.

Alishajua ishu ikibumbuluka hawezi kubakia salama. Mchaga Meja Mushi wa jeshi la wananchi JWTZ asingemuacha salama, lazima angempiga risasi au kumtia kilema kwa kumuharibia binti yake.
Asante-Rabbi huko shuleni alipofika umri wa kusoma akageuka moto wa kuotea mbali kwa jinsi kichwa chake kinavyochaji darasani. Mtoto wa nyoka ni nyoka, kama mama yake mzazi Catherine alivyokuwa mtabe wa masomo darasani na yeye alikuwa hivyo hivyo. Matokeo ya kumaliza elimu ya msingi mwaka 1983 ndio yalimtangaza Asante-Rabbi Mushi mbele ya Watanzania wote kwenye redio na magazeti kuwa ni mshindi.

Aliongoza nchi nzima kwa kupata alama ambazo tokea baraza la mitihani ya taifa "NECTA" lianzishwe kulikuwa hamna mwanafunzi aliyewahi kupata alama hizo. Wapo waliomtabiria Asante-Rabbi mazuri, kuwa huenda akaja kuwa mmoja wa Wanasayansi wa kuheshimiwa dunia mfano wa akina Isack Newton, mwanafizikia bobezi.

Akachaguliwa kujiunga na shule ya sekondari ya wavulana, Mzumbe iliyopo Mkoani Morogoro. Shule ambayo ilikuwa ni maalumu kwa watoto wenye vipaji vya kipekee vya kiakili. Huko nako akauendeleza moto wake wa masomo ule ule aliouwasha tokea shule ya msingi.
Tokea kidato cha kwanza mpaka anahitimu kidato cha nne yeye ndio alikuwa kinara kwenye masomo. Maajabu ilikuwa kuna wakati mpaka wanafunzi wa kidato cha tano na sita walikuwa wakikwama kwenye somo la Hesabu na Fizikia, wanamuona Assante-Rabbi anawatatulia.

Ila chambilecho uzuri wa mkakasi ndani kipande cha mti, asiye na hili ana lile. Asante-Rabbi alikuwa mkimya na mpole kupitiliza, jongoo ana nafuu. Alikuwa ni mtu wa kujitenga hapendi kuchanganyika na makundi ya wanafunzi wenzake. Ni mwanafunzi mmoja tu shuleni pale ndio alizoeana nae sana, mpaka watu wakastaajabishwa.

Mwanafunzi huyo akiitwa Newton Temba. Nae alikuwa na silka za kufanana na Asante-Rabbi. Mpaka watu wakawa wanajiuliza hawa hasa wanaunganishwa na kitu gani hasa ukichukulia ya kuwa Asante-Rabbi alimpita madarasa mawili Newton Temba.
Huyu Newton Temba ndio Man-Temba, ambaye ukubwani kwao waliunda tena uwili mtakatifu kati yake na Asante-Rabbi katika mawasiliano ya utapeli wa zile fedha zilizoibwa ndani ya Mabenki matatu makubwa nchini.

Basi pale shuleni wapo waliosema Asante-Rabbi anaringa kutokana na uwezo wa kiakili alio nao ndio maana hataki kabisa kujichanganya na wenzake anawaona vilaza. Wapo waliosema anajidai kwa kuwa anatokea familia ya kigogo wa Jeshi, Meja Mushi hivyo anajiona ni Mlalaheri na wengine wote ni Makapuku Bin Walalahoi.
Ili mradi kila mmoja alizusha lake, lakini hawakujua kitu ambacho kilikuwa kinamtafuna ndani kwa ndani mpaka kumfanya awe mnyonge kupitiliza kiasi hicho.

Kikubwa kilichokuwa kinamkosesha raha ni kitendo cha kutokumfahamu baba yake mzazi. Alishagundua kuwa Mzee Mushi ni Babu yake sasa Baba yake yupo wapi na kwanini hawaishi nae pamoja ndio kitu kilikuwa kinamkosesha sana raha.
Kila alipokuwa anajaribu kumchokonoa Mama yake mada ya kuhusiana na Baba yake mahali alipo, alikuwa anaitolea mbavuni hataki kuijadili hiyo mada. Ndipo ilipokuwa imebaki wiki tatu tu kumaliza mitihani ya kuhitimu elimu ya kidato cha nne, alipoamua kufanya kituko cha mwaka kushinikiza kumjua Baba yake mzazi.

Alitoweka shuleni bila ruhusa na kurejea nyumbani. Babu yake aliwaka akawa mkali kama pilipili mpaka anamtishia kumshushia kipigo kama asiporejea shuleni, lakini wapi hakuweza kufua dafu. Babu, Bibi na Mama yake mzazi walikuwa tumbo joto, wakijua pepo lililomtoa shuleni Catherine na kumkatiza masomo linataka kujirudia upya kwa mjukuu wao Asante-Rabbi, jambo ambalo waliapa kuwa hawatokubali wapo tayari wakeshe kwa maombi, kunuti na funga ili mradi pepo huyo amtoke mjukuu wao.

Licha ya juhudi zote za kumrai kuwa akamalize shule kwanza ndio wajadili jambo hilo kutokana na unyeti wake lakini wapi, walitoka kapa, Asante Rabbi aliwawekea kigingi, jibu lake lilikuwa ni moja tu, tena kwa kimombo "No Father-No School". Ndipo mama mtu akatwishwa mzigo wa kumpasulia ukweli mtoto wake.

Ndio siku miongoni mwa siku, usiku wa manane Catherine aligonga mlango wa ghulamu wake na kumualika kuwa ana mazungumzo ya faragha na yeye.
Wakaketi sebuleni wawili tu wakiwa na lepelepe la usingizi hamna mtu yoyote anayewashuhudia zaidi ya Mungu na Malaika wake. Fikra za Catherine zikarejea nyuma zaidi ya miaka 18 iliyopita akikumbukia hatua mpaka hatua kuanzia jinsi alivyopata mimba ya mziwanda wake Asante-Rabbi mpaka kujifungua kwake. Alikuwa hajasahau kipengere hata kimoja katika matukio hayo.

Alianza kukumbukia peke yake mawazoni mwake kuwa baba yake Asante-Rabbi, Ngwenyama alikuwa ni Shamba-Boi wao wa kazi za nje aliyetokea nchini Malawi kuja kutafuta kazi za nyumbani Jijini Dar es Salaam. Alikuwa ni kijana mtiifu, mwenye kujituma na mchapa kazi, hali iliyomfanya apendwe na kila mwana familia ya Meja Mushi. Kingine cha ziada alikuwa ni umbile lenye mvuto, ukichanganya na kazi zake za shuruba zikamfanya awe na umbo la kuvutia la kiuanamichezo.

Pia alikuwa ni mcheshi sana mwenye kupenda utani na kila mtu katika nyumba ile. Sasa Catherine alipomaliza shule mwaka 1969 akiwa nyumbani anasubiria matokeo ya kidato cha nne, ndipo majaribu ya Ibilisi yalipoanza. Alijikuta ghafla tu anampenda Ngwenyama toka moyoni. Na kwa kuwa alikuwa ni mtoto wa getikali hamna kuzurura ovyo kama mbwa koko wa uswahilini hivyo mwanaume wa maana kwake aliyemzoea machoni mwake ni Ngwenyama.

Kila dalili alizozionyesha kwa Ngwenyama kuonyesha amekufa na kuoza kimapenzi juu yake, hazikufua dafu. Akabakia anateketea moyoni kwa moto mkali wa huba. Mila za Kiafrika zilikuwa haziruhusu msichana kumtakia mvulana kuwa anampenda minghaili wazungu wao kwao ni kitu cha kawaida tu mtu kuelezea hisia zake.

Fursa ya pekee aliyokuwa anaisubiria Catherine ikajitokeza, baba yake Meja Mushi na mkewe walipata safari ya ghafla kuelekea Rombo-Moshi. Kulikuwa na msiba umetokea Kijijini hivyo walipaswa kwenda kuzika. Mzee Mushi akawausia waishi vizuri ndani ya hizo siku tatu, kuanzia Ijumaa mpaka jumatatu watakaporejea safarini.

Sasa nyumba ikabakia watu watatu, dada wa kazi, Catherine na Ngwanyama. Ijumaa ile ikapita salama mpaka Jumamosi. Tatizo lilikuwa kwa Catherine hawezi kumuambia hisia zake asije akaonekana yeye ni ghashi wa mahonyo. Siku ya Jumapili ndipo mpango wa Ibilisi kuwadondoshea Catherine na Ngwanyama katika dhambi ya zinaa ukatimu.

Ilikuwa ni kawaida ya Catherine kila ifikapo siku ya Jumapili kwenda kusali kanisani misa ya kwanza. Hivyo alikuwa anaondoka saa 12:30 shapu kuelekea kanisani, atakaa huko na kurejea nyumbani saa 3 asubuhi. Ratiba ya kazi ya Ngwanyama siku ya Jumapili ilikuwa ni kusafisha madirisha ya nyumba nzima.

Hivyo alipenda kuanza na madirisha ya chumba cha Catherine ili akirudi kanisani awe huru kujimwayamwaya kutumia chumba chake bila usumbufu. Lakini kumbe siku hiyo Catherine alichelewa kuamka hivyo akapanga aingie kanisani misa ya pili.

Hivyo wakati anaoga bafuni Ngwenyama yupo dirishani anafuta vumbi la madirisha habari hana. Hamadi weeh Ghafla bin Vuu, Catherine akawa anatoka kuoga akiwa amevaa kanga moja tu nyepesi ya Mombasa huku imemnatia mwilini na kulichora vilivyo umbile lake lenye mvuto wa aina yake.

Alikuwa ana umbo lenye kumtetemesha kiimani hata yule Mchamungu mwenye vilemba saba kichwani kama tu atakubali pepesi na tashwishi ya macho yake kushuhudia maajabu ya uumbaji wa Mwenyezi Mungu.

Catherine alikuwa hana hili wala lile amejitawala chumbani mwake, anajikausha maji mwilini sasa akiwa mtupu kama alivyozaliwa akiwa amelipa mgongo dirisha analosafisha Shamba-Boi wao huku akitikisa makalio yake yenye umbile la kifuu cha nazi kimadoido.

Ngwenyama alibaki mdomo wazi huku ameganda pale dirishani kama amenaswa na umeme. Macho yake aliyakodoa upeo wa mwisho wa kuyakodoa bila kufumba macho asije akapoteza fursa hiyo adhimu na ya bure ya kutalii mwili wa mtoto wa Kibosile wake, Catherine.
ITAENDELEA

Sent from my TECNO CC6 using JamiiForums mobile app
 
RIWAYA- HUJUMA NZITO-PART 26

Catherine alikuwa hana hili wala lile amejitawala chumbani mwake, anajikausha maji mwilini sasa akiwa mtupu kama alivyozaliwa akiwa amelipa mgongo dirisha analosafisha Shamba-Boi wao huku akitikisa makalio yake yenye umbile la kifuu cha nazi kimadoido.

Ngwenyama alibaki mdomo wazi huku ameganda pale dirishani kama amenaswa na umeme. Macho yake aliyakodoa upeo wa mwisho wa kuyakodoa bila kufumba macho asije akapoteza fursa hiyo adhimu na ya bure ya kutalii mwili wa mtoto wa Kibosile wake, Catherine.

Alipomaliza kujikausha maji mwilini, akiwa bado hajavaa libasi yoyote ile kugeuka tu wakakutanisha macho yao ana kwa ana na Ngwenyama. Catherine akapatwa na mshtuko na kupiga kelele za uoga hakutegemea tukio kama hilo la kupigwa chabo dirishani.

Haraka haraka akakimbilia mahali ilipo kanga yake na kujifunga mwilini. Lakini alipogeuka bado akamkuta amenasa pale dirishani kama ndege aliyenasa kwenye ulimbo anamsubiria mtegaji wake aje kumnasua.

"Ngwenyama wewee...! Ngwenyama wewe...! Mbona una tabia za kishenzi, kishamba na mbovu za kuchunguliana madirishani. Akija mama nakusemea mwanahizaya mkubwa wewe, akufukuze kazi" alilalama Catherine kwa hasira.

Sauti hiyo ndio ikamzindua toka kwenye mfadhaiko huo hakujibu kitu chochote na moja kwa moja akatupa chini kitambaa cha kusafisha madirisha na kuondoka zake kurejea chumbani mwake.

Catherine safari ya kanisani ikaota mbawa alikuwa anaona aibu sura yake ataitundika wapi akikutana nae uso kwa uso. Ilipofika majira ya adhuhuri wakati wa mlo wa mchana, Catherine akamuuliza dada wa kazi kama Ngwenyama ametoka siku ya leo. Jibu lilikuwa ni kuwa toka asubuhi hajatoka na hata chai hajanywa anasema ameshiba.

Catherine moyo wa huruma ukamtembelea na kuanza kujilaumu kwa nini hata alimtolea lugha ya kebehi na matusi kiasi kile. Huenda amekasirishwa na lugha nilizomtolea hasa ikichukuliwa alikuwa anampenda sana.

Majira ya Alasiri ikabidi Catherine akimbilie dukani akanunua kadi za mapenzi kuomba msamaha huku akichora makopakopa mengi kuonyesha anampenda. Akaenda kuitumbukiza chini ya mlango wa chumba cha Ngwenyama.

Lakini mbinu hiyo haikusaidia kitu mpaka wakati wa usiku wakiwa wanapata mlo wa chajio kwa ajili ya kujiandaa kulala bado kijana wa watu alikuwa hajatoka chumbani mwake. Catherine tayari alishapanda kitandani akiwa amevalia nguo yake nyepesi ya kulalia, lakini usingizi ulipaa kabisa.

Alikuwa anamuwaza Ngwenyama. Akajikuta uzalendo unamshinda anasimama toka kitandani mwake na kufungua mlango wa nyumba kubwa kimya kimya ili dada wa kazi asishtukie dili. Akaenda mpaka chumbani kwa kwake na kugonga mlango. Aligonga sana mpaka akakaribia kukata tamaa ndio akafunguliwa.

Akaingia chumbani mule huku ameinamisha macho chini kwa aibu. Ngwenyama alikuwa amevaa bukta fupi nyeupe na singlendi nyeupe yupo pekupeku. "Unataka nini?, sema shida yako, nataka kulala" aliongea kwa hasira bila kujua anazidi kuziumiza hisia za Catherine.

"Nimekuja kukuomba msamaha, kwa maneno makali yasiyo na adabu za ukumbi niliyokuropokea asubuhi. Nisamehe kwa kuumiza hisia zako, nakupenda sana sipendi kukuona ukiteseka mpaka unasusa kula kwa ajili yangu!" aliongea Catherine huku mashavu yake yakiwa yamelowana kwa mvua ya machozi iliyokuwa inanyesha kutokea machoni mwake.

Hakuna mkate mgumu mbele ya chai ya mkandaa, kijana wa watu alishalegea. Sasa ilikuwa ni muda wa kupindua meza kibabe, matusi na kebehi za asubuhi aliyotukanwa na Catherine ilikuwa ni wakati wa kuizungumzia kesi hiyo, kwenye mahakama ya samadari ya fundi seremala. Kwa jinsi umbile la Catherine lilivyojichora kwenye vazi lile la kulalia, Ngwenyama akajikuta anamvamia Catherine na kumtupa kwenye kizimba cha mahakama tayari kwa kuanza kesi.
Kilichofuatia hapo ikawa ni historia tena, kesi ilihukumiwa usiku kucha.

Kulipopambazuka Catherine aliwahi kurejea chumbani kwake kabla hata dada wa kazi hajaamka bado.
Majira ya Alasiri wazazi wa Catherine wakawa wamerudi tayari. Ngwenyama na Catherine ikawa ndio mwanzo na mwisho wao wa kukutana kimwili, huku Catherine akiwa ndio kavunjwa kizinda chake na Ngwenyama kwa mara ya kwanza tokea aingie duniani.

Baada ya wiki moja tu kupita akaanza kujihisi hali isiyo ya kawaida. Kichefuchefu, kizunguzungu na hata kutapika wakati mwingine. Akaanza kuogopa kuwa huenda amenasa mimba lakini mawazo hayo nilikuwa anayafukuza na kuyalaani kichwani mwake kwa nguvu zote. Mama yake hakufanikiwa kumgundua mpaka alipoenda kubambwa shuleni kuwa ni mjamzito.

Kumbukizi ilipofika hapo pa kufukuzwa shule akaanza kulia kwa kwikwi Catherine, hasa akifikiria kama angesoma huenda angekuwa mtu mkubwa sana serikalini au hata kuwa mtu muhimu katika jamii ya Watanzania. "Mamaaaa....Mamaaa...una nini? Mbona umeniamsha huniambii kitu halafu unaanza kulia tu!" Asante-Rabbi alimgutusha mama yake kutoka kwenye lindi la mawazo.

"Nisamehe mwanangu kwa kukuficha miaka mingi sana, Baba yako ni Mnyasa wa Malawi anaitwa Ngwenyama. Tunamfahamu kwa jina moja tu hilo hilo na hata sifahamu yupo wapi. Alikuwa ni mfanyakazi wetu hapa nyumbani!" Catherine alijikaza kisabuni akafuta machozi akamwaga upupu wa maneno kwa Asante-Rabbi ajiwashe mwenyewe.

Asante-Rabbi akaendelea kumdodosa mama yake kwa maswali lukuki mpaka akajiridhisha. Kulipokucha akarejea zake shuleni huku akiweka nia ya kumsaka baba yake pindi atakapopata fursa.
Alipomaliza kidato cha nne kama kawaida yake akawa kinara tena kwenye matokeo ya kitaifa. Furaha yake Babu yake akaamua kuvunja kibubu chake cha mafao kumpeleka nchini Uingereza kwa masomo ya kidato cha tano na sita mpaka Chuo Kikuu.

Huko nchini Uingereza ndiko alipokutana na Dr.Pius Chilembwa wote wakiwa wanasoma Chuo Kikuu kimoja. Asante-Rabbi alipofahamu Dr.Pius Chilembwa naye ni Mnyasa kama yeye alivyo akajiona ni zaidi ya ndugu kwake. Ndipo Kapteni Wandawanda baba mlezi wa Dr.Pius alipozidi kuwaunganisha na kuwapa fikra zake hadi za kulifuta jina la Tanzania na kuisimamisha Dola ya Nyasa kupitia sanduku la kura ili kukwepa vikwazo vya Umoja wa Afrika "AU" kama wangefanya mapinduzi ya kutumia silaha.

Hivyo akawapa kazi ya kuketi pamoja na kubuni kwa kutumia elimu zao, waje na mpango mkakati wa kupata pesa za kuendesha harakati hizo za kuisimamisha Dola ya Nyasa "Nyasa Empire". Wakati Wanachuo wenzao wanaosoma nao Uingereza toka nchini Tanzania, kwenye muda wao wa ziada walikuwa wanautumia kwenye starehe na kutalii nchi mbalimbali za Ulaya ili wapate picha na simulizi za kuja kuringishia wenzao wakirejea nyumbani, wao Asante-Rabbi na Dr. Pius Chilembwa walikuwa wanajifungia ndani, wakisugua bongo zao, wanapanga mikakati ya kuichukua nchi pindi wakimaliza masomo yao.

Waliporejea nchini, Asante-Rabbi akaajiriwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kama Mhadhiri katika idara ya Uhandisi wa Kompyuta huku Dr Pius Chilembwa akirejea Benki Kuu kama Mchumi Mwanadamizi. Mpango wao ulipokamilika kwa ajili ya utekelezaji, Asante-Rabbi akaacha kazi ghafla akiwa tayari ni Profesa na kwenda kujichimbia nchini Afrika ya Kusini. Huko akawa anakula pensheni yake tu huku akisubiria mpango wa kusimamisha Ufalme wa asili ya Baba yake na Babu zake usimame Tanzania.

Ufalme ambao utawapa Wanyasa wote kutembea kifua mbele na hadhi yao kuwa juu sio hadhi ya kufanya kazi za nyumbani tena.
Baada ya miaka mitano tokea kuacha kazi kwa Profesa Asante-Rabbi kupita, ndipo nae Dr Pius Chilembwa akaandaa igizo la kifo chake nchini Afrika ya Kusini. Sasa Kachero Manu ndio alipata fursa ya kwenda kuonana na Profesa Asante Rabbi ambaye sasa anaitwa Professor Potchefstroom.

ITAENDELEA



Sent from my TECNO CC6 using JamiiForums mobile app
 
Back
Top Bottom