Follow along with the video below to see how to install our site as a web app on your home screen.
Note: This feature may not be available in some browsers.
Inasimutisha tu jinsi mjinga alivyojinadi kuwa ikiwa sio mniue!!! Anaenda kufa kweli yule taahira kwa usaliti wake hahahaaMako amekula msosi kashiba, kapunguza usingizi kidogo kahepa hahahaha
AsanteeeeMfalme Anataka Kuniua
Sehemu ya 14
“Nilimkosea sana Mako kwa kutaka kumuuza kwa tamaa ya ng’ombe!” alisema Oma akishirikiana na mwanae kusafisha nyumba iliyokamilika kujengwa baada ya lile tukio la kuchomwa moto.
“Kwa nini mashetani yameamua kukusaidia, au kwa sababu ulitenda dhambi hivyo yamependezwa na wewe?” aliuliza mtoto Baka ambaye ilibaki miezi miwili atimize miaka kumi na mbili.
“Siamini kama ni mashetani, Mako ni mtu mwenye maarifa mengi… kuna namna!”
“Baba… Mako anawezaje kukusaidia wakati ulitaka kumsababishia kifo?”
“Mako ni mtu mwema sana, ni rafiki yangu wa muda mrefu, namfahamu vizuri. Yeye huweza kusaidia hata watu asiowafahamu. Hivi nimewahi kukusimulia mkasa wake alioufanya katika mji mmoja uliochangamka?”
“Hapana… kama hatutachukua muda, nisimulie,” alijibu Baka akikaa chini kutokana na machovu ya kazi ya siku hiyo. Oma naye akakaa chini na kuanza kusimulia.
“Zaidi ya watoto elfu moja wametekwa na majambazi ambao wamedai hawawezi kuwaachilia mpaka wapewe kiasi cha Shilingi Trilioni saba…” ilisikika taarifa ya habari katika redio ndogo aliyokuwa akisikiliza Bwana Mako mchana saa sita. Mako huishi mjini na kijijini, nchi kavu na majini, na mara chache angani. Leo alikuwa mjini alipopokea taarifa hiyo.
“Juhudi za kuwaokoa zimegonga mwamba,” iliendelea taarifa, “watekaji wametishia kuwaua watoto wote endapo hawatalipwa fedha wanazotaka ndani ya dakika 30. Pia wametaja mfumo wa malipo hayo ufanyike kwa njia ya mtandao na malipo yawe katika Bitcoin.”
Bwana Mako alitambua kuwa siku hiyo kulikuwa na sherehe iliyohusisha watoto wa viongozi na wafanyabiashara wakubwa nchini kwake. Watoto hao wa wakubwa, walikutana pamoja katika sherehe iliyohusisha michezo mingi ikiwemo kuogelea. Bwana Mako hakupenda sherehe za aina hizi kwa sababu kwake yeye hazikuwa na maana yoyote zaidi ya ubaguzi tu, kwani watoto wa hohehahe hawakupata nafasi ya kuwa hapo. Hata hivyo, japo hakukubaliana na sherehe hizo, kitendo cha watoto wasio na hatia kutekwa hakikumfurahisha hata kidogo, alitambua kuwa watoto wale hawakuwa na kosa.
Kwa haraka aliingia katika chumba maalumu, humo alitoka na bunduki aina ya Colt M4 Commando akaipachika ndani ya mfuko wa koti kubwa alilovaa siku hiyo kisha akaelekea eneo la tukio. Bwana Mako hutumia bunduki ya aina hii akiwa na hasira sana.
Bwana Mako aliendesha pikipiki mpaka katika jengo moja refu, akapanda mpaka juu ya jengo hilo kisha akachukua darubini yake ili aweze kuwaona watekaji.
Alifanikiwa kuona wanaume watatu wa kizungu wakiwa wameshika vyema bunduki zao aina ya AK 47. Watekaji hao walikuwa wametawanyika na kutengeneza umbo la pembe tatu, watoto waliwekwa katikati na hakuna aliyeruhusiwa kujitikisa. Alishuka haraka katika jengo na kuanza kuelekea walipo watekaji wale. Njiani aliendelea kutunga njia za kuwamaliza.
Pikipiki aliiacha mbali kidogo kwani sauti yake ingewashtua watekaji na pengine kuhisi wanafuatiliwa hivyo kuwaua mateka wao. Alipofika hatua chache kuelekea eneo la tukio aliona kamba za njano zimezungushwa nazo zimeandikwa, ‘usivuke hapa.’ Kumbe watekaji wale walizungusha uzio ili watu wasiohusika wasivuke msitari huo na labda ndiyo sababu hapakuwa na askari yeyote karibu. Inaonekana watekaji walitumia mbinu hii ili iwe rahisi kwao kurotoka pindi watakapopewa fedha walizotaka.
Bwana Mako aliangaza kila kona ili kujiridhisha kuwa hakuna mtu aliyemuona, haikuchukua muda, aligundua uwepo wa askari wengi waliojificha pembezoni pengine nao walipanga mipango ya kuokoa watoto wale. Pia alitambua uwepo wa kamera ndani ya jengo walilotekwa watoto ambapo watekaji walikuwa wakiona yote yanayotendeka nje na endapo wangeona juhudi zozote za kutaka kuokoa watoto bila fedha, watoto wangekuwa hatarini. Wakati haya yanatendeka, zilibaki dakika 10 zile dakika 30 zilizotolewa na watekaji ziishe!
Bwana Mako hakuwajali askari waliokuwa pembeni, akatambaa kama nyoka mpaka alipoufikia ukuta wa jengo. Akiwa hapo akaukwea ukuta mithili ya mjusi mpaka akawa juu ya jengo. Jengo hili upande wa juu lipo wazi hivyo Bwana Mako akawaona watekaji wote, wakati anawaona watekaji, askari waliokuwa nje nao walimuona wasijue mtu yule katoka wapi.
Kitu kipya alichogundua ni kwamba, watekaji hawakuwa watatu, bali walikuwa wanne, mmoja alikuwa katika kona akiwa na kompyuta ndogo, bila shaka alikuwa akikagua kama fedha walizodai zililipwa au la.
Bwana Mako alitunga upya sheria zake kwani alizotunga awali zililenga kupambana na watu watatu, kumbe sasa wapo wanne. Alipomaliza mpango wake akaanza kazi.
Alilenga shabaha kwa wale watu watatu, waliosimama na silaha, akampiga mmoja, wakati wawili wakitafuta adui alipo, alimdungua mwingine kisha akammalizia yule wa tatu. Bwana Mako alikuwa na uwezo wa kummaliza yule jamaa wa nne aliyekuwa na kompyuta ndogo, lakini aliamua kuwapa burudani watoto.
Aliruka kutoka juu, akatua ndani ya jengo. Yule mtekaji aliyekuwa kashughulika na kompyuta akawa anakimbia kwenda kuchukua moja ya bunduki zilizokuwa zimeshikiliwa na wale watekaji wenzake. Alichelewa, Bwana Mako alimkanyaga teke akadondoka.
Mtekaji yule aliinuka, akakunja ngumi ili apambane, Bwana Mako akawageukia watoto akawaambia, “Watoto, nimekuja kuwaokoa, watekaji wote nimewamaliza isipokuwa huyu mmoja. Sasa nawaomba mnishangilie kwa nguvu ili niweze kumshinda huyu adui, akinipiga ngumi zomeeni, nikimpiga shangilieni mkilitaja jina langu, Maaako… Maaako… Maaako… halafu ili kutunza kumbukumbu, washeni simu zenu muweze kuchukua video za tukio hili!”
Bwana Mako alikuwa na uwezo wa kummaliza adui yule kwa sekunde moja tu, lakini alitaka kuwaburudisha watoto, Bwana Mako wakati mwingine hupenda sifa. Basi Mtekaji akarusha ngumi, Ikampata Bwana Mako watoto wakazomea. Bwana Mako akarusha ngumi, ikampata mtekaji watoto wakashangilia, ikawa ni kurusha ngumi na kujibu mpaka Bwana Mako alipoamua kuhitimisha burudani, aliruka juu kama mwewe akiwa amenyoosha vidole vyake kama panga, alipotua akampiga dhoruba moja mtekaji ambaye aliitikia kwa kudondoka chini akiwa amepoteza fahamu, kisha Bwana Mako kwa kutaka sifa zaidi akalia kwa sauti kubwa akipiga kifua chake, “Hiyaaaaaaaaaa!” watoto walijua kumfurahisha Bwana Mako, wakashangilia, “Maaako…. Maaakooo…. Maaakooo.”
“Watoto…” aliita Bwana Mako akivaa vyema koti lake Jeusi, “Nimekuja kuwaokoa na tayari adui zenu wamekwisha lala chini. Mimi narudi nyumbani, siwezi kubaki hapa kwa sababu askari wakija wataninyang’anya bunduki yangu nami naipenda sana. Wakikuulizeni nani kawaokoa, waambieni ni Bwana Mako, waonesheni video zangu mlizorekodi.”
Alipomaliza kusema hayo, watoto wakamzunguka kila mmoja akitaka kumshika mkono wa kwa heri, wakati zoezi hilo likiendelea, geti la kuingilia likavunjwa, askari wengi wakaingia wakiwa na silaha, watoto wakamtazama Bwana Mako kwa hofu, wakihofia kuwa sasa atanyang’anywa siraha yake anayoipenda, lakini hawakumuona… Bwana Mako alikwisha ondoka eneo hilo na bila shaka alikuwa nyumbani kwake!”
Oma alimaliza kusimulia mkasa wa Mako, akamhamasisha Baka wakamilishe kazi haraka ili majukumu mengine yafanyike kesho.
Baka alibaki kaduwaa, akitafakari kama mkasa aliosimuliwa ni kweli au kamba za baba yake!
Inaendelea Kesho...
Wish ziwe zinakuja 10Mfalme Anataka Kuniua
Sehemu ya 15
Mako aliamua kulichunguza pango lote. Kila alipozidi kusonga mbele giza lilitanda hivyo alizidi kuziwasha zile taa zilizosimama juu ya kuta. Alitembea mwendo wa kilomita nne, akakutana na njia mbili. Akapiga hesabu na kuamua kuifuata iliyoelekea kushoto, ile ya kulia angeichunguza siku nyingine.
Aliendelea kutembea kama umbali wa kilomita tatu hivi, urefu wa pango ukazidi kupungua hata akawa akinyoosha mkono wake, anagusa juu na hapo ndipo akauona mwisho wa njia ile na ndiyo ulikuwa mwisho wa pango. Alisogea akaushika ukuta mgumu wa jiwe akistaajabu. Alipotazama juu ya ukingo wa mwisho, aliona pedali ndogo iliyotosha kushikwa kwa mkono. Aliikamata pedali ile, akaizungusha taratibu, upande wa juu wa pango ukaanza kufunguka na kumfanya Mako awe kama anayefungua mlango wa handaki. Aliendelea kuzungusha pedali mpaka upande wa juu ukafunguka katika duara iliyolingana na mdomo wa pipa.
Akitumia mikono, alijivuta nje. Akawa nusunusu, kichwa na kifua viko nje, tumbo na miguu vimo pangoni. Macho yake madogo yakawaona wafungwa wa gereza la Kanakantale wakioga kwa furaha. Haraka akarudi pangoni na kunyonga ile pedali, mlango wa juu ukajifunga.
Sasa alibaini kuwa, mwisho wa pango lile kwa kufuata njia ya kushoto ulikuwa mlango wa kuingia gereza la Kanakantale! Alijipumzisha kidogo kisha akarudi katika sehemu yake, kule alikoweka mikanda ya nyama, kule ambako aliweza kuchungulia na kuwaona askari wakirandaranda kumtafuta.
Siku iliyofuata aliamua kuichunguza njia iliyoelekea kulia. Aliifuata kwa mwendo wa kilomita nne, ukawa mwisho wa pango katika mazingira yanayofanana na ule mwisho wa njia ya kushoto. Kama kawaida, huko nako kulikuwa na pedali ndogo iliyotosha kuenea mkononi, aliizungusha, pango likafunguka upande wa juu. Alichungulia, akauona uwanja mkubwa katika ikulu ya Kanakantale, ni katika uwanja huu, mfalme hufanya mikutano na askari wake.
Akiendelea kutazama mpaka macho yake madogo yalipogongana na macho makubwa ya askari. Haraka kama sisimizi, akarudisha kichwa pangoni na kuanza kuzungusha ile pedali. Askari aliyeshtuka, alisogea sehemu ile, kadri alivyozidi kusogea, aliona ardhi ikijifunga na mwisho hapakuwa na yule mtu aliyechungulia wala shimo. Askari mtiifu alikaa mahali pale mwenye mawazo. Alitafakari kama alichokiona kilikuwa kweli au uongo. Mwisho aliamua kuamini kuwa, zilikuwa ndoto za mchana. Hakuondoka mahali pale, aliendelea kuzungukazunguka kwa muda mrefu mpaka alipojiridhisha hakukuwa na kitu.
Mako alizama pangoni mwenye hofu juu ya kuonekana kwake. Alihofia nini kingetokea kama wangeamua kuchimba, mwisho aliamua kuendelea na shughuli zake. Mwenye hofu, lakini anayejiamini.
Basi alibaini kuwa, ile njia ya kushoto inaelekea gerezani, na ile ya kulia inaelekea kwa mfalme.
***
Kivuli cheusi kilionekana kikitoka katika shimo usiku wa manane. Kivuli hicho kilitambaa kama nyoka mpaka kandokando ya ukuta, kisha kwa mwendo wa kuficha umbo, kilijisogeza taratibu kikiwapita walinzi ambao hata hivyo walisinzia.
“Sipe… Sipe… Sipe…” kivuli kiliita kwa kunong’ona. Sipe mwenye hofu, alilala peke yake katika chumba kile cha jela, wenzake Sasi na Athu, walinyongwa siku tatu zilizopita.
“Nani wewe?” alihoji Sipe akiwa katikati ya usingizi na kuamka.
“Mimi Mako, sogea tuzungumze.”
“Mako…!” alijibu Sipe akisogea karibu, “Kulikoni ndugu yangu, ni ndoto au kweli?”
“Usiwe na hofu, utafahamu mengi ukiwa na subira. Pokea ujumbe wangu, kesho wakati wa kuoga, kaa pembeni upande wa kulia bila kukaribiana sana na watu, utasikia sauti ikikuita mara tatu, ukisikia hivyo, tazama upande wa kulia, utaniona nachungulia kichwa na mwili mwingine ukiwa shimoni, haraka sogea na ingia katika shimo.”
Baada ya kumaliza mazungumzo, Mako alitambaa kuelekea alikotoka, aliufikia mdomo wa shimo na kuingia ndani kama mchwa. Kisha akanyonga pedali kuifunga himaya yake.
Mfalme Anataka Kuniua
“Juhudi za kuwaokoa zimegonga mwamba,” iliendelea taarifa, “watekaji wametishia kuwaua watoto wote endapo hawatalipwa fedha wanazotaka ndani ya dakika 30. Pia wametaja mfumo wa malipo hayo ufanyike kwa njia ya mtandao na malipo yawe katika Bitcoin.”
Najaribu sana kutafakari setting ya hii hadithi,
mazingira yake ni ya kizamani enzi za utawala wa kifalme au ya kisasa enzi hizi za bitcoin?
[emoji848]
Leo fupiiiiiii hila saaafiMfalme Anataka Kuniua
Sehemu ya 16
Wafungwa walionekana kuyafurahia maji, walioga kwa furaha kwani hiyo ndiyo ilikuwa nafasi pekee ya kuwa nje katika kipindi cha siku nzima. Sipe alijitenga na wenzake kama alivyoelezwa.
“Sipe… Sipe… Sipe,” ilisikika sauti ikimuita, haraka akaanza kutembea kuelekea upande ule wa kulia.
“Sipe… Simama!” askari aliamrisha, kile kichwa chenye macho madogo na nywele za kipilipili kilichokuwa kikichungulia kumsubiri Sipe afike, kikazama ndani.
“Kwa nini hujaoga? Na huku unakwenda wapi? Unataka kutoroka siyo?” askari aliuliza maswali mfululizo.
“Hapana afande, leo sijisikii vizuri, nahisi kuumwa,” alidanganya.
“Macho yako yanaonesha unadanganya,” askari alifoka akiyatazama macho ya Sipe. Sipe wasiwasi ukamjaa, ule uhuru aliokuwa anakwenda kuupata, akaona akiukosa. “Sasa sikia, tunakwenda zahanati sasa hivi kuchukua vipimo, ole wako ukutwe huna ugonjwa,” aliongeza askari kwa sauti ya kufoka.
Sipe hakuwa na ujanja, alikamatwa mkono na askari yule ambaye alianza kumkokota kama mkokoteni kumpeleka zahanati. Lakini ghafla kabla hawajatembea hatua nyingi, alitokea askari mwingine na kumtaka askari aliyekuwa na Sipe afike haraka mapokezi kuna mgeni wake.
“Sipe, rudi eneo la usafi, kesho tutakwenda kufanya vipimo, ole wako. Askari hadanganywi bwana mdogo. Hili ni gereza, siyo jumba la wanafalsafa.”
Sipe alirudi asiyeamini, akapeana mgongo na askari wale, alitembea bila kugeuka nyuma na aliahidi yeyote ambaye angemuita asingemuitikia. Alitembea kwa mwendo wa kunyakua harakaharaka, mpaka alipokuwa Mako, alifika eneo hilo lakini hapakuwa na shimo!
Alisimama kwa muda wa dakika mbili mpaka alipopata hofu ya kuhofiwa na askari, alijitenga mbali kiasi na wenzake waliokuwa wanaoga. Mwenye simanzi, akageuka na kuanza kurejea.
“Sipe… Sipe… Sipe,” Mako aliita mara baada ya kuufungua mlango wa pango.
Sipe aligeuka, akakiona kichwa cha Mako kikimtazama, wote wawili wakatabasamu, haraka akatembea na kuingia ndani ya shimo, miguu ikitangulia, na kichwa kikimaliza.
Usiku wa siku hiyo, iligundulika kutoweka kwa mfungwa mwingine katika gereza la Kanakantale. Zawadi ya ng’ombe elfu moja iliahidiwa kwa yeyote ambaye angefanikisha kukamatwa kwa Sipe. Nchi ikawa katika msako wa kuwatafuta wafungwa wawili waliotoroka gerezani.
Inaendelea Kesho...