Riwaya ya kipelelezi: Wakala wa Siri

Riwaya ya kipelelezi: Wakala wa Siri

WAKALA WA SIRI Season 02 (Episode 5)
Mtunzi; Robert Heriel
WhatsApp 0693322300
Episoed 05


Sajenti baada ya kula chakula, akaagiza Bia ili achambe koo lake, mhudumu akamletea, kisha akabugia fumba mbili na kujaza mdomo wake kisha akameza akiwa amefumba macho akiisikilizia ladha ya bia “ Muda mrefu sana sijachamba koo na vitu kama hivi, acha leo nijifurahishe, maisha yangu yamekuwa ya misukosuko, nimejitoa kwa ajili ya wengine, nimepigana kufa na kupona kwa ajili ya kuilinda nchi yangu, kila kitu nilichofanya ni kwaajili ya kuwapa watu wa nchi hii amani na utulivu; wakati nikiwapa amani mimi sikuwa na amani, tena niliipoteza, wakati nilipopigania utulivu wao, utulivu wangu ulikuwa mashakani. Sina mtoto, sina mke, kumbukumbu hii siipendi, natamani nami ningekuwa na familia kama wenzangu, niwe na mke wakuniita mume, niwe na watoto wakuniita Baba” Sajenti akawaza akiwa yupo Bar, akameza kwa mkupuo kudukudukudu! Mpaka chupa ilipoisha bia, akaiweka chupa kwenye meza alafu akashusha pumzi nzito mithili ya bata dume. Akafungua bia nyingine kwa kutumia meno, hii ikaimimina nusu kwenye Bilauri ndefu iliyokuwa juu ya meza. Kisha akachukua bilauri na kubugia fumba dogo la bia. Akaendelea kuwaza;

“ Ningeweza kupata mwanamke mzuri wa kumuoa, tena angeishi maisha mazuri kutokana na kipato changu walau kinakidhi, lakini roho yangu inasita, roho yangu inakataa kabisa kumuingiza mtoto wa watu kwenye matatizo; Kazi hii lolote huweza kutokea muda wowote, kazi hii ni kama ifananayo na biashara ya kuuza roho na kuanza kuidalalia, sio kwamba naiponda, wala! Naipenda kazi hii na ndio maana naifanya kwa moyo wote. Sikuwa tayari kuiweka familia nitakayoianzisha kwenye kitanzi…” Sajenti akawazaa lakini ghafla akakatishwa na mlio wa simu yake iliyokuwa ikiita. Akapokea na kuweka simu sikioni.

“ Anhaa! Mmeshamaliza! Vizuri! Subiri nakuja sasa hivi” Sajenti akasema, kisha akakata simu.

“ Mhudumu! Wewe Mhudumu!” Sajenti akaita, kisha mhudumu akawa amefika mbele yake.

“ Niwekee hizi bia zilizobakia kwenye mfuko, naondoka nazo sasa hivi” Sajenti akasema, mhudumu akaenda kuchukua mfuko; kitambo kidogo akarejea akiwa na mfuko, akaziweka zile chupa za bia ndani ya mfuko, kisha akamkabidhi Sajenti.

“ Ahsante sana, pesa yako hiyo hapo kwenye meza” Sajenti akasema huku akianza kupiga hatua kuondoka.

“ Wewe kaka! Wewe kaka subiri chenchi yako” Yule mhudumu akasema, Sajenti akageuka akiwa bado anatembea kuukabili mlango wa kutokea, akamuonyeshea ishara yule mhudumu aichukue ile chenchi ni zawadi yake. Yule mhudumu akaachia tabasamu kama ahsante, sajenti akaondoka.

Kutoka katika ile Bar na nyumbani kwa Sajenti hapakuwa mbali sana, ilikuwa kama kilimeta moja hivi. Hivyo haikumchukua muda mrefu kufika. Sajenti alipofika nyumbani kwake akakuta mazingira yakiwa yamebadilika kwa kiasi kikubwa. Ni kama aliingia sehemu ngeni ambayo hajawahi kufika. Kazi kubwa iliyofanywa na Kampuni ile ya usafi ilimridhisha. Alizunguka mazingira yote ya nje na kukuta kile kitu kimewekwa vizuri na kupendeza.

“ Hawa watu kazi wanaijua, sikutegemea kama wangepafanya kuwa hivi” Sajenti akawaza huku akiongozwa na kiongozi wa watu wale waliokuja kufanya usafi. Sajenti akaingia ndani, huku ndiko macho yake yakashindwa kushangaa, kwanza alipokelewa na hurufu nzuri tofauti na ile ya kwanza ambayo ilikuwa na uvundo wa vumbi, Sebule ilikuwa ipangwa ikapangika, ilikuwa imesafishwa haswa; Sajenti akarizishwa na mazingira ya nyumba yake, akawalipa stahiki zao wale watu wa usafi wakaondoka.

************************************

“ Habari za leo Mr. Seba, nipo SHDC hapa, nimemuona Sajenti Warioba humu ndani, sawa! Haina shida” Akakata simu. Yule mzee mwenye Mvi baada ya kumjulisha Mr. Seba uwepo wa Sajenti Warioba Jijini Dar es salaam, akaachiwa maagizo amfuatilie. Yule Mzee mwenye Mvi akatoka kwenye ule ukumbi SHDC 400 akasonga moja kwa moja kwa Belinda.

“ Karibu Mzee Lawi, Bila shaka ushakamilisha” Belinda akasema akiachia tabasamu jepesi usoni mwake.

“ Nashukuru sana Binti yangu, nimekamilisha, nafikiri naweza kwenda” Yule mzee mwenye mvi na ndevu nyingi aitwaye Mzee Lawi akasema.

“ Bila shaka Mzee wangu, karibu sana” Belinda akasema, Mzee Lawi akatoka. Lakini kumbe hakutoka moja kwa moja, alizuga kama anaondoka huku akigeuka geuka nyuma kumtazama Belinda kama anamuangalia, alipoona Belinda anaendelea na shughuli zake akachepuka na kuelekea kwenye kiti cha kukalia wateja ambapo hapo akawakuta watu wawili wamekaa, akawasalimu kisha naye akaketi.

“ Nafikiri zimebaki dakika chache Sajenti atoke” Mzee Lawi akawaza, hazikupita dakika mbili Mzee Lawi akamuona Sajenti Warioba akitoka kwenye ule ukumbi wa SHDC 400 na kuelekea kwa Belinda. Mapigo yake ya moyo yakapoteza utulivu, kijasho chembamba kigusa makwapa yake. Akamuona Sajenti akizungumza na Belinda kwa kuchangamkiana, kisha baadaye akamuona Belinda akiandika kitu Fulani kwenye karatasi na kumkabidhi Sajenti, Moja kwa moja akajua kuwa Sajenti kapewa namba za simu. Kwa kuliona hilo Mzee Lawi akaachia tabasamu jepesi. “ Kazi hii imekuwa nyepesi” Akawaza. Baadaye akamuona Sajenti akija kule aliko, Mzee lawi kwa mshtuko mkubwa akainama na kuuweka uso wake kwenye magoti yake akiwa kakaa, Sajenti akapita pasipo kumuona, Mzee Lawi akainua uso wake akauelekeza upande alikokuwa anaelekea Sajenti, akamuona Sajenti akitoka na kuteremka kwenye ngazi. Mzee Lawi hakutaka Sajenti amputee, akaamka upesi na kutembea kwa haraka wala hakujali mwili wake wa uzee uliokuwa ukimkatili. Akatoka lakini katika hali asiyoitegemea hakumuona Sajenti Warioba,

“ Huyu kijana kaelekea upande upi, haa! Huyu mtoto Jini ama!” Mzee Lawi akasema kwa sauti huku akigeuka upande huu na upande huu kuangalia kama atamuona Sajenti lakini haikuwa hakumuona. Akaingiza mkono wake mfukoni na kubonyeza bonyeza kisha akaiweka sikioni.

“ Naomba tuonane Mr. Seba, ndio….! Ikiwezekana sasa hivi. Mimi bado nipo SHDC huyu Mbwa kanipotea hapa kama Jini, sawa ngoja nichukue” Mzee Lawi akamaliza kuongea na simu kisha akavuka barabara upesi upesi akilakiwa na madereva Teksi,

“ Huna haja ya kunisalimu, naomba unipeleke PARADISE HOTEL, fanya hima” Mzee Lawi akasema akiwa tayari kaingia ndani ya Teksi na kufunga mlango kwa nguvu.

“ Okay Samahani sana Mzee wangu, Hivi hiyo Hotel ipo wapi…”

“ Hee! Wee kijana.. kwani wewe mgeni kwenye jiji hili!! Hee! Kazi hii haifai mtu mgeni, inahitaji wajuvi wa mitaa, huoni kama utanichelewesha?” Mzee Lawi akagomba kwa sauti, teksi ikiwa imeacha eneo lile.

“ Niwie radhi Mzee wangu, usemayo ni kweli, naomba…”

“ Hakuna cha kuomba, twende mpaka Upanga mtaa wa kitonga, ukifika hapo utaiona hotel hiyo, jengo lake ni kubwa na zuri kuliko yote katika mtaa huo” Mzee Lawi akasema zamu hii akiwa hasira zimepungua kidogo, pengine alimuonea huruma Dereva Teksi.

Haikuchukua dakika kumi Teksi ikasimama mbele ya Paradise Hotel, Mzee Lawi akamlipa dereva kisha akashuka. Baada ya Teksi kuondoka, Mzee Lawi akampigia Mr. Seba, wakazungumza kwa dakika moja kisha simu ikakata. Kitambo kidogo akatokea kijana mmoja aliyevalia shati la samawati na suruali nyeusi na tai, yule kijana akamsalimu Mzee Lawi na kumchukua akampeleka kwa Mr. Seba.

“ Karibu sana Mzee Lawi” Mr. Seba akasema akimkaribisha Mzee Lawi.

“ Ahsante sana Mr. Seba”

“ Haya lete maneno, Ama kweli umezeeka, yaani mtu anakupotea machoni mwako hivi hivi kama jinni!” Mr. Seba akasema huku akimdhihaki Mzee Lawi.

“ Hata mimi nafikiri nimeanza kuzeeka. Uzee ni adhabu kali sana Baba yangu aliwahi kuniambia, Baba yangu alisema ni kheri kifo kuliko uzee” Mzee Lawi akasema.

“ Anyway! Tuachane na hayo. Lete maneno, ilikuwaje?”

“ Nilienda kuhifadhi wosia wangu pale SHDC, Wakati namalizia kuhifadhi ili nitoke nikasikia kuna mtu kaingia katika ule ukumbi kwani mwanzoni nilikuwa peke yangu. Kugeuka kumtazama nikashtuka kumuona Sajenti Warioba, na kabla hajageuka upande nilipo nikawahi kuondoa uso wangu kwake hivyo kama aliona basi atajua sikumuona, akaenda kwenye visanduku ambavyo majin yake yanaanzia na J. Nikatoka kwa maana muda ulikuwa umeisha” Mzee akasema wakati huo mhudumu wa kike mrembo aliyevalia sketi fupi iliyoacha mapaja yake wazi akiwa kasimama mbele yao.

“ Niletee kama Kamanda Mkuu hapa” Mzee Lawi akasema, na yule mhudumu akaondoka.

“ Unauhakika ulimuona Sajenti Warioba, isijekuwa uzee unakuja kwa nguvu Bwana Lawi”

“ Nina uhakika ni yeye” Mzee Lawi akajibu yule mhudumu akiwa tayari kaleta vinywaji.

“ Sasa kama amekupotea wakati mimi nilikuambia umfuatilie huoni kama hakuna ulichokifanya! Ni bora hata usingeniambia, mtu anakupoteaje lakini…” Mr. Seba akasema huku akiwa amekereka.

“ Hakuna kilichoharibika, nilimuona Sajenti akimuomba namba yule dada, Belinda akamuandikia Sajenti namba kwenye kikaratasi akampa”

“ Huyo Belinda ni nani?” Mr. Seba akauliza.

“ Ni mdada anayefanya kazi pale SHDC. Bila shaka Sajenti Warioba baadaye atampigia Belinda, hivyo tunatakiwa tuzungumze na Belinda atuwekee mtego tumkamate Sajenti” Mzee Lawi akasema huku akimtazama Mr. Seba.

“ Hahah! Ama kweli ng’ombe hazeeki maini. Mzee Lawi umenifurahisha sana. Yaani kumbe tunaweza kumkamata pasipo kutumia nguvu. Sasa tutampataje huyo Belinda?” Mr. Seba akasema.

“ Hiyo ni kazi rahisi, jioni akitoka kazini itabidi tuagize vijana wakazungumze naye kwa hiyari ama kwa lazima”

“Inabidi jambo hili tulifanye kwa haraka kabla yule panya hajashtukia mitego yetu,” Mzee Lawi akasema.

“ Huyo Belinda anatoka saa ngapi kazini?”

“ Kwa kweli sijui ila kuanzia jioni itanipasa kwenda eneo la jengo kla SHDC kumfuatilia, alafu nitakupigia simu, wewe uandae vijana wawe tayari muda wowote” Mzee Lawi akasema.

“ Vizuri! Lakini nina mashaka!”

“ Mashaka! Mashaka gani” Mzee lawi akasema kwa kuhamaki.

“ Ni kuhusu Sajenti Warioba kukupotea kimazingara. Unauhakika hakukuona? Unajua yule ni mwanausalama mzoefu tena komando, machale kwa mtu kama yeye ni jambo la kawaida” Mr. Seba akasema huku uso wake ukiwa na wasiwasi.

“ Sidhani kama aliniona, lakini hata mimi bado najiuliza alinipoteaje poteaje eneo lile ambalo lilikuwa wazi sehemu zote” Mzee Lawi akasema.

“ Itabidi jambo hili ulishughulikie mapema, kwanza itakupasa urudi tena kule SHDC ukafuatilie kile kisanduku ambacho alikuwa kasimama Sajenti, tujue ndani yake kuna nini, kisha Belinda tutamfuatilia usiku kabisa, wewe unaonaje” Mr. Seba akasema;

“ Sio wazo baya, ila mimi nafikiri, tungeenda wote sasa hivi, wewe utaenda kufungua akaunti pale SHDC na kujifanya unaweka document zako, utaenda na kitambulisho chenye jina linaloanzia na herufi J ili upangiwe kisanduku karibu na Sajenti warioba, hapa itakuwa kazi rahisi” Mzee Lawi akasema.

“ Umetoa wazo zuri sana, haina shida, nitamtafuta kijana ambaye utaenda naye, mimi ni mtu maarufu, sidhani itakuwa vizuri nikienda mimi hapo SHDC”Mr. Seba akasema akiichukua simu yake.

“Sawa! Tuanze muda huu”

*************************

Sajenti akiwa chumbani kwake akakumbuka habari za Belinda, akaenda kwenye suruali aliyokuwa ameivaa akaitoa ile karatasi yenye namba aliyopewa na Belinda, akaitazama akiwa katabasamu, akachukua simu na kuanza kuinakili, kabla hajaipigia akakumbuka jambo, alimkumbuka yule mzee mwenye Mvi kule SHDC, akakumbuka jinsi alivyokuwa akitoka kwenye lile jengo. Akakumbuka akiwa anatembea akiukabili mlango wa vioo wenye sensor wakutokea jengo lile la SHDC, akamuona yule mzee mwenye mvi Kupitia vioo vya mlango ule, hapo akaharakisha kutoka nje lakini kadiri alivyokuwa akiharakisha ndivyo na yule mzee naye alikuwa akikazana kumfuata, sajenti akataka kujua kuwa mzee yule alikuwa akimfuatilia au zilikuwa hisia zake tuu. Akatoka kwa nje na kuvuka kwa upesi barabara na kujibanza kwenye moja ya Teksi zilizokuwa pale nje. Akamuona yule mzee akiwa ametoka nje akibabaika akitazama huku na huku akiwa na wasiwasi mwingi. Kisha akamuona yule mzee mwenye mvi akipiga simu na kuanza kuzungumza maneno ambayo Sajenti alikuwa akiyasikia kwa mbali sana. Sajenti alishtuka alivyosikia jina lake likitajwa na yule Mzee.

Kumbukumbu hizo zikamfanya Sajenti akurupuke na kuvaa nguo harakaharaka, akatoka nje ambapo alikuwa ameegesha gari lake, akabonya rimoti aliyoitoa kwenye mfuko wa suruali, mlango wa mbele wa gari ukafunguka, baada ya kuingia ndani Sajenti akaliwasha gari huku akilirudisha nyuma na mbele mpaka liliposimama kwenye usawa mzuri lilipo Geti la kutokea, akashusha kioo cha dirisha la mlango wa mbele la gari, akatoa mkono na kubonyeza rimoti ya Geti, papohapo Geti likaanza kuteleza polepole na sehemu ya nje ikawa inaonekana. Baada ya Sajenti kulitoa Gari nje akabonyeza tena ile rimoti; geti likateleza polepole kujifunga.

“Yule mzee kwa nini alikuwa akinifuatilia? Kwa nini aliponiona kwenye ukumbi wa SHDC400 uso wake ulikuwa unawasiwasi nilipomtazama! Atakuwa ni nani mzee yule? Na alikuwa akimpigia nani simu? Isijekuwa yule mzee alikuwa anaongea na Kamanda Mkuu? Mmh! Lakini haiwezekani hizi ni hisia zangu tuu” Sajenti alikuwa akizungumza pekeake huku gari likiwa tayari limeshafika Ubungo.

“ Nikirudi nitaifungua ile chipu nione ndani yake kuna nini, kwa nini inatafutwa sana, lazima itakuwa na jambo kubwa ndani yake, tumekuwa tukiilinda pasipo kujua kwa nini tunailinda, kama isingeibwa huenda nisingejiuliza kwa nini tunailinda. Mpaka inaibiwa licha ya kulindwa kiasi kile lazima itakuwa na jambo zito la siri mno” Sajenti akawaza huku mikono yake ikiwa imeshika usukani akiendesha gari kuelekea SHDC, muda huu alikuwa akikatiza eneo la Manzese Darajani. Alipofika kituo cha Manzese Bakhresa akasimamisha gari lake na kununua sigara kwa machinga waliopo pembezoni mwa barabara, akanunua na kiberiti akaitia moto sigara aliyokuwa ameipachika mdomoni, akaendelea na safari yake. Mara hii uso wake ukiwa umezingirwa na moshi wa sigara. Akiwa anavuta sigara punde alimkumbuka yule mwanamke aliyeiba kadava kwenye ile maabara ya Boreti.

“ Yule mwanamke inaonekana ni mwanamke hatari sana. Aliwezaje kuingia maabara ya Boreti na kutoka pasipo kukamatwa na walinzi, alipitia njia ipi?” Sajenti akawaza alafu akaiweka tena sigara mdomoni na kuvuta pafu ndefu kisha akaitoa sigara mdomoni; akabinua kichwa chake kwa nyuma kisha akauachia ule moshi uliomo mdomoni, na mwingine akautoa Kupitia puani, mule ndani kukajazwa na moshi wa sigara.

“Dr. Binamungu ni msaliti, lazima atakuwa anajua mambo mengi kwenye suala hili, kitendo cha kumkuta kwenye lile jengo kule Twangoma, tena nikaisikia sauti ya yule mwanamke aliyeiba kadava ni ushahidi tosha kuwa Dr. Binamungu sio mwenzetu” Sajaenti akawaza mara hii alikuwa keshalikaribia jengo la SHDC; akiwa umbali kama wa mita hamsini hivi alishtuka kuona mlango wa gari jeusi aina ya Brevis yenye tinted lililopaki eneo la jengo la SHDC; ukifunguka na yule mzee mwenye mvi akishuka upande wa kushoto wa mlango wa nyuma wa gari huku upande wa kulia akishuka kijana aliyevalia Kaunda suti nyeusi na miwani. Sajenti akapunguza mwendo na kuegesha gari yake sehemu nyingine umbali wa hatua kumi na tano tuu. Sajenti alimkumbuka yule mzee mwenye kuwa ndiye yuleyule aliyekuwa akimfuatilia wakati wa mchana alipokuja SHDC kuihifadhi ile chipu.

Sajenti akiwa ndani ya gari akawaona wakiingia ndani ya jengo la SHDC wakapandisha ngazi hapo wakapotea machoni mwake baada ya kuzibwa na ukuta, lakini kitambo kidogo akawaona Ghorofa ya pili wakitembea kuelekea ilipomeza ya Belinda, akawaona wakizungumza jambo na Belinda, kisha Belinda akawapa karatasi, yule kijana aliyevalia Kaunda suti nyeusi akapokea ile karatasi akawa anajaza jaza vitu Fulani. Baada ya kujaza akamrudishia ile fomu, Belinda akaihakiki alafu akaingiza zile taarifa kwenye Kompyuta, Belinda akatoa kifaa Fulani na kumkabidhi yule kijana mvaa Kaunda suti nyeusi, yule kijana akaweka dole gumba kwenye kile kifaa. Sajenti akamuona Belinda akinyanyuka akiwaamuru wamfuate; wakamfuata mpaka walipopotea kwenye ukumbi wa SHDC400, hapo Sajenti hakuweza kuwaona tena. Sajenti akashuka kwenye gari, kisha akalisogelea gari walilotoka yule mzee mwenye mvi na kijana mvaa Kaunda suti, akasimama kwa kitambo kidogo akatazama huku na huku, akaona hali iko shwari, akaingiza mkono mfukoni akatoa kifaa Fulani hivi kama simu, akabonyeza bonyeza kwenye kile kifaa alichokitoa mfukoni, kilipowaka akakielekezea kwenye kitasa cha mbele cha mlango wa gari, kitambo kidogo mlango ukafunguka, Sajenti akaingia ndani yake akapekua pekua ndani ya lile gari lakini hakuona jambo lolote la maana, kila mara alikuwa akikagua huku akiangalia nje kwa hofu.

Baada ya kujiridhisha kuwa hakuna jambo la maana ndani ya lile gari akafungua mlango wa gari ili atoke, lakini kabla hajatoka akasikia sauti ya simu ikiita ndani ya lile gari, moyo wa Sajenti ukapiga kwa nguvu, alishtuka sana, akaanza kuitafuta simu iliyokuwa ikiita, akaiona chini ya kiti cha gari, akaichukua. Sajenti akashtuka sana akabaki mdomo wazi baada ya kuona jina la Mr. Nzige ambaye ndiye kamanda Mkuu. Sajenti akabaki anaitazama simu ile asijue aipokee au aiache. Simu ikaacha kuita.

“Bila shaka yule mzee mwenye mvi ndiye aliyekuwa akiongea na Kamanda Mkuu mchana, sasa naanza kuelewa, hawa watu washajua nimeingia mjini” Sajenti akawaza lakini kabla hajafika mbali katika kuwaza sauti ya simu ikamkatisha, Mr. Nzige alikuwa akipiga tena. Sajenti Warioba akapokea na kukaa kimya;

“ Hakikisheni mnaivunja hilo sanduku lake, sio ajabu akawa ameihifadhi hiyo chipu. Sawa!.. Hello!.. Heloo…Mr. Lawi” Kamanada Mkuu akaongea akiwa anababaika baada ya kuona hajibiwi. Sajenti akavuta pumzi nyingi na kuiachia kwa nguvu kama kobe mzee hasira zikimkaba kifuani mwake, punde akashtuka kuona Yule mzee mwenye mvi akitoka pekeake pasipokuwa na yule kijana mvaa Kaunda nyeusi. Kwa upesi Sajenti akatoka ndani ya lile gari pasipo kuonekana, akajibanza kwenye gari jingine. Hapo akamuona yule mzee akiingia ndani ya gari na kuichukua simu.

“ Hapa itanipasa niingie SHDC nimfuate yule Mvaa suti kabla mambo hayajaharibika, huyu mzee muda mfupi ujao atampigia Mr. Nzige, na hili likifanyika inaweza ikawa mbaya katika mipango yangu” Sajenti akawaza. Kisha akatoka pale alipokuwa amejibanza, akajongea jongea kwa kujificha mpaka lilipo lango la SHDC, akaingia ndani.

“ Habari Belinda!”

“ Nzuri tuu Jacob, umerudi tena?”

“ Hahah! Hapa ni kama nyumbani, uwepo wako unanifanya nirudi kila mara”

“ Unatania Mr. Jacob” Belinda akasema huku akicheka hali iliyopelekea uso wake kwenye mashavu vitokee vishimo vidogo vidogo na kuufanya uso wake kuwa mzuri.

“ Kwa nini nitanie Belinda! Kwa urembo wako hapa naweza kurudi hata mara mia” Sajenti akachombeza.

“ Mhh! Makubwa! Haya niambie unataka kwenda SHDC400?”

“ Labda nimekuja kukuona je!” Sajenti akasema akicheka huku akigeuka nyuma kuangalia lango la kioo la kuingilia kuona usalama wake. Bado hali ilikuwa shwari.

“ Acha masikhara bhana J, ujue hapa ninakazi nataka kuimalizia, si unaona muda wa kuondoka umefika?” Belinda akasema.

“ Sawa, nimekuelewa” Sajenti akajibu kisha akapewa kile kifaa cha kuweka dole gumba akaweka dole gumba la kushoto akapewa kodi ya kuingilia, akamuacha Belinda.

Sajenti akaingia ukumbi SHDC400 akakuta hali iko vilevile, ukimya na mwanga hafifu huku eneo lote likiwa halina mtu yeyote yule. Sajenti akasonga mpaka alipokaribia kwenye sanduku lake kama hatua kumi hivi, lakini akili yake ikamtahadharisha huku akijiuliza yule mtu atakuwa yupo upande gani mule ndani, huku na huku macho yake akawa anayarusha kumtafuta kijana yule mvaa Kaunda suti. Mpaka anafika eneo la sanduku lake hakuona mtu. Akakagua sanduku lake kuona kama kuna mabadiliko yoyote lakini hakuna dosari yoyote aliyoiona, lakini akashtuka kuona sanduku jipya ambalo halikuwepo hapo kabla, sanduku lile lilkuwa linamaandishi yaliyosomeka JS18. Akalisogelea, alafu akageuka huku na huku kuona kama kuna mtu anamtazama, hakuona hatari yoyote, akalikagua lile sanduku kuona kama ataweza kulifungua lakini akashindwa, mifumo ya ufunguaji ya zile ndroo za ile sanduku zilihitaji dole gumba la mhusika. Sajenti akaachana nalo, akaenda kwenye sanduku lake na kulifungua, akaitoa ile chipu, hapo akageuka tena kutazama huku na huku, alipoona hakuna mtu akaiweka mfukoni, kisha akachomeka vifaa Fulani, akafunga kisha akapiga hatua ndogo ndogo huku akielekea upande wa pili wa ule ukumbi wenye shelfu nyingi zenye makabati marefu kwenda juu na kwenda kushoto na kulia huku yakiacha hatua mbili za watu kupita. Sajenti akasimama kwenye sanduku lenye alama BL21 ambapo mchana alimuona yule mzee mwenye mvi akiwa eneo hilo. Akalikagua lile sanduku lakini hakuwa na chochote cha kufanya kutokana na mfumo wa visanduku vile vinavyohitaji alama za vidole vya wahusika. Kama sio mhusika ni ngumu sana kufungua visanduku vile. Muda wa kukaa mule ndani ulikuwa umeisha, Sajenti akatoka lakini akiwa anaukaribia mlango wa SHDC400 Akahisi kuna mtu amepita nyuma yake, akageka lakini hakuona mtu, hata kwa nini Sajenti sio mtu wa kupuuzia hisia zake, kwa uzoefu wake aliamini hisia na akili zake ni nyenzo muhimu katika kazi yake ya ujasusi na mambo ye kipelelezi. Sajenti. Akatoka, akafika kwa Belinda.

“Afadhali wewe umewahi kurudi, huyo mwenzako mpaka sasa hajatoka, nimechoka kwa kweli! Muda wa kuondoka umefika” Belinda akasema akiwa amesimama kivivu.

“ Mwenzangu nani? Mbona nilikuwa pekeangu?” Sajenti akasema

“ Kuna mtu aliingia kabla yako, nashangaa mpaka sasa hajatoka mpaka wewe uliyekuja baada yake umetoka, muda wake umeisha, watu wasiojali muda kwa kweli wananikera mno? Belinda akasema huku akiangalia saa yake.

“ Pole sana, lakini ndio wateja wako” Sajenti akasema.

“ Embu ona, saa kumi na mbili na nusu hii. Wenzangu wote wameondoka” Belinda akaongea akitoka ofisini kwake na kuja upande wa wanaposimamia wateja.

“ Ngoja nimfuate huko ndani” Belinda akasema.

“ Mimi ngoja nikuache, nafikiri tutawasiliana tuu, namba zako niko nazo” Sajenti akasema.

“ Sawa Jacob Warioba, utanicheki” Belinda akasema, wakaachana.

Sajenti akatoka; alipoukaribia ule mlango wa vioo wenye sensors akapishana na mtu mmoja aliyevalia suti nyeusi na miwani ya rangi nyeusi; mtu yule alikuwa mweusi, mrefu na mwenye mwili uliojengeka vizuri ambao uliifanya suti aliyoivaa kujivunia kuvaliwa naye, kichwani alikuwa na kipara. Kwa kweli sura yake ilikuwa ya kazi ikiwa mbali na mzaha, Sajenti akapiga hatua kama sita hivi akageuka nyuma, kumbe yule mtu naye alikuwa amegeuka nyuma; macho yao yakakutana na wote nyuso zao zikashtushwa na hali hiyo. Wote kwa pamoja kama watu walioamrishwa wakaondoa nyuso zao na kila mmoja akaendelea na safari zake. Sajenti akafika kwenye ngazi za kushukia chini, akili yake ikaingiwa mashaka, yule mtu hakuwa wakawaida, kumuona mtu kama yule tena akiwa katika mavazi yale na muda ule kulimaanisha kuwa kuna hatari inaenda kutokea. “ Yule kijana mvaa Kaunda mbona sikumuona kule SHDC400, Bila shaka ndiye aliyekuwa anazungumziwa na Belinda; nina uhakika atakuwa kawapigia simu na kuwajulisha wenzake uwepo wangu humu ndani” Sajenti akawaza.

Sajenti hakuwa mbali na ukweli, akiwa anawaza hivyo kabla hajamaliza ngazi ya mwisho ili atokee Ground kabisa, akashtushwa na sauti ya watu zikiongea, akasimama kwa upesi na kujibanza, alafu akachungulia, hapo macho yake kwa mshtuko na hamaki yakapokelewa na kundi la vijana wanne waliovalia suti wakiwa wanaziandaa silaha zao, moyo ukapiga kite alipoangalia nje kabisa akamuona Kamanda Mkuu. Mr Sebastian Nzige akiwa amesimama na vijana waliovalia sare za kiaskari za rangi ya dark blue ambazo nyuma yake zilikuwa na maandishi yaliyosomeka TSFFT ambayo Sajenti alikitambua kikosi hicho. Tanzania Special force for Fighting Terrorism ambacho kifupi chake ndio TSFFT, ni kikosi maalumu kilichoundwa kwa lengo la kupambana na ugaidi. Uwepo wake eneo lile kulileta tafsiri moja kichwani mwa sajenti Warioba, kwamba kuna tukio la kigaidi eneo lile, na ndio maana kikosi kile kimekuja kwa lengo la kudhibiti na kupambana.

Wanajeshi wa TSFFT mbali na mavazi yao ya Dark Blue, pia walikuwa wamevaa kofia ngumu kichwani mwao, chini walikuwa wamevalia viatu vyeusi vya kijeshi, wakiwa wamejidhatiti na silaha za kisasa za moto, walikuwa takribani wanajeshi ishirini. Sajenti akamuona yule mzee mwenye mvi akitoka kwenye lile gari ambalo sajenti aliingia ndani yake na kulikagua akakuta simu inaita. Akamuona yule mzee akimsogelea Kamanda Mkuu, Mr. Nzige. Akawaona wakiteta jambo, lakini ghafla Sajenti akashtushwa na sauti ya wale vijana wa nne waliovalia suti wakitembea kuja kule alipo, hakutaka akutwe pale, akaanza kukimbia kurudi akipandisha ngazi kurudi SHDC, akafika SHDC kwenye zile ofisi za kina Belinda lakini hakukuwa na mtu, akajua Belinda bado hajarudi kutoka ukumbi wa SHDC400. Kwa upesi akasonga kuelekea lango la SHDC400 Akatembea kidogo akakata kulia akakutana na korido akaifuata mpaka kwa mbele alipolakiwa na lango la SHDC400 lakini alipolikaribia wazo likamjia “ Nitaingiaje humu pasipo kuwa na code maalum kwani ule mlango bila ya code kamwe huwezi kuingia, na hata ukipewa code ya kuingia inamuda wake wa kuisha ambayo ni dakika thelasini.

“ Sasa nitafanyaje. hapa sina ujanja tena” Sajenti akasema huku akijaribu kubinya binya vitufe vya ule mlango aone kama ataweza kubahatisha mlango ufunguke, lakini kamwe isingewezekana kwani code ni mpaka zitolewe na computer za wahudumu wa SHDC Kama Belinda. Akiwa anahangaika kutafuta namna ya kuingia mule ndani ghafla akasikia sauti ya wale watu wanne wakiongea upande wa ofisi za mapokezi, joto la mwili likampanda, mapigo ya moyo yakazidi kupiga pasipo mpangilio, kijasho cha wasiwasi kikabusu ngozi yake, akili yake ilikuwa haitulii ikiwaza hili mara lile na kushindwa kujua kipi cha kufanya, hofu ikazidi kujaza moyo wake alipowasikia wale watu wakija kule alipo lilipo lango la SHDC400. Hapakuwa na umbali wowote hivyo dakika moja Sajenti alijua watakuwa pale, na hapo mbilinge ingeanza, Sajenti akavuta pumzi kwa nguvu na kuibana akiwa kaegemea mlango wa SHDC400 akitazama kule ambapo watatokea wale watu waliovalia suti nyeusi, hatua za wale watu zikiwa zimebakiza sekunde tano ili watokee ghafla Sajenti alijikuta akipoteza mhimili kwa kuangia ndani baada ya mlango wa SHDC400 kufunguka, kumbe Yule kijana mvaa Kaunda suti alikuwa ndio anatoka, Kwa vile wote hawakuwa wametarajia tukio hilo wakabaki wameduwaa huku mlango ukijifunga tena wakiwa upande wa pili wa ukumbi wa SHDC400, Yule kijana akamrukia Sajenti na kumchapa ngumi mbili za tumbo, Sajenti akagugumia maumivu, yule kijana hakutaka kumchelewesha, akamuongeza ngumi nyingine lakini mara hii Sajenti akaiona, akaikwepa na kurukia upande wa pili, Yule kijana alikuwa mwepesi, akamrukia kwa teke la upande, Sajenti akainama; teke likapita likikata upepo. Kijana akajiweka sawa wakati Sajenti naye muda huu kasimama wakiwa wanatazamana, Sajenti akajiweka vizuri na kunyoosha mabega yake. Yule kijana akawa anazunguka hukuwa wakitazamana, Sajenti alijua maana yake, yule Kijana akarusha ngumi ya uongo na kweli na kuiunganisha na tikitaka moja maridadi kabisa, Sajenti akazikwepa ngumi lakini mateke yakamkuta, teke moja likimpiga kwenye kiuno jingine likampiga shingo; akaanguka chini. Yule kijana alikuwa mzuri wa kutumia miguu yake, alikuwa bingwa wa kurusha mateke kwa dizaini za hapa na pale. Sajenti akiwa pale chini akigugumia maumivu huku damu zikivuja eneo la kulia palipochubuliwa na kiatu cha yule kijana; akawaza “ huyu kijana anacheza na sharubu za simba” Yule kijana akarusha teke ambalo lingempata tumboni Sajenti lakini Likazuiliwa, sajenti akalikinga na kulisukumia kwa nguvu upande mwingine, yule kijana akapepesuka, kabla hajakaa sawa, Sajenti akaamka kwa upesi na kumvamia na kichwa kilichompata kijana kwenye tumbo, wote wakaangukia kwenye shelfu la kabati, makabati yakaanguka na kutoa mlio uliopoteza utulivu wa mule ndani. Sajenti hakutaka kumchelewesha, wakiwa juu ya kabati akamchanganyia ngumi kumi hivi za uso, kisha akamuinua kwa upesi na kumgeuza na kumzungusha kwa kasi kisha akamkaba shingoni kwa nguvu kwa mtindo wa chatu, alafu akambamiza kwa nguvu kwenye kabati la upande mwingine akaanguka na kabati na kutoa mshindo mkubwa, akamfuata lakini kabla hajafanya chochote sauti kutoka nyuma ikamuamrisha aache. Akageuka hapo akamuona yule mwanaume aliyevalia suti nyeusi na miwani nyeusi. Sajenti hakutaka kupoteza muda, akajirusha upande wa pili lilipoanguka kabati na kujibanza alafu kwa upesi akaanza kutambaa kama mjusi upesiupesi risasi zikimpunyua punyua kila alipoondoa mhimili wake. Alipotokea upande wa pili wa kabari zilizosimama akasimama na kuanza kuimbia akijificha upande huu na ule, kisha kuingilia safu zingine za makabati na kukimbia katikati yake, yule mtu akawa anamfukuza mpaka palipokuwa kimya akiwa hamuoni Sajenti. Tayari Sajenti alikuwa keshampoteza yule mtu. Akiwa kajificha kwenye moja ya safu ya mashelfu ya makabati alimsikia yule mtu mwenye sura ya kutisha isiyo na mzaha ikitembea ikija mahali kule alipo, Sajenti akajikausha akimsubiria atakapojitokeza ili amkabili. Yule mtu akaanza kuita.

“ Sajenti Warioba, jitokeze! Wewe ni mwoga sana. Nilipewa sifa zako kwamba ni jasiri kama simba, jitokeze sasa ukutane na simba dume, sajenti! Sajenti!..” Yule Mwanaume akawa anasema akijaribu kumshawishi Sajenti ajitokeze. Lakini Sajenti hakutaka kujitokeza. Sajenti alijua sifa zikuzote zinaua, na adui mahiri hutumia sifa au vitu vyenye kuvutia kama mtego kwa windo lenye tamaa. Sajenti hakuwa tayari kuwa windo lenye tamaa ya vitu vya namna hiyo.

Sajenti akasikia sauti ya mtu mwingine ikiongea kwa kugugumia, akajua ni yule kijana mvaa Kaunda aliyempiga, yule kijana akamkaribia yule mwanaume atishaye. Sajenti akawasikia wakipeana majukumu, mmoja aende upande huu na mwingine aende upande huu kumtafuta yeye. Sajenti akahama upesi eneo lile na kwenda upande mwingine kwa mbali kidogo. Akajibanza kwenye meza moja kubwa iliyoegema ukutani, wakati anajificha akamuona yule kijana mvaa Kaunda akisogea kwenye ile meza akiwa kashika bastola, yule kijana alikuwa akipumua kwa shida lakini hakusahau kuchukua tahadhari, akapiga hatua huku bastola yake akiwa kainyooshea kwenye ile meza alipojificha Sajenti. Akasogea zaidi lakini kufumba na kufumbua Sajenti alifyatuka kama mshale na kumvamia akiwa ameuwahi mkono ulioshikilia ile bastola, risasi ikafyatuka na kupiga kwenye vioo vya ule ukumbi, mapambano yakaanza upya huku ile risasi ikiwa imetoa taarifa upande mwingine aliokuwa yule mwanaume mwenye roho mbaya. Haikuchukua dakika moja Sajenti akafanikiwa kumuua yule kijana mvaa Kaunda suti, akaichukua bastola yake kisha akahama na kujificha upande mwingine.

Akiwa kajificha ghafla alisikia makelele ya mwanamke, alikuwa ni Belinda aliyekuwa akipiga kelele za maumivu. Sajenti akazidi kuchanganyikiwa, joto la mwili likazidi kupanda, akili yake ikapoteza utulivu asijue afanye nini.

“ Sajenti Warioba jitokeza Upesi, kabla sijamuua huyo dada asiye na hatia” Yule mtu akasema.

“Maisha ya Dada huyu yapo juu yako. Tunafahamu uliomba namba zake, hahah! Unampenda eeh! Sasa leo namuua hapa kama utaendelea kujificha kama panya” Yule mtu akaendelea kumtisha Sajenti warioba. Belinda alikuwa akipiga kelele kila alipokuwa akikabwa au kuvutwa nywele.

“ Sajenti! Embu tumalize jambo hili. Sina muda zaidi wa kupoteza na mpuuzi kama wewe. Nahesabu mpaka kumi. Baada ya hapo nitaumwaga ubongo wa huyu mwanamke asiye na hatia kisa woga wako wa kipuuzi” Yule Mwanaume akasema.

“ Moja! Embu jitokeze ukabiliane na mimi kama kweli wewe ni mwanaume. Mbili! Hutaweza kujificha na kutukimbia, sisi ni kama kivuli chako, popote ulipo tupo. Tatu! Unajua wewe ni komando, mwanajeshi na askari polisi, utakubalui raia wa nchi hii asiye na hatia afe kwa ajili ya woga wako? Nne! Jitokeze nitakuua kwa mikono yangu hii, wala sitatumia silaha. Tano! Sajenti, nimechoka, nampiga risasi huyu mwanamke” Anaacha kuhesabu baada ya Belinda kupiga kelele za maumivu.

“ Tuliaa! Usidhani mimi ni yule panya buku. Nitakuua sasa hivi!” Yule mtu akagomba

“ Usiniue tafadhali! Si umesema utahesabu mpaka kumi, mbona umeishia tano. Jacob sio mwoga atajitokeza tuu” Belinda akasema kwa sauti ya kuchoka, akijaribu kuuiba muda wa yule mwanaume.

“ Kelele…! Malaya wewe! Nitakuua wewe na huyo hawara wako.” Yule mwanaume akamzaba kofi kali Belinda.

“ Huna haja kumuua mtu tena mwanamke mzuri kama huyu asiye na hatia. Kama wewe ni mwanaume kweli, timiza ahadi yako ya kuniua kwa mikono yako miwili pasipo kutumia silaha. Uone kama hautakufa wewe” Sajenti akasema akiwa kajificha umbali mdogo kutoka waliposimama yule mwanaume mbaya na Belinda.

Kisha Sajenti akajitokeza akiwa kaweka mikono juu akisema;

“ Kama kweli wewe ni mwanaume pambana na mimi mkono kwa mkono. Ndio utajua mimi na wewe nani kidume”

Yule mwanaume akaduwaa akiwa anamtazama Sajenti kwa mshangao. Kisha akamsukuma kwa nguvu Belinda upande mwingine. Akasimama kwa kitambo akiwa anatazamana na Sajenti, kisha akapiga hatua polepole akiwa kashika bastola yake mkononi. Alipomkaribia kwa hatua tano hivi akasimama, uso wake ukiwa umekasirika, macho yake yakiwa mekundu na mishipa ikijitokeza kwenye pembe za uso. Sajenti naye akawa anamtazama akiipa akili yake utulivu.Yule mwanaume akaiangusha bastola yake chini alafu akaipiga teke ikaenda mbali. Kisha akavua koti la suti na kulirusha kwenye kabati likawa linaning’inia. Akashika shingo yake na kuitoa tai, akaitupa. Sasa kila mmoja akawa amejiweka tayari kwa mapigano, muda huo Belinda alikuwa amesimama kwa pembeni akiwa amejikunyata kwa hofu.

inaendelea

Kitabu kipo Tayari, lIPIA Tsh, 15,000/= UJIPATIE NAKALA YAKO

0693322300
Robert Heriel
Airtelmoney
 
WAKALA WA SIRI Episode 06
Mtunzi; Robert Heriel
WhatsApp 0693322300

EPISODE 06

ILIPOISHIA

Yule mwanaume akaduwaa akiwa anamtazama Sajenti kwa mshangao. Kisha akamsukuma kwa nguvu Belinda upande mwingine. Akasimama kwa kitambo akiwa anatazamana na Sajenti, kisha akapiga hatua polepole akiwa kashika bastola yake mkononi. Alipomkaribia kwa hatua tano hivi akasimama, uso wake ukiwa umekasirika, macho yake yakiwa mekundu na mishipa ikijitokeza kwenye pembe za uso. Sajenti naye akawa anamtazama akiipa akili yake utulivu.Yule mwanaume akaiangusha bastola yake chini alafu akaipiga teke ikaenda mbali. Kisha akavua koti la suti na kulirusha kwenye kabati likawa linaning’inia. Akashika shingo yake na kuitoa tai, akaitupa. Sasa kila mmoja akawa amejiweka tayari kwa mapigano, muda huo Belinda alikuwa amesimama kwa pembeni akiwa amejikunyata kwa hofu.

ENDELEA
Yule mtu akamsogelea Sajenti na bila kupoteza muda, akarusha ngumi na mateke kwa kasi ambayo hazikuendana na mwili wake. Alikuwa na mwili refu mkubwa uliojazia lakini alikuwa mwepesi mno, kasi yake ya upiganaji ilimpa kazi ya ziada Sajenti kukwepa na kuzuia makonde ya jitu lile. Wakawa wamekaribiana wakashikana, wakaangushana chini na kuanza kuviringishana kama gunzi la muhindi, sajenti akambinua yule mwanaume na kumuachia mvua ya ngumi, lakini yule mtu akajitutumua naye akambinua sajenti na kumuweka chini alafu akamshushia naye mvua ya ngumi, wakafanya hivyo hivyo kwa kupokezana mpaka wote walipochakaa kwa damu, Sajenti akaichoka huo mtindo wa mapigano, akafurukuta na kumpiga teke la tumbo akaangukia upande wa pili, wakasimama kwa kujikokota, wakawa wanapumua kwa kuchoka huku sura zao zikivuja jasho, yule mtu Akaja kwa kasi kumvamia Sajenti lakini hila yake ilishashtukiwa, sajenti akamkwepa na kumsindikiza na teke lililompeleka mpaka lilipokabati akagonga mwamba wa pua ukapasuka, yule mwanaume akageuka akijua kuwa sajenti warioba yupo nyuma yake, sajenti akarusha ngumi yule mtu akaidaka, kisha akampompiga mtama, sajenti akapiga mwereka chini. Yule mtu akampiga mateke ya tumbo sajenti pale chini, kisha akamuinamia akiwa kachomoa kisu mfukoni, akimpelekea sajenti kisu cha kwenye koo. Sajenti akamdaka mkono lakini yule mtu akawa analazimisha azamishe kisu shingoni. Sajenti akajaribu kufurukuta lakini yule mtu alikuwa na nguvu za ajabu, ncha ya kisu ikawa inagusagusa ngozi ya shingo, Sajenti akavuta nguvu zake za mwisho akafurukuta lakini lile jitu likawa limeng’ang’ana tadhani ruba, Sajenti hakuwa na ujanja tena, sasa alisubiri muujiza, akayafumba macho yake huku ameyatunisha mashavu yake mishipa ya kichwa ikiwa imetuna, Ghafla sauti ya risasi ikasikika. Yule mwanaume akamuangukia Sajenti kwa juu akiwa anavuja damu nyingi mno tayari akiwa amekufa. Belinda alikuwa amekichakaza vibaya kichwa cha yule mwanaume mtoa roho.

Sajenti akafumbua macho yake na kuusogeza mwili wa yule mtu, macho yake yakakutana na Belinda akiwa anatetemeka mkononi akiwa na bastola. Sajenti akasimama akiwa hoi taabani.

“Tuondoke!” Sajenti akasema akimshika mkono Belinda wakielekea lango la kutokea kwenye ule ukumbi. Walipofika walishangazwa na hali waliyoikuta, walikuta mlango ukibomolewa kwa baruti.

“ Kuna nini lakini, mbona sielewi?” Belinda akasema akiwa amechanganyikiwa.

“ Hakuna njia nyingine ya kutokea jengo hili” Sajenti akauliza.

“ Jacob kwani kuna nini mbona sielewi, wanakutafuta kwa nini? Hawa watu ni kina nani? “

“ Usijali Belinda, huu sio muda wa maswali, nitakuambia kila kitu, tuondoke kwanza mahali hapa, ni hatari. Hakuna namna nyingine ya kutoka hapa” Sajenti akasema huku akimkumbatia Belinda na kumfariji.

“ lango jingine lipo.,.uuuwiiiii!” Belinda akasema na kuachia yowe baada ya ukuta wa mlango kuzibuka kidogo kutokana na baruti ya kuvunja ule mlango yakiendelea kupigwa na kikundi cha TSFFT.

“ Twende upesi, hatuna muda… huo mlango uko wapi?” Sajenti akasema huku akamvuta Belinda Mkono.

“ Huku..”

Wakaenda mpaka walipotokea upande wenye korido katika ukumbi ule, wakasonga wakiifuata korido hiyo mpaka walipokabiliwa na mlango mbele yao, hawakuwa na muda wa kusubiri, sajenti akavunja kitasa kwa bastola, wakasonga, mpaka walipofika kwenye eneo la lifti, wakaingia ndani ya ile lifti, Belinda akabonyeza vitufe vilivyokuwa kwenye ukuta wa ile lifti, kukafunguka kamlango kadogo, wakapenyeza kwa ndani, na kuanza kuambaa ambaa wakiwa wameinama kwani dari ya njia ile ilikuwa fupi, wakafika sehemu yenye ngazi wakashuka mpaka walipotokea chini kwenye chumba ambacho kilikuwa kinagiza na harufu ya vumbi kama la stoo, Belinda akaenda kuwasha taa, nuru ikafukuza giza la mule ndani, Sajenti akaona vifaa kadhaa vilivyoharibika vya computer na mitambo mingine, ilikuwa ni stoo. Belinda akaufuata mlango wa kile chumba, akabonyeza bonyeza kukawaka lakini kikimuhitaji awe dole gumba, akaweka mlango ukafunguka. Wakatoka wakiuacha mlango ukijifunga, macho yao yakipokelewa na ukumbi mkubwa wenye maegesho ya magari na taa chache zilizofanya ukumbi ule uwe na mwanga hafifu, yalikuwepo magari machache mno mojawapo likiwa la Belinda.

Belinda akatoa rimoti akaibonyeza; milango ya gari ikafunguka, wakaingia ndani ya gari wakaondoka. Gari likapandisha kilima kabla halijafika kwenye lango la ukumbi wa maegesho ili litokeze kwa nje, Sajenti akamuomba Belinda asimamishe gari, Belinda akafanya hivyo. Ndipo sajenti akamwambia Belinda yeye ndiye awe dereva kwa maana eneo la nje lilikuwa limezungukwa kila kona na watu wabaya, Belinda hakuwa na pingamizi. Sajenti akahamia siti ya dereva. Akaendesha gari mpaka eneo la nje kwa kasi huku akiacha bumbuwazi kwa kile kikosi cha TSFFT. “ Mnashangaa nini, mkamateni, ole wenu awapotee!” Sauti ya amri ikatolewa na moja ya viongozi wa lile genge, wakaingia kwenye magari yao upesiupesi na kuanza kulikimbiza gari alilokuwa Sajenti, lakini Sajenti alikuwa tayari amewaacha kwa umbali wa kutosha kuwatoroka, hawakumpata.

*********************************

Fernanda aliangukia katika shimo la maji taka, ambalo lilikuwa lina mtaro unaopeleka maji taka kuyamwaga baharini, harufu nzito ya uvundo wa maji yale ilimfanya ajihisi kutapika, ilikuwa harufu mbaya kama ya mzoga uliooza, giza tororo lilitisha nafsi yake, mwili wake ulikuwa upo katikati ya maji taka yale, yaliyokuwa yanatembea polepole sana, maumivu makali ya jeraha la risasi yalizidi kumlegeza na kumfanya ahisi nguvu kumuishia, ghafla alihisi yale maji taka yakipata nguvu na kuongeza, yakaanza kumsomba kama kikaragosi na kumpiga huku na huku katika kingo za ule mtaro wa chini kabisa ya ardhi, ndani ya dakika tano alihisi uzito wa maji ukiwa umebadilika, hakuwa anabebwa tena, alikuwa anaelea tuu bila kutokea juu wala kugusa chini, harufu mbaya pia ikaondoka, na maji yalikuwa ya chumvi, Fernanda akajua maji yale yameenda kummwaga bahari, akaanza kuogelea kuelekea juu mpaka alipotokea juu ya bahari, bado kulikuwa na giza, usiku ulikuwa haujaisha ingawaje kwa mbali mawingu yalikuwa yameanza kubadilika rangi na kuwa ya njano kwa mbali, hii ilimuambia kuwa yamebaki masaa machache kukuche.

Akaangaza macho yake huku na huku lakini kote alikuwa amezungukwa na maji, ni upande mmoja tuu alipokaza macho yake vizuri kutazama ndipo kwa mbali kama kilomita moja aliona ufukwe, alikuwa amechoka, licha ya kujaribu kuogelea lakini nguvu za kufika ufukweni zilimuishia, baridi na maumivu makali ya jeraha la risasi lilizidi kumnyong’onyesha, alihisi kichwa kizito, polepole akaanza kuzama baharini, mwishowe hakujua kilichoendelea.

****************

“ Hatuwezi kuishi na mtu tusiyemjua tena tuliyemkuta katika mazingira ya namna hii mume wangu, tukaripoti polisi kuwa tumemuokota ufukweni akiwa hajitambui, hii inaweza kuwa salama kwetu kuliko tukae na mtu tusiyemjua”

“ Ni kweli, lakini tusubiri azinduke kwanza, kwa vile tumeshamtapisha maji aliyokuwa ameyameza, haitachukua muda atazinduka tuu, umeshalikanda jeraha lake” Mzee Mpole akasema, huku wakiutazama mwili wa Fernanda pale chini kwenye mkeka.

“ Hili jeraha ni la risasi, sijui atakuwa amekumbwa na nini mtoto wa watu” Mke wa Mzee Mpole akasema, punde Fernanda akaamka akiwa amechoka, mwenye hofu; macho yake yakawa yanawatazama Mzee mpole na Mke wake kwa zamu, “ Ninyi ni kina nani?” “ Nipo wapi hapa” Akasema, Mzee Mpole na mke wake wakatazamana alafu wakamgeukia,

“ Mimi ni Mzee Mpole na huyu ni mke wangu, nilikuokota ufukweni leo asubuhi ukiwa hujitambui, ulikuwa kwenye hali mbaya sana, nikakuchukua nikakuleta kwangu, ndipo mke wangu akakubadili nguo baada ya mimi kukutapisha maji, kisha akalikanda jeraha lako, pole sana” Mzee Mpole akasema, kisha ukimya kidogo ukapita kisha, Fernanda akasema;

“ Hapa ni wapi?”

“ Hapa ni Kigamboni, Tuambie ni mkasa gani mbaya uliokutokea binti yetu?” Mke wa Mzee Mpole akasema,

“ Ni kisa kirefu sana Wazee wangu, naombeni nipumzike kwanza, nimechoka sana” Fernanda akjasema,

“ Mke wangu embu kampikia uji ashtue tumbo huenda ananjaa, akishakunywa atapata ahueni”

“ Kuna uji kidogo wa asubuhi ulibaki, ngoja nikakuletee” Mke wa Mzee mpole akatoka, Fernanda akawa anakumbuka usiku wa jana ulivyokuwa akakumbuka habari ya ile simu ya Meja Venance aliyoiweka mfukoni, Kabla hajasema kitu, Mzee Mpole akafungua kinywa chake; “ Nguo zako tumezifua zipo nje tumezianika, simu yako tumeiweka kabatini, nikakuletee?” Ni kama alikuwa ameyasoma mawazo ya Fernanda.

“ Hapana Mzee wangu, ila itakuwa imeharibika jamani simu yangu” Fernanda akasema, punde akatokea mke wa Mzee Mpole akiwa kabeba bakuli lenye uji,

“ Karibu sana, ila ni uji wa mhogo sijui kama uliwahi kuunywa” Mke wa mzee Mpole akasema huku akiachia tabasamu la ukarimu, Fernanda naye akaachia tabasamu kama kulipa hisani, Akaamka na kujikaza, akaketi na kunywa uji wa mhogo, angalau akapata nguvu na ahueni, sasa tatizo lilikuwa kwenye jeraha la risasi katika bega lake la kulia, maumivu ya ile risasi iliyokuwa ndani ya bega lake yalikuwa makali sana, “ hii risasi nitaitoaje hapa” Fernanda akawa anawaza lakini ghafla yule Mama akasema; “ Baadaye tutaenda kuripoti Polisi ili angalau tuwe salama, si unajua hatuwezi kukaa na mtu mgeni tuliyemuokota tena aliyepigwa risasi mwanangu!”

“ Ni kweli Mama” Fernanda akajibu kisha akaendelea; “ Lakini naomba twende kesho asubuhi tukiwa wote, kwa sasa kwa vile imeshafika mchana mnaonaje ikiwa kesho?”

“ Ni sawa Binti yangu” Mzee Mpole akasema, “ Afadhali, usiku wa leo nitatoroka hapa, sitaki polisi waingilie mambo haya, wala sitaki wanikamate na kunihoji hoji, hii itaharibu na kutibua mpango wangu” Fernanda aliwaza. Baadaye Fernanda akatoka nje kwenda msalani kwani choo kilikuwa ni cha nje, alilakiwa na minazi mingi pamoja na miti ya mikorosho, baada ya kujisaidia na kujihifadhi chooni, aliiona nyumba ya Mzee Mpole ikiwa nyumba ya tofali za kuchoma, yenye bati, ilikuwa kubwa ya vyumba vitatu na sebule, madirisha yake yalikuwa ya nondo ikiwa na eneo kubwa mfano wa shamba, hapakuwa na uzio, Fernanda akaangaza macho yake huku na huko akagundua nyumba za eneo zile zilikuwa zipo mbalimbali, yalikuwa makazi mapya, pakiwa kimya na upepo mzuri wa kuvutia, pia kulikuwa na miti ya kisamvu ambayo mihogo ilitoka kwayo, mazingira yale yalimvutia sana Fernanda kwani aliyachukulia kama sehemu salama kwake kwa muda ule ingawaje hakutaka kumuamini yeyote.

Jioni ikafika, baada ya chakula cha usiku Familia ya Mzee Mpole ilimuomba Fernanda asimulie kisa chake na majanga yaliyomkuta. Mzee Mpole alikuwa mzee wa makamo mwenye miaka kama sitini hivi, alikuwa akiishi na mke wake, jambo ambalo lilimfanya Fernanda atake kuuliza watoto wake wako wapi, “ Samahani Mzee Mpole, unaishi wewe pekee na mke wako, wengine wako wapi? Fernanda akauliza,

“ Wengine kina nani Mjukuu wangu?”

“ Wengine kama wajukuu, au watoto” Fernanda akasema,

“ Mimi na Mume wangu hatukubahatika kupata watoto, hivyo tupo kama unavyotuona, tangu tulipokutana miaka zaidi ya thalasini iliyopita mpaka leo tupo kama unavyotuona, Mume wangu ni Mvuvi, ni mwenyeji wa hapahapa Pwani, mimi mkewe ni mwenyeji wa Lindi, tunafurahia maisha yetu ingawaje hatukujaliwa watoto” Bibi Mpole akasema huku uso wake ukiwa umebadilika sana, ulikuwa na huzuni, alafu akaendelea,

“ Tulipokuwa vijana kama wewe jambo hili lilitusumbua sana, kukosa mtoto inauma na kufanya mtu achanganyikiwe, lakini baadaye tuliamua kukubaliana na hali zetu, huyu ndiye mtoto wangu wa kwanza, na ndiye Mume wangu, kisha baada ya Baba yangu kufariki yeye ndiye akabaki kama Baba kwangu, nami nikawa binti yake, Mke wake na Baada ya mama yake kufariki, nikawa Mama kwake, tuliamua hivyo na hivi ndivyo utuonavyo” Akasema lakini ghafla mlango ukagongwa, Fernanda akaogopa sana, ulikuwa usiku sana kama saa tatu hivi, kwa mazingira ya eneo lile saa moja tuu usiku kulikuwa ni giza na sio rahisi watu kugongeana milango,

“ Nani?” Mzee Mpole akasema, kisha tukasikia sauti ya kike kutokea upande wa nje ikisema;

“ Ni mimi Mjomba”

“ Belinda!” Mzee Mpole akasema baada ya kuitambua sauti ile, akaamka akaenda kufungua mlango, hapo Fernanda akamuona mwanamke mmoja akiwa mlangoni, ndiye huyo aliyeitwa Belinda,

“ Karibu Belinda, vipi usiku wote huu, kuna amani?” Mzee Mpole akasema,

“ Niko na Mgeni Mjomba, huko sio shwari” Belinda akasema, bado hofu iliendelea kuzisigina nyoyo zetu, Ghafla Fernanda alihisi kama macho yake yameona mazingaombwe, alishangaa kumuona Sajenti akitokea nyuma ya Belinda,

“ Otieno!” Fernanda akaita, wote yeye, pamoja na Sajenti wakabaki wanatazamana wakiwa hawaamini, walikuwa kama wanaota ndoto ya ajabu.

“ Fernanda unafanya nini hapa?” Sajenti akasema, Belinda, Mzee Mpole na mke wake wakawa wanawashangaa, walikuwa wametekewa kuona vijana wale wanajuana. Kwa upesi Fernanda akaamka na kumkimbilia Sajenti na kumkumbatia kwa nguvu sana huku akilia, wote wakalia, mioyo yao ilikuwa ikiteta kwa mitetemo mikuu. Sajenti akawa anampapasa Fernanda kwa miikono yake lakini ghafla Fernanda akapiga ukulele baada ya kutoneshwa jeraha lake la risasi.

“ Una nini, kuna tatizo gani Mpenzi?” Sajenti akasema kwa hamaki,

“ Kumbe sio tuu wanajuana bali ni wapenzi kabisa” Mzee Mpole akasema,

“ Nina jeraha begani, nilijeruhiwa na watu wabaya” Fernanda akasema, na kabla hajaendelea Sajenti akampa ishara asije akaendelea kusema, ndipo ukimya ukatokea, mzee mpole na mke wake wakawa wanatazama kwa mashaka,

“ Watu gani hao, embu tuambie binti” Mke wa Mzee mpole akauliza akiwa na woga,

“ Niliwaahidi nitawaambia kila kitu, imekuwa kheri Otieno amekuja itakuwa rahisi kuelezea”

“ Huyu mwanamke ni nani? Kumbe jina lako ni Otieno na sio Jacob. Wewe sio Mtanzania?” Belinda akauliza kwa sauti iliyochanganyika na hasira na wivu wa mapenzi,

“ Sivyo ufikiriavyo, wala sijakudanganya, haya mambo nitakuelezea utanielewa” Sajenti akasema,

“ Nikuelewe kwa kipi, mtu anakuita mpenzi unataka nikueleweje?” Belinda akasema, mara hii hasira zake zikiwa dhahiri usoni mwake.

“ Ulitaka aniite nani, eenhe! Mimi huyu ni mume wangu, ulitaka aniiteje?” Fernanda akaingilia huku akiwa anamsogelea tayari kumkabili Belinda, lakini Sajenti na Mzee Mpole wakaingilia ugomvi na kuwaamulia,

“ Mnataka mtuletee mabalaa usiku huu, nitawafukuza kwangu mkafanye upuuzi wenu huko, mnafikiri nyumba yangu ni uwanja wa fujo, pelekeni ujinga wenu huko” Mke wa Mzee Mpole akasema kwa ukali, wakatulia,

“ Embu kila mmoja aketi, Belinda kaa pale, Nawe kaa hapo(Fernanda), Otieno nisubiri nikakuletee kiti” Mzee Mpole akasema, akaenda kuchukua kiti chumbani na kurejea. Kisha baada ya wote kukaa na utulivu kutawala, mzee Mpole akasema,

“ Hakuna haja ya kugombana, magomvi hayana maana katika maisha,embu tujiulize tunagombania kitu gani, tuishi kwa upendo, tukikwazana tuonyane” Akameza mate kisha akaendelea; “ Haya Belinda tuambie Mbona usiku kama huu, kuna amani?”

“ Hakuna amani Mjomba” Belinda akajibu,

“ unamaana gani kusema hayo?” Mke wa mzee mpole akajibu,

“ Shangazi wee acha tuu, kama sio huyu, leo ningekuwa nimeshakuwa maiti” Belinda akasema huku akamtazama Sajenti, maneno hayo hayakuwa ya kawaida, yaliwatisha sana mzee mpole na mkewe, lakini kwa Fernanda hali ilikuwa tofauti, yeye hakutishwa kwa sababu kazi yake kila siku ilikuwa na matukio ya kutisha na kusisimua, kwa sasa alishazoea hekaheka za wahalifu.

“ Mzee Mpole umesikia, siku ya leo tangu asubuhi imekuwa mbaya kwetu, alianza huyu mwanamke uliyemuokota ufukweni, haya sasa kuna hawa waliokiponyoka kifo, hii maana yake ni nini kama sio kuwa mauti imetembelea nyumba yetu, nahisi harufu ya damu Mume wangu” Mke wa mzee mpole alisema huku machozi yakimlenga lenga, Mzee mpole akamzuia asiseme;

“ Hayo maneno yametokaje kinywani mwako Mke wangu, ulimi ni ufunguo wa uzima na mauti, kusema maneno ya kuzimu ni kuufungulia kifo mlango, je ni nani alikishinda kifo pale alipokifungulia mlango, kifo kikiingia kimeingia, wala hakuna awezaye kukizuia kufanya uharibifu, embu kemea kauli hiyo mke wangu” Mzee Mpole akasema akiwa anatazamana na Mkewe, naye mkewe alikuwa ameangalia chini angali hofu ikiwa imeshaukumbatia mwili wake.

“ Nimekifungulia kifo mlango mimi au wewe? Embu fikiria kumuokoa mtu aliyekiponyoka Kifo, ukaja ukamficha nyumbani kwako, alafu ukafikiri kuna mtu anaweza kujificha ili kifo kisimpate, alafu muda baadaye ukamuokoa na huyu, hivi Mpole tangu lini umekuwa mpokonya Mauti mateka wake, kama sio kutaka mauti ikuangamize”

“ Shangaza usiseme hivyo….” Belinda akamkatisha Mke wa Mzee Mpole,

“ Kelele! Usiseme lolote, kifo kipo nje kinawatafuta, nawe wapiga kelele ili kijue upo humu, sisi hatutaki kabisa kuingia katika uhasama na mauti, tafadhalini ondokeni, nasema ondokeni upesi!” Mke wa Mzee Mpole akasema, Kitambo kidogo kukawa kimya, alafu Mzee Mpole akasema,

“ Mimi kama kichwa cha hii familia nimeamua kuwa watalala kisha kesho asubuhi wataondoka, mke wangu embu kuwa na utu, usiku huu wataenda wapi, kwa sasa hakuna Daladala,” Ghafla Mke wa mzee mpole akaanza kulia, alilia kama mtoto mdogo, labda alikuwa amechanganyikiwa, kwa maana iliwahi kusemwa Hofu humfanya mtu mwendawazimu. Ndipo Mzee Mpole akamchukua mkewe akampeleka chumbani, baada ya dakika kumi akatoka akiwa pekeake,

“ Naomba msahau yaliyotokea, tuwieni radhi, muda umekwenda sana, tutaenda kulala, oooh! Nimesahau; kuna chakula kidogo kilibaki, ngoja nikalete mle kwanza nyie wageni mlioingia usiku”

“ Hapana Mjomba, sisi tumeshakula, tupo vizuri” Belinda akamkatiza Mzee Mpole,

“ Kweli? Sawa! Belinda utalala na Fernanda chumba kile pale, Otieno utalala chumba hiki, subirini nikawaletee mashuka” Mzee Mpole akatoka mbele yao akaenda chumbani, akaja na mashuka matatu, akawakabidhi kila mmoja shuka lake, kisha wakaagana, wakaenda kulala.

Chumba alichopewa Sajenti kilikuwa na ukubwa wa wastani, ndani yake kulikuwa na kitanda kikubwa cha kumtosha chenye godoro ambalo lililokuwa uchi pasipo shuka, pembeni kulikuwa na viroba vitatu vilivyojaa mahindi yaliyopukuchuliwa kwenye kona ya chumba, chini ya sakafu karibu na vile viroba vyenye mahindi kulikuwa na Madafu kama matano hivi pamoja na vipande vya mihogo, sakafu ilikuwa ya saruji, chumba kilikuwa na vumbi nah ii ilimaanisha kilikuwa hakijakaliwa na mtu siku nyingi, madirisha mawili ambayo Kanga ndizo zilikuwa zimetumika kama Mapazia, hakikuwa kimewekwa Dari ya ubao hivyo macho ya Sajenti aliona Bati moja kwa moja, kuta za chumba zilikuwa zimepakwa chokaa huku tandabui wakiwa wameweka makazi yake.

Hayo yote Sajenti hakuyahesabu kuwa kitu chochote, alishukuru kupata hifadhi, kulala ndani ya nyumba kwake ilikuwa kama pepo kwani nyakati zingine kazi yake ilimpelekea kulala mpaka nje kwenye misitu, vichana na mapori ya kutisha huku akiandamwa nyuma na mazimwi yanyonyayo damu. Akili ya Sajenti ilianza kurudisha kumbukumbu kuanzia pale alipofika kwenye nyumba ile, sura ya Fernanda ilimfanya aone kama yupo kwenye ndoto ya ajabu, “ Nini kilimpata Fernanda mpaka kufika hapa, vipi na lile jeraha” Akawaza, licha ya maswali yaliyokuwa yakimjia kama manyunyu ya mvua za mvuli lakini hayakufua dafu kuzima moto wa furaha aliyokuwa nayo kwa kukutana na Fernanda tena,

Kwa upande wa Fernanda, chumbani alikuwa akiwaza mambo yote yaliyotokea, alifurahi sana kumuona Sajenti, akataka kuamka na kumfuata Sajenti lakini akili yake ikamuonya asilete chokochoko kwenye nyumba za watu, msaada wa kuwahifadhi kwenye nyumba yao ulikuwa mkubwa na hawakustahili kutendewa mambo ya hiyana.

“ Nisamehe sana Fernanda, zilikuwa ni hasira tuu!” Belinda akaondoa ukimya katika chumba kile, Fernanda akaacha kuwaza na kumgeukia Belinda kwa maana walikuwa wamelala kwa kugeuziana migongo.

“ Usijali Belinda, mimi nimekusamehe, hata mimi nisamehe ikiwa nilikukosa muda ule”

“ Nimekusamehe Fernanda” Hapo wote wakatabasamu, urafiki ukamea tangu usiku ule, Baada ya ukimya mwingi kupita Belinda akasema;

“ Nawe ni Askari wa usalama wa nchi”

“ Mmmh! Kwa nini wauliza?” Fernanda akasema,

“ Hakuna kitu, nimeuliza tuu”

“ Umejuaje mimi ni Askari?”

“ Kwa sababu Jacob Warioba ni Jasusi” Belinda akasema huku akimdadisi Fernanda.

“ Unamaanisha Otieno?”

“ Ndio! Huyohuyo” Belinda akasema,

“ Wewe ulijuaje Otieno ni Jasusi? Au alikuambia?” Fernanda akasema, ndipo Belinda akamsimulia tangu siku ya kwanza Belinda alivyokutana na Sajenti kule kwenye jengo la SHDC, Akamsimulia matukio yote mpaka kunusurika kuuawa akaokolewa na Sajenti,

“ Baada ya kukimbia kule SHDC tukashauriana wapi tungekimbilia wapi, Sajenti alisema yeye hawezi kukimbia kwa sababu kuna kazi maalumu anatakiwa aimalizie, akaniambia kuwa anipeleke mkoani akanifiche mara moja kwa sababu watu wale waliomfuata ni watu hatari na ambao wanamtandao mkubwa wenye nguvu, baada ya kushauriana sana ndipo nikakumbuka kuna Mjomba wangu aishiye huku Kigamboni, ndiye huyu Mzee Mpole ambaye ni kaka yake ni Mama yangu, Licha ya kushauriana sana nikimshawishi Sajenti anilete huku lakini yeye alikataa katakata, hata hivyo kutokana na muda kuwa umeenda ndio tukakubaliana kuwa usiku wa leo tujifiche kwa mjomba kisha kesho yake ndio tuendelee na mpango wa kwenda huko mafichoni kwake anapopajua” Belinda akasema, akapiga mwayo mrefu kisha akaendelea;

“ Tulipohakikisha tumewachenga na kuwapoteza kabisa, tukarudi mpaka kivukoni, tukavuka, kisha Sajenti akaniambia tuliacha gari kwenye Gereji ambayo haikuwa mbali na hapa, ndio tukaliacha gari kule juu Kwa mzee Mchonga, tukatembea mpaka kufika hapa” akapiga mwayo tena, uso wake ulikuwa umechoka, usingizi ulikuwa umedhamiria kumshinda, hata hivyo Belinda naye alijitutumua kuushinda, akaendelea;

“ Ndipo tukakutana na wewe humu kwa mzee Mpole, sasa nawe utanieleza hadithi yako mpaka unafika hapa, ningependa uanze na aliyekupiga risasi” Belinda akamaliza huku akisubiri kwa hamu kubwa kuisikia simulizi ya Fernanda,

“ Watu wabaya walinifukuza, ubaya wakanifanyia wakitaka kuniua”

“ Hee! Wakuue bila sababu? Hata kama mtu ni mbaya sidhani anaweza kufanya jambo hilo” Belinda akasema akimkatisha Fernanda,

“ Mbaya hana sababu, hata hivyo hawa walikuwa na sababu ya kuuvunja moyo wangu, nimkose Mpenzi wangu, Otieno.” Fernanda akasema, alikuwa anadanganya,

“ Kwamba ni vita ya mapenzi?” Belinda akasema, akiwa amestaajabu,

“ Ndivyo waweza kuiita, lakini wala mimi sikuwa napigana na yeyote, wenye nguvu, wenye utajiri wao hufikiri kila kitu kizuri ni halali yao, sisi wanyonge na fukara wanatuona hatustahili vitu vizuri, wakataka kuniua ili wabaki na Otieno” Fernanda akasema, akiwa anazidi kuongopa, naye Belinda alikuwa karibu kumwamini.

“ Pole sana, sasa hiyo risasi begani ikawaje?” Belinda akasema, hapo Fernanda akaanza kujiliza, hakika alikuwa muigizaji mwenye kipaji cha hali ya juu, labda ungefikiri analia nini, hata yeye mwenyewe asingekuwa anajua kinachomliza; basi tuu ndivyo uongo ulivyo, mara nyingi hauna sababu.

“ Wakanipiga sana kabla, kisha baadae wakanitwanga risasi ya Bega, hapo nikadhani nimekufa kwani sikujua kilichotokea, kumbe nilikuwa nimepoteza tuu fahamu, na hayo yote Mzee Mpole aliniambia kuwa alinikuta Ufukweni nimetelekezwa nikiwa nimepoteza fahamu huku jeraha la risasi likitoa damu. Hivyo ndivyo ilivyokuwa ndugu yangu” Fernanda akamaliza kusimulia kisa cha uongo chenye hitimisho lenye ukweli, basi huyo Belinda alikuwa akitoa machozi wakati akisimuliwa, akamkumbatia na wote wakafarijiana, wote walikuwa wameichoka siku ile, hawakuta iendelee hivyo usingizi ukawachukua, wakalala.
inaendelea

Kitabu kipo Tayari, lIPIA Tsh, 15,000/= UJIPATIE NAKALA YAKO

0693322300
Robert Heriel
Airtelmoney
 
WAKALA WA SIRI Episode 07
Mtunzi; Robert Heriel
WhatsApp 0693322300

EPISODE 07

ILIPOISHIA...
“ Wakanipiga sana kabla, kisha baadae wakanitwanga risasi ya Bega, hapo nikadhani nimekufa kwani sikujua kilichotokea, kumbe nilikuwa nimepoteza tuu fahamu, na hayo yote Mzee Mpole aliniambia kuwa alinikuta Ufukweni nimetelekezwa nikiwa nimepoteza fahamu huku jeraha la risasi likitoa damu. Hivyo ndivyo ilivyokuwa ndugu yangu” Fernanda akamaliza kusimulia kisa cha uongo chenye hitimisho lenye ukweli, basi huyo Belinda alikuwa akitoa machozi wakati akisimuliwa, akamkumbatia na wote wakafarijiana, wote walikuwa wameichoka siku ile, hawakuta iendelee hivyo usingizi ukawachukua, wakalala.

ENDELE
A
Usiku ulizidi kunawiri kadiri masaa yalivyokuwa yanaenda, yapata saa nane giza likiwa linanguvu usoni pa nchi, hakuna aliyekuwa macho, kila mmoja alikuwa katika ndoto yake, hali ya mawingu ilizidi kuongeza sehemu ya giza katika usiku ule, usiku wenye kutisha huwa na vibweka, haukuwa usiku mzuri kwa Fernanda, alikuwa akihangaika kwa kujigeuza upande huu na upande huu kama mtu mwenye kuota ndoto mbaya, labda ni jeraha lake lilikuwa likimsumbua, baridi iliyokuwa ikiingia ikamfanya Fernanda aamke, maumivu kwenye bega lake la kulia ya lile jeraha la risasi aliyopigwa yalikuwa yakimsumbua, akaamka; bado Belinda alikuwa amelala, Fernanda akaamka na kuketi kitandani, kisha akajifunga kanga akatoka kwani alikuwa amebanwa na haja ndogo pia; akiwa amefika sebuleni alishtushwa na minong’ono iliyokuwa kwa nje kwenye dirisha la sebule, zilikuwa sauti za wanaume wawili waliokuwa wakizungumza kwa sauti ya chini kabisa, Akajongea polepole mpaka lilipokuwa dirisha, akafungua pazia kwa tahadhari. Alipigwa na butwaa alipomuona Mzee Mpole akiwa na wanaume wawili wenye miili mikakamavu; Fernanda akajua ni wale watu wanaomtafuta Sajenti; akawasikia wakisema;

“ Lakini mzee mwanzangu nawe unamakosa bhana! Unawezaje kupokea mtu aliyejeruhiwa kwa bastola ukamuweka ndani kwako, huoni hilo ni kosa” Mzee Mchonga akasema, lakini akakatishwa na mwanaume mmoja aliyekuja naye,

“ Hatutaki kukudhuru, ndio maana tumekuja na Mzee Mchonga hapa, ndiye aliyetuonyesha kwako, gari yao waliiacha kwenye Gereji yake, kama sio ile gari wala tusingejua kwa urahisi alikimbia huku kigamboni, samahani kwa usumbufu, amelala chumba kipi?” Yule mwanaume akasema, akiwa anamuambia Mzee Mpole.

“ Sawa nimewaelewa, kwa hiyo mnataka nifanyaje?” Mzee Mpole akasema, Fernanda aliposikia hivyo akasonya; “ Huyu mze ni mnafiki sana, kumbe katusaliti” Fernanda akawaza huku akisonga upesiupesi kuufuata mlango wa chumba cha Sajenti, taa zote zilikuwa zimezimwa hivyo kulikuwa na giza ingawaje taa za nje nuru yake ilifanya mule ndani kuwa na nuru angalau, Fernanda akamuamsha Sajenti, kisha wakatoka sajenti akiwa anafunga vifungo vya shati lake, bastola ikiwa kiunoni, walinyata mpaka sebuleni na kulifikia lile dirisha alipokuwa amesimama Fernanda hapo kabla, lakini walipochungua nje hawakuona mtu; Sajenti akamuambia Fernanda “ Labda ulikuwa kwenye ndoto” Lakini Fernanda akasisitiza kuwa yeye hakuwa anaota, mambo hayo yote waliyafanya kimya kimya bila kuharibu utulivu wa eneo lile.

Sajenti akiwa dirishani bado wanajibishana, akashtuka kuona kitu kama kivuli kwa nje kikipita kule ilipo miti ya mihogo, hapo akamtuliza Fernanda, akaangalia nje akiwa anachungulia kwenye pazia la lile dirisha lakini hakuona kitu, hata hivyo asingejiongopea kuwa macho yake hayakuona kitu, wakati akiwa anatafakari ghafla upande wa chini kabisa akaona wanaume wawili wenye silaha wakiwa wamejificha, kufikia hapo Sajenti akajua kuwa watu wabaya wamewafikia,

“ Tuondoke sasa hivi” Sajenti akasema huku akimshika mkono Fernanda akimvuta, mkono mwingine ukiitoa bastola yake mafichoni na kuikamata vizuri,

“ Sasa tunaenda wapi, mlango wakutokea ni huu tuu” Fernanda akasema, angalia akisema ghafla mlango ukafunguliwa na bila akili yao kujua chakufanya punde akatokea Mzee Mpole akifuatiwa na wanaume wawili wakiwa na silaha, Sajenti hakutaka kupoteza muda akawapiga wale wanaume risasi wakaanguka chini, Mzee Mpole akabaki amesimama kwa hofu akitetemeka,

“ Nisameheni! Tafadhalini msiniue! Sikuwa na namna!” Mzee mpole akawa anajitetea, lakini kabla hajamaliza wanaume wengine wawili walitokea, kitendo cha wanaume wale kuona wenzao wamekufa wakajificha na milio ya risasi ikarindima, vita imeanza. Mzee Mpole akapigwa risasi ya ubavu akaanguka chini, Sajenti na Fernanda walijua nini chakufanya kwenye mazingira kama hayo, kama mtu mmoja waliruka sarakasi na kujiviringa kama Gunzi la mhindi na kujificha huku wakijibu mapigo, Fernanda alikuwa amechukua Bastola ya moja ya wale wanaume wa mwanzoni waliouawa na Sajenti, milio ya risasi iliwaita wale majahili wengine waliokuwa wapo mbali, risasi zilirindima mpaka Mke wa Mzee Mpole na Belinda wakaamka, baada ya majibizano ya risasi kwa zaidi ya nusu saa, wale wanaume waliuawa na kutoa upenyo wa Sajenti na Fernanda kuwakimbia. Walipotelea kwenye miti ya mihogo na kutokomea kwenye giza wakiacha nyumba ya Mzee Mpole ikiwa imevamiwa na shetani mwenye kiu ya damu.

“ No! No! Hapana! Turudi!” Fernanda akasema, akiwa amesimama huku akitaka kurudi,

“ Unawazimu!” Sajenti akasema,

“ Kuna kitu muhimu nimesahau, ingekuwa bora ningekufa kuliko kukiacha kitu hicho”

“ Kitu gani hicho” Sajenti akasema, akiwa amemkatisha Fernanda

“ Simu!” Fernanda akajibu,

“ Simu gani nawe, embu twende, simu tutanunua mbele kwa mbele” Sajenti akasema,

‘ Utainunua simu ya Meja Venance?”

“ Umesemaje Fernanda?”

“ Nimeiacha simu ya Meja Venance” Fernanda akasema, na wote wakaanza kupiga hatua kurudi, hawakuchukua muda kwani hawakuwa wamefika mbali,

“ Wewe baki hapa, mimi ngoja nikaichukue, uliiweka wapi” Sajenti akasema,

“ Hapana, twende wote tuu, ni hatari wewe kwenda mwenyewe”

“ Embu nisikilize ninachokuambia” Sajenti akasema kwa sauti ya hasira,

“ Unaijua hata hiyo simu ilivyo, acha ubishi Otieno” Basi wakaenda wote, walipofika eneo bado lilikuwa kimya lenye kutisha, miili mitatu ilikuwa ipo nje kabisa ya nyumba, miwili ilikuwa mlangoni, wakafika mlangoni ghafla wakasikia sauti ya mwanaume akiwa anafoka, na mwanamke akiwa analia, wakajua aliyekuwa analia ni Belinda kutokana na sauti yake, wakaingia, kumbe walikuwa wanaume wawili wakiwa wamewaweka chini ya ulinzi Belinda pamoja na mke wa mzee mpole, piga nikupige zikaanza, adui wawili wakajificha katika chumba alichokuwa amelazwa Fernanda mchana ambacho ndicho chenye simu ya Meja Venance, mwingine akauawa palepale.

Kisha wale wanaume wakawa wanaongea na simu wakiwa wamejifungia kwenye kile chumba, walikuwa wakitoa maelekezo ya wapi walipo na wapo katika mapigano makali na Sajenti warioba, mazungumzo yao yaliwatahadharisha Sajenti na Fernanda kuwa muda mfupi ujao kikosi kingine kitawasili pale hivyo itawapasa wafanye upesi, Sajenti akawa anafikiria cha kufanya, muda nao ulikuwa ukienda,

“ Hutotukimbia Sajenti, mwisho wako umefika, umechokoza nyuki kwenye mzinga wake, sasa subiri kung’atwa” Mwanaume mmoja akasema akiwa chumbani,

“ Nilisema mauti imekuja mume wangu hukunisikia” Mke wa mzee Mpole alikuwa pale chini akiongea na Mume wake aliyekuwa anakoroma nusu ya kufa,

“ Sajenti! Wewe Sajenti unajifanya haunisikii, hahahah! Subiri tutazibua hayo masikio yako, wewe ni adui wa taifa, Iko wapi kadava, ipo wapi chipu na sampo ya uchunguzi?” Yule mwanaume akaendelea kusema,

“ Ssa tutafanyaje Otieno, tutaendelea kumsikiliza huyo mwehu akisema hayo, au tunawasubiri hao wanaokuja kutukamata?” Fernanda akasema, punde Sajenti akakumbuka jambo, akaingiza mkono mfukoni akatoa dawa Fulani kama panadol kisha akatoa kibiriti cha gesi na kuichoma ile dawa ilipoanza kuwa na kutoa moshi akairusha ndani ya kile chumba cha wale wanaume walikojificha, wale wanaume wakaanza kukohoa huku mmoja akijaribu kuzima ile dawa kwa kuikanyaga, kisha baada ya dakika tano kukatokea ukimya, Sajenti akauvunja ule mlango akaingia ndani na kuwakuta wale wanaume wamelala wanakoroma, ilikuwa dawa ya kulevya ya usingizi, Wakaichukua ile simu ya Meja Venance wakatoka wakiwa pamoja na Belinda,

Lakini kabla hawajafika mbali wakiwa wanapotelea kwenye miti ya mihogo, ndivyo huitwa mkisamvu, wale maadui walikuwa wameshafika na kuwakabila, tena wakati mmoja alipokuwa akimpiga risasi Sajenti ili amuue, ndipo Belinda akajitokeza na kukaa mbele ya Sajenti kama ngao na ile risasi ikampata yeye kifua badala ya Sajenti, papohapo Belinda akaanguka na kufa, lilikuwa tukio lenye kutisha na lililomsononesha sana Sajenti, Fernanda alimvuta Sajenti na kumwambia waondoke kwani Belinda ndio ameshakufa, wakaondoka wakikimbia huku midomo ya risasi yenye uchu ikiachama kuwameza, walitokea kwenye korongo ambapo ndani yake kulikuwa na mto mdogo wenye maji machache huku kukiwa na miti mikubwa na vichaka, walikuwa wakirusha risasi huku wakikimbia na kujificha kwenye miti kulifuata lile korongo, wakapandisha mpaka wakatokea kwenye muinuko ambao juu yake ilikuwepo uzio wa senyenge, wakavuta ile senyenge kwa chini wakapita na kuzama ndani ya lile eneo ambalo halikuwa na nyumba yoyote isipokuwa shamba kubwa lenye mihogo na minazi, Fernanda alikuwa amekimbia akawa amechoka, jeraha lake alikuwa amelichokoza, maumivu makali yalizidi kumpa kero, hata hivyo hakuwa na chaguo zaidi ya kuchagua kuyapuuza, lakini hakuweza kupuuza kuchoka kwake, pumzi ilikuwa imemuishia, walikuwa wamekimbia umbali mrefu sana,


SURA YA 7



“ Ninakupongeza sana Mr. Daniel kwa kazi nzuri unayoendelea kuifanya, sikukosea kukuweka katika nafasi hiyo, njia yetu ni nyeupe lakini inatupasa kuendelea kuhakikisha hakuna wakuvuruga mipango yetu, propaganda zinazoendelea mitandaoni, kwenye vyombo vya habari vinatuweka kwenye hatua nzuri zaidi, wafanyabiashara wakubwa karibu wote tumewaweka kwenye mbawa zetu, watu mashuhuri kama wanamuziki, waigizaji, pamoja na viongozi wakubwa wa kidini wapo upande wetu, kazi iliyobaki ni kufuatilia asitokee msaliti miongoni mwetu akatusaliti, mnajua adhabu ya wasaliti, nitamuua kwa mikono yangu mwenyewe” akameza mate kisha akaendelea “ Kuna mtu mwenye swali au neno lolote la kuongeza” Kisha mwanaume mwingine aliyekuwa kwenye kile Kikao cha siri akanyosha mkono, akaruhusiwa kuzungumza;

“ Mhe. Rais, nashukuru kwa kunipa hii nafasi, sikuwa na jambo kubwa la kusema isipokuwa ni huyu Askofu Joshua Kalima” Yule mtu akasema, Rais akamkatisha,

“ Askofu Joshua Dawa yake inachemka, nafikiri wiki hii tutakuwa tumemalizana, ingawaje nimemtuma mtu amshawishi kwa mara ya mwisho kuwa upande wetu kisha amchunguze yupo na akina nani,akikataa kuwa upande wetu basi hatutakuwa na namna itabidi kumuangamiza” Rais akasema,

“ Lakini Mhe. Rais unafahamu kabisa Askofu Joshua anawafuasi wengi, mbali na hivyo pia mashirika na taasisi kubwa za kimataifa hasa nchi za magharibi wapo nyuma yake, naona itakuwa hatari sana kama tukimmaliza, inaweza kutuletea shida katika kuiongoza serikali” Mr. Gombe akasema, huku watu wengine waliokuwa kwenye kile kikao wakionekana kukubaliana na asemacho,

“ Sikiliza Gombe, Askofu Joshua hana Dola sisi ndio wenye Dola, huna haja ya kumhofia, tunakila nyenzo ya kukabiliana naye, hawezi kututisha na kuwa kikwazo katika kutimiza mipango yetu, kama hatutamuua tupe pendekezo, tumfanye nini akae kimya” Rais akasema, Kilikuwa kikao cha siri chenye watu saba ambao wote walikuwa wanaume, kati yao alikuwepo mzee mmoja mwenye umri upatao miaka sitini na saba hivi, mzee huyu muda wote alikuwa kimya pasipo kusema jambo lolote, baada ya mjadala wa namna ya kukabiliana na Askofu Joshua kila mmoja akitoa wazo lake, yule mzee akakohoa kidogo kisha watu wote wakakaa kimya, na kumtazama,

“ Kuhusu Askofu Joshua niachieni mimi, ndani ya siku tatu nitaleta ripoti hapa, tunaweza kujadili agenda zingine” Yule mzee akasema, watu wote wakatabasamu huku Mhe. Rais akimtania Mzee yule, baada ya kukubaliana kuwa suala la Askofu Joshua litashughuliwa na Yule mzee, Mhe. Rais akaendelea kusema,

“ Mr. Gombe hakikisha mambo yote yanayoendelea kwenye kikundi cha Ambagon unanipa taarifa, zipo taarifa kuwa yule mwanamke komando kutoka taasisi zetu za siri za usalama, aitwaye Fernanda, aliyekuwa ametekwa na kikundi cha Ambagon akatoroka aliokotwa ufukweni huko kigamboni, taarifa zinasema kuwa anasimu ya Meja Venance ambayo aliitoa katika nyumba ya Meja Venance, Kundi la Ambagon linaitaka hiyo simu kwa hali na mali, kama mjuavyo Meja Venance kumbe alikuwa msaliti wetu akitoa siri zetu kwa kundi la Ambagon, baada ya kundi lao kugundua kuwa tumeshajua kuwa Meja Venance anatusaliti, ndipo akauawa” wakati anaongea hayo Mr. Gombe alikuwa kwenye lindi la mawazo, kichwani zilimjia kumbukumbu za siku ile Meja Venance alivyouawa, akakumbuka;

“ Hello Venance kwema” Mr. Gombe alikuwa anaongea na simu na Meja Venance kwenye simu, akiwa ndani ya gari,

“ Kwema Kaka, usalama upo maana simu za usiku sio kawaida” Meja Venance akasema akiwa simuni,

“ Sio kwema kaka, nipo njiani nakuja, dakika kama kumi nitakuwa hapo Mkuu”

“ Kivipi kaka, kuna tatizo gani?” Meja Venance akasema,

“ Nipo njiani, vumilia dakika chache nitakuwa hapo” Mr. Gombe akasema,

“ Wamegundua?”

“ Ungeniambia mapema kuwa nawe ni mshirika wa siri wa Ambagon, subiri nakuja” Mr. Gombe akasema. Akikatisha kwenye barabara inayoingia katika mtaa aliokuwa anaishi Meja Venance, ulikuwa usiku wa saa tano kuelekea saa sita za usiku.

“ Daah! Sasa itakuwaje Ndugu yangu, nimekwisha mimi Kaka” Meja Venance akasema,

“ Hakuna kitakachoharibika usihofu, mimi ni kama ndugu yako, urafiki wetu niwa kufa kupona, ndio maana nikakuambia subiri nipo hapa ndio nakatiza hii kona kuingia kwenye barabara ambayo ipo nyumba yenu.”

“ Subiri kidogo,” Meja Venance akasema akiwa amemkatisha Mr. Gombe,

“ Meja! Venance! Venance!” Mr. Gombe alikuwa akiita kwenye simu lakini hakuitikiwa, alishtuka kusikia milio ya risasi Kupitia simu yake, kisha akasikia na vishindo vya watu wakipigana, kwa haraka akaongeza mwendo wa gari na kwa vile hapakuwa mbali tokea pale alipokuwa haikumchukua dakika moja alikuwa amesimamisha gari mbele ya geti la nyumba ya Meja Venance. Akatoa bastola yake na kuishika mkononi akiwa kajiandaa, alafu akatoka ndani ya gari, akafungua geti akakuta lipo wazi, alipoingia ndani akakuta walinzi wawili waliokuwa kwenye sare wamekufa, akazidisha umakini zaidi, akasonga mpaka kwenye mlango wa ile nyumba, akasikilizia akakuta kuko kimya, akagusa kitasa polepole, mlango pia ulikuwa upo wazi, akaingia, sebule ilikuwa inagiza, akapita kuifuata korido ya kuelekea kwenye vyumba, akiwa ananyata akashtushwa na kelele za mwanamke anayejitahidi kupiga kelele lakini mdomo wake unazuiwa kisha akasikia sauti ya mwanaume ikifoka kumtisha na kumnyamazisha yule mwanamke, Mr. Gombe akajua huyo ni mke wa Venance aliyekuwa analia, upesiupesi kwa tahadhari akakaribia kwenye mlango wa chumba zilipokuwa zinatokea zile kelele, akaufungua polepole huku bastola ikiwa tayari mkononi mwake, akafungua mlango akapokelewa na chumba chenye mwanga ambacho kwa mbele ulikuwepo mlango mdogo kama wa choo na bafu, kisha mkono wa kulia kulikuwa na mlango wa chumba kingine, bado alikuwa anasikia kelele za mwanamke anayefumbwa mdomo, huku mikikimikiki ikiendelea, hiyo ilimuambia kuwa tukio la ubakaji lilikuwa linaendelea; akafungua mlango kwa upesi kama umeme kisha akapokelewa na taswira ya mwanaume mmoja aliyemlalia kwa juu mwanamke, akakimbia na kumpiga kichwani yule mwanaume na kitako cha bastola, muda wote alikuwa kavaa Gloves mikononi, Yule mwanaume akasimama lakini kabla hajafanya chochote akapigwa ngumi ya uso akapepesuka, Mr. Gombe akamtazama yule mwanaume akamtambua ni mtu kutoka kundi la Ambagon, akampiga risasi ya kichwa kabla hajaongea jambo lolote maana alikuwa anataka kuropoka, Mr. Gombe hakutaka Mke wa Meja Venance ayasikie maneno ya yule Mwanaume.

Mr. Gombe akiwa amesimama akipumua kama bata dume, akashtuka alipouona mwili wa Meja Venance ukiwa umelala sakafuni ukitoa damu nyingi zilizotapakaa karibu chumba kizima, huku akiwa na majeraha makubwa ya risasi, Mke wa Meja Venance akiwa amenusurika kubakwa alimkimbilia Mr. Gombe na kumkumbatia akiwa na kinguo chake kilaini cha kulalia. Akawa analia akiwa amekumbatiana na Gombe. Baada ya kumfariji sana, ndipo Gombe akamwambia Mke wa Meja;

“ Hapa sio salama tena, tuondoke nikupeleke kwangu. Mtoto yupo wapi?”

“ Yupo chumbani kwake” Mkewe Meja Akajibu,

“ Vaa tukamchukue tuondoke”

“ Usiku huu huu jamani!”

“ Sio usiku huuhuu, namaanisha sasa hivi” Gombe akasema, Basi Mkewe Venance akavaa kisha akaenda kumuamsha mtoto chumba kingine, mtoto alikuwa akimuuliza mama yake maswali lakini Mama yake alikuwa akimdanganya huku akijizuia asilie na kuficha huzuni usoni mwake, hata alipoulizwa alipo Baba yake, ndiye Meja Venance akadanganya pia kuwa ametoka ameitwa kazini, kutokana na kazi ya baba yake ilikuwa ni kawaida Baba yake kuondoka hata usiku hivyo hilo halikumpa wasiwasi mtoto.

Wakatoka nje lakini Gombe akawaomba wamsubiri aingie ndani kwani kuna jambo amesahau kulifanya, Gombe akaingia ndani, akaufuata mwili wa yule mwanaume muuaji, akampekua katika mifuko yake ya suruali, akakuta namba anayoijua fika ni ya kiongozi wa Ambagon, akaandika ujumbe usemao “ fanyeni haraka nimezidiwa, ingawa nimemuua” kisha akaituma. Baada ya hapo akatoka, akawachukua mke wa Meja Venance na binti yake, wakaingia ndani ya Gari la Mr. Gombe alilokuwa ameliegesha nje ya Geti la nyumba ya Meja Venance, wakaondoka.

Wakiwa njiani wakapishana na Gari ambayo Gombe alikuwa akiifahamu, alijua kabisa gari lile linaelekea kwa Meja Venance, kumbukumbu hizo za Mr. Gombe alizokuwa akiziwaza zilikatishwa na sauti ya Mhe. Rais katika kikao kile;

“ Mr. Gombe unawaza nini?” Mhe. Rais akasema,

“ ooh! Tupo pamoja Mkuu” Gombe akajibu.

“ Tuweni makini, hatutaki uzembe wowote katika shughuli zetu, mwezi ujao ni uchaguzi, nyote mnajua kuwa kushinda kwangu ni kushinda kwenu, kuanguka kwangu ni kuanguka kwenu, kama hamnielewi vizuri, jaribuni kufikiria miradi yenu mlioianzisha ambayo kama sio mimi kuwalinda ingekuwa imeshajifia, hamlipi kodi, na karibu tenda zote zile kubwa tunawapa ninyi na washirika wenu, Kwa mfano Mzee kibangu, kampuni lako la Ukandarasi na Uhandisi tumelipatia mara nyingi tenda ambazo zimekufanya kuwa na pesa nyingi mpaka kufikia hatua umeanzisha biashara za hoteli nchi za ulaya, sijui kama tunaelewana lakini” Mhe. Rais akasema,

“ Mbona tunaelewa sana Mkuu, wewe toa shaka, utashinda kwa kishindo awamu hii, hakuna aliyetayari kuwa masikini, tumeshaonja maji ya maiti hatutaki tena kuyaacha, utashinda, hapa tunachojadili sio kushinda kwako Mhe. Rais kwani hata washindani wetu wanajua wewe ndio utakayeshinda, tunachojadili hapa ni namna ya kuwashughulikia maadui zetu yasijetokea yale ya Meja Venance” Mzee Kibangu akasema, ndiye yule aliyesema aachiwe amshughulie Askofu Joshua.

“ Kesho nitakutana na Vyama vya upinzani mamluki kusudi watoe tamko kutuunga mkono, kuhusu vyombo vya habari wote wanaogopa hawawezi kutangaza habari za mahasimu wetu isipokuwa habari mbaya tuu” Mr. Danieli alisema,

“ Kuhusu masuala ya ulinzi na usalama kila kitu kipo sawa, adui zetu hawana mbinu za maana za kukushinda Mhe. Rais, tunachohangaika ni kuhakikisha tunamkamata Huyo mwanamke aliyekimbia na simu ya Meja Venance bila shaka simu hiyo itakuwa muhimu sana kwetu, maana ile siku tulikagua nyumba yote tukakuta simu moja tuu, hatukujua kuwa kuna simu nyingine sirini, lakini bado nina mashaka sana Mkuu, kuna kitu hakiko sawa!” Mkurugenzi wa idara ya usalama wa taifa alisema,

“ Kitu gani hiko” watu wote kama mtu mmoja wakasema,

“ Unajua ile picha ya tukio la ile siku bado kiusalama bado inaacha maswali mengi, embu fikiria tulipanga wote hapa sisi watu saba kasoro mmoja ambaye ndiye Meja Venance, tulipanga kwenda kumteka Meja Venance na kumhoji juu ya usaliti wake kisha tungemuua, lakini chakushangaza siku ile tumefika nyumbani kwa Meja tukakuta miili miwili ikiwa imeuawa kwa kupigwa risasi, Meja Venance akiwemo, maganda ya risasi yanaashiria zilitumika bastola tatu ingawaje miili ilikuwa miwili pale chini, baada ya uchunguzi ripoti ilipotoka yale maganda ya risasi yalionyesha kuwa bastola iliyotumika niya yule Mwanaume na nyingine bastola ya Meja ambazo zote tulizikuta palepale eneo la tukio, bastola ya tatu iliyotumika haikujulikana ipo wapi hii ilimaanisha alikuwepo mtu wa tatu” Akameza mate kisha akaendelea,

“ Jambo jingine ni kutojulikana alipo mke wa Meja Venance na binti yake, wazo la kusema yeye, yaani mke wa meja ndiye aliyefanya tukio lile la kikatili akaamua kutoroka, nakataa, nina wazo la kuwa ametekwa na mtu asiyejulikana, kwa sababu zifuatazo, eneo lile katika kile chumba kulikuwa na nyayo za viatu zilizokanyaga damu ambazo zilikuwa tofauti kabisa na viatu vya yule mwanaume aliyeuawa pamoja na Meja Venance, vipimo vyake vilikuwa inchi kumi na moja kasoro hii ilimaanisha alikuwa mwanaume mwenye urefu wa kati, pia tulipoishika ile simu ya yule mwanaume ambayo ilikuwa kifuani mwake jambo hilo lilitupa picha kwamba, kuna mtu aliyemuweka ile simu kifuani, isingewezekana simu kukaa kifuani kwa jinsi alivyokuwa amelala, yaani apigwe risasi ya kichwa aanguke chini alafu simu ikae kifuani, hapana kijasusi hiyo inaashiria kuwa kuna mtu alimuwekea simu hiyo kifuani, kama hiyo haitoshi;” Akakohoa kidogo kisha akaendelea;

“ Ile simu tulipoifungua tulikuta ujumbe uliotoka kuandikwa dakika chache tuu zilizopita tangu tulipofika pale, muuaji wa yule mwanaume bila shaka hakumuua Meja Venance, ila inaonyesha yule mwanaume ndiye aliyemuua Meja Venance kisha baadaye akataka kumbaka Mke wa Meja kutokana na namna kitanda tulivyokikuta kilikuwa kimevurugika sana, na mashuka yake yaliyokuwa na nyayo za damu za yule mwanaume, pia mashuka yalikuwa na harufu ya manukato ya yule Mwanaume iliyochanganyikana na marashi ya mwanamke, hata tulivyonusa nguo za yule mwanaume aliyeuawa alikuwa akinukia marashi ya kike yanayofanana na marashi ya kwenye mashuka ambayo bila shaka ni marashi ya mke wa Meja, kisha aliyemuua yule mwanaume akatokea na kumuua yule mwanaume, alafu baada ya kumuua ndio wakaamua kuandika ujumbe kisha kumuweka simu juu yake, Muuaji aliyemuua mwanaume aliyemuua Meja Venance lazima atakuwa anajua kundi hilo la Ambagon au ni mwanachama wa kikundi hicho, lakini najiuliza, kama ni mwanachama wa kikundi hicho iweje wamuue mwenzao? Na kama sio mwanachama, alijuaje namba zile ambazo hata sisi tunazijua nizakiongozi wa Ambagon ambaye mpaka leo tunahangaika kumtafuta?” Hapo akanyamaza, wote walikuwa wakitafakari maneno hayo, Mr. Gombe alikuwa kimya huku hofu ikitembea katika mishipa yake ya damu, yeye ndiye aliyeshuhudia tukio lile, naye ndiye aliyeichukua familia ya Meja Venance na kuihifadhi nyumbani kwake.

“ Nguo ya kulalia ya Mke wa Venance tuliikuta juu ya kitanda, hii ilimaanisha alibadili ndio akaondoka kutokana na kuwa ilikuwa juu ya zile nyayo za damu za viatu vya yule mwanaume. Jambo la mwisho ni kuhusu Marashi na manukato ya ile simu, tulipoinusa ile simu ilikuwa na marashi yenye harufu tofauti na harufu ya Yule mwanaume aliyeuawa, pia ilikuwa tofauti na harufu ya marashi ya Meja Venance pamoja na harufu za marashi ya mke wa meja kwani tuliangalia vipodozi vyake hatukuona hata kipodozi kimoja chenye harufu kama ile, harufu ya manukato yale hutumiwa na wanaume zaidi hasa watu wazima wa kuanzia miaka arobaini wenye vipato vikubwa, hii ni kusema muuaji wa Meja Venance hakuwa kijana mdogo au mtu mwenye uchumi wa kawaida au uchumi wa chini, lazima atakuwa mtu mzima mwenye kipato kinachoeleweka. Huyu aliyemteka mke wa Meja Venance ndiye ananipa mashaka, lazima mkewe Venance atakuwa anafahamiana naye, wasiwasi wangu isijekuwa yupo kati yetu hapa” Mkurugenzi wa Idara ya Taifa akanyamaza, kisha akawa anawaangalia wanakikao kwa zamu, alipofika kwenye uso wa Mr. Gombe akatulia kwa kitambo, jambo ambalo Gombe lilimshtua sana ingawaje alijikaza kuficha hila yake ili asigundulike kuwa ndiye yeye aliyefanya hayo, “ Sikuwa mjinga, nilibadili kutumia marashi na mafuta yale tangu nilipofanya tukio lile, nilijua kuwa haya yangeweza kutokea” Mr. Gombe akawaza. Lakini akiwa anawaza ghafla moyo wake uliingia baridi baada ya Mkurugenzi wa Idara ya usalama wa taifa kusema;

“ Yale marashi niliwahi kuyasikia kwenye vikao vyetu, sikumbuki vizuri ni nani alikuwa anayatumia, ila nina mashaka makubwa mtumiaji wa marashi yale anaukaribu wa kile kilichotokea siku ile”

“ Rafiki yake Meja Venance ni nani hapa kama sio Mr. Gombe?’ Mwanaume mmoja mfupi mwenye upara na kitambi akasema, hapo kila mtu akamtazama Mr. Gombe, lakini Mhe. Rais akamtetea, Mhe. Rais alikuwa akimuamini sana Mr. Gombe kutokana na mishemishe alizokuwa anafanya naye.

“ Tuachana na jambo hilo, hiyo simu ya Meja Venance hakikisha inapatikana, kumbukeni yeye ndiye aliyekuwa katibu na muweka kumbukumbu za vikao vyetu hapa, huyo mwanamke akamatwe ndani ya masaa arobaini na nane, na huyo Sajenti, lakini Mr. Lusingi hawa si vijana wako kabisa, iweje watusumbue hivi?” Rais akasema,

“ Mhe. Rais ni kweli kabisa hawa ni vijana wangu, wote ni wanakitengo katika usalama wa Taifa letu, tatizo lao wao wanapenda sana haki, kimsingi wao ni wanauzalendo uliopitiliza kwa taifa lao” Mr. Lusingi ambaye ndiye Mkurugenzi wa Idara ya usalama wa Taifa akasema, hapohapo akakatishwa,

“ Unamaanisha sisi sio wazalendo?” Mhe. Rais akasema, kisha wote wakacheka,

“ Mhe. Rais, wala hatuna haja ya kujadiliana na mambo hayo, kila mmoja anajua ukweli moyoni mwake kuwa sisi ni wazalendo au wachumia tumbo tukilinyonya taifa hili, tutahangaika kuwatafuta hawa watu, hawawezi kutukimbia, ingawaje jambo hili tunalifanya kwa siri kwa sababu wanausalama wengine wanawajua Sajenti na Fernanda kama Wazalendo, hivyo hatutawahusisha kwa lolote, hatutaki pia waangukie katika mikono ya Polisi, ni bora wakamatwe na hilo kundi la Ambagon, jambo moja la uhakika ni kuwa Sajenti Warioba anaujuzi na uzoefu mkubwa sana wa kijeshi, kiulinzi na kijasusi, hivyo lazima tuwe makini” Mr. Lusingi akasema,

“ Hahahaha! Serikali haiwezi ogopa kinyago ilichokichonga yenyewe, huyo Sajenti ni Mende tuu kwenye kinyesi” Mhe. Rais akasema,

“ Lakini Mhe. Rais, Bwana, Kinyunumba tambua tunachokifanya watu wengi hawakijui, na kama siku wakijua kuwa tupo kwa ajili ya maslahi yetu na wala sio maslahi ya taifa, hawatatuunga mkono, fikiria wafanyakazi wa umma mishahara yao ilivyomidogo, jeshi la polisi watumishi wake nao hivyohivyo, makazi yao duni, mishahara ya bei ya mkaa, hata hilo jeshi halitatusapoti Mhe. Rais, kusema Sajenti hawezi kushindana na Serikali tutakuwa tunajidanganya, yeye hashindani na serikali bali anashindana na wahujumu uchumi na wachumia matumbo” Mr. Lusingi akasema,

“ Kwa hiyo unataka kusema nini, au upo pamoja naye? Unabishana na mimi?” Rais Kinyunumba akasema,

“ Hapana Mkuu, sibishani na wala sina ubavu wakukuzuilia neno lolote”

“ Basi nawataka hao wadudu ndani ya masaa ishirini na nne. Wawe hapa ima wangali hao au mizoga yao, kikao kimefungwa” Rais Kinyunumba akasema, akiwa ameghadhibika,

Kikao cha Siri kiliisha, wanakikao wakaondoka kila mmoja akipanda gari lake kuelekea nyumbani kwake, huku Rais akirejea Ikulu.

INAENDELEA
Kitabu kipo Tayari, lIPIA Tsh, 15,000/= UJIPATIE NAKALA YAKO

0693322300
Robert Heriel
Airtelmoney
 
WAKALA WA SIRI Episode 08
Mtunzi; Robert Heriel
WhatsApp 0693322300
EPISODE 08

ILIPOISHIA.

“ Kwa hiyo unataka kusema nini, au upo pamoja naye? Unabishana na mimi?” Rais Kinyunumba akasema,
“ Hapana Mkuu, sibishani na wala sina ubavu wakukuzuilia neno lolote”
“ Basi nawataka hao wadudu ndani ya masaa ishirini na nne. Wawe hapa ima wangali hao au mizoga yao, kikao kimefungwa” Rais Kinyunumba akasema, akiwa ameghadhibika,
Kikao cha Siri kiliisha, wanakikao wakaondoka kila mmoja akipanda gari lake kuelekea nyumbani kwake, huku Rais akirejea Ikulu.

ENDELEA


Umati mkubwa wa watu ulikuwa umekusanyika kwenye sehemu ya kuuzia magazeti kama ilivyodesturi kwa nyakati za asubuhi maeneo ya mitaa ya jiji la Dar, wengi wao walikuwa ni wanaume wenye umri wa kati, wachache wakiwa wazee. Habari kubwa iliyogonga vichwa vya habari vya magazeti karibu yote ilikuwa habari ya viongozi watatu wa vyama vitatu vya upinzani kumuunga mkono Rais Kinyunumba ambaye anawania kiti cha urais kwa awamu ya pili, “KINYUNUMBA TUTAWEZANA!” moja ya magazeti liliandika, likiwa na habari picha, kuwaonyesha viongozi watatu wa upinzani wakiwa kwenye picha ya pamoja, “ SOLOMON SHIMONI, WENZAKE WAMFUKIA!” Gazeti jingine liliandika likiwa linapicha ya Solomon Ngazi akiwa ameshika Tama! Ndiye mgombea wa kiti cha Urais katika chama kikuu cha upinzani anayemnyima usingizi Rais Kinyunumba. Magazeti mengine yalichora picha za katuni yakimdhihaki Mr. Solomon huku yakimsifia na kumpongeza Rais Kinyunumba,

Gazeti jingine likaandika;” KINYUNUMBA SHUJAA WETU”

“ Hakuna shujaa, uongo na ulafi wa mali za umma ndio ushajaa! Mtu akila haridhiki bado anataka kula tena na tena, imetosha sasa jamani! Hakuna lolote lililofanyika kwenye nchi hii zaidi ya watu wachache kujineemesha wao na familia zao” Kijana mmoja alisema, jambo hilo likazua mjadala,

“ Hakuna kilichofanyika? Wewe Kijana embu chunga mdomo wako, wanasema mdomo uliponza kichwa” Mzee mwenye mvi aliyekuwa karibu na Yule kijana akamkaripia sana yule kijana,

“ Mnatuziba mdomo tusile wala tuseme, tumechoka sasa! Mnatutisha, mnatunyamazisha ili nyie mle wenyewe, tukipaza sauti zetu mnasema mdomo uliponza kichwa. Tumechoka sisi!” Yule kijana akasema,

“ Usiseme tumechoka; sema umechoka kwa nafsi zako, ninyi vijana wa siku hizi mnapenda mambo rahisi sana, kazi hamtaki, mnakalia kupiga soga vijiweni, Acheni Kinyunumba alete maendeleo, hamjui nchi ilipotoka, mmeikuta inabarabara, shule, hospitali, umeme, maji, watu wanaishi kwa amani, kama mngezaliwa wakati wetu labda mngeona maendeleo yaliyoletwa na serikali” Mzee akasema, minong’ono ya chini chini ikaendelea wengine wakimpinga Yule mzee huku wengine wakiungana naye,

“ Hayo yaliyofanyika hayawapi uhalali viongozi kuwa mafisadi na wahujumu uchumi wa nchi hii, embu angalia vijana wa nchi hii walivyokata tamaa, sio ajabu hata wajukuu au watoto wako hali zao ni ngumu na bado wewe unaona hiyo ni sawa, uliwahi kufika kwenye hizo hospitali ukaona kinachoendelea, vipi huko shuleni nako ulienda kuona jinsi watoto wanavyosoma kwa taabu, hakuna vitabu, hakuna waalimu wa kutosha, na zile shule zinazotosha waalimu bado hawalipwi maslahi vizuri, hao Madaktari na wahudumu wa afya uliwahi hata kuuliza changamoto zao? Vipi huko mahakamani, kuna mahakama ngapi hapa nchini za kuhakikisha haki inatendeka, uhaba wa mahakama na serikali kushindwa kuajiri mahakimu na majaji wengi huoni kama inarudisha maendeleo ya jamii!” Yule kijana akawa anaongea kwa uchungu kiasi cha kushindwa kujizuia, akameza mate kisha akaendelea;

“ Pamoja na mambo yote hayo bado viongozi wanatuibia, wanajilimbikizia mabilioni ya pesa bila kuhurumia wananchi, wanawanyonya wananchi, mwaka huu tutaona” Wakati anaongea hivyo wakatokea wanaume wawili wakamkamata yule kijana,”Niachieni! Ninyi ni kina nani? Nimesema niachieni nyie mbwa mwitu!” Yule kijana akawa anapiga kelele lakini hakuonekana wakumtetea, watu wote waliokuwa eneo lile la kununulia magazeti na wapita njia walikuwa wakimshangaa badala ya kumsaidia,

“ Nisaidieni ndugu zangu, hawa watu sio watu wazuri, kosa langu lipi, nimefanya nini mpaka mnibebe kama kikaragosi, nisaidieni enyi watu” Yule kijana aliendelea kulalamika huku akibebwa mpaka alipoingizwa ndani ya Gari lenye vioo nyeusi, akasombwa kusiko julikana, yule mzee akasema; “ Asiyefunza na mamaye hufunzwa na ulimwengu; kijana hana adabu kabisa, anajifanya mjuaji, sasa ngoja wakamshone mdomo” Minong’ono ikazuka tena wengi wakimuunga mkono yule mzee hata kama ni unafiki basi ilimradi kujihakikishia usalama. Wachache walionyesha sana kutokubaliana na tukio lile, kwao waliliona kama unyanyasaji wa raia na kuwanyima haki ya uhuru wa kujieleza, waliuchukulia kama utumwa ndani ya nchi yao wenyewe. Hata hivyo woga wa swala mbugani humfanya kuonewa na kila mnyama porini, na nyati aliyejasiri ndiye hutangulia kuwa kitoweo cha simba, umoja ni nguvu kama wanyonge wangelijua hilo wangeungana kukabiliana na mateso wayapatayo kutoka kwa viongozi wachumia tumbo.

Habari hiyo ikamfikia Solomoni, ikamuumiza sana, Solomoni alikuwa mtu mwenye kupenda haki sana, hakupenda kuona mtu yeyote aonewa, jambo hilo likamfanya azidi kupendwa ndani ya jamii yake hasa katika jiji la Dar na miji mikubwa, na wale wenye kutumia simu zenye kuwawezesha kupata habari mtandaoni, jambo hilo ndilo lilimtisha sana Rais Kinyunumba, kukamatwa kwa yule kijana na kupelekwa kusikojulikana ilizidi kuchochea na kuisimika sera ya uhuru na haki kwa wote aliyokuwa nayo Mr. Solomoni. Alichukua simu yake kisha akaandika Kupitia ukurasa wake wa mtandaoni, “ Free Dotto Ukucha, serikali ya Mr. Kinyunumba bado inakiuka kwa makusudi haki na uhuru wa raia wake, tunataka haki kwa Dotto Ukucha itendeke, mnateka vijana masikini bila kujali wanafamilia zinazowategemea, huo udhalimu lazima mlipie” Ujumbe huo ulipata wachangiaji wengi sana, wengi wao walionyesha kusikitishwa na tukio hilo la kutekwa kwa kijana, Dotto ambaye kazi yake ilikuwa Kupaka kucha warembo, lakini watoa maoni wachache walimkejeli Mr. Solomon na kumuambia yeye ni mzushi na muongo, wengine wakamuambia yeye ndiye aliyemteka basi kila mtu na mawazo yake.

Siku mbili zilizofuata Dotto alipatikana lakini jeshi la polisi likiwa mbele ya vyombo vya habari likasema kuwa linamshikilia Dotto Ukucha kwa Kosa la kujihusisha na biashara ya madawa ya kulevya, luninga zilimuonyesha Mkuu wa jeshi la polisi mkoa wa Dar akiwa na kete za Heroine pamoja na bangi ambazo alisema zimekutwa katika nyumba aliyokuwa akiishi Dotto Ukucha,

“ Vijana fanyeni kazi halali, acheni kupenda njia za mkato, mtajiingiza katika matatizo, oneni huyu mwenzenu, Dotto sijui Ukucha gani; arobaini yake imefika, ukimuona unaweza usimdhanie lakini ndio hivyo tena, niwaombe viongozi wa siasa waache kuingilia majukumu yasiyowahusu, masuala ya ulinzi na usalama sisi jeshi la polisi ndio wenye dhamana, sasa mtu tena mwenye kuwania nafasi kubwa kabisa kuropoka mambo bila kujua ABC zake ni aibu, haya sasa ataweka wapi uso wake, anasema Dotto katekwa, wakati jeshi la polisi lilikuwa limemshikilia kwa ajili ya kufanya uchunguzi, mnataka kila mtu akikamatwa na polisi kwa ajili ya uchunguzi tutangaze? Huo sio utaratibu wetu, Dotto mwenyewe ameshakiri kuwa anajihusisha na biashara hiyo chafu, na kataja baadhi ya watu anaofanya nao kazi, tumeshafungua jalada mahakamani, jumatatu ijayo kesi itasikilizwa” Kamanda mkuu wa Polisi akamaliza kusema,

“ Kabambikwa! Kabambikwa! Free Dotto ukucha” Mitandaoni kulichafuka maneno hayo, watu wengi hasa wasomi na wale wachambuzi wa mambo walijua fika kuwa Dotto Ukucha amesingiziwa, hilo lilikuwa onyo kwa vijana wengine wasiwe viroporopo, Mr. Solomoni kwa kujua kuwa jambo hilo linaweza kuwaogopesha vijana wengine wenye muamko wa mabadiliko katika nchi yao, akaamua kujirekodi Kupitia simu yake, akisaidiwa na wasadizi wake, akasema;

“ Kama hatutatumia nguvu kama wanayotumia wao basi watatushinda, Kama hatutatumia akili na maarifa kama wanayoyatumia wao; watatushinda, na kama hatutakuwa wamoja, mashujaa na jasiri kuwashinda basi watatumaliza na jitihada zetu zitakuwa ni bure. Dotto Ukucha ni shujaa, hata wakijaribu kumchafua watachafuka wao, hilo halitasimamisha harakati zetu. Vijana ninyi ndio nguvu ya nchi, kama watatudharau tukiwa vijana tungali tuna nguvu hii inamaanisha nini siku tukiwa wazee? Eenhe! Embu tufikiri kwa umakini, Kukamatwa kwa Dotto Ukucha na kupewa kesi za hovyohovyo ni muendelezo wa tabia za kinyama walizo nazo viongozi walioko madarakani, huyo anayejiita shujaa, huo ushujaa ndio wakubambikia watu makesi ya mchongo, wakati umefika, tumuambia Kinyunumba, BASI! Kama tunataka Nuru ya nchi hii yatupasa kuwapa viongozi wapenda haki sio hawa majinamizi wala nyama za watu, Nuru! Tumaini, na hatma bora njema ipo mikononi mwenu Watanzania endapo tutaikataa serikali ya kidhalimu, tumkatae Kinyunumba na genge lake, Wiki ijayo ndio uchaguzi, tayari mnajua chakufanya, wakati wa nchi kutoka Gizani kuelekea Nuruni ndio sasa, UHURU NA HAKI KWA WOTE; NURU KWA NCHI YETU” Ahsanteni!”

Ilikuwa ni video fupi yenye maneno mazito yaliyotolewa kwa uchungu na Solomoni, mitandao yote ilisambaa, karibu kila mtu aliisikia, tumaini jipya labda lilizaliwa lakini kumbe ni mche wa unyasi juu ya mwamba mgumu.

*************

“ Mhe. Rais, Mkuu, mambo sio mambo huku!” Mzee Kibangu alikuwa akiongea na simu akiwa na wasiwasi mwingi.

“ Kuna nini Injinia, embu tulia uongee kwa utulivu ueleweke” Rais Kinyunumba akasema,

“ Askofu Joshua!”

“ Kafanyaje?” Rais Kinyunumba akasema, mara hii akiwa ameingiwa na mashaka.

“ Daah! Siwezi kuamini nilichokiona” Mzee kibangu akasema,

“ Kwani umeona nini Mzee, mbona hueleweki, usiniletee utoto, Sawa!” Rais Kinyunumba akasema,

“ Askofu Joshua ameuawa!”

“ Ameuawa!” Rais akasema kwa mshangao.

“ Nimekuta amechinjwa na kukatwa katwa kwa mapanga”

“ Hii haiwezekani! Unauhakika lakini isijekuwa umechanganyikiwa Injinia”

“ Mhe. Rais, wala sijachanganyikiwa, nimeona kwa macho yangu, hapa nilipo nimesimama kwenye sebule ya nyumba ya Askofu Joshua mwili wake ukiwa mbele yangu ukiwa umeharibiwa vibaya sana” Mzee Kibangu alisema akiwa ananong’ona,

“ Ondoka hapo upesi kabla haujakutwa hapo ikawa shida, fanya upesi” Rais akasema, lakini akiwa anaongea ghafla Mzee Kibangu akasikia kitasa cha mlango wa sebule ukifunguliwa na mtu aliyenje. Akageuka kuutazama, mlango ukafunguka akatokea kijana wa kiume aliyekuwa amebeba Mfuko ambao ndani yake kulikuwa na chupa yenye maziwa mtindi, Yule kijana alishtuka kuuona mwil wa Askofu Joshua uliojeruhiwa ukiwa mbali na uhai, akiwa katekewa, Mzee Kibangu akasema;

“ Usipige kelele, tulia hivyohivyo” Alikuwa akimwambia yule kijana huku akiwa tayari ametoa Bastola yake.

“ Injinia! Injinia! Nini tena hiyo?’ Rais akasema akiwa kwenye simu, simu ilikuwa bado hewani,

“ Mhe. Rais kuna kijana kanikuta humu” Mr. Kibangu akasema huku akimtazama Yule kijana kwa macho ya kumuonya asijekuleta ujanja wowote.

“ Ooh! Naona mambo yanataka kuwa mengi, Unajua chakufanya” Rais akasema, kisha kukawa kimya kwa kitambo alafu akasema tena; “ nitakupigia kesho alfajiri mapema kabisa” Simu ikakatika.

“ Tafadhali Mzee wangu, naomba usiniue!” Yule kijana akasema, akiwa anatetemeka kwa wasiwasi. Mzee Kibangu hakumjibu, akawa anamfuata polepole huku akiwa kamuelekezea yule kijana bastola,

“ Nakusihi Mzee wangu, nakuomba tafadhali”

“ Nisamehe sana Kijana, sina namna zaidi ya kukunyamazisha milele” Mr. Kibangu akasema, huku akivuta kilimi cha bastola.

“ Rais ndiye kakutuma kumuua Askofu Joshua?” Yule kijana akasema.

“ Nilikuambia sina jinsi lazima nikuue, Rais hahusiki na Mauaji haya lakini kwa vile ni ngumu kwako kuamini, mpaka nikikuua ndio utaamini na kujua aliyemuua Askofu wako, ukifika Kuzimu utamuuliza hilo swali kuwa nani aliyemuua, mimi siwezi kukujibu” Mzee Kibangu akasema,

“ Subiri kidogo!” “ Paaah!” akapigwa risasi akadondoka chini kama kiroba cha mahindi. Damu zikatapakaa sakafuni; uhai ukiwa mbali na kiwiliwili chake. Mzee Kibangu akatoka kinyemela katika sebule ile, nje kulikuwa na giza kwani ilikuwa usiku wa saa mbili kasoro, akatoka getini kisha akaenda mahali alipokuwa amepaki gari yake akapanda na kuondoka zake.

“ Nani aliyemuua Askofu Joshua” Mzee Kibangu akawaza akiwa ndani ya gari akielekea nyumbani kwake, Askofu Joshua alikuwa akiishi maeneo ya Kimara Korogwe, baada ya Mzee Kibangu kutokea Morogoro Road akachukua uelekeo wa Ubungo, “ Nani aliyetumwa na Rais amalizane na Askofu Joshua, mbona akili yangu inanituma kuwa Rais Kinyunumba anahusika na kisa hiki” Mzee Kibangu bado alikuwa akiwaza, tayari alikuwa amefika Ubungo akakata kushoto kuchukua uelekeo wa Mwenge, mawazo mengi yalikuwa yakizonga kichwa chake, kuna wakati alikuwa akijilaumu kwa kiherehere chake cha kumwambia Rais kuwa suala la Askofu Joshua aachiwe yeye, akili yake ilimwambia kuwa amekuwa mjinga kujiingiza kwenye mtego mbaya sana. “ Lakini hakuna kibaya ambacho kitatokea, nipo upande mmoja na mshika makali ya msumeno, nani ataweza kushindana nasi, mimi na Kinyunumba ni washirika” Mzee Kibangu akawaza, kisha alipokumbuka hivyo akatabasamu na kutoa sigara yake na kuitia moto, kisha akaiweka mdomoni, hapo alikuwa keshafika maeneo ya Mwenge kwenye mataa akielekea Nyumbani kwake Kawe. Alipofika nyumbani kwake alimkuta mke wake, Bibi Kibangu akiwa anamsubiri sebuleni huku akiangalia Luninga, kitendo cha yeye kufungua tuu mlango kilimfanya Bi. Kibangu, mkewe kupiga kelele;” Mzee Kibangu, Askofu Joshua amekufa, tazama habari za hivi punde, yaani wakati unaingia tuu ndio wametangaza, jamani! Jamani! Kijana wa watu, nani kafanya haya lakini” Bi. Kibangu alikuwa akisema sema huku akishtushwa na taarifa za kifo cha Askofu Joshua ambacho kilikuwa kinatangazwa muda ule kwenye luninga, Mzee Kibangu alikuwa kimya akitazama habari hiyo ya majonzi aliyokuwa akiijua fika, huku akijifanya naye ndio kwanza anaisikia muda ule.

“ Isijekuwa haya mambo ya kisiasa, kwa kweli kama aliyefanya hivi ni Rais Kinyunumba atakuwa hajafanya vizuri” Bi. Kibangu akasema huku habari hiyo ikiwa imemalizika kwenye luninga,

“ Rais hawezi kufanya hivyo, tena wakati kama huu wa uchaguzi angewezaje kufanya tukio la namna hii huoni yeye angehusishwa moja kwa moja kutokana na kuwa Askofu Joshua alikuwa akimkosoa na kumpinga vikali, hapo lazima kuna mtu kapita katikati kumchafua Mhe. Rais ili asichaguliwe kesho kutwa” Mzee Kibangu alisema huku akijibwaga kwenye Sofa, maelezo yake yalitosha kumshawishi mkewe, lakini bado mara kwa mara alikuwa akiwaza nani aliyekuwa nyuma ya tukio lile la kushtusha, mkewe alikuwa ameshaenda kumletea juisi ya miwa ambayo Mzee Kibangu alikuwa akiipenda sana.

“ Karibu! Alafu kuna mtu alikuja kukuulizia muda uliokuwa umetoka tuu, nikampa namba zako, hajakupigia?” Bi. Kibangu akasema,

“ Mtu! Mtu gani? Hakuna aliyenipigia tangu nilipoondoka” Mzee Kibangu akasema,

“ Mmmh! Basi atakupigia” Bi. Kibangu akasema, kukatokea ukimya kwa kitambo mzee kibangu akiwa anakunywa Juisi ya miwa, baada ya kumeza fumba la juisi, akasema;

“ Hakujitambulisha jina lake”

“ Alisema ameagizwa na Rais”

“ Ameagizwa na Rais?”

“ eenhe mbona unashtuka!” Bi. Kibangu alisema akiwa anamshangaa Mume wake.

“ Mtu aagizwe na Rais wakati Rais ananamba zangu?”

“ Alisema wewe unajua ujio wake, ndio maana akaniomba namba akupigie kabla haujafika mbali kwa maana nilimuambia kuwa haujafika mbali” Bi. Kibangu akasema huku akiwa anaona amefanya makosa kutoa namba za Mumewe kirahisi kutokana na kumuamini yule kijana kwa haraka.

“ Embu kaniletee Laptop yangu nicheki kwenye Camera” Mzee Kibangu akasema, Punde laptop ikaletwa, ilipoletwa akaanza kukagua, ndipo alipomuona kijana mmoja mwenye mwili wa wastani akiwa kava Kaunda suti, akiwa nje ya nyumba lakini ndani ya geti, akiwa kava Kapero kichwani na miwani nyeusi, akajaribu kuikuza ile picha eneo la usoni ili aweze kumtambua lakini hakuweza kutokana na uvaaji wa ile kapero na miwani nyeusi, wakati akiwa anaangalia Video za CCTV Kamera, ghafla simu yake ikawa inaita, kuangalia, ilikuwa namba ngeni, wakatazamana na mkewe kisha mkewe akamuashiria apokee, akapokea na kuweka sikioni.

“ Hello, habari!, unasema! Wewe nani! Subiri! Wapi, kesho saa ngapi! Lakini wewe nani?” Mzee Kibangu alikuwa akiongea na simu akiwa na wasiwasi mwingi sana, hali hiyo ikamfanya mkewe awe anasogeza masikio yake kwenye simu lakini Mzee Kibangu akawa anamkwepesha ili asisikie.

“ Kuna nini” Bi. Kibangu akasema,

“ Hakuna kitu”

“ Embu acha zako, kijasho chembachemba kinakutoka alafu unasema hakuna kitu?” Bi. Kibanga akasema, akiwa ameghadhibika.

“ Ni kuhusu kifo cha Askofu Joshua”

“ Ennhe! Kuna nini tena?”

“ Kuna vielelezo vimekutwa eneo la tukio, vina ukaribu na mtu mkubwa katika nchi yetu” Mzee Kibangu akasema,

“ Mimi nilijua tuu! Sasa ulichokuwa unakataa ni kitu gani, au kisa huyo Kinyunumba ni mshirika wako wa kibiashara?” Bi. Kibangu akasema, kimya kikatokea kwa kitambo huku Mzee kibangu akiwa mwingi wa mawazo, alikuwa anatoka kijasho huku akitetemeka kwa hofu, jambo ambalo lilimfanya mkewe agundue kuna jambo lisilo la kawaida linaendelea lakini mumewe anamficha.

“ Mbona unawasiwasi sana Mume wangu” Bi. Kibangu akauliza,

“ Hapana! Unajua bado sijaamini hizi taarifa”

“ Mmmh! Ndio uwe hivyo? Kwani huyu uliyekuwa unaongea naye ni nani?” Bi. Kibangu akauliza, swali hilo lilimshtua sana Mzee Kibangu,

“ Achana nalo, kesho nitaenda kuonana na Mhe. Rais”

“ Unataka ukamuulize? Nakuomba usije ukafanya hivyo”

“ Hapana, kuna jambo nataka kulijua, wala sitamgusia kuhusu mambo haya” Mzee Kibangu akasema, huku akiinuka na kuondoka kwenda chumbani. Mkewe alikuwa akimsindikiza mpaka alipopotelea kwenye ngazi ya ghorofa..

INAENDELEA
Kitabu kipo Tayari, lIPIA Tsh, 15,000/= UJIPATIE NAKALA YAKO

0693322300
Robert Heriel
Airtelmoney
 
WAKALA WA SIRI Episode 09
Mtunzi; Robert Heriel
WhatsApp 0693322300
EPISODE 09

ILIPOISHIA.

“ Hapana! Unajua bado sijaamini hizi taarifa”
“ Mmmh! Ndio uwe hivyo? Kwani huyu uliyekuwa unaongea naye ni nani?” Bi. Kibangu akauliza, swali hilo lilimshtua sana Mzee Kibangu,
“ Achana nalo, kesho nitaenda kuonana na Mhe. Rais”
“ Unataka ukamuulize? Nakuomba usije ukafanya hivyo”
“ Hapana, kuna jambo nataka kulijua, wala sitamgusia kuhusu mambo haya” Mzee Kibangu akasema, huku akiinuka na kuondoka kwenda chumbani. Mkewe alikuwa akimsindikiza mpaka alipopotelea kwenye ngazi ya ghorofa..

ENDELEA

OASIS HOTEL, MIKOCHENI.

Kilikuwa kikao cha watu wanne kilichofanyika majira ya saa nane mchana, ghorofa ya kumi na sita, katika Hotel ya Oasis ambayo ni moja ya Hoteli kubwa yenye hadhi ya nyota tano iliyo Mikocheni jijini Dar es salaam. Waliohudhuria kikao hiki ni Mr. Gombe, Mkuu wa majeshi, CDF Ramadhan Toma, Mr. Jumanne Khalfan, na Rais Mstaafu Ahmed Selemani ambaye ndiye alikuwa mwenyeketi wa kikao hiki cha siri kilichofanya mchana jua likiwa kali.

“ Nawashukuru nyote kwa muitikio wenu, napenda jinsi mlivyowaaminifu kwangu, hakika hisani mnayonifanyia ni kubwa sana, wala sijutii kuwatoa kwenye hali duni na kuwapa nafasi kubwa, bila mimi ninyi msingekuwa hapa mlipo, kweli sio kweli?” Rais Mstaafu Ahmed Seleman akasema, wote wakaitikia kweli kukubali kauli yake.

“ Basi ikiwa ni kweli, basi hata mimi nakiri kuwa ni kweli kuwa bila ninyi basi wakati huu sitaweza kufanikiwa katika mpango wangu, ulikuwa mpango wangu kabla sijaachia madaraka kumuweka Mr. Jumanne Khalfan kuwa mrithi wangu lakini kwa bahati mbaya wazee wa chama wakaniambia kuwa utaratibu wa chama ni kupokezana baina ya Mkristo na muislam, basi kwa kigezo hicho mdogo wangu Jumanne akashindwa, ndipo akaingia huyu Kinyunumba ambaye kwa aliyoyafanya nachelea kusema namchukia sana, kaharibu kila kitu nilichokuwa nimekipanga, na watu wangu wengi aliwaondoa kwenye mfumo akaweka watu wake ili kunidhibiti, lakini kwa vile sikuwa na ukaribu na nyie ndio maana akawaacha nyie na kuwapa vyeo vikubwa na kuwafanya baadhi yenu washirika wake kasoro Mr. Jumanne, asijue kuwa hata nyie ni watu wangu, hilo ni kosa ambalo litamgharimu, anafikiri amenishinda lakini kumbe nimeamua kujifanya mfu mbele yake huku nikimvizia kwenye right angle. Wakati umefika kumuonyesha kuwa mimi ni nani, nataka ajue kuwa ile anayoiita ikulu niliingia kabla yake, nataka nimfunze kuheshimu waliomtangulia” Rais Mstaafu, Mr. Ahmed selemani akasema, akameza mate kisha akaendelea,

“ Kila hatua yake tumeihesabu, tangu alipoingia na sasa tunajua amebakiza hatua ngapi atoke kwenye kile kiti, siku zilizobaki hazitamtosha kugundua kuwa amechelewa, tena afadhali asijue kuliko ajue sasa hivi, hahahah! Atachanganyikiwa! Masiikini Kinyunumba wala hajui kinachoendelea, yeye anaona kila kitu kipo sawa. Subiri atajionea. Afadhali angekuwa mzalendo kweli, lakini unafiki wake wa kujifanya muungwana na mzalendo mbele za watu huku akiiba na kuhujumu nchi hii ndio itanipa kibali cha kumuangamiza, anatuzuia sisi tusile ili ale peke yake huyo, mpuuzi sana! Sasa mwisho wake umemfikia” Mr. Ahmed seleman akasema, akachukua Chupa iliyokuwa na pombe kisha akamimina kwenye bilauri yake alafu akameza fumba mbili, kisha akasema;

“ Embu mpigie huyo Injinia Kibangu” Kisha Mr. Gombe akapiga simu akiwa na simu ndogo, alafu akampa ile simu Rais mstaafu, akaweka loud speaker ili kila mtu asikie,

“ Hallo!”

“ Kibangu! Muda ndio huu, kama nilivyokuambia jana usijemwambia mtu yeyote kwamba nimekupigia simu, nakusubiri”

“ Ndio niko njiani nakaribia Mkuu” Mzee Kibangu alisema akiwa kwenye simu.

‘ Usije leta hila yoyote kwa maana upo kwenye njia yetu, embu angalia nyuma” Rais mstaafu, Ahmed akasema. Mzee Kibangu alikuwa kimya akiendesha gari lake kila mtu akiwa kimya kwenye simu bila ya kuongea kumpa nafasi Mzee Kibangu aangalie nyuma ya gari lake.

“ Nafikiri unaona gari nyeusi ikiwa imekufungia Mkia, ujanja wowote utakugharimu” Rais Mstaafu Ahmed Seleman akasema kwa sauti isiyo na mzaha, kisha akakata simu. Mzee Kibangu alikuwa ameona gari lenye rangi nyeusi, Land Cruisser V8 ikiwa inamfuata.

“ Bila shaka atakuwa anajiuliza sauti hii niya nani! HAHAHAAA!” Mr. Gombe akasema huku akicheka,

“ Mkuu unajua kuigiza sauti nzito yenye kutisha, unakipaji sana” CDF Ramadhan Toma akasema huku kicheko kikimshinda,

“ HAHAHAH” Wote wanacheka.

Punde simu ikaita, akapokea; “ mleteni’ Mr. Ahmed Seleman akasema,

“ Amefika mtu wetu” akasema tena, dakika tatu mlango ulifunguliwa wakaingia vijana watatu wakiwa pamoja na Mzee Kibangu, baada ya kumkabidhi wale vijana watatu wakatoka, hivyo mule ndani wakawa watu watano akiwa ameongezeka Mzee Kibangu.

“ Hongera sana Injinia kwa kumuua Askofu Joshua” Mr. Ahmed Seleman akasema, muda huo Mzee Kibangu alikuwa akimtazama Mr. Gombe kwa macho ya kustaajabu, hakutegemea kumkuta Gombe eneo lile, “ Kumbe Gombe ndiye msaliti” Aliwaza.

“ Unaua watumishi wa Mungu? Kwa nini lakini?” Mr. Ahmed akaendelea kumzingua Mzee Kibangu,

“ Mimi sijamuua Askofu Joshua” Mzee Kibangu akasema,

“ Hahahahhh!” Wakacheka wote kasoro Mzee Kibangu.

“ Tunajua hujamuua, uliyemuua ni yule kijana ambaye ni houseboy wake”

“ Mimi sijamuua yeyote yule, hata sijui mnazungumzia vitu gani” Mzee Kibangu akasema, kauli yake ilifanya wote wacheke, :hahahhaha!”

“ Ujue haipendezi Mtu mwenye umri wako kuwa muongo? Unawafundisha nini hawa vijana hapa kwa maana wote wanajua kuwa wewe ndiye uliyemuua yule kijana” Mr. Ahmed akasema, hapo Mzee Kibangu akabaki kimya,

“ Embu muwashie hiyo Projector” Mr. Ahmed akasema, kisha Projector ikawashwa kana kwamba ilikuwa ikimsubiri Mzee Kibangu, hapo mzee kibangu alishtuka kujiona akiongea na simu huku akimtaja Rais Kinyunumbu mbele yake ikiwa maiti ya Askofu Joshua ikiwa imekatwa katwa vibaya sana, kisha akatokea yule kijana, akampiga Risasi, na matukio yote yalikuwa na sauti ingawaje sauti ya Rais kinyunumba hayakuwa yanasikika kwenye simu zaidi ya Mzee Kibangu ndiye aliyekuwa akimtaja jina, pia hata yule kijana alivyouliza swali na kumtaja Me. Rais vyote vilikuwa vinasikika kwenye ile video. “ Nimekwisha” Mzee Kibangu akawaza, huku akihisi shinikizo la damu kupanda, akamgeukia Mr. Gombe.

“ Wewe ndiye uliyefanya yote haya?” Akamuuliza, Mr. Gombe akamjibu kwa tabasamu la dharau lilioashiria kusema; Ndio mimi.

“ Mnataka nifanyaje?” Mzee Kibangu akasema, sasa akiwa amemgeukia Rais Mstaafu Ahmed Seleman.

“ Hayo ndio maneno ya busara. Utatufanyia jambo moja zuri sana ili wewe uwe salama, tunakuahidi kukulinda ukifanya jambo hili, lakini kinyume na hapo utajiingiza kwenye makucha ya simba mwenye njaa wewe na familia yako” Rais Mstaafu Ahmed Seleman akasema,

“ Naombeni mnihurumie ndugu zangu, msiidhuru familia yangu, akheri mnidhuru mimi lakini familia yangu muiache ikiwa na amani, haihusiki na mambo haya” Mzee Kibangu alisema huku akilia akiwa amepiga magoti, alikuwa akitia huruma sana.

“ Mbona wewe hukumsamehe Yule kijana aliyekukuta mule ndani, hukumuonea huruma, kwani kosa lake ni lipi mpaka ukamuua, wewe unajua kanuni za hii michezo, sisi hatuna shida na wewe, tunashida na mipango yetu kutimia, nawe upo sehemu ya kutimiza mipango yetu kwa kufanya sehemu ndogo tuu, ukiweza kufanya hivyo basi utabaki salama, ukileta ukaidi basi kitakupata ulichompa yule kijana” CDF Ramadhan Toma akasema.

“ Nawasikiliza, nitafanya chochote mtakachoniambia kwa ajili ya familia yangu” Mzee Kibangu akasema,

************************

Rais Kinyunumba alitoa salamu za rambirambi kufuatia kifo cha Askofu Joshua ambaye alikuwa maarufu mwenye wafuasi wengi aliokuwa akiwaombea katika kanisa lake la CHURCH IN THE MIDDLE OF THE SUN” yaani “Kanisa katikati ya Jua” kutokana na mahubiri yake alijikuta akipaa katika anga la umashuhuri na kukutana na mikondo mbalimbali ya pepo kali za watawala zivumazo ambazo zilikuwa zinajaribu kumtisha enzi za uhai wake. Watu wengi walimhusisha Rais Kinyunumba na tukio la mauaji ya Askofu Joshua ingawaje Kinyunumba mwenyewe alikanusha kutokuhusika,

Rais Kinyunumba akatangaza Siku tatu za kumuombolezea Askofu Kinyunumba kama ishara ya heshima kwake na kumuenzi kwa mazuri aliyokuwa akiyafanya katika jamii.

Ripoti ya Daktari kuhusu kifo cha Askofu Joshua na Mkewe Ilikuwa yakushangaza; Ripoti ilikuwa inaeleza kuwa, Askofu Joshua alikufa kwa Kunyongwa na wala sio kwa kukatwa katwa na mapanga, hii ilimaanisha kuwa alinyongwa mpaka akafa ndipo akakatwa katwa na mapanga. Mkewe kifo chake kilisababishwa na kupigwa Risasi iliyopigwa kwenye eneo la moyo wake. Wakati kijana alikufa kwa kupigwa Risasi ya kichwa,

Vifo vyote havikuwa na taarifa mpya isipokuwa kifo cha Askofu Joshua ambacho watu wengi walidhani alikufa kwa kukatwa katwa na mapanga, kumbe haikuwa hivyo, aliuawa kwa kunyongwa na kamba ngumu kisha muuaji alipohakikisha amekufa ndipo wakamkata kata na mapanga. Kwa kweli habari hizo zilizua gumzo kwenye vyombo vya habari, mitandao ya kijamii na mitaani, zilikuwa habari za kuogofya sana,

Zikiwa zimesalia siku tatu uchaguzi mkuu ufanyike, siku hiyo ikiwa ndio siku ya mwisho katika zile siku tatu za maombolezo ya kumlilia Askofu Joshua, Rais, Kinyunumba akiwa ametoka kwenye Kampeni akiwa amechoka kutokana na mizunguko ya kampeni, alishtushwa na video aliyotumiwa na Mr. Daniel ambaye alikuwa katibu wa masuala ya uenezi na propaganda, video ile ilikuwa inamuonyesha Mgombea wa urais kwa tiketi ya chama kikuu cha Upinzani, Mr. Solomon Ngazi aliyekuwa akisema;

“ Unaua mpaka maaskofu, wewe ni mnyama, katili usiye na huruma. Afadhali uende porini ukaongoze wanyama wenzako, binadamu hawezi ongozwa na mtu mwenye roho mbaya kama yako. Ulimtuma Mzee Kibangu akamuue Askofu Joshua, ukamuua Askofu Joshua pamoja na mkewe kwa mkono wa Mzee Kibangu, umemtishia mzee wa watu kuwa kama hatamuua utaharibu familia yake na yeye mwenyewe, sijawahi kuona mtu mnyama kama wewe, kijana wa watu amekufanya nini mpaka umuue, kosa lake kukuambia ukweli uache kutumia kodi za wananchi kwa matumizi yako, kosa lake ndilo hilo, hukuwafikiria waumini wake, huna huruma shenzi kabisa, hata watoto wake au wazazi wake hukuwafikiria? Kesho naenda kutoa ushahidi mbele ya jamii wa jinsi ulivyomuua Askofu Kibangu, jinsi ulivyomtuma Kibangu na mpaka kibangu alivyomuua Askofu Joshua, mkewe na yule kijana”

Rais Kinyunumba alihisi kichwa kupata moto, akahisi kuchanganyikiwa, “ Haiwezekani! Haiwezekani! Nimesema hii ni hujuma ya wazi kabisa, ujinga huu! Embu mpigieni Mzee Kibangu” akawa anafokafoka na kusema sema akiwa kama mtu aliyevurugwa, mara asimame mara akae basi ilimradi.

“ Mkuu! Namba yake haipatikani”

“ Haipatikani kivipi, msinichanganye, nimesema mleteni hapa Mzee Kibangu. Wewe pigia simu Ndege ije inichukue sasa hivi turudi Dar es salaam, fanya upesi mnazubaa zubaa nini” Rais kinyunumba alikuwa amebadilika sana, hofu iliyochanganyika na wazimu vilimvaa kwa pamoja, kitambo kidogo sauti ya helikopta ilikuwa ikirindima angani upande wa nje wa ile hoteli aliyokuwa amefikia Rais Kinyunumba, akapanda ndege akiwa na watu wa karibu walinzi safari ya kuelekea Dar es salaam ikaanza.

“ Haiwezekani! Kibangu? Hapana! Haiwezi kuwa kweli! Kibangu hawezi kuwa amenisaliti, lazima kuna jambo linaloendelea ambalo sio la kawaida” akawaza huku ndege ikikata anga.

“ Mr. Lusingi alisema kuna jambo anamashaka nalo, lakini sikubaliani naye kumshuku Mr. Gombe, haiwezekani Gombe kunisaliti tumetoka mbali sana, alafu tuna mambo mengi maovu tumefanya pamoja hata kabla sijawa Rais, siku zote asinisaliti aje kunisaliti wakati huu, hapana. Sasa nini kitakuwa kinaendelea” Akawaza, huku akipokea simu, aliyekuwa akipiga ni kamanda wa Polisi wa Dar, alikuwa akimtaarifu kuwa Mr. Solomoni wameshamkamata na yupo mikono salama ya polisi.

“ Nipo njiani, mshikeni mumbinye mpaka aseme nani wapo nyuma yake, nitakuwa hapo muda mfupi ujao” Simu ikakatika. Mtandaoni habari iliyokuwa inasambaa ni ile video ya Mr. Solomon,

“ siwezi vumilia ujinga hata kidogo” Rais Kinyunumba akawa anasema huku akibonyeza simu yake, kumpigia mkuu wa mamlaka ya mawasiliano, “ Kuanzia sasa huna kazi, huna haja ya kunisalimu” akapaliwa na mate akawa anakohoa, “ majukumu yako huyajui, mpaka afanye mtu mwingine, haya ukabidhi ofisi kesho” akakata simu. Ni baada ya Msaidizi wa mkuu wa mamlaka ya mawasiliano kupunguza kasi ya mtandao ambapo watu wakawa hawawezi kuingia kwenye mitandao ya kijamii wala kutumiana habari, “ Napenda vijana wenye akili za kujiongeza kama huyu, sijui kwa nini sikumuweka awe Mkuu wa mawasiliano, ona sasa hili lilizubaa kidogo taarifa zifike kila mahala” Rais Kinunyumba alikuwa akiwaza.

Katika dunia ya teknolojia hakuna siri, namna bora ya kuikabili tarifa isisambae ni kuzima mtandao au kupunguza uwezo wa kasi yake uwe chini kabisa, hivyo ndivyo alivyofanya Rais Kinunyumba, alipunguza kasi ya mtandao kwa kiasi cha mwisho kabisa kiasi kwamba hakuna mtu aliyeweza kutuma taarifa kwa njia ya mitandao ya kijamii.

Tayari walikuwa wapo kwenye anga la jiji la Dar es salaam wakilakiwa na mataa yaliyokuwa yanametameta kama nyota za angani, wakashuka moja kwa moja Ikulu tayari Mr. Lusingi Mkuu wa idara wa usalama wa taifa alikuwa akimngojea,

“ Bado hamjajua aliyemuua Askofu Joshua, vipi Kale kazee kako wapi? “ Rais Kinyunumba alisema kwa hasira, hawakuwahi kumuona akiwa katika uso ule.

“ Bado mkuu ila kuna taarifa ambazo tunazo ambazo zinatupelekea kuamini kuwa Askofu Joshua na mkewe waliuawa na mtu mmoja, ila yule kijana aliuawa na Mzee Kibangu” Mr. Lusingi akasema,

“ Ndio nasema huyo mtu aliyemuua Askofu Joshua hamjamkamata hilo ndio swali langu kipi haujaelewa mzee” Rais aligomba midomo yake ikitetema.

“ Bado mkuu hatujampata, ili kuna jambo ambalo linajirudia rudia mkuu”

“Jambo gani?”

“ Harufu ya marashi tuliyoikuta eneo lile ni ileile ambayo tuliikuta katika jumba la Meja Venance, hii inamaanisha muuaji ni mmoja, na ambaye kama nilivyosema awali, yupo katika mzunguko wetu wa karibu sana” Mr. Lusingi akasema,

“ Maharufu mimi yatanisaidia nini Lusingi bhana! Mtafuteni huyo mtu haraka iwezekanavyo, vipi mmeshawapata wale panya wawili, Sajenti Warioba na Fernanda?” Rais akafoka, uso wake alikuwa kaukunja,

“ Bado Mkuu wanahangaika kutafuta”

“ Kila kitu Bado, bado! Hivi kazi yenu ni ipi hasa? Embu nieleze kazi yenu ni ipi? Nawapa pesa ili mniambie bado, hii haiwezekani” Rais Kinyunumba alikuwa akiongea huku wakitembea katika korido za Ikulu akiwa na Mr. Lusingi.

“ Naomba nianze kumchunguza Mr. Gombe Mkuu, huku nikiendelea nakuahidi nitakuletea muuaji?”

“ Utamchunguza mtu ambaye muda wote upo naye Lusingi? Anyaway mimi ninachohitaji huyo msaliti aletwe, nataka kupata simu ya Meja Venance, nataka chipu iliyoibiwa maabara, chunguza madaktari wote waliokuwepo siku ya uchunguzi kule maabara ya Boreti, isijekuwa tunamkimbiza kijana wa watu kumbe chipu haipo kwake, anzia hapo” Rais akasema,

“ Sawa Mkuu”

“ Vipi yule paka bado hajasema nani wanaomtuma?”

“ Solomon amegoma kusema ukweli, licha ya kutumia mbinu zote lakini amegoma”

“ Nyie hamna akili” Rais kinyunumba akasema mara hii akiwa amekunja ngumi na kuipiga kwenye nguzo za kuta za ile ikulu. Mr. Lusingi akawa kimya bila kujibu, kisha Rais Kinyunumba akasema;

“ Mumemuweka wapi?”

“ Yupo jumba la mateso”

“ Nipeleke nikamuua kwa mikono yangu” Rais akasema, kisha wakapanda ndani ya gari bado kukiwa na usiku mkuu, walinzi wakiwa wamewafuata nyuma yao na magari. Haikuchukua muda walikuwa wamefika kwenye jumba la mateso ambalo halikuwa mbali kutoka Ikulu, ni maeneo ya Upanga. Rais alipofika jambo la kwanza alimkaribia Solomon na kumzaba kibao kikali kilichomfanya Solomon apoteze kumbukumbu.

“ Mmwagieni maji ya baridi sana” akaamrisha, jambo hilo likafanyika, punde Solomon akazinduka.

“ Huo ushahidi uliokuwa nao kuwa mimi ndio niliyemuua Askofu Joshua upo wapi? Nani yupo nyuma yako? Sema!” Rais akasema kwa kufoka.

“ Vipi unaogopa, kila kitu kimekwisha” Mr. Solomon akasema akiwa amechoka uso ukiwa unavuja maji na kuacha makovu midomoni mwake yaliyotokana na vipigo alivyopewa.

“ Wewe leo ndio umekwisha, hata usiponiambia mimi leo ninakuua” Rais Kinyunumba akasema, akiwa anamkaba kwa nguvu shingoni, muda huo Solomoni alikuwa amefungwa kamba mikononi kwa nyuma na kafungwa kamba miguu akiwa kwenye sakafu yenye kokoto, kilikuwa chumba kikubwa chenye nuru hafifu inayotokana na taa ya chemli ambayo ilikuwa inawaka huku kioo cha yai kikiwa kimeshika ukungu wa moshi mweusi upande mmoja wa kioo cha Yai hali iliyopelekea kuzuia mwanga usiangaze vizuri, juu kulikuwa na kamba za chuma kama za kuanikia nguo, na enka za kutundikia nyama, hakikuwa chumba rafiki kwa binadamu muungwana.

“Niue basi, sitashangaa ukiniua kwa sababu wewe ni muuaji. Umemuua Askofu Joshua na Mkewe, kisha sasa unataka kuniua na mimi, ila nakuhakikishia kuwa kila hatua yako imehesabiiwa, hata hapa ulipo kuna watu wanakuzunguka, yaani upoupo tuu kama mjinga” Mr. Solomon akasema akiwa anamdhihaki Rais Kinyunumba.

“ Kelele! Kenge wee!”Rais akasema huku akimsindikiza na ngumi ya uso iliyopasua mwamba wa pua yake. Hapo Solomon akatoa ukulele wa maumivu kisha akawa anacheka huku damu zikitoka kwenye pua.

“ Ulijua kama Mzee Kibangu anakusaliti, kila kitu mlichokuwa mnafanya kipo wazi, subiri kesho utajionea mwenyewe, kesho kutwa ndio uchaguzi, nakuhakikishia nitashinda, nami ndio Rais wa nchi hii” Mr. Solomon akasema huku akiwa anapumua kwa shida,

“ Wewe uwe Rais wa nchi hii! Hahahhaha! Kweli unaugua ukichaa, sijui kwa nini hata mlinileta kumuona huyu chizi hapa, unafikiri kuwa Rais ni sawa na kubwabwaja kama unavyofanya wewe huko mitandaoni?” Rais akameza mate kisha akaendelea;

“ Kibangu yupo wapi?”

“ Nisikilize wewe muuaji, embu niue mimi usinisumbue, sitaki kuona aibu utakayoipata hiyo kesho, isubiri hiyo kesho utajua wapi alipo huyo Kibangu” Solomon akasema,

“ Muacheni hapo, naona amechanganyikiwa, muogesheni, kisha mumvike nguo vizuri alafu mumtafutie sehemu nzuri ambazo atakaa chini ya uangalizi” Rais akasema,. Kisha akatoka.

Jeshi la polisi kwa amri ya Rais kinyunumba likatangaza kumtafuta Mzee Kibanga kwa kosa la mauaji ya Askofu Joshua na mkewe pamoja na kijana msaidizi wa kazi za nyumbani. Kwa yeyote ambaye atamuona basi jeshi lilimuahidi kumpa donge nono la zawadi kama ahsante, “ Ukaribu wa Mzee Kibangu na Rais wetu ni Mkubwa, kitendo cha mauaji alichokifanya sio tuu ni uvunjifu wa sheria bali pia ni kumharibia jina Rais wa nchi yetu ambaye ni jemadari mkuu wa nchi yetu. Sio ajabu baadhi ya viongozi wa kisiasa kumhusisha Rais na mauaji ya Askofu Joshua na mkewe kwa sababu ya ukaribu wa Muuaji na Rais. Adhabu kali itachukuliwa kwa yeyote atakayebainika kumficha Mzee Kibangu” Lilikuwa ni tamko la jeshi la polisi

Kesho yake asubuhi mbali na habari ya kutafutwa kwa Mzee Kibangu pia kulikuwa na tukio la wanachama wa chama kikuu cha Upinzani waliandamana katika majiji yote makubwa wakiwa na mabango yenye jumbe mbalimbali pamoja na picha zilizokuwa zinamuonyesha Kiongozi mkuu wa chama cha Upinzani, Ndiye Mr. Solomon. “ Free Solomon” “Utekaji sasa basi” Kinyu umekwisha” hizo zilikuwa baadhi ya jumbe zilizokuwa zikisomeka kwenye Mabango waliyokuwa wameyabeba Waandamanaji waliojitambulisha na kujulikana kama wanachama wa chama kikuu cha upinzani au wafuasi wa Mr. Solomon.

Juhudi za jeshi la polisi kuzima maandamano hayo ziliendelea kwa siku nzima huku vijana wengi wakijeruhiwa na kukamatwa na askari, maandamano yaliendelea lakini hayakudumu kwa muda kwa masaa mengi kutokana na woga wa vijana wengi wa nchi hii. Polisi walisema kuwa Solomon ameshikiliwa na polisi kwa kuzusha maneno ya uongo dhidi ya Rais yenye lengo la kumchafua Rais wa nchi.

Ilikuwa imebaki siku moja kufikia uchaguzi, Rais Kinyunumba asubuhi ya leo alienda kumtembelea Solomon kwenye maficho waliyokuwa wamemficha, siku ya leo alikuwa ameambatana na Mr. Gombe, pamoja na Mkuu wa idara ya usalama wa taifa, Mr Lusingi, pamoja na Mr. Daniel.

“ Tutakuachia sasa, ila chunga mdomo wako ukamalize kampeni yako, unajua leo ndio siku ya kufunga kampeni, na kesho ndio uchaguzi, nataka nikushinde kwa kishindo ili ujue kuwa watu wananipenda” Rais Kinyunumba akamwambia Mr. Solomon.

“ Huwezi kunishinda Kinyunumba, nakuhakikishia huwezi kuwa Rais sijui kwa nini haulioni jambo hili” Mr. Solomon akasema,

“ Embu kaa kimya panya mdogo” Rais akasema, angali anasema simu yake ikawa inaita, akaitoa mfukoni, kisha akaweka sikioni;

“ Hello”

“ Mkuu! Kuna habari mbaya ipo kwenye televisheni, embu angalia” sauti ya upande wa pili wa simu ikasema, Rais akakata simu, akamtazama Mr. Solomon, kisha baadaye ujumbe ukaingia kwenye simu yake upande wa WhatsApp, ilikuwa video, akaifungua, alishtuka na kuwashtua wote waliokuwa kwenye ile sebule. Alimuona Mzee Kibanga akiongea;

“ Ndugu watanzania. Mtaniwia radhi kwa yote yaliyotokea, Nipo tayari haki itende, nipo tayari kuhukumiwa kunyongwa kwaajili ya haki, nitasema ukweli wote, watu wengi wanajiuliza ni nani aliyemuua Askofu Joshua na mkewe, leo nitatoa ushahidi wa wazi kuwa ni nani aliyemuua Askofu Joshua Kalima. Muuaji wa Askofu Joshua Kalima ni Rais Bosco Kinyunumba, nitaweka ushahidi wa kila kitu hapa, nitaanza na mimi mwenyewe. Rais alinituma mimi kwenda kwenye makazi ya Askofu Joshua aliyekuwa akiishi Kimara korogwe kwa lengo la kumuua, alinitisha kama nisipomuua Askofu Joshua basi yeye mwenyewe angenishughulikia na kuiangamiza familia yangu, sikuwa na namna, nilifanya yote yale kulinda Familia yangu, naipenda sana familia yangu kama vile ninyi mpendavyo za kwenu.” Mzee Kibanga akakohoa akiwa anaonekana kwenye video iliyotumwa kwenye simu na ambayo inaonyeshwa kwenye chombo cha habari cha nchi za nje. Akaendelea;

“ Nilienda kumuua Askofu Joshua nikiwa sina lengo la Kumuua Mkewe, kwani hilo sikuwa nimetumwa, lakini nilipofika nilikuta Mauaji ya kikatili sana, niliukuta mwili wa Askofu Joshua ukiwa umekatwa katwa na mapanga, wala sikujua kuwa mkewe naye wamemuua, niliogopa sana wala siwezi kueleza nikaeleweka, ikabidi nimpigie Mhe. Rais kumpa taarifa kuwa nimekuta mauaji, nikampigia wakati nazungumza naye ndio akatokea yule kijana kwa kuogopa kuwa yeye ndiye kanikuta pale nikamuua ili habari zisitoke, hivyo ndivyo ilivyokuwa, mazungumzo yangu yote na Rais kwa njia ya simu niliyarekodi, nitayaambatanisha hapa” Mzee kibangu Kupitia video akaonekana akitoa mfukoni simu janja yake, kisha akabonyeza bonyeza kisha mazungumzo yake na Rais yakaanza kusikika. Kwa jinsi mazungumzo yale ya Mzee Kibangu na Rais; mtu yeyote ambaye angeyasikiliza angeamini ni kweli Rais ndiye aliyemtuma Mzee Kibangu kumuua Askofu Joshua ingawaje Kibangu alikuta tayari Askofu na Mkewe walikuwa wameshauawa.

Rais Kinyunumba alihisi tumbo kujagaa gesi, kila kitu aliona kama ndoto za mchana, “ Haya mambo yapo Sirius kumbe, nani yupo nyuma ya mambo haya” akiwa anafikiria jambo hilo, ile video ikamshtua zaidi baada ya kumuona kijana mmoja, Rais akajikuta akiropoka “ Joramu Kolowa” hapo wengine wakawa wanamshangaa, Solomon akiwa kafungwa kamba akiwa pale chini. Yule kijana ambaye alionekana kwenye video ambaye Rais Kinyunumba alimuita Joramu akaanza kuongea kwenye ile Video.

“ Jina langu ni Joramu Kolowa, nilipewa kazi maalum na Mhe. Rais Bosco Kinyunumba ya kumuangamiza Askofu Joshua, kazi hii alinipa muda mrefu tangu mwezi uliopita ila kila mara nilipokuwa nataka kuikamilisha alikuwa akiniambia nisitishe kwanza, nitatoa ushahidi wa kila neno langu hapa, sikujua kama kuna mtu mwingine alikuwa amempa kazi hiyo, siku ile alinipigia simu akaniambia saa moja nikakamilisha kazi ya kumuua Askofu Joshua, nikaondoka mpaka kwenye nyumba ya Askofu, nikaruka uzio na kuzama eneo la ndani, kulikuwa na giza lakini sio sana kwani ndio kwanza ilikuwa saa moja jioni. Nikaingia ndani lakini nilishtushwa nilipokuta mwili wa Askofu Joshua ukiwa umening’inia juu ya dari ya sebule, kwa kweli niliogopa sana, tukio lile la kusisimua lenye kutisha, ule mwili ulikuwa ukizunguka zunguka ukiwa unaning’nia, nikaushusha, baada ya kuushusha nikagundua tukio la mauaji limetoka kufanyika dakika chache zilizopita kutokana na kuwa mwili ulikuwa unajoto na viungo vilikuwa bado havijakaza. Nikatoka jambia langu nikaanza kuukata kata kwa maana niliambiwa na Rais Kinyunumba afe kifo cha kikatili cha kukatwa katwa na mapanga, nisingeweza kumjulisha Rais kuwa nimekuta Askofu amekufa ilhali nilikuwa nataka kujenga uaminifu zaidi kwa Rais na kusifiwa kuwa najua kazi” Akameza mate kisha akaendelea kusema,

“ Wakati namkatakata nikagundua kuna mtu ananichungulia, nikahisi mlango wa chumba kimoja ukijifunga, lakini sikuwa na uhakika, nikataka kujihakikishia kuwa nipo mwenyewe mle ndani jambo ambalo ningetakiwa kulifanya mwanzoni, nikausogelea ule mlango nilipoufika, nikajaribu kuufungua nikaona umefungwa, nikauvunja na hapo nikashtuka kumuona Mke wa Askofu Joshua akiwa amejificha chini ya kitanda, kilichofanya nimuone ni kamba ambayo nahisi ndio iliyokuwa imemnyonga Askofu Joshua, nilijua kuwa kwa kujificha kwake itakuwa alioniona, nikamtoa chini ya uvungu, kisha nikambembeleza aniambie nani aliyemuua Askofu Joshua lakini akakataa katakata, ndipo nilipompiga risasi ya moyo akafa palepale, nikiwa natoka chumba cha Askofu na mkewe nikamsikia mtu akibisha hodi getini, nikatoka na kujificha kwenye bustani ya maua, hapo nikamuona Mzee Kibangu akiingia, akaingia mpaka sebuleni bila kujua kuna mtu anamtazama, baadaye nikasikia geti likifunguliwa tena hapo nikamuona kijana mmoja ambaye alikuwa amebeba mfuko ambao ndani yake sikujua unanini, kuona hivyo nikaondoka zangu, nikaona kuzidi kupoteza muda pale ni kutengeneza mazingira ya kukamatwa:” akanyamaza kwa kitambo akiwa anapumua kama mtu mwenye hofu, kisha akaendelea;

“ Hivyo mimi sikumuua Askofu Joshua, ila ndiye niliyemuua Mke wake, nipo tayari kutoa ushahidi mahakamani haki itendeke, lakini Rais Bosco Kinyunumba ndiye chanzo cha yote haya. Ahsanteni” Akamaliza.

Rais Kinyunumba alihisi kichwa kinamzunguka, akili yake inamkimbia, hakuamini alichokuwa anasikiliza ni kweli au ndoto, “ Upuuzi Gani huu!!!!!” Rais Kinyunumba akaipiga ile simu chini puu! Ikapasuka vipande vipande akiwa amevura kwa hasira.

Hapa ndio mwisho wa simulizi hii kwa njia ya mtandao, Kujipatia simulizi yote, jipatie Nakala yako,
Kitabu kipo Tayari, lIPIA Tsh, 15,000/= UJIPATIE NAKALA YAKO

0693322300
Robert Heriel
Airtelmoney
 
Back
Top Bottom