Shemsa Mohamed wa CCM kabla hujatoa kibanzi kwa Luhaga Mpina anza kutoa boriti jichoni mwako

Shemsa Mohamed wa CCM kabla hujatoa kibanzi kwa Luhaga Mpina anza kutoa boriti jichoni mwako

Rege

Senior Member
Joined
Jul 9, 2022
Posts
117
Reaction score
153
IMG-20240426-WA0035.jpg

Naandika ujumbe huu kwa masikito makubwa juu ya Kauli zako ulizozitoa kwenye mkutano wa ndani wa viongozi wa CCM pale Tarafani Kanadi Wilaya ya Itilima siku ya Tarehe 25.4.2024 kuhusu Luhaga Mpina, Mbunge wa Jimbo la Kisesa.

Umeutumia mkutano huo wa ndani wa Viongozi wa CCM Itilima badala ya kuwasilisha salamu na maelekezo ya Chama ngazi ya Mkoa wewe umetumia muda wote kutoa shutuma za uongo dhidi ya Mheshimiwa Mpina kuwa ameshindwa kutekeleza majukumu yake ya kuwawakilisha wananchi bungeni na ameshindwa kuwaletea wananchi wake maendeleo na wanalia na shida za Tembo, Maboma hayajamilika na mambo kadha wa kadha. Tuhuma za jimbo jingine zikasemewe kwa jimbo jingine kwa watu wasiohusika.

Nikajiuliza maswali mengi wewe kama Mwenyekiti wa Mkoa na Mjumbe wa Kudumu wa Vikao vya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa kupitia nafasi yako umesaidiaje kulitatua tatizo la tembo na maboma, ambalo sio tatizo la kisesa pekee bali mkoa mzima wa Simiyu, ikiwemo Itilima yenyewe ambayo umeipa sifa bandia lukuki, lakini pia umewasaidia nini wananchi wa Mkoa wa Simiyu tangu uchaguliwe kuwa Mwenyekiti?

Wewe ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC) nafasi nyingi za uteuzi zinapatikana kwa ushawishi na kujuana. tangu wana Simiyu tumekupa nafasi hii, umesaidia viongozi wangapi kutoka simiyu walioteuliwa katika nafasi mbalimbali, nafasi za Mawaziri, Naibu Waziri, Wakuu wa Mikoa na Wilaya, Makatibu Wakuu, Makatibu Tawala Mikoa na Wilaya, Wakurugenzi wa Halmashauri na Mashirika ya Umma hadi nafasi za Maafisa Tarafa.

Kiukweli sisi Mkoa wa Simiyu hizi teuzi tumekuwa tukizisikia tu ukilinganisha na wenzetu wa mikoa mingine kumbe shida tuliyonayo tuna viongozi ambao kazi yao kubwa ni kuwachongea na kuwapakazia mabaya wawakilishi wetu na vijana wetu wa Simiyu katika mamlaka za uteuzi. Huku Viongozi wa maeneo mengine wakiwemo wenyeviti wenzako wa CCM wa mikoa wakitumia malumbano hayo kama mtaji wao wa kufanikiwa.

Mfano mwenyekiti mwenzako wa Mkoa wa Pwani karibia kila jimbo lake limetoa Waziri, angalia Jimbo la Kisarawe ( Mh. Suleiman Jafo Waziri waMazingira), Jimbo la Rufiji (Mh. Mohamed Mchengerwa Waziri wa Tamisemi), Jimbo la Mkuranga (Mh. Abdalah Ulega Waziri wa Mifugo), Jimbo la Chalinze (Mh. Ridhiwan iKikwete, Naibu Waziri Utumishi) Jimbo la Mafia ( Mh.Omari Kipanga Naibu Waziri waElimu). Mawaziri 5 Mkoa mmoja tena wa sekta nyeti.

Ukienda Mkoa wa Tanga nako karibia majimbo yote yametoa mawaziri, angalia Jimbo la Tanga ( Mh. Ummy Mwalimu Waziri wa Afya), Jimbo la Pangani (Mh. Jumaa Aweso Waziri waMaji), Jimbo la Bumbuli (Mh. January Makamba Waziri wa Mambo Nje), Jimbo la Mkinga ( Mh. Dastan Kitandula Naibu Maliasili na Utalii), Jimbo la Muheza (Mh. Hamisi Mwinjuma Naibu Waziri Utamaduni). Mawaziri 5 mkoa mmoja tena wa sekta zote nyeti.

Pia Mkoa wa Tanga umebarikiwa kuwa na Makatibu Wakuu wengi kama Katibu Mkuu Maliasili, Dk. Abasi, Katibu Mkuu Mifugo, Prof. Shemdoe, Katibu Mkuu Mambo ya Nje Balozi Shelukindo, Katibu Ardhi Kijazi, Dk. Shekalaghe, Katibu Afya, Makatibu wakuu 5 mkoa mmoja. Hii ni mifano michache ukifuatilia nafasi za Mabalozi, wakuu wa mashirika, Ma-Ded, Ma-Dc, Ma-RC, Ma-RAS, Ma- DAS wengi wanatoka kwenye mikoa ya Tanga na Pwani wewe umekalia kulumbana na kuwatengenezea fitina wabunge na vijana wetu wenye sifa lukuki.

Je, wangapi umetetea upande wa Chama, Shemsa jitokeze hadharani utueleze umetetea nani kufanikisha ajira na teuzi ngapi za vijana wetu wamkoa wa simiyu ndani ya serikali na ndani ya chama, ajira nyingi za mgao wa simiyu wanapewa watu wa mikoa mingine, wewe upo na unaona ni sawa tu, Kazi unayoifahamu ni kueneza chuki, kuugawa mkoa kupambana na watetezi wa wananchi ili kulinda maslahi binafsi na genge lako.

Kwa kipindi kirefu Wakulima wa Pamba mkoa wa Simiyu wana nyanyasika kwa kupewa bei ndogo ya pamba inayotokana na makato makubwa ya shilingi 400 kwa kilo yanayofanywa na watuwa bodi ya pamba, Baraza la Madiwani la iBariadi lilishatoa hadi tamko kupinga suala hili bila mafanikio na wewe mwenyekiti wa mkoa uliingilia suala hili na kuitisha hadi halmashauri kuu maalum ya mkoa kuzungumzia suala hili lakini badae ajenda hiyo imefia mikononi mwako. Pia kaa ukijua kuwa tunajua mlivyomalizana na Waziri wa Kilimo.

Shemsa umeigeuza nafasi ya Mwenyekiti wa mkoa wa Simiyu kuwa mali yako binafsi ya kujipatia kipato na ndiyo maana unatumia nguvu kubwa kutetea genge lako pale linapoguswa ukitumia shati na kofia ya CCM.

Shemsa kumbuka kuwa huna jambo ambalo umewahi kulisimamia mpaka mwisho na likaleta matokeo, kila siku tunasikia unagombana na MNEC, Gungu Silanga kuhusu suala la mgodi. Kila siku tunakusikia ukimfokea MNEC hadharani tena mbele ya vyombo vya habari lakini mgogoro haufiki mwisho, wachimbaji wadogo wanalalamika, Mnec Gungu naye analalamika. Suala hili halifiki mwisho kwa sababu umeligeuza kitega uchumi chako.

Shemsa wewe kila Katibu wa CCM Mkoa akiletwa Simiyu wewe unampiga vita ahamishwe au afukuzwe kazi kwa kuwa tu hawakubaliani na biashara zako binafsi unazozifanya kwa kutumia koti la CCM. Kumbuka mambo uliyomfanyia Mama etu Haula Kachambwa na hata Katibu wa CCM Mkoa wa sasa Dada etu Eva Degeleki uko naye kwenye bifu kubwa kwa sababu hakubaliani na mambo yako unayofanya ambayo ni kinyume na maadili na miiko ya CCM. Wewe ni kiongozi wa aina gani na unapata wapi ujasiri wa kuwatungia uongo na kuwasema vibaya viongozi wenzako?

Chuki na uhasama uliouonyesha dhidi ya Mbunge wa Kisesa kumtungia uongo na kumsaka mahadharani ni tabia yako ya kila siku hasa unapotafuta na kutetea masirahi yako binafsi. Ambapo huwa hujali hata kama ni kukiua Chama cha Mapinduzi. Mfano siku unamshambulia Mpina, CHADEMA walikuwa na maandamano mjini Bariadi ya maelfu ya watu lakini wewe haikuwa ajenda kwako.

Ukiangalia tuhuma zote ulizozitoa Shemsa dhidi ya Mpina, hazina mashiko na ni za uongo, wabunge wakiwa Bungeni wanaongozwa na Kanuni za Bunge, na kila Mbunge ana haki ya kutoa mawazo yake na kama kuna sehemu amekosea anachukuliwa hatua kwa mujibu wa sheria. Shemsa leo unajigeuza kuwa Kiongozi wa Bunge au Kiongozi wa Serikali na kuwajibia mawaziri hoja wanazoulizwa na wabunge bungeni. Huku ni kulewa madaraka na ni kujikweza kulikopitiliza.

Kutunga uongo wa waziwazi eti katika jimbo la kisesa umefanya ziara kwenye kila shina na kufanya vikao na wanachama, eti wananchi wanalia matatizo yao hayatatuliwi Mbunge yuko bize kuichafua serikali na kuhoji kifo cha Magufuli. Huu ni uongoa ulioutunga na kuusema wewe mwenyewe katika kikao cha Viongozi wa CCM Jimbo la Itilima na hakuna mwananchi wala raia aliyekulalamikia.

Katika ziara ya Mwenezi Makonda mjini Bariadi ambapo ndio makao makuu ya CCM mkoa, Wananchi walikuja na mabango mkutano mzima wakiwa na malalamiko mbalimbali ambayo yamekosa ufumbuzi wewe Shemsa mbona hukuambiwa na Makonda uacheie umwenyekiti wa Mkoa. kwanini wewe unataka mpina aachie ubunge?

Upande wa shughuli za maendeleo na matatizo ya wananchi, Serikali imekuwa ikipeleka miradi ya maendeleo kila jimbo kama ujenzi wa madarasa, zahanati, vituo vya afya, maji, umeme, barabara, madaraja nakadharika. sasa kusema kwamba eti Kisesa hakuna utekelezaji miradi ya maendeleo hiyo ni kashfa ya moja kwa moja kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan na Bunge linalogawa fedha za maendeleo kila jimbo.

Mheshimiwa Mpina tumekuwa tukimshudia Bungeni akipambania maendeleo ya jimbo lake, Mkoa wa Simiyu na Taifa kwa ujumla, na kwa kusema ukweli maendeleo Kisesa yanaonekana dhahiri na jimbo hilo huenda linaongoza kwa maendeleo kati ya majimbo ya vijijini nchini Tanzania.

Mara Mpina hatetei wananchi wake juu ya madhara ya uvamizi wa tembo, huo ni uongo wakati suala hili amelihoji mara kwa mara Bungeni na wote tunasikia…Hata Mzee wetu Mstaafu Job Ndugai akiwa Spika wa Bunge aliwahi kumtania Mpina bungeni kwamba anavyozungumzia suala la tembo mara kwa mara wabunge kutoka Zanzibar wanashangaa kwa sababu kule kwao tembo ni matusi. Amepigania hadi Serikali ikajjenga vituo vya kupambana na tembo jimboni kwake na wewe mwenyewe umewahi kufika na kuviona Leo hii Shemsa unasema Mpina hazungumzii shida za tembo Bungeni?.. una maana gani?

Kiufupi naweza kusema Shemsa, unatumiwana CHADEMA kuiparanganyisha CCM na inawezekana unapewa mulungula na baadhi ya mawaziri ili utumie nafasi yake kulegeza misimamo ya Mpina ya kukataa dhuluma na ufisadi nchini hasa kipindi hiki cha Bunge la Bajeti ambapo mawaziri mbalimbali wanaleta bajeti zao zijadiliwe na wabunge na baada ya kutoka Ripoti ya CAG. Mnatufanya wajinga, mnazani tumesahau Hata mwaka jana ilipofika msimu wa Bunge la bajeti na Ripoti ya CAG kama muda huu tulisikia propaganda nyingi za mashamba huko Morogoro ambapo hadi leo haijulikani ziliishia wapi.

Ushauri wangu kwa Ruhaga Mpina asiyumbe wala asiteteleke kuendelea kuwatetea wananchi wajimbo lake na kutetea raslimali za taifa letu. Tunajua uzalendo wako na ukubwa wa vita uliyonayo, Mungu yupo ataendelea kukutetea. Kwa bahati mbaya au nzuri maadui zako hawakufahamu laiti wangefahamu historia yako hata kidogo wasingepoteza muda kwa porojo na propaganda zao. Wadau tujipe muda mtakuja kuyaamini maneno yangu.

Shemsa umesahau uchaguzi wa mwaka 2010 majimbo ya mkoa wa Simiyu karibia yote yalichukuliwa na upinzani isipokuwa majimbo 3 tu kati ya 7 ikiwemo Jimbo la Kisesa la Mbunge Mpina ambaye yeye unamsakama.

Pia Shemsa watu wanafahamu kuwa hadi una wagombea wako wa mfukoni wa nafasi ya ubunge mwaka 2025 ulioanza kuwauza kabla ya wakati kwenye majimbo ya Maswa Mashariki (wewe mwenyewe Shemsa), Meatu (Salum Mbuzi) Kisesa (Ali Mwarabu) na Busega (Chegeni), Bariadi (Kadogosa). Umeanza kuwachafua wabunge wa maeneo husika huku ukiwaahidi watiania hao kuwa utawapigania kufa na kupona katika teuzi za majina yao kwenye chama kuanzia ngazi ya Wilaya, Mkoa na Hata vikao vya vya NEC huku akiwahakikishia kwamba yeye ana ukaribu sana na Rais Samia.

Mwisho, Ndugu zangu WanaSimiyu inapotokea suala la uchaguzi tusifanye majaribio ya maisha yetu na kizazi chetu, leo mkoa wetu umegeuzwa biashara za watu huku dhuluma na uonevu zikitetewa kwa nguvu zote, tulifikiaje uamuzi wa kumchagua Shemsa kuwa Mwenyekiti wa Mkoa? Mtu ambaye hana rekodi yoyote juu ya jambo lolote alilowahi kulifanya, kwanini hatma ya maisha yetu naustawi wa watoto wetu tunaiweka lehani?.

Wazee wetu mko wapi hadi mkoa wetu unachezewa kiasi hiki? Mmekubaliana na haya yanayoendelea? Mkoa wetu wa Simiyu tunao wazee wengi wenye hekima wanaostahili kupewa nafasi ya Mwenyekiti wa Mkoa na sio huyu Shemsa, tunao wazee kama Mzee Bulu, Mzee Nkenyenge, Mzee Shilingi, Mzee Nghindi, Mzee Makondeko, Mzee Malongo,Mzee Shibuda, Mzee Yuma, Gofilo, Peter Bunyongoli na wengine wengi.

WASALAAM,

Gafalala Nchilu
Simiyu
 
Mkuu bado ndoano iko mdomoni kwa Luhaga Mpina.
CCM imetoa tamko kupitia yule bibi mzuri mashallah.
Kauliza, Luhaga Mpina UMETUMWA?
Yule mama hakukurupuka!
Muda si mrefu ndoano itavutwa!
 
Angalau mkoa wa morogoro na rukwa imekumbukwa baraza la mawaziri hongera uliyepaza sauti mikoa ya tanga na pwani kupewa upendeleo uwaziri
 
Back
Top Bottom