KwetuKwanza
Member
- Mar 13, 2023
- 82
- 150
Sisi Wananchi wa Kijiji cha Imalamate katika Halmashauri ya Wilaya ya Busega Mkoani Simiyu, tunaomba tupaze sauti zetu kwenye hili jukwaa la Jamii Forums.
Kijijini kwetu kuna mgodi wa dhahabu unaitwa EMJ, unamilikiwa na kiongozi mmoja wa CCM Mkoa wa Simiyu (MNEC) anaitwa Gungu Silanga, akishirikiana na wawekezaji ambao raia wa kigeni (kutoka China).
Kijijini hapa kuna mto ambao unapita karibia kijiji kizima (Mto Imalamate) ambao ni tegemeo kubwa sana kwetu kwa shughuli mbalimbali ikiwemo shuguli za kilimo, unyeshwaji mifugo, matumizi ya ndani kama kufulia, kuoga na ufugaji wa samaki.
Kutokana na urefu wake, ndani ya mto huo kuna mito midogo mingi ambayo nayo inaingiza maji kwenye huu mto, moja ya mto mdogo ni unatoka kwenye eneo la mgodi huu wa EMJ.
Miezi miwili imepita, tuligundua hali ya hatari kwenye huu mto, kwanza tuliona samaki wengi ambao wanafugwa kwenye huu mto walikufa, ng’ombe walipokunywa yale maji wakadhoofika.
Mbaya zaidi ndege ambao huwa wanakuja kwenye huu mto kula visamaki, wote walikufa na kukauka kabisa, tumewakuta kando kando ya mto wakiwa wamekufa tayari.
Baada ya kugundua hiyo hali, tulianza kufuatilia kutaka kujua nini tatizo, tulibaini wahusika wa huu mgodi, wamechepusha maji ambayo inadaiwa yana kemikali zenye sumu ambayo wanayahifadhi kwenye bwawa lao, na kuelekeza kwenye mto mdogo ambao unaleta maji kwenye huu mto wetu.
Walichofanya wenye mgodi, walichimba mtaro unaotoka kwenye bwawa la maji yenye sumu lililoko ndani ya mgodi, huo mtaro ukaanza kutiririsha maji hao yenye sumu na kuletea kwenye hicho kijito na kisha kuja huku kwetu.
Ukikanyaga haya maji mwili mzima unawasha, au ukuoga kwa kutumia haya maji, baadhi ya Wananchi ambao walitumia haya maji kuoga, wamekutwa na hiyo hali ya mwili mzima kuwasha.
Kuna mama mmoja miguu yote inawaka moto baada ya kutumia haya maji, amekuwa akitumia madawa mbalimbali lakini hali yake bado ni mbaya.
Tumebaini haya maji yana sumu kali ambayo inatoka kwenye huu mgodi, kwani hadi ndege ambao kila siku walikuwa wakitumia haya maji tumekuta wamekufa.
Kuanzia kule kwenye mtaro ambao walichimba, tumekuta ndege wengi wamekufa ambao walijaribu kutumia hayo maji, yanaonekana yana sumu kali sana.
Uongozi wa kijiji ulihitisha kikao na kututangazia hali ya hatari kwa haya maji, Wananchi kuambiwa tusitishe kuyatumia, mpaka sasa hatujui hatma yetu maana hatuna mbadala wa maji hapa kijijini.
Kwa sasa tunahangaika sana kupata maji ya kutumia hasa kweye kilimo, mifugo yetu na matumizi ya nyumbani ambayo ndiyo muhimu sana, bado mgodi unaendelea kutiririsha maji yenye sumu.
Hakuna kiongozi yeyote wa Mkoa au Wilaya ambaye amefika hapa kusikiliza hii kero yetu, uongozi wa kijiji ulifanya mazungumzo na wenye mgodi lakini hakuna kilichofanyika, bado maji yanatiririshwa.
Tumeamua kuleta hii kero hapa, tukiomba Waziri husika au Mheshimiwa Rais kutusaidia juu ya kero hii, wananchi hatuna mbadala wa maji kwa sasa kwenye kijiji chetu, maji yote yamechafuliwa na huu mgodi.
Pia soma ~ DC Busega: Madai ya Mgodi wa Dhahabu kutiririsha maji yenye sumu kwenye mto lilifanyiwa kazi