Simulizi: Dokta Ivo (Dr. Evil)

Simulizi: Dokta Ivo (Dr. Evil)

JOTO LA MOTO

JF-Expert Member
Joined
Apr 11, 2018
Posts
758
Reaction score
555
Dr Ivo copy.jpg

TITLE: DOKTA IVO

MTUNZI: JOTO LA MOTO
SEHEMU YA KWANZA

NJE-KUNDUCHI BEACH HOTEL-KWENYE BWAWA LA KUOGELEA-MCHANA.
KAZI, kijana mtanashati, miaka 35,akiwa amevalia bukta ndefu ya bluu iliyobana sambamba misuli yake ya miguu, huku akiwa kifua wazi anatembea pole pole kuelekea kwenye bwawa la kuogelea.

Pembeni yupo Nora,Mwanadada mmoja mrembo mwenye muonekano wa kisomali kama sio kihabeshi, miaka kati ya 24 na 27, amejilaza juu ya kitanda kidogo cha mbao kilichopo mita chache kutoka lilipo bwawa lile, mkononi akiwa na glasi yenye juisi ya machungwa, huku macho yake kayaelekeza kwa Kazi.

Kazi anafika kwenye ubao maalum wa kunesanesa uliopo pale kwenye bwawa na kwenda mpaka ulipoishia ubao ule juu ya bwawa,ananesanesa mara kadhaa kisha kwa ustadi mkubwa anaruka juu na kuchumpa kwenye maji. Tukio lile linamfanya Nora kutoa tabasamu moja matata linaloashiria kuvutiwa na anachokiona, huku kwa mapozi akifyonza juisi kutoka kwenye glasi yake akitumia mrija.

Kazi anaogelea kwa ustadi mkubwa mpaka katikati ya bwawa na kisha anageuka kuangalia alipotokea, macho ya Kazi yanatua moja kwa moja kwa Nora hali inayopelekea macho yao kugongana, Nora analegeza macho yake mithili ya Mtu anayejaribu kutuma ujumbe fulani kwa Kazi, hali hii inamfanya Kazi kubaki ameduwaa kama Mtu aliyenaswa na umeme, “Mr Kazi” sauti nzito ya kiume inamshtua Kazi na kumfanya ageuke haraka pembeni na kumuona Bw Jako, Bwana wa makamo, mwembamba wa miaka kama 50 hivi, akiwa amevalia miwani nyeusi na suti maridadi ya kijivu mikono yake ikiwa mifukoni.

Kazi anapiga mikambi kuelekea ukingoni mwa bwawa aliposimama Bw Jako, Jako anatoa bahasha ya kaki kutoka mfuko wa koti lake. “kuna ujumbe wako hapa kutoka ofisini” anasema Jako, “lakini nipo likizo Mr J” anasema Kazi, “sasa unataka nifanyeje..mjumbe hauwawi?” anasema Jako huku akimpa Kazi mkono na kumsaidia kutoka mule kwenye bwawa.

Kazi na Jako wanaelekea zilipo meza na viti mita chache kutoka pale, “kuna muda wa kazi na muda wa kupumzika” anasema Kazi, “unaita haya ni mapumziko?” anasema Jako huku akisindikiza maneno yale kwa kicheko kifupi cha kebehi, “ona wale..wale sasa ndio wapo kwenye mapumziko” anasema Jako huku akimuonyesha Kazi pale alipojilaza Nora, huku kando ya Nora anafika Kijana mmoja mtanashati, wa miaka kama 25 hivi,anafika pale alipo Nora na kuonekana akianzisha mazungumzo na Nora.

Kazi anashusha pumzi mithili ya Mtu aliyekata tamaa ya jambo fulani, anageuka kwa Jako, “hiyo barua ni ya nini?” anauliza Kazi huku akiketi kwenye moja ya viti vile, “kadi ya mchango wa harusi”, anasema Jako huku akimpatia Kazi ile bahasha huku naye vile vile akiketi, “acha utani bro”, anasema Kazi huku akifungua bahasha ile na kutoa karatasi iliyokuwa ndani, “wewe unaoa lini Mzee?” anauliza Jako, Kazi anabaki kimya akionekana kuzingatia ile barua anayoisoma, zinapita sekunde kadhaa Kazi anaisogeza barua pembeni na kushusha pumzi nzito. “kwa nini Mzee kawaacha watu wote kanichagua mimi niliye kwenye likizo?” anasema Kazi, “labda ni kwa sababu wewe ni bachela au labda anakuamini sana kuliko wengine?” anasema Jako huku akitoa pakiti ya sigara mfukoni na kutoa sigara moja na kuiweka mdomoni, anatoa kibiriti cha gesi na kuwasha ile sigara kisha anapiga pafu moja na kupuliza moshi hewani. “nimekuuliza unaoa lini Mzee?“ anauliza Jako, “nitaoa vipi wakati sipati hata muda wa kutumia likizo yangu?” anasema Kazi, “mbaazi ukikosa maua husingizia jua” anasema Jako kwa sauti ya chini, “mmeshaandaa kila kitu?” anasema Kazi baada ya kushusha pumzi ya kichovu, “tiketi ipo tayari na muamala utasoma muda wowote”, anasema Jako, “na uwe makini maana huyo Bwana ni kigogo wa vigogo pale Arusha ni mfupa uliomshinda Fisi” anaongeza Jako huku akibofya simu yake na kusimama kumuonesha Kazi picha iliyopo kwenye ile simu, “huyu Dogo anaitwa Muso.. ana taarifa nyingi muhimu za uchafu wa huyo bwana” anasema Jako huku akimpatia Kazi simu ile, “maelezo mengine yapo kwenye email yako” anaongeza Jako na kisha anapiga pafu kadhaa za sigara, “bila shaka utamaliza kazi mapema ili uje kuendelea na mapumziko yako”, anasema Jako kwa sauti yenye mirindimo ya kebehi.

Kazi anamaliza kuangalia picha ile kwenye simu na kuirudisha simu kwa Jako, “kila la kheri kamanda”, anasema Jako huku akipokea simu yake, anaiweka mfukoni na kuanza kuondoka pole pole, Kazi anabaki ametulia huku amejiiegemeza kwenye kiti kama Mtu anayetafakari jambo, zinapita sekunde kadhaa Kazi anaangalia pale alipokuwepo Nora na kuona kitanda kikiwa bila Mtu, anainuka na kuelekea vyumba vya kubadilishia nguo.

Muda mchache baadae Nora anarudi na kujilaza tena kwenye kile kitanda, amamuita Muhudumu, “yule Kaka aliyekuwa pale yuko wapi?” Nora anauliza, “ameshaondoka” anasema Muhudumu, “shit” anasema Nora kwa sauti ya kukata tamaa.

JIJINI ARUSHA-NDANI YA NYUMBA ALIYOFIKIA KAZI-MCHANA
Kazi na Muso, kijana mdogo, 22, wameketi wote wakiwa na vinywaji mbele yao, Kazi akiwa na kifaa maalum (I pad) akionekana kubofya mara kwa mara akifuatia maelezo ya Muso,“kwa nini umeamua kumgeuka huyu rafiki yako wa muda mrefu?” anauliza Kazi, Muso anashusha pumzi, “nimemchoka tu bro” anasema Muso. “huo sasa ndio ujasiri..Vijana mnatakiwa kuwa hivi..mkiona Mtu anaharibu mambo mtoe taarifa bila kujali nafasi yake” anasema Kazi, “Kwa niaba ya jeshi la Polisi nakupongeza kwa hilo..na ninaamini utanipa ushirikiano mpaka tutakapomfikisha Dokta Ivo kwenye mikono ya sheria” anaongeza Kazi, “tupo pamoja Bro” anasema Muso, “hebu niambie kwa kifupi kuhusu shughuli za Dokta Ivo?” anasema Kazi, “ni mfanya biashara maarufu hapa Arusha..ana biashara za wazi na za chini ya kapeti” anasema Muso, “zipi za wazi unazozijua?” anasema Kazi, “ananunua na kuuza madini ya Tanzanite..ana Migahawa kadhaa hapa mjini..ana kampuni ya ujenzi” anasema Muso, “na za chini ya kapeti ni zipi?” anauliza Kazi, “ana vituo vya kuchezesha kamari ambapo huwa wanaruhusu hata Watoto washiriki na hakuna anayemchukulia hatua yoyote..pia nasikia ana kiwanda bubu cha kuzalisha bidhaa gushi..na anauza dawa za kulevya” anasema Muso, zinapita sekunde kadhaa, “endelea..zipo nyingingine” anasema Kazi, “hizo ndio ninazozifahamu bro” anasema Muso, Kazi anashusha pumzi, “ok..walau tuna kwa kuanzia” anasema Kazi. “na kwa muda huu wote utalazimika kuwepo hapa nyumbani tufanye hii kazi” anasema Kazi, “sawa bro..ila kuna jambo moja” anasema Muso, “ni lipi?”, “kuna rafiki yangu anaitwa Gabu..naomba tuwe nae hapa..maana ni Mtu wangu wa karibu na huwa tunakuwa naye mara nyingi” anasema Muso na kumfanya Kazi atulie kwa muda, “anajua kama uliwasiliana na IGP kuhusu Dokta Ivo?” anauliza Kazi, “anajua kila kitu..hata yeye hampendi Dokta Ivo” anasema Muso, “ok..anaweza kuja..ila awe tayari kufuata masharti yangu” anasema Kazi, “nitahakikisha inakuwa hivyo bro” anasema Muso.

NDANI YA OFISI YA DOKTA IVO-MCHANA.
Ndani ya ofisi moja kubwa nzuri iliyosheheni samani za kifahari na vipande vya madini ya Tanzanaite kwenye moja ya kabati dogo zuri la kioo lililopo kati kati ya ofisi ile, vinavyotoa mvuto wa kipekee.

Dr Ivo, Bwana wa makamo mtanashati, wa miaka kama 55 hivi, ameketi akipitia moja ya faili lililopo mezani kwake. Simu ya mezani inaita, anaiinua na kuiweka sikioni, “Mgeni wako ameshafika Boss” inasema sauti ya kike kwenye simu, “mwambie aingie” anasema Dr Ivo na kurudisha simu mezani, sekunde chache baadae mlango unagongwa na kufunguliwa, anaingia Kazi, “Karibu sana Mr Kazi” anasema Dokta Ivo huku akisimama na kuelekeza mkono wake kwa Kazi, “nashukuru sana Dokta” anasema Kazi huku akijongea na kupokea mkono wa Dokta Ivo, “karibu kiti” anasema Dokta Ivo huku akimuelekeza kwenye moja ya viti vilivyopo mbele ya meza yake, “nashukuru sana..ila nadhani nitaokoa muda..naomba niende moja kwa moja kwenye kazi iliyonileta hapa” anasema Kazi, Dokta Ivo anainua mkono wa simu ya mezani na kubofya mara moja, “niitie Sinta” anasema Dokta Ivo na kurudishia mkono wa simu mezani, “karibu” anasema Dokta Ivo huku akionyesha mkono kwenye meza ya pembeni iliyosheheni thermos kadhaa, vikombe, Jagi za juisi, vitafunwa mbali mbali na makopo kadhaa ya kahawa, milo, cocoa n.k.”usijali Dokta..nipo sawa” anasema Mr Kazi, “habari ya Dar?” anasema Dokta Ivo, “tupo tunapambana Kaka” anasema Kazi na mara mlango unafunguliwa anaingia Sinta, Dada mrembo, 25, mwenye umbo la kuvutia, “Sinta huyu ndio mgeni wetu kutoka Dar..anaitwa Kazi Wajibu” anasema Dokta Ivo, Kazi anamuangalia Sinta na kushindwa kuficha hisia zake huku akipokea mkono wa Sinta, “karibu sana” anatamka Sinta kwa sauti nyororo na ya upole, “nashukuru sana Dada Sinta” anasema Kazi, “ok..huyu ndiye ofisa uhusiano wetu, atakutambulisha kwenye vitengo vyote unavyohitaji kufika kwenye kampuni yetu..na ndiye atahakikisha unajisikia upo nyumbani” anasema Dr Ivo, “nadhani upo tayari” anasema Sinta, “tangu jana” anasema Kazi na kumfanya Sinta kutoa tabasamu moja pevu linalosababisha kuonekana kwa meno yake meupe yaliyopangika vizuri mdomoni, “karibu” anasema Sinta huku akielekea mlangoni na kutoa ishara kwa Kazi amfuate, Kazi anaenda hatua mbili na kugeuka kwa Dokta Ivo, “karibu Arusha Mr Kazi” anasema Dokta Ivo baada ya kuona Kazi amesita kwenda na kugeuka kwake, “upo vizuri Kaka” anasema Kazi, “ila kumbuka sio kila king’aacho ni dhahabu” anasema Dokta Ivo na kumfanya Kazi kubadili uso kama Mtu anayejaribu kutafakari maneno yale, “nadhani tuonane baadae Mr Kazi” anasema Dokta Ivo na kukatisha ile ganzi ya Kazi na kumfanya aelekee mlangoni na kutoka.

.......itaendelea......
 
MTUNZI:JOTO LA MOTO
TITLE: DOKTA IVO
SEHEMU YA PILI

OFISINI KWA DOKTA IVO.
Dokta Ivo anaketi na kuendelea kupekua lile faili lililopo mezani kwake, zinapita dakika kadhaa, mlango unafunguliwa anaingia Jepe, bwana wa makamo, 50, “bado sijaona muamala wowote Mzee” anasema Jepe huku akirudishia mlango na kujongea meza ya Dokta Ivo, “labda ni taratibu za benki tu..lakini umeshatumiwa” anasema Dokta Ivo, “umeweka kiasi gani?” anasema Jepe, “kwani ulikuwa unatarajia kiasi gani?” anauliza Dokta Ivo, “kama ni chini ya ishirini nitakurudishia” anasema Jepe, “kwa kazi gani uliyofanya Jepe..na siku ukitolewa kwenye hiyo ofisi ya uma utanyauka kama Senene wewe”, anasema Dk Ivo, "tatizo lako ni mdomo Ivo" anasema Jepe na kubaki kimya kwa sekunde kadhaa, "huyo Mgeni wako wa Dar ameshafika?” anauliza Jepe, “na kazi ameshaanza” anasema Dokta Ivo, “sasa kwa tarifa yako huyo bwege sio Ofisa wa TRA..huyo Mtu anatokea kitengo” anasema Jepe na kumfanya Dokta Ivo kuweka umakini kumsikiliza Jepe, “angalia usije ukakaa vibaya ukachunguliwa mpaka maini” anasema Jepe na kumfanya Dokta Ivo kubaki kimya, “nakulinda kwa mengi hapa mjini lakini shukurani huna Ivo” anasema Jepe. “upo siriazi kuhusu huyo jamaa?” anauliza Dokta Ivo akiwa bado kwenye hali ya mshangao, “nimekabidhiwa ofisi nyeti kwa sababu wenye nchi wananiamini..kwa hiyo sijali kama wewe hutaniamini”, anasema Jepe, “nasubiri huo muamala..na naomba isiwe chini ya ishirini” anasema Jepe na kugeuka kuelekea mlangoni na kutoka.

Dokta Ivo bado yupo kwenye hali ya kuduwaa, anainua simu na kubofya, “niitie Ndao” anasema Dokta Ivo na kisha kuirudisha simu mezani na kubaki amejiegemeza pale kwenye kiti kama Mtu aliyechoshwa na kazi ngumu, mlango unafunguliwa anaingia Ndao, kijana wa miraba minne aliyekomaa mwili na mikono yenye misuli inayoonekana wazi juu ya ngozi yake ya mikono, wa miaka kama 30 hivi,”hebu mfuatilie huyo inzi tuliyempokea leo asubuhi” anasema Dokta Ivo, “tumalizane nae kabisa ama?” anauliza Ndao, “sio haraka hivyo..we mfuatilie kwanza” anasema Dokta Ivo huku akiwa ameinamisha kichwa chake chini, “pita na idara zote wakae nae chonjo” anaongeza Dokta Ivo, “sawa Boss” anasema Ndao na kisha anageuka na kutoka.

NDANI-OFISINI KWA DOKTA IVO-JIONI
Dokta Ivo ameketi akiwa na glasi yenye pombe kali mezani akipiga funda kadhaa akifuatilia kinachoonekana kwenye televisheni kubwa iliyopo pale ofisini. Anaingia Kazi, “yes boss” anasema Kazi kwa bashasha, “karibu” anatamka Dr Ivo kwa sauti ya chini bila kuonyesha uchangamfu wowote huku bado macho yake yapo kwenye TV, hali inayomfanya Mr Kazi kusita kidogo, “asubuhi uliongea fumbo fulani kaka?” anasema Kazi, “niliongea mambo mengi labda unikumbushe” anasema Dokta Ivo kwa sauti iliyopoa huku bado macho kaelekeza kwenye televisheni, “ulisema sio kila king’aacho ni dhahabu..natamani kujua ulimaanisha nini?” anasema Kazi, “sikumaanisha chochote..wewe kama una mpango na huyo bibie kazi kwako.. jimbo lipo wazi hilo Mkuu” anasema Dr Ivo huku akitoa tabasamu la mbali la kujilazimisha, “ok..jioni njema tutaonana kesho” anasema Kazi na kutoka.

NYUMBA ALIYOFIKIA KAZI-NDANI-USIKU
Kazi, Muso na Gabu, kijana wa miaka 20, mwenye hali ya ualbino, wapo mezani kila mmoja akiwa na sahani ya chakula mbele yake wakipata chakula,“ilikuwaje mkawa marafiki na Dokta” anauliza Kazi, “alikuwa chawa wa Dokta Ivo” anasema Gabu, “nilikuwa msaidizi wake sio chawa”, anasema Muso kwa kumkatisha Gabu, “chawa ni nini?” anauliza Kazi, “yule Dokta si ni Mtu wa totos..sasa Muso ndio alikuwa dalali” anasema Gabu, “kwa hiyo ulikuwa kuwadi wa Dokta Ivo?” anasema Kazi, “nilikuwa msaidizi sio kuwadi” anasema Muso, “sasa ikawaje mkakosana nae?” anauliza Kazi, “Dokta alipita na Demu wa Muso” anasema Gabu, “funga mdomo Gabu” anasema Muso kwa ukali, “kwani uongo man..Mzee hakupita na Chiku” anasema Gabu, “acha umbea..kwani umeulizwa?” anasema Muso kwa ukali, “kwa hiyo ndio sababu ya kumchoma Dokta Ivo kwa Polisi?” anasema Kazi, “hapana hiyo haikuwa sababu” anasema Muso kisha kila mmoja anabaki kimya na kuendelea kula.

NJE YA KAMPUNI YA DOKTA IVO-JIONI
Kazi na Sinta wanatoka mlangoni wakielekea kwenye maegesho ya magari, kila mmoja akiwa na begi dogo la Lap top mkononi, “sitarajii kama na leo pia utakataa mualiko wangu?” anasema Kazi, “Kaka yangu naomba tujikite kwenye kazi iliyokuleta” anasema Sinta kisha anajongea kwenye gari yake na kuingia na kuondoa gari akimuacha Kazi amesimama. Mita chache kutoka pale kwenye ghorofa ya kwanza dirishani amesimama Dokta Ivo, akiwa na glasi yenye whisky mkononi, kupitia dirishani akiangalia pale kwenye maegesho.

NDANI YA OFISI YA DOKTA IVO.
Nora ameketi kwenye moja ya viti vilivyopo ofisini pale akiwa anatumia simu yake ya kisasa. “Asichojua huyu tumbili ni kwamba hakuna aliyewahi kunichimba akabaki salama”, anasema Dokta Ivo kwa sauti ya chini kama Mtu anayejiongelesha mwenyewe, hali inayomfanya Nora kushtuka na kuinua kichwa kumuangalia Dokta Ivo, “unaongea na nani?” anasema Nora huku akisimama na kujongea dirishani pale aliposimama Dokta Ivo, “naongea na yule inzi” anasema Dokta Ivo huku Nora akijaribu kumuangalia Kazi ambaye wakati ule alikuwa anamalizia mguu wake wa kulia kuingia kwenye gari yake, “yule ni nani?” anauliza Nora baada ya kushindwa kumtambua, “ni mbuzi mmmoja tu asiye na maana” anasema Dokta Ivo na kisha kuondoka pale dirishani kurudi kwenye kiti chake, Nora naye anaondoka pale na kwenda kurudi alipokuwa ameketi. “Enhe..ulisema ni nini kimekurudisha mapema?” anauliza Dokta Ivo, “pesa zimeisha Daddy” anasema Nora, “umemalizia dola elfu kumi zote Dar?” anasema Dokta Ivo kwa mshangao, “nilienda na Zanzibar..nimefanya shopping..nimebakiwa na dola mia saba” anasema Nora na kumfanya Dokta Ivo kushusha pumzi, “nakupa dola nyingine elfu kumi tu” anasema Dokta Ivo, “Daddy..basi fanya at least kumi na mbili” anasema Nora kwa sauti iliyojaa kudeka, Dokta Ivo anabaki kimya kwa sekunde kadhaa, “unaenda wapi this time?” anasema Dokta Ivo, “Nairobi then Dubai” anasema Nora, Dokta Ivo anainua simu ya mezani na kuibofya, “niletee dola elfu kumi na mbili” anasema Dokta Ivo na kurudisha mkono wa simu pale mezani, “thank you Daddy” anasema Nora kwa sauti ya kudeka.

NDANI YA MGAHAWA WA DOUBLE K-MCHANA
Kazi ameketi kwenye moja ya meza,ndani ya Mgahawa wenye pilika pilika nyingi kati kati ya jiji la Arusha, huku mezani kwake kuna glasi yenye mvinyo mwekundu akiwa anapiga funda mara kadhaa huku akitumia simu yake kubwa ya kisasa. Anakuja Muhudumu na kumpatia Kazi kipande cha karatasi, Kazi anashtuka na kupokea karatasi ile, anaifungua, “kweli hii dunia ni ndogo..namba yangu hii 09652345” maandishi yanasomeka kwenye karatasi ile, “nani kakupa hii?” anasema Kazi, “yule dada pale” anasema Muhudumu huku akionyesha mkono mita kadhaa kutoka pale ambapo Kazi anamuona Dada mrembo akiwa amesimama huku akikusanya vitu vyake pale mezani na kisha anaelekea mlangoni na kutoka, Kazi anainuka kwa haraka na kwenda dirishani, anamuona Dada yule mrembo akielekea kwenye Gari na kugundua kuwa yule ni Nora, Nora anafika kwenye gari moja jeupe la kifahari aina ya BMW, anafungua mlango na kugeuka kutizama dirishani, Nora anatabasamu huku akipunga mkono na kisha anaingia kwenye gari na kuondoka. Kazi anabaki ameduwaa kwa muda kisha anarudi kuketi kwenye kiti huku akitoa ishara na kumuita Muhudumu, Muhudumu anafika,“unamfahamu yule Dada?” Kazi anauliza, “hapana..mimi ndio leo nimemuona” anasema Muhudumu, Kazi anabaki kwenye hali ya mshangao huku akiangalia kile kipande cha karatasi.

..........ITAENDELEA........
 
SEHEMU YA TATU.

NDANI YA NYUMBA YA KAZI-USIKU

Kazi ameketi juu ya kitanda akiwa anatumia Lap top na simu ikiwa sikioni, “kila kitu kinaenda vizuri Mr J..ila nimelazimika kuhama pale nilipofikia mwanzo” anasema Kazi, “kwa nini?” inasema sauti ya Jako kwenye simu, “machale tu yamenicheza” anasema Kazi, “kwani umeona nini?” anasema Jako, “kuna Dada sijamuelewa” anasema Kazi, “hizo ni hisia zako tu..wewe hakikisha kabla ya kesho unatuma hiyo ripoti kwa ulipofikia mpaka sasa” anasema Jako kwenye simu kisha unasikika mlio wa simu kukatika, Kazi anaitoa simu sikioni na kuendelea kutumia Lap top yake kwa sekunde kadhaa kisha anachukua kipande cha karatasi na kukiangalia kwa muda kisha anachukua simu na kuibofya huku akifuatilizia namba zilizopo kwenyekipande cha karatasi, anaiweka simu sikioni, “hallow” anasema Kazi kwa sauti ya upole, “hallow nani mwenzangu” inasema sauti nyororo ya kike kwenye simu, “tulikutana kwenye mgahawa wa dabo K leo..nikapewa namba zako na Muhudumu” anasema Kazi,kinapita kimya cha sekunde kadhaa, “twaweza kuonana kesho mchana..kama hutojali?” anasema Kazi, kinapita tena kimya cha sekunde kadhaa, “kesho mchana nipo bize” inasema sauti ile na kumfanya Kazi kuonyesha uso wa kukata tamaa, “ila saa moja jioni nitakuwepo Mount Meru Hotel” inasema sauti ile ya kike na kisha simu inakatika, Kazi anaitoa simu sikioni na kushusha pumzi nzito.

NDANI YA OFISI YA KAMPUNI YA DOKTA IVO-MCHANA
Mlango unafunguka wanaingia Kazi na Sinta wakiwa wote wamebeba mafaili kadhaa, wanayaweka mezani, Sinta anageuka na kutaka kuondoka, “Mama anaendeleaje?” anauliza Kazi, “anaendelea vizuri” anasema Sinta, “naomba leo nije kumuona” anasema Kazi, “nitampa salamu zako itatosha tu” anasema Sinta,”sijawahi kuona Mtu anakataliwa hata kwenda kumuona mgonjwa” anasema Kazi, Sinta anashusha pumzi na kisha anaondoka bila kuongea chochote na kumfanya Kazi anabaki anatabasamu, anaketi na kuanza kufungua faili moja baada ya lingine.

NDANI YA HOSPITALI YA MKOA WA ARUSHA-MCHANA
Mama Sinta, Mama wa makamo, 65, amelala kitandani, wanaingia Kazi na Sinta na kufika kitandani pale, “Mama unaendeleaje?” anasema Sinta, “Mungu mkubwa naendelea vizuri..naona umeniletea mgeni” anasema Mama Sinta huku akitoa tabasamu kwa mbali, “ni mgeni wa Kampuni..anatokea Dar..anaitwa Kazi” anasema Sinta, “Mama shikamoo” anasema Kazi, “marahaba mwanangu” anasema Mama Sinta, “vipi hali yako?” anasema Kazi, “namshukuru Mungu mwanangu” anasema Mama Sinta, “Mama tumeambiwa muda bado kidogo..tunasubiri hapo nje kwa dakika kumi na tano alafu tutarudi” anasema Sinta kisha Kazi na Sinta wanatoka, hapo hapo anaingia Chiku, binti mrembo mwenye mapepe, 22,huku akiwa ameachama mdomo wazi kuashiria anashangazwa na jambo analoliona,“Dada Sinta kapata mchumba?” anasema Chiku huku akifikia kitandani kwa Mama Sinta, “hebu fuata mambo yako ukoje wewe lakini?” anasema Mama Sinta kwa sauti ya chini lakini yenye kuashiria kuwa amekwazika,”umepata hiyo dawa?” anasema Mama Sinta,”nimeipata” anasema Chiku huku haraka haraka akitoa boksi dogo kutoka kwenye pochi yake na kuliweka juu ya meza ndogo iliyopo pembeni mwa kitanda, kwa haraka anaelekea mlangoni na kutaka kutoka, “unaenda wapi?” anasema Mama Sinta, “narudi sasa hivi” anasema Chiku, “njoo hapa nataka kukutuma tena” anasema Mama Sinta na kumfanya Chiku kusimama na kuvuta mdomo, kabla ya kurudi na kuketi kinyonge pale juu ya kitanda pembeni ya Mama Sinta, “umezidi umbea..sijui kwa nini huna heshima kwa Dada yako wewe” anasema Mama Sinta huku Chiku akibaki anamkata jicho la kiburi Mama Sinta.

NDANI YA MGAHAWA ULIOPO NJE YA HOSPITALI-MCHANA
Kazi na Sinta wapo mezani wakiwa kila mmoja na chupa ya soda mezani, “Mama yako bado kijana kabisa” anasema Kazi, “ana miaka sitini na kitu pale” anasema Sinta, “duuh..anaonekana kama yupo kwenye arobaini na kitu hivi” anasema Kazi na kumfanya Sinta kuguna, zinapita sekunde kadhaa “nitafurahi sana kama tutapitia mahali kwa chakula tukitoka hapa” anasema Kazi, Sinta anabaki kimya kwa sekunde kadhaa, “nilishakuambia Kaka yangu..naomba tubaki kikazi zaidi” anasema Sinta, “Sinta nimeshapeleleza nikaambiwa huna Mwenza kwa sasa..kwa hiyo sioni ni wapi unabanwa na majukumu”,anasema Kazi, Sinta anaguna, “huko ulipopeleleza nadhani hujapeleleza vizuri” anasema Sinta, “una maana gani Sinta” anasema Kazi, “kwa sababu hujafahamu kila kitu unachopaswa kufahamu” anasema Sinta, “hata wewe unaweza kunifahamisha Sinta” anasema Kazi, wote wanabaki kimya kwa muda, Sinta anaangalia saa ya mkononi na kustuka, “muda tayari”, anasema Sinta huku akisimama, Kazi naye anasimama na wanatoka.

NDANI NYUMBANI KWA KAZI-MCHANA
Muso na Gubu wameketi wanaangalia TV huku wakila pop corn zilizopo kwenye bakuli kubwa pale mezani, mlango unagongwa, Muso anaenda kuufungua mlango, anaingia Chiku huku akiwa kama aliyetoka kukimbizwa na Mtu au Mnyama, “kaeni niwape umbea wa moto moto” anasema Chiku huku anahema na kuenda kuketi kwenye kochi, “nimemuona yule Kaka yenu yupo na Dada Sinta” anasema Chiku, “wapi?” anauliza Muso, “hospitali” anasema Chiku, “leo?” anasema Gabu, “leo hii nilikuwa pale” anasema Chiku, “yaani Sister wangu yule akiona Mwanaume handsome hachezi mbali..kama mnampenda Kaka yenu mwambieni akae nae mbali asije akanaswa” anasema Chiku huku akiwaacha Muso na Gabu wameduwaa wakimtazama anavyobugia zile popcorn kwenye bakuli.

NDANI YA HOTELI YA MOUNT MERU-USIKU
Kazi na Nora wapo mezani, wote wakiwa na sahani zenye vitafunwa na glasi zenye mvinyo “naitwa Nora” anasema Nora, “nashukuru kukufahamu, “mimi naitwa Mr Kazi..nipo mamlaka ya mapato..nadhani nilikuona Dar siku chache zilizopita?” anasema Kazi, “unajua sana kuogelea” anasema Nora, “na leo nipo Arusha na wewe upo Arusha” anasema Kazi, “nilikodisha spy akufuatilie popote uendapo” anasema Nora na kisha kuachia kicheko laini, usoni Kazi akionekana kujitahidi kuficha hali ya mshtuko, “nina imani kabisa haiko hivyo” anasema Kazi, “nahitaji Mwalimu wa kunifundisha kuogelea”, anasema Nora kwa sauti iliyojaa mapozi, Kazi anashusha pumzi, “mimi huwa nalipisha mamilioni kumfundisha Mtu” anasema Kazi, “basi kumbe nipo na Mtu sahihi..wewe una ujuzi mimi nina pesa” anasema Nora, wanabaki kimya kila mmoja akimega kitafunwa na kunywa mvinyo “jinsi tulivyokutana tena..naona ni kama muvi vile” anasema Kazi baada ya kushusha pumzi, “wanasema milima ndio huwa haikutani sio binadamu” anasema Nora, kinapita kimya kifupi, “naomba niambie kidogo kuhusu wewe” anasema Kazi, “wewe ni spy?” anasema Nora na kumfanya Kazi kushtuka huku akijikaza kutoionyesha hali hiyo, “noo..kwa nini unauliza hivyo?” anasema Kazi, “kwa sababu unauliza swali la ki spy” anasema Nora, “hapana..ningetamani tu kujua mrembo kama wewe unatokea wapi na unafanya nini kuishi hapa mjini?” anasema Kazi, “ok..mimi ni mfanya biashara wa vito..Mama yangu ni Mnyarwanda..Baba ni Mtanzania” anasema Nora, “nilihisi tu utakuwa na damu ya Rwanda” anaseama Kazi, “kwa nini?” anauliza Nora, “mwenye macho haambiwi tazama” anasema Kazi na kumfanya Nora kutoa kicheko chepesi cha uongo, unapita ukimya kwa sekunde kadhaa “Mama yangu alikuwa ofisi ya ubalozi hapa Arusha..ndio wakakutana na Baba..Baba alikuwa ana kandarasi ya kusambaza vifaa vya ofisi”, anasema Nora. Kinapita kimya kifupi, “umeolewa?” anauliza Kazi, “nipo kama wewe tu” anasema Nora, “una maana gani?” anauliza Kazi, “sioni pete kidoleni kwako” anasema Nora na kumfanya Kazi kujiangalia vidoleni huku akiachia kicheko cha kujilazimisha, “miaka mitano iliyopita niliozeshwa kwa Mwanaume kule Rwanda..baadae nikamtoroka maana hakuwa chaguo langu” anasema Nora, “duuh..sasa huyo mwenzako umemuacha kwenye hali gani?” anauliza Kazi, “ni muda mrefu kila mtu anaendelea na maisha yake” anasema Nora, “mlijaaliwa Mtoto au Watoto?” anauliza Kazi, “Watoto wawili..wote bado anaishi nao” anasema Nora, zinapita sekunde chache kila mmoja akipiga funda la mvinyo, “kwa hiyo makazi yako ni Rwanda au Tanzania?” anauliza Kazi, “kote..Rwanda na Tanzania..ila nikipata kampani Bongo nitabaki Bongo muda wote” anasema Nora na kumuacha Kazi akibaki anamuangalia Nora anayepiga funda ya mvinyo wake.

NDANI YA CHUMBA CHA HOTELI YA MOUNT MERU-USIKU
Kazi na Nora wapo kitandani wamelala usingizi, Kazi anafungua macho huku Nora bado akiwa bado usingizini, zinapita dakika chache Kazi anawasha tochi kutoka kwenye simu yake na pole pole anaingiza mkono chini ya mto aliolalia Nora na kuitoa simu ya Nora, anatoka kitandani pale pole pole na kuelekea chooni, anaingia na kurudishia mlango, anaketi kwenye siti ya choo na kuanza kupekua simu ya Nora, zinapita dakika kadhaa, Kazi anatoka na kwenda kwenye dressing table, anafungua pochi ya Nora iliyopo juu ya meza ile, anapekua akiangalia hiki na kile, anatoa kadi ya benki yenye jina, “Nora Seba Ivo”, anarudisha na kutoa leseni ya udereva inayosomeka jina “Nora Seba Ivo”, Kazi anabaki na mshangao, anatoa picha inayomuonesha Nora akiwa na Dokta Ivo

Kazi anatoa macho akiwa kwenye mshangao mkubwa,kwa haraka anarudishia vitu kwenye pochi na pole pole anarudi pale kitandani na kumkuta Nora akiwa amefungua macho, “vipi?” anasema Nora, “nilikuwa bafuni” anasema Kazi kwa sauti yenye uoga huku akiificha simu ya Nora, anapanda kitandani, “ni saa ngapi?” anasema Nora, “saa tisa” anasema Kazi, Nora anaguna na kisha anarudi kulala fo fo fo, Kazi pole pole anairudisha simu ya Nora chini ya Mto.

NDANI YA CHUMBA CHA HOTELI YA MOUNT MERU-ASUBUHI
Kazi anavaa shati na kufunga vishikizo, Nora anatoka bafuni akiwa na taulo kiunoni, “unafahamiana vipi na Dokta Ivo?”, anasema Kazi na kumshtua Nora, “ni baba yangu..kwa nini unauliza?” anasema Nora akiwa amemkazia Kazi macho, “no nimeuliza tu” anasema Kazi huku akijitahidi kuficha hisia zake za mshtuko, “unamfahamu?” anasema Nora, “ni bilionea kila Mtu anamfahamu” anasema Kazi, “nilikwambia Baba yangu ni Mtanzania Mfanya biashara?” anasema Nora, “nakumbuka” anasema Kazi, kinapita kimya kifupi, “Mzee wako ana kiwanda?“ anasema Kazi, “mmh..ni kama godauni hivi..ndani ndio kuna viwanda bubu..yeye hupaita Wen shu”, anasema Nora, “naweza kutembelea hapo Wen shu?” anasema Kazi, “wee” anasema Nora kwa sauti kali ya kutahadharisha, “hataki Wageni waende pale” anasema Nora, “ila mimi sio mgeni” anasema Kazi, “no way..hata unipe dola milioni kumi” anasema Nora, wanakuwa kimya kwa muda, “kwa hiyo si tunaenda wote Dubai ama?” anasema Nora, Kazi anabaki kimya, “gharama zote za safari juu yangu..na shopping juu”, anasema Nora, “nitakujibu baada ya kunipeleka Wen shu” anasema Kazi huku akimalizia kuvaa viatu na kusimama, “hivi upo siriaz?” anasema Nora, “wewe upo siriaz na safari ya Dubai?”, anasema Kazi, “unataka kuniletea balaa Kaka yangu” anasema Nora na kushusha pumzi, “mimi ngoja nawahi ofisini” anasema Kazi na kumfanya Nora kuinuka pale kwenye dressing table na kumkumbatia Kazi na kumpa busu zito, “tuonane muda wa lunch” anasema Nora na kumuachia Kazi, Kazi anafungua mlango na kutoka.

NDANI YA OFISI KWENYE JENGO LA DOKTA IVO-MCHANA
Kazi ameketi akitumia Lap top yake, anasikia mlio wa gari kufika, anainuka na kuangalia dirishani, anawaona Nora na Dokta Ivo wakiteremka kwenye gari nakuanza kuja kwenye ofisi aliyopo, Kazi anashtuka, anarudi kuketi na kuchukua faili lililopo mezani na kujiziba usoni kama Mtu anayejaribu kusoma kitu kwa makini kutoka faili hilo, Nora akiwa mbele ya Dokta Ivo anakaribia alipoketi Kazi, “ni huku” anasema Dokta Ivo na kumfanya Nora kugeuza njia na kumfuata Dokta Ivo, Kazi anatoa faili usoni na kushusha pumzi, Zinapita dakika kadhaa. Anakuja Sinta akiwa na thermos na kikombe, anaweka mezani na kumimina chai kwenye kikombe, “karibu” anasema Sinta huku akisogeza kikombe kile kwa Kazi, “shukran Sinta” anasema Kazi,”natamani haya unayonifanyia hapa yangeendelea kwa maisha yangu yote” anaongeza Kazi, “futa hayo mawazo Kazi..hilo haliwezi kutokea” anasema Sinta, “usiseme hivyo Sinta, anasema Kazi huku Sinta akianza kuondoka pale, “kuna kitu ulisema utaniambia” anasema Kazi na kumfanya Sinta kusimama na kubaki ametulia, “nitakwambia muda si mrefu” anasema Sinta na kisha kufungua mlango na kutoka.

.............ITAENDELEA.........
 
SEHEMU YA NNE.

NDANI NYUMBANI KWA KAZI-MCHANA

Kazi ameketi kwenye kochi, mlango unagongwa, Kazi anainuka na kwenda kuufungua mlango, anaingia Mr Jako, “nilidhani utapotea” anasema Kazi, “kwa kazi yangu siruhusiwi kupotea” anasema Jako huku akiingia na kwenda mpaka pale sebuleni na kubaki amesimama, “enhe umefikia wapi mpaka sasa?” anasema Jako, “nimefikia pazuri” anasema Kazi, “sio kweli Kazi” anasema Jako, “taarifa zilizopo ofisini ni mbaya” anasema Jako na kumfanya Kazi kushtuka, “Bwana mkubwa anasikitika sana..maana siku zote aliamini kwako linapokuja suala la kazi Mwanamke hana nafasi” anasema Jako, “wakati huu imekuwa kinyume chake..Wanawake ndio wamekuwa kipaumbele” anasema Jako huku Kazi akibaki ameduwaa, “umekuwa wa kukimbizana na Wanawake badala ya kazi” anaongeza Jako, “sijui hayo mmeyatoa wapi Mr Jako” anasema Kazi, “dunia inakuona Kazi” anasema Jako, wanakuwa kimya kwa muda, “umetuangusha sana Kazi..Bwana mkubwa anaomba tu urudi Dar atateua Mtu mwingine” anasema Jako na kisha anaondoka, Kazi anaketi kwenye kochi kama Mtu aliyechoka. Zinapita dakika kadhaa mlango unafunguliwa anaingia Muso, “afadhai nimekukuta bro” anasema Muso, “kuna nini?” anasema Kazi, “kuna kitu nataka kukuambia..kuhusu Dada Sinta” anasema Muso na kumfanya Kazi kushtuka, “umemfahamia wapi?” anasema Kazi kwa mshangao,
“mdogo wake ni rafiki yangu..na juzi alikuona nae” anasema Muso na kumshtua Kazi, “hebu sema unachotaka kusema” anasema Kazi, “Dada Sinta anaishi na vvu" anasema Muso na kumuacha Kazi ameduwaa kwa muda akimuangalia Muso “una uhakika Muso?” anauliza Kazi, “Mwanaume aliyekuwa anaishi nae alifariki mwaka juzi” anasema Muso na kumfanya Kazi kubaki kimya pale kochini, Muso anainuka na kubaki amesimama kwa sekunde chache, “pole bro” anasema Muso na kisha anaondoka akimuacha Kazi ameketi ametulia.

NJE KWENYE BUSTANINI YA JIJI ARUSHA-MCHANA.
Kazi ameketi kwenye benchi, anakuja Sinta na kufika alipo Kazi, “karibu” anasema Kazi huku akitoa tabasamu pevu, “nashukuru..ila ni kama nilivyokuambia kwamba sitakuwa na muda” anasema Sinta huku akiketi kwenye benchi, “nilitaka tu kukuomba usipoteze muda wako kwangu” anaongeza Sinta, “kwa sababu mimi nilishachagua maisha yangu mengine..sipo tayari kwa mahusiano tena maishani kwangu” anasema Sinta kwa sauti ya chini yenye mitetemo ya hofu, “kwa nini iwe hivyo Sinta?” anasema Kazi kwa sauti ya upole, “ninaishi na..” “Sinta..nafahamu hali yako” anasema Kazi na kumkatisha Sinta, Sinta anashtuka na kumuangalia Kazi, “umefahamu lini?” anasema Sinta, “ni muda sasa” anasema Kazi na kumfanya Sinta kubaki ameduwaa, “sasa inakuwaje kama unafahamu hivyo bado unahitaji kuwa na mimi?” anauliza Sinta kisha anainuka, "lengo lako ni nini kwangu" anasema Sinta na kuondoka, “Sinta” anaita Kazi huku akiinuka na kumfuata Sinta, “kwa heri Kazi” anasema Sinta huku anaendelea kwenda, Kazi anasimama na kubaki amejishika kiunoni.

NJE YA DUKA KUBWA LA BIDHAA MCHANGANYIKO-MCHANA
Kazi akiwa na mfuko mdogo mkononi kwake anafika lilipopaki gari la Nora, anafungua mlango na kuingia, “wameniambia mpaka kesho asubuhi hati yangu ya kusafiria itakuwa tayari..tuanze safari yetu ya Dubai” anasema Kazi, “safi sana” anasema Nora na kumbusu Kazi shavuni, “tuanzie wapi?” anasema Nora, “wen shu” anasema Kazi na kumfanya Nora kutoa tabasamu, “hujasahau tu?” anasema Nora huku akiwasha gari, anarudisha nyuma na kuondoka.

NJE KWENYE MSITU MKUBWA WA MERU-MCHANA
Gari la Nora linafika na kusimama, “lile ndio godaini la wen shu” anasema Nora, Kazi anataka kuteremka, “wee” anasema Nora kwa sauti wa kumshtua Kazi na kumfanya Kazi kuufunga ule mlango kwa haraka, “Mzee anaweza kutokea saa yoyote akiniona nipo na Mtu ataniua” anasema Nora, “kwa nini amepaita wen shu?’ anasema Kazi, “wanabandika majina bandia kwenye bidhaa bandia” anasema Nora,”Baba yako ni giniaz” anasema Kazi, “hata baadhi ya vinywaji vikali wanachanganya na kubandika lebo” anasema Nora, “duuh” anasema Kazi,zinapita sekunde chache, “nimekwambia tu kwa sababu umekubali twende wote Dubai…naomba usije ukamwambia Mtu yeyote” anasema Nora na kumfanya Kazi kutikisa kichwa kama ishara ya kukubali anachokisema Nora, kinapita kimya kifupi “si umeshaona tuondoke kabla hajatokea” anasema Nora baada ya kushusha pumzi kidogo, na kisha kuwasha gari na kuweka gia ya kurudi nyuma, anageuza kichwa na kuona landrova nyeusi imepaki nyuma yao, “my God” anasema Nora kwa mshtuko mkubwa na kumfanya Kazi nae ageuke nyuma kwa mshtuko, “ni kina nani?” anasema Kazi, “watu wa Mzee..laza hicho kiti chako” anasema Nora na kisha anateremka, Kazi analaza kiti na kujilaza, wanashuka Kebwe na Ndao kutoka kwenye landrova, “kuna shida gani?” anasema Nora, “kumbe ni wewe” anasema Kwebe, “nimekuja kutembea kidogo nimechoka kukaa mjini” anasema Nora, “uwe unatoa taarifa ukitaka kuja” anasema Ndao, “ilikuwa maamuzi ya ghafla” anasema Nora, “upo mwenyewe?” anasema Kwebe huku akisogelea gari la Nora, “siku zote nipo mwenyewe” anasema Nora, “yule ni nani” anasema Nora kwa sauti kali na kuwashtua Kwebe na Ndao, “wapi?” anauliza Ndao kwa mshtuko, “nimeona kama pikipiki imepita kwenda hivi” anasema Nora huku akielekeza kwa mkono na kuwafanya Ndao na Kwebe kurudi kwenye landrova na kuondoa gari kwa kasi, Nora anarudi kwenye gari, anashusha pumzi, “ilikuwa almanusura”, anasema Nora huku akiweka gia ya rivasi na kisha kuondoa gari kwa kasi, Kazi anarudishia kiti sawa, “inaonyesha Baba yako anatisha” anasema Kazi huku akimuangalia Nora kwa mshango, “hanaga urafiki kwenye biashara zake” anasema Nora huku akivurumisha gari kwa mwendo wa kasi, zinapita sekunde kadhaa, “naona gari unaimudu” anasema Kazi na kumfanya Nora kugeuka kumuangalia huku akiachia tabasamu laini, “nataka na wewe uwe gari langu” anasema Nora huku akiongeza wigo wa tabasamu. Gari linaendelea kwenda kwa kasi.

NJE.BARABARA YA MOSHI ARUSHA-MCHANA.
Gari la Nora likiwa kwenye mwendo wa kasi linafika ulipo Mti mkubwa pembeni ya bara bara na kusimama chini yake, Nora anashusha pumzi huku Kazi akibaki anamuangalia Nora kwa mshangao, "Kazi" anaita Nora kwa sauti laini inayomfanya Kazi kutoa macho kama ishara ya kuongeza umakini wa kumsikiliza Nora ambaye naye anamuangalia Kazi kwa macho yaliyojaa hisia, "nimefanya hii yote kukuonyesha jinsi gani nina mapenzi kwako..kwa ukatili wa Baba yangu sijui angetufanya nini kama angetukuta pale" anasema Nora na kutulia kwa muda, "tangu siku ile nimekuona pale Dar moyo wangu umepigwa muhuri wa moto wa picha yako..nadhani hata kukutana kwetu mara ya pili ni mpango wake Mungu..I love you" anasema Nora na kumfanya Kazi kushusha pumzi laini, "naomba tusimalize yote hapa Nora...tusubiri tufike Dubai" anasema Kazi na kubaki wanaangaliana na Nora kwa muda, kisha Nora anafungua mkanda wa kiti chake na kujiinua na kumkumbatia Kazi na kuanza wakipeana busu nzito nzito.

NDANI NYUMBANI KWA KAZI-USIKU
Kazi, Gabu na Muso wapo meza ya chakula, “nyumbani hayupo na wala hapatikani kwenye simu” anasema Kazi kwa sauti ya chini ya kukata tamaa, “labda amesafiri nje ya Arusha” anasema Muso. Kunapita kimya kwa sekunde kadhaa, “natoa laki moja kwa yeyote atakayeniwezesha kujua alipo Sinta”, anasema Kazi na kuwafanya Muso na Gabu kushtuka na kuangaliana, “ngoja tuingie kazini bro”, anasema Gabu, “kesho tunakupa jibu bro” anasema Muso, “chiku lazima anajua Sinta alipo” anasema Gabu, “Chiku ni nani?’ anasema Kazi, “ni mdogo wake Sinta” anasema Muso.

..........ITAENDELEA.......
 
Back
Top Bottom