Simulizi: For You

Simulizi: For You

FOR YOU

Story by Elton Tonny

Familia, Urafiki, Mapenzi, Tamaa, Hila, Usaliti, Unyanyasaji, Uhalifu, Mauaji, Visasi, Vita, Mambo yasiyotazamiwa

R-rated 18+

Enjoy!

★★★★★★★★★★★★★★★★

SEHEMU YA KUMI NA NNE

★★★★★★★★★★★★★★★★


MIAKA NANE BAADAE.....

Miaka hupita haraka, na katika kisa hiki hali haikuwa tofauti. Miaka nane ilikuwa imepita tokea wakati ule mbaya sana kuwahi kuikumba nchi. Watu wengi waliuawa kipindi kile ambacho kama ungemuuliza mtu fulani siku za wakati huu kuhusu kipindi hicho, angekwambia kilikuwa kinaitwa "enzi za Demba Group," ijapokuwa haukuwa umepita hata muongo (miaka 10).

Raisi Paul Mdeme bado alikuwa madarakani, pamoja na wasaidizi wake wengi kwenye vyeo vyao vya kisiasa ambao walikuwa wafisadi na wanafiki kama yeye tu. Kipindi cha miaka miwili nyuma kilikuwa kipindi cha uchaguzi mkuu wa viongozi nchini, naye kama kawaida yake alisaidiwa kushinda tena uraisi kupitia udanganyifu uliofanywa na watu waliomuunga mkono na aliowalipa kuchakachua matokeo. Alipenda kutupa pesa za sifa kwa "chawa" wake wengi na kufurahia anasa sana.

Kuna vitu vipya alivyovijenga kwenye nchi ambavyo vilifanya ionekane kwamba yeye ni Raisi mzuri sana, lakini ukweli ni kwamba alikuwa akiwanyonya watu kwa njia ambazo hawakutambua kirahisi. Si wote waliokuwa na maisha mazuri, kwa sababu matajiri wangeendelea kubaki matajiri, na masikini, masikini. Sera yake ya kuboresha maisha ya wananchi WOTE ilikuwa imeshindwa sana, naye aliendelea kufanya mambo mengi haramu (illegal) bila kujulikana, kama tu kipindi kile cha Demba Group.

Jenerali Jacob Rweyemamu. Ah! Shetani wa mashetani. Bado alikuwa kwenye cheo chake hicho, naye pia aliendelea kufurahia anasa kutokana na unyonyaji walioufanya yeye na kundi lao lote lililoshiriki vitendo vile vya ukatili miaka nane iliyopita. Alikuwa pia aina ya kiongozi wa jeshi mwenye kuogopwa sana, na hata ingeweza kupita mwaka kaonekana hadharani mara mbili au mara tatu tu, kwa sababu kazi nyingi aliwaachia wengine wafanye huku yeye akifurahia starehe na wanawake tu. Bado waliendelea kuungana mkono na Raisi Paul Mdeme, hivyo kihalisi taifa lilikuwa kwenye hali inayoweza kuitwa "siyo sawa."

Weisiko naye alikuwepo, akiwa bado na cheo chake cha Luteni Jenerali kilichofuata cha Jenerali Jacob. Bado alikuwa mtu makini sana, aliyetekeleza mambo yote ambayo Raisi na Jenerali walimwagiza kufanya. Alifurahia pia mali nyingi alizojichumia kwa kuwa upande wao, na mambo ya kikatili hakuwa ameacha. Nyakati ambazo watu fulani wangezingua utendaji wa Raisi au Jenerali, Weisiko aliongoza mauaji yasiyo ya moja kwa moja kwao ili kuwanyamazisha, na hivyo kufanya kelele ziwaondokee wakuu wake.

Kulikuwa na maoni mchanganyiko kutoka kwa wananchi kuhusiana na utendaji wa viongozi na maendeleo ya nchi. Kwa asilimia kubwa, wengi waliona ni kama walikuwa wakinyonywa na hakukuwa na maendeleo ya aina yoyote, huku ile ndogo ikiwa yenye kuiunga mkono serikali hiyo na uongozi wake. Asilimia hii ndogo ndiyo ya wale "chawa" ambao walikuwa wanapenda tu kushabikia viongozi ili wapate faida. Wabunge wengi, mawaziri, madiwani, na hata maaskari walitenda kwa njia zenye ubinafsi sana zilizowaumiza wananchi wengi. Kwa wengi wa viongozi ilikuwa ni kufanya tu safari za nje ya nchi na kuishi maisha ya gharama sana, huku watu sehemu mbalimbali wakipitia magumu ambayo yalihitaji uangalizi wao lakini hawakupata.

Kwa hiyo hivyo ndivyo jinsi maisha yalivyokuwa chini ya utawala wa Mdeme ambao kwenye runinga ulisifiwa sana lakini kwenye uhalisia ulikuwa ukikashifiwa sana. Lakini muda si mrefu, mambo mengi yangebadilika kwa njia ambayo haingetazamiwa.


★★★★


Ikiwa ni ndani ya kipindi hiki hiki cha utawala wa Mdeme, jambo fulani lenye kushangaza sana lilitokea. Majengo ya benki kuu ya nchi yalivamiwa na kundi la wezi lisilojulikana, na kundi hilo lilibeba pesa nyingi sana kupita maelezo. Yaani, hakukuwahi kutokea kitu cha namna hiyo popote pale, kwa sababu ziliibiwa jumla ya pesa taslimu za kitanzania TRILIONI 20! Yaani trilioni 1 ni sawa na bilioni 1000, sasa piga hesabu trillioni 20 ni sawa na billioni ngapi. Haloo... si mchezo! Hizo zilikuwa ni pesa nyingi sana, na ilishangaza wengi kuhusu ni jinsi gani ziliweza kutolewa kwenye majengo hayo, zikiwa za karatasi kabisa (cash), na watu hao wasikamatwe.

Kwenye majengo hayo siku hiyo ya wizi yalilipuka mabomu mawili, moja kwenye kila jengo. Zilipita SIKU MBILI bila ya waandishi wa habari kuruhusiwa kuingia maeneo hayo ili kujua ni nini hasa kiliendelea, ndipo baada ya hapo wakaruhusiwa na taarifa hizo zikaanza kusambaa sasa. Viongozi walichanganyikiwa balaa. Yaani maneno yalisemwa na kusemwa mpaka ikawa kama kituko. Raisi Paul Mdeme alikuja kutoa tamko lake la hadharani na kusema wezi hao wangekamatwa tu, kwa sababu hawangeweza kutoroka na kitita kikubwa namna hiyo cha pesa. Sehemu za mipaka zilifungwa kutoruhusu yeyote kuondoka mpaka wahakikishe wanawakamata watu hao.

Lakini wadau wengi bado waliuliza; iliwezekanaje kweli, eti wezi waibe trillioni 20 kwenye makao makuu ya pesa yenye ulinzi mkali, wasikamatwe, halafu waje kukamatwa baadae? Wengi waliona huenda kuna mchezo umefanywa na viongozi kuiba pesa hizo na kusingizia wezi, kwa sababu ni kitu ambacho hakikupatana na akili kabisa, lakini hakuna aliyekuwa na uhakika. Msako ulioendelea ulihusisha maaskari na wanajeshi, wataalamu wa mambo ya teknolojia na mitandao ili kuweza kuwapata wezi hao, lakini hawakufanikiwa hata kidogo!

Kama ni kitu ambacho kiliachwa na wezi hao nyuma, ilikuwa ni kibandiko (sticker) chenye mchoro wa sura ya mnyama kama simba mweupe anayeonyesha meno yake kwa ukali, na chini ya mchoro huo yalikuwa maneno "MESS MAKERS." Kwa hiyo wezi hao walikuwa kama wameacha alama ya utambulisho wao, kama kundi fulani hivi la kigaidi, na jina lao lilikuwa likimaanisha "watu wanaochafua mambo." Watu wengi, hasa wahuni, waliwaita "chafu." Mitandao ya kijamii ilifurika kwa mijadala yenye ucheshi mwingi kuhusiana na tukio hilo, na haikupita siku yoyote ile bila jina "Mess Makers" kutajwa kwenye vipindi vya habari kwenye runinga.

Ilikuwa ni jambo liliohitaji kufanyiwa ufumbuzi mapema sana, kwa sababu pato la nchi liliporomoka kwa asilimia kubwa kuwahi kutokea, na mipango mingi ya kimaendeleo iliyokuwa imewekwa isingefanikiwa hata kidogo......


★★★★


DAR ES SALAAM

Ndani ya jengo la makao ya muda mfupi ya viongozi wa Jeshi la nchi, kulikuwa na mgeni maalumu kutoka kwenye Wizara ya Polisi, ambaye alikuwa ni "Principal Secretary" wa mambo ya ndani yaliyohusiana na jeshi la polisi. Aliitwa Joachim Uwesu, naye alikuwa amefika hapo ili kuwapatia taarifa muhimu Kanali Oswald Deule na Kapteni Erasto Shimuye wa Jeshi la Nchi, iliyogusiana na suala zima la msako wa wezi wale kwenye makao makuu ya benki kuu nchini. Alikuwa amefika kwa niaba ya Inspekta Jenerali wa Polisi, IGP Donald Ngassa, ambaye alikuwa sehemu nyingine ya mkoa akiendesha operesheni zingine maalumu.

"Zimepita siku kumi na moja toka watu hao walipoiba mabilioni ya pesa na mpaka sasa hawajajulikana na kukamatwa. Maneno mengi yanazagaa, na hali ya kiuchumi nchini imeanza kuporomoka kwa huge estimates za asilimia.... jamani, ndani ya mwezi mmoja mambo mengi kimiradi yataanza kuporomoka zaidi na zaidi. Nimeagizwa kukuletea pendekezo katika suala la kuwakamata watu hao..." akasema Secretary Joachim.

Akampatia faili fulani Kanali Oswald, naye baada ya kulifungua, akalitupa mezani kwa kukerwa.

"Principal Secretary... unafikiri mimi sijui jinsi ya kufanya kazi yangu?" Kanali Oswald akamuuliza.

"Hapana mkuu, siyo hivyo, ni kwamba...."

"Sijali umeagizwa na nani. Sihitaji msaada wake kwa kuwa kila kitu kiko under control. Nenda kawaambie waliokuagiza kwamba ninashughulikia mambo yote ipasavyo, sihitaji babysitter," Kanali Oswald akasema.

"Kumradhi mheshimiwa Kanali, lakini hili ni pendekezo muhimu sana. ACP Lois...."

"Hakukuwa na haja ya kumwita hapa! Hili suala tunaweza kulishughulikia sisi wenyewe, kwa kuwa tunajua zaidi ya hao maaskari," akasema Kanali Oswald.

"Ninaelewa Kanali, na ninaheshimu sana kila jitihada ambayo mmeweka katika hilo. Lakini tunahitaji sana msaada wake kwa kuwa kwenye masuala ya namna hii amethibitisha kuwa na kipawa kikubwa sana, na mbinu nzuri katika kuwakamata wahalifu sugu. Ni kwamba...."

"Ninajua anachoweza kufanya. Lakini kama nilivyosema, tunalishughulikia hili suala sisi wenyewe. Nimepewa mamlaka yote na Jenerali kuongoza operation nzima ya kuwakamata wezi hao, kwa hiyo ninachosema ni kwamba simhitaji ACP hapa," akasema Kanali Oswald.

"Hii siyo kuhusu wewe Kanali..." akasema Secretary Joachim.

"Nini?" Kanali Oswald akauliza.

"Ni amri kutoka kwa Raisi kwamba ACP Nora Lois ajiunge katika kuwasaidia na operation hii," akasema Joachim.

"Raisi? Una uhakika na unachokisema? Una uthibitisho gani?" Kanali Oswald akauliza kiukali.

"Kila jambo liko kwenye hilo faili ulilotupa mezani," Secretary Joachim akasema kwa uthabiti.

Kanali Oswald akalichukua tena na kuanza kulipitia. Kweli aliona pendekezo hilo lilikuwa limetoka kwa Raisi kwa kuwa hata muhuri wake ulikuwepo hapo. Akamwangalia Kapteni Erasto ambaye alikuwa akimtazama kwa umakini pia, naye akalitupa tena mezani faili hilo na kumsogelea karibu Secretary Joachim.

"Kwa hiyo wanataka kumleta huyo mtoto mdogo ndiyo afanye kazi yangu? Kwa nini? Wanafikiri nimeshindwa?" Kanali Oswald akauliza.

"Hapana. Unatakiwa tu kushirikiana naye kwa sababu ana level nzuri ya ujuzi katika kushughulika na masuala haya. Bado nguvu ya command utakuwa nayo, lakini yeye ataongoza mbinu zote zitakazohitajika kufuatwa," akasema Joachim.

"Ataongoza? Yaani mimi Colonel niongozwe na ACP wa Jeshi la Polisi?" Kanali akauliza.

Secretary Joachim akashusha pumzi, kisha akasema, "Kama nilivyosema, hii siyo kuhusu wewe Kanali. Ni kuhusu nchi yetu sote. Shida hii inapaswa kupatiwa utatuzi haraka sana, na hii ni kati ya njia zitakazosaidia kufanikisha hilo. Ikiwa una tatizo lolote na badiliko hili unaweza submit lalamiko kwa General. Lakini nakuhakikishia hata yeye...."

"Of course, of course. Hata yeye atasema ni sawa tu. Hawa wezi washenzi wamekuwa mwiba kwangu na sasa naongezewa mwingine... ahah... eti kisa damu ni nzito kuliko maji," Kanali Oswald akasema kwa kejeli.

"ACP yuko wapi sasa?" akauliza Kapteni Erasto.

"Alikuwa agency moja ya CHRAGG kule Dodoma juzi, lakini tayari amepokea mwito huu hivyo atafika kesho," akasema Joachim.

"Wow! Kumbe tayari ilikuwa imeshapigwa na tiki kabisa kwamba mtoto wa mwenyewe aje kujipodolesha huku, halafu ndiyo ningepewa taarifa baada," akasema Kanali Oswald kwa kuudhika.

Wote wakamwangalia Kanali kwa sekunde chache, kisha Kapteni Erasto akauliza, "CHRAGG alikuwa anafanya nini?"

"Alikuwa tu akisaidia kuwafundisha baadhi ya maafisa wa level za juu. Anaweza akawa "mtoto" kama Kanali asemavyo, lakini atakuwa msaada mkubwa sana katika hili," Secretary Joachim akasema.

Kanali Oswald alimwangalia kwa kukerwa sana. Hivyo bila kukawia, Secretary Joachim akawaaga wakuu hawa na kuondoka kwenye jengo hilo. Kanali Oswald akapiga meza kwa ngumi yake.

"Msako nchi nzima, zaidi ya wiki nzima wa wajinga wachache tu lakini mpaka sasa hatujawashika... najua hii ni njia ya Weisiko ya kutaka kuniharibia,' akasema Kanali Oswald.

"Kwa nini unasema hivyo?" Kapteni Erasto akauliza.

"Toka kitambo hakupenda kabisa kwamba na sisi tulijiingiza kwenye mambo yao na General, kwa hiyo kwa sababu yuko tight naye anataka tu kunishusha ili General asini-favor."

"Kwa hiyo huu mpango wa kumleta ACP ni wazo la Weisiko? Unajuaje hilo?"

"Aagh... sijui Erasto, lakini ninahisi ndiyo iko hivyo. Hivi kweli operation ya namna hii wamtume huyo.... aah..."

"Si amempendekeza Raisi?"

"Mdeme hana muda wa kufatilia nani ni mjuzi kwenye haya masuala, yeye atakubaliana tu na lolote ambalo General atapendekeza. Na aliye nyuma ya General kumfanyia haya yote ni nani kama siyo Weisiko?" Kanali Oswald akasema kwa ukali.

"Mh... ngoja tuone kama kweli kataweza kuleta kitu kipya hapa. Nafurahi tu hatujazinguliwa kwa kutoweza kuwashika hao washenzi..."

"Umeshafikiria ni nini kitatokea ikiwa tutawashika na huyo ACP akiwa hapa?"

"Kwamba credit yote itaenda kwake?"

"Kwamba tutaonekana wapuuzi tu wasiojua kazi wanayoifanya!"

"Kanali... nimefatilia kazi zake... na kiukweli yuko vizuri. Ngoja tumpe nafasi tuone..."

"Nafasi siyo yetu kumpa, kashapewa... mbona huelewi Erasto? Muda si muda tutakuwa tunafanya mambo chini ya kivuli chake," Kanali Oswald akasema.

"Sawa mkuu, nimeelewa. Lakini hatuwezi kufanya lolote zaidi ya kwenda na muziki," akasema Kapteni Erasto.

"Wanafikiri kwa kuwa kamefanikiwa kwenye mambo kadhaa ya kipelelezi basi kataweza kuipindua na hii meza... ngoja waone ikiwa itakuwa rahisi kama wanavyofikiria," Kanali Oswald akasema.

Kanali Oswald alikuwa amekerwa sana na uamuzi huu wa kumleta ACP Nora Lois katika utatuzi wa wizi huo kwenye makao makuu ya benki ya nchi, kwa sababu alitaka sana kujionyesha kuwa bora zaidi ya yeyote endapo angefanikisha kuwakamata wahalifu wale kwa njia zake. Kwa hiyo alihisi ni kama alishushwa thamani kutokana na hili kwa kuwa yeye alikuwa Kanali kwenye Jeshi la Nchi, huku ACP Nora Lois, yaani Kamishna Msaidizi wa Polisi, akiwa wa cheo cha kadiri kwenye Jeshi la Polisi, lakini akaendelea kuamini kwamba ikiwa wangefanikiwa kuwashika wezi hao, basi isingekuwa kwa jitihada yoyote ila ya kwake tu.

Wakajiweka tayari kwa ajili ya kumpokea ACP Nora Lois ili waweze kuona ni nini ingekuwa hatma ya msako huo.


★★★★


Siku iliyofuata, viongozi hao wawili wa jeshi pamoja na Secretary Joachim walikuwa ndani ya chumba maalumu cha mkutano kujadili suala hili la wizi wa matrilioni kwenye benki kuu. Aliyekuwepo hapo pia ni Luteni (Lieutenant) wa cheo kilichofuata cha Kapteni Erasto, aliyeitwa kwa jina la Michael Mwakasiba, ambaye alikuwa mwanajeshi (na jasusi) mwenye mwili wa kikomando na mwenye uzoefu katika masuala ya kivita. Katika operesheni hii ya kuwasaka wezi wale, alikuwa ameitwa pia ili kuongoza timu yake maalumu katika msako huo, kwa kuwa alikuwa na kiwango cha huu cha umakini kwenye kazi. Alikuwa ni mtu wa kamata, piga, weka ndani, na asingesita kuua mtu yeyote ambaye angejaribu kumletea ushenzi mbele ya kazi yake.

Secretary Joachim alikuwa amewaambia viongozi hawa (Kanali Oswald na Kapteni Erasto) kuwa IGP Donald Ngassa angefika hapo pia pamoja na ACP Nora Lois, na kwa kejeli Kanali Oswald akasema bila shaka wangewasubiri maana muda wote duniani wa kusubiri walikuwa nao. Kapteni Erasto alimfahamu vizuri sana Luteni Michael, naye alijua mara tu atakapotia nyayo zake katika msako huu, basi matokeo yangekuja vizuri. Luteni Michael ndiye aliyekuwa amevalia T-shirt yenye rangi nyeusi na suruali ya kijeshi, huku wengine wakiwa wamevalia suti za kazi zenye nembo za vyeo vyao. Kapteni Erasto alikuwa akizungumza na Luteni Michael, huku Kanali Oswald akizungumza na watu fulani kwa simu.

Baada ya muda mfupi, akaingia ndani humo IGP Donald Ngassa, akiwa amevalia nguo za kipolisi na kofia. Nyuma yake alifuatwa na mwanamke fulani aliyevalia T-shirt nyeupe yenye kubana na suruali ya jeans, naye alikuwa na umbo lililonawiri kiasi lakini siyo nene sana. Nywele zake ndefu na laini zililazwa kufikia mabegani, naye alikuwa na macho mazuri pia. Mikononi hakubeba chochote kile zaidi ya 'tablet' ndogo ambayo alitunzia mambo yake muhimu kwa ajili ya kazi. Huyu alikuwa ni ACP Nora Lois.

IGP Donald alipiga saluti ya heshima kwa wakuu hapo, naye ACP Nora akafanya hivyo hivyo, kisha wote wakaanza kuwasalimu wa hapo ndani. Luteni Michael alibaki kumwangalia tu mwanamke huyu, na kwa haraka akawa amevutiwa naye sana. Secretary Joachim ndiye aliyefanya kama kuwatambulisha kwa waliokuwa ndani hapo, na wakati ACP Nora alipotambulishwa kwa Luteni Michael, Luteni akamfata na kumnyooshea mkono ili waiunganishe kwa salamu. ACP Nora akatabasamu na kukubali hilo, naye Luteni Michael akawa anamwangalia kwa macho yaliyoonyesha upendezi mwingi.

Baada ya hapo, wote wakaketi na kumwacha Kanali Oswald aelezee mambo kwa ufupi kwa wote.

"Na sasa, sijui kama kuna jambo jipya ambalo mnaweza kuleta hapa kwa kuwa kila njia tumeipitia... kwa hiyo uwanja ni wenu sasa," akasema Kanali Oswald.

"Bado inasugusha kichwa kuhusu ni jinsi gani waliweza kuingia na kutoka sehemu kama ile... hawajaacha clue zozote, fingerprint, wala nini... ndiyo maana imekuwa ngumu sana kuwajua. Ni jambo la ajabu sana trilioni 20 kubebwa bila kuonekana! Walitumia njia gani hawa watu?" akasema Secretary Joachim.

"Speculation za juu zikiwa ni kwamba huenda wameshirikiana na baadhi ya waliofanya kazi pale ndiyo zimefanya mpaka sasa wafanyakazi wa hapo waendelee kushikiliwa na kuhojiwa. Lakini hakuna chochote kilichopatikana chenye kusaidia," akasema Kapteni Erasto.

"CCTV camera zote zilichekiwa?" akauliza Luteni Michael.

"Mara mia," akajibu Kapteni Erasto.

"Timu zetu zina mafunzo ya hali ya juu. Watu wako makini sana, wanatumia mbinu zote kwa kuwa wana uelewa mzuri kutokana na taarifa wanazopata hata kama ni chache ili kutatua hii kitu... lakini mpaka sasa hakuna matokeo... tunafeli wapi? Unaweza ukasema labda hao wajinga walitumia uchawi lakini hakuna kitu kama hicho. Labda tu walichagua siku na wakati ambao bahati ilikuwa upande wao, because this is impossible," akasema Kanali Oswald.

"Hapana siyo impossible, kwa sababu wameshathibitisha kwamba ni possible," akasema ACP Nora.

"Well hatujaja hapa ili kuwasifia hao wajinga ACP. Ongea point yako," akasema Kanali Oswald kwa kukereka.

"See, hilo ndiyo tatizo Kanali. Unafikiri kwamba ni wajinga, lakini kihalisi hawa watu wana akili nzuri sana ya kile wanachokifanya," akasema ACP Nora.

"Katika vita, viongozi wenye experience kama sisi sikuzote huwa tunapangilia mambo kwanza kwa ufasaha kabla ya kuishinda, na siyo kwenda kichwa kichwa tu," akasema Kanali Oswald.

"Ndiyo lakini, mara nyingi viongozi wanaojenga uelewa wa haraka na kuchukua hatua za vitendo mapema ndiyo hupata mafanikio kwa kuwa wana faida ya kukimbizana na adui kwa ukaribu, siyo kusubiri afike mbali. Huu muda wote uliopotea unafanya hao watu wazidi kukimbia tu na kutuacha mbali. Kinachoangaliwa hapa sikuzote huwa ni mambo makubwa makubwa tu, lakini mki-pay attention kwa detail hata ndogo nawaambia mtaona mambo mengi sana," akasema Nora.

Kanali Oswald alimwangalia ACP Nora kwa mkazo sana. Ilikuwa ni kama mwanamke huyu alikuwa akishindana naye, lakini kihalisi alikuwa anamwambia tu ukweli.

"Umeona nini ACP?" Luteni Michael akamuuliza Nora.

"Nilipitia tape za CCTV za nje. Sijui waliwezaje kuingia kule ndani na hata kutoa zile pesa, lakini nafikiri natambua walichofanya ili kutoka," akasema ACP Nora.

Wote wakabaki kumwangalia kwa umakini.

"Bomu la kwanza lilipolipuka, clamor zilikuwa nyingi, vurugu na sintofahamu kubwa. Ukifatilia utagundua kuwa bomu la kwanza lililipuliwa karibu kabisa na...."

"Milango ya vault, ambazo baadae zikawa tupu," akamalizia Luteni Michael.

"Ndiyo. Sijui ikiwa walikuwa wameshatoa pesa au la, lakini bomu la kwanza halikuumiza yeyote pale; wote walitoka salama. Ilichukua dakika zaidi ya 20 kwa maafisa kuingia kule ndani bomu la pili lilipolipuka, na hata hapo hakuna kifo kilichotokea, sana sana baadhi yao na wafanyakazi kadhaa waliumizwa. Timu special ilipotumwa kwenda kule ndani kuwatoa nje na kuwapeleka hospitali, haijulikani kama bado pesa zilikuwepo ama zilikuwa zimeshaondolewa..." akaeleza ACP Nora.

"Kwa nini unarudia kutuambia mambo ambayo tunajua?" Kanali Oswald akauliza.

"Kanali, zilifika ambulance 13 kuwaondoa waliojeruhiwa. Lakini hospitali zilikoelekea zilikuwa ni ambulance 12 tu," akasema Nora.

Luteni Michael akamtazama kwa umakini sana ACP Nora, na kwa kuelewa alichomaanisha, akachekea kwa chini. Wote wakawa wameelewa alichomaanisha.

"Unataka kusema kwamba... yaani... hao wezi walikuwa hapo hapo?!" akauliza Kapteni Erasto kwa mshangao.

"Ndiyo," Nora akajibu.

"Unbelievable!" akasema Secretary Joachim.

"Kwa hiyo... walikuwa ndani... wakiwa wamevaa kama wanajeshi au walinzi au wafanyakazi... wakati walipokuwa wanawatoa waliojeruhiwa na wenyewe walikuwepo, halafu wakaingia kwenye ambulance fake ambayo labda iliendeshwa na mwenzao... wakatoroka wakiwa hapo hapo!" Kapteni Erasto akasema.

"Hiyo mbona kama ni kitu ambayo haiwezekani? Kama ni hivyo basi pesa zingekuwa pale pale... maana wasingeweza kuzibeba huku wakijifanya kujeruhiwa," akasema Luteni Michael.

"Kuhusu kuziondoa pesa, ni kwamba kuna njia fulani walitumia ambayo... bado haijaelezeka. Lakini hata kwa njia ndogo namna hiyo ya kutoroka wameonyesha wanaweza ku-toy na defence zinazojiita za hali ya juu. Siyo wajinga hawa watu... wanajua wanachokifanya," akasema ACP Nora.

"Kwa hiyo kujua haya yote kutatusaidia vipi kuwakamata?" akauliza IGP Donald.

ACP Nora akaanza kubofya kwenye tablet yake, kisha akampa IGP Donald ili ampatie Kanali Oswald.

"Nilichukua copy tape za CCTV za nje kuzunguka majengo hayo na kuzipitia kuangalia watu waliopita maeneo hayo ndani ya wiki tatu za nyuma. Kwa kawaida kama ni watu wanaojirudia kupita eneo fulani, huwa ni nadra kukaa sehemu moja kwa muda mrefu, au hata kubadili sehemu ya kukaa IKIWA tu walikuwa wapita njia; isipokuwa huyo," akasema ACP Nora.

Kanali Oswald alikuwa anaangalia picha kwenye tablet hiyo, nayo ilikuwa ya mtu mwenye mwonekano mchafu sana na nywele zilizovurugika. Kwa haraka Kanali Oswald akatambua huyu alikuwa mtu kichaa.

"Nini hiki?" Kanali Oswald akauliza.

"Huyo mwanaume anayeonekana kama mwehu hapo, ndiye ambaye ame-appear mara nyingi zaidi eneo hilo kuliko mtu yeyote, na sehemu anazopitia ni tofauti KUZUNGUKA majengo yale, halafu anakaa sehemu moja akijifanya kama anapumzika. Hilo linakwambia nini?" ACP Nora akasema.

"Kwamba ni mmoja wao ndani ya disguise?" Kanali Oswald akauliza.

"Ndiyo," akajibu ACP Nora.

"Unawezaje kuwa na uhakika na hilo?" Secretary Joachim akamuuliza.

"Hakuhitajiki uhakika hapo. Hili ni kweli kabisa. ACP anachotaka kusema ni kwamba watu hawa wamekuwa wakifanya kama... reconnaissance ya maeneo haya kwa muda mrefu ili kujua udhaifu wa eneo hilo na kupangilia jinsi ya kuingia na kutoka. Wanajua wanaofanya kazi hapo, walinzi, wakuu, na kadhalika. Ili kuficha utambuzi wao wanatumia disguise. Hapa tunadili na ma-professional, siyo mchezo," akasema Luteni Michael.

"Na huo ulikuwa ni mwanzo tu," akasema ACP Nora.

"Subiri kwanza. Huyu anaweza akawa ni chizi kama machizi wengine tu. Hivi kweli unataka kuleta ndani chizi, si utaonekana chizi?" akauliza Kapteni Erasto.

"Hivyo ndivyo wanavyotaka kuwafikirisha Captain. Baada ya hiyo... heist... huyo chizi hajaonekana eneo hilo tena, wakati alikuwa anafika hapo kila siku kwa wiki tatu mfululizo, and then the next day kabla wizi kufanyika poof... akapotea," akasema ACP Nora.

"Ikiwa walikuwa wanajiamini kupita mpaka ndani na kuiba pesa zile zote kama vile siyo kitu, kwa nini watumie njia ya namna hii... kama kweli ni ma-professional?" akauliza IGP Donald.

"Kwa sababu haikuwa rahisi kwao kupata blueprint za ndani ya jengo. Kujua pesa zinakaa wapi, watumie muda gani, na njia gani kulihitaji planning za hali ya juu, ndiyo maana wakamweka huyu 'chizi' hapo nje. Huwezi kujua... labda hata walitumia disguise za sura kwa baadhi ya wafanyakazi wa pale ili kuingia ndani kule... anything is possible," akasema ACP Nora.

"Ahahah... ACP unaigeuza hii kuwa kama movie," akasema Kapteni Erasto.

"Hapana, yuko sahihi," akasema Kanali Oswald.

"Kanali, kweli hapa nchini kuna mtu anayeweza kufanya hayo yote na tukashindwa kugundua mapema?" Kapteni Erasto akauliza.

"Tumeshindwa kugundua mapema kwa sababu tumekuwa tukiangalia mambo mengi kwa juu-juu. Ilitupaswa tutulie, tuangalie njia walizotumia kwanza ndiyo tujue jinsi ya kuwakamata. ACP Nora umefanya kazi nzuri sana. Na imenishangaza kwa sababu umepewa ishu hii ndani ya siku mbili tu, umewezaje kutambua haraka mambo yote hayo?" akasema Kanali Oswald.

"Kama nilivyokwambia Kanali, yuko vizuri sana," akasema Secretary Joachim.

"Kweli. Unastahili cheo cha juu zaidi ya hapo aisee," akasema Luteni Michael.

ACP Nora akatabasamu na kusema, "Shukrani, lakini niko sawa na nilipo kwa sasa."

"Kwa hiyo picha hii inahitaji kusafishwa vizuri ili huyu mpumbavu akamatwe na awataje wenzake," akasema Kanali Oswald.

"Ndiyo. Lakini... tunahitaji kufanya mambo kwa umakini zaidi. Hawapaswi kutuona tukija kwa sababu wanaweza kubadili nyendo zao haraka," akasema ACP Nora.

"Tunajuaje kwamba hawajaondoka nchini?" akauliza Secretary Joachim.

"Kwa sababu ya pesa walizoiba. Kuziondoa nchini haingekuwa rahisi, kwa hiyo ni lazima kuwe na sehemu fulani wamezificha, na wao kujificha," akasema Kanali Oswald.

"Ndiyo ni kweli," akasema IGP Donald.

"Hii taarifa tumfikishie General haraka," akasema Kapteni Erasto.

"Hapana, nataka tufanikishe kwanza zoezi hili. Luteni, utakuwa ukifanya kazi hii sambamba na ACP Nora. Chochote mtakachopata mnanipa taarifa haraka. Na hakikisha unawafunkurunyua hao jamaa huko waliko na kuwaleta kwangu mapema, inaeleweka?" akasema Kanali Oswald.

"Ndiyo mkuu. Ondoa shaka," akasema Luteni Michael.

"Kwa hiyo kila sehemu atakayokwenda Luteni...."

"ACP Nora atakuwa pamoja naye. Kuna tatizo na hilo?" Kapteni Erasto akamkatisha IGP Donald.

"Ah... hapana, Itakuwa sawa kabisa," akasema IGP Donald.

"Sawa. Kusanya timu yako mwanze kazi Luteni. Nileteeni nyama jioni," akasema Kanali Oswald kitamathali.

Luteni Michael akasimama pamoja na wengine, nao wakapiga saluti za heshima. Kanali Oswald akamrudishia ACP Nora tablet yake, kisha ACP Nora, IGP Donald, pamoja na Luteni Michael wakatoka ndani ya ofisi hiyo.

"Mtoto yuko vizuri," akasema Kapteni Erasto.

"Yeah, Raisi anajua machaguo yake," akasema Secretary Joachim.

"Just to be clear, hii mission siyo ya ACP Nora. Ameletwa kusaidia tu kwa sababu ana kichwa kikubwa na siyo command, lakini hapa kila jambo nitaongoza mimi, sijui mnanielewa?" akasema Kanali Oswald.

Secretary Joachim na Kapteni Erasto wakatazamana kwa kutopendezwa na wivu usio na maana yoyote wa Kanali Oswald. Alikuwa anaona ni kama vile ACP Nora angepata sifa kubwa badala yake endapo mission hii ingefanikiwa kwa sababu ya akili yake nzuri ya kuchanganua mambo, kwa kuwa kihalisi alichotaka ilikuwa ni kujinufaisha tu yeye mwenyewe na matokeo mazuri kwa upande wao. Baada ya muda, Secretary Joachim akawaacha viongozi hao wa jeshini na kurudi kwenye harakati zingine.


★★★★


Luteni Michael aliambatana na ACP Nora kwenye gari lake kuelekea kwenye jengo dogo ambalo timu yake yenye watu saba wenye uzoefu wa kijeshi/kijasusi walikuwa. Hapo walikuwa na vifaa vya kiteknolojia vya ufatiliaji na taarifa mbalimbali ambazo walikuwa wanafanyia kazi ili kuweza kubaini wezi wale walikuwa wapi. Kihalisi Luteni Michael pia pamoja na timu yake walikuwa wameshaanza kufanyia kazi suala hili siku chache za nyuma, lakini hata wao hawakuwa wamepata ufumbuzi mzuri. Kwa hiyo kile ambacho Nora alikuwa amegundua wangeanza kukifanyia kazi ili kufanikisha zoezi la kuwakamata watu wale.

Wakiwa njiani, waliongelea mambo kadhaa waliyofikiria kuhusiana na matukio haya yote ambayo kwenye vichwa vya watu wengi yalikuwa yenye kushangaza sana.

"Kwa hiyo ulikuja huku kwa usafiri kumbe?" Luteni Michael akamuuliza wakiwa bado mwendoni.

"Yeah. Gari yangu ilipatwa na trouble kidogo, nikaiacha itengenezwe. Ila kuna mtu ataileta huku kufikia kesho," akasema ACP Nora.

"Okay. Nimefatilia kazi zako. Uko vizuri sana. Najua pia huwa haupendelei kuvalia sare za kaki, na kiukweli inakupendezea," Luteni Michael akamwambia.

ACP Nora akatabasamu.

"Hawa jamaa wanaumiza vichwa," Luteni Michael akasema.

"Wanajiita eti Mess Makers. Waliacha sign yenye hayo maneno ili waonekane kama kundi fulani jipya la kigaidi," akasema ACP Nora.

"Ni utoto wenye utoto wa kitoto," akasema Luteni Michael.

"Ila mchezo wao ni wa kikubwa," akasema Nora.

"Unajua... ni sawa kwamba wanafanya mambo kitaalamu na nini... lakini, bado najiuliza hizo pesa walizitoje pale... it just doesn't make sense yaani wangehitaji lori au malori kabisa," akasema Luteni Michael.

"Tukiwashika watasema tu," akasema Nora.

Luteni Michael akamtazama kwa makini. Aliona jinsi mwanamke huyu alivyokuwa makini sana. Uso wake ulizama kwenye tablet yake, akifanya tafiti zake na kuchanganua mambo.

"Ulini-impress sana leo," akasema Luteni Michael.

Nora akamwangalia.

"Kuona umetambua mchezo wa hawa jamaa ndani ya siku moja wakati bado Kanali inamwasha huko chini kwa wiki nzima... kiukweli uko vizuri sana," akasema Luteni Michael.

"Ahahah... watu wako hao wanapenda kujikweza sana lakini jambo dogo namna hiyo hata Koplo angeona mbona," Nora akatania.

"Ahahahah... yeah, ni vyeo vyao tu ndo' vinawasumbua akili, hawana tena ile passion waliyokuwa nayo mwanzoni iliyowafikisha hapo... zaidi tu ni kusema 'kawafunkurunyueni' hao watu... sijui hata hilo neno linamaanisha nini," akasema Michael.

"Ahahahah... me sisemi sana, isije ikawa naongea na mmoja wao..."

"Ahahahah... me siko hivyo. Kazi kazi. Hawa mafala wanasumbua vichwa sana, lakini ndiyo nafurahia hivyo. Mwizi anapenda kukimbizwa, siyo kukamatwa. Kwa hiyo tukishawakamata unakuwa unataka kupumzika kwa kuwa ulikimbiza haswa. Lakini mimi sijui ni kwa nini tu ila...."

"Huwa ni kama bado unataka kuendelea kuwakimbiza," Nora akamalizia.

"Yeah. Ndo' nafurahia," akasema Luteni Michael.

"Mimi napenda zaidi ku-solve puzzle. Kwa hiyo nilipopigiwa tu simu, nikakubali hii ishu. Tunakoelekea sidhani kama itakuwa ngumu sana, ikiwa tu tutakuwa makini," Nora akamwambia.

"Alikupigia simu huyo Secretary?"

"Hapana. Ilikuwa ni Mdeme."

"Una ukaribu sana na Raisi eeh?"

"Siyo kihivyo."

"Mmmm... okay. Kwa level yako ya intelligence ungekuwa sehemu pana zaidi. Kwa nini unabaki kuwa ACP?"

"Napenda hivyo. Napenda... kuwa chini ya mwongozo. Sijui nisemeje yaani... vyeo vya juu huwa viko off sana kwangu. Nafurahia zaidi position niliyonayo," akasema Nora.

Luteni Michael aliweza kuona kama kuna historia fulani nzito ndani ya maisha ya mwanamke huyu. Lakini hakutaka kupeleka mambo sehemu ya kibinafsi zaidi wakati huu kwa kuwa walikuwa wamekutanishwa kikazi, hivyo akaona aiendeleze tu safari yao na mazungumzo zaidi wangefanya wakati mwingine.

Baada ya kufika kwenye jengo ilipokuwepo timu yake, Luteni Michael akawatambulisha watu wake kwa ACP Nora. Wote walikuwa ni wanaume, kwa majina ya Vedastus, Omari, Bobby, Alex, Mishashi, Mario, na Hussein.

Walimkaribisha kirafiki na kwa heshima, kisha Luteni Michael akawajuza kuhusiana na taarifa mpya aliyowaletea ACP Nora. Bila kukawia, Bobby akaanza kuifanyia kazi picha ile, akiisafisha kwa kompyuta ili kuweza kuuona vyema uso wa "chizi" yule. Kisha akaanza kutafuta ulingani na sura za watu ambao walikuwa mkoani hapo kwa miezi michache iliyopita zilizoendana na hiyo, na moja ikawa ndiyo "perfect match," yaani yenyewe kabisa.

Kwa kutumia kompyuta zao maalumu waliweza kubaini mtu huyo alikuwa ni nani kwa kitambulisho alichotumia kama mwananchi. Aliitwa Kevin Dass, miaka 34, naye alifanya kazi ya ujenzi wa nyumba za kisasa kwa muda wa miaka zaidi ya kumi nchini. Huyo ndiyo aliyekuwa chizi wanayemtafuta! Kupitia namba zake za mawasiliano, waliweza kubaini kwamba kwa sasa hakuwa ndani ya mkoa huu, bali mkoa mwingine kabisa wa mbali, yaani Mwanza. Hivyo Luteni Michael akaamuru upesi kwamba waondoke na kuelekea kule ili kumshika haraka sana.

Kwa msaada wa ACP Nora wakawa tayari wamepiga hatua ya haraka mno katika msako huu, na ambacho kilitarajiwa baada ya hapo ingekuwa ni kumaliza kabisa utata uliokuwa umeanzishwa na hao "Mess Makers."


★★★★★★★★★★

ITAENDELEA

★★★★★★★★★★

WhatsApp +255 787 604 893
 
FOR YOU

Story by Elton Tonny

Familia, Urafiki, Mapenzi, Mahaba, Tamaa, Hila, Usaliti, Unyanyasaji, Uhalifu, Mauaji, Visasi, Vita, Mambo yasiyotazamiwa

R-rated 18+

Enjoy!

★★★★★★★★★★★★★★★★

SEHEMU YA KUMI NA SITA

★★★★★★★★★★★★★★★★


Wataalamu wa kazi ya wizi wa Trilioni 20 kwenye majengo ya benki kuu walifanikiwa kumpeleka Kevin sehemu ambayo ilikuwa salama kwa usiku huo. Walifika kwa pamoja kwa kutumia gari lao kwenye nyumba ndogo maeneo ya ziwani, ambayo ilikuwa imejitenga mbali sana na makazi ya watu wengine. Nyumba hii ilijengwa kwa mabati makuukuu tu na hivyo kuonekana kama ya hali ya chini, lakini kwa ndani watu hawa walikuwa wameweka vitu vyao kadhaa vya kitaalamu sana, na kwa huku ilikuwa ni sehemu nzuri ya kujifichia.

Kevin Dass alikuwa amepewa egamio na mwenzake ili aweze kutembea vizuri, kwa kuwa alihisi maumivu mengi mwilini. Walipofika ndani akakalishwa na kuvulishwa T-shirt yake, kisha wenzake, mmoja baada ya mwingine, wakaanza kuvua viziba uso vilivyoficha sura zao. Kati ya wenzake waliomwokoa, watatu walikuwa wanaume, na wawili wanawake.

"Aahh... haki ya mungu nitamuua huyo mpumbavu! Nitampa kifo ambacho hatakaa kusahau!" Kevin akasema kwa hasira.

"Atakikumbukaje akiwa ameshakufa sasa?" akauliza mmoja wao, mwanaume aliyeitwa Victor.

"Anajishaua eti atamuua wakati jamaa amemponda ka' kiazi hahahah..." akatania mwanaume kijana aliyeitwa Oscar.

"Shut up! Kilichowachelewesha ilikuwa nini wakati nilikuwa nimewapa signal tokea kitambo?" Kevin akauliza kwa ukali.

"Okay first, hatukufanyii kazi wewe. Second, unapaswa ku-respect chain ya command. Unawezaje kujiachia namna hiyo wakati unajua jinsi ilivyo hatari kwetu?" Victor akamuuliza Kevin.

Mwanamke mmojawapo akawa ametoa vifaa vichache kwa ajili ya kutumia kumponya Kevin sehemu alizoumia; kama dawa za kunywa, kuchua, na sindano. Akamsogelea na kuchuchumaa kisha kuanza kumpaka dawa.

"Hatari kivipi? Siyo kwamba hata nyie mlijua hawa wajinga wangenifikia mimi... je kama wangekufikia wewe ukiwa chooni, tungesema hau-respect chain of command? Aagh... taratibu bwana!" Kevin akasema na kumwambia hivyo mwanamke huyu aliyekuwa anamchua.

"Hey tulia, haunilipi!" mwanamke huyu aliyekuwa anamchua akamwambia hivyo. Jina lake lilikuwa LaKeisha.

"Ulikuwa wapi walipokukamata?" akauliza mwanaume mwingine aliyeitwa Mensah.

"Sokoni," akajibu Kevin.

"Maeneo gani?" Mensah akauliza tena.

"Wanapaita Mabatini..." akasema Kevin.

"Ulikuwa umeenda kutafuta mabati ya nini?" Oscar akamuuliza kiutani.

"Ili nije niya-shove in your ass," Kevin akasema kwa kukerwa.

"Unajua kabisa huku kilichotuleta haikuwa kuzurura. Ulitakiwa kufata Buzuruga ulichoambiwa na kugeuka, wewe ukaona free time una yote duniani mizunguko yako kufanya, nini unategemea? Ni lazima tu wangekukamata!" Mensah akasema kwa ukali.

Kevin akanyanyuka na kumfata Mensah mpaka karibu, akionyesha ubabe. Mensah naye akamsogelea karibu zaidi usoni, nao wakawa wanaangaliana kwa hisia kali.

"Here we go (haya sasa)," Victor akasema.

LaKeisha akasonya na kusema, "Mkimaliza utumbo wenu chuaneni wenyewe."

Kisha akaelekea upande mwingine akiviacha vifaa vile chini.

"Unanifokea namna hiyo wewe kama nani?" Kevin akamuuliza Mensah kwa sauti ya chini.

"Kama mtu ambaye anaweza kukutandika ukawa mpaka mwekundu zaidi ya nyanya!" Mensah akajibu kiutulivu pia.

"Usijipaishe kwa kuwa niko weak kidogo sa'hivi. Nitakuonyesha ngozi yako yote ya ndani inafananaje siku moja hadi uweze kuongea Kiswahili vizuri," Kevin akamwambia.

"Ulishawahi kuliona fuvu lako wewe mwenyewe? Nitakuonyesha hiyo siku ikifika," Mensah akasema.

Midomo yao ikakaribiana zaidi wakiwa wanaangaliana kwa hasira sana.

"Busu hiyo inakuja, busu hiyo inakuja, busu hiyo inakuja..." Oscar akawa anasema huku anampiga-piga Victor mgongoni.

"Kawasaidie kugonganisha vichwa basi," Victor akamwambia Oscar.

"Usijifanye wewe ndiyo mwenye neno hapa, hauko karibu na hilo hata kidogo," Kevin akamwambia Mensah.

"Nikija kumalizana na wewe kuutumia ulimi wako hautaweza tena, ndiyo utajua nani amebaki na neno," Mensah akasema.

"Enough!"

Mwanamke yule mwingine aliyekuwa anawatazama tu muda wote huu akasema hivyo kiukali. Wawili hawa wakaendelea tu kutazamana kibabe.

"Kevin... back off! (Kevin..rudi nyuma)," mwanamke huyu akamwambia.

Kevin akaendelea kumwangalia Mensah kwa sekunde chache, kisha akaanza kurudi nyuma taratibu. Mensah akatabasamu kwa kejeli. Mwanamke huyo akaanza kumfata Kevin mpaka aliposimama. Akaanza kumshika polepole sehemu za mwili wake zilizoumia, naye Kevin akawa anamwangalia kwa hisia.

"Utahitaji uangalizi wa kina Kevin... umeumia sana," mwanamke huyu akasema.

"No biggie wala, niko sawa," Kevin akasema.

"Ndiyo, kwa nje. Lakini kwa ndani unavuja damu. Torres atahitaji kukupa attention," mwanamke huyu akamwambia.

"Siyo kama vile yuko hapa," Kevin akasema.

Mwanamke huyo akampatia Kevin kifaa fulani mkononi.

"Utamfikishia Torres," mwanamke huyu akasema.

Kevin akashangaa.

"Unamanisha nini?" akauliza.

"Unaenda chini," mwanamke huyu akamwambia.

"Nini? Lakini... subiri, kwa muda gani?" Kevin akauliza.

"Mpaka nitakaposema utoke," mwanamke huyu akamwambia.

"Why?" Kevin akauliza kimshangao.

"Wanajua wewe ni nani sasa hivi, utasakwa kila kona. Kwa hiyo hauna jinsi tena... ltttaah... CHINI... hahahaah..." Oscar akamtania Kevin.

"Lakini Lexi..." Kevin akawa anataka kupinga.

"Oscar yuko sahihi. Silaha yetu kubwa ni kutojulikana, na unajua hii ni lazima ili uwe salama," mwanamke huyo akasema.

"Usingefanya uzururaji isingekuwa hivi. Sasa hautazurura tena," Mensah akamwambia.

"Hapana Mensah, hiyo siyo sababu iliyofanya akamatwe. Kevin, nahitaji uniambie wale watu walikuwa wakina nani," mwanamke huyu akasema.

"Sijui sana, ila nadhani ni wanajeshi," Kevin akasema.

LaKeisha akawa amefika usawa wa mwanamke huyu mwingine, ambaye jina lake lilikuwa ni Lexi, na kusimama karibu yake akiwa amezungushia mkono wake mmoja begani kwake.

"Tunajua walikuwa wanajeshi. Anamaanisha ni nani hasa. Kichwa chako kina nini, au bado kipigo kimekukolea?" LaKeisha akamuuliza Kevin.

Kevin akamwangalia LaKeisha kwa kuudhika, kisha akasema, "Walikuwa wanamwita jamaa Luteni. Aliniambia anaitwa Michael."

"Luteni Michael? Boom! Kazi imeanza hahah..." Oscar akasema.

"Na yule mwanamke... alikuwa nani?" Lexi akauliza.

"Walimwita ACP, lakini sijapata jina lake. Yeye ndiye aliyekuwa wa kwanza kujua hereni niliyovaa ni TD," Kevin akasema.

Mwanamke huyu, Lexi, akaangalia pembeni kwa umakini.

"Lexi... tufanye nini sasa?" LaKeisha akamuuliza mwanamke huyu.

"Kwani ni lazima nikae kule chini kuanzia sasa? Si tunaweza tu kuendelea na..."

"Hatuwezi, boya wewe. Kwa kuwa wamekujua utapaswa kulay low, na hata kama ni mission tukifanya now utatakiwa uwe unagusa mara moja tu. Boss atakutafuna," Mensah akamwambia Kevin.

"Hivi sababu ilikuwa ni nini mkamwingiza huyu kunguni kwenye hii mission, mbona ananichokonoa vibaya sana?" Kevin akauliza kwa hasira.

Oscar na Victor wakacheka.

"Victor, Oscar, LaKeish... nendeni pamoja na Kevin chini upesi, mmpatie Torres info za leo, kisha mmwambie anitumie majibu. Mensah uko nami, tunaenda Dar," Lexi akatoa amri.

"Yes ma'am," akasema Oscar.

"Dar kufanyaje sa'hivi? Na pia Lexi... kwa nini Mensah asiende na hawa wengine halafu mimi niende nawe huko?" LaKeisha akamuuliza.

"Usijali, mtakuja tu. Ila nataka kuhakikisha Kevin mnamfikisha salama," Lexi akajibu.

"Kama litoto lililopotea," Victor akatania.

"F(...) you," Kevin akamwambia.

Victor akacheka.

"Jiandae kuhusu ni hotuba gani utatoa ukifika kwa boss," Mensah akamwambia Kevin.

Kevin akamwangalia kwa kuudhika na kurudi taratibu pale alipokuwa amekaa.

Lexi akamwangalia LaKeisha, kisha akasema, "Chukueni gari mwondoke now, kabla ya saa 6 mchana kesho muwe mmeshafika chini."

"Aagh... yaani hatuna hata muda wa kupumzika," LaKeisha akasema kwa maringo.

Lexi akamwangalia Oscar, naye jamaa akamrushia funguo kwa ajili ya gari lingine tofauti na lile walilokuja nalo.

"Mkitoka choma kila kitu," Lexi akasema.

Oscar akampigia saluti kuonyesha ameelewa.

LaKeisha akawa anachezea-chezea nywele za kichwa cha Lexi huku akimwangalia kwa hisia, naye Victor pamoja na Oscar wakaangaliana na kuchekea kwa chini bila kutoa sauti. Kisha LaKeisha akambusu Lexi kwenye shavu, naye Lexi na Mensah wakatoka ndani hapo na kuelekea nje.

"Hivi we' hauachagi tu?" Oscar akamuuliza LaKeisha.

"Kuacha nini?" LaKeisha akauliza.

"Hayo mambo yako," Oscar akasema.

"Kwa Lexi? Sahau," LaKeisha akasema kwa uhakika.

"Okay, mtoto wa mama kama umemaliza kulialia hapo chini vaa shati tuondoke. Haraka!"

Victor akamwarisha hivyo Kevin kikejeli na kutoka akiwa anacheka. Oscar alikuwa anacheka pia huku akimsonta Kevin ambaye alikuwa amenuna na kuvimba nusura ya kupasuka.

"Ooouh... mbona mnamwandama hivi baby wangu? Eti sugar wanakuonea kwa kuwa umebamizwa leo? Usijali wasikuonee hawa, sawa? Am here for you," LaKeisha akamwambia Kevin kimadoido lakini kwa kejeli.

Kevin alikuwa amekasirika kwelikweli, na sababu ilikuwa ni kilichompata muda mfupi nyuma, na kile ambacho kingefuata. Sehemu ile ambayo Lexi aliiita "chini," ilikuwa ni sehemu yao ya mwisho kwa ajili ya maficho; yaani ikiwa jambo kama hili lililompata Kevin lingempata yeyote kati yao, basi walipaswa kwenda sehemu hiyo na kutulia huko mpaka wakiambiwa vinginevyo na "boss" wao, kwa kuwa tayari wangekuwa wamejulikana.

Hawa walikuwa ni vijana kutoka kwenye kundi la watu wale waliofanya wizi kwenye Benki Kuu, lililofahamika kama Mess Makers. Walikuwa ni wataalamu katika mambo yote waliyofanya, na waliyokuwa wamejiweka tayari kufanya. Kwa ujumla, kundi hili la "Mess Makers" lilikuwa na watu nane; nane tu! Lakini mambo waliyokuwa wamefanya mpaka sasa na ambayo walikuwa wameazimia kufanya yalikuwa makubwa kupita maelezo. Kama Lexi alivyosema, nguvu yao kubwa ilikuwa ni kutojulikana wao walikuwa akina nani, kwa hiyo kwa jambo kama lililompata Kevin, nguvu yao ingepungua kwa kadiri fulani. Kwa hiyo kuanzia wakati huu wangejitahidi kuweka umakini wa hali ya juu.

Kevin Dass alikuwa mwanaume mwenye nguvu, mwenye kujiamini sana, na mwenye ustadi mwingi katika masuala yote yaliyohusisha ujenzi wa majengo ya aina zote. Hivyo kwa kundi hili yeye alikuwa muhimu sana ilipokuja kwenye masuala yaliyohusisha michoro ya majengo, maeneo mbalimbali, na kujua ni vifaa vipi vingehitajika sehemu mbalimbali walizotaka kuingia. Alikuwa na miaka 34, naye alikuwa mweusi, mwenye mwili mpana wenye nguvu, na mrefu kiasi. Lakini alikuwa mtu mwenye kukasirika upesi sana pia. Mara kwa mara alikosa subira kwa mambo mengi waliyofanya, hivyo ilikuwa jambo la kawaida kwa wenzake kumsahihisha endapo angejaribu kufanya mambo kwa njia ambayo haikupatana na mipango yao wakiwa kama timu.

Oscar Amari alikuwa ndiye kijana mdogo zaidi kwenye kundi hili; akiwa na miaka 26 tu. Alikuwa kijana mwenye mwili usio mpana sana lakini uliojengeka vizuri kimazoezi. Alikuwa mcheshi, mtundu, mwepesi kuongea, na utaalamu wake ulikuwa ni ujuzi mwingi wa mitambo ya aina zote za kielektroni. Angeweza hata kutengeneza bomu dogo kwa kutumia betri za simu na kulitumia kushtua watu ili kujifurahisha alipokuwa na miaka 14 tu. Alikuwa muhimu sana ilipokuja kwenye masuala ya kukorofisha mitambo mingi ya ulinzi, CCTV camera, kuondoa password ngumu kwenye vyumba au mashine kubwa kubwa za kielektroni, na hata kutengeneza mabomu yenye nguvu kubwa sana. Ni huyu ndiye aliyetengeneza mabomu yaliyotumiwa kulipua majengo ya Benki Kuu, hivyo pamoja na kwamba alikuwa "mdogo," mambo yake yalikuwa makubwa sana.

Victor Quawey alikuwa mwanaume mwenye miaka 44, mweusi, mnene wa kadiri na mrefu kiasi. Alikuwa mtaratibu, msikivu, na mwenye utulivu pia. Lakini chonde! Huyu alikuwa mtu mwenye hila balaa! Alikuwa na ustadi mzuri wa kutengeneza vitu bandia ambavyo vilifanana kabisa na vile vilivyokuwa halali. Hii ilimruhusu kutengeneza pesa, vitambulisho, vito, ngozi kama za watu, na hata sura za watu ambazo zilikuwa za bandia. Alikuwa mtaalamu sana kwenye jambo hili, lakini pia alijua mambo mengi kuhusiana na siasa na biashara. Hivyo alikuwa na umuhimu wa pekee kwenye kundi hili la Mess Makers.

Halafu kuna LaKeisha Uatu, ama kwa jina walilozoea kumwita wenzake, LaKeish. Huyu alikuwa mwanadada mwenye miaka 28, mwenye ngozi isiyo nyeusi sana wala nyeupe sana; maji ya kunde. Alikuwa na sura nzuri, mwenye mwili mwembamba kiasi lakini hips zake zilikuwa nene na kufanya achoreke vizuri sana kutokea kiunoni. Alikuwa mwepesi kuongea, mjeuri, na mwenye kujiamini kupita maelezo. Ustadi wake muhimu zaidi ilikuwa ni kuiba kwa njia isiyoonekana wazi. Yaani kama vile mtu unayepishana naye halafu mkapamiana akakuomba samahani, kisha ukifika mbele unakuta kwenye pochi au wallet yako hakuna kitu, ndiyo alikuwa LaKeisha sasa. Alipenda sana kukwapua vitu vya watu kwa kuwa alikuwa na mikono yenye kasi sana, naye alijua kuchora pia. Kwa kundi hili, yeye ndiye aliyekuwa "kipenzi" cha wote kutokana na njia yake ya kufanya mambo kimadoido, lakini kwenye kazi alikuwa makini sana.

Mensah Dodzi alikuwa mwanaume mwenye miaka 41. Alikuwa mrefu kiasi, mwenye mwili mkubwa wa mazoezi na mweusi pia. Alifuga rasi kichwani na ndevu nyingi, naye alikuwa na uzoefu katika kutumia silaha za kila aina. Aliwahi kuwa kwenye moja ya makundi yaliyofanya ujambazi tokea alipokuwa na miaka 21 mpaka 30 kwenye nchi aliyotokea. Aliwekwa gerezani mara kadhaa, lakini hakuacha tabia zake za kikorofi mpaka baadae alipopatwa na msiba wa familia yake; iliyouliwa kikatili na watu wengine wabaya waliotaka kumkomoa. Kwa hiyo baada ya hayo, akiwa anataka kujijengea maisha mengine sehemu nyingine, alijiunga na kundi hili. Huyu alikuwa mwanaume aliye makini sana. Hakupenda mchezo na kazi, naye angefuata kile alichoongozwa kufanya bila kujali nani wala nini kingekuwa mbele yake. Ni moja ya wale watu wanaoitwa "damu baridi," kwa sababu ilipokuja kwenye suala la kuua asingesita hata kidogo.

Kijana mwingine wa kundi hili aliitwa Torres Dela Robia. Huyu ndiyo yule mtu unayeweza kusema ni "ubongo" wa timu. Jamaa alikuwa na ustadi mmoja ambao ulimfanya awe wa muhimu sana kwenye timu hii, na ustadi huo ulikuwa ni kwamba alijua mambo mengi. Yaani huyu ndiyo alikuwa "genius" kwenye kundi la Mess Makers, kwa sababu alikuwa na ubongo mwepesi sana wa kuchanganua mambo mengi kwa wakati mmoja. Alijua kila aina ya somo. Alijua sayansi, alijua biashara, alijua teknolojia, alijua siasa, alijua falsafa, alijua sheria, alijua kila aina ya mazingira, yaani alijua vitu vingi sana, hivyo ili mipango mingi ya kundi hili ifanikiwe, alihitajika sana kuipangilia kwa njia ambayo mwisho wa siku ingefanikiwa tu. Kwa kuwa na umuhimu huu, yeye alikaa sehemu moja ambayo angeitumia kwa ajili ya kuwaongoza wenzake endapo wangekuwa kwenye "mission" fulani; kule kule walikopaita "chini." Alikuwa na miaka 37, lakini mwonekano wake ulimfanya aonekane kuwa mdogo sana. Alikuwa na mwili wa wastani tu, mrefu pia, mwenye rasi fupi kichwani, naye alipendelea kuvaa miwani yenye kuonyesha macho lakini isiyo ya dawa.

Kisha kuna Lexi, aliyekuwa na miaka 29. Mwanamke huyu ndiyo alikuwa kama roho ya kundi, iliyowaunganisha kwa pamoja licha ya wao kutofautiana kwa mambo mengi. Alikuwa mtu mwenye akili kwelikweli, na ustadi wake ilikuwa ni werevu wa kuchukua maamuzi ya haraka ambayo yaliwasaidia wanakundi kutenda upesi chini ya hali mbalimbali. Yaani sikuzote kulikuwa na mipango ambayo tayari iliwekwa, lakini siyo sikuzote matokeo yangekuwa kwa njia ambayo kila mmoja alitarajia. Hivyo mtu kama Lexi alikuwa wa muhimu sana katika kutokeza njia mpya za kushughulika na mambo kwa vitendo zaidi, na kama kungetokea tatizo kwenye mfumo wao mzima, basi angetokeza njia ili mambo yakae sawa. Tofauti na Torres ambaye alitoa suluhisho kwa njia ya mawazo, Lexi alikuwa mtu wa kuyaangalia mawazo hayo na kutafuta njia za kuyatekeleza kwa vitendo kulingana na hali walizonazo na kile ambacho Torres angekuwa ameshauri. Hivyo wawili hawa walikuwa na ushirikiano wa karibu sana katika kufanya maamuzi ambayo yangeiletea timu yao hii manufaa.

Lexi pia alikuwa mtaalamu wa kupigana. Alijua kupigana kwa mitindo mingi, naye alikuwa na mwili ulioimarika ijapokuwa kwa njia ya kike, wenye ngozi nyeupe, na nywele zake laini (zenye mwonekano kama wa manyoya yenye kuchoma) alikuwa amezipunguza kuzungukia pande za kichwa chake na kuziacha nyingi upande wa juu. Kutokana na njia yake ya kushughulika na mambo kwa umakini, wenzake walimheshimu sana kutokana na busara zake katika mipango na maamuzi, hivyo kwa hawa wengine alikuwa kama kiongozi. Ikiwa angesema kitu, basi wenzake wangefuata.

Lakini mtu wa mwisho kwenye kundi hili ndiye aliyekuwa kama mkuu wao, kwa sababu wengine walimwona kama "boss." Yeye ndiyo aliwapa kila kitu walichohitaji ili kutekeleza mipango yao, kutokana na kuwa na pesa nyingi sana, na pia yeye kuwa mwanzilishi wa kundi hili.

Hawa ndiyo walikuwa "Mess Makers." Wote walikuwa na nia zao za kufanya haya yote waliyokuwa wamejiingiza kuyafanya. Baada sasa ya Lexi na Mensah kuwa wameondoka, waliobaki kwenye nyumba ile pia wakabadili mavazi na kuvaa ya kawaida tu, kisha wakaenda kwenye gari wakiwa wameacha vitu kadhaa kwenye nyumba ile na kubeba vichache kwenye mabegi ya mgongoni.

Walipoanza kuliondoa gari sehemu hiyo, Oscar akatumia kifaa kidogo kama rimoti na kubonyeza, na ndani ya nyumba ile waliyoiacha likalipuka bomu dogo tu ambalo jamaa alikuwa ameliweka. Hivyo nyumba hiyo na kila kitu kilichokuwa ndani yake kikateketea kwa moto. Oscar alipenda sana kufanya mambo kama vile yuko kwenye filamu za kuigiza, na kwa kuwa wenzake walikuwa wameshamzoea kwa njia hiyo walimwacha tu awaburudishe kwa lolote lile alilofanya.

Safari ya kumpeleka Kevin kule "chini" ikaendelea usiku huo huo uliokuwa umetokeza mambo mazito ambayo yangezidi kuufanya mchezo huu wa paka na panya uwe mtata zaidi.


★★★★


Siku iliyofuata, Luteni Michael pamoja na wenzake waliamkia kwenye safari ya kurudi Dar es Salaam. Walikuwa wamechukua helicopter ili kuweza kufika kule haraka iwezekanavyo. Kufikia wakati ambao walikuwa wamefika Dar es Salaam, tayari vyombo vya habari nchini vilikuwa vimeshaanza kusambaza taarifa muhimu kuhusu Kevin Dass kuwa mmoja wa watu walioshiriki katika wizi uliofanyika benki kuu. Wananchi waliombwa ushirikiano kutoa taarifa haraka ikiwa wangemwona mtu huyo sehemu yoyote ile. IGP Donald Ngassa ndiye aliyetoa tamko kupitia vyombo vya habari na kusema kwa kutoa taarifa haraka, wananchi wangekuwa msaada mkubwa sana katika kuwakamata wahalifu wote waliohusika na wizi huo.

Luteni Michael, ACP Nora, Mishashi, Hussein, Mario, pamoja na Alex walielekea kwenye jengo lile ambalo kikosi kilichobaki cha timu ya Luteni Michael kilikuwepo. Waliwakuta akina Bobby, Omari na Vedastus wakiwa hapo, na wanajeshi hawa wakawapokea vizuri na kuwapa pole kwa kilichowapata kule Mwanza. Bila kukawia, Luteni Michael akamuuliza Vedastus ikiwa kazi ambayo alikuwa amemwachia yeye na Omari wafanye waliitekeleza.

"Ndiyo Luteni. Tumefatilia makazi ya huyo Kevin na sehemu ambazo amefanyia kazi, lakini hatujapata mtu yeyote ambaye anaweza kuwa wa familia au rafiki wa karibu," Vedastus akasema.

"Na watu ambao amefanya nao kazi wanasema wanamjua tu kikazi, lakini hata kutoka naye kupata kinywaji hawajawahi. Majirani wa sehemu anayokaa wanasema hana urafiki na mtu yeyote, na hawajawahi kumwona akipeleka mtu pale," akasema Omari.

"Unataka kusema hana historia yoyote? Vipi kuhusu address za zamani, shule alizosomea, vyeti vya masomo, vyeti vya kuzaliwa?" akauliza Luteni Michael.

"Wazazi wake wote wameshafariki. Record zake za zamani za masomo na maeneo aliyoishi ziko blank. Hakuna uhusiano wowote wa kiukoo alionao na yeyote huku. Yaani ni kama jamaa amesafisha maisha yake ya zamani ili kuwa na maisha mengine kabisa," akasema Vedastus.

"Dah! Kwo' ndiyo tumempoteza yaani! Hawa watu wanafanyaje hivi?" akauliza Hussein.

"Hatujawapoteza. Kuna njia nyingine tu itakayosaidia kuwakamata haraka. ACP Nora... una jambo lolote?" Luteni Michael akasema.

"Ndiyo... aam... kuna jambo nimefikiria, lakini nahitaji kufanya uchunguzi kwanza," akasema Nora.

"Umefikiria jambo gani?" Alex akamuuliza Nora.

"Nilipompiga risasi nne yule jamaa, zote zilidunda na hata nikaona cheche. Nataka kujua ni aina gani ya fabric iliyotumiwa kwenye nguo yake maana kwa bulletproof za kawaida risasi zingeingia ndani na kuganda," Nora akasema.

"Lakini zake kudunda inamaanisha ilikuwa ngumu sana. Kevlar labda..." akasema Omari.

"Labda. Tukishajua ni aina gani zilizo ngumu sana namna hiyo kuagizwa nchini ndani ya miezi michache iliyopita na kwenda sehemu tofauti na vyombo vya usalama, basi huenda tukapata clue yoyote ya mtu aliyetumika kuzitengeneza ziwe nguo overall... na kama ziliuzwa..."

"Basi ziliuzwa kwa nani," Luteni Michael akamalizia maneno ya Nora.

"Ndiyo," Nora akasema.

Luteni Michael akatabasamu na kuwaambia wenzake, "Mmeona? Hii ndiyo sababu tunaye huyu dada hapa. Bobby, fuata kila kitu atakachoomba ufanye kwa masuala ya utafiti."

"Sure boss," Bobby akasema.

"Alex, Mishashi, nifuateni. Tunaenda kuonana na watu fulani. Wengine, mpeni hospitality nzuri dada yetu," Luteni Michael akawaambia.

"Ah... usijali boss. ACP Nora ndiyo malkia hapa," akasema Mario na kugongesha kiganja chake kwa kiganja cha Nora.

"Una akili nzuri sana dada," Omari akamwambia Nora.

"Asante. Lakini... sina uhakika sana kama hii ita..."

"Usijali. Instinct zako zina nguvu sana, ninajua tutapata jambo fulani tu. Na... usijikakamue mno, we ukimaliza kuwaelekeza hawa mbwa toka ukapate chips mayai u-relax kidogo, sawa?" Luteni Michael akamwambia.

Nora akacheka kidogo.

"Dah! Kwo' sisi wengine ndo' tukae kupiga kazi mpaka basi?" akauliza Mario.

"Ndiyo maana yake," Luteni Michael akasema.

Kisha akamwangalia Nora na kutabasamu kirafiki, naye Nora akatabasamu pia.

Baada ya hapo, Luteni na wanajeshi wake wawili wakaondoka wakimwacha ACP Nora na wengine kwenye utafiti huu mpya.


★★★★


LaKeisha, Victor, Oscar, na Kevin walifanikiwa kufika salama sehemu yao muhimu ya maficho kwenye mida ya saa 4 asubuhi. Ilikuwa ni kwenye mkoa mwingine sasa, na baada ya wao kufika huko "chini," walimkuta Torres Dela Robia akiwa ametulia tu akisoma mambo fulani kwenye kitabu. Alipowaona tu, alitambua kuwa Kevin alikuwa ameumia, naye akamwambia aketi ili amchunguze vizuri na kumpatia tiba sahihi.

Kevin akakaa, akiwa bado ameudhika sana kwa mambo yote yaliyotokea, na akiwa anahisi maumivu mwilini mwake. Wengine wakawa wameelekea kufata vyakula upande mwingine wa sehemu hiyo na kuvileta ili wale. Akiwa anamchunguza Kevin, Torres aliuliza yaliyotokea Mwanza, naye Oscar akaanza kumsimulia lakini kwa kutia chumvi nyingi sana kwamba Kevin alipigwa na mwanamke mwembamba tu na mfupi mno.

"Hivi Torres, hakuna dawa yoyote hapa ya kukata maumivu yangu haraka ili niyahamishie kwa bwege mmoja hapa?" Kevin akasema kwa kuudhika.

Torres akatabasamu na kusema, "Hapana."

"Hey, umeshampatia?" LaKeisha akamuuliza Kevin.

"Kunipatia nini?" Torres akauliza.

Kevin akatoa kifaa kile ambacho Lexi alimpa na kumwambia Torres kwamba Lexi alisema ampe.

"Halafu anataka uchunguze kuhusu watu waliomw-attack Kev, umwambie unafikiri nini kuwahusu maana anahofia njia waliyotumia kumfikia inaweza kutuletea shida," Victor akamwambia.

"Mmm... okay. Twendeni," Torres akasema.

Akawa amemaliza kumfungia bendeji Kevin na kuanza kuelekea upande mwingine wa sehemu hiyo. Walifikia chumba ambacho kilikuwa na mitambo mingi pamoja na "screen" kadhaa zilizounganishwa kupitia kompyuta zake maalumu kwa ajili ya mambo mengi aliyofanyia utafiti. Chumba hiki kilijaa makolokolo ya kiteknolojia ya kila aina, naye Torres bila kukawia akaketi na kuanza kupekua taarifa kuhusu watu ambao walimkamata Kevin.

"Kwa hiyo tokea walipokushika mpaka wakati ambao wakina Oscar walikufata, hakuna aliyetambua una tracking device, isipokuwa huyo mwanamke?" Torres akamuuliza Kevin.

"Ndiyo. Sijui hata alitambuaje yaani, ka' mchawi vile," Kevin akasema.

"Eeh, inaonekana ndiyo mchawi wao. Luteni Michael nilitegemea angehusishwa na hili sakata lakini huyu... ACP... inabidi nisake picha za maACP wa kike kwa mikoa yote unionyeshe ni yupi," Torres akasema.

Kisha akaanza kubofya haraka-haraka sana 'keyboard' yake hapo, akitafuta mafaili ya haraka ya picha za Makamishna wasaidizi wa polisi nchini.

"Bado huwa sielewi unafanyaje hayo madude yako haraka haraka hivyo bila hata kuangalia halafu...." Oscar akawa anaongea.

"Hizi hapa, njoo unionyeshe ni yupi," Torres akamwambia Kevin.

"...boom! Tayari unapata unachotaka," Oscar akamalizia alichokuwa anasema.

Kevin akasogea karibu zaidi na kuanza kuziangalia picha hizo, naye akamwonyesha picha ya Nora baada ya kumwona.

"Well, well, well... ACP Nora Lois Nahaman," Torres akasema.

"Ndiyo nani?" LaKeisha akamuuliza.

"Ni Kamishna Msaidizi wa Polisi Dodoma. Lakini jina la cheo hiki lisiwadanganye. Huyu mwanamke ana level za hali ya juu sana kwenye masuala ya upelelezi, na mara nyingi wahuni wanapofanya uhalifu halafu wakashindwa kupatikana, huyu ndiyo huwa anaitwa kuwachokonoa huko waliko mpaka wanawapata," Torres akawafahamisha.

"Mbona anaonekana kama contestor wa Miss Tanzania, siyo kwa uzuri huo! Ameolewa? Kuna namba zake hapo chini?" Oscar akauliza kimasihara.

"Hivi hauwezi kufocus kwa dakika moja tu?" Kevin akamuuliza Oscar kwa kukereka.

"Kinachofanya awe na huo uwezo ni nini? Maana haonekani kuwa mtata kihivyo," Victor akamwambia Torres.

"Looks huh? Hapana. Nora unaweza kumchukulia kama FBI agent Victor. Amesomea Marekani, na hata kuna wakati alialikwa kwenye darasa muhimu la wapelelezi vijana na General wa Ufaransa... tena Ministère De La Défense! Ame-specialize kwenye masuala yote ya decisive action, offensive, defensive, stability, forms of maneuver, reconnaissance, infiltration... yaani ni mtu ambaye sikuzote atakuwa na tentative plan ikiwa moja haitafanikiwa ili kufanya mbili ifaniki...."

Torres akaendelea kumwelezea ACP Nora kwa njia yake yenye ujuzi mwingi. Oscar, Victor, Kevin na LaKeisha walikuwa wanaangaliana tu wasielewe alikuwa anabwabwaja hayo yote kwa ajili gani. Ikabidi Victor aingilie kati.

"Okay, okay, kaka... slow down. Siyo wote humu tunaelewa lugha yako," Victor akasema.

"Na Kevin kuielewa ni mpaka Nora amshushie kipigo kingine," Oscar akasema.

"Sekunde tano zitakazofuata ukitaja jina langu nakushona mdomo," Kevin akamwambia Oscar, naye Oscar akacheka.

"Mtu wa hivyo anawezaje kuwa na cheo cha kifala namna hiyo?" akauliza LaKeisha.

"Well... kwa ninavyojua, Nora mwenyewe ndiyo alichagua hiyo position. Ni mtu fulani asiyependa makuu sana, na sijui ni kwa nini ila ni kama huwa hataki vyeo vya juu kwa sababu fulani. Labda baba yake ndiyo sababu," akasema Torres.

"Baba yake ni nani?" akauliza Victor.

"You'll never guess. Baba yake ni...."

"Vijana..."

Torres alikatishwa na sauti hiyo, na wote wakageuka na kumwona mwanaume waliyemfahamu vizuri sana.

"Boss!" Oscar akaita kwa shauku.

LaKeisha akatabasamu na kumfata Boss wao huyu, kisha akamkumbatia na kusimama karibu yake. Kevin akawa anamwangalia kwa wasiwasi kiasi.

"Boss... uhali gani?" Victor akamsalimu.

"Niko poa. Naona mmerudi," Boss akasema.

"Yaani! Isingekuwa ya huyu mpaka sasa ningekuwa Gold Crest napigwa sunscreen... angalau pale ndiyo pamekaa vizuri Mwanza nzima," LaKeisha akasema, akimaanisha Kevin.

"Boss... ishu yote haikuwa jinsi ambavyo unadhani kwamba...."

Kevin alikuwa ameanza kujitetea, lakini Boss wao akanyanyua kiganja chake juu kumzuia asiendelee.

"Ajali huwa zinatokea, hatuzipangii. Imeshapita hiyo, kilichopo sasa ni stage inayofuata. Torres?" Boss akaongea.

"Yes boss. Lexi ameituma tayari. Kevin ndiyo amekuja na kunipatia, kwa hiyo nitaangalia ni jinsi gani watayaingiza nchini na wakati gani ili tufanye interception haraka," Torres akamwambia.

"Good," Boss akasema.

"Sa'hivi tumeshaanza kupigana hadi na wajeshi. Boss... its so cool," Oscar akamwambia.

Boss wao akamwangalia Kevin, kisha akauliza, "Lexi yuko wapi?"

"Dar. Ameenda na Mensah," Kevin akajibu.

"Amekwenda huko bila sisi boss, naona kama siyo fair. Kwanza ameenda kufanya nini? Maana hata wewe inaonekana hukujua angeenda huko," LaKeisha akauliza.

"Hajaenda kuzurura LaKeish, anafatilia ishu ya Kevin kukamatwa, ndiyo maana anataka nimtumie taarifa juu ya ACP Nora. Sasa hivi mambo yatakuwa complicated kiasi maana Nora ni kichwa. Itatubidi tuwe makini zaidi," Torres akasema.

"ACP Nora?" Boss akauliza.

"Ndiyo boss... huyo huyo," Torres akasema.

"Yeye pia alikuwepo wakati umeshikwa?" Boss akamuuliza Kevin.

Kevin akatikisa kichwa kukubali.

"Ulikuwa unasema ni mtoto wa nani?" Victor akamuuliza Torres.

Torres akanyoosha kiganja chake kumwelekea boss wao ili atoe jibu. Wote wakamwangalia na kuona uso wake ukigeuka na kuwa 'serious' zaidi.

"Nora ni binti ya Jacob," Boss wao akawaambia.

"Jacob as in...." Oscar akauliza.

"General Jacob Rweyemamu?" Victor akauliza kimshangao.

"Yeah," Torres akajibu.

"Umesema anaitwa Nora Lois Namahan, inawezekanaje awe mtoto wa Jacob?" Victor akauliza.

"Anatumia jina la pili la mama yake, siyo baba yake. Na... ni Nahaman, siyo Namahan," Torres akamwambia.

"Kumbe! Kwa hiyo kumbe ndani ya huu mzunguko kuna father-daughter love wanayotaka ituandame? Haitakuwa na shida tena lakini. Lexi ana akili, ndiyo maana ameenda na Mensah ili autungue ubongo wa huyo malaya. Problem solved," LaKeisha akasema.

"Sidhani sana kama anapanga hivyo, itabidi nimtumie info zote then tusikie atasemaje. Bado hajaongea nawe kabisa?" Torres akamuuliza Boss.

"Fanya tu alivyokwambia. Kevin...." Boss akasema.

"Ndiyo boss..." Kevin akaitika.

"Ukimaliza kula, msafishe Zelda," Boss akasema, kisha akawaacha wote.

Kevin akabaki amesimama huku pozi likiwa limemwisha. Oscar akaigiza kama anataka kucheka lakini akaziba mdomo; makusudi tu ili Kevin akasirike.

"Bro, una mikosi. Maliza kula kamwoshe mbwa huyo. Ila angalia asikung'ate," Victor akasema, naye Oscar akaangua kicheko cha kukera sana.

"Usimwite Zelda mbwa bwana," LaKeisha akasema.

"Agh... whatever," Victor akasema na kuondoka hapo.

Kisha LaKeisha na Oscar wakaendelea na mambo yao mengine, wakimwacha Torres anafanya vitu vingi kwenye kompyuta yake kutia ndani kumtumia Lexi taarifa alizohitaji, na Kevin bado akiwa na hasira sana moyoni kwa kuhisi ni kama anadharauliwa. Akaamua tu kuondoka hapo pia na kwenda kufanya kazi ambayo boss wao alikuwa amempa, akitambua ilikuwa ni kama adhabu isiyo ya moja kwa moja.


★★★★★★★★★★★★

ITAENDELEA

★★★★★★★★★★★★

WhatsApp +255 787 604 893
 
Back
Top Bottom