Simulizi:The President and I(Mimi Na Rais)

Simulizi:The President and I(Mimi Na Rais)

The President And I(Mimi Na Rais)- Sehemu Ya Kumi Na Tisa

Misheni Imevurugika


Gideon alikuwa kwenye ofisi yake akiendelea kuandaa ile barua ya majibu ya Rais Costa kwa Rais Chriss wa Marekani. Alikuwa akiweka sawa yale marekebisho aliyopewa na Rais Costa ili ikae kama Rais Costa anavyotaka. Hakuwa na wasiwasi wala kuelewa kinachoendelea. Hakujua kama Macha anaweza kumtaja moja kwa moja kwa Rais Costa.

Gideon alikuwa kama kiungo aliyewekwa kati na Joe na Macha, yeye alikuwa akitumika tu na wala hakuwa akiujua mpango kamili umekaaje na unaendaje. Joe na Macha pia waliaminiana tu hakuna aliekuwa akijua nia au dhumuni la dhati la mwenzake kushiriki mpango ule. Walikuwa wakijua dhumuni la pamoja tu kuwa wanaitaka Stanza mpya lakini nini kimewasukuma haswa waitake Stanza mpya hilo kila mmoja alibaki nalo moyoni mwake.

Ukweli ni kwamba mbali ya Joe kuitaka Stanza mpya kilichomsukuma zaidi ni hasira na kisasi kwa mambo aliyotendewa na Rais Costa. Hivyo kwake yeye hata kama Stanza mpya isipopatikana ilikuwa ni lazima Rais Costa ang’oke kwa njia yoyote ile, japo kama mwanadiplomasia mbobezi alitamani itokee bila umwagaji damu.

Yeye Macha alibaki kuwa fumbo, mbali ya nia ya pamoja hakuna aliejua kinachomsukuma kwa hakika na kama kweli alikuwa na nia ya dhati ya kumng’oa Rais Costa ama alikuwa kazini. Watu wa usalama wa Stanza ni hatari sana.

Gideon akiwa amekaa anamalizia kuandaa yale majibu ya Rais Costa akili ilimtuma kuwasiliana na Meja Byabato. Aligundua kuwa tangu alipofanikiwa kumpa ile ‘code’ ya Sienta-Go hajawahi kumrudia kumuuliza nini kinaendelea. Alishika simu yake ya mkononi na kumpigia.

“Meja, salama mkuu?”, Gideon alimsalimia meja Byabato

“Gideon, salama hapa kweli? Meja alimjibu Gideon akionyesha wasiwasi wake wa njia aliyotumia Gideon kuwasiliana nae.

“It’s a secure line Meja” Gideon alimtoa wasiwasi

“It all depends it is secure to whom’’. Please, let us meet in person as we did last time” (Inategemea ni salama kwa nani. Tafadhali tuonane uso kwa uso kama tulivyofanya mara ya mwisho). Meja alimjibu Gideon na kukata ile simu.

Gideon aliingia kwenye mtandao wa WhatsApp na kumuuliza Meja waonane wapi. Meja Byabato alimtajia eneo na walikubalina wakutane usiku wa saa mbili eneo hilo wapate kinywaji na kujadili mawili matatu.
****************************************

Joe na Habibu walikuwa bado nchini China katika jiji la Beijing. Waliishi eneo la Beixinqiao. Eneo hili lipo katikati ya mtaa wa Yonghegong na Dongzhimen. Ni eneo liliojaa migahawa mingi, baa na viwanda vya bia lakini pia ni eneo linalokaliwa na wageni wengi kutoka mataifa mbalimbali waliopo China kikazi.

Habibu alijitahidi sana kumdodosa Joe ni kwa namna gani alipata chumba kile walichokuwa wakikaa kwasababu hata hati zao za kusafiria zilishaisha muda wa wao kuwa nchini China. Isitoshe wao walikuwa wakitumia hati za kusafiria za kidiplomasia na ukweli walipo hata ubalozi wa Stanza nchini China haufahamu.

Habibu alijitahidi kumwelewesha Joe kuwa kwa wakati huo kama ubalozi wa Stanza utakuwa umetoa taarifa kwa serikali ya China basi watakuwa wapo hatarini lakini pia alitaka aambiwe nini kinaendelea na wataishi maisha hayo kama ya digidigi mpaka lini. Maisha ya kujifungia ndani muda wote bila uhuru yalianza kumchosha Balozi Habibu.

Muda mwingi Joe alionekana akiwa ‘busy’ na simu akifanya mawasiliano ya hapa na pale akipata taarifa na mirejesho kutoka kwa Gideon lakini pia akiwasiliana na mkewe Elizabeth huku akifuatilia kwa ukaribu taarifa za habari za ulimwengu.

“Habibu mdogo wangu, nimeanza kuwa balozi kwa kuiwakilisha Stanza miaka kumi kabla ya wewe kupewa ubalozi. Najua taratibu za kidiplomasia, nyumba hizi tunazokaa si vyema sana nikakwambia ninazipataje kwasasa lakini fahamu kuwa kabla ya mimi kuhamishwa ubalozi na kwenda kuiwakilisha Stanza nchini Urusi, nilishakaa hapa China kwa miaka saba.

Hiyo itoshe kukuonyesha kuwa hapa tulipo, kwangu ni sawa na Stanza. Nina marafiki, nina ‘connections’ hivyo toa mashaka. Jambo la pili mdogo wangu ni kuwa nimefuatilia kutoka kwa watu wangu wa karibu hapa China wamenihakikishia kuwa Stanza wala Balozi Kimweri hajapeleka shauri lolote kwa serikali ya China ya sisi kutafutwa la sivyo tungeshakuwa tumekamatwa. Unadhani jambo hilo linaashiria nini?”, Joe alimalizia kwa kumuuliza Habibu.

“Maana yake Rais Costa anataka kutumaliza kimya kimya”, Habibu alijibu.

“Exactly, na ndio maana nataka uwe na moyo wa ushujaa. Tumekaribia kuimaliza safari japo bado siuoni mwanga. Nilikuuliza kama unataka tukusalimishe kwa Rais Costa kama mwenzako Pius ukakataa sasa, hang in there. We will be fine’’. Joe alimalizia kumpa risala fupi Habibu.

Walimalizia kuzungumza na walikubaliana watoke waelekee kwenye baa ya jirani ili kwenda kupata bia mbili tatu.
*****************************************

Bwana Zhang Wei na Bibi Whang Xiu Ying ni raia wa China. Ni moja ya wafanyabishara wakubwa wa China wenye kampuni zao na biashara zao nyingi barani Africa. Kuanzia miaka ya 2000 wakati China alipoamua kwa dhamira moja kuingia kwa nguvu na kuwekeza kwenye bara la Africa, Zhang na Whang walikuwa ni wafanyabiashara wa awali kabisa kuanza kuwekeza sana nchini Stanza.

Zhang aliwekeza zaidi kwenye viwanda vya kusindika matunda ili kutengeneza juisi, viwanda vya nyuzi na mbolea. Bi Whang yeye aliwekeza zaidi kwenye teknolojia na miundombinu na kwa hakika walitajirika vilivyo kutokana na uwekezaji huo kwenye nchi nyingi za Afrika hasa Stanza.

Wakati maazimio ya China kuingia Africa chini ya utawala wa Rais wa China Kamaradi Hu Jintao yakiafikiwa miaka ya 2003, Joe alikuwa ni Afisa wa ubalozi wa Stanza nchini China. Stanza ikiwa chini ya utawala wa Rais Jonathan Edward ilikuwa na hofu ya kuwakubali Wachina sawa na nchi nyingi za Afrika.

Japo ni ukweli kwamba mahusiano ya China na nchi za kiafrika yana mizizi mirefu ya enzi lakini propaganda za nchi za kimagharibi zikiongozwa na Marekani ambayo kwa wakati huo ndiye alikuwa mshirika mkubwa wa kibiashara na Afrika zilisababisha viongozi wengi wa nchi za Afrika kuingiwa na hofu na ujio wa China kwa kuhofia kupoteza urafiki na Marekani.

Joe akiwa afisa mdogo wa ubalozi wa Stanza huko China alichangia pakubwa kufanikisha Zhang na Whang wanapata fursa ya kuwekeza nchini Stanza. Ni Joe pia alishiriki kama kiungo muhimu wa kumsaidia aliyekuwa balozi wa Stanza nchini China wakati ule ndugu Benson Rwengereza kutengeneza daraja zuri la kuhakikisha China inaingia Stanza na kuwekeza na hivyo kuleta manufaa kwa Wanastanza.

Ni katika mahusiano hayo ya Zhang na Whang waliendelea kuwa marafiki wakubwa wa Joe kiasi kwamba ilifikia hatua hawakuwa tayari kumuona Joe akipata shida kwani alikuwa na mchango mkubwa katika mafanikio yao.

Baada ya sakata la Pius kusaliti kambi ya Joe, ilibidi awasiliane na marafiki zake hawa. Aliwaeleza kuwa yupo nchini China kwa muda kidogo kwa mambo ya kidiplomasia na masomo hivyo aliwaomba wamsaidie nyumba ya kuishi kwa mwezi mmoja mpaka mitatu.

Wafanyabiashara hawa walikuwa na nyumba nyingi katika miji tofauti tofauti. Nyumba hizi zilikuwa za kibiashara hivyo ombi la Joe lilikuwa ni dogo sana kwao. Walimruhusu kukaa na kumwambia popote watakapokuwa wanakwenda kama kuna nyumba zao basi watakuwa tayari kumpa makazi Joe.

Isitoshe, walikuwa wakigharamia chakula na huduma zote ambazo Joe alikuwa akihitaji. Joe alishawasababishia utajiri mkubwa na wao walikuwa wakimwambia kwa kichina Wǒmen méiyǒu shé me kěyǐ huíbào nǐ de yaani hawana cha kumlipa Joe.
*********************************************

Rais Costa alisikia kuchanganyikiwa alipotajiwa kuwa Gideon anahusika kwenye mpango wa kumpindua. Alishindwa kuelewa inakuwaje mtu anaemwamini kiasi kile anaweza kuwa anapanga njama kama zile. Lakini alianza kuunganisha nukta baada ya kukumbuka suala la Meshack kumvamia Sylvanus. Akipata jibu ni nani atakuwa amewasiliana na Meshack, alimwamini Macha. Rais Costa alitaka kutoka kwa hasira.

“Costa unakwenda wapi”, Macha alimwita Rais Costa kwa jina lake bila kutanguliza heshima yoyote.

“Huyu mshenzi Gideon hawezi kunichezea namna hii”, Costa alijibu huku akibonyesha kitufe kinachowapa ishara vijana kuwa wafungue mlango anataka kutoka.

“Sylvester, unarudia kosa lilelile ulilonitendea mimi, kutaka kuchukua maamuzi bila kutafakari”, Macha alimwambia Rais Costa.

“Macha usinitukane, I am your president! Ina maana Stanza inaongozwa na kichaa? Unaniambiaje nafanya maamuzi bila kutafakari?”, Rais Costa alimfokea Macha.

“Samahani Mheshimiwa Rais lakini nakuomba uketi sijamaliza kukwambia ninayotaka kukwambia”, Macha aliomba radhi. Alikumbuka kuwa anaongea na mkuu wa nchi hivyo alipaswa kuongea nae kwa nidhamu.

“Mh. Rais, Gideon ni kiungo tu wa mpango huu ambaye nilikwishamng’amua lakini wapo wengine, nina uhakika na kama nilivyoshughulikia suala la jeshi kutaka kukupindua na kuhakikisha ninang’oa mpaka mizizi suala hili pia latakiwa kushughulikiwa hivyo kwasababu bado wewe na mimi hatujui limejichimbia mizizi kiasi gani.

Masuala haya kwa sisi watu wa usalama tunashauri usiyapeleke kwa pupa, ni mambo nyeti na pengine yamepangwa kiustadi na labda hata kuna mkono wa nje. Gideon si mtu wa kumchukulia hatua bali ni mtu anayepaswa kutufanya tuwajue wengine kwenye mpango huu’’, Macha alipumzika na kumeza mate.

Wakai Macha akiongea Rais Costa alikuwa akimkodolea macho kwa umakini huku akitafakari mambo mengi. Alikuwa akiunganisha nukta kichwani lakini ni kama muunganiko ulikuja na kukata, yaani tungeseama alikuwa akiwaza maruweruwe kwasababu ya taarifa nyingi na mchanganyiko anazoendelea kupokea kuhusu jaribio la mapinduzi.

Hoja ya Macha kutaka kujua mzizi wote wa wanaotaka kumpindua ilimwingia, hoja ya kutomgusa Gideon alisita kidogo. Hoja ya Gideon kuhusika nayo ilikuwa ikisumbua kukubalika kweye ubongo wake lakini akikumbuka suala la Meshack ni kama anaielewa hoja ile. Hakika alianza kutoka jasho pasi kujijua.

“Umejuaje kama Gideon anahusika, mbona ni yeye aliyeomba mimi kuonana na wewe?” Rais Costa alihoji.

“Hajui kama mimi najua na imekuwa vyema kuwa hivi, lakini hivi karibuni utafahamu kwanini anahusika”, Macha alijibu.

“Siyo kwamba siamini, naamini sana kwa sababu hivi ninavyoongea na wewe yule kijana wako Meshack amemvamia Sylvanus tuliyemtuma kwenda kumdhibiti Joe na hakuna aliyekuwa anajua mwingine zaidi yangu na Sabinas isipokuwa siku nilipokuwa ninasaini ile ruhusa ya Joe kuuawa Gideon alikuwepo ingawa sina hakika kama aliona, hivyo bado napata shaka sana”, Rais Costa alifunguka mazima kwa Macha.

“Meshack alifanikiwa kumdhibiti Sylvanus?”, Macha alihoji ili apate kujua nini kiliendelea kwa kuwa habari hiyo hakuwa ameipata.

“Nadhani Sylvanus alimuua Meshack japo bado sijapata taarifa sawasawa”, Costa alijibu.

Macha aliposikia juu ya uwezekano wa Meshack kuwa ameuawa alishtuka kwa ndani ndani. Aliumia sana. Meshack alikuwa ni kijana mwaminifu na kipenzi wa Macha, na ikiwa ni kweli ameuawa basi ni wazi ni pigo kwa kambi yao ya mapinduzi.

“Ndiyo maana nakushauri Mh. Rais utulie nilishughulikie hili suala mpaka mwishowe. Ni wazi basi hata Meshack alikuwa akihusika na sasa nadhani unanielewa ninavyosema mpango huu ni mkubwa. Sabinasi peke yake kamwe hawezi kuujua kwa undani na kwa haraka kama mimi niliyekwishaanza kuufatilia”, Macha aliongea kwa shida maana mdomo wake ulikuwa umevimba.

“Macha sitaweza kukaa na kutazamana na Gideon. Sitaweza”, Rais Costa alijibu kwa hasira.

“Hata mimi sikutaka nikushauri hivyo. Ipo Sehemu nzuri ya kumuweka Gideon ambayo nitapata nafasi ya kufuatilia nyendo zake kwa ukaribu”, Macha alimwambia Rais Costa.

“Wapi Macha? Wapi nimuweke ambapo sitapata hasira kila nimwonapo na uniambie ni baada ya muda gani utakuwa umeweza kugundua wahusika wote ili niwachukulie hatua” Rais alihoji kwa hasira.

“Gideon ni mbobevu wa masuala ya Sayansi ya Siasa ni mtu mwenye weledi sana wa uongozi, mimi nilikuwa nadhani mteue awe Katibu Mkuu wa Chama chetu cha Ukombozi Stanza. Kwa uchapakazi wake huko atakusaidia sana kuleta mapinduzi na wanachama wa kutosha nadhani unajua mipango mikakati yake kisiasa Mh. Rais”, Macha alishauri.

“Unasema nini wewe? Yani mtu anaepanga kunipindua nikampe utendaji mkuu wa chama?”, Rais Costa aling’aka.

“Mh. Rais kwenye chama kuna viongozi wengi na hawezi kufanya lolote la ajabu. Lengo langu la kukwambia umpeleke kule ni mawili. Mosi, nataka umtoe karibu na serikali ili kama kuna watu huku anaoshirikiana nao akose muunganiko nao, lakini pia kama wataendelea kuwasiliana basi watakuwa wakitumia simu ambazo mimi nitaanza mchakato wa kuzifuatilia. Sababu ya pili ni kutaka asione ametupwa nje na hivyo kukatisha mpango ama kumwachia mtu mwingine ambaye itanichukua muda kumtambua hivyo nataka ajione ni sehemu ya utawala wako mpaka pale tutakapomaliza kuwajua washiriki wote.

"Wewe una uwezo wa kuteua leo na kutengua kesho, una wasiwasi gani?”. Macha alisisitiza

Rais Costa alibaki kama dakika mbili akimtazama tu usoni Macha. Hesabu zilikuwa zikikataa kubalansi lakini alikuwa hana namna. Kwake Macha alikuwa ni mkweli kwa wakati huo.

Walizungumza na kukubaliana mengi na Macha. Macha alimwambia Rais Costa hataki kurudia nafasi yake ya Ukurugenzi wa Idara na hivyo amruhusu Sabinasi aendelee ila yeye ataimaliza hiyo kazi maalumu ya kuhakikisha anawaweka hatiani wote wanaoshiri kwenye mpango wa kumpindua Rais Costa kisha atastaafu. Aliomba kijana wake Daudi wa mambo ya mawasiliano nae aachiwe huru na kutaka wapewe ruhusa ya kufikia baadhi ya vitu ili vimrahisishie kazi.

Rais Costa alikuwa ni mtu rahisi kujazwa upepo na kujaa, alitawaliwa na hisia kuliko mantiki na hivyo alikubaliana na Macha kwa yote. Alisikitika sana kwa kitendo chake cha kumtesa bila kumsikiliza. Alimbembeleza pia kama akitaka aendelee na Ukurugenzi wa Idara aseme lakini Macha alishauri kuwa wakati wake wa kutumikia nafasi hiyo umefikia kikomo.

Alimwambia kwa yaliyotokea anawachia tu wadogo waendeleze gurudumu na kuwa kazi hiyo ya kumuweka Joe, Gideon na wengine wote wanaohusika na mpango ule haramu itakuwa kazi yake ya mwisho, ama kwenye lugha ya kigeni wanasema ‘Last assignment’.

Rais Costa alitoa ishara kuwa mlango ufunguliwe na alitoka akiambatana na Macha wakitembea taratibu kuelekea nje. Kagiza kalikuwa kameanza kuingia kwa mbali.

“Pius anaendeleaje? Amesharejea?”. Macha alimuuliza Rais Costa.

“Yes, infact we had a discussion with him and General Ndutta that shortly, he will succeed Ndutta as our new CDF” (Ndio tena nilikuwa na mazungumzo nae yeye na Jenerali Ndutta kuwa wiki chache zijazo nitamteua Pius kama mkuu wetu wa majeshi ya ulinzi na usalama kurithi mikoba ya Ndutta) Rais Costa alimjibu Macha.

“Ni jambo sahihi. Pius ameonyesha uaminifu mkubwa. Angeweza kukubaliana na Joe na kazi ingekuwa kubwa zaidi. Kwa hivyo ni lini utamtangaza”, Macha alihoji.

“Well, I told General Ndutta when he is comfortable, and transition plan is in place they will let me know. I did not want him to feel that this is a forced retirement. He served this country with honor and loyalty and he deserve to be treated as such”

(Nilimwambia Jenerali Ndutta siku akiwa tayari ataniambia. Unajua sikutaka aone kana kwamba ninamlazimisha astaafu. Ameitumikia nchi hii kwa mapenzi na uaminifu mkubwa na anapaswa kufanyiwa hivyo), Rais Costa alimjibu Macha huku wakiwa wamefika mlango wa kutokea nje.

Wakiwa wanasindikizwa na Sabinasi pamoja na walinzi wa Rais walikuta tayari msafara wa Rais umeshajipanga tayari kwa kuondoka.

“Sabinas, Macha amerudi kwa kazi maalumu. Tafadhali mpe ushirikiano wowote atakaohitaji”, Rais Costa alikuwa akimpa maelezo Sabinas Paulo anayekaimu nafasi ya Macha kwa wakati huo katika Idara ya Usalama wa Taifa Stanza.

“Sawa mkuu. Ni bosi wangu bado huyu. Ha ha ha!” Sabinas aliitikia kwa kujichekesha kinafiki.
Macha alimkata jicho la chini chini kwani alijua fika kicheko kile ni cha kinafiki mbele ya Rais.
Rais Costa aliagana na wote na kuingia kwenye gari na kuondoka kurudi Ikulu ya Stanza pale jiji la Peron
*****************************************

Jioni ya siku hiyo kama walivyokubaliana Gideon na Meja Byabato walitafutana ili waonane na kuongea.

“Meja hebu niambie kinachoendelea kwa upande wako maana mimi nipo tu kati kati natoa taarifa huku napeleka huku sasa hali hii siipendelei sana. Nataka kujua kinachoendelea kila upande”

“Gidi mbona mimi sikuwa najua kama wewe ndio utaniletea ile code? Mambo haya huenda kwa namna hii, unachotakiwa kufanya ni kutimiza wajibu wako na kumwachia mwingine atimize wake. Wewe hujasomea masuala haya ya usalama lakini ni kitu cha kawaida kabisa hiki”

“Sawa Meja naelewa lakini sasa nisichoelewa ni kama tunakaribia mwisho, tupo katikati ama tumeshashindwa kwa sababu unakuwa huelewi nini kinaendelea wapi”

“Hilo lisikusumbue kichwa Gidi. We fahamu kuwa nilichotumwa nimeanza kukitekeleza. Mambo haya hufanyika hivi ili kuzuia kama kuna anaetaka kuharibu ama kuwachomea wenzake asipate ushahidi ama kuzuia mpango mzima. Mfano mimi nilikuwa namjua Macha tu na nimekujua na wewe kwa sababu umeniletea lile neno la siri. Hivi ndivyo hutakiwa mambo kuwa tunakwenda kwa alama, ishara na maneno ya siri”

“Sasa kwa mtindo huu nitashindwa kukuuliza nilichotaka kukuuliza Meja”

“Jambo gani Gidi? Niulize”

“Yule kijana aliekuwa akimlinda ‘Eagle’ inasemakana ameuawa, sasa natafuta wa kunihakikishia taarifa hizo nakosa”

“Vijana wengi wanamlinda ‘Eagle’, nawajua baadhi maana sipo sana huko kwenye mambo ya Idara ya Usalama sasa sijajua unamwongelea nani”

“Kuna yule alikuwa mrefu hivi kama wewe mweusi karibu mfanane weusi. Ha ha ha”

“Unamaanisha Meshack?” Meja Byabato alihoji.

“Huyo huyo. Nimesikia ameuawa sasa sijaelewa kwenye mazingira gani na sijui nimuulize nani, mimi na Sabinasi hatuelewani kabisa hivyo siwezi kumuuliza suala lolote”, Gidieon alimwambia Meja Byabato.

“Ameuawa? Kauawaje tena…ngoja nimuulize huyu…” Meja Byabato alihoji kwa kushangaa huku akitoa simu yake ya mkononi na kuanza kumpigia mtu ambae Gideon hakumfahamu.

Eagle ni neno wanalotumia watu wa usalama kumuita Rais Costa. Meja Byabato japo hakuwa akijua mengi ama kujuana na wengi katika idara ya usalama wa Taifa Stanza lakini kutokana na urafiki wake na Stanley Macha aliweza kujuana na wachache, Meshack akiwa mmojawapo.

“Kwa hiyo unasema mwili wake haukuonekana pale Casino? Sasa hapakuwa na Camera kule vyooni?..........Aisee basi sasa endelea kufatilia, utanijuza kamanda huyu kijana wetu bwana si unajua tena sisi watu wa mazoezi vijana kama hawa ndio wetu hawa” Meja Byabato alimaliza kuongea na ile simu.

“Ni kuwa ninasikia Meshack alipambana na kijana anaitwa Sylvanus huko Casino sasa inavyoonekana alishindwa nguvu na Sylvanus alitoa taarifa kuwa amemuaa lakini sasa wao walipofika pale hawakuukuta mwili wa Meshack hivi wanafatilia upo wapi na wameshikilia uongozi wa ile Casino”, Meja Byabato alikuwa akimpa mrejesho Gideon.

Gideon alianza kupatwa mashaka sana juu ya nini kimempata Meshack. Je yupo hai, amekufa ama nani aliuwahi mwili wake na kuupeleka wapi. Hakutaka kuuliza mengi waliongea na Meja kwa muda mchache kisha waliagana.
****************************************

Rais Costa aliingia Ikulu ya Peron akiwa na mawazo mengi sana. Alikuwa kwa hakika haelewi nini kinaendelea kwenye utawala wake, alikuwa hana hakika amuamini nani. Alikuwa akitembea kwenye korido za Ikulu akielekea kwenye makazi yake huku akisindikizwa na walinzi wawili.

Akiwa anapiga hatua simu yake ya mkononi iliita na alikuwa ni Sabinas Paulo akipiga.

“Mh. Rais nimejikaza lakini nimeshindwa nimeona nami niwahi kukupa tahadhari kabla hujatekeleza jambo lolote”, Sabinas alianza maongezi.

“Unasema nini Sabinas?”, Rais Costa aliuliza kwa wasiwasi.

“Kwanza unisamehe kwa kukiuka utaratibu na kuwa nasikiliza maongezi yako na Macha ya faragha. Ila nimeona uongo mkubwa wa Macha ulioniachia mashaka makubwa juu ya alichokuambia. Macha anakuchezea akili Mh. Rais”, Sabinas alikazia.

“Kwanini unasema hivyo? Wakati mpaka sasa hujajua ni nani alimtuma Meshack kumvamia Sylvanus na alijuaje. Kwanini nisimuamini Macha?”, Rais Costa alihoji mfululizo.

“Mh. Rais sijakataa kuwa labda Gideon hayupo kwenye mpango huu lakini nashawishika kabisa kuwa hata Macha yupo na wote wanakuchezea akili. Inakuwaje Gideon alikuwa akikubembeleza sana uonane na Macha? Huoni kama ni mpango huu Rais wangu?”

“Na kama wote wapo kwenye mpango, kwa nini Macha amtaje mwenzake?” Rais Costa alihoji.

“Kwanini akuzuie kumuwajibisha? Kwanini akusihi umpange utendaji mkuu wa Chama? Mh. Rais think deeply”, Sabinas alimsihi Rais Costa.

Rais Costa alibaki kimya kwa dakika kadhaa akitafakari sentensi zote za Sabinas. Alijitahidi kuchekesha akili ikae sawa.

“You are probably right Sabi, Macha is fooling around, bastard! Do not provide him with any access till tomorrow”, Rais Costa alimpa maelekezo Sabinas na kukata simu.

Rais Costa aliendelea kuchanganyikiwa kwa mawazo mgongano kila baada ya muda mchache.
**************************************

Wakati Stanza ikiwa ni jioni ya saa mbili usiku katika jiji la Beijing China ilikuwa ni alasiri ya saa tisa. Joe na Habibu wakiwa amekaa kwenye moja ya baa umbali mchache tu kutoka kwenye nyumba wanayoishi aliwaona watu wenye asili ya Afrika wengi wakiwa nao wanapata kinywaji maeneo yale.

Habibu akiwa hana lile wala hili mwenzake Joe alikuwa akipepesa macho sana kama mlinzi. Ilikuwa ni kawaida yake pindi anapokuwa nje ya nyumba kukaa kwa tahadhari kubwa. Akiwa anapepesa macho ghafla alimwona kijana kwa mbali akikatiza huku akimtupia jicho.

Joe, alikazana kumwangalia vizuri lakini kijana yule alijichanganya na watu wengine hivyo hakuweza kumwona vizuri. Akili ya Joe ilianza kwenda kwa kasi sana katika eneo lake la ubongo kitengo cha kumbukumbu ili kung’amua mtu yule amewahi kukutana nae wapi, kwa kingereza tungesema ni ‘memory searching’.

Haraka Joe alishtuka baada ya kukumbuka kuwa amefanana na picha moja wapo aliyowahi kutumiwa na Gideon. Haraka alichukua simu yake na kuanza kupekua kwenye picha alizokuwa nazo. Hakuamini alipokuta sura ile inafanana na sura ya picha aliyotumwa na Gideon na kuambiwa huyo ndiyo Sylvanus.

“Habibu be prepared. Tunaondoka”, Joe alimwambia Habibu kwa haraka.

“Kuna nini?”, Habibu alihoji kwa hofu akijua labda wanakuja kukamatwa.

“Ni kama nimemuona Sylvanus”, Joe alimwambia Habibu huku akimpa ile simu ili aangalie ile picha.

“Haiwezekani, amejuaje kama tupo hapa Joe. Ngoja na mimi apite nimuone”. Habibu alimjibu Joe baada ya kuangalia ile picha na kuanza kupepesa macho taratibu kuzunguka lile eneo.

Wakati akizungusha kichwa huku na kule kwa kasi ya ajabu yule kijana alikatiza tena kurudi eneo alilotokea huku akiwakata jicho kina Joe.

“Holy shit, he is the one. Sylvanus is here. Tunafanyaje Joe?”, Habibu alishtuka na kuongea kwa kutetemeka.

“I honestly do not know. Tayari tumeshaingia kwenye ‘target’ yake na nina hakika tumezungukwa na wenzake. My God!” Joe kwa mara ya kwanza alionyesha woga wa Dhahiri.
*************************************
Je Huu Ndio Mwisho Wa Misheni?.Tukutane Kwenye Sehemu Ijayo.

the Legend☆
[emoji33][emoji33][emoji33]mission. ....!


Sent using Jamii Forums mobile app
 
The President And I(Mimi Na Rais) - Sehemu Ya Ishirini

Simanzi

Usiku ule haukuwa mzuri kwa Rais Costa, alilala usingizi wa mang’amung’amu. Mawazo yalijaa akili yake na kila alipopata usingizi kidogo basi aliota kuwa anapinduliwa. Hofu ilizizima moyoni, hakuwa akijua amwamini nani, na nani ni adui yake. Akiwaza maneno aliyoambiwa na Sabinas anaona yana mantiki lakini pia alichoambiwa na Macha aliona kina mantiki vilevile.

Hakupata suluhu au kuelewa afanye nini kuzuia hali ile ambayo alianza kuona ipo nje ya uwezo wake. Mtu pekee wa karibu yake ambaye angeweza kumshauri na aliyemuamini ni Gideon na sasa anahusishwa na mpango huo muovu dhidi yake na serikali ya Stanza.

Mke wake, Bi Sara alikuwa ni mfariji mkuu kwa miaka mingi, lakini uwepo wa Ketina na mkewe kuhusishwa na mpango wa mapinduzi uliwaweka mbali kwa kiasi fulani. Walipofika chumbani, kila mtu hakumsemesha mwenzake ingawa wakitoka nje mbele za watu wanaonekana kutabasamu na kucheka pamoja. Ndoa zina siri nyingi.

Rais Costa alijilaza kitandani usiku kucha akisubiri kesho yake atakapouona uso wa Gideon, angemuangalia kwa namna gani. Lakini je, ataweza kustahimili kuficha hisia zake Gideon asijue kama anamshuku kwa lolote kama alivyoambiwa na Macha?

Wakati huo huo alifikiri angemrudiaje Macha kumkatalia mapendekezo aliyotoa wakati alishayakubali na, ni vipi ikiwa Sabinas anampotosha na akapinduliwa, atajutia kutosikiliza ushauri aliopewa na Macha? Hakika Rais Costa alipoteza uwezo wake wa kufikiri na kuchanganua masuala baada ya wiki chache tu za misukosuko ya mapinduzi.
*********************************

Kama Sabinasi alivyoelekezwa na Rais Costa kuwa asimuwezeshe Macha kufikia taarifa na vifaa vyovyote hadi hapo atakapoongea nae tena kesho yake, alifanya hivyo. Hata hivyo Macha hakuomba kupewa ushirikiano wa suala lolote zaidi ya kuomba simu yake ya mkononi ili awasiliane na mkewe.

Macha hakutaka kurudi nyumbani kusalimia familia japo aliikumbuka sana maana likuwa bado na uvimbe usoni kutokana na mateso. Hakutaka kuishtua familia yake kwa kumuona katika hali ile hivyo alitaka tu awasiliane na watoto na mkewe na kuwataarifu kuwa yupo salama na ana kazi itakayomchukua muda kidogo hivyo wamvumilie.

Familia za watu wa usalama huelewa mambo kama haya. Mzazi aweza kutoweka nyumbani hata kwa miezi mitatu kwa kazi maalumu hivyo kwa Macha alitaka asirudi mpaka ahakikishe amepona vidonda na uvimbe wake wote. Aliwasiliana na mkewe kwa njia ya simu ya kawaida. Alifanya hivyo kusudi akijua fika simu zake zitakuwa zikifuatiliwa na alitaka atengeneze mazingira ya yeye kuonekana kile wazungu wanakiita ‘free soul’.

Baada ya hapo alipakua ‘game’ ya clash royale haraka na kuingiza nywila (passwords) zake ili kuweza kujiunga na Gideon na Joe.

“Che, Saddam, Tiger hapa najua tuna mengi ya ku ‘catchup’, lakini la muhimu nijue yafuatayo. Che upo wapi na kama upo salama. Sadam uliweza kuwasiliana na Meja?” Macha aliandika na kusubiria jibu.

Macha akiwa kwenye nyumba moja wapo ya Usalama wa Taifa Stanza alikuwa amepelekwa huko kupumzika. Alisubiri kama dakika kumi na tano na hakuna aliemjibu.

“Tiger, nilifikisha ujumbe na kanihakikishia anaufanyia kazi. Mambo yaliyotokea ni mengi. Kijana alizidiwa nguvu na mpaka sasa yamkini ameshafariki. Umeongea nini na Eagle?”. Alikuwa ni Gideon akijibu kwa shauku ujumbe ule kutoka kwa Macha huku akiwa nyumbani kwake.

“Nimesikia taarifa za kijana nitazifanyia kazi. Nimeumizwa sana. Che ni lazima aseme kama yupo salama kwasababu jamaa wakishafika China na wakifahamu Che alipo, tutampoteza tusipokuwa makini. Kuhusu nilichoongea na Eagle, Saddam uwe na moyo mgumu na lazima ujionyeshe kuwa hujui kinachoendelea.

Nimemwambia mpango huu ni hakika na kweli na kuwa wewe unahusika kwa namna moja ama nyingine. Ni ukweli kuwa atakuwa anakuchukia sana na ni lazima uwe katika hali ambayo hutamfanya ajue kama nimekwambia haya. Nimemwambia akuache nitadili na wewe ila akupange nafasi ya Katibu Mkuu wa Chama”, Macha aliandika.

“Tiger unaongea nini? Umenitaja kuwa Nashiri katika jaribio hili? This is insane! Nitawezaje kufanya asinitambue? Tunapambana kumnasua Che wakati huku unafanya mambo ya ajabu? What is in your mind Tiger?”, Gideon alionekana kushindwa kuvumilia, aliandika mfululizo.

Alisahau kabisa kama sehemu ile haitakiwi uandike kwa uwazi namna ile. Alitamani Macha atokee mbele yake ampige hata ngumi. Suala la Macha kumtaja Gideon kwa Rais Costa kuwa anahusika katika mpango wa kumpindua ulimvuruga akili kabisa. Ni jambo aliloshindwa kufikiria na kung’amua ni nini matokeo yake.

“Come down kid. Kwa hali ilivyo Eagle hawezi kukufanya chochote, ananisikiliza mimi. Utapelekwa kuwa Katibu Mkuu wa Chama na ukifika kule Che atakuelekeza cha kufanya lakini kikubwa ni kuandaa namna ya kumpokea Habibu huko. Ikumbukwe misheni hii ni kufanya mapinduzi yasiyotoa mlio hata kwa Raia. Eagle tunamtoa katika hali ambayo tutaingia kwenye vitabu vya historia, yeye atakuja kugundua tulimtoa labda baada ya miaka mitatu. Itakuwa imebaki historia.

Mpango huu umewekwa kwa namna ambayo raia hawatoshiriki na wala hakutakuwa na umwagaji damu kama ukienda kama ulivyopangwa. Dunia na wanastanza wanapaswa kuamini na kuona kuwa utaratibu huu ni wa kawaida tu kwani hakutakuwa na fujo wala matumizi ya silaha yasiyo na ulazima. Mchakato huu unahitaji umakini na kujitoa. Usihofu”, Kwa mara ya kwanza Macha aliandika kwa urefu sana ndani ya game ile.

“Ninakuheshimu, lakini niseme katika hili mmenikosea sana. Hauwezi kufanya mambo ya hatari kama haya bila kumshirikisha mlengwa kabla ya utekelezaji” Aliandika Gideon.

“Tiger pole sana. Umetenda yote kwa umaridadi mkubwa lakini niseme jamaa wameshafika hapa Beijing na wametuona kwenye mgahawa. Tumeondoka kwa haraka maeneo ya nje na sasa tumekuja ndani kuwapoteza. Ukweli ni kuwa tupo katika hali ya hatari lakini tutajua cha kufanya tu, hatuwezi kukata tamaa. Alikuwa ni Joe amejibu kiufupi.

“Che, naelewa hali mliyo nayo hapo, lakini kuna machaguo mawili tu. Moja muwasiliane na Korea au usubiri na kukabiliana na jamaa wakifika kukudhuru. Chaguo la kwanza litaokoa maisha yako lakini litasimamisha hii misheni kwa muda mrefu kwasababu nyingi ambazo sitaweza kuzitaja hapa. Chaguo la pili litaweka Maisha yenu hatarini na mnaweza kupoteza maisha, kwani nimefanya kazi na jamaa na ninafahamu uwezo wao katika mauaji ya siri. Njia zote zina hasara na faida zake. Uchaguzi ni wako katika hali hii”, Macha aliandika.

Gideon alibaki kimya akitafakari kitendo cha Macha kumtaja kuhusika na jaribio la mapinduzi ya Rais Costa, akili yake ilisimama kufikiri kitu chochote isipokuwa aliwaza ataangaliana vipi na Rais kesho yake asubuhi.

Joe aliwaza sana kisha, “Tiger, nipo tayari kwa lolote ili misheni iendelee. Nitajaribu kupambana, aidha wao ama mimi. Mashushushu wa Korea walinipa silaha baada ya tukio la uwanja wa ndege ingawa uwezo wangu wa kutumia silaha kitaalamu ni mdogo. Najua wanaamini nimemshikilia Habibu na hatakuwa na mengi ya kujibu wala hataguswa na hawa jamaa waliotumwa huku. Nipo tayari kufa”, Joe aliandika.

Kulitokea ukimya wa muda. Hakuna aliyekuwa akiandika chochote. Ilikuwa ni simanzi kubwa kwani kumkosa Joe kwenye misheni hii ingewaweka katika wakati mgumu. Joe alikuwa ni mtu muhimu katika kupanga na kutekeleza misheni ya mabadiliko ya uongozi wa Stanza.

Kitendo cha Joe kukubali kuwa Maisha yake hayana thamani Zaidi ya misheni na kukubali lolote litokee kwake ili misheni iendelee kilimfanya kila mmoja asikitike kwa namna yake. Japo walikuwa hawaonani lakini hakika Gideon na Macha waliiona dhamira ya dhati ya Joe kutaka Rais Costa ang’oke na kuleta pumzi mpya katika kusogeza maendeleo ya Stanza mbele.

“Che, if you will not survive, we shall always honor your commitment in this great mission, forever and for always.” Aliandika Macha na alitoka hewani.

Hakutoka hewani kwasababu aliamua bali betri ya simu yake ilizima chaji na ilimbidi kutafuta chaji aweze kumalizia maongezi yake. Alikumbuka kuwa aliporudishiwa simu hakurudishiwa na chaja. Aliomba muhudumu mmoja wa nyumba ile amtafutie chaja lakini badala yake muhudumu yule alimwambia anaihitaji simu yake.

Wahudumu wote katika nyumba ile ni vijana wa Idara ya Usalama wa Taifa Stanza. Macha alipitiwa na kushindwa kutambua kuwa ule ulikuwa ni mtego aliotegewa na Sabinasi. Alifanya kusudi kumrudishia simu iliyo na chaji kidogo ili aanze kufanya ayafanyayo kwa simu izime na kisha kijana mmoja aichukue hata ikibidi kwa kutumia nguvu na kwenda kunyonya data kujua alikuwa akifanya nini au kuwasiliana na nani.

Kwasababu Macha mara ya kwanza alipokamatwa alifuta taarifa zote kwenye simu yake na walishindwa kupata taarifa hata moja, wakati huu walikuwa na hakika hatakuwa na wazo hilo wala muda wa kufanya hivyo.

Walijua kwa vyovyote vile angekuwa ameweka nywila kwenye simu yake hivyo kwa kutumia utaalam waliouita ‘Phone excavation’ waliamini kuwa watakuwa na uwezo wa kuona kila alichokuwa ukifanya kwenye simu yake kwa kuchukua ‘operating system’ ya simu yake na kuiweka kwenye kadi ndogo na kuiunganisha na mfumo wao ya ‘Phone excavation’. Kwa sababu hajafuta kitu chochote wakati huu wangeweza kupata taarifa zote.

“Abdul, kwa nini unaninyang’anya simu yangu badala ya kunipa chaja?”. Macha alimuuliza yule kijana aliyekuja kuichukua ile simu yake kwa sauti ya upole. Hakuwa anaamini kinachotokea.

“Nimepewa maagizo tu mkuu”, alijibu kwa ufupi.

“Maagizo kutoka kwa nani? Nimepewa kazi na Rais, ni nani mkubwa kuliko Rais?”, Macha alihoji tena.

“Sijui Chief, ila Mkurugenzi ameniambia niichukue. Samahani sana Mkuu”, yule kijana alimjibu Macha na kutoka.

Macha alipata mshtuko mkubwa kwa kujua kuwa kulikuwa na lengo la kufuatilia mawasiliano yake. Alijilaumu sana ni kwa nini amekuwa mjinga namna ile kwa kutong’amua mapema. Alikuwa amekwepa mishale mingi kwa umahiri aliwaza imekuwaje huu umemchoma. Aliumia sana. Alikuwa akijihisi apige kelele kwa nguvu lakini aligundua haitosaidia, macho yalianza kubadili rangi kwa kasi na kuwa mekundu.

“My God, my God, My God….”. Macha kwa mara ya kwanza baada ya miaka mingi aliita jina la Mungu na kuvuta pumzi ya kina.

Ni mara chache hofu ya kifo ilimwingia na uchungu wa dhahiri ulimfika, hii ikiwa mojawapo, Uchungu ulizidi kwa kufikiria ikiwa simu yake ingeweza kudukuliwa na Usalama wa Taifa basi angeiachaje familia yake kwasababu ni Dhahiri kuwa Costa angehakikisha anauawa kwa kosa la uhaini. Alijilaumu sana kwa uzembe huo.
********************************************

Kitendo cha Macha kutoka kwenye maongezi bila kuaga kiliwaacha na maswali mengi Gideon na Joe. Hawakujua nini kimemkuta japo walihisi atakuwa yupo na mtu maana ni kawaida mtu kutoka hewani ghafla kama ameona hali isiyomruhusu kuwa hewani kwenye mawasiliano yale.

“Che, stay safe my brother it was an honor working together and you have been my good friend all long”, Gideon aliandika ili na yeye atoke hewani. Hakuwa na msaada kwa wakati huo.

“You too, kama jamaa wakifika hapa nitakuageni kwa mara ya mwisho. Nikifa, utamwambia Eliza na Derick kuwa nawapenda sana”, Joe aliandika kwa huzuni. Walitoka hewani.
**********************************

Fredrick Nyari alikuwa ni mwenzake na Sylvanus, wote walikuwa Idara ya usalama wa Taifa Stanza kitengo cha Mauaji na Uhujumu. Siku ile mara baada ya Sylvanus kumpigia simu Nyari kumweleza uwepo wa Meshack pale Casino, Nyari alihisi hali ya hatari baina ya watu wawili.

Nyari na Meshack ni watu walioingia pamoja katika Idara ya Usalama wa Taifa. Japo waligawanywa wakati Meshack akipangwa kitengo cha ‘Executive Protection Section’ yaani ulinzi wa watu muhimu Nyari alipangwa ‘Assasination and Sabotage Section’, yaani kitengo cha Mauaji na Uhujumu.

Kugawanywa huku hakukuzuia urafiki wao ulioshibana kuendelea. Ukweli ni kuwa aliewaingiza kwenye Idara ya Usalama wa Taifa alikuwa ni babaye Meshack. Meshack alipopata nafasi alimuombea sana Nyari nae apate nafasi kwani hakuwa amefanya vizuri kwenye matokeo yake ya kidato cha nne wakati ule.

Nyari akiwa mtoto wa kwanza na pekee wa kiume kutoka kwa baba yake ndiye aliyekuwa akitegemewa kuikomboa familia yake kutoka kwenye dimbwi kubwa la umaskini waliokuwa nao.

Meshack ndiye aliekuwa akimsaidia Nyari baadhi ya fedha ili aiwezeshe familia yake pindi ilipokuwa ikimuomba msaada, hivyo deni alilokuwa nalo Nyari kwa Meshack lilikuwa halilipiki.

Simu ya Sylvanus ya kuulizia uwepo wa Meshack pale Casino na jinsi Sylvanus alivyokuwa anaongea vilimtia mashaka Nyari. Alipomaliza tu kuongea na Sylvanus haraka sana aliwasha gari lake na kuelekea Casino muda ule ule. Aliingia na hakuwaona lakini pia alipojitahidi kupiga simu hakuna aliyepokea kati ya Meshack wala Sylvanus. Alipata hofu kuwa suala linaweza kuwa limeshatokea.

Kama zilivyo hulka za wanausalama wengi, hufanya uchunguzi wa haraka katika eneo husika ili kutambua hali ya kiusalama. Nyari hisia zake zilimwelekeza akawaangalie kule vyooni. Aliamini kuna jambo halipo sawa. Nyari akiwa anatembea kuelekea vyooni alimwona Sylvanus akitoka. Nyari alijibanza nyuma ya mtu na kujaribu kumpigia Sylvanus simu aone kama angeipokea.

Huku akiwa anamwangalia akiwa anakatiza kati kati ya watu akielekea nje Sylvanus hakupokea ile simu. Hapo alijua fika kuwa Sylvanus atakuwa amekabiliana na Meshack. Alikimbia haraka vyooni na kuanza kufungua mlango mmoja mmoja kuangalia kama atamuona Meshack. Hakumuona.

Haraka alielekea sehemu maalumu ya kuvutia na sigara na baada ya kuangaza macho huku na kule alimuona Meshack amelala chini akionekana kutokujitambua au kufanya mjongeo wa aina yoyote wa kimwili. Moyo wa Nyari ulilipuka kwa majonzi makubwa. Alimsogelea haraka na kumgusa sehemu muhimu za mwili ili kumkagua dalili yoyote ya uhai. Huu ni utaratibu wa wanausalama na au hata madaktari na watoa huduma ya kwanza sehemu zote duniani.

Kabla ya kuchukua hatua yoyote hupaswa kukagua mazingira ikiwa yanaruhusu kutoa msaada kwa kuangalia pande zote, kisha husogea kwa uangalifu kuelekea alipo muathirika na kufuata taratibu fulanifulani ili kuangalia ikiwa kuna dalili zozote za uhai ili kufahamu ni aina gani ya huduma ya kuifanya kwa haraka ili kuokoa uhai wa muhusika.

Alimgusa kila mahali walipofundishwa kugusa kuangalia kama mtu ana uhai au amepoteza Maisha. Alipogusa eneo la shingo alishtuka baada ya kusikia kwa mbali mapigo ya moyo, lakini Meshack hakuwa akijigusa wala kujibu komandi yoyote aliyofanyiwa ikiwemo kufinywa na kutikiswa.

Nyari alianza kumpulizia mdomoni kuona kama ataweza kushtuka. Alikuwa akifanya yote hayo huku machozi yakimlenga kwani ana historia ndefu na Meshack tangu katika ngazi ya familia zao. Hakuamini anachokishuhudia.

“Aaanghh”, Meshack alishtuka lakini akiwa ameishiwa nguvu.

“It’s fine Shack, mimi Nyari. Twende”. Nyari alimwambia Meshack kwa kumuita jina lake kwa kifupi, jina alilozoea kumuita tangu walipokuwa wadogo.

Meshack hakuwa anajitambua hivyo Nyari alimvua ile kofia ya kininja aliyokuwa amevaa pamoja na ‘gloves’ kisha alimnyanyua na kumsimamisha na kumuegamisha kwenye mabega yake na kuanza kutoka nae nje. Alitembea nae akimkokota kama vile mtu anaemsaidia mwenzake aliyelewa chakari. Walitoka na kuelekea nae anapoishi Nyari.

Kutokea siku ile hakuna aliyejua Meshack yupo wapi. Taarifa za Sylvanus kwa Sabinas juu ya kifo cha Meshack hakuna aliekuwa amezithibitisha kwasababu hakuna aliyeona mwili wake. Meshack alipozinduka alimsihi Nyari asiseme lolote.
**************************************

Gideon alikuwa amelala lakini mwenye mawazo mengi. Alifumba tu macho lakini hakika hakuwa na usingizi. Akiwa amelala alisikia mlio wa ujumbe wa WhatsApp kutoka kwenye simu yake. Aliichukua na kufungua, alikuta ni namba mpya imemtumia ujumbe kwa kuandika jina lake yaani “Gideon”

“We ni nani?”, Gideon aliandika.

“Tafadhali naomba ukae mahali ambapo nitaweza kukupigia simu ya video’’

Gideon alitoka chumbani kwake na kuelekea chumba wanachokitumia watoto wake kama maktaba na alipofika yeye ndiye alipiga ile simu ya video.

“Naitwa Fredrick Nyari”, Kijana yule alijitambulisha huku macho yake yakionekana kulengwa na machozi na akiongea kwa sauti yenye masikitiko makubwa.

“Sikufahamu, na kuna nini basi mbona unanipigia siku usiku wote huu? Na kwanini unalia?” Gideon aliuliza maswali mfululizo kwa hofu.

“Ni Rafiki yake na Meshack na nipo Idara ya Usalama wa Taifa. Kaka Meshack amefariki muda huu” Nyari alimwambia Gideon na kuielekezea kamera kwenye mwili wa Meshack aliokuwa ameulaza kitandani.

“Nyari, please….pl….pleas…Oh God” Gideon alishindwa kuuangalia mwili wa Meshack.

Nyari alimwelezea kila kitu Gideon kuanzia historia ya udugu wao hadi mwisho Meshack alipofariki. Alimwelezea jinsi alivyojitahidi kuokoa maisha ya Meshack lakini ameshindwa kwani anahisi mapafu yalishindwa kufanya kazi na alikuwa akipumua kwa shida huku akikohoa damu mfululizo toka siku ya tukio.

Alishindwa kumpeleka hospitali kubwa kwasababu ya ombi la Meshack na alichokuwa akifanya ni kumpa matibabu yeye kwa kuuliza madaktari. Nyari alimwambia Gideon uhusiano wake na Meshack na kuwa ni Meshack aliempa maagizo yale kuwa siku akifa basi amtafute Gideon na kumpa taarifa hizo. Wote walihuzunika sana.

“Nyari, naomba unipigie picha mwili wa Meshack. Na utauhifadhi vipi? Gideon alihoji.

“Ninajua cha kufanya, mimi ni mwanausalama. Nitauharibu mwili kwa namna ambayo hata vipimo havitoonesha kuwa alishawahi kukutana na mtu mwingine yeyote zaidi ya Sylvanus. Kisha nitakwenda kuutupa kandokando ya barabara ili upatikane na familia yake iweze kumpa heshima za mwisho. Inaniuma sana lakini lazima nifanye hivi ili familia yake ipate mwili huu na wauzike na kubaki na kumbukumbu”, Nyari aliongea kwa huzuni kuu.

“I can’t say a lot. Utakuwa ukinipa taarifa watakapouokota ili niangalie namna ya kushiriki kwenye mazishi yake. Thank you Nyari” Gideon alimalizia na kuagana na Nyari.

Baada ya hapo, Gideon nae alianza kutokwa machozi. Meshack alikuwa na kumbukumbu kubwa kwa kila mmoja na waliumia kumpoteza kwa namna ile. Hakuna aliyeamini kama Meshack amefariki na ule ndio ulikuwa mwisho wake. Meshack aliondoka duniani kwa kuuawa katika kutelekeza majukumu yake ya kimisheni.

Haraka Gideon alichukua simu na kumpigia Joe simu kwa njia ya WhatsApp. Alimweleza kila kitu kama alivyoelezwa na Nyari na alimtumia picha ya mwili wa Meshack.

Ilikuwa ni siku ambayo simanzi ilitawala miongoni mwa wanamisheni. Gideon alishindwa kujizuia na kuanza kulia kwa sauti hali iliyosababisha mkewe Lucia kuamka na kuja kwa haraka kumuuliza mumewe kulikoni. Alimweleza mmoja wa wafanyakazi wa ikulu aliyekuwa rafiki yake mkubwa amefariki.

Lucia mkewe na Gideon alimbembeleza na kumtia moyo lakini haikusaidia sana kwa wakati ule. Ulihitajika muda ili huzuni ile ipungue na hatimaye kwisha. Siku moja haikutosha. Lucia aliondoka na kumwacha Gideon aendelee kuongea na Joe.

“I wasn’t trained to handle the pain for loosing someone close to me. I am breaking. I may as well loose you anytime. Be sure to be safe mate’’, Gideon alilalamika.

“Stop crying Gidi. Some sacrifices must happen in the process. I am as well very low for his ultimate demise”, Joe alimjibu Gideon kwa kujikaza sana. Joe alishakubali kuwa lolote linaweza kutokea na alipunguza hofu ya masuala yaliyo nje ya uwezo wake kuyatawala.

Wote walisikitika kwa namna yao. Habibu alikuwa kimya ila mishipa ya kichwa ikiwa imevimba huku akihuzunika na kutafakari kwa kina. Hakumfahamu marehemu moja kwa moja lakini alijua wazi kuwa alikuwa ni mtu muhimu katika misheni ile.
********************************************

Usiku ulikuwa mrefu, lakini kila liwialo ni lazima lichwee, na kila lichwalo lazima liwie. Hatimaye asubuhi ilifika. Ingawa wakati Stanza kukiwa kunapambazuka, nchini China alipo Joe na Habibu bado ilikuwa usiku wa manane.

Gideon akiwa amejikaza kana kwamba hakuna ajuacho japo alikuwa akijua mengi na akiwa amegubikwa na uchungu mkubwa aliwasili Ikulu za Peron zilipo ofisi zake.

Alipofika tu lango kuu alikutana na Katibu Mkuu Kiongozi Bwana Jabir Salehe.

“Rais anakuulizia sana toka alfajiri. Yaani leo amewahi sana kufika ofisini kunani mdogo wangu?”, Jabir alimuuliza Gideon.

“Sijui kaka mbona hajanipigia simu? Lakini leo ndio aliniambia nirudi na yale marekebisho ya ile barua yake labda ndo hayo anayasubiri”, Gideon alijibu lakini akiwa amejawa hofu. Sauti yake ilitoka kwa kutetemeka.

“Mbona sauti yako inatetemeka leo Gidi. Unaumwa?”. Jabiri aligundua Gideon hayupo sawa. Gideon alikuwa anaona anaongea kawaida kumbe mtu wa pili alimwona kabisa hayupo sawa.

“Najihisi Malaria kaka”, Gideon alijibu kwa kudanganya.

“Sasa mdogo wangu wewe wa Ikulu ukiumwa Malaria yule wa kijijini aumwe nini? Ha ha ha. Haya kaonane na Mkuu”, Jabir alimalizia na kuacha na Gideon.

Gideon aliingia ndani na kuanza kushika korido iliyoelekea ofisini kwake. Alifika ofisini na kujiangalia kwenye kioo. Alijiongelesha mwenyewe kuwa ajikaze. Aliichukua ile karatasi iliyokuwa na marekebisho ya majibu ya Costa kwa Rais wa Marekani na kuanza kutembea kuelekea chumba cha ofisi ya Rais.

Alifika na kufunguliwa mlango na walinzi na kuingia. Alikutana uso kwa uso na Rais. Costa alimwangalia Gideon machoni kama dakika mbili hivi mfululizo bila kumsemesha. Hata Gideon alipojaribu kumsalimia hakumjibu. Kadiri Gideon alivyotazamwa na Rais Costa ndivyo alivyozidi kutetemeka na kupata hofu ya suala aliloambiwa na Macha. Alitetemeka mpaka viliota vile vipele vya mtu anaesikia baridi kali.

“Gideon, nataka nikupangie kazi kubwa kidogo. Nimekuamini sana na sasa nataka ukaninyooshee Chama. Nataka nikupe Ukatibu Mkuu wa Chama Chetu Cha Ukombozi Stanza, kama kumbukumbu zangu zipo sawa nadhani hata shahada yako ya Uzamili ulisomea Sayansi ya Siasa sasa umepata pa kuifanyia kazi. Niambie unataka nini chochote nitakupatia ili ukafanye kazi kwa uhuru na ufanisi”, Rais Costa alimwambia Gideon kwa sauti kubwa baada ya kimya kirefu.

“Mh. Rais hapana. Nashukuru kwa uaminifu wako lakini sitaweza. Najua ni heshima kubwa na ninajua ni nafasi kubwa kuliko hii niliyo nayo sasa lakini kwa nidhamu kubwa naomba umpe nafasi hiyo mtu mwingine mwenye uzoefu na siasa zetu za Stanza”, Gideon alijibu kwa nidhamu kubwa.

“Gidi, unanishangaza. Wewe ndiye umekuwa ukinishauri yote ninayokwenda kuyaelekeza kwenye chama sasa inakuwaje useme huwezi? Lazima uende kule bwana”, Rais Costa alionekana kusisitiza.

“Mh. Rais, unajua sijawahi kuweka pingamizi ya jambo ulilowahi kushauri na unajua utii wangu kwako. Ninakuomba sana kama sikufai hapa, basi Mtukufu Rais naomba unipe ruhusa nikapumzike na kufanya majukumu mengine kwa amani kabisa. Kazi yangu hapa ninaifurahia na inanipa nafasi ya kujifunza mengi zaidi.

Pia ninakusudia kufanya Shahada ya Uzamivu ya Mahusiano ya Kimataifa na ninaamini katika nafasi yangu ya sasa ninajifunza mengi zaidi hasa kupitia wewe unavyoendesha mahusiano na mataifa mengine”, Gideon alijibu kwa heshima kubwa.

Rais Costa alimtazama tena usoni Gideon kwa sekunde kadhaa bila kumwambia neno. Kisha alimruhusu aketi.

Ule ulikuwa ni mtego. Rais Costa aliamua kumpa zile taarifa Gideon ali amuone angezipokea kwa namna gani. Nafasi ya Ukatibu Mkuu wa Chama ilikuwa na maslahi makubwa kuliko nafasi aliyokuwa nayo Gideon kwa wakati huo. Isingewezekana mtu yeyote akatae nafasi ile.

Lakini jambo la pili kabla ya kwenda kuonana na Macha alitaka ajaribu kuona kama Gideon angekubali. Kwa kufanya hivyo basi ingeleta kiashirio kuwa ni mpango wamepanga Macha na Gideon kama alivyoambiwa na Sabinasi. Kitendo cha Gideon kukataa na kuwa tayari kuacha hata kazi na kurudi nyumbani kilimpa uhakika kuwa Gideon hana ajualo na kuwa Sabinas ana wasiwasi wa bure.

Rais Costa alianza kuona pengine utendaji wa Sabinasi unasukumwa na hisia za wivu kuwa ikiwa angeruhusu yeye Rais amuamini Macha tena, basi angeweza kurudishiwa Ukurugenzi wa Usalama wa taifa na yeye kuondolewa

“Nipe hiyo barua. Halafu unaumwa? mbona umenyong’onyea namna hiyo Gidi?”, Rais Costa alimuuliza Gideon huku akichukua ile barua na kuisoma.

“Ndiyo mkuu, nahisi nina malaria”, Gideon alijibu.

Rais Costa alikaa kimya akiwa anasoma na kuhakikisha kama yale marekebisho aliyoagiza yamewekwa sawa na Gideon.

“This is now perfect. Mpe Jabir aitengeneze kwenye muundo maalum kisha nipatiwe niweke sahihi aitume. Pole sana Gidi. You need to consult a doctor if the situation persists. Ukiona umezidiwa ukapumzike”, Rais Costa alimwambia Gideon.

“Asante Mheshimiwa”, Gideon alijibu huku akiichukua ile barua.

Akiwa anajikusanya pale ili atoke simu ya Rais Costa iliita na Rais aliipokea.

“Mh. Rais you need to come and see this”, Alimsikia Sabinas kwa mbali akimwambia Rais Costa.

“Nini Sabinas, nije wapi? Huwezi kuniita mimi kiholela hivyo unajua sitembei tu kiholela kama wewe there is a process comeon” Rais Costa alionekana kufoka.

“Msafara nimeshauweka tayari unakusubiri nje mkuu, nakuomba sana hapa kwenye nyumba yetu anayoishi Macha”. Sabinas alisikika.

“Gideon twende”, Rais Costa alikata simu kwa hasira na kumuamuru Gideon aongozane nae.

Baada ya dakika kama kumi na tano walifika kwenye nyumba aliyokuwa amelala Macha na walipokelewa na Sabinas pamoja na maafisa wengine waandamizi wa Idara ya Usalama wa Taifa Stanza na kutembea moja kwa moja kuelekea kwenye chumba alichokuwa amelala Stanley Macha.

Sabinasi alifika na kuusukuma mlango.

“Holy shit” Rais Costa alipata mshtuko mkubwa mara baada ya kuuona mwili Stanley Macha ukiwa umelala pale sakafuni huku povu jingi likiwa limemtoka mdomoni.

Gideon alisogea kwa kupiga hatua kama mtu anaenyata asitake kushuhudia anachotaka kukitazama. Alijihisi kama anaota lakini ulikuwa ni ukweli Stanley Macha, aliyekuwa amelala pale chini alikuwa AMEFARIKI.

Chumba kizima kilizizima kwa ukimya. Rais Costa alipiga magoti chini na kumshika shavu Macha huku akitokwa na machozi pasi kusema neno lolote. Aligugumia kwa uchungu lakini hakutaka kuachia kilio.

Gideon alipatwa na huzuni kuu na alitaka kuuliza sababu za kifo cha Macha lakini akasita. Alitoa simu yake akapiga picha mwili wa Macha kwa siri kisha akamtumia Joe bila kumwambia neno lolote. Aliogopa sana. Kifo cha Meshack na sasa Macha kilizidi uwezo wa Gideon wa kuhimili huzuni.

Mwili ulishindwa kuhimili simanzi iliyojaa moyo wake. Aliifanyia simu yake ‘Hard reset’ ili kufuta kila taarifa kwenye simu yake maana alijiona anaanza kupoteza nguvu, na haikuchukua dakika hata tatu Gideon alidondoka na kupoteza fahamu.
************************************

Huko Beijing China ilikuwa ni usiku wa manane. Joe hakuwa amelala, alijawa huzuni kwa kifo cha Meshack lakini pia hofu ya uwepo wa Sylvanus ilimtanda pasi kawaida. Akiwa amekaa anatazama luninga alisikia mlio wa simu wa WhatsApp. Aliinyanyua simu yake haraka na kufungua kuangalia ni taarifa gani imeingia.

“Jesus Christ”, Joe aling’aka kwa nguvu kitendo kilichomfanya Habibu aliyekuwa amejilaza kwenye kochi pembeni ya Joe kushtuka.

Joe alikuwa ameipokea ile picha ya mwili wa Macha aliyotumiwa na Gideon.

“Nini?”, Habibu alishtuka kwa hofu.

Joe bila kusema neno huku akitoa machozi mengi kabisa alimpa Habibu ile simu ili aitazame.

“Ya Allah!” Kwa mara ya kwanza Habibu alianza kutokwa na machozi.

Joe aliinamisha kichwa juu ya meza huku akiwa ameuficha uso wake kwa viganja vya mikono lakini machozi yalipenya kwenye vidole vyake kwa jinsi yalivyokuwa mengi. Kila mmoja alikuwa kimya.

Baada ya dakika kama tatu hivi Joe aliichukua simu yake na kuanza kumpigia Gideon kwa kutumia WhatsApp lakini siku haikuweza kuunganishwa. Alijaribu mara nyingi bila mafanikio. Wakati akiendelea kujaribu mlango wao uligongwa.

“Habibu nasikia mlango umegongwa”, Joe alishtuka na kumwambia Habibu kwa sauti ya chini kabisa.

“Hata mimi nimesikia”, Habibu nae alikata kilio na kumjibu Joe.

Waliangalia saa ya ukutani na waliona ilikuwa ni saa tisa usiku kwa saa za China.

“Nenda kwenye dirisha lile utaweza kuchungulia nani amesimama mlangoni. Hakikisha unachungulia kwa kujificha. Tumia upande ule ambao hatujawasha taa” Joe alimwelekeza Habibu.

Haraka Habibu alinyanyuka na kufuata maelekezo ya Joe. Joe alibaki amekaa pale chini asijue afanye nini.

Habibu alifika na kuchungulia kisha akiwa pale dirishani alimgeukia Joe na kumtazama kwa jicho la kukata tamaa. Alirudi na kumsogelea Joe karibu.

“Joe, ni Sylvanus anagonga. Na kwa mbali nimewaona watu kama watatu hivi, nadhani wapo pamoja. Tunafanyaje”. Habibu alionekana kumwambia Joe kwa sauti ya chini sana na ya mtu aliekosa Tumaini.

Joe, hakumjibu neno lolote Habibu. Alinyanyuka na kumkumbatia kwa nguvu na kwa ufupi na kuchukua bastola yake aliyopewa na mashushushu wa Korea kwa ajili ya ulinzi wake binafsi. Alisogea na kukaa kwenye moja kati ya kona za chumba kile na kumuelekeza Habibu akae kwenye moja ya kona akiwa amenyoosha mikono yake juu ili wakiingia basi wasimpige risasi kwa kuona kuwa hakuwa na madhara kwao. Yeye aliamua kuwa ni bora afe kuliko arudi Stanza na kuangukia mikononi mwa Rais Costa.

“I pray that you stand your ground and you shall become a great leader one day. Do not forget us in your story. Joe alikuwa akimwambia Habibu kutokea kwenye kona aliyokuwepo.

Mlango ulizidi kugongwa. “Nenda kamfungulie”, Joe alimwachia Habibu na kumwagiza.

“Joe siwezi. Siwezi kuhalalisha kifo chako. Tuombe msaada Ubalozi wa Korea tafadhali.” Habibu alishindwa kustahimili.

“Hapana. Hata hivyo tumechelewa sasa natamani tufanye hivyo baada ya kuona kifo kimenifikia na kifo cha Macha na sintofahamu ya Gideon lakini hapana. Kafungue mlango”, Joe alisisitiza huku mlango ukigongwa tena kwa fujo.

“Hapana sitafungua Joe. Hapana” Habibu aligoma.

Joe alimtazama Habibu machoni kwa sekunde kadhaa na kuuelekea mlango ili akaufungue mwenyewe.

Wakati akielekea kwenye mlango, alisikia milio isiyo ya kawaida masikioni mwake ingawa alifahamu ni nini hasa. Alisikia risasi zikifyatuliwa lakini mlio wake haukwenda mbali kwasababu silaha zilizotumika zilifungwa kiwambo maalumu cha kuondoa sauti au kwa Kingereza wangeita ‘bullet silencer’. Joe aliondoka kwa haraka eneo la mlango na kurudi kwenye kona aliyokuwapo huku akiishikilia bastola yake kwa makini. Mikono ilikuwa ikimtetemeka.

Habibu aliendelea kuwa na hofu kuwa huu ndiyo mwisho wa Maisha yao. Aliamini kuwa wahudumu wa eneo lile walipigwa risasi na kina Sylvanus ili waweze kuingia kwa uhuru zaidi kutekeleza majukumu yao.

Wakiwa bado hawajui wafanye nini mlango ulizidi kugongwa Zaidi na wakati huu uligongwa kwa fujo. Kwa sababu walisikia ile milio ya risasi wakati huu hata ujasiri mdogo aliokuwa nao Joe wa kutaka kupambana na Sylvanus uliondoka. Alikiona kifo hiki hapa kunamwita hadharani. Alishindwa hata kuishikilia vizuri bastola aliyokuwa nayo.

Wakiwa kila mmoja amesimama kwenye kona yake wakitazamana kwa macho ya kupeana buriani Joe alisikia mlango ukifunguliwa kwa nguvu kwa kitu kuingizwa kwenye kitasa cha mlango na loki ikafyatuka.
****************************************
Taarifa.

Nini Kimeendelea Katika Kisa Hiki?Joe Amepona?Misheni Itafanikiwa?Usikose Mwendelezo Kwa Kusoma Nusu iliyobaki Ya Simulizi Hii Kwa kununua Kitabu Kitakachokuwa Mtaani Muda Mfupi Ujao.

Kisa Hiki Kimeboreshwa Tena Tangu Mwanzo Na Kitakupa Ladha Tamu Zaidi Kuliko Iliyokuwa Mwanzo. Tumalizie Nusu Iliyobaki Ya Kisa Hiki Kwenye Kitabu.

Asanteni.

the Legend☆
 
Back
Top Bottom