Simulizi ya Kijasusi: Jiue Mwenyewe (Jimwangi)

Simulizi ya Kijasusi: Jiue Mwenyewe (Jimwangi)

Usiku huo tayari Kamanda Amata alikuwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwl. Nyerere akaijaribu kuona kama anaweza kuwakamata watu wake, alikuwa amezinasa picha zao kichwani. Aliegesha gari akateremka na kufunga mlango nyuma yake. Akiwa ndani ya suti nadhifu iliyoficha moja ya bastola zake anayoipenda sana, Kamanda Amata akatembea taratibu kuelekea ofisi ndogo ya KLM. Pale alimkuta mwanadada mrembo akiwa ametulia ofisini mbele akitazama kompyuta kubwa aliyokuwa akiitumia kutatulia matatizo yake kikazi. Akakaribishwa naye akakaribia, akavuta kiti akakaa.

“Naitwa George Kamasi,” akajitambulisha uongo kisha akampa kitambulisho yule mwanadada, akakipokea na kukisoma, kilimwelezea Kamanda Amata kama George Kamasi, mwajiriwa wa Wizara ya Mambo ya Ndani katika jeshi la Polisi kitengo cha uchunguzi wa makosa ya Jinai. Yule mwanadada akamrudishia, “Ehne bwana Kama… mh! Na hilo jina lako mpaka linatapisha,” akasema yule mwanadada.

“Uwe na adabu unapoongea na watu usiowajua,” Kamanda akapiga mkwara.

“Nikusaidie nini?” akauliza kwa utulivu baada ya kuona bastola iliyolazwa mezani kwa utulivu.

“Naomba unipe orodha ya wasafiri wako hasa wanaoelekea Uingereza, Canada na Honolulu,” Kamanda akaomba. Yule mwanadada akafanya harakaharaka kuitoa orodha hiyo kwenye mashine yake akaprinti na kumpa Kamanda Amata. Amata akaitazama haikumfurahisaha sana kwani Honolulu hakukuwa na abiria yoyote anayekwenda huko, Uingereza kulikuwa na abiria kumi na tano lakini wote walikuwa wanafunzi wa chuo kimojawapo cha huko ambao walikuja kwa utalii wa kimasomo na Canada kulikuwa na watu wawili, lakini wote wanawake. Akashusha pumzi. Ina maana wametucheza shere? Akajiuliza, akachukua zile karatasi na kuzikunja kisha akazitia katika mfuko wandani wa koti.

“Umeridhika?” yule mwanadada akauliza.

Kamanda Amata akamkazia jicho baya, “sijaridhika,” akamwambia.

“Sasa mimi nifanyeje ili uridhike?”

“Ulale na mimi leo,” Kamanda akamjibu bila kucheka.

“Ha ha ha ha huwa silali na wanaume ovyo ovyo, mi matawi ya juu nalala na Mapedeshee,” akajibu huku akinyanyuka.

“Hebu tulia hapo unaenda wapi? Unafikiri mi nimekuja kucheza hapa, akatoa karatasi nyingine na kumpatia, zilikuwa karatasi tatu, zenye picha za watu watatu tofauti.

“Hawa ni nani?” akauliza.

“Nataka uwatambue hao watu, kama wamekuja hapa kukata tiketi siku za nyuma, au unao katika ndege yako, hao ni majambazi wa Kimataifa na ukiwatetea leo unalala selo mwanamke jeuri,” Kamanda akazungumza kwa sauti kavu. Yule mwanadada akatazama zile picha, akachukua namba za tiketi zao na kuingiza kwenye mfumo wao wa kompyuta.

“Hamna watu kama hawa kwenye ndege yetu, kwanza tiketi zao ni feki, ona,” akamgeuzia kioo cha kompyuta, kisha akaongeza, “kama waliwaambia kuwa wanasafiri na ndege yetu leo, hatuna hawa abiria kaka.”

Kamanda Amata au Amata Ric akachukua zile karatasi zake na kurudisha kunakohusika. Akanyanyuka na kusimama wima.

“Ok, asante, na lile nililokwambia la kulala na mimi, tumeishia wapi?” Kamanda akachokoza.

“Heee! Hebu nitokee huko, we unafikiri mi wa kulalwa hovyo hovyo tu, nina watu wangu wenye pesa sio kama wewe unayetegemea kamshahara ka Wizara mwisho wa mweli, go fish,” akasema huku akimtazama Amata kwa jicho la dharau, mwisho akasonya.

“Ok, una maneno machafu wewe, ila ujue tu utaishia mikononi mwangu iwe kwa heri au kwa shari,” Kamanda akatoka na kuondoka.


“Yaani bila shaka yoyote tulitekwa, nakumbuka tukiwa tuko angani dakika thelathini baada ya kuruka kutoka Mara, hewa ndani ya ndege ilikuwa nzito sana, mzunguko wake ukawa hafifu, nilipotazama kwenye vipimo vyetu, vikaniashiria kuwa kuna shida katika mfumo wa oksijeni, hivyo sikuwa na budi ili kuokoa abiria wangu nikawaamuru kutumia hewa ya mtungi kwa kuvaa barakoa maalum kwa kazi hiyo, baada ya kuzivaa nikajikuta nashindwa kupumua sawasawa, kifua kinakuwa kizito, mwili unaishiwa nguvu, nikaitoa na kuitupa kando,” Rubani wa serikali aliyekuwa katika ndege ya msafara wa waziri alieleza kinagaubaga.

“Baada ya hapo uliona nini?” Madam akauliza.

“Baada ya hapo niliona kama kivuli cha mtu anayeingia ndani ya chumba cha rubani na kuwatoa wenzangu vitini, hapo sikuona tena kilichoendelea,” akajibu.

“Pole sana Kepteni. Kuna wizi mkubwa sana uliofanyika na ndege yako imetumiwa kubeba kasha tano za almasi zenye thamani ya Shilingi za Kitanzania Trillion moja kwa hesabu ya haraka haraka,” Madam akamweleza. Yule Rubani akashtuka na kupigwa na hamaniko, “Lo! Itakuwa walewale wazungu, maana hata kabla hatujaondoka walikuwa wadadisi sana, mara waniulize aina ya ndege ninayoirusha, mfumo wake ukoje, mara hiki mara kile, ah, mi nikawa nawapotezea tu,” akawaambia.

Baada ya saa moja ndani ya chumba hicho cha mahojiano alikuwamo mwanadada mmoja mrembo tu, aliyesuka nywele zake kwa mtindo wa rasta za Kimasai zilizomkaa vizuri, Madam S alimkaribisha kitini na kuketi katika mtindo wa kutazama. Madam S alimtazama mwanadada huyo kwa dakika tano bila kumsemesha neno, kisha akafungua kinywa chake.

“Umeolewa?” akamwuliza.

“Hapana,” naye akajibu kwa sauti ya unyonge.

“Una bwana au mchumba?”

“Ndio, nina mchumba tutafunga ndoa mwezi ujao,” akaeleza.

“Nieleze Historia yako kwa kifupi,” Madam alimwomba na yule dada akafanya hivyo.

“Kwani samahani mama, hapa ni wapi nafanya nini? Ni haki yangu kujua kama Mtanzania,” yule mwanadada akauliza.

“Ok, we ni Mtanzania mzuri unayejua unachotakiwa kujua, hapa ni Hospitali ya vichaa, wewe umeletwa hapa baada ya kukamatwa ukitembea bila nguo mitaani,” Madam akamweleza.

“What? Mimi?” akashtuka na kusimama.

“Ndiyo wewe, ulikuwa unazunguka mtaani bila nguo kabisaaaaaa, ndio maana nikakuuliza una mchumba au Bwana,” Madam akamwelewesha.

Upande wa pili wa chumba, Chiba alipasua cheko aliloshindwa kuzuia, lakini bahati nzuri sauti haipiti chumba cha pili na wala haiwezi kuingilia ile rekodi anayoifanya ya mahojiano hayo.

Gina naye alikuwa hoi kwa kucheka, “mwe! Huyu bibi huyu anajijua mwenyewe, sasa ona alivyomvuruga dada wa watu halafu mwenyewe yuko sirias,” Gina alimwambia Chiba.

“Hebu nambie, cha mwisho unachokumbuka katika maisha yako, ulikuwa wapi?” Madam akaanza.

“Nilikuwa Musoma katika mgodi wa North Mara,” akajibu.

“Ulienda kufanya nini?”

“Nilifuatana na msafara wa waziri na wawekezaji wake katika kutembelea migodi ya serikali.”

“Enhe baada ya hapo,” Madam akahoji.

“Sijui kwa kweli na hisi tulipata ajali, maana tukiwa kwenye ndege hali ya hewa ilikuwa mbaya sana, sikumbuki kilichotokea zaidi isipokuwa nikajikuta hospitali,” akajibu. Kisha Madam S akamweleza kila kitu juu ya sakata la madini, yule mwanadada aliishiwa nguvu kabisa, macho yakamtoka pima.

“Usiposema ukweli, unafungwa, kwa maana wenzako wote wametoroka we ndio tumekukamata,” Madam akamtishia, “Uliwaonaje hao wawekezaji?” akaongeza swali.

“Aaa nimekutana na wawekezaji au wafanyabiashara wengi pale wizarani kwa kuwa mimi ofisi yangu ni mambo ya mawasiliano, ila hawa walikuwa walikuwa wahuni sana, halafu walikuwa hawatulii kwenye; mara chooni, mara kwa mhudumu wa ndege, mara sijui vitu gani, mmoja akawa ananitaka kimapenzi pindi tukirudi Dar,” akaeleza. Maneno haya yakamgusa Madam S, tofauti na wengine wote, huyu alijibu zaidi.

“Ulimkubalia?” akauliza.

“Hapana, ila alinipa kadi yake ya biashara kuwa tukirudi nimtafute ikiwezekana nikamtembelee Ulaya au yeye angekuja tena kwa ajili yangu,” akaeleza.

“Hongera mwenzetu umejipolea ‘Nyanyamkala’ la kizungu, sasa ungewasiliana naye vipi?” akauliza tena. Madam S alikuwa na maswali madogo madogo lakini yaliyoleta tija kwa kazi hiyo. Yule mwanadada akatoa kadi ya kibiashara akampa Madam S.

“Alinipa card yake hii hapa,” akamwonesha Madam S. akaichukua na kuigeuza geuza, akaitazamisha kwenye kioo kikubwa ambacho kama si mjanja huwezi kujua kama ni kioo, kisha akaigeuza upande wa pili na kuiweka mezani.

Kitendo cha kufanya hivyo, upande wa pili Chiba alielewa, hivyo aliipiga picha ile kadi kutoka upande wa pili na kuingia kumbukumbu zake kwenye kompyuta yake bila mwenye nayo kujua. Kutoka upande wa pili walipo Chiba na Gina, Chiba akaiingiza ile taswira ya kadi katika kompyuta maalum, iliyounganishwa na mtandao wa uhalifu duniani, akaagiza imletee majibu juu ya namba za simu, picha na maelezo mengine.

Madam S, akamruhusu yule mwanadada akapumzike, Dr. Jasmine akaingia na kumchukua kisha akampeleka katika chumba chake cha siri.
 
JOPO LILE LA WATU WATATU lilikutana tena mahala palepale, kama kawaida kila mmoja huwa ana njia yake ya kufika hapo, wakamkuta mkuu ameketi akiwasubiri, lakini alikuwa katika hali tofauti sana.

“Ndiyo Mkuu tumekutana kama ilivyo ada, tupe ripoti yako ulivyotuahidi kisha tujue tunafanya nini,” alipendekeza mjumbe mweusi.

“Tunahitaji kufanya kazi ya ziada ndugu zangu, kama tetesi zilivyokuwa kwanza lakini sasa nimeanza kuogopa, vijana wetu wamerudi, mzigo wa Almas umefika tulipoutaka ufike bila tabu, lakini njama imeteguliwa, wale jamaa wa TSA wameweza kugundua kuwa wizi ule haujafanywa na waziri wao, na hii inanitisha kwa sababu mpango wetu ulikuwa yule waziri afie mle ndani ili asionekane tena, kwa mtindo huo tungewajengea imani Watanzania kuwa ni waziri aliyefanya hivyo. Sasa wamempata, kambi yetu ya Mwanza imepekuliwa na kila kitu kiko wazi, hawa jamaa wanataka kupiga hatua ya pili, wanataka kuachana na ya nyumbani na kuwasaka wale makomandoo wetu tuliowatuma. Wakianza kuwachunguza na kufanikiwa kuwagundua, mambo yataharibika,” aliwaambia wajumbe walioonekana kupigwa na butwaa la mwaka.

“Yaani kanchi kale kanajifanya kana idara nzuri ya usalama? Tumewashinda CIA kwenye sakata la kuiba data pale Langley na mpaka leo wamekili kushindwa, tumewazidi kete KGB na tukapata siri za wanaotafutwa na majasusi hao, nini TSA? Ni kuwamaliza tu kabla hatujafanya kazi nyingine, kama ni kikwazo ni kuwapoteza tu, mbona kazi hiyo ni ndogo, kisha Tanzania itajikuta inaamka bila Jasusi hata mmoja,” akaongea kwa hasira yule Mwarabu.

“Sawa lakini tunafanyaje?” yule mkuu akawarudishia uamuzi.

“Tupeleke kikosi chetu cha siri, kikawapeleleze kikiwagundua na udhaifu wao basi ni kuutumia na kuwamaliza, wakati wao wanaomboleza, sisi tunamalizana na mtu wetu,” yule mweusi akaongea.

“Good Idea,” (wazo zuri) Mkuu akaitikia.

“Sasa naomba kila mmoja kwenye idara yake akahakikishe analifanya hilo, tukutane tena masaa sita yajayo tumalize kazi.

DAR ES SALAAM – SHAMBA

MADAM S ALISHUSHA FAILI DOGO yaani lenye kurasa chache mezani pake, katika ofisi ya siri huko ‘Shamba’, alijiridhisha na taarifa zote zilizowekwa na Chiba katika faili hilo juu ya mtu anyeitwa George Mc Field, Komandoo mtoro wa jeshi la Serbia, anayejihusisha na kazi za kukodi kufanya matukio yenye utata kama haya. Alikuja Tanzania mara ya pili akiwa bado ana kumbukumbu juu ya sakata la walilolipa utambulisho kama ‘Mwanamke Mwenye Juba Jeusi’ jinsi alivyoponea chupuchupu dhidi ya mkono wa Kamanda Amata, na mwenyewe alikiri kuwa huyo ni ‘Mwanaume wa chuma’. Kwa jinsi alivyoweza kujibadili kitaalamu akiwa huko kwao, aliamini wazi kuwa hatoweza kugundulika na mahasimu wake ambao walisikitika kuikosa roho yake akiwemo Madam S.

Madam S analikumbuka jina hili, anatabasamu anapogundua kuwa, mtu huyo kajibadilisha sura na muonekano wake lakini kashindwa kujibadilisha mbinu zake. Bomu dogo la misumari lililolipuka kwenye moja ya vyumba vya lile jumba kule Mwanza na kumuumiza Madam S mkononi lilimkumbusha lile ambalo lililipuka miaka kadhaa nyuma katika jumba la daktari mmoja huko Keko na kumuumiza kijana wake Amata, lilitegwa na Mc Field, hivyo hakuona ajabu kukutana tena na jina hilo.

“Ndege mjanja hunasa katika tundu bovu,” akajisemea huku akilisukuma lile faili pembeni na kulivuta lingine nalo akalichambua kutazama ndani yake kuna nini, mauaji tata ya Khumalo mwaka mmoja na nusu uliopita, lakini faili hilo halikukamilika kwani hakukuwa na taarifa za kutosha kutoka Afrika Kusini kama sakata hilo lilipatiwa ufumbuazi au la. Chiba alimaliza kurasa ya mwisho kwa kuweka kiulizo na kishangao, na chini akaweka sentensi moja yenye maneno ‘Khumalo na wizi wa almasi Tanzania,’ Madam S akagonga gonga kidole chake kwenye faili hilo, hii ilionesha mwanamama huyu anahitaji kujua jambo katika kisa hicho. Alikuwa peke yake ofisini, wakati wengine wote wametawanyika, isipokuwa Dr. Jasmine ambaye daima alikuwa jirani sana na Madam S hii ilitokana pia na umri kumtupa mkono. Akainua mkono wake, akacheza na saa yake kisha akaongea maneno fulani, akatulia na kusubiri.


Simu ya Kamanda Amata ikaita kwa sauti ya chini, akaichomoa mfukoni, akajua tu kuwa ni simu ya kirafiki ambayo haina madhara yoyote.

Akaitoa na kutazama, akatabasamu, Jenny.

Kamanda Amata alikwisha msahau mrembo huyu kutokana na kubanwa na majukumu, alipoona jina hilo likirukaruka kwenye kioo cha simu yake moyo wake ukachanua kwa furaha kama ua la saa sita, akavuta kumbukumbu za msichana huyo, katibu muhtasi wa ofisi ya mkurugenzi wa Mgodi wa Mwadui ambaye sasa ni Marehemu, Mc Lean.

Akabonyeza kitufe cha kijani na kuiweka jirani naye sio sikioni.

“Za saa hizi bro,” sauti ya Jenny ikasikika ikiongea kwa chini kidogo kana kwamba anaogopa kufumaniwa.

“Nzuri, unaendeleaje?” Kamanda akamjibu.

“Niko poa, sasa sikiliza…”

Kamanda kichwa chake kikafunguka mara moja, mrembo huyu anataka kumwambia nini, “Nakusikia, niambie,” akamjibu.

“Kuna kitu nimekiokota hapa lakini sijui ni kitu gani, labda wewe unaweza kukitambua, nimekihifadhi,” akamwambia Kamanda.

“Kikoje?”

“Sijui nikielezeeje, ni kama kikadi fulani laini kina rangi ya kijani, hiki kitu sijawahi kukiona ofisini, nimekikuta chooni,” akaeleza. Kamanda Amata hakuona umaana sana lakini hata hivyo kutokana na kazi yake huwa hatakiwi kumpuuza hata kipepeo au dondola, kila kitu kwake huwa kina maana na kinahitaji kufanyiwa kazi.

“Ok, usikitupe, kifiche, nitakupigia na kukuelekeza cha kufanya,” Kamanda akajibu na kukata simu. Alijaribu kuvuta taswira kuwa ni kitu gani lakini hakupata jibu la haraka haraka. Akampa Chiba hiyo taarifa, Chiba akamsisitizia Amata kutopuuza hata unyoya wa kuku.

“Kaka fanya juu chini tukipate inawezekana ikawa ni moja ya vitu vitakavyotusaidia,” alimwambia. Kamanda Amata akainua simu na kumpigia Jenny.

“Kesho, hakikisha unafika Mwanza na kuchukua ndege ya mchana kuja Dar, usikiache hicho kikadi maana ninakihitaji kuliko wewe,”nakamwambia na kukata simu. Wakati huohuo saa yake ikamfinya kuashiria kuna ujumbe unaingia. Akaruhusu na kuuvuta nje mkanda mdogo wenye ujumbe huo.

…Wahi kabla pilau halijachacha…

Akacheka kwa luga hizo za Madam S. Akafungua mlango wa gari na kuuyaacha maegesho ya Uwanja wa Ndege, polepole akaondoka zake.


Ndani ya afisi ya mwanamama huyo, Kamanda Amata akatua faili alilokuwa akilisoma, akaliweka mezani na kumtazama Madam S, akatikisa kichwa.

“Mbona kazi hii inataka kututoa jasho? George Mc Field yupo hapa, tena katika sakata hili? Sasa nimeelewa, nimeelewa nini kinaendelea, tuna kazi nzito sana,” akasema huku akinyanyuka na kulielekea jokofu lililokuwa likibaridisha vinywaji.

“Achana na hilo, nataka uende Afrika Kusini nakupa masaa sita tu ya kufanya kazi pale na kurudi, hivyo siku 2 tu uwe hapa kuanzia sasa ninavyoongea,” Madam S akamwambia Amata.

“Madam, hili halijaisha linakuja lingine tena?” akauliza.

“Hapana, ni hilihili, nataka ukafanye uchunguzi juu ya mauaji ya Khumalo, mazingira ya kifo, muuaji ikiwezekana uje na picha ya muuaji kama aliwahi kuonekana au ni shetani, maana hata shetani picha yake ipo, nimemaliza, potea! Hilo ni moja ya kesi hizihizi, na mimi utanikuta hapahapa siondoki mpaka urudi,” akamaliza.

“Sawa Madam, nimekuelewa,” akajibu.

Ilikuwa ni safari ya dharula lakini ni moja kupata majibu ya mambo fulani fulani ambayo yangeweza kutoa mwelekeo wa sakata zima linalosumbua vichwa vya wanausalama hawa. Baada ya saa moja Kamanda Amata alikuwa angani kuelekea Durban Afrika ya Kusini, akiwa ndegeni kwenye chumba cha V.I.P alikuwa akifikiri wapi pa kuanzia.

Saa sita maana yake sihitaji kulala, aliwaza bila jibu.

UWANJA WA NDEGE WA KIMATAIFA

WA LUIS BOTHA-DURBAN S.A

‘Ukipita kwenye nyayo za mbwa utajua tu kaelekea wapi’ Kamanda Amata alikumbuka sentensi ya mwisho ya Madam S alipokuwa akiagana naye.

Nianzie wapi? Polisi, ofisini au nyumbani kwake? Alijiuliza na kukosa majibu. Akaitazama saa yake, ilikuwa ni saa tatu asubuhi, akateremka kutoka katika ndege hiyo, akakaribishwa na hali ya hewa ya upepo wa bahari. Kwa hatua za taratibu sana akajivuta kuelekea kwenye jengo la ukaguzi na moja kwa moja akaiendea kaunta na kukutana na mwanadada mmoja aliyekuwa hapo.

“Hauna mzigo wowote?” yule dada akauliza.

“Hapana, niko hivi unavyoniona,” Kamanda akajibu.

“Ok, karibu sana Durban Mr. James Ka..”

“..Kariuki, James Kariuki,” akamalizia Kamnada.

“Jisikie upo nyumbani,” yule mwanadada akamkaribisha.

“Asante.”

Saa nne na dakika tano ilimkuta mbele ya ghorofa la wastani, lililopambwa kwa maandishi mazuri yanayosomeka, KHUMALO TOWER, aliyatazama na kisha akavuta hatua na kuifikia kaunta ya mapokezi iliyokuwa na askari wanne wa kampuni binafsi ya ulinzi. Alipowaeleza kuwa anahitaji kufika katika ofisi za The Great Khumalo, akakaribishwa bila taabu. Akavuta hatua na kuchukua lifti akapanda mpaka ghorofa ya saba.

Mbele yake kulikuwa na meza kubwa ya kisasa ambayo ilitanguliwa na mwanamke mmoja wa miaka thekathini hadi thelathini na tano hivi, alionekana kuwa ndiye aliyechukua cheo cha Mkurugenzi wa kampuni hiyo. Haikumchukua muda Kamanda kujua kuwa binti huyo ana unasaba wa karibu na marehemu kwani mbele kabisa ya meza hiyo kulikuwa na kibao chenye maandishi ya dhahabu Ms. Lereti Khumalo M.D.

“Karibu sana, japokuwa sina miadi na wewe ila nitakusikiliza kwa kuwa umetoka mbali kama ulivyonieleza,” yule mwanadada alimwambia Amata mara baada ya kujitambulisha.

“Asante kwa ukarimu wako mrembo, naitwa Mr. James Kariuki, ni Mkenya ninayeishi Tanzania, nimekuja bila miadi lakini nina jambo muhimu la kibiashara la kuzungumza,” akajieleza, lakini akaona kamshtuko fulani kutoka kwa yule mwanadada.

“Biashara gani? Kama almasi za wizi hatununui,” Lereti akamkatisha.

“Ha! Umejuaje?” Kamanda akajifanya kushangaa.

“Najua, nina habari zote za juu ya huo wizi kupitia vyombo vya habari, lakini ninyi Watanzania mmekuwa mabwege sana hata mnaibiwa kijinga na waziri wenu! Mnakamata na kunyonga tu,” akaeleza, mara hii alioneka kutulia vizuri kitini, “haya niambie biashara hiyo!”

“Nataka almasi,” Kamanda akaanzia hapo.

“Unataka almasi?” yule binti akarudia hiyo sentensi kwa kuuliza.

“Ndiyo, almasi hii imepotea mwaka mmoja na nusu, na mi nimetumwa kuitafuta, nimeambiwa wewe utanisaidia,” wakacheka pamoja na kugongesha mikono yao.

“Eeeh, Lereti, samahani, ninahitaji kujua mambo fulani kutoka kwako kwani nimekuja kikazi zaidi,” akaeleza mara hii kwa utulivu.

Lereti akatega sikio.

“Nahitaji ikiwezekana tuwe wawili tu,” akamwambia. Lereti akakunja uso na kuukunjua.

“Ni ngumu sana, ongea hapa, kama haiwezekani basi haiwezekani kwani ufalagha daima nakuwa nao na mpenzi wangu tu, sina falagha nyingine mimi.”

“Nipe nafasi.”

Baada ya mvutano, Lereti akakubali lakini kwa masharti magumu sana.

“Itabidi uvumilie kwa sababu bado nina machungu na kifo cha baba yangu, naogopa falagha na watu nisiowajua,” akaeleza huku akisimama. Mara vijana wanne wakaingia, wakamkagua Kamanda wakachukua bastola zake mbili na vitu vyote vya hatari, wakaweka pembeni, wakamfunga pingu mikono yake kwa nyuma na miguu pia ili asiweze kufanya lolote la hatari. Akaingizwa katika chumba cha wastani chenye kitanda kimoja kidogo, akaketishwa hapo na wale jamaa wakaondoka, dakika chache akaingia Lereti, na kuketi mbele yake.

“Haya unasemaje? Dakika kumi tafadhali.”

“Lereti, pole sana kwa kifo cha baba yako lakini hongera kwa kuweza kuendeleza biashara na kampuni yake, huu ni urithi tosha kwenu,” Kamanda akazungumza, “hivi gawio lenu la hisa kutoka kwa Robinson Dia-Gold LTD mlichukua?” akauliza.

Lereti alimkazia macho Kamanda, “wewe ni nani mbona unataka kujua mambo ya ndani sana?” akauliza, “hatukuchukua kabisa na wala sitaki kusikia.”

“Ok, je unafikiri kifo cha baba yako kinahusiana na hili?” Kamanda akarusha swali. Lereti akabaki midomo wazi, hakuwahi kufikiri wala kuwaza juu ya mambo hayo mawili kuwa na uhusiano.

“Kiukweli sijui kama vina husiana ijapokuwa ni wiki ileile baba alitakiwa kwenda Canada ila ndo hivyo,” akajibu.

“Mlifanikiwa kumpata au kumgundua muuaji?”

“Hapana, hata polisi na wana usalama wameshindwa kumpata mpaka leo mpaka kesho,” akajibu. Kamanda akatikisa kichwa juu-chini.

“Unataka tuongee nini Mr. Kariuki?”

“Juu ya kifo cha baba yako,” akamjibu kwa mkato. Lereti alishtuka sana.

“We kama nani?” akauliza.

“Mpelelezi pekee duniani aliyepewa kazi ya kuchunguza kifo cha baba yako,” akajibu.

Lereti akajikuta kwenye dimbwi la sintofahamu, amwamini au hasimwamini? Kitendawili.

“Mpelelezi, ina maana wewe ni mwenyeji wa South Africa?” akauliza.

“No, mimi nimetoka Tanzania, kumbuka Tanzania na Afrika Kusini tuna urafiki wa enzi na enzi, sasa serikali ya Tanzania haikuona haja ya kufumbia macho mauaji ya baba yako ambaye ni mfanya biashara maarufu hakuna asiyemjua, nami nimetumwa, usione kimya, tupo kazini na nina saa nne tu nirudi kwetu ili uchunguzi zaidi uendelee, tumkamate muuaji,” Kamanda akaeleza.

Lereti akatabasamu baada ya habari hiyo, akabonya kitufe fulani na wale vijana wakaingia.

“Mfungueni, mpeni vitu vyake,” akawaambia, wakafanya hivyo. Amata akawa huru tena.

“Sasa labda twende polisi wakakueleze kiundani walipofikia au kuishia,” Lereti akamwambia Amata.

“Haina haja, niambie wapi baba yako alipouawa, hapo ndipo ninapopataka hasa,” Kamanda akamwambia, baada ya hapo yakafuatia mazungumzo kidogo na baadae wakatoka wote mpaka nje ya jengo hilo, binti huyu alikuwa akilindwa na watu watatu wenye silaha na walioekana ni wapiganaji haswa.

“Mr. Kariuki, familia yangu ina maadui wengi ndio maana unaona mazingira yako hivi, samahani kwakukuona na kukufanya kama mhalifu,” akamwambia.

“Usijali,” akamtuliza. Wakaingia garini na kuondoka.

Bila shida, akamtajia jina akampa na jina la gereza. Kamanda akaagana naye, akaondoka na kurudi kwenye gari, akamkuta Lereti akimsubiri.

“Vipi?” akauliza kwa shauku.

“Unamjua Mesobhuja Annie?” akauliza Kamanda.

“Ndiyo, amefungwa kuwa yeye ni muuaji,” akajibu.

“Nataka kumuona,”

“Yupo gerezani huwezi kumuona kiurahisi namna hiyo,” Lereti alijibu.
 
GEREZA KUU KWAZULU NATAL

BAADA YA ITIFAKI MBALIMBALI na kujitambulisha kwa uwazi kwa wakuu hao wa gereza, Kamanda Amata alipewa dakika nne tu kumuona mwanamke huyo.

“Nihakikishie nitatoka humu, nimechoka si mimi niliyeua,” akajieleza Mesobhuja.

“Ndiyo, ukinieleza ukweli, utaachiwa na ndiyo maana nipo hapa,” Kamanda akamfariji.

“Alikuwa mwanamke, sijui aliingiaje ndani ya kile chumba cha kutolea huduma, nilikuwa nammasage mteja wangu akiwa kalala kifudifudi, mara ghafla niliondolewa na mwanamke huyo, Mzungu mwenye nywele ndefu, sikumjua, akanipa ishara ya kutulia kimya, nikaogopa sana, alifanya mauaji ya haraka kwa kumvunja uti wa mgongo, yule alikuwa ni muuaji by professional. Kisha aliwaita walinzi kuwa kuna shida. Nao akawaua kwa kuwagonganisha vichwa vyao kwa nguvu, kisha akaondoka. Basi! Nimejitetea sana kuwa si mimi muuaji lakini wapi, nimefungwa hapa kifungo cha maisha, nisaidie jamani, unihurumie dada, sikumuua baba yako.”

Maneno hayo toka kwa Mesobhuja yalimtoa machoa Lereti.

“Niambie, unakumbuka alivaaje mwanamke huyo?” Kamanda Amata akamwuliza.

“Ndiyo, alivaa suruali bluu angavu, brauzi nyeusi, na kikoti chenye rangi kama ya suruali yake, nywele alizifunga nyuma kwa kutumia mpira, alikuwa na miwani nyeusi, na alipovua mara moja kuniangalia, macho yake yanatisha kwa jinsi alivyojiweka make up,” akajibu.

“Unakumbuka muda? Hata kwa kuhisi,”

“Ilikuwa ni kati ya saa tatu narobo asubuhi na saa nne hivi,”

“Ok, asante, usijali tunalifanyia kazi,” Kamanda Amata akamwambia na kisha wakatoka.

Lerethi na Kamanda Amata wakatoka na kuwashukuru viongozi wa gereza hilo, akamwamuru dereva amrudishe katika jengo la Monte Blanc.

“Huko kuna nini?” Lereti aliuliza.

“Naenda kumalizia kazi, kisha naondoka zangu,” akajibu.

Walifika na kuingia tena, kama kawaida watu walikuwa wakimtazama sana mwanadada huyo kwa jinsi alivyo na umbo la kibantu, aliyependeza kwenye suti yake nadhifu kabisa, akizunguka na walinzi huku na huku.

“Mtoto wa Khumalo,” sauti zenye maneno au minong’ono kama hiyo zilisikika kwa waliosimama.

Kamanda Amata kwa utundu wake alifanikiwa kufika katika chumba kinachohifadhi kumbukumbu zote za usalama za jengo hilo, kulikuwa na kijana mmoja anayefanya kazi ndani yake. Alimsikiliza Kamanda Amata shida yake na baada ya kuoneshwa kitambulisho halisi cha Kamanda kinachomueleza kama Mpelelezi namba moja Tanzania na Afrika alikuwa haishi kutetemeka. Akavuta droo na kuchomoa disc moja akakiendea chombo maaluma na kuitumbukiza, kisha akawa anaangalia matukiao ya siku hiyo.

Akarudisha picha zile za CCTV mpaka picha ya mwaka mmoja na nusu uliopita, tarehe ile aliyouawa Khumalo, 16 Julai akairudisha mpaka saa 3:15 asubuhi na kutazma matokeo. Kama alivyotarajia, picha ya saa 3:47 ilimuonesha muuaji wa Khumalo, alivaa vilevile kama alivyoelekezwa na Mesobhuja, akarekodi kipande hicho na kisha kuondoka nacho, akamwachia randi 100 kijana huyo kisha akapotea.


Katika Uwanja wa Ndege wa Louis Botha, Kamanda Amata alikuwa akiagana na Lereti Khumalo. Binti huyu alishindwa kujizuia akamkumbatia kijana huyu shababi.

“Asante Kariuki, kwa saa hizi chache nimefurahi kuwa nawe, nakutakia kila lakheri ufanikiwe kumkamata huyo hayawani, na ukifanikiwa nitakupa zaidi nzuri sana ambayo sijawahi mpa yeyote duniani, unijulishe,” akamwambia Amata huku chozi likimtoka, “you are so Intelligency person,” akamalizia.

Lereti hakutaka kumwachia Kamanda, alibaki kumkumbatia huku chozi lake likitua kwenye koti la suti ya kijana huyo.

“Nahitaji kwenda,” akamwambia Lereti huku akiitazama saa yake kutokea mgongoni mwa mwanadada huyo, ilikuwa zimetimia saa tano. Kumbe nimeweza, akawaza. Lereti akamuachia kamanda, “ni muda mfupi lakini nahisi moyo wangu umekuamini sana kwa kila kitu,” Lereti akaeleza ya moyoni.

“Usihofu ni kawaida,” Kamanda akajibu huku akimpa kadi biashara kwa ajili ya mawasiliano, na Lereti akafanya vivyo hivyo.

Daima huwa ni vigumu sana kwa Kamanda Amata au mtu yeyote mwenye kazi kama yake kujitambulisha waziwazi ijapokuwa alichokifanya yeye ni kujitambulisha wazi lakini bado kwa kujificha, alijikuta anaukonga moyo wa mwanadada huyu mrembo mtoto wa Marehemu Gervas Khumalo, binti pekee katika familia lakini aliyeaminiwa sana na wazazi wake kuliko hata kaka zake watatu waliomtangulia. Alikuwa msomi anayejua maswala ya utawala mwenye Shahada ya Uzamivu katika nyanja hiyo, aliogopwa na wasomi kwa kuwa alikuwa ‘ngangari’ katika kutetea hoja au kitu, alikuwa na uwezo mkubwa wa kugeuza uongo kuwa ukweli na ukweli kuwa uongo. Wanaume walimdondoshea mate ya tamaa na uchu lakini hawakuwa na nafasi hata chembe ya kusema lolote, waliishia kula kwa macho. Kila mtu, hata walinzi wake walimshangaa pale uwanja wa ndege kumkumbatia mwanaume, tena aliyemuona kwa mara ya kwanza tu, asiyemjua kwa undani, ama kweli ‘Mapenzi yamerogwa’ aliandika mwandishi mmoja mashuhuri nchini Tanzania, Hussein Wamaywa.

07

IKULU – DAR ES SALAAM

MHESHIMIWA RAIS, HAKUAMINI KILE anachokiona mezani pake. Alikuwa katika ofisi yake ya siri kabisa, Kilimanjaro Square. Ofisi ambayo hata katibu wake hakuwahi kuingia na funguo zake daima alijua yeye anaziweka wapi. Akatikisa kichwa, akauma meno kwa hasira. Kabrasha moja lenye jalada jekundu lilikuwa mkononi mwake likibeba maandishi makubwa ya rangi ya dhahabu ‘The Order Of Being a President’, ndani yake mlikuwa na makubaliano au mkataba kati yake na wale waliokubali kumuweka madarakani kwa makubaliano maalumu. Kwa kuwa alishaambiwa kuwa nusu ya utawala wake akabidhi migodi yote mikubwa kwa maswahiba hao au tuwaite wahisani na wafadhili kwa lugha tuliyoizoea alijikuta hana la kufanya baada ya kugundua kuwa kipindi cha utawala kinamtupa mkono.

Kumbe miaka mitano si mingi, aliwaza huku akikuna kichwa chake ilhali hakikuwa kikiwasha.

Mshtuko mkubwa ulimfika pale alipokutana na sentensi finyu chini ya ukurasa wa mwisho kuwa, hatuwezi kufika kurasa ya mwisho bila kutekeleza kurasa inayoitangulia, moyo ulimpasuka, midomo ikamcheza, akashika pini ya dhahabu na kuifungua kurasa iliyobanwa barabara ambayo hakutakiwa kuifungua kabla. Kurasa yenye pini za dhahabu.

Utakuwa umetugeuka kwa kukiuka makubaliano yetu

Tutachukua madini na na mali nyingine kwa nguvu ili kurudisha gharama ulizotuingiza wakati wa kukupeleka Ikulu.

Tutachukua madini kwa jinsi tunayojua sisi, na hata ukijua kuwa ni sisi basi pia ujue kuwa umechelewa, usifanye lolote, bali utulie katika kiti chako, legeza ulinzi ili tufanikishe.

Kumbuka mkataba wetu, faida yetu lazima irudi mara tatu ya pesa tuliyowekeza.

Mwisho wa mkataba wetu ni huu, ukifungua kurasa hizi, ukazikaidi, tunaondoka na Roho yako

Kumbuka tupo kila mahali, mpaka kwenye kiti ulichokalia

Marafiki zako tunaokupenda sana.

Akashusha pumzi ndefu, mikono ilikuwa ikimtetemeka.

Nimekwisha, kwa nini nilijiingiza huku? Akawaza na kuwazua, hakuna jibu.

Tama mbaya, tena mbaya sana, Mh. Rais alijikuta katika hali ngumu, mwili ulilowa jasho wakati ofisi hiyo ilijazwa kwa baridi la mashine ya kupoza hewa.

Akajiuliza mengi, akagundua migogoro mingi na vita vya wenyewe kwa wenyewe katika nchi mbalimbali hasa nchi za dunia ya tatu ni inaweza kuwa ni ‘matekelezo ya mikataba’. Akaikumbuka Nigeria, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Mali, Afrika ya Kati, Somalia na nchi mbalimbali za Kiafrika zilizoingia kwenye migogoro mizito, akakumbuka marais waliouawa wakiwa nyadhifani, wakiwa bado wanakula maisha ya ufalme wao. Akajikuta akili yake ikitengana na ubongo.

Migogoro mingi katikla nchi zinazoendelea inasababishwa na mabwanyenye kutoka mataifa beberu ya nchi za dunia ya kwanza, ambazo zinapanga nani atatawala pale na nani kule ili wao wapenyeze fikra na tawala zao dhalimu. Bara la Afrika ni bara lililoathirika sana na Siasa za mtindo huu. Vita vilitawala kila kona, hakuna aliyejua amani, kila mtu alijijengea mazingira ya kujilinda yeye na familia yake, vikundi vya kigaidi viliiibuka kila wakati na kila mahali, jiuliuze vinapigania nini kwa maslahi ya nani, hata wapiganaji wenyewe hawajui na hawana jibu.

Kila kukicha, kule kumelipuliwa, 500 wametekwa, 200 wameuawa. Vyombo vya habari vya mataifa makubwa vinawekeza katika nchi masikini kutengeneza habari mbaya za Afrika, wanazisababisha wao na wanazitengeneza wao, wanaieleza historia mbaya ya bara letu. Sisi wenye bara letu hatukumbuki hata kutangaza historia nzuri na ya kupendeza ya Afrika na kubadili fikra za ulimwengu huu, kwa kuwa tunafanya kila kitu chini yao, basi hata habari za Afrika tunanakili kutoka katika vyombo vyao wenyewe. Hao ndio ‘King Makers’, nipe madini nikupe Bunduki, Jiue mwenyewe.

“No! Nooooooooooo!!!!” alipiga kelele bila kujijua akiwa katika ofisi ile, na hakuna aliyesikia kutoka nje, akaanza kuhema kwa nguvu, ofisi ile aliiona ndogo kama kiberiti, alihisi hatoshi.

Wataniua, akawaza. Aibu, akajijibu.

Haiwezekani, nina Askari Polisi watalinda migodi, nina Jeshi la Wananchi watapambana na udhalimu wowote dhidi ya nchi yangu, nina Askari Magereza watawafunga wote watakaoleta shida dhidi ya utawala wangu awe mweusi au mweupe, nina watu wakakamavu wa Usalama wa Taifa watanilinda kila ninakokwenda hakuna risasi itakayokifikia kichwa change. Hawaniwezi, hawaniwezi kabisa. hapa nitamuweka yule, mgongoni kwangu atakaa yule kule, nitaongeza body guards kutoka wanne wa sasa watakuwa nane wa karibu, na kumi na sita watakaotawanyika, nitabadilisha gari la kutembelea, nitaagiza jipya, la kisasa lisilopenya risasi wala kulipuka kwa moto. Ah! Lakini wanaotengeneza gari si ni wao wenyewe, sasa nifanyeje, simwamini mtu, kama waziri katumiwa kuonekana kaiba almasi kumbe ni wao wenyewe waliojigeuza katika maumbo na sura, hawa ni hatari, nifanyeje, nisitoke ndani. Sasa nikialikwa kwenye shughuli za hadhara, itakuwaje, watanidungua.

Aaaaaa, ok sasa nakumbuka, walinidungua pale Bunju, lo! Hawakuniua, hawakushindwa kufanya hivyo, kwa nini nimechelewa kujua hili? Nani alitekeleza anayeweza kuupenya usalama wa nchi yangu uliotukuka ndani na nje, atakuwa mtaalam sana huyo, dereva wangu naye ni mwanajeshi, mpiganaji anayejuwa kuendesha gari katika ‘Defensive Driving’, ilikuwaje hakuona kama tunadunguliwa?

Yote yalikuwa ni mawazo, akiwa anatazama saa aliyokuwa akiiona mishale yake ikikimbia kuliko kawaida, akiwa amelowa jasho kuliko, Mheshimiwa Rais alichanganyikiwa, yote yalikuja kwa mara moja. Aliona saa 24 za siku hazotoshi labda mchana uwe na saa 72, miezi kumi na mbili ya mwaka michache sana, labda ingekuwa ishirini hivi. Akajiegemeza kitini, akashusha pumzi, mwanga wa taa ulimpiga machoni, akayafinya.style='font-size:7.5pt'>
Alihisi kuetetemeka mwili mzima, akafungua tai na kuitupa huko, akalegeza vifungo vya koti na shati lake apate hewa ingawaje mashine ya kupoza hewa ilikuwa ikiunguruma kwa nguvu zote.

Akafunga lile kabrasha, akalitia kwenye droo, akafunga kwa namba anazojua yeye.


Katika ofisi za wanausalama ndani ya jengo la Ikulu, mlio wa hatari ulisikika, Johnson Cheka, mwanausalama mwenye amri ya mwisho ya kusema Rais afanye hivi au asifanye alikuwa wa kwanza kutoka na kupiga hatua kumi na tano kufika pale kwenye mlango wa kuingia katika makazi ya Rais ambayo yapo ndani ya Ikulu, akafungua mlango na kuingia haraka, akaufikia mlango wa ofisi hiyo ndogo, akautikisa, umefungwa, akajaribu kuufungua umefungwa, akachomoa funguo zake za ajabu na kufanikiwa kuufungua, akamkuta rais amejilaza mezani akivujwa jasho jingi. Mara moja akamsogelea na kumwinua, kwa taabu kidogo akamfikisha kwenye kochi kubwa sebuleni, akainua redio yake na kumwita daktari huku yeye akiifuna afisi ile. Dakika moja tu daktari akafika, mara moja na kumchukua mpaka ghorofa ya chini ambako kuna hospitali ndogo yenye kila kitu iliyojengwa maalumu kwa familia ya Rais.

Johnson Cheka alisimama pembeni mwa kitanda akitazama pilikapilika za daktari na muuguzi wake. Dakika tano baade hali ikatulia. Cheka akamwita Mkuu wa itifaki akamweleza kubadili ratiba zote za Rais kwa siku tatu, hakutakiwa kuonana na mtu yeyote, alitakiwa kupumzika. Ilileta mshtuko kwa kila aliyejua, lakini bado ilikuwa ni siri kubwa sana.

Madam S alipata taarifa ya hali ya Rais, hakuweza kuchelewa, siku hiyohiyo alifika Ikulu kumjulia hali Mkuu wa Nchi kwa namna moja, bosi wake. Yeye haina tabu kufika anapotaka, alikaribishwa na kuongozwa mpaka aliko mkuu huyo. Mara baada ya kuwasili, Rais akatabasamu kumwona, akawataka wengine kutoka nje ili abaki kwa muda na mwanamama huyo.

“Nahitaji kufuma upya kikosi cha ulinzi,” ilikuwa ni kauli ambayo ilipenya masikioni mwa Madam S.

“Kwa nini,” Madam akauliza.

“Hali ya kiusalama ni mbaya, kwangu na kwa nchi,” akamweleza.

“Najua, sasa wataka kufanya nini?” Madam akauliza kwa kuwa alijua wazi kuwa kubadilisha au kuimarisha kikosi cha ulinzi cha Rais au kuwa na wasiwasi na walinzi wake tayari kuna jambo na jambo lenyewe kubwa si dogo.

“Nitakwambia, maana nikishaweka mambo sawa, wewe utahusika kujua,” akamwambia Madam S.

Kamanda amata aliwasilisha ripoti yake kwa Madam S na jopo zima la TSA juu ya mauaji na muuaji wa Mr. Gervas Khumalo.

“Sasa tuna nini lingine la kutafuta?,” Madam aliuliza, kisha akaongeza, “ huyu mwanamke, ndiye huyu tuliletewa picha kutoka Ufaransa, ndiye huyu tulicholewa picha na mchoraji wetu baada ya sakata la msafara wa rais, hizi hapa zinafanana kabisa, ni nani mwanamke huyu? Yuko wapi na anataka nini? Hilo ndilo la msingi sasa kuona, siwezi kusema akamatwe au aachwe, kwanza huyu ni nani?” Madam S akang’aka, alionekana wazi kuwa na hasira siku hiyo. Ukimya ukachukua nafasi yake, hakuna hata aliyekohoa. Kisha akaendelea kuleta utata mwingine.

“Sikilizeni, tena sikilieni kwa makini sana, rais anataka kufumua kikosi cha usalama na kukipanga upya, mimi nimemhoji sana kwa nini akanipa siri ifuatayo, siku msafara wake ulipodunguliwa, amegundua uzembe wa hali ya juu sana kiasi kwamba sasa anataka hata dereva wake achunguzwe…”

Kamanda akamkatisha, “sasa atafumua wapi ataacha wapi…?”

“Mi sijui, lakini yeye atakapokutana na mkurugenzi wa Usalama wa Taifa watajua,” akajibu.

“Inabidi kweli dereva achunguzwe, vipi kama hakuwa dereva tunayemjua? Chiba akauliza.

“Ndiyo utata, maana waziri walimtengeneza watashindwaje dereva, hakuna haja ya kupoteza muda, dereva inabidi afanyiwe uchunguzi haraka,” Madam akaongeza na kumpa kazi hiyo Scoba aitekeleze haraka iwezekanavyo.

ITAENDELEA
 
ONTARIO CANADA

ROBINSON QUEBEC alikuwa kimya katika bustani yake kubwa iliyoizunguka nyumba yake kati jiji la Ontario nchini Canada, sura yake ilikuwa imekunjana kwa hasira. Akashusha sigara yake anayovuta na kukung’uta jivu lake katika kibweta kilichoandaliwa kwa kazi hiyo, kisha akamtazama aliyekuwa mbele yake.

“Tracy!” akaita.

“Yes, Boss!”

“Nilikuwa nikikuandaa kwa miaka yote kwa kazi ngumu na za hatari kama hizi, na zote umenifanyia vizuri kabisa zikapelekea hata ukapata kazi na mashirika makubwa kama KGB na wengine, sasa nataka nikupe kazi moja, hii naweza kuiita ngumu lakini wewe utaipima,” Robinson alimwambia Tracy Tasha aliyekuwa ameketi pembeni yake akisikiliza kwa utulivu sana kila kitu.

“Nakusikiliza,” alisema.

“Nakutuma tena Afrika Mashariki,” Bwana Robinson akatulia akimwangalia Tracy usoni.

“Kazi ileile au?” Tracy akauliza.

“Ndiyo, sasa ukaimalizie,” akavuta tena pafu moja, “mara hii nataka ukaondoe Roho ya rais wa Tanzania, kwani amekiuka makubalino yetu, nasi hatuna budi kutekeleza mkataba wetu,” akarudisha sigara kinywani, “sikia, iwe kwa sumu, kwa ajali au njia yoyote ile wewe ndiye ujuaye la kufanya, hakikisha ndani ya siku chache tu uwe umemaliza kazi na hapo watakaposhtuka juu ya kifo hicho ndipo tutapita nyuma kukusanya tunachotaka,” akamaliza.

“Ok, na vipi juu ya usalama wake? Yaani vikwazo vya kiusalama,” Tracy akauliza.

“Hivi kuna nchi ya Kiafrika ambayo ina usalama wa kukushinda wewe? Tanzania! Ah wapi, wala usiogope, hawana lolote ni kelele za ubahatishaji tu mbona mpaka leo hawajagundua kuwa dereva aliyemwendesha Rais siku ya tukio lililopita alikuwa Breyman?” Robinson akamwuliza Tracy.

“Ok, kesho nitaondoka,” akajibu.

“Sawa, uwende Kesho na ukafanye kazi kikamilifu, George Mc Field yuko pale kukusaidia kwa lolote, usihofu tumejipanga,” Robinson akamweleza.

“Sawa, hilo limepita,” Tarcy akanyanyuka na kubaki wima. Ni mwanamke mzuri kuwa mpenzi au mke wa mtu lakini dunia imembadili kimaisha amekuwa mnyama mbaya kuliko mnyama mwenyewe.

“Sikia Tracy, ulinzi wa Rais umebadilishwa saa chache zilizopita, nimepata hiyo taarifa kutoka vyanzo vyangu. Ameongeza watu wanaomzunguka na kuimarisha maeneo nyeti, hivyo nahitaji utumie weledi wako wa juu kabisa kuifanya kazi hiyo. Ukikamilisha, utajiri wako utaongezeka mara nne,” Robinson akamaliza huku akimshika makalio mwanadada huyo katili, alisahau kabisa kama anaweza kumgeuka na kumtoa roho.

UWANJA WA NDEGE WA

J.K NYERERE-DAR ES SALAAM

NDEGE KUBWA YA LUFTHANSA ilitua katika ardhi ya Dar es salaam, Rubani wa ndege hiyo na wasaidizi wake hawakujua kabisa kuwa wameiletea Tanzania maafa, maafa makubwa.

Tracy Tasha alikuwa wa mwisho kushuka katika ndege hiyo kubwa ya kisasa, hakuwa mgeni na nchi hii, kwa kuwa alishafika mara moja na hii ilikuwa ni mara ya pili. Alikuwa na kijibegi kidogo na mkoba mkononi mwake, akapita eneo la ukaguzi wa hati za usafiri bila tabu akitambulika kwa jina la Naomi Schubety, raia wa Venezuela, mwanafunzi wa chuo kimoja cha afya huko Marekani, John Hopkins.

“Karibu sana!” George Mc Field alimlaki mwanamke huyu, hawakuwahi kukutana, ilikuwa ni mara ya kwanza, Tracy akabaki kimya akimwangalia mtu huyu ambaye sasa alionekana katika mavazi nadhifu, mwenye mwenye ndevu nyingi.

Tracy akatoa noti ya Paundi 100 akamwonesha, na Mc Field akatoa noti ya Shilingi 10000 akamwonesha, hiyo ilikuwa ni ishara ya utambulisho wao ambayo kila mmoja aliambiwa kwa wakati wake. Wakaingia garini na kuondoka kuelekea mjini.

“Umekuja kufanya kazi, siyo?” Mc Field akamwuliza Tracy.

“Ndiyo, ni hilo tu,” akajibu.

“Unapenda kufikia hoteli gani?”

“Aaa yoyote lakini nafikiri ya hali ya kati ingenifaa zaidi,” Tracy akaeleza.

“Ok,” Mc Field akaiacha barabara ya Nyerere na kuichukua ile ya Mandela kuelekea Ubungo.

“Land Mark Hotel, hapa patakufaa siyo?” akamwuliza.

“Yap, pako poa,” akajibu hukua akishuka katika gari. Akaagana na Mc Field kwa miadi ya kuonana usiku wa siku hiyo kwa mipango ya mwisho.

08

CANADA

ROBINSON QUEBEC alikutana na washirika wake kama kawaida, hii ilikuwa mara tu baada ya kuondoka Tracy kuelekea Tanzania.style='font-size:7.5pt'>
“Tumemaliza kazi! Tusubiri matokeo,” Robinson akawaeleza swahiba zake wawili.

“Safi sana, kama Tracy amekwenda, hilo ni amuzi sahihi, mwanamke yule huwa hashindiwi, na wala haogopi kitu, kuua ni starehe yake,” akajibu yule mjumbe mweusi.

“Ndiyo, na wameshakutana na Mc Field, kila kitu kiko sawa, tusihesabu hasara basi tuhesabu faida katika hili,” Robinson akaeleza.

“Sir. Robinson Quebec, uishi milele!” wakamtukuza. Baada ya hapo wakatawanyika wakisubiri kazi ya Tracy ikamilike ili nao wasonge mbele.


REJEA – SHAMBA

“Sasa ipo hivi, almasi za Mwadui hazikuibwa na waziri kama ilivyojulikana mwanzo,” Madam S alikuwa akifanya hitimisho la uchunguzi wa taasisi hiyo, akaendelea “sasa ni nani aliyeiba almasi hizo? Mpaka sasa tuna mtu huyu George Mc Field na nina uhakika hajaondoka nchini, na yeye atakuwa ndiye aliyejigeuza kuwa kama waziri, Amata anamjua huyu jamaa, huyu ni Jasusi mwenye uwezo wa kujigeuza hata akawa mjusi,” akatulia na kuwatazama vijana wake, “sasa tunaingia kazini, asakwe George Mc Field apatikane akiwa anapumua au hapumui, na swahiba zake, wakati huo ufanyike uchunguzi juu ya chanzo cha wizi wa almasi hizi, sote tunaingia kazini, na tutajipanga kama ifuatavyo…”

Kila mtu alibaki kimya, kila mmoja moyoni mwake aliona wazi kuwa haya ni maji mazito mpaka Madam S anahusisha watu wake wote kikazi kwa wakati mmoja, haikuwa kawaida kwa mwanamama huyo, yeye daima alimpa mtu mmoja kazi moja labda itokee inahitaji msaada wa karibu ndipo mngekuwa wawili, hata hivyo bado aligawa kazi pasi na wao kujua kama nani ana kazi ipi. Lakini mara hii wote watano na yeye mwenyewe wa sita, kila mmoja aliona kazi ni kubwa na nzito. Baada ya kushusha bilauri yake iliyojaa sharubati ya embe akafungua kabrasha lake na kuliacha wazi mezani.

“Hali ya Mheshimiwa Rais ni mbaya, amepatwa na presha ya kushuka, sasa dawa yake tunayo sisi kuhakikisha utatuzi wa hili umepatikana, nimeongea naye kasema mabadiliko aliyoyazungumza kayakamilisha katika sekta ya ulinzi wa nchi hivyo msishangae. Sasa nataka tufanye kazi hii kwa kasi ya ajabu kidogo. Kamanda Amata utakuwa mstari wa mbele kabisa ukisaidiwa karibu na Gina katika mapambano, kila anayenukia harufu ya almasi za wizi, awe mkubwa awe mdogo, toa taarifa tumkamate mara moja, na atakayekataa kutii sheria bila shuruti basi we unajua jinsi ya kumtuliza. Scoba kama kawaida, utakuwa makini katika kuokoa na kukamata anayetakiwa kufanyiwa hivyo. Chiba utahakikisha unawaunganisha wote bila kuwapoteza katika mtandao, kunasa mawasiliano ya kila unayemhisi na kuto mwongozo kwao, nikiwa na maana kuwa ofisi yako sasa itaamia hapa au ndani ya gari yako maalumu kwa kazi hiyo wakati mimi na Jasmine tutakuwa hapa kwa msaada wa haraka…” akiwa hajammializa kusema hayo, mara sauti ya simu ya Chiba ikawashtua, akaitoa mfukoni na kuitazama, akawapa ishara ya kutulia.

“Terminal Two,” akawaambia na wote wakatega sikio kwa kuwa aliweka sauti kubwa.

“…Hello…” akaita

“Hello, Terminal Two hapa…”

“Nakusoma, endelea,”

“Kuna mzigo hapa umeingia, nina wasiwasi nao kwa picha ulizonipatia…”

“Ok tuma taarifa zote hapa haraka…” akamwamuru mtu huyo ambaye daima humtumia kunasa watu anaowahitaji. Mtu huyu ana kifuniko ‘undercover’ cha Idara ya Uhamiaji lakini kitengo cha usalama wa Taifa kinachofanya maswala ya utambuzi.

“Copy!”

Chiba akakata simu na kutulia.

“Kumekucha…. Kwa umakini wa huyu kijana lazima aliyeingia ana jambo,” Chiba akasema.

Wakati wakiendelea na mzungumzo, kompyuta ya Chiba ilikuwa imekwishapokea taarifa kutoka uwanja wa ndege, akazifungua na kuprint nakala kadhaa na picha zilizotumwa pamoja nazo.

Picha kumi na mbili za mnato zilizomuonesha mwanamke katika ‘engo’ mbalimbali, mbele nyuma, kutoka juu, usoni kwa karibu kifuani, mgongoni na mazingira mengine, kisha kulikuwa na picha ya mjongeo ambayo Chiba aliicheza kwenye kompyuta kubwa ya ofisini kwa Madam S na wote wakaishuhudia. Mwanamke huyo akipita katika ukaguzi, akitoka mlango wa ‘wanaowasili’ akisalimiana na mwenyeji wake, kisha wakiondoka lakini picha hiyo haikuweza kuonesha mtu huyo kaondoka na gari gani.

Kamanda Amata akazitazama zile picha kisha akampatia Chiba. Chiba akaziweka kwenye kifaa chake. Pamoja na zile ambazo Kamanda alizileta kutoka Afrika Kusini, na zile zilizotoka Ufaransa na zilizochorwa katika tukio la Bunju, kisha kwa kutumia kompyuta, softiwea maalumu akazioanisha ‘crossmatching’ kama ni mtu mmoja au ni watu tofauti. Ndani ya dakika kumi walipata jibu alikuwa ni mtu mmoja hata kama alijibadili namna gani. Softiwea hii iliyotengenezwa na Chiba akishirikiana na wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es salaam ilikuwa ikifanya kazi kwa ufanisi wa hali ya juu sana, ikikufananisha pua, macho au maziwa kama we ni mwanamke au ndevu kama we ni mwanaume kwa kuwa waliiaminisha kuwa hata mtu ajibadili vipi kuna sehemu hatoweza kujibadili, hivyo ilitafuta sehemu ambayo ilikuwa na unasaba kisha ikaoanisha kutoka hapo.

Baada ya kupata picha kamili ya mwanmke huyo, akaiingiza katika mtandao wa usalama unaowatambua watu hatari duniani, kwanza alianza na ule wa CIA ambao ulimpa jibu lenye utata, akaingiza kwenye mtandao wa MOSSAD kama unamtambua mtu huyo nao ukaleta majibu kama yale yale baada ya kupitisha kwenye kioo picha zaidi ya 250.

“Shiit!” Kamanda Akang’aka.

Mtandao mwingine wa kijasusi wa KGB nao ukaleta majibu yanayofanana.

Tracy Tasha, raia wa Marekani, mzaliwa wa Jimbo la Arizona, mwenye miaka thelathini na moja, maelezo yaliendelea kumweleza kama muuaji hatari asiyekamatika, anayetafutwa kila kona ya dunia na kila kitengo kiwe cha kipolisi, kijasusi au mashirika binafsi. Ulimweleza kuwa hakamatiki, mitandao mingine ikampa jina la The Devil, wengi walieleza wazi kuwa wamekamata nyayo zake tu lakini mwenyewe hawakumkamata. Mtandao mwingine uliwafanya Madam S na jopo lake kucheka maana ulijitamba kuwa kamera zake za CCTV ndizo zenye uwezo wa kumkamata kila apitapo eneo fulani.

Taarifa zile zilimfanya Madam kushusha pumzi ndefu, akavua miwani yake na kujifikicha jicho la kushoto.

“Tutoe taarifa kwa wadau wanaomtafuta? Maana sisi huyu sio wa kwetu,” Madam S akauliza.

“Hapana, usitoe taarifa kabisa, kwani itakuwa vurugu kubwa hapa, na sisi lazima tumchunguze kwanza kaja kufanya nini, kisha tumuoneshe kuwa sasa kafika mwisho wa maisha yake…” kabla Kamanda hajamaliza kusema hayo Gina akadakia.

“Ningemshauri aandike urithi kama ana watoto,” wote wakacheka.

Waliona baadae kuwa Mwanamke huyo na kama kuna wengine wasakwe kimyakimya bila kelele ili kutowagutusha, hali ya tahadhari ikatolewa kwa watu wa idara ya Usalama wa Taifa kuwa makini na kila wanayekuwa na wasiwasi naye, ulinzi mpya ukaanza kazi mara moja, safu zikapangwa upya, mkuu wa kitengo kile akaondolewa akawekwa mwingine, akatolewa huyu kule akapelekwa kule, huyu na yule wakapelekwa mikoani, yule wa mkoa ule akaletwa huku ilimradi tu kuiweka safu mpya.


Kamanda Amata alikuwa na Chiba wakijadili hili na lile, “enhe nambie Jenny anasemaje?” akauliza.

“Oh, nilisahau, alileta kitu muhimu sana, alileta kadi inayotumiwa kubadili sauti ya mtu, na tumeichunguza ndipo tukapitisha moja kwa moja kwamba waziri hakuusika na ule wizi kwani alibanwa akalazimisha kusema maneno fulani wakati ile kadi ikirekodi na kisha aliyejifanya waziri ndiye akaitumia sauti hiyo,” Chiba akaeleza.

“Lazima tujivunie kuwa na wewe Chiba, ni mtu wa juu sana kwenye hii midude unajua wewe ndiyo huwa unanifanyia mi mambo kuwa mepesi,” wakacheka pamoja.

“Acha Bwana, sasa unataka kumwona Jenny?” Chiba akaanza.

“Mmmm hajaondoka?”

“Hapana, nilimwambia asiondoke mpaka utakaporudi, nimempangia chumba pale Rombo Green View, Sinza, naye amefurahi sana kusikia aonane nawe,” Chiba akaeleza.

“Aaa, wakati mbaya sana huu, unaweza kuwa kitandani na wenzako wanaiangamiza nchi,” Kamnda akajibu.

“Aaaa kaka! Kamanda leo wa kusema hivi! Hivi hivi! Siamini itakuwa umeokoka labda,” Chiba akatania.

JINIA – saa 3:25 asubuhi.

KAMANDA Amata alikuwa katika ofisi ya uhamiaji ndani ya Uwanja wa Ndege wa Dar es salaam sambasamba na Gina.

“Unasema ulimwona,” akauliza.

“Ndiyo nilimwona, akapokelewa na kasisi wa kanisa,” akajibu kijana wa uhamiaji aliyetuma taarifa za Tracy kwa Chiba.

Kasisi wa kanisa, akawaza Kamanda, “haya makanisa nayo yana mambo! Utakuta wanahifadhi majasusi humu humu si’ tumekaa tu,” akaeleza Kamanda, “hukuwaona hata wamepanda taksi gani au gari gani?” akauliza.

“Waliondoka na gari binafsi, Peugeot 404, TX 768 M,” akajibu yule kijana.

“Ok. Asante sana, nitafanyia kazi, tujue kaja hapa kwa nini,”

Kamanda na Gina walitoka eneo la Uwanja wa Ndege na kuliendea gari lao, wakaingia na kuketi, nyuma ya usukani alikuwa Gina. Kamanda akawasha simu na kupiga mamlaka ya mapato Tanzania na kuuliza namba za gari hilo TX 768 M ni mali ya nani. Baada ya dakika kumi hivi akapewa jibu kuwa ni mali ya kampuni moja ya kijerumani inayofanya kazi za kijamii huko vijijini, lakini ofisi yao ipo Dar es salaam, wakatajiwa anwani na mahali ilipo.

“Gina, twende Mtaa wa Mkwepu, plot namba 45C, “ Kamanda akamwamuru na Gina akaondoa gari kama alivyoelekezwa.

Walipofika walipandisha ngazi moja kwa moja mpaka ghorofa ya tatu ya jengo hilo, wakakuta kuna duka kubwa la kuuza vifaa vya maofisini, walipouliza wakaambiwa hao Wajerumani waliamisha ofisi kuelekea mtaa wa Ali Khan Upanga. Bila kusita Gina na Kamanda wakaongoza njia kuelekea huko, haikuwa tabu kuipata ofisi hiyo kwani walipopita tu shule ya Zanaki wakaiona kwa mbele wakaegesha gari, wakateremka kuingia katika nyumba hiyo yenye uzio mkubwa wa miba. Mlangoni palikuwa na mlinzi wa kampuni binafsi.

“Hawa jamaa waliondoka kwa likizo, ila watarudi, kwa sasa hawapo,” alieleza yule mlinzi.

“Ok, ni muda gani ambao hawapo hapa,” akauliza Gina.

“Ni kama wiki moja sasa,” akajibiwa.

“Sawa asante basi tutakuja wakati mwingine,” Gina akashukuru, wakaondoka na Amata kurudi garini.

Kamanda Amata alipoketi tena na Gina garini, akamtazama mwanadada huyo mrembo wa sura na ngozi nyeusi inayong’azwa kwa lishe bora na virutubisho makini, “sasa naongea na wewe kama mshirika wa kiofisi na sio wa kikazi, unafikiri kwa nini hawa watu wameenda likizo ndani ya wiki moja ambayo hiyo hiyo imetukia tukio hili?” akamwuliza.

“Hata mimi hapo moyo wangu unapiga chogo chemba, nashindwa kupata jibu, nahisi kuna jambo kati yake, any way, tunafanya nini sasa?” Gina akajibu na kuuliza.

“Hapa hatuna budi kulisaka gari lenye namba hizo, kwa kuwa mpaka sasa ni ufunguo pekee wa kazi yetu, hebu twende leo tukamtembelee rafiki yetu wa muda mrefu, nafikiri huyu anaweza kutusaidia kwa namna moja au nyingine,” Kamanda akamwambia Gina.

“Nani huyo?”

“We endesha gari mpaka kituo cha polisi kati,” Kamanda akaamuru.

“Aaaaa ok, nimeshamjua, na kweli ni wa siku nyingi sana,” Gina akaitikia.

Dakika nyingine ishirini na tano ziliwafikisha katika kituo cha polisi kati, walipoegesha gari wakashuka moja kwa moja na kuifuata kaunta kabla hawajapandisha ngazi ghorofa ya kwanza ambako walimkuta yule wanayemhitaji, Inspekta Simbeye.

“Karibu kijana, naona leo umefuatana na mrembo wako!” akakebehi.

“Ee Bwana si unajua tena lazima alinde,”

“Kabisa; hongera bibiye nasikia umeteuliwa katika idara nyeti ambayo wenzako wanaililikutwa kucha hadi wanagongana kwa waganga, lakini wewe aaaaa kiulaini umeikwaa,” Inspekta Simbeye kama kawaida yake akawa akimwaga utani, akawakaribisha na kuketi nao, “ndiyo Bwana Amata , najua tu kuwa ukija hapa basi huko yamekushinda,” akamwambia.

“Hapana, nikija hapa basi nataka usaidizi wa mapana na marefu, kuna hii namba hapa ya gari, naihitaji hii gari ama nijue sasa hivi iko wapi au imepita mtaa gani,” akamwambia Simbeye, akampa kijikaratasi kilichoandikwa hiyo namba. Inspekata Simbeye akakitazama kwa udadisi sana kile kijikaratasi, akafinya macho akafinyua, kisha akawatazama Gina na Amata, “ ok kwa hiyo mnataka vijana waingie kazini?” akauliza.

“Ndiyo maana tukaja kwako kwa maana wao vijana wako wanajua kunusa vitu kama hivi kwa haraka kutokana na mtandao walio nao,” Kamanda akeleza.

“Ok, nipe dakika kadhaa,” akainua simu ya mezani na kuzungurusha namba fulani kisha akamwita kijana mmoja. Dakika mbili yule kijana alikuwa kasimama kwa ukakamavu kabisa mbele ya Inspekata wake akiwa katika sare yake nadhifu nyeupe katika mkono wake wa kushoto akining’iniza ‘V’ tatu yaani alikuwa Sajini.

“Nataka upeleke taarifa kila point huko barabarani wakiiona hii gari leo wanipe taarifa haraka iwezekanavyo,” akatoa amri.

“Sawa Afande!” akajibu yule kijana na kutoa saluti ya utii kisha akaondoka zake.


Siku hiyo askari wa usalama barabarani waliongezeka mpaka kila mtu alishangaa, gari nyingi zilisimamishwa hii ikakuguliwa pale na ile kule ili mradi tu wajaribu kuipata ile wanayoitaka. Haikuwa kazi rahisi bali ilikuwa ngumu, madereva walikasirika sana maana walisimamishwa hata zaidi ya mara tano lakini hawakujua ni nini ambacho wenzao wanakitafuta. Siku ilienda kasi hakuna jibulolote lililoleta maatumaini. Kamanda Amata akiwa katika mgahawa wa Steers alianza kukata tamaa, maana alitegemea taarifa hiyo ingeweza kumpa njia ya kupenyea katika kulikabili swala hilo.

Akiwa anaweka weka vitu vyake vizuri tayari kuondoka katika mgahawa huo mara simu yake ikapata uhai mpya, namba iliyosomeka kiooni ilikuwa ni ile ya Simbeye. Kumekucha, akawaza, kisha akaibonyeza kile kidubwasha cha kusikilizia na kuiweka sikioni.

“Windo lako limeonekana, limetoka barabara ya Mandela na kuingia barabara ya Morogoro…” Sauti ya Simbeye ilieleza.

“Ok, nimekupata, naomba taarifa kila point anapopita mpaka atakaponikaribia, nipo mjini kati na sasa naelekea barabar ya Morogoro kutokea Mtaa wa Samora,” Kamanda akaeleza.

“Wrong, pita barabara ya Ohio ukatokee ile ya Bibi Titi kisha kunja kurudi Maktaba nafikiri atatumia njia hiyo,” Simbeye alieleza kana kwamba anajua mtu huyo anakwenda wapi. Kamanda Amata akatia gia na kuondoka pale Steers, moja kwa moja akaiacha Ohio na kuikamata ile ya Bibi Titi kuelekea Maktaba akiwa makini kabisa kutazama gari zinazokuja mbele yake, akafyatua nobu ya simu ya upepo yenye uwezo wa kunasa mawimbi ya simu zote za mtindo huo zinazopita ndani ya mita mia tano za mraba, akaweka vizuri signali za redio ya polisi akazipata na kusikiliza wanavyoelekezana juu ya gari hiyo.

“…Imepita hapa mataa ya Magomeni ova….”

“….Imeelekea Kinondoni, point ya Kinondoni tafadhali, ova!…”

Kamanda Amata alipiga U – turn pale maktaba na kurudi haraka akakunja kushoto kwenye makutano ya barabara ya Bibi Titi, Ohio na ile ya Ally Hassan Mwinyi, akaifuata hiyo kwa kasi akiwa na malengo mawili, ama kukutana nalo kwenye makutano ya Barabara ya Ally Hassan Mwinyi na Ile inayotoka Kinondoni.

“… imepita mataa ya Mwananyamala. Imenyoosha kuelekea Morocco, Ova…”

“….Endelea kunipa ripoti Ova!…”

Kamanda Amata akakaza mguu na kuongeza kasi kuwahi katika makutano ya Morroco maana kutoka hapo hakujua hasa ni wapi anaweza kuwaona tena.

“…imeelekea barabara ya Hali Hassan Mwinyi, ova…”

Kamanda Amata aliposikia taarifa ya mwisho alikuwa tayari amefika karibu na Mbuyuni njia ya kwenda Kanisa la Sant Peter, akakunja kulia na kuifanya kama inataka kuingia barabara ya pili kuelekea mjini, akasimaman katikati akisubiri, wakati huo taa ziliwaka nyekundu, gari zikasimama. Kamanda Amata akatazama kwa haraka haraka, akaiona ile gari ikiwa imesimama ikisubiri foleni, akatazama kwa umakini ndani yake, alimuona mtu mmoja tu, mwanaume aliyekuwa ameketi nyuma ya usukani. Gari zilizpoanza kutembea, akavizia nyuma ya hiyo gari zikapita gari mbili kisha yeye akaingia hapo na kuifuatilia taratibu. Ile gari ilikwenda na kuingia katika maegesho ya Motel ya Agip katikati ya mji, mtu aliyekuwa humo akashuka, mwanaume mwenye tambo la haja, kwa harakaharaka Kamanda alimuona mpiganaji huyo akivuta hatua fupifupi na mguu wake akiwa akichechemea kwa mbali, akamkumbuka, George Mc Field, akatikisa kichwa, kisha akacheka, baada ya kugundua kuwa mtu huyo miaka kumi ilopita hakuwa akichechemea lakini kwa kipigo alichokipata kwa Kamanda Amata mara ya mwisho katika sakata la Mwanamke Mwenye Juba Jeusi kumbe lilimuacha na mguu mbovu. Akamtazama mpaka alipoingia ndani, akateremka garini na yeye kuiendea kaunta ya moteli hiyo.

Moustache alioubandika juu ya mdomo wake ulimbadili kiasi, na kofia kubwa aliyovaa ilimfanya aonekane mmoja wa ‘watumia pesa’. Amata akasimama jirani kabisa na Mc Field ambaye alikuwa amejibadili kiasi ila kwa Amata alimtambua kwa alama zake alizokuwa akizikumbuka. Kabla hajaongea na mhudumu wa kaunta jicho lake kali lilikuwa likitazama katika kaitabu ambacho Mc Field alikuwa akiweka saini, akaona namba ya chumba 206. Akajifanya anaulizia mtu fulani ambaye hayupo kabisa katika hoteli hiyo. Kisha akatoka mara baada ya kujibiwa kuwa mtu huyo hayupo. Akarudi garini na kuiondoa gari yake kisha akenda kuiegesha upande wa pili. Alijua wazi upande gani ambako kile chumba kilitazama, akaiacha gari yake na kurudi upande wa pili.

Chumba alichokitegemea, kikafunguliwa pazia, Amata hakuwa na haja ya kujua nini kinaendelea ndani ya chumba hicho, akatulia akisubiri. Ilichukua dakika arobaini na tano, pazia likafungwa tena. Kamanda akawa makini kuona nini kinatokea, mara gari ile ikawashwa na kuondoka maegeshoni.

Kama kawaida, akasubiri dakika kumi na tano akaingia ndani ya hoteli ile na kukwea ngazi mpaka chumba namba 206 akautazama mlango kwa makini kama kuna alama yoyote iliyoachwa ambayo mtu huyo itamfanya agundue kuwa alitembelewa. Hakuona, akachukua funguo yake inayoweza kufungua vitaza 999, akaipachika na kucheza nayo sekunde nne tu mlango ukatii, akausukuma taratibu lakini alikumbuka lililompata Madam S, akatanguliza mkono wake huku akikubali kitakachotokea, alitegemea kutobolewa na misumari mibaya inayotegwa na Jasusi huyo mara nyingi, hakukuwa na kitu.

Akaingia kwa hatua mbili ndani, hakuwasha taa ijapokuwa giza lilikwishakijaza chumba hicho, akaichukuwa miwani yake na kuivaa, chumba chote kwake kikaangazwa na mwanga usioonekana na mtu mwingine, akatazama kwa macho, akakagua chumba hicho kwa macho, hakutaka kugusa chochote kile, kisha akachukua kijitufe kidogo mfano wa big G, akakiendea kitanda akakitazama na kupachika kile kidubwasha uvunguni kwenye chaga, kisha akatoka taratibu na kukiacha chumba hicho, akarudi kwenye gari yake, akafungua saraka ya gari na kutoa kidubwasha kingine kama redio ndogo sana ukubwa wa kiberiti, akakiwasha ili kurekodi kila sauti itakayotokea ndani ya chumba hicho kisha yeye akaondoka zake kwa usafiri, mwingine huku ile gari akiiacha pale pae.

“Las Vegas Cassino!” akamwambia dereva aliyekuwa kimwendesha. Dakika chache baadae alikuwa katika Cassino hiyo kubwa iliyopo kwenye njia panda ya kuelekea Agha Khan kutokea Barabara ya Ally Hassan Mwinyi.

“Yes Kamanda,” Madam S akaiita kutoka nyuma yake wakati Amata akiwasha sigara kana kwamba yeye ni mvutaji.

“Agip Motel namba 206,”

“Maelekezo mengine,” akahoji Madam.

“Baada ya saa kadhaa, watoto wanacheza,” akajibu.

“Ok,” Madam akamalizia kwa kuitikia, akampita Kamanda na kuondoka zake, akaiendea gari yake, kukamata kitasa.

“Subiri!,” Kamanda akamshtua Madam S, kisha akampa ishara ya kurudi kwake, Madam akataii. Wakati Madam S alipokuwa anataka kufungua mlango wa gari, Kamanda Amata alimuona mmoja wa walinzi wa Cassino hiyo akichomoa kitu kama remote mfukoni mwake. Hiyo ilimpa ishara Kamanda kuwa kuna hatari inakaribia kutokea, Madam alaiporudi kwa Kamnda yule mtu akarudisha ile remote mfukoni mwake, na kupotea eneo lile mara moja.

“Hakuna usalama,” akamwambia Madam S

“Umeona nini?” Madam akauliza

“Gari yako lazima ina mlipuko, ngoja kidogo,” akajibu na kuifuata gari ya Madam S, akawasha saa yake na kuisogeza jirani, ikapiga kelele na kuwaka taa nyekundu, akamtazama Madam S.

“Wamejuaje kama niko hapa mpaka waniwekee bomu?” Madam S akauliza.

“Muwinda huwindwa mama! Acha hiyo gari tumia usafiri mwingine, tuonane kesho asubuhi,” Kamanda akamuaga mwanamama huyo na kutoka eneo lile. Kwa mwendo wa miguu akarudi kuifuata barabara ya Ally Hassan Mwinyi, akiwa taratibu njiani, nyuma yake kulikuwa na watu wawili wakija nao wakiwa wametokea katika casino ileile. Aliporudisha uso mbele akaona mtu mmoja akija upande huo, hakuonesha kugwaya, alitembea kwa mwendo uleule. Alipofika katikati, wa nyuma na wa mbele wakiwa umbali sawa, akasimama na kugeukia katika maua yaliyo mbele yake, akafungua zipu ya suruali na kujifanya anakojoa, akisubiri aone watu hao watachukua hatua gani. Alijua kama watasita basi ni wabaya kwake lakini kama si wabaya watapita na Hamsini zao.

Wale wawili wakasita kidogo, wakawa kama wanajiuliza jambo, yule mmoja akajifanya anafunga kamba za viatu, kwa vitendo hivyo Kamnda Amata akajua wazi kuwa anawindwa na amekwishwekwa katikati, akageuza na kurudi alikotoka kule kwenye wale wawili, akaona wakiwa na woga Fulani, akaongeza mwendo kuwaendea, akachanganya miguu kama anatroti.

“Simama!” wakamwamuru.

“Mna amri gani ya kunisimamisha mimi? Ninyi ni nani?” akauliza huku akiwapita.

Wale jamaa walimpa hatua mbili tu za kupita, wakageuka na mmoja wao akatoa kitu kama mpira akauzungusha katika viganja vyake, mwisho huu huku na huu kule tayari kwa kumkaba. Kwa haraka akaupachika shingoni mwa Amata, hilo alilitegemea tangu mwanzo, na aliigundua hiyo mbinu. Akanyosa juu mikono kwa kuikunja mikono yake na ule mpira ukaivaa mikono, akaisukuma mbele na yule jamaa akajigonga kisogoni mwa Amata. Akajivua ule mpira na kugeuka haraka, konde moja alilolitupa, lilipiga shavuni mwa Yule mjing akaenda chini, yule wa pili akarusha ngumi akadakwa mkono, akauzungusha na kuuweka begani akauvunja, yowe la uchungu likamtoka yule jamaa. Wakati huo yule mmoja aliyekuwa akitokea mbele akawa amefika, mkononi alikuwa amekamata kitu kama bastola. Amata akamwacha yule jamaa na kuchumpa kuingia kwenye maua, lo! Hakuangalia vizuri, kwenye yale maua kulikuwa na seng’enge yenye ncha kali sana, zikamchoma, kabla hajajinusuru yule jamaa akafyatua ile bastola yake, kitu kama msumari kikamchoma shingoni. Amata akajisikia ganzi, miguu akahisi ikipata ubaridi, taratibu akaanza kupoteza nuru. Kila alipojaribu kujitutumua hakuweza, akatulia na kukumbwa na giza nene.

“Mmemkamata?” sauti hiyo aliisikia kwa mbali sana.

“Aaa nimempata lakini Shebby kavunjwa mkono msaidieni,” akaendelea kuwasikia kwa taabu na mwisho masikio yake hayakuwa na nguvu tena za kusikia chochote.

SIKU ILIYOFUATA saa 3:30 asubuhi

MADAM S ALIINGIA OFISINI kwa kuchelewa kidogo, akamkuta Chiba akiwa anamsubiri.

“Vipi Chiba?” akuliza.

“Nimekuwa nakusubiri sana maana kila simu nikikupigia sikupati, nikaanza kuwa na wasiwasi,” Chiba akajibu.

“Ah, mbona simu zangu zilikuwa on zote? Kwa nini ulikuwa hunipati?” Madam S akatoa simu zake na kuziangalia zote zilikuwa sawa.

“Shida za mitandao hizi,” akamwambia kisha akaingia ofisini.

“Nipe jipya,” Madam S akamwambia huku akivuta kiti chake na kukaa.

“Hakuna jipya, ila sina taarifa yoyote ya Kamanda tangu jana nilipokuwa nawasikia mara ya mwisho pale Cassino ya Las Vegas,” akamweleza Madam.

“Aaaa Kamanda tuliachana kama saa nne hivi, na tangu hapo hata mimi sikumtafuta,” Madam S akajibu, akafikiri jambo kisha akaendelea kusema, “jana aliacha gari pale Motel Agip mtaa wa pili hivi, kuna information alikuwa anainasa, nafikiri atakuwa ameiendea, hebu mtafute kwa simu yake ya kwenye gari”.

Chiba akajaribu lakini simu iliishia kuita tu.

“Hayupo garini!”

“Jaribu nyumbani”.

Chiba akajaribu simu za nyumbani, zote hazikupatikana kabisa, “hakuna connection kabisa,” akamwambia Madam S.

“Mpigie Gina,” akatoa maelekezo. Chiba akampigia Gina akampata, akamwulizia juu ya Kamanda Amata, Gina hakuwa na jibu sawasawa, akamwambia atapita nyumbani kwake Kinondoni akamwone.


Kamanda Amata alikuwa kwenye kiti cha chuma, hakuwa na fahamu, mikono yake ilifungwa nyuma ya kiti hicho ilhali miguu yake ilikuwa imefungwa pamoja kwa kuzungushwa nyuma ya miguu ya mbele ya kiti hicho. Alikuwa amelala usingizi, shingo yake imeeinamia chini, udenda ukimtoka. Ndani ya chumba hicho cha wastani kulikuwa na vijana watatu wenye Sub Machine Gun kila mmoja iliyoshiba vizuri. Hawakuwa wakiongea, kila mmoja alisimama kona yake akiweka ulinzi madhubuti. Waliambiwa watoe taarifa pindi tu atakapoamka. Ilikuwa zimekwishapita saa kumi na mbili tangu adungwe dawa ile mbaya kabisa mwilini mwake ambayo huenda na kuudhoofisha milango yote ya fahamu.

Amata alianza kuhisi baridi kwa mbali sana, fahamu zilianza kumrudia, kidole chake cha kalulu kilianza kuchezacheza.

“Anaamka huyu! Oya waite jamaa!” mlinzi mmoja alitoa amri kwa walio nje. Ijapokuwa alikuwa kamanda peke yake katika chumba hicho kama mateka lakini walinzi wa ndani walikuwa watatu waliobeba SMG zilzizoshiba risasi, nje ya mlango kulikuwa na walinzi wengine wapatao watano nao walikuwa na silaha kama zizohizo. Kwa ujumla walimwogopa, labda kutokana na habari walizopewa juu ya uhatari wa mtu huyo.


Peugeot 404 iliegeshwa nje ya nyumba fulani katika eneo la Upanga, mtaa wa Ali Khan. George Mc Field ambaye tangu ameingia nchini alikuwa ameuvaa Uafrika-butu, alionekana Mwafrika lakini aliyepauka kidogo, hiyo ilitokana na kujibadilisha kwa ngozi yake kwa madawa maalumu na kuupoteza uhalisia wa uraia wake. Alikuwa Jasusi aliyetafutwa kila kona, alitekeleza mengi sana ya kuua, kuiba, kuteka, kutesa na mambo yanayofanana na hayo. Alijishauri mara kadhaa siku alipoapewa kazi ya kuja kufanya wizi wa almasi katika mgodi wa Mwadui, lakini kutokana na donge aliloahidiwa alikubali.

Akachagua watu watatu makini kati ya vijana wake, akawafundisha Kiswahili, mapigano, jinsi ya kutembea kama Watanzania, akaandaa mkakati makini wa kuiba almasi kwa kujifanya yeye ni Waziri wa Nishati na Madini. Kazi hii kwa Mc Field haikuwa ngumu sana, kwa kuwa yeye alikwishapitia kozi mbalimbali za Kijasusi na Ukomandoo aliiona kazi ndogo ila aliipenda kwa kuwa ilihusisha pia kuwapoteza watu uhalisia wa wanachokiona.
 
WIKI MOJA NYUMA

FORKER FRIENDSHIP, ndege ya serikali, iliondoka katika uwanja wa ndege mdogo wa mgodi wa North Mara kuelekea Mwadui. Wageni waliotumwa na makampuni kutoka nje kuja kwa ajili ya kutazama fursa za uwekezaji, walitulia vitini, walikuwa watatu, wazungu. Ndege ilipokaa sawa hewani na kuruhusiwa kufungua mikanda, mmoja wao alinyanyuka na kuelekea maliwato.


“Vipi, kuko sawa huko?” Mc Field aliuliza akiwa katika eneo la mizigo, amekaa akisubiri wakati, yeye aliingia ndegeni bila mtu yeyote kujua, alijifanya mmoja wa wafanyakazi wa ndege hiyo pale North Mara, akajificha katika behewa ya mizigo, akijibadiliasha hapa na pale mpaka akafanana kabisa na Mheshimiwa Waziri. Utaalamu wa hali ya juu unaotumiwa na Majasusi au wapelelezi mbalimbali huko nchi zilizoendelea. Mission ilishapangwa, kila kitu kilitengenezwa, ilibaki kuvaa tu.style='font-size:7.5pt'>
“Yeah, tuko level nzuri kutoka usawa wa bahari,” akajibu yule mtu.

“Ok, zima pale, kisha pachika hako kamtungi katika hiyo pipe,” akamwelekeza, yule kijana akafanya hivyo, “subiri kidogo, dakika tano hivi, nitakujulisha,” akamwambia, kisha ukimya ukawakabili kati yao.


Ndani ya chumba cha rubani, mashine za kuonesha vipimo vya hewa, presha, kani mvuto, mwendo kasi na kadhalika, vilionesha hitilafu hasa katika upande wa presha na hewa safi. Rubani alijitahidi kurekebisha hapa na pale lakini ilikuwa ngumu, akainua kidubwasha cha kuongelea na kuwatangazia abiria kutumia hewa ya ziada inayotoka katika mitungi maalumu ndani ya ndege hiyo. Juu ya kila kiti, kwenye saraka kubwa za mizigo ya ndani zikachomoka barakoa za kuvaa puani kuweza kuvuta hewa safi.

Wakati huohuo kule chini kwenye mizigo, Mc Field na mwenzake wakaondoa mtungi wa oxygen kwenye ‘Chemical Oxygen Generator System’ na kupachika mtungi wao wenye dawa kali ya kulevya katika njia za kupitisha hewa safi. Haikuchukua dakika moja wote walikumbwa na usingizi mzito isipokuwa wale Wazungu tu ambao hawakugusa kabisa barakoa zile.

“Tayari, waambie wenzako mulete waziri huku chini. Yule kijana akafanya hivyo. Waziri akaletwa chini kwenye mizigo akiwa anapumua kwa tabu, Mc Field akachomoa kijikadi kidogo kilichounganishwa vizuri kwenye kompyuta ndogo.

“Soma hapa,” Mc Field akamwambia waziri. Mheshimiwa akabaki kakodoa macho tu, hakujua la kufanya, “soma hapa!” akamlazimisha na kumchapa kofi la usoni.

“Tu-na-hitaji -makasha ma-ta-no ya almasi sa-sa ni amri ku-to-ka I-ku-lu ba-ru-a hii – ha-pa”.

Kisha mmoja wa wale vijana akamdunga sindano na waziri akalala usingizi wa maana. Wanaume wakafanya walichotumwa.


Rejea sasa: Tracy Tasha…

TRACY TASHA ALIVIRIGA nywele zake na kuzifunga kwa nyuma, akaiweka miwani yake usoni, akachukua kitu kama kalamu iliyokuwa na rangi inayofanana na ngozi yake akakiendea kioo kikubwa na kuanza kujitengeneza uso wake vizuri kwa namna anayoijua yeye, alipohakikisha kajiweka tofauti, akafungua mkoba wake na kutoa stika moja ambayo aliibandika kwenye shavu lake. Stika ile ilitengenezwa taswira ya mtu aliyeshonwa jeraha kwa nyuzi saba. Akatoka nje ya hoteli na kuingia katika tax iliyokuwa ikimsubiri, “mtaa wa Ally Khan mkabala na Zanaki Sekondari,” almwambia dereva kisha yeye akaketi kiti cha nyuma bila kuongea zaidi hata pale alipoulizwa maswali kadhaa na dereva huyo hakujibu zaidi ya kutikisa kichwa tu.

Dakika arobaini na tano ziliwatosha kupambana na foleni na kuingia katika eneo husika. Tracy alilipa na kuachana na dereva huyo, alipopotea, akavuka barabara na kuingia kwenye geti dogo katika nyumba aliyihitaji. Ilikuwa nyumba kubwa ambayo nyuma yake kulikuwa na banda kubwa lililojengwa kwa matofali ya kupangwa, ndani yake kulikuwa na kitu kama handaki ambacho watu wengi hawakujua hilo.

“Karibu sana, this way please,” George Mc Field alimkaribisha Tracy na kisha wote wakashuka handakini.


Kamanda Amata alikuwa ameendelea kuketi palepale alipofungwa, akili yake ilisharudiwa na fahamu kamili, lakini bado alijifanya hajaamka sawasawa, aliweza kusikia kila kitu kilichoendelea, alijuwa wazi kuwa ni nani anayesubiriwa na alisubiri kuona kama hao wanaokuja ndio wale anaowahitaji, alihitaji kuwajua. Kwa mara kadhaa alijaribu kujitikisa na kuona kama kamba zile zimemfunga sawasawa, mikononi alishindwa hata kujitikisa lakini miguuni nako ilikuwa hivyo hivyo, akatulia na kufumbua jicho moja kwa mbali, akawahesabu wote waliokuwa ndani, ni watatu tu na bunduki zao.

Nikileta makeke tu natobolewa kwa risasi zenye hasira, akawaza. Mara akasikia lango likifunguliwa upande wa juu na watu waliokuwa wakiongea kwa lugha ya Kiingereza wakaingia ndani ya eneo hilo.

Sekunde chache tu watu wawili walikuwa mbele yake, yule mgeni wa kiume akatikisa kichwa chake na kijana mmoja akaweka pembeni bunduki yake, akakunja mikono ya shati lake. Kamanda Amata akajua sasa kumekucha. Yule bwana alimsogelea, akamatazama Amata. Akamwinua uso wake, Kamanda akafumbua macho yote mawili akamwangalia, yule jamaa akasita kidogo maana alishaambiwa uhatari wa kiumbe huyo. Akaita wenzake wamuweke sawa. Amata akafunguliwa kamba na kuondolewa kitini, kamba za miguuni zikarudishhiwa kisha zile za mikononi zikafungwa kwa nyuma lakini wale vijana wakamkamata huku na huku upande wa nyuma na yule mwingine akaanza kumshindilia makonde ya tumboni, makonde ya nguvu. Amata alivumilia lakini nguvu za mikono za yule Bwana zilikuwa zikimwingia kisawasawa, damu zikaanza kumtoka kinywani.

“Ha! Ha! Ha! Haaaaaa! Mwacheni! Kamanda Amata, leo au niseme sasa, umefika mwisho wako, na lazima ufe sambamba na yule tunayemtaka au tuliyetumwa kumtoa roho yake,” Mc Field akamwambia Kamanda huku akimgeuza uso wake uliowiva kuwa mwekundu. Alihema kwa taabu sana, “Mc Fi-e-ld, uta-lipa, utalipa, na-kwa-mbia utalipa,” akamwambia kwa sauti ya taabu. George Mc Field akastuka kidogo baada ya kusikia jina lake likitajwa, akajiuliza pamoja na kujibadili inawezekanaje kuwa kajulikana kirahisi namna hii, akajikaza.

“Nani anayekudanganya hayo? Sikia mpumbavu wewe, kabla hujafa nitataka kukupa siri moja nzito ambayo utakufa na hautaweza kuifikisha popote pale, na siri hiyo ni kuwa kesho tunaondoa roho ya mtu mkubwa sana hapa katika Taifa lenu,” Mc Field alizidi kutamba wakati Tracy akiwa kasimama kando mikono yake kaifungamanisha kifuani mwake, akitafuna pipi mpira isiyokwisha.

Konde moja zito la Mc Field lilitua katika shavu la Kamanda Amata, akahisi taya lake limevunjika, kabla hajatulia akapata lingine la upande wa pili.

“Sikia we Bwege, nimekuja tena nikiwa na hasira mbili, na kazi moja! Nadhani umenielewa, leo hutoona jua la nje, kibibi chako kinahaha huko duniani kukutafuta na hakitakuona tena,” Mc Field alimweleza Amata.

“Utalipa, ha-ta mimi ukiniua, yu-po nyu-ma atakayekuua kwa kwa niaba yangu, atakutenganisha kichwa na kiwiliwili chako,” Kamanda akaeleza.

“Ha! Ha! Ha! Ha! Haaaaaa!!!!” Mc Field akacheka sana, “nani unayemtegemea, huyu hapa au mwingine?” Mara mlango mwingine ukafunguliwa, Gina akasukumiwa ndani na kuanguka sakafuni. Kamanda Amata alitamani aruke kumdaka Gina ambaye alijibwaga vibaya sakafuni.

“Tunapotaka kufanya kazi, huwa tumejipanga, wewe na huyu malaya wako wote leo mnaenda kuzimu,” Mc Field alijigamba. Kamanda Amata alikuwa amefura kwa hasira kali, akimtazama Gina aliyekuwa chini hajiwezi, ilionekana amepata kipigo kisicho cha kawaida.

Tracy Tasha alivuta hatua na kumsogelea Gina, alivuta mguu wake na kumtandika Gina teke kali la usoni. Gina akatupwa upande wa pili, akabaki chali damu zikimvuja puani na kinywani. Mguu wa Tracy ulienda juu na kubaki hewani kwa sekunde kadhaa kabla hajaushusha chini kwa maringo, kisha akatembea kama Miss kumwendea Amata.

“Huyu ndiye ulienipa vitisho juu yake? Eti Kamanda, kamanda? Makamanda wametulizwa kwa mkono huu,” akaupunga mkono wake hewani, akamtazama Mc Field, “hakuna mwanaume wa chuma wala nini, hapa ni utepetevu tu,” akamalizia kisha akarudi alipokuwa. Mc Field alitabasamu huku akitikisa kichwa chake juu chini, akimwangalia mwanamke huyu anayetembea kwa madaha, mrembo wa sura na mzuri wa shepu, lakini mwenye roho iliyojaa kutu.

“Kamanda Amata una la kusema? Sasa ni saa saba inaenda saa nane, muda wetu unayoyoma, huyu mwanamke ndiye atakayekuua wewe usiku wa leo kwa kukukata kichwa chako,” Mac Field alimwambia Kamanda.

“Hata kama, La- la-ki-ni, kwa-nza nitaku-ua we-we,” akimaanisha Mc Field, “pili we-we mwana-m-ke uta-ji-ua –mwenye- we,” aliongea kwa tabu. Mc Field na Tracy wakaondoka ndani ya chumba kile wakiacha maagizo kuwa watu hao washughulikiwe ipasavyo.


Ilikuwa ni vigumu sana kwa Madam S kuamini kuwa Kamanda na Gina wametekwa, haikuingia akilini. Wamempataje kirahisi hivyo? Alijiuliza bila ya kupata jibu. kila mara alikuwa akimwita Chiba ofisini na kumwambia hili au lile, alionekana wazi amechanganyikiwa. Chiba alijaribu kumtafuta Kamanda kwa simu zake lakini ilikuwa ni ngumu sana kwake kupata jibu kuwa wapi yupo kwani simu zake zilikuwa zikisoma eneo la mwisho la Upanga, Las Vegas Cassino.

“ Wameniweza!” alijiambia moyoni, “Scoba!” akaita.

Scoba akageuka kumtazama Chiba.

“Harakati lazima ziendelee kaka, hatujui Gina na Kamanda wako wapi mpaka sasa, na wala wako katika hali gani, hivyo tufanye juu chini kupata jibu,” Chiba, TSA 2, ilikuwa ni nafasi yake sasa kutoa majukumu.

“Iendee gari ya Kamanda pale Motel Agip kuna information inayoweza kutusaidia,” akaamuru na Scoba akawasha gari yake na kuondoka. Kama alivyoeelekezwa. Gari ya Amata ilikuwa palepale, Scoba kwa tahadhari ya hali ya juu sana akiendea ile gari, hakuhitaji kuiendesha, moja kwa moja aliifungua droo iliyokuwa imefungwa kwa lock maalum, akachukua anchotaka, alipogeuka tu kuondoka kuiacha ile gari, nyuma yake mlipuko mkubwa ukatokea, ile gari ikanyanyuliwa juu na kuvingirishwa mara kadhaa kabla haijatua juu ya gari nyingine ambazo nazo zilidaka moto, kizaazaa.

Scoba, alitupwa na ule msukumo uliotokana na mlipuko, akatua katika mlango wa vioo wa duka moja la madawa, akaanguka nao mpaka ndani. Mtaa mzima ulikuwa ni hekaheka kila mtu akitaka kunusuru gari yake na kusahau uhai, wapo waliofanikiwa lakini pia wapo ambao gari zao ziliteketea kabisa.

Tukio hilo lilivuta wengi sana mahala hapo, hii ilimsaidia Scoba kuondoka taratibu na kuielekea taksi iliyokuwa jirani. Ulikuwa ni mlipuko ambao mtu yeyote hakuutegemea hasa kwa jiji kama la Dar es salaam ambalo utulivu na amani zimekuwa ni desturi kwa wakazi wake.


“Pole Scoba, lakini haujaumia sana,” Dkt. Jasmine alimpa pole Scoba huku akimpa huduma ya kwanza katika chumba cha siri kilicho ndani ya ofisi ya Madam S. Damu kiasi zilikuwa zikimvuja katika upande mmoja wa kichwa chake baada ya kujikata vibaya kwa kioo pale alipoangukia, akaufungua mkono wake na kumpa Madam S kile kidubwasha.

“Mpe Chiba,” akamwambia.

Ilikuwa ni kinasa sauti kidogo kilichofichwa katika gari ya Kamanda Amata, Chiba alikichukua na kukiunganisha na mitambo yake, kisha akafuatilia mazungumzo yaliyokuwa humo kwa makini. Ndipo alipogundua kuwa Kamanda Amata ametekwa kadiri ya mazungumzo ya mtu aliyekuwa akiongea na simu katika chumba cha Motel hiyo. Aliendelea kufuatilia mazunguzmao hayo lakini hakujua kabisa ni wapi watakuwa wamemficha Amata. Chiba na wengine vichwa vilianza kuwazunguka.

“Tutapajuaje? Kumbuka Mc Field anamjua vizuri sana Amata, hawezi kumpa nafasi zaidi ya kumuua tu. Ndiyo, Amata anaweza kujiokoa lakini ni kazi ngumu sana kwa mtu kama Mc Field ambaye anauju uwezo wa kamanda, mtu kama yule hawezi kurudia kosa,” Madam S alimwambia Chiba huku akijifuta machozi.

“Ok, Madam, najua cha kufanya ila sasa tuandae Kikosi cha Ukombozi,” Chiba alitoa ushauri.

“Sawa, ni wewe mwenyewe na Scoba mtafanya kazi hiyo, hakikisheni inazaa matunda,” akampa maagizo, kisha akamsogelea Chiba, “ukikutana na Mc Field usijipime kupambana naye, tumia silaha, mmalize,” akamnong’oneza kisha akarudi kitini.

Chiba akairekodi ile sauti kwenye kompyuta yake na kuwasiliana na rafiki yake wa karibu sana katika moja mitandao maarufu ya simu, akampa kazi ya kutafuta watu hao walikuwa wakiongea wapi na wapi.

Dakika tano baadae alipewa taarifa kuwa mmoja alikuwa eneo la Mjini Kati maana mnara uliosoma ulikuwa ni ule wa jirani na jengo la Kitega Uchumi la Bima na mtu wa pili alionekana kuwa mitaa ya Zanaki Sekondari kwani mnara uliomsoma ni ule wa jirani na chuo cha ufundi cha Dar – Tech, upande wa nyuma. Chiba alijiridhisha na maelezo hayo na akamuomba mtu huyo amwambie namba hizo kwa sasa zinasoma wapi ili waweze kuwafuatilia watu hao. Jibu alilopata ni kuwa moja ya namba hizo ilikuwa imezimwa lakini nyingine bado ilionekana ipo mitaa hiyo ya Upanga, Mtaa wa Aly Khan.

“Scoba, upo poa? Tunaweza kuingia kazini?” Chiba alimwuliza. Scoba akaitikia kwa kichwa kushiria kuwa yuko fiti na anaweza mapambano, wakatoka katika chumba hicho na kufungua kijistoo kidogo, wakachagua silaha zinazofaa kwa kazi hiyo.

“Vipi mbona mnapakaua?” Madam akauliza.

“Tunaenda kupambana na jeshi, so lazima tujiweke kamili,” Chiba akajibu. Scoba akachagua Short Gun double barell, akaijaza risasi, bastola mbili aina ya PK 380 akazitia kibindon. Chiba akatazama huku na kule akainua silaha inayoitwa Heckler and Koch UMP , akaitia begani na nyingine ndogo ndogo kama visu, kamba za plastic, wakatoka wakavitia kwenye buti la gari na wao wakabaki na bastola mbilimbili zilizosheheni risasi. Wakaondoka na kuelekea Upanga.

10

AMATA ALIKUWA MDHOOFU sana baada ya kipigo alichokipata kutoka kwa wale jamaa mara baada ya Mc Field na Tasha kuondoka katika eneo lile, walikuwa wakimpiga huku wakimcheka sana na kila mmoja alijiona mshindi katika hilo, damu zilikuwa zikimvuja, wakati huo Gina hakuwa na nguvu hata ya kusimama.

“Sasa kinachofuata ni kufanya mapenzi na huyu malaya wako huku wewe ukiangalia,” mmoja wale jamaa akamwambia Amata.

Yule jamaa akamwendea Gina na kuanza kumfungua suruali aliyokuwa amevaa, huku wenzake wakishangilia na kupiga picha za video. Kitendo kile kilimuuzi sana Amata, kikampa hasira, hasira ambayo ilirudisha nguvu za ziada mwilini mwake. Mmoja wa wale vijana akamsogele Amata.

“Usijifanye huoni, angalia huku tunachomfanya malaya wako kisha picha zote tunapeleka kwa wakubwa zako,” akamwambia Kamanda huku akimshika kidevu kumgeuzia sura kule alikokuwa Gina. Ni dakika au nukta hiyo ilikuwa ikisubiriwa kwa hamu sana na Amata, aligeuka ghafla na kudaka kidole cha yule jamaa kwa meno, akamuuma na kukikata kisha akakitema chini.

“Aiiiiiigggggghhhhhh!!!!! Ananing’ata mjinga huyuuu!” yule bwana akalia kwa uchungu sana, wenzake wakagutuka na kusogea kumsaidia. Kamanda Amata aliruka akiwa na kamba miguuni na mikononi, akajikunja kisha miguu yake akaipitisha katikati ya mikono yake na kutua nyuma huku mikono sasa ikiwa mbele. Akaanguka kwa kuwa hakuwa na uwezo wa kusimama sawasawa, akabiringita na kuifikia nguzo iliyosimikwa kushikia jengo hilo, akajiinua na kuketi, harakaharaka akashika ile kamba ya miguuni na kuifungua haikumpa tabu aliivuta tu ikalegea.

Kabla hajamaliza, alipata teke la mgongoni, mtu mwingine akaja kwa mbele na kurusha teke ambalo lingetua usoni au kifuani lakini Amata akalizuia kwa mikono yake iliyofungwa, akaunasa ule mguu na kuubana vizuri.

Kamba ya miguuni ikawa imekwishauacha mguu wake, akazungusha mguu na kumtia ngwala yule aliyemdaka mguu, jamaa akajibwaga chini akifikia kisogo, akatoa ukelele wa kifo. Mara hii alijikuta amezungukwa, akajiinua haraka na kuruka samasoti, risasi zikachimba chini na nyingine kwenye nguzo. Wakati yeye akitua chini alitua na wawili, mmoja alimshindilia vipepsi viwili vya pamoja na mwingine, akamshushia mateke makali, wote wakaenda chini, akabiringita na kujificha nyuma ya kasha kubwa la bati gumu, likamkinga dhidi ya adui zake.

“Oya, akitoroka huyo, tumekwisha!” Sauti ya mmoja ikasikika.

“Hatoki mtu hapa! Mzungukeni,” mwingine akatoa amri.

“We Chulubi, hakikisha huyo mwanamke umemfungia ndani, tushughulike na huyu mbwa koko,” sauti hii na maneno hayo yalimtia hasira Amata. Akiwa tayari ameiondoa kamba mikononi mwake kwa meno, alilisukuma lile kasha na kisha akajitumbukiza na kuseleleka nalo, risasi zikapiga juu yake lakini hazikuweza kuliathiri kwa lolote. Liliposimama akaruka nje na alipotua akambamiza mmoja mwenye bunduki, akaenda chini na bunduki ikitoka mikononi, akaruka samasoti akatua na kuiokota ile AK 47, akaitekenya na wawili walikuwa chini wakitupwa hewani na kugalagala wakigombania roho zao.

“Uwiiiiii! Mi nilisema, nilisema mimi!” mmoja akapiga kelele huku akikimbia kupanda ngazi za kutokea juu, lakini mara naye akarudishwa ndani kwa risasi, akajibwaga chali katika sakafu isiyokwisha.

Kamanda Amata akashangaa, alipotazama juu akaona vivuli vya watu vikiteremka katika ile ngazi, akajibana nyuma ya nguzo akiwa anatweta.

“Kamanda Amata!” ile sauti ikaita, mara moja aliitambua sauti ya Chiba.

“Chiba!” Naye akajibu huku akishusha bunduki yake na kutoka nyuma ya nguzo, hakumaliza hata hatua mbili, alihisi kitu cha moto kikipita katika mkono wake, ilikuwa ni risasi iliyopigwa kutoka nyuma na mtu mmoja aliyebwagwa hapo kwa kipigo. Kamanda aligeuka akiwa na maumivu lakini kabla hajafanya lolote risasi ilipenya katikati ya paji la uso la yule kijana huyo na kufumua sehemu ya nyuma ya kichwa chake.

Kamanda alipogeuka mbele alikuta bastola ya Scoba ikiwa bado imekamatwa barabara mkononi mwake.

“Asante Scoba, Gina hali yake ni mbaya, tumsaidie,” akawaambia na mara wakaweka silaha zao vyema lakini Scoba alibaki kasimama na bunduki mkononi kuhakikisha ulinzi.

“Tufanye haraka kabla polisi hawajafika,” Chiba alieleza. Pamoja na jeraha mkononi mwa Kamanda Amata lakini alijitahidi kusaidia na Chiba akambeba Gina mabegani mwake.

Scoba alikuwa wa mwisho kutoka katika ile nyumba pale Upanga, wakaliendea gari na kuingia kisha Scoba akabonyeza kitufe fulani na mlipuko mkubwa ukatokea kwenye ile nyumba, akaiondoa gari eneo hilo na kuacha kelele za wafanya biashara zikiita ‘Majambazi, Majambazi’


“Haujaumia sana Kamanda, risasi haijagonga mfupa, imejeruhi nyama tu,” Jasmine alimtia moyo Kamanda huku akiendelea kumshona jeraha lake.

“Ndani ya saa 24 lazima watu hawa wawe mikononi mwetu ama marehemu au wazima,” kamanda alikuwa akiongea huku akionekana kuwa na hasira sana juu ya adui zake.

Gina alikuwa amelazwa juu ya kitanda, chupa ya maji ikiwa juu ya linga, alikuwa na bendeji kiasi usoni na nyingine mkononi, alikuwa macho na alikuwa anaelewa kila kitu.

“Kamanda upumzike, tutafanya kazi ya kuwanasa sisi tuliobaki,” Chiba alimwambia Amata.

“Hapana, nasema hapana, nichome ganzi tafadhali, nataka kuingia katika mapambano, mpaka nijue mwisho wao au mwisho wangu,” Kamanda aliongea kwa hasira.

Madam S alisimama mbele ya Amata aliyekuwa sasa ameketi, akijaribu kuvuta akili na kuyapitia matukio.

“Kamanda,” akaita kwa upole, “unajisikiaje sasa?”

“Najisikia hasira Madam,” akajibu huku akigeuka, alionekana wazi mwili wake umejeruhiwa.

“Upumzike,” Madama akamsihi.

“No! hiyo haipo kwenye kamusi yangu, kumbuka adui ataona kambi yake imefumuliwa je atakaa hapa? Nikipumzika mpaka nipate nguvu tayari atakua London,” Kamanda akaeleza. Madam S akajifuta uso wake kwa viganja vya mikono, “Gina, anaendeleaje?” akauliza.

“Kaondolewa kapelekwa Shamba kwa matibabu zaidi, Gina amepigwa sana, ameumia sana,” Kamanda akajibu huku akiinuka, akasimama sambamba na Madam S, “sikia Madam, naongea kwa sauti ya chini, kuna mkakati mzito unaoendelea, hawa jamaa wametumwa kuondoa roho ya Mkuu wan chi, that is it!” akamtazama Madam.

“Ndiyo, lakini hatujajua kwa nini mpaka sasa wanataka kutekeleza hilo,” Madam akaongeze huku akimpita Kamanda na kukivuta kiti chake, akaketi na kuegemea meza, “Keti Kamanda!” akamwambia.

“Hii ni kitu nzito Kamanda, ni ya siri na ni nzito, sana lazima ishughulikiwe kikamilifu. Kwanza tushughulike na hawa waliokuja, tukiwatia mkononi wao sasa watatuambia nani aliyewatuma, hao sasa tutawafanyia kazi baadae kwa siri,” Madam akamwambia Kamanda.

“Ndio, lazima tukate mpaka shina sio matawi tu,” Kamanda akaongeza, “Mheshimiwa Rais anaendeleaje na afya yake?”

“Alipata mshtuko, sasa yuko sawa, na kesho ataongea na waandishi wa habari asubuhi saa nne palepale Ikulu, kuhusu hali halisi ya yaliyotokea, moja la kudunguliwa msafara wake na pili la kuibwa kwa almasi,” Madam akajibu.

“Hapana, sio wakati sahihi wa kufanya hivyo, Mheshimiwa hasijitokeze hadharani, akijitokeza anaweza kuwa amejianika wazi mbele ya muuaji,” kamanda akamwambia Madam.

“Amata, nimemwambia hayo, lakini inaonekana kuna kitu anaficha, sasa hii ni hatari kwa usalama wa nchi, sisi tunamlinda wakati mwingine inabidi atusikilize, ila safari hii amelazimisha kuongea na waandishi,” Madam akaeleza huku akipigapiga meza.

“Nimekuelewa, wacha iwe!”

Akanyanyuka kitini na kujitazama huku na huku, “naondoka Madam,” akarudisha mlango na kushuka ngazi taratibu, akaingia kwenye gari moja wapo ya ofisi na kutoka eneo hilo.

Simu ya kwenye gari ikaanza kuita, akainyakua na kuiweka sikioni.

“…Uwe mwangalifu we mtoto bado nakuhitaji,” Madam akamwambia. Kamanda Amata akaongeza kasi ya gari akaiacha barabara ya Ohio na kukamata ile ya Ally Hassna Mwinyi, akapita daraja la Surrender na kupinda kushoto mpaka nyumbani kwake Kinondoni. Akaegesha gari karibu na baa ya jirani. Akateremka na kuiendea nyumba yake. Alipoufikia mlango tu, akasita kidogo, kwa akili ya harakaharaka akajua nyumba yake imeingiliwa, akaichomoa bastola yake kutoka kwenye soksi, akaiweka tayari, akafungua mlango taratibu akaingia ndani kwa kunyata, kila alipotazama palipekuliwa, lakini hakukuwa na dalili yoyote ya mtu, akafungua chumba chake na kukuta hali ni hiyohiyo, kila kitu shaghalabaghala, akajua kwa vyovyote kulikuwa na purukushani. Akaenda mahali anapoficha zana zake za kazi na kabrasha za muhimu. Ni picha kubwa ya ukutani, akaibofya upande mmoja, ikaachia na kuteremka, akabonyeza tarakimu fulani na mahala hapo pakafunguka, akatazama kila kitu kipo sawa. Akapaacha na kwenda kwenye chumba chake cha siri ambako huficha kompyuta yake inayoweza kuona kila kitu kinachotukia umo ndani ikisaidiwa na vijikamera vidogo vidogo zilivyofungwa katika kona tofauti. Akafungua mlango na kujifungia ndani.

Ni chumba kidogo ambacho mlango wake kwa upande wa nje ni kabati lililoja viatu na makorokoro yasiyo na maana. Akawasha kompyuta hiyo iliyo mezani. Akarudisha nyuma matukio mpaka alipoona tukio lililotukia, akaanza kutazama.

Kwanza aliona mlango ukifunguliwa, Gina akaingia na kuita, kisha akaingia katika chumba cha Kamanda, akiendelea kuita. Hapo Kamanda akajua bila shaka Gina alikamatiwa hapo nyumbani kwake. Mara akaona kwenye ile picha mlango ukifunguliwa na watu watatu wakiingia, wakamvamia Gina kule chumbani. Gina akapigana nao kwa nguvu zote, akawaumiza vibaya mpaka ikabidi watumia kitu kizito kumpiga kichwani akazimia, wakambeba na kuondoka naye.

Kamanda Amata akashusha pumzi ndefu. Akainuka na kutoka ndani ya kile chumba, akaingia chumbani mwake na kuoga kisha akajilaza kwa dakika kadhaa akisubiri muda muafaka wa msako, lakini kichwani alijiuliza aanzie wapi, hakupata pengine zaidi ya Motel Agip.

Muda ulipotimu, akajianda kwa mavazi ya kazi, akachukua silaha zake muhimu na kuzitia kwenye kona mbalimbali za nguo yake, kisha bastola moja akaitupa kitandani na kuilalia kwa mgongo, yeye akiwa chali. Kichwa chake kilikuwa kikipanga na kupangua.


Mc Field aliikusanya mikono yake kifuani, kichwa kilikuwa kikimzunguka, hakujua nini anapaswa kufanya. Hata alichokuwa anakiangalia hapo dirishani hakukielewa, ndipo alipokumbuka kuwa hata hajarudi hotelini kwake. Akashusha mikono yake na kugeuka kumtazama Tracy aliyekuwa katingwa na kompyuta yake ndogo.

“Tracy,” akaita, Tracy akainua uso, “umeona kazi ilivyo nzito ee? Yule ndiyo Kamanda Amata, katorokaje pale, hawa ndio TSA, wanatisha,” akamwambia.

“Na sasa tunafanyaje, maana tumeambiwa tuwadhibiti hawa ndio tutimize lengo letu,” Tracy akajibu, “Lazima wameokolewa, uwezo wa huyo Kamanda sijui Amata ni mdogo sana, hawezi kunitisha mimi,” akajigamba.

“Ok sasa tunabadilisha program,” Mc Field akamwambia Tracy.

“Enhe, tunafanyaje, maana mimi haya mengine siyajui, mi nataka kumaliza kazi yangu tu niondoke,” Tracy akadakia na kuifunga kompyuta yake. Mc Field akachomoa kipande cha gazeti moja la kiingereza, akamtupia mezani. ‘Rais kulihutubia Taifa’, ilikuwa ni habari iliyopewa uzito wa juu mbele ya gazeti hilo, akaisoma habari hiyo na kukiweka mezani.

“Asante Mc Field, kesho naenda kumaliza kazi yangu, naomba niandalie usafiri wa kuondokea tafadhali, maana hiyo ndiyo kazi yako,” Tracy akasema huku akijifunga nywele zake vizuri.

“Hilo lisikuumize kichwa, nitanunua tiketi usiku huu huu, nafikiri kutoka hapa tuondoke na ndege ya kukodi mpaka Nairobi kisha pale wewe utachukua ndege na mimi nitarudi kwa kutumia usafiri wa barabara. Uzuri wa ndege ya kukodi unachagua muda wa wewe kuondoka, kwa hiyo, ukimaliza kazi, mara moja nitakutorosha, hilo niachie mimi,” Mc Field akamtoa hofu Tracy.

“Sawa, kama mambo yakienda sawa basi kesho saa tatu hivi tayari bendera zao zitakuwa nusu mlingoti, huwa sibahatishi kabisa,” Tracy alisimama na kuagana na Mc Field.

“Sasa mpango wote mimi nitaupabga usiku huu, wewe relax maliza kazi na mi nitakuwa pale tayari kukuondoa salama,” MC Field alipokwisha kusema hayo akatoka katika hotel ya Land Mark na kuchukua gari ileile anayoitumia ,TX, akaondoka zake.

Tracy alisogelea kabati la nguo katika chumba cha hoteli hiyo, akavuta kijibegi chake na kukitupia mezani, akakifungua katika mfuko wa pembeni kabisa kuangali kama zana zake zipo, naam zote zilikuwepo, zimetulia tuli kama alivyoziweka.

“You have got a job,” akazinong’oneza. Kisha akaufunga na kuurudisha mahala pake. Akaitazama saa yake mkononi ikamwambia ni saa nne za usiku.


ITAENDELEA
 
Gina alijisikia vizuri kiasi chini ya matibabu ya hali ya juu kutoka kwa Dr. Jasmine, aliweza hata kusimama na kutembea kidogo japo alilalamika kuwa kichwa ni kizito sana. Kila mtu alifurahi.

“Walinipiga kichwani kama si rungu basi gongo kubwa sana, niliona sayari zote tisa kisha giza,” akamweleza Jasmine, “Kamanda Amata yuko wapi?” akahoji.

“Yupo, yeye ni mzima na sasa yupo kazini kama kawaida,” Jasmine akamjibu.

“Dr Jasmine, wale jamaa ni wauaji, naomba nikamsaidie Kamanda, atakuwa matatani sasa,” Gina alikuwa akiongea kama anayeweweseka.

“Hapana, we ni mgonjwa bado, pumzika kwanza,” Jasmine alimshika mkono na kumlaza kitandani kisha akamchoma sindano ya usingizi ili apate kumpumzisha mwili wake, Gina akalala fofofo.

Simu ya mezani ikaita kwa fujo, Dr. Jasmine akaiwahi na kuiweka sikioni.

“Hello!”

“Yeah, unaongea na Kamanda Amata, Chiba yuko wapi? (…) mwambie afanye juu chini anione usiku huu nina shida naye nyeti sana”.

“Umesomeka Kamanda,” Dr Jasmine akajibu na kukata simu.


CLUB BILICANAS – saa 6:23 usiku

KULIKUWA NA WATU WENGI kila kona ya jumba hili la starehe, jumba linalotikisa jiji zima la Dar es salaam kwa umaarufu wake. Wavulana wa kisasa na wadada wao walijazana, wanaocheza disco twende wanaovuta sigara au bangi sawa tu, wanaouza miili wakiwa nusu uchi kila kona walikuwa wakijivinjari kutega mawindo yao. Hapa ndio palikuwa mahala pa kila uovu, wapo waliokuwa wakipanga mbinu za kuvunja, kutia mimba, kutoa mimba na kila jambo lilizungumziwa humo.

Akiwa ndani ya suruali yake ya cadet nyeusi, fulana nyeusi na kizibao cheusi juu ambacho ndani yake kilisheheni zana za kijasusi za kuua na kutoa pumzi za watu, kwenye soksi zake akiwa kabana bastola mbili, moja huku na nyingine kule, akapanda juu ya kiti kimoja kirefu, kati ya viti vingi vilivyokuwa hapo mbele ya kaunta hiyo kubwa ya kisasa, akiangalia kushoto, na kulia kila mmoja alikuwa na kinywaji kizito mkononi mwake, ama akinywa yeye au akimnywesha binti aliyekuwa naye hapo, kisha wanapigana mabusu. Akawatazama kwa wote kwa tuo, akawaona jinsi walivyo safi, hakuna mwenye mawaa yoyote zaidi ya funguo za gari mfukoni au sarafu za mia mia na mia mbili mia mbili, akatabasamu, akaishusha miwani yake na kuiweka kwenye mfuko wa kile kizibao, kisha akatoa kofia pama yake iliyokunjwa huku na kule kama ya Marlboro, mandevu yake yalimfanya aonekane kama jambazi sugu. Kila mtu alimgwaya kwa mawazo kama si kukaa mbali naye.

Kama kawaida ya warembo, mmoja akajipitishapitisha ili apate chochote kwa mtu huyo, lakini kama angejua kuwa mtu mwenyewe kaja kwa kazi zake asingepoteza muda.

“Unataka nini?”kamwuliza yule binti.

Binti akamtazama usoni mtu huyo na kumrembulia macho.

“Sihitaji hiyo biashara, chukua unachokunywa upotee,” yule mtu akamwambia yule binti, kisha akageukia kaunta.

Nipe Tonic Water na Konyagi ndogo, usisahau vipande vya barafu,” akaagiza, na kinywaji kikaletwa.

Mara akahisi anaguswaguswa mgongoni, akaelewa maana yake nini, akainua glass na kujimiminia kinywani, kisha akateremka na kuacha vinywaji pale kaunta na noti ya elfu kumi, akamfuata huyo aliyemgusa. Wakatoka pamoja mpaka nje. Wakaingia kati kichochoro kimoja.

“Kamanda! Hata mimi sikukujua,” Chiba alizungumza.

“Kawaida tu, leo nina kazi kubwa kaka, nataka uwe nami,” Kamanda Amata akamwambia Chiba.

“Usijali nipo jirani yako,” akaingiza mkono katika kimkoba chake, akatoa bastola moja nyeusi safi kabisa, ukiitazama unaweza kusema ni ya plastiki. Kamanda akaitazama, akatikisa kichwa.

“Ya Kirussia,” akatamka.

“Ndiyo, lakini nimekaa chini nikaimodifai tena, sasa ni ya Kitanzania,” aliposema hayo Chiba waote wakacheka, “tazama hapa,” akashika katikati mahala kwenye tumbo panapojaa risasi kabla hazijafyatuliwa, akapazungusha kwa namna yake na kufyatua kitu kama pini akakiamishia mahala pengine lakini vyote hivyo alivifanya kwa mkono mmoja.

“Ukishaweka hapa, Kamanda, Umejiua!” akamwambia. Kamanda Amata akaitazama na kujaribu kufanya vile alivyoambiwa, “safi sana Chiba, tunajivunia kuwa na mtu kama wewe.” Akaipachika ile bastola katika kizibao chake.

***

Majira kama ya saa saba hivi, Amata alikuwa akiambaa ambaa na korido za maduka na maofisi, akaufuata mtaa wa Samora na kuipita picha ya Askari akaikuta barabara ya Pamba na kukunja kulia, kisha akaingia kwa ndani kidogo akapita kituo cha mafuta na kuibukia katika ukuta wa hoteli anayoitaka, Motel ya Agip.

Kama mwenyeji, aliingilia mlango wa nyuma ambao hutumika na watu wa usafi kuingilia ndani, akapenyapenya mpaka alipoukuta mlango wa pili akautikisa umefungwa, akachukua funguo zake na kuchezesha kidogo tu, mlango ukakubali, alipoufungua ili apite, kulikuwa na watu wanatokea upande huo, akaurudishia na kujibana nyuma yake. Walipopita naye akafuata, viatu vyake havikufanya kelele hata kidogo, akazikwea ngazi mpaka mlango namba 206. Akasimama kwa sekunde kadhaa, akatzama huku na huko, hakuna mtu, zaidi ni miungurumo ya mashine za kupoza hewa zilizokuwa zikiunguruma ndani ya vyumba hivyo, ukiacha hiyo ni sauti za watu walio kwenyea raha zao, wakipiga kelela za malalamiko ya raha. Akachukua kamera ndogo yenye umbo ka waya na akaipenyeza kwenye tundu la ufunguo mpaka upande wa pili, akapiga picha na kuitoa, akachomeka katika simu yake na kutazama, ndani kote ni salama, hakuna mtu. Akairudisha, akatia funguo na kuufungua mlango na kuingia ndani. Alipohakikisha kila kitu kipo sawa, na usalama wa kutosha, akavuta kiti akaketi nyuma ya mlango akitazama kitandani, pembeni akajiwekea pombe kali akinywa.

Mwanga hafifu ulikuwa ukimulika ndani ya chumba hicho, akiwa kajibana nyuma ya mlango kwenye kiti kidogo, akachomoa bastola yake kwenye soksi, akaiweka chini sakafuni kisha kwenye kizibao chake akatoa kiwambo cha sauti akaichukua ile bastola na kuifunga barabara ili isilete kelele itakapokuwa kazini. Akaitazama saa yake, inakimbilia saa nane usiku.

Mara akasikia sauti ya viatu ikija upande huo kutoka kwenye korido upande wa nje, akaiinua bastola yake na kuiweka tayari, lakini akili yake ilitambua kuwa sauti ya viatu hivyo ni kama vya kike na pia mwendo akautambua kuwa ni wa kike, akasubiri aone maana alijua wazi kuwa Mc Field ana uwezo wa kujifanya hata Mwanamke ili tu atimize lengo lake.

“Ulinitoroka kipindi kile leo huchomoki,” akajisemea huku akijikuta hasira zikimtawala taratibu. Mara funguo ikapachikwa katika tundu lake, ikafungua mlango, Kamanda Amata akatulia kungoja kuona nani anayeingia.

Mwanamke, aliyeonekana kama Mwarabu, mweupe, mrefu kiasi, mikononi alikuwa na mkoba, vazi jeusi linalometemeta lilikuwa limefunika mwili wake juu kabisa ya mapaja na kuishia juu kidogo ya matiti. Kamanda Amata akameza mate, kisha akalegeza mkono ulioshika bastola yake. Yule Mwanamke akaiendea swichi, alipotaka tu kuwasha, akashangaa taa ile inawaka sekunde mbili kabla yeye hajawasha, akashtuka. Mara akasikia kitu kama glass ikiwekwa mezani, akageuka na kukutana uso kwa uso na domo la bastola ya Amata. Mwanamke yule akaanza kutetemeka.

“Usiniue nakusihi!” aliongea kwa sauti ya woga na kubembeleza.

“Huwa siui warembo kama wewe, jibu maswali yangu mawili tu,” Kamanda akamwambia huku akiweka sawa kofia yake aina ya pama kichwani, “wewe ni nani?”

“Aaaa! Aaaa! mimi naitwa Amba,” akajibu, lakini lafudhi yake ilionesha kabisa kuwa hakuwa Mtazania.

“Swali la nyongeza kabla ya la pili, unatokea wapi na unafanya nini hapa?” akamuuliza.

“Mimi natokea Afrika ya Kusini, nipo Tanzania kwa miaka miwili sasa, nafanya kazi Las Vegas Cassino, huyu ni mteja wangu tangu afike hapa miezi mine ilopita, huwa nakuja kumstarehesha kwa ujira mnono, nafikiri umenielewa, niache niende,” akajibu haraka haraka huku akirudishia viatu vyake miguuni tayari kuondoka.

Amata akamuoneshea ishara ya kuwa hawezi kuondoka.

“Swali la pili, mteja wako yuko wapi?” akamhoji tena.

“Anakuja, amesema kuna kazi anamalizia kufanya lakini anakuja akanambia mimi nitangulie huku anikute,” akajibu kwa ufasaha.

“Good girl, sasa huwezi kuondoka, panda kitandani umsubiri mteja wako, tena tulia kimya, lete mkoba wako hapa,” akamwamuru, yule Mwanamke akaupeleka mkoba, Kamanda akaukagua ndani, akakuta vipodozi, simu, pedi, helleni, pete ya dhahabu na mikufu, bangili za kisasa, kitita cha pesa za kigeni na funguo za gari.

“Ok,” akauweka ule mkoba chini huku mkononi akiwa kabaki na simu ya yule Mwanamke, “Msubiri mteja wako kama ulivyopanga kumsubiri,” akamwambia. Lakini yule Mwanamke akabaki haelewi anachoambiwa.

“Huelewi? Vua nguo zako panda kitandani jifunike umsubiri, mi sina shida na wewe nina shida na mteja wako ambaye hata mimi ni mteja wangu vilevile,” akamwambia. Yule mwanamke akavua kigauni chake, akabaki na sidiria nyeusi, na chupi mchinjo ya rangi hiyo hiyo. Akavua sidiria, lo, Amata akaona akili ikimwenda mbio maana titi zilizojaa vizuri zilikipendezesha kifua chake, wekundu wake uliweza kumfanya Mwanaume yeyote rijali apate shida katika suruali yake, akaondoa na ile chupi akabaki kama alivyo, Kamanda Amata alilisanifu umbo mwororo la Amba. Yule Mwanamke akapanda kitandani na kuvuta shuka mpaka kidevuni, Amata akazima taa.
 
Majira ya saa tisa usiku, Kamanda Amata alihisi mlango ukitikisika, mara ukafunguliwa kwa kasi kwa minajiri ya kumbamiza pale alipo. Mc Field aliingia haraka bastola mkononi na kuwahi kutazama nyuma ya mlango, hamna mtu, isipokuwa chupa ya pombe na bastola.

“Shiit!” akashangaa na kutamka kwa sauti ya chini. Wakati huo Amba nae alikuwa amekurupuka kwa kishindo kile.

“Tulia vivyohivyo, umeingia mikononi mwangu tena,” Sauti ya Kamanda ilisikika nyuma yake.

Kumbe Kamanda Amata baada ya kuhakikisha kuwa Amba amepitiwa na usingizi alitoka pale alipo na kujificha bafuni akiwa amejua wazi hila za adui wake kwani alishajua kwa vyovyote huko aliko anafuatilia mazungumzo yake na mwanamke huyo, na alijua kwa vyovyote atajua ni wapi alipokaa kutokana na vyombo vyake vya mawasiliano jinsi alivyoviunganisha. Mc Field alijikuta hana ujanja, amewahiwa, akataka kugeuka kumtazama mtu huyo.

“Tulia, weka bastola yako chini. No! No! usiiname irushe chini,” akamwambia, maana alijua kujitikisa kidogo mtu huyo anaweza kuleta madhara makubwa, “safi sana, umekuwa kijana mpole sana siku hizi na si mtukutu kama zamani,” maneno hayo ya dharau yalimtia hasira Mc Field. Alitamani amrukie Amata lakini alijikuta hana ujanja, alibakiwa na mbinu moja tu na alikuwa akitafuta jinsi ya kuitumia.

“Geuka, mikono yako ikiwa juu,” akamwamuru. Mc Field akageuka.

“Ha ha ha ha leo una sura ya Kihindi, hivi wewe kwa nini umekuwa mwoga namna hiyo siku hizi? Umeanza kuzeeka ee? Basi leo ndiyo mwisho wako, roho yako nitaitia kwenye mfuko wa ruruali yangu. Nani amekutuma kuja huku tena? Kufanya nini?” akamtupia maswali baada ya kumkejeli.

“Hilo hupaswi kujua mbwa mweusi kama wewe, waume zenu wanaowalisha ndiyo walionituma, nimetumwa kuua, kukuua wewe!” alipojibu tu, akashusha mkono haraka, Kamanda Amata alikuwa keshaona hiyo, aljirusha akabiringita upande wa pili wa chumba, risasi nyembaba ikapiga kwenye kabati la vioo likatawanyika. Amata akajinyanyua haraka, alipotulia tu, ngumi kali ya Mc Field ikatua shavuni, ya pili ikadakwa sawia.

Amba alikurupuka kutoka pale kitandani akajikunyata kwenye kona ya chumba. George Mc Field akatumia kichwa kumpiga Amata, Amata akamwachia ule mkono, akayumba na kuanguka chini, akajibamiza ukutani, akamwona Mc Field akimjia na kisu mkononi, akavuta stuli ndogo na kuirusha kwa mikono ikampiga Mc Field usoni, kisu kikamtoka mkononi. Kamanda akanyanyuka, akapiga round kick, miguu yake ikamchapa Mc Field sawia kichwani ikampeleka mpaka kitandani. Mc Field akajirusha upande wa pili wa kitanda kulikuwa na ua la plastic lililowekwa katika bilauri kubwa la kioo, akaliinua na kwa kutumia mkono wake wa kulia uliojaa vizuri akalirusha kwa Amata. Hakika kama angekuwa mtu wa kawaida bilauri lile lingemuumiza vibaya lakini Amata alilipiga kiustadi kwa mikono yake na likatawanyika vipande vipande, akamwona Mc Field hewani akija kama Mbogo aliyejeruhiwa, Amata akamuepa, jamaa akatua chini peke yake.

Mzungu huyo akatega mikono yake katika mtindo mahili wa kung fu kumkabili Amata, miguu yake aliipanga katika namna ya kupendeza na mikono yake ilizunguka taratibu ikionesha jisi pigo lijalo litakavyomaliza kazi. Usoni mwake tayari damu zilikuwa zikitiririka. Kamanda Amata naye akaweka mtindo mwingine wa Kung fu naye akasimama kwa namna yake kumkabili Mc Field, hakuna aliyetabasamu wala kucheka, kila mtu alikuwa na ‘pepo la mauti’.

Amba, alinyanyuka pale kwenye kona na kuiwahi bastola ya Mc Field iliyokuwa chini, Kamanda Amata akaona hilo, alipogeuka kidogo tu, maana alijua hatari inayokuja, alijikuta akipata mapigo matatu ya Kung fu ambayo hakuweza kuyakinga hata kidogo, maumivu makali yakalifikia bega lake akahisi kama limevunjika. Mc Field akaanza kumpelekea mashambulizi ya haraka haraka ambayo yalimpoteza kabisa Amata, akaanguka chini kama gunia la karanga, akajigeuza na kulala kifudifudi.

“Mwisho wako umefika, unafikiri kila mtu ni wa kuchezea, sasa leo Tanzania itakuomboleza wewe na Rais wako,” Mc Field alimwambia Amata kwa hasira huku akiuma meno, alikuwa akimsogelea taratibu pale alipo.

“Inuka, nikumalize, mbwa mweusi we! Akamkamata ukosi wa kizibao alichovaa na kumburuza, nitakuuwa kwa kukuchinja, nitatenganisha kichwa na kiwiliwili chako,” alimwambia huku akimburuza kumpeleka bafuni. Amata alikuwa hoi, mkono wake ulikuwa umevimba, damu zikimtoka upya kwenye jeraha lake, lakini hakuona haja ya kuuawa kikondoo. Aliukamata mguu wa Mc Fiel kwa mkono uliobaki, Mc Field akashtuka na kuinama kumtazama, kwa kutumia mkono uleule uliovimba alimdaka shati na kumvuta mpaka chini kisha akamshindilia konde zito la kwenye koromeo, Mc Field akalegea na kukohoa sana.

“Vipi?” Madam S aliuliza.

Chiba akamtazama kabla ya kumjibu, “saa kumi inakaribia,” akajibu. Scoba bado alikuwa kwenye usukani akiendesha taratibu.

“Gari ya Mc Field hii hapa maegeshoni,” Chiba akamwambia Madam.

“Kamanda yuko kwenye mtanange,” akamwambia Madam S huku akiweka bastola yake vyema, “nisubirini hapa,” akawaambia Scoba na Madam S.

Utulivu ulitawala katika mitaa ya katikati ya jiji, na hata katika Motel. Hata wahudumu wa mapokezi walionekana wanasinzia kwenye makochi wakiangalia TV, hakuna aliyejua wala kuhisi nini kinatukia muda huo ghorofa ya pili, ya jengo hilo. Maana mapambano ya watu wazima yalikuwa ni mapambano ya kimya kimya.

Madam S alikuwa na mawazo mengi sana usiku huo, maana alijiuliza maswali yasiyo na majibu, umri nao ulimfanya ashindwe kupata majibu ya haraka haraka. Alikuwa ametulia tuli katika gari kiti cha nyuma.

“Bora hata sikuwahi kuolewa!” akasema. Scoba akamtazama na kucheka, “kwa nini?” akamwuliza.

“Namna hii si ngeshaachika maana hata huyo mume angenipa talaka, saa tisa hii mwanamke niko nje sihudumii ndoa,” akaongea huku akicheka.

“Hivi Madam huna hata mtoto wa dawa?” Scoba akauliza.

“Ninao!” akajibu.

“Wangapi?”

“Watano,”

“Watano!” Chiba akashangaa.

“Ndiyo, watano, wa kike wawili na wa kiume watatu ila ni watukutu balaa, ndio wananifanya mi nisilale mpaka sasa,” akawajibu. Wote wakacheka kizungu bila kutoa sauti.

Chiba akiwa katika kujiandaa kuelekea katika ile motel, mara walisikia sauti ya kioo kinachovunjika na sekunde chache kitu kama jiwe au furushi kilitua juu ya gari moja iliyokuwa imeegesha upande mmoja wa motel hiyo.

“Nini ?” Madam akauliza. Akaivuta bastola yake na kuelekea kule alikoenda Chiba, Scoba alibaki nje ya gari akitazama lakini akiwa tayari kwa lolote.


Amata akatazama dirisha lililopasuka ambalo Mc Field alipita hapo baada ya kuchezea kichapo kikali.

Baada ya kumshindilia lile konde pale chini, Mc Field alijifanya bado ana uwezo mkubwa wa mapambano, ndipo alipojikurupua na kumbwaga Amata kando, lakini kabla hajajiweka sawa, alichezea karate kali zenye mapigo ya kifo kutoka kwa Amata kiasi kwamba aliona hawezi kujitetea hasa alipopigwa pigo kali na kuvunjwa mbavu tatu, aliamua kujiokoa kwa kujirusha dirishani lakini hali yake tayari ilikuwa mbaya.

Akarudisha macho kwa yule mrembo, Amba, “vaa nguo zako!” akamwambia huku akijitazama ule mkono uliovimba. Amba akavaa harakaharaka. Saa ya Kamanda Amata ikaanza kumfinya mkononi, akaingiza mkono kwenye moja ya mifuko ya kizibao chake na kutoa kifaa maalum cha mawasiliano.

“Yes!” akatamka.

“Tupo, tumefika!” ilikuwa sauti ya Madam S.

“Ok, kama unaweza panda 206 haraka uone cha kuona. Chiba hifadhi huo mwili kama hauna uhai,” akamaliza.

“We mwanamke, usipende kuwa na wapenzi usiowajua, angekuua huyu, ni jambazi,” Amata akamwambia Amba.

Mlango ukagongwa na Madam S akaingia.

“Pole Kamanda, naona mkono wako umepata shida,” Madam alisema.

“Ndio, nahisi kama mifupa imepishana,” akajibu.

“Scoba akuwahishe kwa Jasmine ukapate matibabu, hili la hapa niachie mimi na Chiba,” Madam akamwambia Amata.

“Sawa!” akajibu na kumtazama yule Amba, “twende huku,” akamwamuru huku moyoni akimmeza mate.

Madam S ndipo akagundua kuwa kuna mtu wa tatu mle ndani, akamtazama binti huyo kwa tuo, “nani huyu?” akauliza.

“Ah, wafanyabiashara hai,” Amata akajibu huku akimswaga nje Amba. Wakafika mahali pa mapokezi wakakutana na mhudumu wa hapo. Kamanda Amata akamatzama bila kuongea kitu.

“Unalala sana, unaweza kuvamiwa na kuuawa hivihivi!” akamwambia, “haya, sasa hakuna kupokea wageni kwenye hotel hii mpaka mpate kibali kingine cha serikali, tunaiweka chini ya uangalizi kwa masaa machache na kufanya ukaguzi wa chumba kwa chumba naomba uhakikishe wageni wote wasitoke kuanzia sasa,” Kamanda akatoa amri huku akimwonesha kitambulisho uinspekta wa polisi.

“Sawa, lakini ni swala la kumwambia meneja, maana wengine wana ndege alfajiri hii,” yule mhudumu akamwambia Amata.

“Mpigie simu meneja mwambie afike hapa haraka,” alipomalisa kusema hayo akaongoza nje, akamchukua Amba na kumtia kwenye gari.


“Ulifikiri safari hii utatoroka tena? Utafia hapa hapa,” alimwambia Mac Field aliyekuwa hoi na pingu mkononi ilhali mnyororo miguuni mwake.

“Mtie kwenye buti,” Kamanda akamwambia Scoba, Mc Field akatiwa kwenye buti ya gari, kisha yeye na Amata wakaingia ndani.

“Shamba,” akamwambia Scoba.

“Na huyu mwanamke?” akauliza.

“Hapana, huyu tunamtupa shimoni hapo mbele,” Amata akajibu na gari ikaondolewa, mtaa wa kwanza, wa pili.

“Simama hapa,” akamwambia Scoba kisha akamtazama Amba, “teremka, ondoka na usimsimulie mtu chochote ulichokiona,” akamwambia kisha akaketi vizuri. Amba akateremka na kukimbilia mitaani.


Gari ya Scoba ikaegeshwa vizuri mahala pake, Kamanda Amata akateremka na kufungua buti, wakamshusha Mc Field kisha wakamkokota na kumwingiza kwenye chumba kimoja kisicho na madirisha wala ndani hakikuwa na chochote isipokuwa sakafu na choo tu.

“Kaa humu, nakuja unijibu maswali yangu kabla sijakuua,” Kamanda akafunga mlango kwa namba maalumu.

Dr. Jasmin akampokea Kamanda na kumpa tiba zote zinazowezekana, akamfunga bendeji maalum mkononi na kumwekea kamba ya kuvalia shingoni.

Dakika arobaini na tano baadae, Madam S na Chiba waliwasili, wakiwa na begi moja na suitcase kubwa, wakaliweka mahali. Kisha likafunguliwa kila mtu akiwa anaona.

“Mnaona kazi hii?” Madam aliwaeleza vijana wake. Ndani ya begi hilo waligundua vitu vingi sana vinavyotumika kujibadili sura, dawa za kunenepesha kwa muda mfupi na kukondesha kwa muda mfupi, vitambulisho zaidi ya hamsini vya idara mbalimbali kilichowagusa zaidi ni kile cha dereva wa Rais, hati za safari za nchi mbalimbali, maburungutu ya Kitanzania na za kigeni, silaha za kila aina, bastola, viwambo vyake na silaha nyngi za kijasusi.

“Hii ni hatari sana,” Gina aliongea kwa sauti ya chini. Wote walibaki midomo wazi, begi hilo lilikuwa limetengenezwa kwa malighafi ambayo ukilipitisha kwenye mashine za ukaguzi zinazotumia x-rays itakuonesha tu ndani kuna nguo na vitabu hata kama ndani hamna kitu, na hii ilimfanya mtu huyu kuweza kupenya kwenye vizuizi vya viwanja vingi vya ndege.

“Kamleteni hapa!” Madam akatoa amri. Chiba na Scoba wakaenda kwenye kile chumba kumleta Mc Field, wakamkamata huku na huku na kwenda naye. Wakamtupa sakafuni na kuchomoa bastola zao, risasi ya kwanza ya Chiba ikapiga kanyagio la mguu wa Mc Field, yowe la maumivu likamtoka.

“Sasa tutuambie lengo zaidi la kuja hapa ni lipi, na nani kakutuma?” Kamanda Amata alimwuliza Mc Field aliyekuwa akigugumia kwa maumivu ya mguu wake pamoja na mbavu zake, hakujibu kitu.

Amata akamwendea pale chini, “hutaki kujibu sio? Niambie aliyekutuma na madhumuni yakuja hapa”. Badala ya kumjibu akamtemea mate usoni. Amata akashikwa na hasira, akampiga teke la kilo nyingi na jamaa akarudi chini chali, akatulia tuli huku povu likamtoka mdomoni.

Chiba akamuwahi na kumbana mashavu yake kwa vidole, maana alijuwa kuwa tayari mtu huyo anajiua kwa kidoge cha sumu. Hakuna aliyemwona wakati gani kameza kidonge hicho.

“Shiiit!” Chiba akapiga ukelele alipomwona mjinga huyo keshalegea na macho kumtoka, akawatzama wenzake waliokuwa kimya, “limejiua!” akasema.

“Awasalimie babu zake,” Madam S akasema.

11

ONTARIO – CANADA

WAKATI HUKU KWETU ILIKUWA ni alfajiri ya saa kumi kule kwao ilikuwa saa mbili usiku. Sir Robinson Quebec alikuwa akiweka sawa miwani yake akiwatazama wale washirika wake wa karibu sana katika sakata lao hilo. Kila mmoja likuwa na shauku ya kusikiliza nini kimejiri huko Afrika Mashariki.

“Usiku wa manane, ambapo kule ni asubuhi ya saa nne, ukurasa wa mwisho wa mkataba wetu na yule mheshimiwa utafungwa,” akawaambia.

Yule mjumbe mweusi naye akatoa taarifa yake, “Na pia alfajiri hii kutafanyika tukio lingine katika mgodi wa Tanzanite kule Mererani kwa kupata kasha zingine tano za madini hayo, kila kitu kipo sawa unasubiriwa muda tu”.

“Kwa ujumla tumepata ushindi kwa kutekeleza makubaliano ya mkataba wetu, upande mmoja umeshindwa na sisi tunatekeleza kile tulichokubaliana, hakuna wa kutulaumu, kama tulivyofanya Congo, Liberia, hivyo hivyo tu,” akaeleza yule mjumbe wa tatu.

Watu hawa watatu walikuwa ni matajiri sana huko ughaibuni, walifadhili nchi nyingi sana na kutengeneza Marais wengi sana hasa Afrika na Asia wakikuwezesha upate utawala na wao uwape sehemu ya mali asili ili wafaidi, kurudisha gaharama zao na kupata faida juu. Kwa jina lingine ni ‘King Makers’.

Walipanga kukutana siku hii ili kupiga mstari mwekundu kati yao na yule waliyemweka madarakani katika nchi ya Tanzania, kwa kuwa alikuwa amekiuka makubaliano. Waliketi hapo wakisubiri taarifa mbili, moja ni wizi mwingine wa madini huko Arusha Mererani, pili ni kifo cha mtu wao, mteja wao, Rais wa nchi. Kila mara walikuwa wakiangalia saa, masikio yao yakiwa makini kusubiri mngurumo wa simu iliyotegwa mezani hapo.

IKULU saa 4:00 asubuhi

NJE ya jengo la Ikulu, Makao Makuu ya Rais kulikuwa na watu wengi wakiwa kwenye viti na wengine wakiwa wamesimama hapa na pale. Walijulikana kuwa ni waandishi wa habari kwa kamera walizokuwa wamebeba mabegani mwao, wengine wakionekana kuandika hiki na kile. Bado katika lango kuu kulikuwa na wengine wanaongia, wakikaguliwa kila kona na vijana wa jeshi la polisi na askari kanzu waliowekwa hapo kuhakikisha ulinzi unakuwepo.

Watu wa televisheni nao walitega kamera zao hapa na pale ili kuhakikisha wanapata picha nzuri kadiri iwekanavyo, wakirekebisha vinasa sauti vyao na huku magari yao makubwa yenye mitambo ndani yake yakiwa tayari kupeleka maangazo hayo moja kwa moja kwa wananchi.

Huko majumbani nako kila mmoja alifanya kazi harakaharaka ili awahi kutazama au kusikiliza nini Rais wa nchi anataka kuliambia taifa. Na hali hii ilitokana na utata wa mambo makubwa mawili, kudunguliwa msafara wa Rais kule Bunju na wizi wa almasi uliofanyika Mwadui ukimhusisha Waziri wa Nisahati na Madini. Ilikuwa siku ya aina yake. Kila mtu aliisubiri saa nne na nusu ifike. Kwenye migahawa, mabaa, maofisini wote walikuwa tayari kusikiliza hotuba ile, na kila mmoja akisubiri jibu la maswali yake.


Kila mtu alikuwa tayari kajipanga kwa tukio hilo, hawakuwa na amani kabisa ijapokuwa Mc Field alikuwa tayari marehemu lakini bado hawakufanikiwa kumpata mshirika wake.

“Nina wasiwasi anaweza akafanya maajabu hapa,” Kamanda Amata akawaeleza wengine.

“Ndio, daima inabidi tuwe katika tahadhari,” Chiba akaongezea. Punde tu Madam S akawasili ofisini.

“Poleni najua mmenisubiri sana lakini foleni za jiji letu mnazijua na sote ni wahanga, haya bila kuchelewa, si mnajua Mkuu atahutubia asubuhi hii? Basi tujiweke tayari. Chiba kazi yako unaijua, hakikisha unakamata mawimbi yoyote ya sauti chochote katika maeneo hayo, hakikisha unakata mawimbi yote ya simu kilomita nne za mraba. Scoba utakuwa tayari kuratibu usafiri kama itahitajika, Gina unajisikiaje sasa?” Madam akakatisha maelekezo.

“Niko sawa Madam,” Gina akajibu.

“Ok, Gina na Kamanda nawarudisha katika kazi yenu, mtakuwa kwenye viwanja vya Ikulu kuangalia kila kinachoendelea, mimi nipo hapa wala sitoki, mawasiliano yasikatike mpaka itakapoamriwa. Chiba kumbuka usikate frequency tunayoitumia, sawa?” Madam akamaliza.

Wote wanne ukimuacha Jasmine ambaye alibaki ofisini na Madam, walichukuwa vifaa vyao vya mawasiliano na kupachika masikioni, wakajaribu vyote na Chiba akawapata sawia kabisa, wakabeba bastola na vifaa vingine muhimu katika kazi zao kadiri walivyoweza.

Taksi yenye rangi ya kijani, ilisimama karibu kabisa na lango la Ikulu, eneo ambalo liliandaliwa kwa waandishi wote kushuka hapo. Mwanamke mwenye shepu tamu kwa kuiona kwa macho aliteremka akiwa na video kamera kubwa mkononi mwake, akalifikia lango akasimamishwa kwa ukaguzi. Ndani ya chumba kidogo alikaguliwa na kuonekana yuko sawa hakuwa na silaha wala kitu chochote cha hatari. Kitambulisho chake kilionesha kuwa ni mwanahabari kutoka kituo kikubwa cha luninga duniani NBC. Akapita na kuungana na waandishi wengine.

Katikati ya kamera nyingi akaweka ile ya kwake na kuhakikisha amekwishaiweka sawa kwa kazi.


Saa nne na nusu kama ilivyopangwa, Rais wa Jamhuri alijitokeza na kukaribishwa kwa makofi baada ya kutoonekana kwa takribani siku tano.

Mbele ya jopo la waandishi na wanausalama, Rais alianza kutoa hotuba yake iliyojawa na maneno mazuri na matamu.

Tracy Tasha aliingiwa na wasiwasi, kila alipojaribu kumtafuta Mc Field hakumpata simuni, mpango waliopanga ilikuwa wakutane hapo, lakini alishangaa kutomuona swahiba wake, akajua kwa vyovyote atakuwa tayari katika kona aliyomwambia atamkuta. Kupitia kamera yake alikuwa akiitembeza kuangalia wote waliokuwa mbele, licha ya Rais na walinzi wake walioonekana kuwa makini katika kutazama huku na kule, alimwona mtu ambaye alimfanya moyo wake ulipuke.

Kamanda Amata alisimama pembeni kabisa mwa jukwaa kuu, akiwa na ile plasta yake kubwa mkononi na mkono huo kuuning’iniza shingoni, Tracy akatabasamu, akajua hapa hana mkono mmoja hawezi chochote. Akatazama na wengine wote akaona walivyojipanga na jinsi walivyojiweka bastola zao ndani ya makoti yao. Tracy alitazama tena kwa makini sana hali nzima ya usalama, akaangalia wapi na wakati gani ataweza kuifanya kazi yake, akakumbuka maelekezo ya Mc Field wapi pa kutokea pindi akikamilisha hilo.


Kamanda Amata, alitulia kama sanamu, macho yake yaliyofichwa kwa miwani nyeusi yalikuwa yakimtalii kila aliyekuwa mbele, ilikuwa ikipiga picha, ikivuta na kurudisha na kuhifadhi katika kadi sakima ndogo iliyokuwa imepachikwa katika kona moja ya miwani hiyo.

“Point one, ova!” Chiba akaita

“Point one, Clean, ova!” sauti ya Kamanda Amata ikajibu na wote wakaisikia vizuri.

“Point two, ova!”

“Point two, Clean, ova!” Gina akajibu kutoka juu dirishani ambapo aliweza kuwaona watu wote kwa chini.

Chiba alikuwa akiangalia kila tukio kupitia luninga zake ndogo ndani ya gari aliyoiegesha nje ya ukuta wa Ikulu, picha zote alizipata kupitia miwani ya Gina na Amata. Alikuwa akikamata mawimbi mbalimbali ya mawasiliano yaliyokuwa yakikatisha eneo hilo, alizima mawasiliano yote ya simu kilomita nne za mraba, aliweza kuchuja kila frequency inayokatiza usawa wake. Tracy aliiangalia saa yake mara kwa mara. Kitendo hicho kilimfanya Kamanda Amata kumuona na kumtambua, aliishika miwani yake na kumvuta karibu, picha yake haikuwa ngeni hata kidogo.

“Ground zero! Ground Zero! Ova!” akaita. Chiba akaipokea na kutazama kwenye kijiluninga chake, akaona sura ya Tracy Tasha akiwa nyuma ya kamera kubwa ya video.

“Roja, point one kazini, Ova!” Chiba akaita lakini ilikuwa ni kupeleka ujumbe.

“Copy, point one kazini, ova” Kamanda akajibu.

“Point two, stand by! Ova” Chiba akatoa ujumbe tena.

“Copy, point two standby, ova!” Gina akajibu, akashusha mkono chini na kuinua bunduki aina ya SR 25 iliyotengenezwa huko USA. Bunduki ya maana, maalumu kwa kudungua, ilibuniwa na Eugene Stoner yenye urefu wa inch 44.0. Gina aliipachika dirishani na kuweka jicho lake katika lensi iliyofungwa juu yake na kumwangalia vizuri yule mwanamke.


Tracy Tasha aligeuza kamera yake na kumtazama tena Kamanda Amata, hakumuona. Alihisi akili yake inaganda ghafla, alitazama kwa chati huku na kule lakini hakumuona Amata mahala aliposimama, akahisi kuchanganyikiwa. Hakuhitaji kupoteza muda, hakuona sababu ya hilo, aliigeuza kamera yake kwa Mheshimiwa Rais, akamweka vizuri katika kioo chake cha kuvuta, akakijaza kifua cha Mkuu huyo, kisha kidole chake chembamba kikabonyeza kitufe chekundu cha kuiruhusu kamera hiyo ianze kunasa picha. Kizaazaa.

Ni nukta ileile, Rais alitupwa hewani, walinzi wake walichanganyikiwa, wale wa nyuma walijitahidi kumdaka lakini wote sita wakarudi chini bila kipingamizi, wale wa mbele wakageuka mara moja, na kumwendea Mkuu, haraka sana tayari eneo lile likawa katika hali ya taharuki. Waandishi wa habari walihaha kupata picha ya hiki na kile, askari wa FFU waliingia na kuzingira eneo lile kujua nini kimetokea.

Tracy Tasha, alijishika kiuno katikati ya watu waliokuwa wakihaha huku na kule. Alikuwa akiangalia nini cha kufanya. Macho yake yalitazama juu ya jengo la ikulu na kujikuta akitazama na domo la SR 25, akajua pamenuka, akabinya kijitufe kingine kwenye ile kamera yake na yote ikalipuka na kutoa moshi mzito uliowafanya watu kuchanganyikiwa na kukohoa huku wengine wakitokwa na machozi yaliyochanganyika na kamasi jembamba.

Gina alitoa jicho lake katika lensi ya lile bunduki kwani alishachelewa kupiga, Tracy alipotea katikati ya ule moshi.

“Shiiit! Mwanaharamu wa kike,” Gina aling’aka alipojikuta kazidiwa kete na Tracy. Aliendelea kutazama kwa lenzi mtu mmoja baada ya mwingine huku kinywani mwake akiendelea kutukana matusi anayoyajua yeye mwenyewe.

Kamanda Amata alipata wakati mgumu, alikuwa akimfuatilia Tracy kwa utaratibu maalumu kabla hajafanya kile anachotaka kufanya, mara kizaazaa kilipoanza alijikuta akibabaika, hakujua amuendee Tracy au arudi kumsaidia mheshimiwa, ilikuwa ngumu. Lakini alipokuwa akitafakari hilo, ni nukta hiyohiyo aliposikia kishindo cha pili kilichozua mtafaruku, moshi mzito uliomfanya hata yeye achanganyikiwe ulizagaa.

“Point one, point one!” Chiba aliita.

“Hali tete, mheshimiwa kaangushwa!” kamanda Amata alijibu haraka.

“Man down!” Chiba alipigwa na butwaa.

“Ametoroka! Ametoweka!” Gina alipeleka ujumbe.

Kamanda Amata bastola mkononi, alihaha kutafuta huku na kule akiwa tayari ameweka miwani yake usoni ili kumtambua mtu huyo hakumuona.


Madam S alikurupuka katika kiti chake, “Jasmin, nifuate haraka chukua silaha!” akatoa amri nia Dr. Jasmine akafanya hivyo, hawakuwa na haja ya kutumia gari.

“Vipi Madam, kuna nini?” akauliza.

“Mkuu wa nchi amedunguliwa,” akajibu huku akimalizia kuchomeka bastola katika kiuno cha suruali yake ya suti. Wakatoka nje na kuvuka barabara, kizaa kilionekana, gari za polisi zilikuwa zikipiga ving’ora kwa fujo zikitanda katika njia zote, kila mtu aliye karibu na ukuta wa Ikulu aliondolewa na aliyetiliwa mashaka alitupiwa kwenye gari za polisi. Mitaa ilichafuka, kuanzia Hazina Ndogo mpaka Magogoni kuzunguka mpaka hospitali ya Ocean Road, kwa ujumla kila upande ulimwagwa askari wakipekuwa mpaka kwenye vichaka.

Madam S aliingia getini na kukuta kizaazaa bado kikiendelea, waandishi wote walikamatwa na kuwekwa mahala pamoja. Ilibidi kwa haraka lifanyike gwaride la utambuzi.

Kamanda Amata aliifuata gari ya polisi iliyokuja na mbwa, akamwomba askari mmoja ashuke na mbwa wake. Wakafuatana mpaka pale kwenye mabaki ya kamera ya Tracy, yule mbwa alinusa hapa na pale huku akitoa kilio chake cha ajabu, kisha akaanza kufuata uelekeo fulani, Kamanda na yule polisi walifuatana kumfuata mbwa huyo. Mbwa aliwaongoza mpaka kwenye ukuta, umbali wa mita kama 200 hivi kutoka eneo la tukio, kisha yule mbwa akasimama mahala na kuendelea kunusa hapa na pale bila kwenda popote.


Tracy alipoona tayari domo la SR 25 linamwelekea yeye alijuwa wazi kuwa sasa mambo yameharibika. Kamera yake ambayo ilikuwa na bunduki ndani yake yenye kubeba risasi tatu tu, pia ilifungwa mabomu mawili ya machozi, akayafyatua mara moja, ikatawanyika vipande vipande. Tracy alijiangusha chini na kubiringita kisha akaibukia nyuma ya waandishi wa habari. Wakati watu wakiendelea kukohoa, na kutokwa machozi, Tracy alivuta hatua ndefu na kuufikia ukuta kisha bila hata kuugusa alijirusha sama soti akatua nje ya ukuta huo. Lakini alijikuta na wakati mgumu sana pale alipojua kuwa Mc Field alitakiwa kuwa hapo, hakuwepo. Akachanganyikiwa, hivyo ikabidi ajiokoe mwenyewe kwa nguvu zake, alivuka barabara ya Magogoni kwa haraka na kuingia katika Chuo cha Utumishi wa Umma, akiwa jirani na ofisi za chuo, alikutana na mwalimu mmoja wa kike, akamwita na kumwambia kuwa ana shida naye ofisini, wakaingia.

Tracy alitoka nje ya ofisi hiyo akiwa na mavazi ya yule mwalimu. Wakati wanafunzi na wafanyakazi wakikimbilia mbele ya jengo hilo kujua kulikoni, Tracy alipita katikati yao na kutokomea. Ving’ora vya polisi vilimchanganya kiasi Fulani, alishindwa upande gani aelekee, akapita jengo la kwanza na la pili, akaibukia nyuma, hakuona njia nyingine ya kutoroka, akaivuta hijab aliyoipata kutoka kwa yule Mwalimu, akajiweka vizuri kichwani mwake.


Kamanda Amata akiwa na mbwa wa Polisi, walizunguka nje ya ukuta na mbwa yule akaipata tena harufu ya Tracy na kuvuka barabara mpaka kwenye ofisi za Chuo cha Utumishi, walipoingia ofisini, walimkuta yule Mwalimu akiwa hana uhai, nguo zote za Tracy zikiwa pembeni, na yule Mwalimu alikuwa kama alivyo.

“Shiit! Katuweza, Mtuhumiwa ameruka kihunzi!” aliongea kwenye kinasa sauti chake.

“Lazima akamatwe!” Gina akajibu.

“Point one! Upande wa Mashariki tafadhali, kuna mtu anayejaribu kujipenyeza katika kundi la wachuuzi wa samaki akielekea upande tofauti na wengine wote,” Chiba alitoa hadhari hiyo, akiwa anakamata picha kutoka katika satellite.

“Point One kazini,” Kamanda akajibu.

“Point two, ongeza nguvu tafadhali,” Chiba akaomba.

“Point two kazini,” Gina akajibu.

“Ground zero…. Ground zero…” sauti ya Madam ilifika kwa wote, aliyekusudiwa akajibu.

“Nakusoma,” akajibu Chiba.

“Nipe dira yako!” akamwambia.

“Mashariki, soko la samaki, usawa wa bahari,”

“Copy!” Madam S akajibu.


Tracy, alijitahidi kupenya kwenye kundi la watu kwa minajiri ya kufika baharini, aliamini akifika tu baharini, kamanda na kikosi chake hawatamwona tena kwani mbinu za kutoroka kwa njia hiyo alikuwa akizijua vyema. Kila alipogeuka nyuma alimwona Kamanda Amata akimfuata kwa umakini wa hali ya juu huku mkononi mwake amekamata bastola ndogo sana.

“Hey! Stop!!” Kamanda alitoa amri lakini Tracy hakusimama. Kamanda Amata akpiga risasi hewani na watu wote wakatawanyika, wengine wakianguka chini na kukanyagana vibaya. Tracy akapata kipingamizi kipya, lakini bado hakuonesha udhaifu, alichomoa bastola yake, akageuka nyuma na kumfyatulia Amata, ambaye tayari aliliona hilo, Kamanda Amata akajitupa na kubingirita chini ile risasi ikamkosa na kujeruhi mwingine nyuma yake. Akanyanyuka haraka na kumtazama Tracy, hakumuona.

Akiwa na bastola yake mkononi, akatazama huku na huku.

“Point one, Chumba cha kuhifadhia Samaki,” Chiba akatoa maelekezo kwani alikuwa akiendelea kumfuatilia Tracy kwa mtandao.

“Point one kazini,” Kamanda akajibu huku akiingia katika chumba kikubwa kilichopangwa majokofu mengi makubwa makubwa.

Ukimya ulitawala, harufu ya samaki ilikijaza chumba hicho, kelele za pepezo za pangaboi zilisikika. Bastola mkononi, Amata alikuwa makini kupekuwa uchochoro mmoja baada ya mwingine.


Katika chumba cha siri kabisa, Rais aliteremshwa kwa lifti maalum na kuingizwa ndani ya chumba hicho chenye kila aina ya mtambo tiba kwa huduma ya kwanza. Akiwa na chupa ya maji iliyokuwa ikiendelea kuingia mwilini mwake, alikuwa kimya kayafumba macho yake. Wanausalama wa Ikulu walihaha huku na kule kujaribu kuokoa maisha yake kwa maana walijua wazi kuwa Taifa liko kwenye taharuki kwani hakuna cha kuficha, hotuba ile ilikuwa ikienda moja kwa moja hewani na watu waliitazama kwa televisheni. Walimlaza juu ya kitanda na wote wakasogea pembeni kutazama kinachoendelea maana mshangao na bumbuwazi ulikuwa dhahiri shahiri nyusoni mwao.

Ni siku moja ilikuwa imepita tangu Rais ajiimarishie ulinzi wake binafsi kwa kuifumua idara ya Usalama wa Taifa na jambo hilo linatokea, kila mtu alichanganyikiwa.

Ukimya ulichukua nafasi ya kila kitu katika chumba hicho, watu wachache wasiozidi watatu ukiachana na Daktari walikuwa wamebaki, wengine walitoka nje kuhakikisha mtuhumiwa anatiwa mkononi.

Polisi nao walizingira jengo lote la Ikulu na viunga vyake, barabara za kuingia na kutoka ziloikuwa zimefungwa haikuruhusiwa gari kuingia eneo hilo wala zilizo katika eneo hilo kutoka. Kila kona mbwa wa Polisi walifanya kazi ya kukagua kwa kunusa kila gari na kila mtu. Mbwa hao wenye mafunzo maalum waliweza kutambua harufu ya kitu chochote hatari hususan milipuko.

Madam S, aliingia katika chumba alichokuwa amelazwa Rais, akifuatana na Dr. Jasmine nyuma yake. Mlango mzito ukajirudisha nyuma yao, mlango uliotengenezwa kwa madini ya kutokuingiza risasi. Walimkuta Mheshimiwa amelala kimya kabisa kitandani, daktari akiwa kasimama pembeni.

“Vipi mbona hakuna tiba yoyote inayoendelea?” akauliza.

“Amenipa ishara nimuache,” yule daktari akajibu.

Kisha akamgeukia mtu wa kwanza ambaye ni afisa usalama wa Taifa mwenye mamlaka yote ya juu kwa Rais. Yeye alikuwa amesimama pembeni mwa kitanda, “kinachoendelea?”

“Usafiri unaandaliwa na muda si mrefu tutaondoka kuelekea London kwa matibabu, “ akajibu. Madam S akasimama na kumtazama Mheshimiwa ambaye alikuwa kajilaza kwa utulivu na suti yake ileile ikiwa mwilini, damu nzito iliyoganda juu ya kifua chake ilitengeneza jeraha zito na la kutisha ambalo lilijificha nyuma ya au ndani ya suti hiyo.

Kamanda Amata alijikuta akipewa dhoruba kali ya mapigo ya karate yaliyodhamiria kuua, yakitokea nyuma yake, akayumba na kujiweka sawa, kisha akageuka nyuma na kukutana na mapigo mengine yaliyopigwa kiufundi, haraka haraka na yaliyomchanganya kupita kawaida.

Huyu mwanamke si wa kawaida, akawaza Amata wakati tayari yupo chini akijifuta damu iliyokuwa ikimtoka katika pachipachi za kinywa chake. Tracy akasimama sakafuni kwa mtindo wa kuvutia, akiwa tayari kwa mapigano na kijana huyo mtanashati. Wakati wanawake wenzake walikuwa wakitafuta nafasi ya kufanya nae mapenzi ili tu wajisifie, yeye alikuwa anatafuta nafasi ya kupigana naye. Kamanda Amata alijizoazoa pale chini, alihisi mkono wake kutonesheka tena. Tracy alijirusha kwa namna ya ajabu kwa minajiri ya kutua na shingo ya Amata lakini hapo ndipo alipopajutia. Amata alijitupa pembeni na Tracy akatua peke yake, alipomtazama Amata tayari alikuwa mbele yake; pigo moja la maana likapiga katikati ya sura yake nzuri, Tracy alishuhudia nyota nyingi mbele yake, kabla hajatulia pigo zito la pili likatua mbavuni, Tracy akajikuta analegea, hana la kujitetea. Pigo la tatu lililokuwa linalenga kutoboa tumbo la Tracy na kufumua takataka zote za tumboni, lilikingwa kiustadi sana. Tracy akaunyonga mkoni wa Amata ule ambao umefungwa bendeji ambao mwenyewe aliutumia bila kujali. Akaunyonga kwa nguvu, maumivu makali yakapenya kwenye mishipa ya Amata, akabana meno kwa maumivu hayo, alijifyatua na kupiga kichwa kimoja maridadi, Tracy alihisi kama jiwe limepiga kwenye mwamba wa pua, akamwacha Kamanda na kurudi nyuma, akasimama akihisi kama kitu kinatoka ndani ya pua yake, damu.

Tracy akawa kama mbogo aliyejeruhiwa, sasa alimkamia adui wake, akajiwekea yamini moyoni mwake, ama zangu ama zake. Aliruka na kutua juu ya moja ya jokofu kubwa akinuwia kushusha kipigo kwa Kamanda kutokea juu, lo, alicheza pata potea, kwani hilo adui yake alilitegemea baada ya kusoma macho ya mwanamke huyo kabla, aliunyanua mguu wake na kupiga ngwala moja safi iliyopita millimita chache juu ya jokofu hilo huku mguu mwingine bado ukiwa umesimama juu ya sakafu. Miguu ya Tracy ilitua na kukutana na mguu wa Kamanda Amata. Tracy alijikuta akirudishwa hewani sasa kwa mtindo wa kuangushwa vibaya lakini kwa ustadi wake na ufundi wa mapigano alijigeuza hewani mara ya pili na kupoteza lengo la Amata, akatua chini na kukutana na guu lenye nguvu lililotua kifuani mwake, akatupwa nyuma na kupiga mgongo kwenye jokofu. Alipokaza macho yake ambayo yalikuwa yakipoteza nuru, alimwona Amata bado akiwa kaweka mguu juu, hajaushusha chini.

Tracy alihema kwa nguvu, damu zikiendelea kumvuja puani.

“Umekamatika Tracy Tasha, muuaji mwenye taaluma, na wewe utauawa kitaalamu vile vile na amini usiamini utajiua mwenyewe,” Amata alimwambia kwa Kiingereza safi huku akishusha mguu wake chini.

“Si-we-zi ku-fa ki-ko-ndoo,” alijibu kwa lugha hiyo hiyo, lakini kwa shida sana, sauti yake ilikuwa ikimezwa na maumivu makali.

“Sasa utanyongwa Tanzania, Mzungu muuaji wewe, uliona haitoshi kumuua Khumalo, Touzony na sasa ukaamua kuja Afrika Mashariki? Basi aliyekutuma amekuuza, alijua wazi kuwa hapa ndiyo kaburi lako kama mwenzako Mc Field ambaye tangu jana tayari yuko motoni bila shaka na wewe anakusubiri kule ili mkamuue shetani kama mnaweza kuua,” Kamanda alimwambia Tracy.

Tracy alikunja sura baada ya kusikia kuwa Mc Field alikuwa tayari marehemu, mara picha ya karatasi ya mwili wa Mc Field ikadondoka mbele yake, akaiokota na kuitazama.

“Tunakufahamu sana, na tulikuwa tunakusubiri, Serikali ya Tanzania haiwezi kuangushwa na nguvu yenu vibaraka na sasa utanambia ni nani aliyekupa kazi ili naye nikamshughulikie hata akiwa na ulinzi wa namna gani,” Kamanda alimweleza.

“Maneno mengi hayavunji mfupa,” Tracy alijibu huku akiikunja ile picha na kuitia kinywani. Alifyatuka kutoka pale alipo na kushusha kipigo kizito kwa Kamanda Amata. Kasi aliyokuwa anaitumia Tracy kupeleka mapigo kwa mikono na miguu ilimshangaza Amata. Tangu alipoanza kupambana na watu wenye ujuzi mbalimbali huyu alikuwa tofauti. Amata alikuwa makini, alikinga mapigo yote kumi na nane na hakuna hata moja lililopata, pigo la mwisho Tracy alijinyoosha na kupiga msamba akiwa anakwepa teka kali la Amata ambalo lingetua ubavuni mwake basi bila shaka lingevunja mbavu za kutosha. Akajikuta akimkosa, akajirusha upande wa pili na Tracy aliyedha, aliyenuia kushusha pigo kwenye korodani alimkosa na kujikuta kabaki peke yake. Akanyanyuka harka na kukutana na konde zito la usoni, akapepesuka kidogo kabla hajatulia, konde la pili, la tatu, la nne, la tano, la sita, la saba, Tracy chali, sura ya urembo yote ilikuwa nyekundu.

Akajinyanyua tena haraka na kusaimama wima, akamfuata Amata kwa kasi. Mwenzake akamkwepa na kumtwisha konde la kilo nyingi lililotua tumboni, Tracy akaganda akiwa kajishika tumbo, damu ikimtoka kinywani na macho yakimtoka pima. Kamanda Amata alikuwa katulia palepale, akisubiri Tracy ajibwage chini maana alijua kwa kilo za ngumi hiyo hawezi kupona tena na akipona hatokufa tena.
 
Watu walikuwa wamejazana katika mlango mkubwa wa jengo hilo wakiangalia mapigano yale yaliyokuwa yakiendelea, walishangaa mwanamke huyo alivyokuwa akifanya minyumbuliko ya ajabu katika mpambano huo.

“Huyu atakuwa Cynthia Rothrock huyu!” mmoja akamwambia mwenzake, wengine wakacheka.

Mara ving’ora vya polisi vikasikika kuja eneo hilo, watu wakaanza kusogea nyuma.

“Eeeee wanoko haooo!!!” akasikika kijana mmoja mchuuzi wa samaki.

Gina akiwa na bastola mkononi, alikuwa akikimbia nyuma yake akifuatiwa na Chiba kisha polisi na maafisa wengine wa usalama wote walikuwa wakielekea huko.

Katika soko hilo la samaki kulikuwa ni mshike mshike, kila mmoja alitaka aone kinachotukia lakini gari ya FFU ilifika na kuwataka watu wote kusogea mbali na eneo.


Tracy Tasha bado alijiinamia mkono wake mmoja ukishika tumbo lake na mwingine ukiwa umeushika ule mkono wa Amata uliopiga ngumi, alitulia kwa sekunde chache, damu zikimtoka kinywani na puani.

“Nani boss wako? Nani kakutuma?” Kamanda akauliza.

Tracy hakuweza kuongea chochote, akajiachia kutoka katika mwili wa Kamanda na kuanguka chini, akiwa hana nguvu ya kufanya lolote. Amata akamtazama mrembo yule aliyelala kwa ubavu sakafuni, akamsukuma kwa mguu na kumuweka chali. Tracy akajiinua kwa tabu, akajivuta na kuegemea moja ya jokofu lililo hapo, akipumua kwa shida. Kamanda akachuchumaa akimwangalia usoni.

“Bado kidogo utakufa, kama ulivyoua wengine wote, lakini kabla hujafa, nani boss wako, nani unayemfanyia kazi hii?” akamwuliza.

“Rho-bin-son Que-be-bec!” akajibu kwa tabu kisha akamtemea Kamanda mate yaliyochanganyika na damu usoni.

“Huna maana kama mkia wa mbuzi, mwanamke hayawani kabisa! Kwa kuwa sina desturi ya kuua warembo kama wewe,” akachomoa bastola yake aliyokabidhiwa na Chiba jana yake, “shika hii, ina risasi mbili tu ndani, jiue mwenyewe!” akamshikisha kwenye kiganja chake. Kamanda Amata akasimama pembeni.

“Jiue mwenyewe, mi nasubiri hapa,” akamwambia. Tracy Tasha hakuwa na nguvu yoyote ya kufanya lolote. Kamanda Amata akageukia mlangoni na kuvuta hatua kuondoka eneo hilo wakati alipowaona Gina, Chiba na baadhi ya polisi wakiingia katika jengo lile.

“Pole sana Kamanda!” Gina alitoa pole huku akiipachika bastola yake kiunoni mwake, na kumwendea Amata.

“Pole Kamanda na hongera sana!” Chiba nae alitoa pongezi, lakini mara ghafla wote wakasimama na kutazama kwa mshangao kule alikokuwako mwanamke adui.

Tracy Tasha, alisimama wima, mkononi mwake akiwa na bastola inayomtazama Kamanda Amata kisogoni.

“Hautapata nafasi ya kujutia kosa ulilofanya, nimehakiki kuna risasi mbili, moja itakuua wewe na nyingine itanimaliza mimi,” Tracy aliongea kwa sauti ya kichovu. Kamanda Amata akasimama kimya, mara akasikia mlio wa kilinda usalama cha bastola hiyo kikiondolewa.

“Hah! Hah! Hah! Hah! Hah! mwili wangu hauwezi kuguswa ukiwa hai na ninyi watu weusi, hamna hadhi, na we huwtopata nafasi ya kujisifu kuwa umeniua na kuandika historia hiyo duniani katika duru za usalama, adios amigos,” Tracy aliendelea kusema huku shabaha yake ikiwa sawia.

Akapachika kidole kwenye kifyatulio na kufyatua bastola ile, bastola ikaruhusu risasi moja kutoka kuelekea kwa Kamanda Amata.

Trace alishangaa kuona bastola ile inapiga kinyume, risasi ilitokea upande wa nyuma na kupiga kifuani kwake, Tracy akatoa yowe la uchungu na kujibwaga chini, kifua chake kilikuwa kikivuja damu.

Kamanda Amata hakugeuka nyuma, “asante Chiba kwa teknolojia yako, nimekukubali,” akampigia salute na kisha akaondoka eneo hilo.


MADAM S alijikuta akiruka kwa furaha alipopata taarifa ya kifo cha Tracy Tasha, hakuweza kuvumilia. Akampa taarifa hiyo Dr. Jasmine ambaye naye alikuwa mwenye furaha sana kwa hilo.

“Unaweza kupona sasa Mheshimiwa Rais, adui zako tumewamaliza,” madam akamwambia Rais aliyekuwa amelala kimya kitandani. Mara akainuka na kuketi.

“Asante sana Selina, uliloliota ndilo haswa lililotokea,” akaongea, kisha akavua shati lake kila mtu akashangaa isipokuwa Madam S. kifuani mwake alivua kitu cha plastiki chanye madonge ya damu ndani ya mapakiti, risasi moja kubwa ilikuwa imenasa katika dude hilo. Haikumdhuru, alikingwa, akalitoa na kulitupa pembeni.

“Naomba muwaambie waandishi wa habari, wasitoe habari yoyote zaidi ya kuwa Rais amedunguliwa basi, na hali yake ni mbaya, waandike hivyo hivyo,” maneno hayo alimwambia msemaji wa Ikulu naye akatoka na kwenda chumba maalumu ambako alionana na waandishi waliokuwepo.

“…kwa kifupi, kama mlivyoona, Rais ameshambuliwa, ameumia vibaya na hali yake ni mbaya, hivyo Ikulu itamsafirisha mchana huu kwenda London kwa matibabu, taarifa yoyote mpya mtapewa kutoka hapa tu, asanteni.” Msemaji wa Ikulu alimaliza mazungumzo yake, akanyanyuka. Waandishi wa habari waliokuwepo walianza kumgombania kumtupia maswali lakini aliondolewa mara moja na watu wa Usalama wa Taifa, mlango ukafungwa, na dakika hiyo hiyo gari maalumu ya wagonjwa ikawasili Ikulu, kama ilivyopangwa, akafungwa vizuri katika kitanda.

“Mchome sindano!” Madam S akamwambia daktari wa Rais. Naye akafanya hivyo na usingizi mzito ukamchukua.

Ni watu wasiozidi watano waliojua kuwa Rais ni mzima kabisa lakini wengine wote waliaminishwa hivyo kuwa Mheshimiwa ana hali mbaya.

Msafara wa gari za Ikulu ukaondoka kuelekea Uwanja wa Ndege.

***

“Kamanda Amata,” sauti iliita kutoka nyuma yake. Akageuka na kumwona Madam S akiwa na faili moja mkononi. Amata alikuwa amesimama katika sehemu ya mbele ya nyumba kubwa huko Gezaulole, mkono wake ukiwa na bandeji nyingine kubwa. Akageuka na kumtazama Madam S.

“Yes Mom,” akaitikia na kuitoa miwani yake usoni.

“Mheshimiwa Rais anakupongeza kwa kazi ulioifanya, anakubali sana uwepo wako hapa nchini na hususan katika idara nyeti kama hii, nimetoka kuzungumza naye sasa hivi, tumekubaliana jambo moja,” akamkabidhi lile faili ambalo juu yake lilikuwa limeandikwa Rhobinson Quebec na chini yake maandishi mazito ‘Wanted’, akatazama na kumwangalia Madam S.

“Roho yake tu wala hatumwitaji akiwa hai,” kisha akageuka na kuondoka.

11

SIKU TATU BAADAE

“Ooooh babe, you are so sweet hubby!” Lereti binti wa Khumalo alikuwa akilalamika kitandani, juu yake Kamanda Amata alikuwa akimfanyia manjonjo ya maana.

“Mmmh! Oooh yeah utainjoy sana mama!” akambembeleza.

“Again, please…” malalamiko yakaendelea, miguno ya mahaba ikachukua nafasi kila mtu alikuwa kazama katika dunia nyingine kabisa. Amata alilihusudu umbo la Lereti kwa jinsi lilivyo katika katikati na kutengeneza nane, mapaja yaliyojaa vyema na kuzungukwa kwa nyama nzito na ngozi laini yalizidi kuupeleka mbio moyo wake.

“Hii ndio zawadi yangu kama nilivyokuahidi, na kwa nini hukunambia kama wewe ni mpelelezi mashuhuri Afrika na Ulimwenguni?” Lereti akamwambia.

“Aaaaa hayo hapa si mahala pake mtoto mzuri,” akamjibu.

“Sasa roho yangu kwatuuuu!!! Umemuua yule hayawani aliyeniulia baba yangu kipenzi, sasa niue na mimi niue kimapenzi,” Lereti alibembeleza kimahaba, kwa sauti ya kitoto huku akichezea kifua cha dume hilo. Akamtazama usoni na kumyonya ulimi.

“Kamanda Amata, kuua kwako kama chai ya asubuhi” akamwambia.

“Na mapenzi kwa watoto wazuri kama pumzi ya kila siku,” kamanda akamalizia.

“Niue na mimi ….” Akazidi kulalama huku akijinyonganyonga.

“Jiue mwenyewe!” Amata akamjibu.

MWISHO
 
Nawapa kongole kwa kufikia tamati ya Jiue Mwenyewe!! Tutakutana kwenye thread nyingine hivi karibuni inshallah
 
Back
Top Bottom