Simulizi ya Kijasusi: Kiguu Na Njia

Simulizi ya Kijasusi: Kiguu Na Njia

Abdallahking

JF-Expert Member
Joined
Mar 19, 2018
Posts
3,985
Reaction score
10,840
kiguu-na-njia.jpg


Simulizi : KIGUU NA NJIA
Mwandishi : BEN R. MTOBWA
Imeletwa kwenu na: BURE SERIES

SEHEMU YA 1

likuwa mara yangu ya kwanza kumuona baba akitokwa na machozi. Kwa kweli, ilikuwa mara yangu ya kwanza kumuona mwanamume yeyote mwenye
umri wa baba akilia, iwe sirini au hadharani. Kitendo cha mwanamume kutokwa na machozi, iwe kwasababu ya maumivu au majonzi, hakikupata kukubalika katika jamii yetu.
Nakumbuka nilipokuwa mtoto mdogo, wa miaka mitatu au minne hivi, nilipojikwaa na kuumia au kupigana na wenzangu nikalia. Baba alikuwa akinicharaza bakora huku akisema, “Mwanaume gani wewe unalia? Mwanaume halii!”
Babu yangu pia, mzee Karimanzila, aliwahi kunicheka sana kwa suala hilo la kulia. Siku hiyo mtego nilioutega mwituni ulikuwa umemnasa kanga mkubwa sana. Rafiki yangu mmoja tuliyekuwa naye porini aliniita kwa sauti kubwa kuniarifu juu ya kanga huyo. Lakini nilipofika kwenye mtego huo nilimkuta Katato, ambaye alituzidi sana kwa umri na umbile, akimfungua kanga huyo kwa madai kuwa ni mtego wake. Tulibishana naye sana. Kwa kunikomoa Katato alimwachia kanga wangu, ambaye aliruka na kutokomea zake mwituni. Nilijaribu kupigana naye lakini akanizidi nguvu na kunitia ngeu katika paji la uso. Nililia njia nzima hadi kijijini. Babu



aliposikia habari hizo aliniita na kunidhihaki kwa kusema, “Ukiona mwanaume analia ujue na roho ya kike. Angestahili kuvaa gauni badala ya kaptula.”
“Lakini yule alikuwa kanga wangu wa kwanza. Nimekwishanasa njiwa, hondohondo na kware. Leo
 
SEHEMU YA 2

nimebahatika kumnasa kanga. Ningefurahi sana kumchinja na kumla!” Nilimjibu babu.
Babu alitabasamu kidogo kisha akasema, “Kanga elfu moja utawala. Tatizo ni hayo machozi. Machozi ya mwanaume yanatakiwa kuwa adimu sana. Leo jioni uje nikusimulie kisa cha mwanaume aliyepokonywa mke kwa ajili ya machozi.”
Nilizipenda sana hadithi na simulizi za babu. Kwa ujumla, kijiji kizima na hata vile vya jirani vilipendelea sana kuja kwetu kumsikiliza babu akisimulia matukio mbalimbali yaliyomkuta katika maisha yake. Hadithi zake zilijaa miujiza na maajabu kiasi kwamba baadhi ya watu walidiriki kumwita ‘mwongo’ au ‘anatia chumvi’. Lakini yeye aliwacheka watu wa aina hiyo na kuwaambia, “Hamjaiona dunia. Dunia yenu ni kijiji hiki pekee. Mimi nimeizunguka. Nimefika upande wa pili wa dunia!”
Hiyo ilikuwa kauli yake ya mara kwa mara, kauli ambayo iliongeza utamu wa simulizi zake. Hakika babu mwenyewe alikuwa hadithi, tena hadithi ya kusisimua kuliko zile simulizi zake. Inadaiwa kuwa, utotoni, akiwa na umri wangu, alitoweka kijijini hapo kama mzuka. Alitafutwa kwa siku kadhaa bila mafanikio. Watu walidhani kuwa ameliwa na simba au mamba. Lakini alipoibuka miaka kadhaa, baadaye, akiwa na simulizi tele za ‘kuizunguka dunia,’ watu walibadilika na kuamini kuwa alichukuliwa na mashetani ya chini ya bahari.



Pamoja na kuzipenda hadithi zake, pamoja na kiu ya kusikia kisa hicho cha ‘machozi ya mwanamume’ bado hasira dhidi ya kanga wangu aliyepeperushwa kwa
 
SEHEMU YA 3

makusudi na maumivu toka kwenye ngeu ya paji la uso kwa mara ya kwanza vilinifanya nikatae kwenda kumsikiliza. Hivyo, kumwona baba akilia lilikuwa jambo jipya kabisa katika maisha yangu. Alikuwa kaketi juu ya gogo, mikono yake yote miwili ikiwa imekishika kichwa chake huku macho yake yakitazama mbele yake, ingawa ilikuwa dhairi kuwa haoni kitu chochote kutokana na wingi wa machozi. Nilijikaza na kumsogelea kwa nia ya kumuuliza kulikoni. Lakini mara nilipomfikia ushujaa ulinitoka. Nikajikuta nikiambulia kukaa ubavuni mwake, juu ya gogo lilelile. Kwa mshangao wangu, baba alifanya kitu ambacho hakupata kukifanya huko nyuma.​

Alinikumbatia kwa mkono wake mmoja huku mkono wake wa

pili ukifuta machozi ambayo yalimiminika kwa wingi zaidi. “Mwanangu!” nilimsikia akiniita kwa sauti ndogo

yenye kigugumizi.

Sikumbuki kama niliitikia au la.

Wala yeye hakuzungumza neno jingine.

Nilipopata nafasi nilijichopoa toka katika mikono yake na kuingia ndani kwa dhamiri kuu mbili. Dhamiri ya kwanza ilikuwa kuficha machozi, ambayo mie pia yalianza kunilengalenga. Dhamiri ya pili ikiwa kumpata mama ili anifafanulie kisa na mkasa wa hali hiyo.

Mama hakuwepo. Wala hakuwepo mtu wa kumuuliza kwani mimi nilikuwa mtoto pekee katika familia hiyo. Na nilipatikana kwa shida baada ya mama na baba kuhangaika kwa waganga kwa zaidi ya miaka kumi. Hatimaye, walimpata mganga mmoja aliyebobea, ambaye alimtibu mama kwa kuchanganya mitishamba aina ya Mhusu na Mnywanya ambayo
 
SEHEMU YA 4
mama alitakiwa kunywa kwa siku mbili. Siku chache baadaye alitangaza kuwa yu mjamzito. Hapo mganga alimbadilishia dawa na kumnywesha mti uliotajwa kuwa Sagamba mara kwa mara hadi nilipozaliwa.

Miaka mingine kumi tayari ilikuwa imepita bila dalili za kupatikana mdogo wangu. Mganga wake alishakufa na hakupata kumwonyesha mtu yeyote miti ile. Hivyo, mimi nilikuwa kama mboni ya jicho kwa baba na mama, ingawa hawakutaka kamwe nijisikie hivyo.

Wakati nikihangaika bila mafanikio kuwaza na kuwazua namna ya kumnyamazisha baba, mara nilimwona mama akirudi nyumbani, huku kafuatana na babu. Kumbe yeye pia alikuwa amehangaika sana kumtuliza baba na kumuuliza kulikoni bila mafanikio. Ndipo lilipomjia wazo la kutembea mwendo wa zaidi ya dakika ishirini hadi kwa babu ambaye kwa bahati alikuwa nyumbani.

Kama kawaida yake, tofauti na watu wengine wote kijijini hapo, babu alikuwa amevaa kaptula yake nyeupe, shati jeupe, soksi nyeupe na viatu vyeusi. Akiwa miongoni mwa watu wengi waliovaa lubega za kaniki, miguu yao ikikanyaga chini, siku zote babu alionekana mtu wa aina ya pekee.

“Kuna nini?” babu alimuuliza mwanawe akiwa ameketi pale nilipoketi mimi muda mfupi uliopita. “Kuna nini?” alirudia na kuongeza, “Nasikia tangu umetoka kuonana na Mwami umerudi unalia. Kuna nini?”

Baba hakujibu mara moja. Alimtazama baba yake kwa muda kabla hajainuka taratibu na kumshika babu mkono. “Ni mambo mazito yaliyonipata leo. Twende faragha nikusimulie, ingawa nimekula kiapo cha kutotoa siri hii nje.”


 
SEHEMU YA 5
Walikwenda pembeni, mahala ambapo masikio yangu na ya mama yasingeweza kusikia wanachozungumza. Hapo waliteta kwa muda mrefu, baba akizungumza babu akisikiliza. Baadaye, nilimwona babu akicheka na kuzungumza kwa muda kabla hawajarudi na kuketi tena kwenye gogo. Mama alipoona wametulia, aliingia ndani na kuwaletea kibuyu cha togwa ya mahindi. Waliinywa taratibu huku wakiwa kimya.

Nadhani togwa hii ilikuwa kali kwani baada ya muda mfupi nilimwona baba akichangamka huku babu akizungumza kwa sauti ya juu kidogo.

Sikubahatika kupata mtiririko wa maongezi yao. Lakini mawili matatu niliyoweza kudonoa katika matamshi yao yalinifanya nipate hisia kuwa nilihusika kwa njia moja au nyingine na majonzi yao. Imani hiyo ilijengeka zaidi pale nilipomsikia babu akisema kwa sauti ya juu kidogo, “Mjukuu wangu mie! Nadhani mwanangu hunifahamu hata kidogo. Haiwezekani!”

Baba: Lakini wamesema itakuwa siri. Huenda hata mimi mwenyewe hawatanishirikisha.

Babu: Nasema haiwezekani. Enzi za utukufu na uhuru wa kufanya chochote wanachotaka zimepita zamani. Wakithubutu nitahakikisha wananyongwa.

Baba: Watanyongwa kabla au baada?

Babu: Hawawezi kuthubutu!

Mmoja wao alinitupia jicho. Wakabaini kuwa nafuatilia maongezi yao. Wakapunguza zaidi sauti zao na kuendelea kunywa.


 
SEHEMU YA 6

Usiku huo babu alinichukua nikalale kwake. “Twende zetu mjukuu wangu. Leo nina hadithi nyingi za kukusimulia, hadithi za kweli ambazo sijapata kumsimulia mtu yeyote.”

Nikiwa na hakika kuwa kwa kiasi fulani mwaliko huo ulitokana na kisa au mkasa nisioufahamu, wa hapo nyumbani, niliafiki kufuatana na babu hadi kwake. Bibi alinipokea kwa furaha huku akiniita ‘mume’ wake. Akanipa kata kubwa iliyojaa togwa tamu, tofauti kabisa na ile waliyokunywa babu na baba. Baada ya hapo nilipewa ugali na pande kubwa la nyama ya nyati. Babu alikuwa mwindaji, bibi akiwa mkulima.

Nyumba yao katu haikupata kupungukiwa na chakula. Nilikula hadi nikavimbiwa, kabla sijatandikiwa mkeka na bibi kunipa moja ya kaniki zake nitumie kama shuka. “Tutazungumza kesho, leo pumzika mapema.” Babu​

aliniambia alipoona dalili za usingizi katika macho yangu.



* * *​

Hakuna mtu aliyeujua umri wa babu, ikiwa pamoja na yeye mwenyewe. Ilikadiriwa tu kuwa alizaliwa miaka ya 1850 au baadaye kidogo, kwani wakati huo zilikuwepo habari nyingi za nchi kuvamiwa na watu weupe wenye mianzi inayotoa moshi wenye uwezo wa kuua tembo hata akiwa mbali. Watu hao walidaiwa kutembea hovyo katika misitu na kushangaa kwa kila walichokiona.

Miongoni mwa watu hao alitajwa sana mtu mmoja anayeitwa Hanning Speke na mwenzie Richard Burton. Hawa walitembea hadi maeneo yetu ya Buha na kupita na kushangazwa sana pale walipoliona ziwa kubwa la Tanganyika ambalo lilitenganishwa au kuunganisha nchi yetu na zile
 
SEHEMU YA 7
za Kongo na Burundi. Inasemekana pia kuwa walitembea porini kwa miezi kadhaa hadi walipofika ziwa Lweru, ambalo walilibadili jina na kuliita Victoria huko katika nchi ya Wahaya na Wasukuma.

Wakati huohuo zilikuwepo habari za mtu mwingine aliyeitwa David Livingstone aliyeweka makazi yake Ujiji na akafia nchini Zambia. Wasaidizi wake maarufu, Susu na Chuma wanaelezewa kuwa waliibeba maiti yake hadi upande wa pili wa nchi, pwani ya Bahari ya Hindi ambako ilisafirishwa hadi kwao Ulaya.

Niliyajua yote hayo kutokana na simulizi za babu mwenyewe. Katika enzi hizo alikuwa tayari ana akili zake, nguvu za kutosha na uwezo wa kuanzisha mji wake mwenyewe, ingawa alikuwa hajaoa. Na ni wakati huo aliopatwa na ule mkasa wa aina yake, mkasa ulioacha gumzo hadi leo, na aliporudi, kimiujiza vilevile kama alivyoondoka, akiwa na simulizi za ajabuajabu, gumzo likaongezeka.

Moja ya maajabu aliyokuja nayo ni mavazi. Nguo zake zilikuwa sawa na zile zilizodaiwa kuvaliwa na watu weupe. Na siku zote alihakikisha kuwa ni safi.

Ajabu ya pili aliyoileta babu ni taarifa kuwa watu weupe kumbe siyo kabila moja bali ni watu wa makabila mbalimbali, wanaotoka nchi mbalimbali na kuzungumza lugha mbalimbali. Alizitaja nchi kama Uingereza, Ujerumani, Sweden, Ureno na nyinginezo kuwa ni nchi tofauti, zenye utawala tofauti na lugha tofauti kabisa.

Ajabu ya tatu, na pengine kubwa zaidi ni pale alipodai kuwa alikuwa na uwezo wa kuzungumza lugha mbalimbali za makabila hayo, kama Kiingereza, Kijerumani na Kisweden. Kwa hilo watu walielekea kutomwamini. Lakini pale Wabelgiji



 
SEHEMU YA 8
walipovamia Buha, na kuzunga wakitokea Kongo, miaka ya 1916, babu alidhihirisha uwezo wake wa lugha kwa kuzungumza na mmoja wa makamanda wao waliopotea njia na kujikuta wamefika kijijini kwetu. Wageni hao walishangaa sana kumkuta mtu anayezungumza Kiingereza ambayo ni lugha ya jirani zao katikati ya pori kama hilo. Walijaribu kumshawishi babu afuatane nao ili awe mkalimani wao lakini alikataa katakata kwa kusema, “Nimekaa kwao na kukataa kuwa mtumwa wao, vipi nikubali kuwa mtumwa wao katika nchi yangu mwenyewe?”
Umaarufu wa babu kwa lugha uliongezeka maradufu miaka mitano baadaye, pale Uingereza ilipochukua madaraka ya utawala wa Tanganyika toka kwa Mjerumani ambaye alikuwa pia ameupokonya toka kwa Wabelgiji katika eneo hilo la Buha. Mwaka 1931 chifu, ambaye tulimwita Mwami wa Heru juu alifariki. Amri toka kwa Gavana G. S. Symes ilimtaka DC kuteua ‘Mwami’ mpya. DC akaamua kupata mawazo ya wananchi kabla ya uteuzi wake. Ujumbe wake ulipofika kijijini kwetu na kumkuta mzee mmoja aliyevaa kama wao, akizungumza lugha ya Kiingereza kwa ufasaha kabisa mara moja babu alipendekezwa kuwa Mwami. Lakini kwa mshangao wa wengi babu alikataa cheo hicho katakata. Kwa maelezo yake alidai cheo hicho ni kidogo sana kwa upeo wake na kwamba thamani yake ni sawa na kilemba cha ukoka.
Hicho kilikuwa kitendawili kingine cha babu kwa jamii yetu na kwa Waingereza wenyewe. Kwa kuwa walimhitaji sana, walao kuwa karibu na uongozi ndipo walipomwomba babu amruhusu walao baba akawe babarike, yaani mmoja wa wasaidizi wa Mwami. Babu alimruhusu.
Uamuzi wa babu kukataa cheo hicho ulipelekea DC



 
SEHEMU YA 9
kuteua machifu wengine wa Heru Juu, Kalinzi, Bushingo na Buhambwe kutoka katika makabila ya mbali kama Mmanyema aliyetoka Tabora na mwalimu Mfipa aliyetoka Sumbawanga kuwa machifu wa eneo letu kwa nyakati tofauti.

Simulizi, visa na mikasa ya babu haikuwa na mwisho. Kila siku alikuwa na kitu kipya cha kusimulia, ambacho ama kilishangaza ama hakikuaminika miongoni mwa wasikilizaji wake.

Kwa mfano, alizungumza juu ya vitu kama nyumba ndogo ambazo watu huko Ulaya huzitumia kwa kusafiri umbali mrefu bila kutuma miguu yao wala kuchoka. Pia, alisema kulikuwa na kijumba ambacho alikitaja kuwa kinaitwa gari.

“Uchawi?” mtu mmoja alipata kumuuliza.

“Hapana,” babu alimjibu. “Hayo ni maendeleo tu ya Sayansi na Teknolojia.”

“Sayansi na Teknolojia ndio nini?” “Ni aina fulani ya elimu na ujuzi.”

Hadithi nyingine ya babu inayofanana na hiyo ni ile ya madai yake kuwa kuna vyombo vingine vikubwa zaidi ya gari ambavyo huruka angani, toka mji hadi mji, au nchi hadi nchi, kwa muda mfupi zaidi, vikiwa vimebeba abiria. Alivitaja vitu hivyo kuwa ni sawa na ndege mkubwa aliyeumbwa na binadamu.

“Huo sasa ndio uchawi wenyewe!” mzee mmoja aliyekuwa akimsikiliza alipata kumwambia. “Nikiwa mdogo mie pia nilipata kuchukuliwa katika ungo na babu yangu hadi pwani ya Tanga. Lakini safari hizo tulizifanya usiku tu, tukiwa tumejifunika sehemu za siri pekee. Kwa bahati mbaya, mpaka nakufa babu hakupata kuniambia siri ya uwezo ule.”

Babu alicheka sana kabla ya kumjibu mzee mwenzake


 
SEHEMU YA 10
huyo akisema, “Nafasi ya uchawi inazidi kuwa ndogo katika dunia ya leo ya Sayansi na Teknolojia. Nani atakubali kusafiri usiku tu, tena bila nguo; wala kuiona mashine ya ndege hiyo?” Utamu wa aina mbalimbali za vyakula, urahisi wa maisha, barabara za juu na chini ya ardhi, magari, ndege na meli kubwa, matibabu ya kisasa na mambo mengine tele ni miongoni mwa simulizi nyingi ambazo wasikilizaji wake​
walizifurahia sana.

* * *​

Naam, huyo ndiye babu yangu, mzee Kionambali Mtukwao, kama alivyofahamika katika eneo lote hilo la wilaya ya Kasulu na vitongoji vyake. Ni babu huyu ambaye siku hiyo niliamka nikiwa nimelala chini, kando ya kitanda chake cha kamba, kilichotandikwa ngozi ya ng’ombe na blanketi nzito iliyoanza kuchakaa, ndani ya nyumba yake ya tembe. Niliamka alfajiri, lakini tayari babu alikwishaamka kitambo na kukoka moto nje ya nyumba. Bibi pia alikwishaamka na kuelekea mtoni kuchota maji.
Nikatoka nje na kumsalimu babu. Aliitikia kwa furaha kisha aliniamuru kumkamata jogoo mmoja mweupe na kumchinja ili awe kifungua kinywa cha siku hiyo. Ilikuwa kazi rahisi niliyoipenda sana. Kwa kuwarushia punje mbili tatu za mahindi, huku nikipiga mluzi, kuku wote ambao walishaanza kutawanyika huko na huko vichakani walirejea. Nikaendelea kurusha mahindi kwa karibu zaidi. Dakika mbili baadaye jogoo niliyemtaka alikuwa miguuni mwangu. Nikamdaka mara moja na kisha kumchinja. Bibi aliporudi alianza kumshughulikia mara moja.



 
SEHEMU YA 11
Nikaenda mtoni ambako nilioga maji baridi yaliyouchangamsha mwili wangu. Nikasafisha meno yangu kwa mti wa mdaa ambao pia ni dawa ya kinywa na meno. Niliporudi bibi alikuwa akimalizia kutenga ugali wa muhogo kwa kitoweo cha kuku wa kuchomwa. Mimi na babu tuliketi mkao wa kula na kuanza kumshambulia jogoo yule ambaye muda mfupi alikuwa akiwika kama mfalme wa mji huo.

Pamoja na utamu wa kuku, pamoja na simulizi nyingi za babu, shahuku yangu kubwa ilikuwa kufahamu kile ambacho kilimfanya baba atokwe na machozi hadharani. Nikijua kuwa ni jambo hilo lililomfanya babu anichukue jana na pengine hata jogoo huyu amechinjwa kuhusiana na kisa au mkasa huo nilistahimili kwa muda nikimsubiri babu azungumze. Lakini babu alikuwa kimya. Chakula kilipokwisha nilitoa vyungu na kuvipeleka ndani. Niliporejea nilimsogelea babu na kumwambia taratibu, “Nadhani ulikuwa na jambo la kuniambia babu.” Babu alitabasamu na kuruhusu meno yake yote kuonekana, tofauti na wazee wengi wa umri wake ambao walibakiwa na magego machache tu vinywani mwao. “Mbona una haraka mjukuu wangu? Tuna mengi sana ya kuzungumza. Tusubiri kidogo bibi yako aende shamba. Nataka tuzungumze kama wanaume wawili, si mtu na mjukuu wake.”​

Kauli ambayo iliniongezea shahuku.

Mara bibi alipochukua jembe lake na kuelekea shambani babu alianza simulizi zake. Ajabu ni kwamba alianza kwa kunirushia maswali badala ya mimi kumrushia yeye.​

Babu: Unajua wenzetu walioendelea zaidi huko Ulaya maisha yao ni bora zaidi yetu?

Mimi: Najua, umesema hivyo mara nyingi.

Babu: Umepata kujiuliza nilifikaje huko na kutembea​

nchi zote hizo?

 
SEHEMU YA 12

Mimi: Niliwahi kukuuliza. Unasema ulienda Ulaya kwa

Babu: ni kwlei. Nilienda kwa ajali.
Babu: mtu kwao mjukuu wangu. Maisha yangu yote ya

ugenini sikupata kujisikia.​

Babu alisitia kidogo akitafakari jambo. Nikatumia mwanya huo kutumbukiza swali langu badala ya kuwa mtu wa kuulizwa, “Kwa hiyo babu, pamoja na raha zote hizo kwa nini ulirudi? Au kurudi kwako pia ilikwua ajali nyingine?”

Babu: Hapana nilirudi kwa hiari.

Mimi: Kwa nini?

Babu: Mtukwao mjukuu wangu. Maisha yangu yote ya ugenini sikupata kujisikia nyumbani. Baadhi ya mila na desturi zao haziendani kabisa na zetu. Mvulana mkubwa kabisa anamkumbatia mama yake na kumbusu mdomoni! Msichana wa makamo anamvalia baba yake nguo fupi na pengine kumkalia mapajani!

Alisita kabla hajaendelea, “Halafu waliniudhi kwa jambo moja kubwa.

Mimi: lipi hilo?

Babu: La kudharau utamaduni na mila zetu na kuamini zao ndio sahihi. Kwa mfano makabila mengi ya Kiafrika yalimkataza mwanamke mwenye mimba kula mayai au maini kwa visingizo mbalimbali. Lakini walikuwa na sababu kubwa za msingi kabisa.

Mimi: Zipi hizo kama sio uchoyo na uroho?

Babu: (Akicheka) Uchoyo? Kwa kweli ulikuwa ukarimu wa hali ya juu sana. Unajua mwanamke mwenye mimba akila mayai mengi wakati wa ujauzito wake atanenepa yeye na mtoto aliye tumboni pia?



 
SEHEMU YA 13
Mimi: Hilo najua.

Babu: Basi kwa hekima za wazee wetu walibuni hila ya kuwatishia hivyo. Ukweli ni kwamba walihofia mtoto akinenepa sana tumboni asingezaliwa. Hatukuwa na vifaa vya upasuaji kama wao. Na hatukutaka kuhatarisha maisha ya mama na mtoto; wazee wetu walikua na hekima sana.

Mimi: kweli uzee ni dawa…!

Babu alisita tena, kama mtu aliyejisikia kichefuchefu kwa mambo yale. Halafu akaendelea, “Si hayo tu. Hata nchi na mazingira yao hayafikii kabisa ya kwetu. Ndiyo, wana barabara kubwa na magari. Ndiyo, wana majengo mapana na bustani za kuvutia. Lakini hawana ardhi nzuri, misitu ya asili, mbuga za kuvutia, wanyama na ndege wa kusisimua kama sisi. Wengi wao hawana mito wala maziwa wenye samaki wengi kama yetu. Hata hali ya hewa kwao ni taabu tupu. Zipo nchi zenye baridi kwa mwaka mzima. Ziko zile zenye vipindi vya baridi kali na joto la kutisha katika mwaka mmoja. Sisi tumejaliwa sana.” Nilimwona babu akitabasamu kidogo na kisha kuangua kicheko. Nikamwuliza kulikoni. “Nitakuambia jambo moja,” alisema akiendelea kutabasamu. “Lakini naomba iwe siri kati yetu. Moja ya mambo yaliyonifanya nitamani sana kurejea nyumbani ni uhuru wa kujisaidia porini. Miaka yote niliyokuwa huko vyoo viko ndani ya nyumba. Ukipanda meli choo, ukipanda treni choo, ukipanda ndege choo. Hata mara moja hupati fursa walao kujisaidia haja ndogo porini, uone faraja ya maji yaliyochujwa na mwili wako yakipokelewa na nyasi za kijani na baadaye kumezwa na ardhi yenye kitovu chako.” Sikuweza kujizuia. Nikaangua kicheko kirefu. “Hapa tunazungumza kama mtu na rafiki yake.​

Nitakuambia sababu ya pili iliyonifanya niamue kurejea nyumbani.” Babu aliendelea.


 
SEHEMU YA 14
“Lakini babu,” nilidakia, “Shida yangu kubwa ni kujua baba alikuwa analia nini jana. Hayo mengine tutayazungumza baadaye.”

“Tunaelekea hukohuko,” babu alisema. “Ungependa

kujua sababu nyingine iliyonirejesha huku?” aliongeza swali. “Nadhani ningependa kujua.”

“Nina tatizo kubwa. Sijui kusoma wala kuandika.” Babu

alitamka ghafla.

Tamko ambalo lilinipiga kwa mshangao kama radi. Babu hajui kusoma wala kuandika! Pamoja na kujua lugha mbalimbali za dunia! Pamoja na kutembea huko na huko. Nilihisi huo ulikuwa utani mwingine wa babu na mjukuu wake. “Naona huniamini. Sikubahatika kwenda shule. Baba​

yako vilevile hajui kusoma wala kuandika. Ninachotaka kufanya ni kuhakikisha wewe unapata kile ambacho wazazi wako hatukubahatika kupata. Tunataka upate elimu. Dunia inatawaliwa na kuongozwa na wenye elimu. Siri zote za dunia zimefichwa na kuhifadhiwa katika vitabu.” Aliongeza.

Wakati nikiitafakari taarifa hiyo ya kushangaza nikapambazukiwa na jambo moja. Ili kuhakikisha nikamuuliza babu, “Niambie ukweli babu. Ulikataa cheo cha uchifu kwa ajili ya kutojua kusoma na kuandika?”

“Mjukuu, naona una akili nyingi,” Babu alisema. “Ni kweli kabisa. Chifu gani ambaye atalazimika kupeleka barua kwa mtu mwingine ili asomewe? Ningekubali, ningeumbuka.”

“Hizo lugha ulizijuaje bila kusoma?”

“Uzoefu. Huwezi kuishi na mtu miaka kumi bila kujua lugha yake. Labda uwe na kichwa cha boga.”

“Na kwa nini hukujifunza kusoma na kuandika?” “Umri.”

“Umri?”


 
SEHEMU YA 15

“Umri ulishapita. Ningeweza wapi mzee mzima kuketi na vitoto vya miaka sita kufundishwa a e i o u. Tena wanaokufundisha wakiwa watoto au wajukuu wako?”

Kwa kiasi fulani, nilimhurumia babu. Si kwa kukosa elimu ya vitabuni, bali kwa jitihada alizofanya za kujiweka wazi kiasi hicho mbele yangu hata akatoa siri ambayo naamini hakupata kumwambia mtu mwingine.

“Hawakukulazimisha?” nilimuuliza.

“Nini? Wanilazimishe kusoma? Baadhi yao pia walikuwepo wachache wasiojua kusoma wala kuandika. Wawili watatu walijaribu kunilazimisha kwa kuwatuma watoto wao wanifundishe. Lakini nilijifanya naumwa macho, kwa hila nikajitia vitunguu machoni na kutokwa na machozi kila kitabu au daftari lilipofunguliwa mbele yangu. Wakaniacha nilivyo.”

“Ni hilo la kutojua kusoma hasa lililokurejesha nyumbani?” niliuliza.

“Hilo ni moja wapo. Nisingerudi ningefia hukohuko nikiwa mpishi au mfagizi wao milele. Lakini kuna sababu nyingine”

“Ipi hiyo?”

Babu alikohoa kidogo kabla hajasema, “Ujinga ni mzigo mjukuu wangu. Wale watu waliojifanya wafadhili wangu, kumbe mimi ndiye niliyekuwa mfadhili wao. Walinitegemea mimi ili kupata mkate wao wa kila siku.

“Kwa vipi?”

Kwa sauti ya huzuni kiasi babu alieleza, “Wale jamaa kumbe walikuwa wakinifanyia maonyesho na kupokea fedha lukuki kwa jina langu. Unajua watu wa nchi nyingi Ulaya bado hawajapata kumwona mtu mweusi? Wengine ni wajinga kama wengi wetu tulivyo wajinga kwa kutopata kumwona mtu mweupe.”


 
SEHEMU YA 16

“Kwahiyo walinigeuza biashara. Zile safari nyingi za hapa na pale, toka nchi hadi nchi, kumbe zilikuwa za kunifanyia maonyesho. Watu walitoa pesa nyingi ili wamwone ‘nyani mweusi’ anayekula kwa uma na kuzungumza Kiingereza. Kuna wakati niliombwa kuimba, au kualikwa kucheza muziki na wasichana wa Kizungu. Picha nyingi zilipigwa na kuuzwa kwenye vyombo vya habari.”
“Nikiwa nchini Sweden, katika mji mmoja uitwao Jonkoping niliajiriwa na familia moja ya watu ambao walikuwa wakiendesha shamba la wanyama. Wengi kati ya wanyama hao walikuwa wa porini ambao walikamatwa wangali wadogo na kufundishwa ama kuishi na binadamu. Wale wakali kama simba, chui na vifaru walifungiwa katika maeneo maalumu.”
“Ajira yangu kama nilivyoambiwa awali ilikuwa kusaidia kuwatunza wanyama hao. Niliingizwa katika mikataba ambayo sikuielewa na kushawishiwa kuweka dole gumba kwenye karatasi zao kama sahihi. Niliiona kazi rahisi na kuziona mia tatu kila wiki nilizokuwa nikilipwa kama za bure. Lakini nilishangaa pale nilipoanza kuvalishwa mavazi yaliyoandaliwa kitaalamu na kuonekana kama nyani dume. Hayo yalianza pale nyani aliyekuwa shambani humo alipofariki kwa uzee, wamiliki wakaifanya habari hiyo siri kwa hofu ya kupoteza wateja wao waliokuwa wakimiminika kila siku kumtazama nyani huyo anavyoruka toka tawi hadi tawi la miti iliyooteshwa shambani humo.”
“Nikaelekezwa kujifanya nyani yule. Kwa kuwa nilikuwa hodari sana wa kupanda miti, kuachia tawi moja na kudaka jingine halikuwa jambo geni kwangu. Niliwafurahisha sana watazamaji, hasa watoto. Nadhani niliwafurahisha zaidi kwa kuwa nilikuwa binadamu nikisoma hisia zao na hivyo kufanya



mengi ambayo hawakuyatarajia.”
“Waajiri wangu walifurahi sana. Muda wote walikuwa na kamera za video ambazo walizitumia kunukuu kila kitendo changu. Baadaye wateja walipoondoka waliendelea kunipiga picha hata wakati navua mavazi yale ya kinyani na kuvaa ya kibinadamu. Mara kwa mara walinihoji vilevile, kwa lugha zote nilizoweza kuzungumza na kunukuu maongezi yangu kwa vinasa sauti.”
“Ikaja siku ya balaa. Wakati nikiruka toka tawi hadi tawi la mti uliokuwa juu ya zizi la simba dume ilitokea bahati mbaya nikateleza na kudondokea ndani ya zizi hilo kando kidogo ya simba yule. Nadhani nilipiga ukelele wa hofu, kwani nilijua nimefika mwisho wa maisha yangu. Nilitetemeka zaidi pale simba huyo alipoanza kuninyatia taratibu akinguruma. Wakati nikijiandaa kwa vita ya kuipigania roho yangu nilishangaa kuona simba huyo akiweka kinywa chake kando ya sikio langu na kuninong’oneza, “Usiogope, mimi ni binadamu kama wewe!”
“Kweli? Wewe mtu wa wapi?” nilinong’ona vilevile. “Mimi ni Mmarekani. Nipo hapa mwaka wa tatu.” Alisema.
“Nilipigwa na butwaa. Lakini walioduwaa zaidi ni watazamaji ambao kwao kitendo cha simba kuteta na nyani kilikuwa muujiza wa pekee. Walitegemea kuona nikiliwa hadharani, badala yake nanong’ona na simba!”
“Toka siku hiyo shamba hilo likawa linafurika wateja. Walitoka miji ya mbali na hata nchi za jirani kuja kushuhudia maajabu ya ‘nyani’ na ‘simba’ waliojenga urafiki.”
Lakini kwangu hiyo ilikuwa siku ambayo niliamua kuacha kazi hiyo. Pamoja na kulipwa fedha nyingi, nilikichukulia kitendo hicho kama udhalilishaji mkubwa.
 
Back
Top Bottom