Simulizi ya Kijasusi: Kiguu Na Njia

Simulizi ya Kijasusi: Kiguu Na Njia

SEHEMU YA 17

Hivyo, mara tu nilipopata mshahara wangu wa mwezi huo, ambao uliongezwa mara dufu, nilitoweka.”
Nilicheka sana. Kwangu ilikuwa habari ya kusisimua sana. Ilinisisimuazaidikumsikiababu,kwamarayakwanza,akisimulia tukio lililomuhusu kwa kirefu kiasi hicho. Mara nyingi yeye alikuwa mtu wa simulizi na kujibu maswali kwa mkatomkato. Nilikuwa na kila sababu ya kumhurumia babu. Kwa upande mwingine, maelezo yake yalizidi kunithibitishia jambo moja kubwa; umuhimu wa elimu. Lakini mara nikakumbuka kuwa babu alikuwa hajafikia au kugusia kiini cha maelezo hayo. Sababu ya kulala kwangu kwake na kuchinjwa kwa jogoo wake bora kuliko wote; kwa kila hali kulihusiana na
majonzi aliyokuwa nayo babu. Nikamkumbusha hilo.
“Nakumbuka vizuri sana,” Babu aliniambia. “Lakini,” aliongeza. “Kama nilivyosema awali unahitaji kuwa na kifua. Taarifa nitakayokupa huenda ikakutisha au kukuogofya. Lakini unatakiwa kupokea kama mwanamume na kuichukulia kwa upande wa pili kama msukumo wa ufunguo mpya wa maisha yako.”
Niliona kama babu anazidi kunichanganya. Nikamtumbulia macho ya mshangao na kumtegea sikio kwa makini.
“Inabidi uondoke kijijini hapa mara moja,” babu
aliniambia ghafla.
Kati ya yote niliyotarajia, hilo la kuondoka halikuwemo katika mawazo yangu, “Nani? Mimi!”
Babu akakubali. “Kwa nini?” “Wanataka kukuua.”



Sikuyaamini masikio yangu, “Wanataka kuniua mimi, watu gani hao?”
“Wanakijiji. Wakazi wa eneo hili.”
Bado sikumwelewa babu. Nilihisi huo ulikuwa utani wake mwingine, pengine kwa nia ya kupima ujabari wangu. Ili kumthibitishia hivyo niliangua kicheko na kumwambia taratibu, “Babu acha utani huo. Unanichulia kifo.”
Lakini macho ya babu yalikuwa hayana utani wala mzaha wa aina yoyote alipoongeza, “Wanataka kukutoa kafara. Lazima uondoke haraka iwezekanavyo.”

* * *
Kwa takribanimiakamitatuiliyopita eneo letulilikumbwa na ukame. Mazao yaliyopatikana yalikuwa machache sana. Mimea mingi ilinyauka, hata baadhi ya vyanzo vya maji vilianza kukauka. Mbaya zaidi ni pale ilipoonekana wazi kuwa mwaka huo pia hakukuwa na dalili ya mvua.
Zaidi ya tatizo hilo la ukame lilikuwepo tatizo jingine kubwa zaidi, tatizo la ugonjwa wa malale. Eneo kubwa la mapori na misitu iliyovizunguka vijiji vyetu ilikuwa na mbung’o wengi sana ambao walidaiwa kusababisha malale. Mbung’o hao walianza hata kuvamia mifugo iliyokuwemo zizini na hivyo kusababisha maradhi ya usingizi na hatimaye vifo vya ng’ombe wengi. Wala haikuwa mifugo pekee. Zaidi ya watu wanane kijijini hapo walikuwa wamekwishakufa kwa malale huku wengine wasiopungua ishirini, wakiugua ugonjwa huo ambao haukusikia dawa.
Kwa mujibu wa babu, Mwami, wasaidizi wake na wazee wenye busara kijijini hapo waliketi vikao vingi kujadili namna ya kupambana na matatizo hayo bila mafanikio. Hali
 
SEHEMU YA 18
hiyo ilisababisha wachukue uamuzi wa kuomba msaada wa bingwa wa ramli katika eneo hilo. Kwa mujibu wa mtaalamu huyo miungu ilikuwa imekasirika kwa kusahauliwa kwa muda mrefu. Hivyo, ilidai kafara ya damu ya mtu ili iwafukuze mbung’o na kuamuru mvua inyeshe kama kawaida.
Kwa maelezo ya mtaalamu huyo, kafara huyo alitakiwa azikwe hai, usiku wa manane; katikati ya msitu mnene wenye mbung’o wengi. Aidha, mtu huyo alitakiwa awe msichana au mvulana anayetoka kwa baba na mama mwenye mtoto mmoja. Ni hapo nilipoingia mimi. Katika eneo lote hilo wazazi wangu walikuwa watu pekee wenye mtoto mmoja. Kwa bahati, baba alikuwa mmoja kati ya babarike walioteuliwa kufanya mawasiliano na mtabiri yule. Vinginevyo, zoezi hilo lingefanywa kwa siri. Mwami na viongozi wengine walimweka kitako na kumtaka apige moyo konde na kumtoa mwanae wa pekee ili
kuiokoa nchi na maafa zaidi.
Ni hilo lililomfanya baba arudi nyumbani huku akibubujikwa na machozi. Alikuwa katika mtihani mkubwa wa kuchagua kati ya mwanae wa pekee na ukombozi wa nchi yake ili iondokane na maafa.

* * *
“Nadhani sasa umeona umuhimu wa kuondoka kwako hapa haraka,” babu aliniambia mara baada ya maelezo yake. “Ni sawa na kuua ndege wawili kwa jiwe moja. Utakuwa ukikimbia kifo, wakati huohuo ukiifuata elimu.” Alifafanua.
Nilimsikiliza babu kwa makini. Hata hivyo, moyo wangu ulikuwa mzito sana kwa ukubwa wa suala zito lililokuwa kichwani mwangu. Kwamba watu walikuwa wamekaa vikao na kufikia hatua ya kuamua kunizika nikiwa hai ili wapate mvua!



Haikuniingia kabisa akilini. Ndiyo, siku za nyuma nimewahi kusikia hadithi za aina hiyo. Hadithi za watu, hasa watoto, kutolewa kafara. Lakini sikupata hata mara moja kumfahamu mtu yeyote au mtoto wa mtu yeyote aliyepata kutolewa kafara. Pengine kafara hizo zilitolewa kwa siri? Pengine hilo ndio jibu la hadithi za kutolewa kwa baadhi ya watu kijijini hapo miaka ya nyuma?
Tishio la maisha yangu lilikuwa kubwa. Tishio la kulazimika kuondoka kwangu lilikuwa kubwa zaidi. Mimi, ambaye sijapata kutoka nje ya vijiji viwili vitatu vinavyotuzunguka katika eneo hilo, nitakwenda wapi? Na nitarudi kweli? Nilihisi chozi likinitoka na kuteleza hadi kidevuni kwangu. Nikalifuta harakaharaka kuchelea babu asilione. Aliliona. Lakini, kwa mara ya kwanza, hakunishutumu kwa kitendo hicho cha Mwananume kulia.
“Najua hiki ni kipindi kigumu sana kwako, mjukuu wangu. Lakini wewe ni mwanamume. Ulitarajia nini katika maisha yako? Uzaliwe hapa, ukulie hapa, ufie hapa? Bahati ya mwanamume iko miguuni mwake. Lazima utoke. Lazima ukatafute elimu ili ubadili maisha yako. Chukulia tishio la maisha yako kama changamoto inayokupa msukumo wa kuondoka hapa haraka zaidi, si vinginevyo.” Babu alinihubiria. Aliongeza kuwa siku zote alikuwa na nia ya kuhakikisha naondoka hapo kijijini kwenda nchi za mbali kutafuta elimu ya maisha mapya. Lakini wakati ulikuwa haujajiri. “Wakati huo
sasa umefika. Huna budi kuacha kijiji na kuikabili dunia.” “Nitakwenda wapi?” niliuliza ghafla. Hisia fulani rohoni
mwangu zikinishangaza. Nilihisi kama ambaye nilikuwa tayari nimeridhika na maelezo yake na kuanza kujenga shahuku ya kuifanya safari hiyo mara moja.
 
SEHEMU YA 19

“Swali zuri sana,” babu alinijibu. “Ni swali ambalo nilikwishalifikiria kwa muda mrefu na kulipatia ufumbuzi. Utaelekea kaskazini, katika nchi ya Wahaya. Huko Wazungu wanaotangaza dini yao, tayari wamejenga shule na wanapokea watoto na kuwafundisha kusoma na kuandika.”
Nitafikia kwa nani? Nitakula nini? Nikiugua atanisaidia nani? Ni miongoni mwa maswali lukuki ambayo yalijaa katika kichwa changu. Nilitamani kumuuliza hayo babu, lakini nilisita kwa kujua kuwa angeyapuuza mara moja. Si alikwishaniambia kuwa bahati ya mwanamume iko miguuni mwake? Nikapiga moyo konde na kufikia uamuzi. Lazima niondoke.
Babu aliusoma uamuzi wangu katika macho yangu. Akatabasamu. Kisha akasema, “Wewe ni mwanamume. Siku zote nilijua kuwa mwanangu amezaa dume la simba. Kazi iliyobaki sasa ni maandalizi ya safari yako. Si unafahamu kuwa tunataka iwe siri?”

* * *
Kuagana na wazazi wangu lilikuwa jukumu zito kuliko nilivyodhania, hasa ukizingatia kuwa zoezi hilo lilikuwa la ghafla sana na lilifanyika kwa siri sana. Mara tu baada ya maafikiano yangu na babu tulirejea nyumbani ambako babu alimweleza mwanae uamuzi wangu. Baba hakuwa na hiari ingawa aliipokea habari hiyo kwa majonzi makubwa.
Tatizo kubwa lilikuwa kwa mama. Kwanza, hakuamini masikio yake. Kulikuwa na mpango wa mtoto wake wa pekee kutolewa kafara kwa siri. Hilo la kuondoka kwangu pia kwake lilikuwa pigo jingine. Mama alichukulia safari yangu sawa na kifo changu. Aliangua kilio cha kwikwi, huku akisema, “Sikubali mwanangu aondoke. Sikubali kabisa.”



Babu na baba walimsihi aache kulia na kisha kumfahamisha umuhimu wa kuondoka kwangu. “Ataokoa maisha yake na atapata elimu.” Walimwambia.
“Nani atampikia chakula? Akiugua nani anajua dawa zake? Akifa huko tutajuaje?” Mama aliendelea kulalamika. “Sikubali! Labda niondoke na mwanangu!”
Ilichukua muda mrefu kumshawishi mama. Aliporidhika alinitemea mate kwenye paji la uso kuniombea baraka, “Mwanangu, Mtukwao, nenda salama, urudi salama. Kumbuka wazazi wako tupo na tunakupenda sana. Usitusahau asilani.” Alisema huku akiwa ameweka mkono wake wa kushoto kifuani mwangu.
Nilishindwa kujizuia. Machozi yalinitoka. Hakuna aliyenishutumu.
 
SEHEMU YA 20

2SURA PILI

Porini… Simba.

afari ilianza alfajiri sana, yapata saa tisa au kumi hivi. Nyasi na majani yalijaa umande mwingi ambao ulifanya tulowe chapachapa, dakika
chache tu baada ya safari. Kiza pia kilikuwa kimetanda huko na huko kuongeza ugumu wa safari. Kwa kweli, mimi sikujua kama tunaelekea upande upi; mashariki au magharibi, kaskazini au kusini. Nilichofanya ni kumfuata babu ambaye alikuwa mbele yangu, akitembea kwa ule mwendo wake mkali, wa hatua ndefundefu ambao mara nyingine ulifanya nitembee huku nikikimbia ili niwe naye sambamba. Babu alikuwa amejitolea kunisindikiza hadi atakaponiacha katika mikono salama. Uamuzi wake, kwa kuzingatia umri wake na urefu wa safari, ulipingwa sana na baba. Lakini haikuwepo njia nyingine. Babu alionya kuwa umri wangu haukuniruhusu kusafiri maporini peke yangu. Hali kadhalika, alichelea kuwa kama baba angetoweka kijijini hapo pamoja na mimi ingekuwa dhahiri kuwa amenitorosha, jambo ambalo lingemletea matatizo makubwa na wanakijiji wenzake. Zaidi, kwa kuwa babu alijua lugha mbalimbali za kigeni aliamini kuwa wamisheni wenye shule wangemsikiliza kwa makini zaidi na kunipokea, kwani shule nyingi alisema
zimejengwa kwa ajili ya watoto wa Machifu.



“Lakini kuna sababu nyingine. Kwa umri wangu huu huenda mjukuu wangu atakaporudi hatanikuta nikiwa hai, wakati bado nina mengi ya kumfundisha. Hivyo, katika safari yetu ndefu nitapata wasaa wa kumrithisha hiki na kile ambacho kitamfaa katika maisha yake.” Babu aliongeza hoja ambayo si baba wala mama aliyeipinga.
Usiku huo wa kuamkia safari sikupata usingizi. Kichwa changu kilijaa maswali mengi pasi ya jibu hata moja. Kiwingu cha hofu kilitanda katika fikra zangu kiasi kwamba hata nilipopata lepe dogo la usingizi, ulikuwa wa mang’amung’amu; ukiambatana na ndoto za kutisha. Hali hii ilisababisha nikurupuke mara kwa mara na kukodolea macho kiza kilichotanda chumbani humo.
Kitu kingine kilichonikosesha raha ni mlio wa bundi. Katikati ya usiku bundi mmoja alitua juu ya paa la nyumba yetu na kuanzisha kile kilio chake chenye sauti mbaya ya kutisha. Hakuna mtu ambaye hakujua kuwa bundi kukesha katika mji wako akilia ni dalili mbaya. Mara nyingi huashiria msiba au nuksi itakayoipata familia hiyo. Hivyo, wakati babu aliponiamsha na kuninong’oneza ‘tuondoke’ hata kabla jogoo hajawika nilianza safari nikiwa na moyo mzito sana.
‘Kwa heri Buha…. Kwa heri Kasulu… Kwa heri Heru…’ nilihisi moyo wangu ukinong’ona wakati nikichukua furushi langu dogo, lenye ngozi, kipande cha kaniki na akiba ya chakula njiani. Nje ya nyumba babu alikata fimbo mbili toka kwenye matawi ya miti na kunipa moja. Sikuhitaji kuambiwa kazi ya fimbo hizo. Zilitumiwa kupiga majani ya mbele yako kwa ajili ya kupunguza umande. Fimbo hizo hazikufua dafu kutokana na ukubwa wa pori ambalo katika sehemu fulanifulani nyasi zilitumeza kabisa.
 
SEHEMU YA 21
Tulimsikia jogoo wa kwanza akiwika toka mbali baada ya mwendo wa dakika zipatazo arobaini hivi. Muda mfupi baadaye jogoo wengine walianza kuwika toka huko na huko wakiashiria mapambazuko. Hawa walifuatiwa na milio ya ndege wa alfajiri toka katika matawi ya miti mbalimbali. Muda mfupi baadaye dalili ya mapambazuko zilijidhihirisha zaidi. Hali ya hewa ilibadilika kwa namna fulani na kiza kuonekana kama kimetamalaki zaidi. Kisha, mashariki ilianza kubadilika na miale yenye rangi ya dhahabu kuanza kuchomoza toka nyuma ya vilima na mti toka mbali.
“Kumekucha,” babu alisema taratibu.
Nadhani hakutarajia jibu. Hivyo, sikumjibu chochote. Nilichofanya ni kuongeza hatua zangu ili kuwa naye karibu zaidi.
Jua lilichomoza kwa maringo, hatua baada ya hatua. Tahamaki miale yake murua yenye rangi ya dhahabu ilianza kupenya na kuifikia miili yetu ambayo ilikuwa taabani kwa baridi. Taratibu joto la miale hiyo lilikausha umande katika miili yetu na kuifariji. Nilijihisi nikichangamka si mwilini tu, bali pamoja na moyoni pia.
Nadhani babu alichangamka pia kwani nilimwona akitabasamu na baadaye kusema taratibu, “Jua ni Mfalme, unajua kuwa nchi nyingine huko Ulaya waliabudu jua na kulichukulia kama Mfalme wao?”
Sikumwelewa. Wakati bado natafakari kauli yake hiyo aliongeza nyingine, “Unajua huko Ulaya kuna nchi ambazo huwa hawalioni jua kwa karibu mwaka mzima?”
Babu alinichanganya zaidi.
“Sasa wanaishije bila jua?” nilimuuliza.
“Wanaishi kwa kuvaa makoti makubwa na



kujifunika mablanketi mazito. Mchana na usiku wanakoka moto majumbani mwao kutafuta joto.” Alieleza. Kwajinsinilivyomfahamubabunilijuabaadayakuchangamshwa na jua hilo amepata nguvu na kuanza hadithi zake zisizo na mwisho. Nilikuwa nimechoka. Nilikuwa tayari najisikia njaa. Nilichelea kumjibu kungemfanya aongeze hadithi nyingine. Nikakaa kimya nikifikiria namna ya kumwomba tupumzike kidogo.
Kana kwamba alikuwa akiyasoma mawazo yangu babu mwenyewe alishauri tupumzike. Nilishukuru kimoyomoyo.
Nikamwonyesha babu mbuyu mkubwa wenye kivuli mwanana na kumtaka tukapumzike pale. Babu alitikisa kichwa kukataa. “Mbuyu sio mti mzuri sana wa kukaa chini yake. Unajua mbuyu unaishi maisha marefu pengine kuliko miti yote duniani? Mara nyingi mizimu na mashetani pia hufanya mibuyu makazi yao. Jitahidi kuiepuka.” Babu alinieleza na kunishauri.
Haikuwa hadithi mpya kwangu. Mara kwa mara tulikuwa tukionywa kucheza chini ya mibuyu na hasa kuingia katika mapango makubwa ambayo huchimbika katika mashina ya mibuyu mikongwe zaidi. Tunaambiwa humo wanaishi majini au mashetani katika sura mbalimbali. Pia tunaambiwa kwamba baadhi ya viumbe hai huonekana katika sura ya nyoka, ndege au wanyama wengine.
Tulitembea zaidi ya dakika tano nyingine kabla hatujafikia eneo lililozagaa mivule mingi na kufanya kuwe na kivuli kikubwa. Tuliketi juu ya magogo ya miti iliyokufa na kuifungua akiba yetu ya chakula. Tulikuwa na mihogo ya kuchemsha, ndizi, nyama kavu ya nyati na ugali wa lowe. Tulikula kimyakimya, ndege wadogo wakitumbuiza kwa
 
SEHEMU YA 22
nyimbo zao tamu toka kwenye matawi ya miti hiyo. Baadhi ya ndege hao, tetere na kitororo, waliruka juu yetu mara kwa mara kama wanaotushangaa kwa kuwepo kwetu pale. Muda mfupi baadaye kundi kubwa la tumbiri lilivamia miti hiyo na kuanza kuruka toka tawi hadi tawi juu ya vichwa vyetu kwa namna ya kutudhihaki
“Dalili njema.” Babu alisema. “Safari yetu itakuwa nzuri,” aliongeza.
Nikaona huo ulikuwa wasaa muafaka wa kutoa dukuduku langu. “Lakini babu,” nilimwambia. “Mbona usiku wa leo bundi amekesha akilia juu ya paa la nyumba yetu? Si wanasema bundi kulia juu ya nyumba usiku ni ishara ya balaa?”
Babu alitafakari hilo kwa makini. Baadaye alisema, “Bundi ni ndege wa usiku. Haoni mchana ndio maana kutwa nzima hushinda amelala. Usiku hutoka na kuanza mawindo yake. Anapenda kula panya na ndege wengine wadogowadogo. Kuna imani nyingi juu ya bundi katika makabila na mataifa mbalimbali. Kwa mfano, wakati huku kwetu wengi tunamchukulia bundi kama nuksi, nchi nyingine huko Ulaya bundi akikesha analia kwenye nyumba yao wenyeji hufurahi sana na hata kufanya sherehe. Wao wanakichukulia kitendo hicho kama dalili ya neema.”
Ilikuwa habari mpya kwangu, “Umejuaje yote hayo babu?” nilimuuliza.
“Kutembea mjukuu wangu, wanasema, ‘kutembea ni shule.’ Halafu kuna wale waliosema. ‘kuishi kwingi ni kuona mengi. Mimi nimetembea sana, halafu nimekula chumvi nyingi.”



Kwa muda tuliendelea kula kimyakimya. Tulipotosheka tulifunga vibuyu vyetu ambavyo bibi alituandalia maziwa ya ng’ombe kwa ajili yangu na togwa kwa ajili ya babu. Tukanywa taratibu huku tukiwa tayari tumewapuuza ndege waliokuwa wakicheza juu ya vichwa vyetu. Nadhani baadaye nao pia walitupuuza kwani walishika hamsini zao na kuendelea na shughuli zao kana kwamba hatupo.
Babu alishauri tupumzike kidogo chini ya mti huo, uamuzi ambao niliupokea kwa mikono miwili. Nikajinyoosha chali, juu ya majani makavu na kuyafumba macho yangu kwa matarajio ya kupumzika kidogo. Kwa mshangao usingizi mtamu ukanipitia. Ama babu pia alilala, ama aliamua kuniacha nilale kwani nilipofumbua macho tena ilikuwa jioni, jua likielekea kuzama. Babu alikuwa kaketi palepale akinitazama.
“Umepumzika vya kutosha,” Babu aliniambia. “Tuendelee na safari. Leo ningependa tulale karibu na Makere, kesho jioni tuamkie Mto Malagharasi na kulala Nyakisogo ili ikiwezekana keshokutwa tufike Kibondo.”

* * *
Laiti babu angejua ratiba aliyopanga ingetibuliwa mara moja, bila shaka asingefuata njia hiyo tuliyokuwa tukiifuata.
Ratiba yake iliharibika kesho yake tu, wakatitukiukaribia Mto Malagharasi. Tulikuwa tumejipumzisha chini ya mti, baada ya kula na kunywa maji safi toka katika kimojawapo cha vijito vingi vilivyokuwa vimetapakaa katika eneo hilo, vijito ambavyo kwa ajili ya ukame vingi vilianza kuonyesha dalili ya kukauka.
Mara tulisikia mlio wa bunduki, ukifuatiwa na vilio na kelele za watu wanaolia au kukimbia kwa hofu. Babu
 
SEHEMU YA 23

aliniamuru kupanda mti mara moja kwa nia ya kujificha. Yeye pia akapanda mti huo. Tulienda hadi kwenye matawi ya juu na kutulia huku tukiangalia purukushani toka mbali. Tuliwaona watu wapatao kumi wakiwa wamefungwa mikono wawiliwawili, wakiongozwa na watu waliovaa kaptula za kaki na viatu vizito. Hawa walishika marungu. Nyuma yao kulikuwa na watu weupe wawili waliobeba bunduki.
Watu hao walipofika chini ya mti na kuona mizigo yetu hawakuangaika kututafuta. Walitupa macho yao juu na kutuona tulivyoning’inia kwenye matawi kama nyani.
“Shuka chini.” Mmoja wao aliamuru kwa sauti kubwa.
Nilimtazama babu kwa hofu. Nikamwona akianza kushuka taratibu. Nikamfuata.Tulipofika chini tuliamriwa kukaa chini pamoja na wale mateka wengine, amri ambayo babu alikataa.
“Nyie nani?” aliwauliza watu hao ambao walikuwa bado wameduwaa kwa kitendo chake cha kugomea amri yao.
“Huoni kama sisi ni askari?” wale askari weusi walijibu. Mmoja wao aliongeza, “Wale pale ni maafisa wa kodi.” Alielekeza kidole chake kwa Wazungu waliokuwa wakitazama zoezi hilo kana kwamba haliwahusu.
“Enhe! Mkiwa askari kwangu mnataka nini?” babu aliwahoji tena.
“Tunakamata watu wote wanaoishi juu ya miti kama tumbili,” mwingine alijibu.
Babu: Kwa nini?
Askari: kwasababu watu wanaoishi juu ya miti ni wale ambao hawajalipa kodi.
Tuonyeshe kipande chako cha kodi.
Hadi hapo nilijua mambo yameharibika. Babu alikuwa



mbishi sana katika suala la kodi. Kama nakumbuka vizuri hakupata kulipa kodi hata mara moja. Kila ulipofika msimu wa kodi yeye alibadilika na kuwa mkali kama pilipili. Ilifikia hatua askari wa kodi walimkwepa na kumkimbia kwa ukali na ubishi mwingi aliokuwa akiutoa kiasi cha wao kujiona wapumbavu mbele yake.
Nilimwona babu akitabasamu. Kisha aliuliza, “Kodi hiyo nimlipe nani?”
Askari: Unailipa serikali ya Uingereza. Ni amri halali ya Malkia. Wale pale ni wawakilishi wa Gavana.
Babu alicheka tena. “Majuzi,” alisema “Walipita Waarabu wakikamata watumwa na kuwauza kwa kisingizio cha kodi. Baadaye walikuja Wabelgiji na kuanza kudai kodi. Siku chache baadaye tukawaona Wajerumani. Wao pia walitudai kodi kwa jeuri na ukatili mkubwa. Leo tunaambiwa ni zamu ya Waingereza. Na nyie weusi kama mimi, ndio mko mbele kunidai kodi! Vichwa vyenu vinafanya kazi kweli nyie?” Askari hao waliduwaa. Mmoja alikasirika na kuinua rungu lake tayari kumtwanga nalo babu kichwani. Mmoja wa askari wa Kizungu, aliyeelekea kuvutiwa na mdahalo huo alimzuia askari huyo na kisha yeye mwenyewe kumkabili
babu, “Weye iko nani?” alihoji kwa Kiswahili chake kibovu.
Askari huyo alipigwa na butwaa pale babu alipomjibu kwa Kiingereza fasaha, “Mimi ni raia wa nchi hii. Nimekaa kwenu nikawalipa kodi. Nimerudi kwetu mnataka niwalipe kodi! Tena mnadai kwa mtutu wa bunduki kama majambazi! Sijawahi na wala haitanitokea kamwe kumlipa kodi mgeni!”
Wazungu wale walipigwa na butwaa, kitendo ambacho yule askari mweusi, mwenye jazba, alikitafsiri kitendo hicho
 
SEHEMU YA 24

kuwa ni kashfa kwa maafisa hao. Bila subira wala simile aliinua rungu ili ampige nalo babu kichwani. Lilikuwa kosa ambalo askari huyo atalijutia milele kwani babu alimkwepa na hapohapo kumpiga ngumi tatu za usoni ambazo zilimfanya askari huyo ateme mate yenye damu na jino lake moja. Pua yake pia ilitokwa na damu nzito. Askari wa pili alipotaka kuingilia kati Wazungu wale walimzuia. Badala yake walimkodolea babu macho ya mshangao mkubwa zaidi. Kwa umri wake, hawakuamini kuwa babu angeweza kuwa mwepesi na mwenye nguvu kiasi kile.
“Wewe ni nani?” walimuuliza tena taratibu. “Naitwa Kionambali, Mtukwao.”
“Unatoka wapi, unakwenda wapi?”
“Natoka Buha. Nakwenda nchi ya Wahaya.”
“Unajua kutolipa kodi ni kosa kubwa? Unajua kumshambulia mtumishi wa Malkia ni kosa kubwa zaidi?”
Babu hakujibu.
“Unajua adhabu ya makosa yako? Kwa umri wako huo unajua kuwa tukikupeleka jela utafia huko na kupigwa viboko vitano kila siku ya uhai wako gerezani?”
Babu hakujibu vilevile.
“Mfungeni mikono,” mzungu huyo alitoa amri. Babu alipotaka kuanzisha vurumai jingine mzungu huyo aliinua bunduki na kufyatua risasi moja hewani. “Risasi ya pili hapana kwenda hewani. Takwenda moja kwa moja katika kifua yako.” Alionya.
Babu alinywea na kuruhusu mikono yake yote miwili ifungwe kwa pamoja.
“Twende,” Mzungu huyo alimsukuma babu kwa tako la bunduki yake.



Babu aligeuka kunitazama. Kisha alimgeukia Mzungu yule na kumuuliza “Mjukuu wangu nitamwacha na nani?
“Hapana kazi yetu,” Mzungu alimjibu kikatili. “Taishi kwenye miti kama nyama. Takula matunda ya porini kama ndege. Kama nachoka tarudi nyumbani yenu.”
Babu alipojaribu kubisha tena yule askari aliyeumizwa aliitumia fursa hiyo. Alimpiga babu kichwani kwa rungu lake kwa nguvu zake zote. Babu alipepesuka na kuanguka chini. Damu nyingi zilimtoka kisogoni.
Sikuweza kuvumilia. Nilikurupuka na kumvamia yule askari kwa nia ya kumpiga tumboni. Aliniwahi. Akanipiga makofi makali na kunisukuma. Nilipepesuka na kumfuata tena. Safari hii alinipokea kwa rungu la kichwa ambalo lilinifanya nipoteze fahamu na kudondoka chini kama mzoga

* * *
Sikumbuki nilipoteza fahamu kwa muda gani.
Nadhani ilikuwa zaidi ya saa sita. Ninachokumbuka ni pale nilipokurupuka baada ya kupatwa na hisia za hatari. Kitu kama kishindo au mlio fulani ndio ulionizindua ghafla. Kweli. Mara nilipoinuka niliona kitu au mnyama fulani mkubwa akiruka na kukimbia. Tukio hilo lilifuatiwa na kicheko au kilio cha kuogofaya.
Fisi!
Wala hakuwa fisi mmoja. Milio yao iliashiria kuwepo kwa fisi wengi katika eneo hilo. Bila shaka walikuwa wakininyemelea kwa matumaini kuwa ningekata roho ili waule mzoga wangu!
Nilipatwa na hofu kubwa. Fisi ni mnyama mwoga lakini mwenye nguvu nyingi. Taya na meno yake pia yana nguvu sana kwani mifupa uliomshinda yeye hakuna mnyama mwingine
 
SEHEMU YA 25

anayeuweza. Fisi huenda kushambulia wanyama wadogo au wagonjwa, ingawa mara nyingi uwa yuko nyuma ya simba akisubiri aue mnyama, amle ili yeye aambulie mabaki. Fisi ni mnyama mvumilivu pia. Anaweza kumfuatilia, mnyama au binadamu mgonjwa hata kwa siku tatu atakapoishiwa nguvu ili amle.
Sikuwa tayari kufanya mzaha na fisi. Mara moja nilitafuta mti uliokuwa karibu na kuuparamia. Pamoja na kiza totoro kutanda huko na huko niliufahamu mtu huo kuwa ni uleule ambao muda mfupi mimi na babu tuliutumia kujificha. Nikapanda hadi mahala penye tawi zuri ambapo niliweza kulala chali, nikajipumzisha. Ni hapo nilipopata wasaa wa kusikiliza maumivu makali niliyokuwa nayo toka kichwani, pale rungu la askari yule liliponipiga barabara.
Aidha, ni wakati huo nilipoweza kutafakari kwa kina masaibu yaliyonipata. Sikujua babu amepelekwa wapi. Sikujua kama alikuwa hai au tayari ameuawa. Sikuwa na hakika kama nitamwona tena mzee yule mwenye mengi ambayo nilitegemea hadi mwisho wa safari yetu awe amenichotea kiasi fulani, mzee niliyemchukulia kama fimbo au kitendawili ambacho kimetoweka kabla ya kuteguliwa.
Machozi yalinitoka.
Nikajifikiria mimi mwenyewe jana tu niliishi raha mustarehe kwa baba na mama leo nimekuwa yatima katikati ya msitu mkubwa wenye hatari zote. Sikujui ninapokwenda wala ninapotoka. Hata kama ningeweza kurudi nyumbani hatari ya kifo bado inanisubiri. Kuendelea na safari niliona ni kifo vilevile. Sikuwa mwerevu wa kutembea porini. Sikuwa na chakula. Zaidi ya yote sikujua njia. Sikujua kama nilipaswa kuelekea kushotoa au kulia, nyuma au mbele.



Machozi yalinitoka.
Sikuthubutu usingizi unipitie. Hofu ya kudondoka toka juu ya mti huo ni moja ya sababu zilizoninyima usingizi. Milio ya kuogofya ya ama wanyama wa porini ama ndege na wadudu wengine ni sababu ya pili. Lakini sababu kubwa zaidi iliyochangia kupaisha usingizi wangu ilikuwa mawazo tele yaliyojaa kichwani mwangu. Kwa kweli mawazo hayo yalinizidi kimo na hata umri. Iwapo ilinipasa kurudi au la iwapo ningeweza kuijua njia ya kurudi au la! Na kadhalika na kadhalika.
Hofu yangu iliongezeka maradufu, nusura nipige kelele pale nilipopata hisia za kitu kama mnyama au nyoka anayepanda taratibu juu ya mti huo. Huku nikitetemeka niliyakaza macho yangu kwa nguvu zote ili niweze kuona kitu hicho. Hofu yangu kubwa ilikuwa ya chui, mnyama ambaye anapenda sana kujificha juu ya mti wakati akiwinda. Aina fulani ya chatu pia wana tabia ya kuparamia miti na kujipumzisha juu ya matawi. Nilihisi maisha yangu yamefikia ukiongoni, kwani yeyote kati yao, angenishambulia ama kwa hofu ya kunikuta huku ama kwa njaa.
Kitu hicho kiliendelea kupanda juu, taratibu na kimyakimya kama kivuli. Nilianza kupapasa huku na huko kwa matarajio ya kupata tawi la mti lililokatika ili nilitumie kujitetea katika kupigania roho yangu. Sikupata. Akili fulani ikanishauri nijitetee kwa kukitisha kiumbe hicho kwa sauti. Nikakohoa kwa nguvu. Kwa mshango wangu kiumbe huyo alikohoa kwa sauti ya binadamu. Sikuyaamini masikio yangu. Nikakohoa tena.
Kitendo hicho kilifuatiwa na sauti ya binadamu iliyoita taratibu, “Mtukwao?”
Ilikuwa sauti niliyoifahamu fika, sauti ambayo


ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 26

sikutarajia kuisikia tena katika maisha yangu! “Babu,” niliita kwa sauti ya chini vilevile. “Naam,” alinijibu.
Nilitamani kupiga ukelele wa furaha. “Umerudi?
Wamekuachia?”
Nilimsikia babu akicheka kabla hajasema, “Wale ni watoto wadogo. Msitu huu ni wetu na ni mkubwa sana kwao. Umejaa miti na miti. Kwao kila mti ni mti. Kwangu mie kuna miti na mitishamba. Liko jani dogo tu, ambalo nimelichuma na kulitafuna, wakawa hawanioni wala hawanikumbuki tena. Nimewaacha wakihangaika ovyo, wasipoangalia hata njia ya kurudi walikotoka hawataiona.”
Zamani kidogo nilikuwa nikishangazwa na vitendo na simulizi za babu. Lakini baada ya kuishi nae kwa muda mrefu nilikoma kushangazwa naye. kila alilofanya, kila alilosema, nililichukulia kama lilivyo. Kwa mfano, sikuwa na uhakika iwapo ujio wake huo kweli ulitokana na ujuzi wake wa mitishamba au wa watekaji wake walikuwa wamwachie kutokana na ukubwa wa umri wake. Kwa kweli, sikujishughulisha kutafuta ukweli. Sikuwa na nafasi. Moyo wangu ulikuwa umefura kwa furaha ya kumwona tena. Matumaini ya kuendelea na safari yetu.
Nilitamani kushuka chini, ili nikutane naye na kumkumbatia. Lakini kana kwamba anayasoma mawazo yangu nilimsikia akisema, “Lala kama uko mahala pazuri. Kesho tutaanza safari mapema sana. Wale wajinga tayari wametuchelewesha sana.”
Sikuweza kulala.

* * *



Safari ilianza mapema kama ilivyokusudiwa. Tulishuka kwenye mti huo alfajiri sana, wakati kiza bado kimetanda. Tukakata miti ya kupunguzia umande na kujitoma tena katika vichochoro, katikati ya pori. Nilimfuata babu mgongoni mwake kiasi nikitetemeka kwa baridi kwa kweli sikujua tunaelekea upande gani wa dunia.
Aidha sikujua kama tunakwenda mbele au tunarudi nyuma.
Ilikuwa safari ngumu kuliko ilivyoanza. Akiba yetu ya chakula na maji ya kunywa ilikuwa imetoweka. Bila shaka vifurushi vile vikiwa vimeporwa na fisi au mbweha ambao walikesha chini ya mti ule tuliolala wakirandaranda huku na huko kwa matarajio waliyoyafahamu wao. Hata blanketi langu na nguo za babu za kubadili pia zilikuwa zimetoweka lakini kilichomsikitisha zaidi babu ni rupia zake kumi zilizokuwa ndani ya mzigo huo. Zilikuwa zimepotea pia.
Pamoja na kuficha hisia, zake niliweza kumsoma babu kuwa hana raha kabisa. Ile hamasa ya safari tuliyoanza nayo ilikuwa imetoweka tangu alipozitafuta pesa zake bila mafanikio. Hata hivyo hakutamka neno lolote la kunung’unika zaidi ya kunihimiza niongeze mwendo kila alipogeuka na kubaini kuwa ameniacha hatua nyingi nyuma.
“Tutakula nini?” Nilimchokoza kwa nia ya kuanzisha maongezi.
“Msitu huu unawalisha ndege wasio na mikono na wanyama wasio na akili za kutosha. Itashindwa kutulisha mimi na wewe?” Alinijibu kwa swali jingine.
Wakati jua linachomoza tulikuwa tuko mbali sana. Jua lilileta neema kwa kutuzawadia nuru. Pia lilituondolea umande toka kwenye matawi ya miti yaliyotufunika. Lakini
 
SEHEMU YA 27

neema hiyo haikudumu. Muda mfupi baadaye jua liligeuka kero. Lilisababisha joto kali kiasi cha kufanya miili yetu iliyokuwa ikitetemeka kwa baridi, muda mfupi baadaye ilianza kuloa kwa jasho. Nadhani jua pia lilileta njaa na uchovu. Nilitamani kumwambia babu tupumzike. Nikasita. Nilimwona kama mtu aliyekuwa mbali kimawazo ambaye hangefurahia kubughudhiwa kwa wakati huo.
Hata hivyo, tulipofika kwenye mti mmoja wenye matunda ya porini, ambayo sikubahatika kuufahamu jina babu alisimama. Akanyoosha mkono na kuangua tunda moja lililoiva akalila. Nilifuata mfano wake. Matunda ya karibu yalipopungua niliamua kuyafuata hukohuko juu ya mti.
Tulikula kefu yetu. Kisha tukaendelea na safari. Huku mbele tulipata kijito chenye maji murua ambayo tuliyatumia kwa kunywa na baadaye kuoga. Tulipumzika chini ya kivuli cha miti mingi iliyoneemeka kando ya kijito hicho kwa muda kabla ya kuendelea na safari yetu.
Sikumbuki tulitembea maporini humo kwa siku ngapi. Wala sikumbuki idadi kamili ya matukio tuliyopambana nayo na yepi yalikuwa ya kutisha, yepi ya kuchekesha na yepi ya kusisimua. Nilichokumbuka ni kwamba ilikuwa safari ndefu, ngumu na ambayo iliambatana na kila aina ya visa na matukio. Baadhi ya matukio hayo yalikuwa ya kusisimua yaliyonipa ari ya kuendelea na safari.
Kwa mfano, lilikuwepo tukio la kukutana ana kwa ana na simba dume. Siku hiyo babu aliapa kuwa lazima tule nyama badala ya matunda na mizizi kama ndege. Alitafuta vichochoro vya wanyama na kujificha kando ya kimojawapo huku mkononi akiwa na pande kubwa la gogo. Haikuchukua muda mrefu kabla hajapita nguruwe mwitu katika uchochoro huo. Babu



hakuwa amejitayarisha vizuri. Hivyo, aliporusha gogo lake kwa nia ya kupiga kichwa cha mnyama huyo, alikosea shaba. Gogo lilianguka kando ya kichwa hicho. Nguruwe alikurupuka na kutimua mbio kali. Nilishangaa kuona babu akiokota gogo lake na kujificha palepale akitazama kwa makini upande alikoelekea mnyama yule.
Babu aliusoma mshangao wangu. Akacheka kidogo kabla ya kusema, “Atarudi njia hiihii. Nguruwe ni mnyama wa ajabu. Nadhani ana ubongo mdogo kuliko wanyama wengine wote. Huko mbele atachoka. Atakapojipumzisha usingizi mzito utamchukua. Akiwa amelala ataota ndoto ya tukio hili la leo. Ataliona kama la miaka mingi sana. Ataona kwamba aliwahi kupita njia fulani. Akakurupushwa na kitu fulani. Atakuwa hakumbuki ni kitu gani. Hivyo, atakapoamka ataamua kurudi njia ileile ili akaone kitu gani kilichomkurupusha. Hivyo ndivyo ambavyo wawindaji huwapata nguruwe kwa urahisi. Wanachokihitaji ni subira tu.”
Nilitamani kucheka. Lakini kwa kuhofia sauti ya nguruwe ingefichua maficho yetu, nilikaa kimya nikiutafakari ubongo wa nguruwe.
Kweli! Haikupita muda mrefu tulimwona nguruwe yuleyule akirudi njia ileile kwa kasi ileile. Nilimwona babu akiwa ameshangaa. Bila shaka alitarajia nguruwe yule aje taratibu, alitazama huko na huko kutafuta kulichomkurupusha mwaka jana. Safari hii babu alikuwa amejiandaa. Pigo la gongo lake lilitua barabaraba juu ya kichwa cha nguruwe. Nguruwe akapepesuka na kisha alianguka chali huku akirusha miguu yake huko na huko katika harakati za kuzuia uhai wake ulikuwa ukitoweka.
Mara jambo la ajabu likatokea. Hata kabla nguruwe huyo hajakata roho, mnyama mwingine mkubwa zaidi mwenye
 
SEHEMU YA 28

shada la manyoya mabegani mwake alichupa na kutua juu ya nguruwe huyo!
“Simba!” babu alisema kwa nguvu. Mara moja mkono wake ukaelekea kiunoni mwake. Palipokuwa na kisu chake.
Inaelekea, kama babu, simba huyo hakuwa na ndoto ya kukutana na binadamu mahala hapo, muda huo. Ni wazi kuwa yeye ndiye aliyekuwa amemkurupusha nguruwe huko alikokimbilia kabla hajalala na kuota ndoto zake ambazo zingemfanya arudi njia hiyo. Simba alimkazia babu macho ya mshangao ambayo pia yalibeba dalili za hofu. Babu naye alimkazia simba macho yake. Akimtazama jicho kwa jicho. Mara nilimwona simba akiepuka macho ya babu kwa kuinama chini, kisha alipiga hatua za taratibu, moja baada ya nyingine akiliacha windo lake na kutokomea porini.
Mara alipoondoka babu naye aliniashiria kuondoka mara moja. Anaweza kurudi na akirudi hatakuwa na simile tena.” Babu aliniambia wakati tukiondoka harakaharaka.
“Simba amekukimbia!” Nilimwuliza babu hali ya kutetemeka mwili ilipoanza kunitoka.
“Binadamu ni mfalme wa dunia hii.” Babu alinieleza. “Pamoja na ukweli kuwa sisi ni dhaifu kuliko viumbe wengi duniani, bado tunauwezo na utukufu fulani juu ya viumbe wengine. Wajuzi wa mambo wanasema kuwa, tuna uwezo wa kutawala hata majini na mashetani. Simba yule alishindwa kustahimili. Nuru yenye madaraka yaliyotoka katika macho yangu ilikuwa silaha tosha.”
Niliyatafakari maelezo yake kwa muda mrefu. Jambo hilo nahisi babu alilichukulia kuwa natilia mashaka maelezo yake. Hivyo, akanigeukia na kuniambia, “Zaidi ya utukufu huu tuliopewa na Muumba nina hii.” Toka kifuani mwake



alichomoa hirizi ndogo nyeusi iliyokuwa ikining’inia kifuani mwake siku zote.
“Hii ndio hasa inayotulinda,” alisema. “Niliirithi kwa babu yangu ambaye naye aliirithi kwa babu yake. Haijapata kutuangusha kamwe. Ilinipeleka Ughaibuni na ikanirudisha hapa salama.”
Tukio la pili ambalo pia sitalisahau ni lile la kujikuta tukiingia katika kundi la tembo wasipungua arobaini waliokuwa katika kitu kama tafrija au halaiki ya aina fulani.
Ilikuwa majira ya saa tisa au kumi za jioni. Mimi nilikuwa taabani kwa uchovu na njaa. Mayai mabichi ya kanga tuliyokula na matunda ya pori hayakukidhi haja yangu. Nilitamani sana kula ugali wa muhogo na kisamvu kisha nipooze koo kwa togwa tamu. Nadhani babu pia alikuwa amechoka. Alikuwa mkimya kuliko kawaida yake na alitembea taratibu kinyume na mazoea yake. Nilimwona akitazama huko na huko kama anayetafuta ama chakula ama mahala pa kupumzika. Wakati huo tulikuwa ndani kabisa ya msitu mnene wenye miti mingi mikubwa kwa midogo ambayo ilifanya nuru iwe hafifu na jua tulione kwa nadra sana. Mara tukasikia mlio wa waaa… waaa… waaa… uliosikika kwa sauti kubwa. Mlio huo ulifuatiwa na sauti kama hizo toka pande mbalimbali za msitu huo.
Tembo!
Wakati nikiwaza hilo niliona tembo watatu wakiwa wamesimama mbele yetu wakituangalia. Niligeuka kutaka kukimbia. Nyuma yetu walitokea tembo wengine huku mikonga yao ikielea huku na huku, pua zao zikichezacheza kama waliojaribu kuipata harufu yetu halisi. Mara tembo mkubwa zaidi alianza kusagasaga miguu yake ardhini huku akitumia
 
SEHEMU YA 29

mkoa wake kukatakata matawi ya miti na kukanyagakanyaga kwa hasira.
Kamababuasingenivutamkonokwanguvunakuniashiria kukimbilia mti mkubwa uliokuwa karibu na kuupanda, pengine tembo huyo angenifuata na kunikanyagakanyaga huku nikiwa nimeduwaa kwa hofu na taharuki iliyonishika. Kwa jinsi nilivyokuwa nikitetemeka, miguu na mikono yangu ikawa imeishiwa nguvu kabisa. Sijui nilipata wapi uwezo wa kuparamia mti huo na kuupanda hadi juu, babu akinifuatia. Tulipofika mahala salama, ambapo tembo hao wasingeweza kutufikia, tuliketi na kuwatazama.
Wakati huo, zaidi ya tembo ishirini walikwishakusanyika chini ya mti huo wakipiga kelele kwa sauti zao mbaya, za kutisha. Yule tembo mkubwa alitufuata mbio na alipoufikia mti wetu alijaribu kuung’oa kwa mkonga wake lakini mti ulikuwa mkubwa mno. Mkonga wake haukuweza kuuzunguka ili aweza kuuongo’a. Alipokata tamaa, alianza kuupiga kwa pembe zake kubwa. Pia hazikufua dafu. Akaamua kumalizia hasira zake kwa kung’oa miti midogomidogo ya jirani na kuturushia. Haikufika.
Nilikuwa bado natetemeka mwili mzima hivyo nilimshangaa kumsikia babu akiangua kicheko ambacho kilifuatiwa na maneno ambayo katika mazingira tofauti na hayo, yangeweza kunichekesha pia. “Kweli ukubwa wa pua sio wingi wa kamasi.”
“Una maana gani?” Baadaye nilimuuliza kwa sauti ya mnong’ono.
“Si unaona tembo hawa,” alinijibu. “Ni mkubwa kuliko wanyama wote wa nchi kavu. Baadhi yao wana ukubwa wa



nyumba ndogo na uzito upatao hadi kilo mia nne au zaidi. Lakini ubongo wao ni mdogo tofauti na maumbile yao. Wameshindwa kung’oa mti huu. Sasa wanashambulia miti midogomidogo isiyo na hatia. Kama sio ufinyu wa akili ni nini?”
Sikumjibu babu. Hali haikuniruhusu.
Tembo walipochoka waliamua kukaa chini ya mtu huo kana kwamba wanatusubiri hapohapo. Tukalazimika kulala juu ya mti huohuo na njaa yetu na kiu zetu.
Mimi sikulala.
Tembo waliondoka alfajiri sana kuendelea na safari zao.
Mie na babu pia tuliondoka na kushika hamsini zetu.
Ndiyo, ilikuwa safari ya kutisha iliyojaa visa na mikasa. Lakini kwa upande mwingine ilikuwa safari ya kusisimua ambayo kwangu ilitosha kuwa darasa mahususi ambalo si aghalabu sana kila mtu kukutana nalo. Ni safari ambayo ilinipa fursa na wasaha wa kuona mengi na kujifunza mengi.
Kwa mfano, tukiachana na tishio la simba na tembo, nilibahatika pia kukutana na burudani toka kwa ndege na wanyama wengine. Tuliweza kuingia na kutoka katika uwanda mpana uliojaa twiga na pundamilia kana kwamba wako zizini. Wakati pundamilia wanavutia kwa miramba yao iliyozunguka mwili mzima walitukimbia kidogokidogo kama mbuzi amkimbiavyo binadamu, twiga na mashingo yao marefu walitupuuza kana kwamba hatupo. Twiga walitumia shingo zao hizo kula majani na miche iliyochipukia juu kabisa ya matawi na miti. Miili yao mikubwa, miguu na shingo ndefu pamoja na rangi ya kuvutia yenye mabaka ya udongo kwa njano mpauko zaidi ule mwendo wao usio na haraka viliwafanya twiga waonekane kama wanaoringa na kujivunia umbile lao.
 
SEHEMU YA 30

“Kama simba ni mfalme wa msituni basi twiga ni malkia wa mwituni.” Babu alisema baada ya kuona nilivyowakodolea macho yao kwa husuda kwa muda mrefu. “Nani kama twiga?” Kabla ya twiga hao, nilikuwa nimevutiwa sana na ndege ambao tuliwakuta eneo moja lenye mabwawa mengi. Babu aliniambia kuwa eneo hilo linaitwa Moyowosi nje kidogo ya
Kibondo.
Kando ya mkondo mmoja wa mto huo tuliwaona heroe, wenye miguu na shingo ndefu mfano wa twiga na mdomo ulipinda pia. Na ndege hao wekundu walipenda kuwinda ndani ya maji. Pia tuliwaona ndege waliofanana na jogoo ambao babu alinielekeza kuwa waliitwa jogoo mwitu Kwembe - Kisunzu ambao wanamkia mfupi na manyoya yaliyoota katikati ya paji la uso kwa mpangilio kama panga la jogoo. Hondohondo, kibeti, kisi, kiguudani kiparara na ndege wengine ainaaina pia tuliwaona katika safari hiyo. Kila mmoja alikuwa na rangi yake, mlio wake na tabia zake.
Jambo jingine lililonifuraisha katika safari hiyo ngumu ni jinsi babu alivyotumia kila fursa kunielimisha juu ya kile alichokiita, “mitishamba”. Alinionyesha majani haya na yale na kunieleza matumizi na manufaa kwa binadamu.
“Unaona mti hule? Unaitwa Mguluka. Ule ni mti muhimu sana. Jitahidi kuukariri. Unatibu magonjwa mengi sana hata yale sugu. Unatibu ngiri, degedege na magonjwa ya kina mama. Unachukua magamba au mizizi yake na kuichemsha kisha unainywa kwa siku saba, kwisha.”
Babu alinionyesha miti aliyoitaja kama mvumbasa, mshashu, muuka, mzungwa, ulenge, ungwia na mlonge kuwa ni matibabu muafaka kwa maradhi mbalimbali. “Si hiyo tu.”



Babu alinieleza, “Kabla hatujafika mwisho wa safari hii pia, nitakuonyesha pia mnyembe, uwe na mingineyo ambayo si tu kuw inatibu bali pia hurefusha maisha ya mtumiaji.”
Kuna wakati babu alinishtua ghafla, “Angalia! Usikanyage jani hilo. Ukilikanyaga kama uko porini peke yako, utapotea siku nzima bila kuona njia ya kurudi nyumbani! Litazame uzuri jani hilo na ulikariri!”
Wakati mwingine babu alisikiliza mlio wa ndege au mnyama fulani na kuniamulu kubadili mwelekeo kuwa huko mbele kuna hatari fulani, “Ama simba wanawinda au wameua wanyama ama sokwe mtu wametanda.” Alionya.
 
Back
Top Bottom