Simulizi ya Kijasusi: Kiguu Na Njia

Simulizi ya Kijasusi: Kiguu Na Njia

SEHEMU YA 44 & 45

yake. Jambo hilo liliifanya serikali ya mkoloni imkamate na kumhukumu kunyongwa. Lakini hakuna aliyethubutu, kwani kabla ya hukumu hiyo kutekelezwa alifungwa katika kimojawapo cha visiwa vidogovidogo vilivyo baharini katika pwani ya Bahari ya Hindi, huko Dar es Salaam. Hata hivyo, ilielezwa kuwa Ng’wanamalundi huyo kila jioni alionekana katika vilabu vya pombe Dar es Salaam akiwa amevuka bahari kwa kutembea juu ya maji. Wakoloni wakalazimika kumwachia.
Sifa nyingine ya nchi ya Wasukuma ni zile hadithi kuwa kulikuwa na milima ya mawe, ama majini ama nchi kavu. Baadhi ya milima hiyo ilielezewa kuwa ilikuwa katika maumbile ya binadamu, ikiwa imesimama miaka nenda rudi kama inayosubiri mwujiza fulani utokee, ili ipate uhai na kuanza kutembea kama binadamu wengine.
Nchi hiyo pia ilikuwa ikisifiwa sana kwa ukubwa wa ardhi na wingi wa rutuba yake. Kilimo cha mazao ya chakula na yale ya biashara kama pamba na katani kilielezewa kuwa hakikupata kumtupa mtu. Kwa bahati mbaya, mimi sikupata kuwa mkulima wa haja. Wala sikuona kama ningeweza kuwa na ustahimilivu wa kulima leo kusubiri mavuno miezi au miaka kadhaa baadaye. Mimi nilikuwa mtu wa maji. Mtu wa kutupa nyavu na kuzitupa huku tayari zimejaa samaki! Hivyo, sababu kubwa iliyonipa msukumo wa kutamani kufika huko hasa lilikuwa ziwa. Jiografia yangu ilionyesha kuwa Wahaya na Wasukuma walichangia ziwa hili. Wakati Wahaya wakiwa Magharibi wakilitumia kwa shughuli zilezile.
Kwa kuzingatia hali yangu ya kutokuwa na kazi wala ujuzi wowote wa kuweza kupata ajira nyingine nililichukulia ziwa hili kuwa mkombozi wangu pekee. Nilitegemea ziwa



liniajiri, linilee, kwani taaluma ya uvuvi niliyoipata katika likizo zangu ilitosha kabisa kunipatia ajira hiyo.
Ni kwa mtazamo huo ndipo nilipojikuta nikijiunga na vikundi mbalimbali vya uvuvi kwa lengo la kujipatia fedha. Siku zote za uvuvi wangu nilifuata ziwa kuelekea upande wa kushoto kwangu badala ya upande wa kulia. Kama ningeelekea kushoto, ningelazimika kufika Uganda na baadaye Kenya, kabla ya kuingia Tarime, Musoma, Bunda hadi kufika Mwanza. Ingekuwa safari ndefu isiyo na sababu yoyote.
Mimi nilielekea kulia. Nilivua katika pwani na visiwa mbalimbali kama Bambire, Iroba, Rubondo na Nyamiende. Ilikuwa safari ndefu na ngumu sana. Takribani mwaka mzima uliishia njiani. Ama nilikwamishwa na ukosefu wa majahazi yanayoelekea huko nilikokuwa nikielekea, ama upepo mkali wa siku kadhaa ziwani ulifunga kabisa njia. Msimu wa masika ulioambatana na mvua kubwa za radi na mingurumo ya kutisha ni miongoni mwa sababu nyingine iliyonichelewesha njiani. Nililazimika kusubiri kwa zaidi ya miezi minne katika kijiji fulani huko Biharamulo.
Urefu huo wa safari ulikuwa na faida moja. Kwanza, ulinipa fursa ya kupata ukomavu na uvumilivu mkubwa katika pilikapilika za ziwani na nchi kavu. Ningeweza kuvumilia mvua ya siku mbili au tatu ikinipiga mwilini, niliweza kustahimili jua kali linalochoma kama mkaa wa moto. Niliweza pia kuipuuza njaa kwa muda mrefu. Zaidi, mwili wangu ulijenga uwezo mkubwa wa kuyashinda maradhi madogomadogo kama homa au tumbo bila haja ya kutumia dawa za madukani au mitishamba tele niliyopata kuelekezwa na babu.
Faida nyingine kubwa niliyoipata kutokana na urefu wa safari hiyo ilikuwa udugu. Nilikutana na watu mbalimbali,



nikashirikiana nao kwa hili na lile na kujikuta nimepata ndugu na marafiki tele, ambao kila nilipoondoka kuendelea na safari yangu walisikitika sana, lakini haikuwa kabla ya kunitakia kheri na baraka za safari.
Nilikosa raha kiasi pale tulipofika kisiwa cha Kome tukikaribia kabisa Mwanza. Rafiki zangu hao walishauri tubadili mwelekeo na kwenda kwanza Ukerewe. Tulifika Nansio. Tukafanya shughuli zetu za uvuvi hapa na pale, katika kijiji hiki na kile hadi tukajikuta tumeingia katika kisiwa kingine kidogo kiitwacho Ukara.
Ulipata kuona au kusikia juu ya mawe yanayocheza muziki? Kama hujapata hata kusikia mwenzio niliyaona kwa macho yangu katika kisiwa hicho cha Ukara. Kisiwa hicho kina mawe yaliyokaa kiajabu ajabu. Mtu anaweza kufikiria kuwa yalipangwa na binadamu, kwani baadhi yako juu ya mengine, yakiwa yamegusana kwa sehemu ndogo sana lakini hayadondoki si kwa mawimbi wala dhoruba la ziwani. Nilikuwa nikiyakodolea macho mara kwa mara mawe yale hadi mwenzangu mmoja aliposema, “Unashangaa kuyaona yalivyokaa, jee ukiyaona yanacheza?”
Nilidhani ni mzaha. Tulipobishana jamaa hawa walinipeleka katika kijiji cha Kome, ambako tulipata mwenyeji aliyetupelekeka eneo la Kululibha yalipo mawe haya ya ajabu. Mwenyeji wetu alitoa amri kwa lugha yake ya Kikara. Mara mawe hayo yakaanza kucheza kama watoto mapacha moja juu ya jingine. Hadi leo sijui ni kitu gani kinachotokea hadi mawe hayo yamtii binadamu.
Lakini huo si muujiza pekee wa Ukara. Pale kijijini kuna kisu chenye makali pande mbili. Unapotokea uhalifu wa aina yoyote watuhumiwa hupelekwa kwa mtaalamu na kuamriwa

ITAENDELEA
Ngj niagize alkhasus yangu hapa na miogo mibichi kusubiri jukwaa
 
SEHEMU YA 46 & 47

kukalia kisu hicho. Lakini si kwa mhalifu. Yeye hukatwa mara moja, hata awe amevaa nguo nzito kiasi gani. Kwa yale niliyoyaona, ya mawe kucheza, sikuwa na ubishi wowote kwa jambo hilo.
Maajabu mengine ambayo niliyaona kwa macho yangu, ni mti mmoja kijijini Chilabi huko Ukara. Mti huo ulipigwa na radi ukang’oka. Wenyeji wakaanza kujipanga ili waupasue mbao na kuni. Wakati kabla kazi hiyo haijaanza, mti huo ukiwa umesimama na kuota tena palepale ulipokuwa awali. Hata hivyo, haukuwa na majani. Mti huo upo hadi leo. Niliutazama, nikaupapasa. Unaonekana mkavu lakini unaishi.
Maajabu hayo yalifanya tulipoanza tena safari ya Mwanza niwe nimechangamka zaidi.






SURA YA TANO
Nawa Chifu Wa Wasukuma


akati huo nchi ya Wasukuma ilikuwa eneo kubwa kuliko yote nchini Tanganyika, lililojumuisha wilaya za Shinyanga, Maswa,
Mwanza, Kwimba na Geita. Wilaya tatu za mwisho zikiwa zinapatikana na ziwa Vitoria.
Isipokuwa kwa tofauti ndogo za kimatamshi baina ya Wasukuma na Wanyamwezi ambao walienea zaidi maeneo ya Tabora, wakazi hawa walichukuliwa kama kabila moja ambalo liliongozwa kwa idadi ya watu. Eneo hili lililokadiriwa kuwa na ukubwa wa kilometa za mraba 20,000 miaka ya 1945 na 1950 lilikisiwa na kuwa na watu wapatao milioni moja hivi.
Kabla ya wahamiaji wengi walioingia eneo hili kwa sababu zile na hizi makabila mengine ya asili katika eneo hilo yalikuwa pamoja na jirani zao wa sasa Wanyamwezi, ndugu zao Wanyantunzu na Wasukuma wenyewe.
Zaidi ya mandhari ya kuvutia ya ziwa, eneo hili lilifurika utajiri wa asili. Licha ya ardhi ya kandokando mwa ziwa kuwa na rutuba tele iliyokubali mazao mbalimbali, mbuga kama zile za Serengeti, zaidi ya kuvutia macho zilijaa wanyama wa kila aina. Aidha, licha ya mibuyu mikubwa yenye umri wa miaka nenda rudi ilikuwepo misitu mikubwa iliyobeba miti ya asili



aina mbalimbali ambayo baadhi ilipanda juu kwa takriban mita mia moja.
Kama ilivyo kwa Wahaya, Wasukuma na Wanyamwezi waliunganishwa na watawala na kijadi, ambao wengi wao walikuwa na asili ya wa Hima waliotokea Uganda baada ya kuwashinda maarifa ya utawala wale wa kibantu waliokuwepo. Watawala hawa ambao waliitwa Watemi, wasaidizi wao waliitwa Banagwa, walikuwa na nguvu nyingi za kiuchumi kutokana na kodi walizokuwa wakitoza raia wao na maeneo makubwa ya ardhi walizomiliki. Kiutawala, pia walikuwa na mamlaka makubwa kiasi kwamba kutoa hukumu ya kifo na ikatekelezwa lilikuwa jambo la kawaida.
Hayo na mengine mengi niliyajua siku mbili tatu tu baada ya kufika Nyamagana ambako kwa namna ya ajabu nilipata hifadhi katika himaya ya Chifu Masanja mwana Kasanga.
Hadi leo sijui kama tukio hilo lilikuwa mwendelezo wa bahati iliyotokana na hirizi au la baada ya hirizi kupotea. Ilikuwa ndio kwanza tumemaliza safari yetu, ambayo ilituchukua muda mrefu. Tulikuwa wanne, mimi, mzee mmoja na vijana wawili walionizidi kidogo umri.
Nilikutana na wavuvi hao katika kisiwa cha Kome ambako walikuwa wakivua samaki aina ya sato na kuwakausha kwa moto. Nilikaa nao kwa zaidi ya wiki moja kabla hawajaamua kurudi Nyamagana ambako walinielekeza kuwa ndiko yalikokuwa makazi yao.
Mara tulipofika nchi kavu na kuvuta mtumbwi ule, tulijikuta tumezungukwa na vijana wapatao kumi waliovaa nguo za aina moja na kufunga vitambaa vyekundu kichwani. kila mmoja alikuwa na mkuki mkono mmoja, rungu mkono



wa pili. Tuliamriwa kuketi chini, juu ya mchanga na kuanza kuulizwa maswali kwa lugha za Kiswahili na Kisukuma.
Mimi, nikiwa sijui Kisukuma, sura yangu ikiwa ngeni mbele ya watu hao ambao baadaye nilifaahamishwa walikuwa vijana wa Chifu, nilijikuta nikiwa mtuhumiwa namba moja mara hiyohiyo.
“Tuambie wewe ni nani… Unatoka wapi… Na unakwenda wapi…” aliamuru mmoja wao huku wenyeji wangu wakiruhusiwa kurejea makwao.
Waliniuliza kwa Kisukuma. Lafudhi yao haikutofautiana sana na Kiha au Kihaya. Niliwaelewa lakini sikuweza kuwajibu kwa lugha yao. Niliamua kuwajibu kwa Kiswahili “Mimi ni mimi. Sijui niendako wala nitokako.”
Walishindwa kuona mzaha katika jibu langu. Mmoja wao, mfupi, mnene mwenye tumbo kubwa zaidi ya umbile lake lilivyoruhusu alionyesha kukasirika sana. “Mnaona?” alisema “Huyu ni mrugaruga, mfungeni kamba twende naye.”
“Twende wapi?” nilihoji hofu ikianza kuniingia “Halafu nyie ni nani kwanza?”
“Unaona?” alifoka tena yule mnene ambaye alionekana kiongozi wao. “Anatuuliza sisi ni nani, mfungeni kamba.” Aliamuru tena.
Amri yake ilitekelezwa. Nilifungwa kamba za mkononi na kiunoni. Mmoja wao alishika ile ya kiunoni na kunivuta kama mbuzi. Ili kukwepa kuburuzwa nilikaza mwendo na kuwa nao sambamba.
Tulipita hapa na pale. Watu wengi waliwaona wakija, hasa vijana wa kiume, walitimka mbio na kutokomea maporini. Ajabu ni kwamba baada ya kunipata mimi hawakuonyesha nia ya kukamata mtu mwingine.
 
SEHEMU YA 48 & 49

Katika maongezi yao, ingawa walipenda sana kuzungumza kisukuma, nilibaini kuwa mmoja wao alikuwa ‘akida’ ambaye ni mwakilishi wa serikali katika kaya mbili tatu za eneo hilo. Wale wengine walikuwa wasaidizi wa ‘Mwanangwa’ aliye msaidizi wa Chifu. Aidha, nilibaini kuwa jukumu walilopewa na chifu lilikuwa la kukamatwa kijana au vijana wenye umri wangu na kuwakabidhi kwake. Hakuna kati yao aliyefahamu Chifu alimhitaji kijana huyo kwa lipi, nilibaini kupitia maongezi yao.
Laiti wangefahamu hofu iliyonishika kwa taarifa hiyo, nina hakika kuwa watekaji wangu hao wangenihurumia na kuniacha niendelee na hamsini zangu badala ya kunipeleka kwa mtemi huyo. Hawakujua kuwa nilitoroka nyumbani kuja Uhayani kwa ajili ya Watemi haohao ambao walitaka kunitoa kafara ili kuleta mvua! Hivyo, ni dhahiri kuwa hawakujua pia kujihusisha na mtu yeyote mwenye madaraka au mamlaka ya Utemi au Uchifu kwa namna yoyote ile, kwani lolote lingeweza kutukia.
Nilitetemeka! Machozi yalinilengalenga. Kwa bahati nilikuwa nyuma yao, hawakuiona hali yangu. Nikaamua kujikaza huku nikianza kubuni njia za kutoroka mara itakapotokea fursa yoyote ile.
Wakati huo kichwa changu kilikuwa kikijiuliza maswali mengi kuliko majibu. Inawezekana kuwa mganga mwingine ametabiri shida ya mvua na kupendekeza kafara ya binadamu ambaye ameondokea kuwa mimi tena? Au watu weupe huko kwao wamenzisha vita nyingine kubwa kama ile iliyoitwa vita kuu, ya mwaka 1914 hadi 1918 ambayo waliwakamata babu zetu kwenda kuwasaidia bila khiari yao? Au ameibuka Mtemi Milambo mpya, aliyewachachafya sana Waarabu na



kuwakomboa mateka wao hadi alipofariki 1884, ambaye Mwingereza ameona hana jinsi ya kumshinda bila vijana wenye asili yake? Au kazi ya ujenzi wa reli ya kati, uliokamilika mwaka 1914 imeibuka tena hivyo wanahitajika manamba wenye damu changa?
Nilijiuliza mengi. Hadi tunafika katika himaya ya Mtemi au Chifu Masanja mwana Kasanga, sikuwa na jibu lolote zaidi ya mzigo wa hofu, mshangao na mashaka tele kichwani.
Mapokezi niliyoyapata katika himaya hiyo yalikuwa muujiza mwingine. Nilipelekwa moja kwa moja katika nyumba ambayo baadaye nilifahamu kuwa ilikuwa ya mke mkubwa wa Chifu. Mmoja kati ya wake zake kumi, ambao kila mmoja alijengewa nyumba yake na kuishi na wasaidizi wake, wake kwa waume, jambo lililoufanya mji huo wa Chifu kuwa kama kijiji kidogo chenye watu wapatao mia mbili hivi. Ng’ombe mia saba, mbuzi elfu moja, kuku, bata na njiwa wasio na hesabu walifanya kijiji hicho kiwe kama mji mdogo ndani ya mji.
Mama Chifu, mtu mnene wa maungo, ambaye mvi zilianza kumeza sehemu kubwa ya nywele zake fupi, alinitazama kwa makini kwa dakika mbili au tatu. Akatikisa kichwa. “Mara akawageukia wale walionikamata na kuwauliza, “Kwa nini mmemfunga kamba?” hakusubiri jibu lao, “Mfungueni mara moja,” aliamuru, amri ambayo ilitekelezwa mara moja.
“Chifu amepumzika,” mama huyo aliongeza. “Hapendi kuamshwa katika usingizi wake wa mchana. Kijana huyu amefika. Mwache aoge, ale, alale. Kesho ataonana na Chifu.”
Watekaji wangu waliondoka zao. Wasaidizi wa mama huyo wakapokea jukumu hilo. Nilitayarishiwa maji ya moto, ambayo sikupata kuyaoga kwa muda mrefu. Nilipotoka kuoga nilipewa ugali mkubwa kwa kuku mzima. Niliula karibu wote.



Nikaushushia kwa kibuyu cha maziwa ambayo pia nilikuwa na hamu nayo. Baadaye nilionyeshwa chumba cha kulala ambacho kilikuwa na kitanda chenye godoro la sufi. Kama haya ni maandalizi ya kunitoa kafara, kwa fadhila hii niko radhi! Niliwaza wakati nikijibwaga kitandani na kuchukuliwa na usingizi mnono uliofanya nisahau shida za mkesha, uchovu na malazi mabaya ya muda mrefu katika safari yangu hiyo.

* * *​
Sikuonana na Chifu hadi baada ya siku tatu. Zikiwa siku za kula vizuri, kulala vizuri na kupumzika, huku tayari nimepewa nguo na viatu vipya, nywele zangu zikiwa zimekatwa vizuri, nilimwona Chifu akinitazama kwa makini kabla ya kutikisa kichwa kama alivyofanya mkewe na kisha kutabasamu.
Nilikuwa nimepelekwa kukutana naye katika ‘Ikulu’ yake, chumba kikubwa chenye viti vipatavyo mia moja vilivyoelekea kwenye kiti chake cha enzi, ambacho kilichongwa kwa mbao za mpingu na fundi anayejua kila aina ya nakshi. Sehemu kubwa ya kiti hicho kilimeremeta kwa aina fulani ya mawe ambayo baadaye nilikuja kufahamu kuwa ni almasi.
Chifu alikuwa amekikalia kiti hicho, mimi nikiwa nimesimama wima mbele yake. Tulikuwa wawili tu chumbani humo baada ya walinzi ambao huwa wako nyuma yake siku zote kuamriwa kuondoka.
“Karibu mwanangu!” Chifu alitamka baada ya kunitazama kwa muda mrefu. “Karibu katika himaya ya Masanja mwana Kasanga, Msukuma halisi aliyewashinda wavamizi na wahamiaji wote. Jisikie uko nyumbani.”
Nilitikisa kichwa kumkubalia ingawa nilikuwa sijamwelewa.



“Hata hivyo, ningependa kukufahamu vizuri, wewe ni nani, kabila gani, ulikuwa ukitokea wapi na kwenda wapi kabla vijana wangu hawajakuleta hapa?” Chifu aliniamuru. Sauti yake ilionyesha upole na upendo kama ya mkewe. Ikanitia moyo.
Nilieleza ukweli juu ya kwetu, Buha, ambako nilizaliwa na kukulia. Kwa hofu kuwa ule mweleka ulikuwa umemwua padri Backhove na kwamba habari za kifo chake zilikwishawafikia huku, nilidanganya juu ya maisha yangu ya elimu. Nilimwambia Chifu kuwa ingawa nilifuata elimu huko kwa Wahaya niliishia kuvua samaki katika ziwa kwa kukosa mtu wa kunisomesha.
Kwa mshangao wangu habari hiyo ilimfurahisha sana Chifu. Alipotabasamu, akacheka kabla hajakohoa kwa kupaliwa na kicheko chake. Baadaye alisema, “Mungu amekuleta nyumbani, upate elimu uliyokuwa ukiitafuta. Utasoma shule ya watoto wa Machifu. Kama ubongo wako unachemka barabara utafika hadi Ulaya. Utakuwa Cheyo lakini Cheyo ataendelea kuwa Cheyo.
Sikumwelewa. Nikamtumbulia macho ya mshangao na kutoamini, macho yaliyojaa maswali ambayo Chifu aliyaona na akaamua kuyajibu, “Nitakuibia siri moja. Nataka ibakie siri, kati yangu na wewe tu. Unaweza kutunza siri?”
Nilikubali.
“Pamoja na umri huu,” Chifu alisema. “Pamoja na kuwa na wake tele hadi leo nimejaliwa kupata mtoto mmoja tu, wa kiume. Anaitwa Cheyo. Tena ana umri kama wako.” Alisita kidogo kabla hajaongeza, “Himaya yangu iko mashakani. Nikifa himaya itapotea mali zangu zitaparanganyika. Hivyo, walipokuja wazungu kutaka kumchukua mwanangu huyu wa
 
SEHEMU YA 50 & 51

pekee ili wampeleke nchi ya mbali akapate elimu, naona tukio hilo litaiweka mashakani zaidi himaya yangu. Nani atarithi Ufalme wangu?”
“Na hata kama akirudi, akiwa amepoteza maadili ya utawala na mila za kabila langu na kuambulia tamaduni za mila za wageni nitakuwa nimejiweka katika nafasi gani?” Chifu alihoji na kuishia kujijibu mwenyewe, “Hapana. Nimekataa. Cheyo ni mwanangu. Nitamlea na kumfundisha mwenyewe. Sitaki kuchekwa na Machifu wenzangu wenye watoto lukuki.” Alisita kwa muda akiwa amejiinamia. Alipoinuka alinikazia macho, “Mwanangu,” akasema “Ni hapo unapoingia katika familia. Kama kweli unataka elimu, kama kweli unaweza, nitakupeleka wewe badala yake. Utatumia jina langu na hadhi yangu. Utalelewa kwa upendo na amani maisha yako yote,
kama mtoto wangu wa damu.”
Alinikazia tena macho, kwa muda mrefu kama anayejaribu kuusoma moyo wangu. Kisha akaniuliza taratibu, “Unasemaje?”
Niseme nini? Kwanza sikulitegemea swali hilo. Lakini sikutegemea kabisa kuwa matokeo ya kutekwa kwangu majuzi yangekuwa habari njema kama hiyo. Shule! Ni kitu nilichoondokea kukipenda kuliko chochote kile katika uhai wangu. Jambo lililofanya nishindwe kuamini iwapo nilichokuwa nimesikia ilikuwa ukweli au niko ndotoni. Niseme nini? Sikuwa na la kusema zaidi ya kuhisi machozi ya furaha yakinitoka na kuteleza juu ya mashavu yangu. Nilijaribu kuyafuta kwa mkono wangu ambao pia ulikuwa ukitetemeka.
Chifu hakuhitaji sauti yangu kupata jibu langu. Alielewa. Akainuka na kunikumbatia. “Hutajutia uamuzi wako. Naapa…” alininong’oneza.



Siku mbili tatu zilizofuata zilikuwa za maandalizi ya safari. Niliandaliwa vizuri sana kwa kufundishwa historia ya ukoo na majina ya mababu zao, ambao walikuwa wangu pia. Nilitakiwa kukariri majina hayo pamoja na mambo mengine tele ya kifamilia, kiukoo na kikabila. Haikuwa kazi rahisi.
Kiafya niliandaliwa pia. Ilikuwa nile mayai sita, kuku mmoja, ugali au ndizi za kutosha na kunywa kibuyu kimoja cha maziwa kila siku. “Ili ukifika pale ufanane na mtoto wa Chifu,” mzee Masanja alisisitiza. Amri hiyo iliambatana na kulala mapema, kuoga mara mbili kutwa, kuchana nywele zangu na kujipaka mafuta ya mgando mwili mzima. Hilo liliambatana na kununuliwa nguo za maana, viatu vya bei, mfuko wa safari na noti ya shilingi kumi ambayo Chifu alisema ni ya ‘kulinda mfuko.’
Matokeo ya kazi hiyo yalimshangaza kila mtu, ikiwa pamoja na mimi mwenyewe. Liliibuka dume lililopanda juu, lenye maungo yenye nguvu na afya tele, dume ambalo ile sura ya hofu na mashaka ilitoweka, nafasi yake ikachukuliwa na sura ya ucheshi, iliyojaa matumaini. Sura ya Mtanganyika halisi, aliyependwa na kupendeza kwa kila aliyemtia machoni. Sura ya Mtukwao au Petro mwana wa Karimanzira, mjukuu wa Kionambali. Hapana, sasa nilikuwa Cheyo mwana Masanja mwana Kasanga!
Nilikuwa mimi yuleyule, lakini mpya! Msomi mtarajiwa! Pamoja na maandalizi hayo ya kusisimua, kitu kimoja kilikuwa kikisumbua sana akili yangu. Toka nilipokuja katika familia hiyo na kupewa nafasi ya kuwa mwana familia na fursa ya kupata elimu sikuwa nimebahatika kukutana ana kwa ana na mrithi halali wa familia, ambaye nafasi yake ya elimu nilielekea kuipokonya. Ningependa sana kumwona mtu huyu.



Nijue ni mtu wa aina gani kitabia na kimaumbile. Lakini zaidi ningependa kujua msimamo na fikra zake juu ya uamuzi wa baba yake wa kumnyima fursa ya elimu ili awe mrithi na Chifu wa baadaye wa eneo hili.
Nilipata kumuuliza Chifu juu ya hilo, iwapo mwanawe ameridhia maamuzi hayo au la, lakini, kwa mshangao nilimwona Chifu akionyesha dalili za kukasirika kabla hajanijibu kwa mkato, “Yule ni mwanangu. Atafuata matakwa yangu,” jibu ambalo lilinitia mashaka zaidi.
Nilipopata wasaa nilimuuliza bi mkubwa juu ya jambo hilo. “Ni kweli mwanao hataki shule. Ni kweli atafurahi akisikia kuwa nakwenda kule kutumia jina lake na nafasi yake kujipatia elimu? Halafu yuko wapi mbona hajaonekana?”
Mama Chifu alinifumbua macho kidogo. Alisema, “Cheyo alikuwa anapenda shule. Hiyo sio siri. Lakini anatupenda zaidi wazazi wake. Hawezi kututupa kwa ajili ya kujua kusoma na kuandika. Alikubaliana na baba yake na ameachana na ndoto zote za kwenda shule. Amejiandaa kuja kuchukua nafasi yake mara Mungu atakapomchukua baba yake.”
“Yuko wapi?” nilimuuliza.
Nilimwona mama akisita kidogo. Baadaye alisema, “Nitakuibia siri. Chifu amemficha, hadi suala hili litakapokwisha.”
“Amemficha wapi?” nilisisitiza.
“Amemsafirisha. Yuko Misungwi kwa wajomba zake. Watamrudisha hapa mara wewe utakapoondoka na kuingia shule ili Wazungu waache kutuma matarishi wa kumtaka Chifu apeleke mtoto wake shule.”
Kiasi nilifarijika, walao kwa kuelewa ukweli.
Hata hivyo, usiku wa kuamkia safari yangu mashaka



yangu yaliibuka pale mmoja wa wajomba hao wa Misungwi alipofika kwa Chifu akiwa na taarifa ambayo ilimchanganya Chifu mwenyewe na kila mtu katika familia hiyo. Kwamba Cheyo alikuwa ametoweka kwa wajomba zake na hajulikani aliko!
Chifu aliduwaa. Alimtolea shemeji huyo macho makali, yaliyojaa hasira. “Kwa nini hamkumwangalia?” alifoka. “Mtafuteni, arudi hapa!” aliamuru.
 
SEHEMU YA 51 & 52

SURA YA SITA
Kwa treni hadi Tabora

Ben R. Mtobwa


afari ya Mwanza hadi Tabora ilikuwa ya kusisimua sana. Ilikuwa safari yangu ya kwanza maishani kusafiri bila kutumia nguvu za miguu
au mikono yangu. Toka Kigoma hadi Kagera hadi Mwanza nilitumia mikono au miguu yangu. Toka Kigoma hadi Kagera hadi Mwanza nilitumia mikono yangu kupiga makasia hadi tulipowasili majuzi. Safari hii kazi yangu ilikuwa kukaa kitako, kando ya dirisha, huku macho yangu yakifaidi kilometa zote 453 za safari kwa kuburudishwa na mazingira aina aina.
Tulisafiri kwa aina mpya ya usafiri iliyotambulishwa nchini na utawala wa Mjerumani, gari moshi. Ujenzi wa reli, vyuma imara ambavyo vilitumiwa na gari moshi hiyo kuteleza juu yake, ambao ulianza huko Darisalama mwaka 1912 uliweza kufika Mwanza 1923, ikiwa moja ya matawi ya reli hiyo lililoanzia Tabora. Reli hiyo, maarufu kama reli ya kati inayokata nchi toka mashariki hadi magharibi na toka kaskazini hadi kusini inakadiriwa kuwa na urefu wa kilomita 2600. Ni moja kati ya kumbukumbu za utawala wa mjerumani, ambazo kamwe hazitafutika katika historia ya nchi hii.
Reli hii ni kiungo pekee muhimu kinachoiunganisha nchi toka bahari ya hindi kwa upande mmoja hadi ziwa



la Tanganyika kwa upande wa pili, jambo linaloifanya iwe tegemeo kubwa kwa usafirishaji wa watu na mizigo si kwa nchi yetu pekee bali pamoja na zile za Burundi, Kongo na Rwanda pia.
Licha ya sababu hizo za kiuchumi reli ilikuwa pia mshirika mkubwa katika masuala ya kiutamaduni na kijamiii nchini. Kwanza iliwezesha makabila yapatayo mia na ishirini ya Tanganyika kufahamiana kwa urahisi. Mzaramo wa pwani angeweza kukutana na Mmanyema wa Kigoma, au Mchaga wa Kilimanjaro kufahamiana na Mfipa wa Mpanda kwa urahisi zaidi ya siku zile za akina Livingstone kutumia miaka maporini toka pwani ya Bahari ya Hindi hadi pwani ya ziwa Tanganyika.
Na hilo halikuwa kwa makabila ya ndani tu. Ujenzi wa reli hiyo ulimfanya mkoloni wa Kijerumani alete vibarua wengi wa kazi hiyo toka nchini India. Hawa ni chanzo cha msamiatai wa ‘kuli’ neno lililozaliwa kutokana na lile la kiingereza ‘Coolie’ wakatii huo likitumiwa kama kashfa kwa vibarua wasio na ujuzi wowote. ‘Kuli’ haikutofautiana sana na ‘manamba’ wa hapa nyumbani ambao walikamwatwa kwa visingizio mbalimbali kubwa ikiwa kushindwa kulipa kodi ya kichwa, na kupelekwa kufanya kazi za mikono katika mashamba ya mkonge kaskazini magharibi mwa nchi yetu.
‘Kuli’ wengi walitoka India, ama walinogewa, ama hawakuwa na uwezo wa kurudi kwao, ama yote mawili, wakaishia kuwa wakazi wa hapa. Leo hii jamii mpya ya akina Gulamali, Manji, Adamjee; na kadhalika inapatikana sehemu yoyote ya Tanganyika; hasa vijijini.
Jing – janga – jing – jang – jing - jang garimoshi lilihangaika kuvuta mabehewa sita wa abiria na manne ya mizigo yaliyofanya tuwe kama joka refu linaloteleza kwa kujikongoja.



Injini ya garimoshi hilo, ambayo sikuhitaji kuambiwa kuwa ilikuwa ikitumia kuni kutengenezea mvuke wa kuiendesha ilikuwa ikitoa moshi mwingi na mzito sana. Moshi ambao ulilala juu ya treni kama wingu jeusi lisilopendeza machoni. Nadhani hiyo ni sababu pekee iliyowafanya waswahili waamue kuita usafiri huo wa ‘garimoshi.’
Nikiwa nimeketi raha mustarehe dirishani pangu nililitazama kwa masikitiko ziwa nililolipenda la Nyanza likitokomea machoni mwangu taratibu. Ziwa hilo lilinilea, lilinihifadhi na kunifadhili kwa muda wa kutosha. Ndilo lililonifundisha kuogelea na kutafuta pesa. Ziwa lililonitoa Kagera na kunifikisha Mwanza. Hilo ndilo ziwa ambalo leo naliacha bila kuwa na uhakika wa kuliona tena. “Nitarudi!” nilinong’ona taratibu.
“Nini?” jirani yangu, mzee wa makamo ambaye tulichangia kiti, alinihoji akidhani nazungumza naye.
Sikumjibu.
Tukapinda na kupenya katikati ya majabali marefu mfano wa milima. Tuliacha jabali moja baada ya jingine, mbuyu mmoja baada ya mwingine huku tukivuka vijito na mito ya hapa na pale.
Mara tukazama katika mapori na misitu mikubwa, kwa mbali tukawaona wanyama mbalimbali kama ngedere waliokuwa wakirukaruka kwenye miti au mbuzimawe ambao walirandaranda juu ya majabali ya hapa na pale. Katika eneo moja lenye mabwawa tuliwaona ndege aina ya flamingo wenye miguu mirefu na midomo myekundu wakiwinda samaki au wadudu ndani ya maji hayo. Ndege wengine, aina mbalimbali pia walikuwa wakiruka huku na huko kama wanaotushangaa au kutushangilia hadi tulipotokomea.
 
SEHEMU YA 53 & 54

“Mantare!” Yule jirani yangu aliropoka.
Ikawa zamu yangu kumshangaa, “Nini?” nilimuuliza.
“Tumefika stesheni ya Mantare,” alifafanua.
Kweli. Nililiona garimoshi likipunguza mwendo na hatimaye kusimama kando ya nyumba mbalimbali ambazo zilionekana kuwa za wafanyakazi wa reli hiyo.
Palikuwa na purukushani fulani, watu wakipanda wengine wakishuka. Miongoni mwa watu hao walikuwepo pia wafanyabiashara wenye bidhaa mbalimbali kama vyakula, mapambo na mifugo. Walionunua walinunua, wasionunua tulijifanya hatuoni.
Tulisimama hapo kwa dakika kumi tu. Mara garimoshi hilo lilianza tena safari yake kwa mwendo wake wenye maringo, taratibu kama halitaki na baada ya kuchochea huku likikohoa kwa uzito wa mabehewa.
“Kwimba!” mzee aliropoka tena. Nilikuwa nimeanza kusinzia. Nikafunga macho na kuona tukiingia katika stesheni nyingine. Nikatoa kichwa dirishani na kuwatazama wanaoshuka na kupanda.
Tukaondoka.
Jirani yangu huyo alikuwa amejipa kibarua. Kila tulipokaribiakituofulani nilimsikiaakitamkakwanguvu,“Malya,” kisha “Seke.” Sikufumbua macho yangu hadi pale aliponitikisa kwa nguvu huku akiniambia, “Amka tumefika Shinyanga!” nilifumbua macho. Jina la Shinyanga lilikuwa na uzito wake katika kumbukumbu zangu. Hata hivyo, nilimwambia taratibu “Siendi Shinyanga. Nakwenda zangu Tabora.”
“Tabora! Kuna nini Tabora?”
Sikumwelewa, “Kuna nini Tabora?” nikamjibu kwa swali jingine. “Kwani Shinyanga kuna nini?”



Kumbe mzee alikuwa na hamu ya maongezi. Alianza kwa kutabasamu. Baadaye aliporomosha sifa za Shinyanga. Kuna kila kitu ambacho binadamu anahitaji. Ardhi bora yenye rutuba tele. Misitu imejaa wanyama kila aina. Ng’ombe wa hapa wamenenepa na wanatoa maziwa mengi kuliko popote pale. Hata Wazungu wengi siku hizi wanatembelea milima yetu mara kwa mara. Kuna fununu kuwa huko ardhini kuna mali nyingi ambazo huko kwao ni utajiri mkubwa.”
Nilitabasamu lakini sikumjibu. Sikuwa na jibu la haraka.
“Enhe na Tabora?” alihoji. “Tabora nini?” nilimuuliza. “Kuna nini Tabora?”
Niliamua kumnyamazisha kwa kumpa kile ambacho nilikipata vitabuni, ambacho nina hakika kuwa alikuwa hakijui. “Tukianza na reli hii tunayoitumia sasa. Roho yake iko Tabora.”
“Kwa vipi?” alihoji akicheka.
“Tabora ni kituo pekee muhimu sana. Pale Tabora ndipo ambapo reli hii inajigawa, moja ikienda Kigoma, ambako inafika hadi ziwa Tanganyika linalotuunganisha na nchi za Kongo, Burundi na Zambia. Pia, kuna reli inayokwenda hadi Mpanda, kusini mwa nchi yetu.”
Wakati akitafakari hilo nilimpa la pili. “Unaijua eropleni?” nilimuuliza.
“Ndege Ulaya!” alisema akicheka. “Sio naijua, nimeipanda mara nyingi.”
“Kutoka wapi kwenda wapi?” nilimuuliza kwa mshangao. “Burma,” alinijibu. “Kwenye vita kuu ya kwanza nilikuwa mmoja wa wapiganaji tuliorushwa kwa ndege kwenda kusaidia



wenzetu waliozingirwa na maadui,” alisita kidogo kabla ya kuniuliza, “Ndege ina uhusiano gani na Tabora?”
“Tarehe 22 Julai mwaka 1920 ndege ya kwanza kutua nchini Tanganyika ilitua katika uwanja wa ndege Tabora. Ndege hiyo ndogo ya Mwingereza iliruka toka Nairobi Kenya hadi hapa na kuweka historia ya pekee kwa nchi ya Tabora.
Mzee alicheka. “Hilo tu?” aliniuliza.
“Yako mengi, “ nilimjibu. “Yule kiboko wa Waarabu, Mtemi Milambo, aliishi katika ngome yake Iselemagazi iliyokuwa Tabora. Yule Mwingereza Davidi Livingstone aliyekataa kurudishwa kwao na akafia Zambia alipata kuishi Tabora kwa muda, kabla hajahamisha makazi yake Ujiji, Kigoma. Tabora ulikuwa mmoja kati ya miji michache nchini iliyokuwa na watu wengi, toka miaka ya 1700, mji mdogo huo?”
Mzee aliyatafakari maneno yangu. “kichwa chako kinafanya kazi vizuri sana, mjukuu wangu. Naweza kutabiri unakwenda Tabora kufanya nini.”
“Naenda kufanya nini?” nilimjaribu. “Kusoma,” alinijibu. “Kweli au uongo?” “Kweli tupu.”
Mzee akacheka kabla hajaongeza, “Naweza hata kukuambia jina la shule unayokwenda.”
“Shule gani?”
“Unakwenda Tabora School. Shule ya misheni inayopokea watoto wa machifu. Kweli au uongo?”
“Ni kweli,” nilimjibu kwa mashangao. “Umejuaje mzee?” “Uzee dawa. Uzee ni kuona mengi ni kuona mbali. Jinsi ulivyovaa, jinsi ulivyotulia, jinsi unavyoongea, ni wazi kuwa wewe ni mtoto wa Chifu. Na nina imani kuwa utafika mbali
katika safari yako ya maisha.”



Nilitamani kucheka, nilitamani kulia. Sikujua nifanye lipi katika hayo. Kwa mara ya kwanza, baada ya muda mrefu nikamkumbuka babu yangu, mzee Kionambali.
Mtoto wa Chifu!
* * *
Tulifika Tabora siku mbili baadaye.
Stesheni ya Tabora ni sehemu moja yenye kila aina ya pilikapilika. Ilikuwa na watu wengi wenye purukushani hii na ile, huyu akihangaika kupanda behewa, huyu akishuka, yule akibadili behewa kuhamia lile, huyu akipiga kelele kuuza asali na bidhaa nyingine na kadhalika na kadhalika. Lakini purukushani kubwa zaidi ilikuwa ya magarimoshi yenyewe. Vichwa vilikuwa vingi mno, vikienda hapa au pale, kuhamia reli hii au ile huku vikicheua moshi na honi za mara kwa mara, hali iliyofanya pawe mahala ambapo mtu asingependa kukaa kwa muda mrefu.
Nilishuka, nikachukua mzigo wangu na kutoka nje ya stesheni. Huko nje kitu cha kwanza kilichovuta macho yangu ni wingi wa maembe. Barabara nzima toka stesheni hadi mjini zilizingirwa na miembe mikubwa, kila upande kwa namna iliyofanya iwe na kivuli murua cha kusisimua. Nilipiga hatua moja kwenda nyingine kuifuata barabara hiyo ya aina yake. Kila hatua ilinifanya nione kuwa wingi huo wa miembe haukuwa wa kando ya barabara pekee. Mapori yote ya mji yalitawaliwa na miembe mingi, mikuwa, ambayo baadhi ilikuwa na maembe yaliyoiva, ambayo yalionyesha kuwa watoto wa mji huo walishachoka kuyala.
Mji wa Tabora ulikuwa mdogomdogo, wenye nyumba za kawaida, ambazo hazikutofautiana sana na zile za Mwanza. Tofauti pekee kubwa niliyoiona ni mavazi na lafudhi. Kimavazi
 
SEHEMU YA 55 & 56

nilishangaa kuona watu wengi wakiwa wamevaa mavazi yenye asili ya Kiarabu, kanzu nyeupe na kiko mdomoni kwa wanaume na baibui jeusi lililofunika moja ya kumi ya mwili isipokuwa sehemu ndogo ya uso kwa wanawake. Katika mazungumzo yao nilibaini pia kuwa lafudhi ya wengi wao ilikuwa ya Pwani zaidi. Japo walizungumza kwa namna iliyofanya nihisi ama wanaibembeleza lugha ama inateleza kwenye ndimi zao.
‘Karibu Tabora mwanangu!’ nilijikaribisha.
Nikauliza njia ya kwenda shule ya Tabora School. Nikaelekezwa. Nikaifuata njia hiyo taratibu, mzigo mkononi, mluzi mdomoni, ndoto za mafanikio zikiwa tele moyoni.
Nilipokelewa na mlinzi nje ya geti la kuingilia shuleni. Nikajitambulisha kwake. Alinifungulia geti na kunielekeza iliko ofisi ya mkuu wa shule. Nilikwenda kwa mwendo wa kujiamini, huku nikiwa tayari nimetoa barua yangu ya utambulisho toka kwa ‘baba yangu,’
Chifu Masanja mwana Kasanga. Wanafunzi wenzangu tayari walikuwa madarasani. Niliweza kuwasikia baadhi ya walimu wakifoka kwa sauti kubwa katika jitihada za kujaribu kuingiza kitu fulani katika vichwa vigumu vya wanafunzi.
Karani wa mkuu wa shule alinipokea, akaipokea barua yangu na kuiingiza chumbani kwa bosi wake. Muda mfupi baadaye niliitwa katika ofisi hiyo.
Mkuu wa shule alikuwa Mzungu. Mtu mnene miraba minne, ambaye angefaa zaidi kuwa mwalimu wa ngumi badala ya taaluma. Nilimkuta kasimama nyuma ya meza yake, barua yangu ikiwa mkononi mwake. Alinikazia macho makali kwa dakika moja au mbili kabla hajatamka neno moja tu “Keti.” Nikaketi kwenye kimoja wapo cha viti viwili vilivyomuelekea mwalimu mkuu, miguu yangu ikianza kupoteza nguvu, mikono



ikianza kutetemeka kwa sababu ambayo sikuifahamu. “Barua yako hii?” alinihoji baadaye.
“Ndiyo.” “Umeipata wapi?”
“Kwa nini? Nimepewa na Chifu… baba… nikuletee.” “Chifu nani?”
“Masanja mwana Kasanga.”
Mkuu huyo wa shule alinitazama kabla hajaongeza swali jingine, “Unaitwa nani?”
Nusura nitaje jina langu halisi. “Cheyo,” nikatamka.
Nilimwona mkuu wa shule akizidi kushangaa. Mara akawa kama kakumbuka jambo. Akatoka na kumnong’oneza jambo karani wake. Kisha akarudi na kuketi. Muda mfupi baadaye mlango uligongwa, mwanafunzi mmoja akaingia na kuelekezwa kuketi kiti cha pili kilichokuwa wazi.
Mkuu wa shule akimkazia macho kama alivyofanya kwangu kabla ya kumuuliza, “Ulisema wewe ni nani, unatoka wapi na baba yako ni nani?”
“Naitwa Cheyo. Kwetu Mwanza. Mimi ni mtoto wa Chifu Masanja mwana Kasanga.”
Miguu yangu iliishiwa nguvu. Nilitamani ardhi ipasuke, inimeze yaishe. Ardhi haikufanya hivyo. Nikahisi nimeanza kutetemeka mwili mzima, jasho jembaba likinitoka.
Mkuu wa shule alikuwa akinitazama kwa makini. “Nani anasema uongo, nani anasema ukweli kati
yenu?” aliniuliza. “Juzi tu,” aliongeza. “Alikuja huyu kijana, akatuambia kwamba anaitwa Cheyo na ni mtoto wa chifu Masanja. Kwa maelezo yake baba yake hataki aje shule, anataka akae nyumbani kusubiri kurithi Uchifu wake atakapokufa. Kwamba amekuja hapa shuleni kwa kutoroka baada ya



jitihada za kumsihi baba yake kumruhusu kushindikana. Na kwa jina na nafasi yake ilikuwa wazi bado tumempokea na kumruhusu kuendelea na masomo. Leo umekuja wewe. Unadai wewe ni Cheyo mtoto wa Chifu Masanja na una barua yake ya kuomba upokelewe hapa. Nataka kujua nani mkweli nani mwongo kati yenu,” aliniuliza akitutazama kwa zamu. Cheyo naye alishangaa. Akageuka kunitazama. Nilijitahidi kuinua uso wangu nimtazame pia, ilikuwa kazi ngumu kuliko zote nilizopata kufanya. Hicho kidogo nilichobahatika kuona katika uso wake kilionyesha wazi kuwa si kwamba hatufahamiani tu, bali pia tulikuwa hatufanani kwa namna yoyote ile. Pale ambapo mimi nilikuwa mng’avu yeye alikuwa mweusi tii, pale nilipokuwa mrefu yeye alikuwa mfupi na mwenye kiribatumbo. “Mnafahamina?” mkuu wa shule aliuliza baada ya
kutupa dakika za kutumbuliana macho.
Wote tulitikisa vichwa kukataa.
Mkuu wa shule akacheka, “Iweje watoto wa mtu mmoja, tena waotumia jina moja wawe hawafahamiani?”
Hatukumjibu.
Haikumchukua mkuu wa shule muda mrefu kubaini ukweli wa mambo hayo. Kutokana na udadisi wa Chifu Masanja juu ya kumpeleka mwanae shule, bila shaka kwa muda mrefu sasa, ndipo akabuni hila ya kuteua mtu mwingine ili aache kusumbuliwa, jambo ambalo limetibuka baada ya mwanawe kutoroka nyumbani na kuja shuleni bila ridhaa wala khiari yake.
Mkuu huyo alinikazia macho kama anayesubiri uthibitisho wa kile kinachopita katika fikra zake bila kutamka. Nilitamani asome jibu la ‘ndiyo’ katika nafsi yangu ili yaishe, niondokane na aibu hiyo. Nadhani alisoma hilo katika macho



yangu, kwani nilimsikia akisema taratibu, “Sipendi kuchezewa. Sipendi kudanganywa. Natoa dakika kumi tu, yule ambaye anafahamu kati yenu kuwa si mtoto halali wa Chifu masanja aondoke mbele yangu na ndani ya eneo la shule yangu. Vinginevyo, nitamchukulia hatua kali za kisheria.”
Sikungojea dakika hizo kumi. Moja tu ilinitosha. Niliinuka, nikachukua begi langu na kutoka taratibu. Nyuma yangu nilisikia kicheko, kicheko ambacho kiliashiria mwisho wa ndoto yangu ya kupata elimu zaidi ya ile ndogo niliyokuwa nayo.

* * *
Niliduwaa kwa muda nje ya eneo la shule. Nilihisi akili yangu ikiwa imedumaa kiasi kwa kuwa mvivu wa kufikiri, hali ambayo ilitokana na uchovu wa ubongo wangu kwa ajili ya tukio hilo zito. Nikatafuta kivuli na kukaa.
Kelele za wanafunzi ambao walikuwa wakitoka, ndizo zilizonizindua hapo chini ya mwembe nilipoketi. Nikainuka nikachukua begi langu na kuitumia miguu yangu kuniondoa hapo. Sikujua naelekea wapi. Lakini sikushangaa pale miguu yangu iliponifikisha stesheni ya treni, mbele ya dirisha la mkata tiketi.
“Nipe tiketi,” nilimwamuru. “Ngapi?”
“Moja.”
“Ya kwenda wapi?”
Niende wapi? Nilijiuliza. Sikuhitaji kujiuliza sana, “Tiketi yoyote ile. Kigoma, Dar es Salaam au Mpanda,” nilimjibu.
Mkata tiketi huyo alinitazama kwa macho ya mshangao wa muda, akinichungulia toka katika kijidirisha chake.
 
SEHEMU YA 57 & 58

“Unaumwa?” baadaye alinihoji.
Sikutarajia swali hilo, “Kuumwa! Kuumwa nini?” “Chochote kile. Kama akili hivi?”
Ikawa zamu yangu kumshangaa, “Kwa nini uniambie hivyo?” nikafoka.
“Mtu yeyote asiyejua anakokwenda ama ni mngonjwa wa akili, ama ameiba anataka kukimbia. Wewe uko katika kundi gani katika hilo?”
Lilikuwa swali la kifedhuli kuliko yote. Lakini nadhani alikuwa akinitendea haki. Mwenyewe pia nilianza kujishuku. Ninakwenda wapi? Ninakimbia nini? Nimechanganyikiwa kwa kupoteza nafasi yangu nyingine ya kupata elimu? Lakini mara ngapi nimesikia kuwa kukosa elimu ya darasa siyo mwisho wa elimu duniani? Wangapi duniani wamefanya maajabu na kuingia katika vitabu vya kihistoria kwa kiwango cha elimu kama yangu au ndogo zaidi.
Wazo hilo lilinifanya niangue kicheko. Nilicheka kwa muda wa dakika mbili nzima mpaka nikapaliwa. Nikaanza kukohoa.
Kicheko changu kilifanya mkata tiketi huyo aamini hisia zake, kuwa naumwa. Na siumwi kitu kingine zaidi ya akili. Nilimwona akichukua simu na kuzungusha namba kadhaa. Alizungumza kwa sauti ya kunong’ona huku akiwa amenikazia macho ya tahadhari. Baada ya hapo alifunga dirisha lake.
Huku nikicheka niliinua begi langu na kuanza kuondoka eneo hilo. Lakini sikuweza kupiga zaidi ya hatua kumi kabla sijajikuta nikivamiwa na watu wawili waliovaa sare za polisi, shati na kaptula za kaki, kofia zilizovaliwa upande, soksi na viatu vyeusi. Mkononi kila mmoja alikuwa na rungu.
“Polisi! Tulia kama unanywolewa!” mmoja aliniamuru.



Nikiwa nimeshikwa na mkanda wa suruali kwa nyuma, hali iliyofanya nining’inie juu juu na kutembelea ncha za vidole vyangu sikuwa na nguvu zozote za kujitetea. Niliburuzwa hadi katika chumba chao kidogo ambako nilisukumwa na kufungiwa kwa nje bila kuulizwa swali lolote.
“Nimefanya nini jamani?” niliwapigia kelele. Hakuna aliyenijibu.


SURA YA SABA
Lyampa Mfipa


ilipohoojiwa na polisi kwa dakika kumi tu kabla hawajathibitisha kuwa nilikuwa na akili zangu timamu. Lakini ilikuwa baada ya kufungiwa
chumbani humo kwa siku nzima.
Alikuja mmoja kati ya wale walionikamata, akiwa amefuatana na mtu mwingine mfupi, mnene, ambaye alinukia dawa za hospitali. Sikuhitaji kuambiwa kuwa mtu huyo alikuwa daktari, pengine wa maradhi ya akili, toka hospitali ya Kitete. Walipoingia ndani yule daktari aliketi mbele yangu na kunikazia macho. Mie pia nikamkazia macho. Hata hivyo, nusu dakika baadaye niliyakwepa macho yake kwa kuinamisha uso wangu.
Akiwa bado amenikazia macho daktari yule alitabasamu, mimi sikutabasamu. Aliangua kicheko. Mimi sikufanya hivyo. Kisha alitikisa kichwa chake kwa kujiyumbisha huku na kule kama aliyekusudia nifuate mfano wake. Sikufanya hivyo. Nikamwona kama mtu aliyepatwa na mshangao.
“jina lako?”
Nikamjibu kwa kutaja lile nililopewa na chifu Masanja, “Cheyo.”
“Kabila lako?”



“Msukuma. Ingawa sikijui vizuri.” “Kwa nini?”
“Nilizaliwa na kukulia Buha. Nafahamu Kiha kuliko kisukuma.”
“Mwakeye!” Akanijibu.
“Saa hizi sio mwakeye, ni mwidiwe,” nikamsahihisha.
Akatabasamu. Nadhani akiba yake ya Kiha ilikuwa inaishia pale, kwani alirudi kwenye Kiswahili. “Enhe, una tatizo gani?” alihoji.
“Nadhani hawa walionifungia hapa ndio wenye matatizo. Wamenikamata bila sababu na kunifungia humu bila maelezo,” nilisema kwa sauti yenye hasira.
Daktari huyo alinitazama kwa makini, toka kichwani hadi miguuni. Mavazi yangu yalikuwa safi, viatu vyangu viking’ara kwa kiwi. Hata mwili wangu pia ulikuwa safi, ukimeremeta kwa afya na mafuta niliyopaka kabla ya kwenda mbele ya mkuu wa shule ile iliyonikataa. Begi langu pia lilikuwa safi, jipya, lililofura mali ambazo mgonjwa wa akili hawezi kuwa nazo. Daktari huyo aliacha kunitazama mie akawa akimtazama yule askari. Nilihisi kuwa alikuwa katika wakati mgumu wa kuamua nani mgonjwa wa akili kati yangu na hao walionikamata. “Wamekuhangaisha bure,” alisema baadaye. “Ilikuwa tukukamate, upelekwe Dodoma kwenye hospitali ya wenye maradhi ya akili. Unaonekana huna tatizo loolote.”
Askari huyo hakuweza kunitazama usoni kwa aibu.
Mara niliporuhusiwa, nilichukua begi langu na kurudi katika dirisha lilelile la mkata tiketi. Nilimkuta karani yuleyule bado akiwa kazini. “Nataka tiketi,” nilimwamuru.
Aliponitazama alishtuka kama aliyeguswa na waya wa umeme. “Ya kwenda wapi?” alinihoji kwa sauti ambayo
 
SEHEMU YA 59 & 60

haikuwa imara kama awali.
“Popote,” nilimjibu kama awali.
Alitazama huko na huko kama anayetaka kuomba msaada. Kisha akasema, “Leo kuna treni mbili. Moja inakwenda Kigoma, itapita usiku. Nyingine inakwenda Mpanda, itaondoka hapa baada ya nusu saa.”
Nipe ya Mpanda.” Nilisema bila ya kufikiri sana.
“Shilingi tano, njia moja.”
“Nipe,” nilimjibu nikimlipa. Nikapokea tiketi na chenji zangu na kuzitia mfukoni. Nikaenda mgahawa mmoja uliokuwa karibu ambapo nilinunua wali kwa maharage, nikayashushia kwa chai ya rangi. King’ora cha abiria wa treni ya Mpanda kilipolia nilikuwa mmoja wa abiria wa kwanza kuiparamia.

* * *
Sikuhitaji kufikiri sana kabla ya kukata tiketi hiyo kwa sababu nyingi. Kwanza, nilikuwa na hisia kuwa Tabora haukuwa mji wangu wa bahati. Kuumbuliwa na mkuu wa shule kwa kiwango kile kulinitia doa na dosari kubwa iliyofanya nijisikie aibu isiyo na kifani. Mimi sio yatima. Nina baba na mama. Nina babu mwerevu kuliko mamia ya mababu ninaowajua. Kiu ya elimu haikuwa sababu nzuri ya kunifanya nikubali wazo la kipuuzi la kufanywa mtoto wa kambo wa Chifu Masanja.
Ni wazo hilo lililofanya nitupilie mbali wazo la kurejea Usukumani. Ningemwambia nini Chifu?
‘Nimebainika. Mtoto wako halisi yuko shuleni, kwa hiyo nitafutie hifadhi mpya!’ Aibu iliyoje. Ningemwambia nini mkewe na watumishi wa himaya yake ambao bila shaka wengi waliijua kinachoendelea?



Ndipo nilipowaza juu ya kurudi nyumbani. Nipande garimoshi hadi Kigoma, huko nitafute njia ya kufika Kasulu. Huenda tayari kulikuwa na malori ambayo yalibeba watu na mizigo kama sehemu nyingine za nchi.
Hata hivyo, hilo pia sikulitekeleza kwa sababu tele. Moja ilikuwa aibu. Mwanamume akitoka ametoka. Akirudi ana kitu cha kuonyesha kijijini. Ama vyeti vya kuhitimu masomo yako ama fedha au mtaji au kujenga nyumba bora zaidi. Mimi ningerudi na aibu tupu. Sikuwa tayari kufanya hivyo.
Sababu nyingine iliyonizuia kwenda nyumbani ni babu yangu. Ni kweli alinipenda sana na angefurahi sana kuniona. Lakini sikupenda kujitokeza mbele yake kichwa kitupu, mikono mitupu. Alitegemea nirudi na elimu. Alitegemea nirudi na mali. Kamwe asingefurahi kuona nikirudi mnyonge, kama kinda la ndege, linalotegemea mama akutafutie, akutafunie, umeze.
Lakini kuna sababu nyingine, kubwa zaidi, iliyonifanya nisijisikie kumtazama babu machoni. Hirizi yake. Hirizi hiyo ya familia, ambayo kwa mujibu wa maelekezo yake ilivaliwa na babu yake, baba yake na kisha yeye mwenyewe. Hirizi ambayo ilimpeleka Ughaibuni na kumrejeshha salama. Naam, hirizi ambayo aliivua na kunivisha mimi, badala ya baba, ili nipate kile ambacho aliamini kingeinua ukoo na familia yetu.
Hirizi ambayo niliipoteza kwa uzembe!
Haikuwa kweli kuwa chanzo cha migogoro yangu hii mipya, ikiwa pamoja na kukataliwa nafasi ya kusoma, kwa namna moja au nyingine ilihusiana na kupotea kwa hirizi ile? Mara kwa mara niliwaza.

* * *



Gari moshi liendalo mpanda hulazimika kueleka magharibi kwa kilometa kadhaa kabla ya kuchepuka kuelekea kusini. Kwangu mimi ilikuwa sawa na kuelekea nyumbani, Kigoma. Tuliiacha stesheni ya Tabora, tukatafuna reli hadi Usoke. Toka hapo tuliingia Urambo. Tuliacha Urambo na kufika Kaliua ambako tulianza safari ya kusini.
Kama ilivyokuwa safari ya kutoka Mwanza safari hii pia ilikuwa sawa na kusafiri katikati ya bustani ya Eden. Kila upande tulizungukwa na ama misitu minene iliyoashiria kila aina ya hazina, ama mapori ya kutisha yaliyoonya juu ya wingi wa mbolea katika ardhi yake.
Mara kwa mara tulipishana na wanyama ainaaina waliokuwa kando wakitushangaa, pamoja na ndege ainaaina walioruka hapa na pale juu ya miti, wakifaidi asali ya maua na wadudu wadogowadogo. Baadhi ya maeneo kulikuwa na mabwawa makubwa yaliyoshawishi kilimo cha mpunga au mito ambayo ilinikumbusha samaki wa ziwa Nyanza.
Toka Kaliua tuliingia Mfulu, baadaye Ugalla na hatimaye tukawasili Mpanda. Huo ulikuwa mwisho wa reli hii, lakini haikuwa mwisho wa safari yangu.
Pamoja na shahuku yangu kubwa ya kuondoka Tabora, ndoto yangu ya kuja Mpanda ilikuwa na malengo yake. Zilikuwepo fununu za hapa na pale kuwa maeneo mbalimbali ya huku yalikuwa dhahabu. Uchimbaji wa dhahabu hiyo sikuona kama kwa namna yoyote ile ungenishinda. Kuchimba udongo hadi ufikie mchanga maalumu kuchekecha mchanga huo hadi uone chembechembe za dhabahu na kuiokoteza, vipi kungenishinda?
Hilo lilikuwa wazo la kwanza. Wazo la pili, ambalo nilikuwa na hakika nalo zaidi ni uvuvi. Toka Mpanda hadi



Ikola au Kerema ambayo ni miji ya kandokando mwa ziwa Tanganyika haikuwa safari ndefu. Ningeweza kufika huko hata kwa miguu. Nilipanga, kama kazi ya kuchimba dhahabu ingeshindikana ningeelekea huko na kujiunga na uvuvi. Ndiyo, nasikia ziwa Tanganyika lina kina kirefu kuliko maziwa yote duniani. Kama kuna ukweli kwa hilo bila shaka samaki wake pia ni wengi zaidi na watamu zaidi. Ningekuwa mmoja kati ya walaji wake. Wala nisingeishia kula tu; samaki hao wangenipatia fedha za mtaji ili nirudipo kwetu nirudi kishujaa. Hivyo ndiyo ilikuwa ndoto yangu. Kwa bahati, nzuri au mbaya, haikwenda kama nilivyotarajia. Hali hiyo ilitokana na kukutana kwangu ana kwa ana na mtu ambaye sikutarajia kamwe kumwona tena katika maisha yangu, mtu ambaye sikupata hata kulifahamu jina lake. Alikuwa mmoja kati ya wale Wamanyema wawili waliofuatana na Mwarabu katika safari yetu ya miguu toka Buha hadi kwa Wahaya, miaka zaidi
ya mitano iliyopita.
Ni yeye aliyeniona kwanza, “We mtoto wewe! Kama nakufahamu vile?”
Nikageuka kumtazama. Mara moja nilimkumbuka, “Mmanyema! Unafanya nini huku?” niliuliza kwa mshangao.
“Wewe je? Umefikaje huku?” Sikujua nimweleze nini. “Babu yako hajambo?”
Sikuwa na jibu. Nikainamisha uso kwa aibu.
Nadhani Mmanyema alisoma kitu fulani katika uso wangu, kwani alinitazama kwa muda kabla hajanikaribisha chai kwa mihogo ambayo alikuwa akiila. Nikapokea kikombe cha chai ya maziwa na kipande cha muhogo. Njaa iliyoanza kuninyemelea ikakimbia mara moja.

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA 59 & 60

haikuwa imara kama awali.
“Popote,” nilimjibu kama awali.
Alitazama huko na huko kama anayetaka kuomba msaada. Kisha akasema, “Leo kuna treni mbili. Moja inakwenda Kigoma, itapita usiku. Nyingine inakwenda Mpanda, itaondoka hapa baada ya nusu saa.”
Nipe ya Mpanda.” Nilisema bila ya kufikiri sana.
“Shilingi tano, njia moja.”
“Nipe,” nilimjibu nikimlipa. Nikapokea tiketi na chenji zangu na kuzitia mfukoni. Nikaenda mgahawa mmoja uliokuwa karibu ambapo nilinunua wali kwa maharage, nikayashushia kwa chai ya rangi. King’ora cha abiria wa treni ya Mpanda kilipolia nilikuwa mmoja wa abiria wa kwanza kuiparamia.

* * *
Sikuhitaji kufikiri sana kabla ya kukata tiketi hiyo kwa sababu nyingi. Kwanza, nilikuwa na hisia kuwa Tabora haukuwa mji wangu wa bahati. Kuumbuliwa na mkuu wa shule kwa kiwango kile kulinitia doa na dosari kubwa iliyofanya nijisikie aibu isiyo na kifani. Mimi sio yatima. Nina baba na mama. Nina babu mwerevu kuliko mamia ya mababu ninaowajua. Kiu ya elimu haikuwa sababu nzuri ya kunifanya nikubali wazo la kipuuzi la kufanywa mtoto wa kambo wa Chifu Masanja.
Ni wazo hilo lililofanya nitupilie mbali wazo la kurejea Usukumani. Ningemwambia nini Chifu?
‘Nimebainika. Mtoto wako halisi yuko shuleni, kwa hiyo nitafutie hifadhi mpya!’ Aibu iliyoje. Ningemwambia nini mkewe na watumishi wa himaya yake ambao bila shaka wengi waliijua kinachoendelea?



Ndipo nilipowaza juu ya kurudi nyumbani. Nipande garimoshi hadi Kigoma, huko nitafute njia ya kufika Kasulu. Huenda tayari kulikuwa na malori ambayo yalibeba watu na mizigo kama sehemu nyingine za nchi.
Hata hivyo, hilo pia sikulitekeleza kwa sababu tele. Moja ilikuwa aibu. Mwanamume akitoka ametoka. Akirudi ana kitu cha kuonyesha kijijini. Ama vyeti vya kuhitimu masomo yako ama fedha au mtaji au kujenga nyumba bora zaidi. Mimi ningerudi na aibu tupu. Sikuwa tayari kufanya hivyo.
Sababu nyingine iliyonizuia kwenda nyumbani ni babu yangu. Ni kweli alinipenda sana na angefurahi sana kuniona. Lakini sikupenda kujitokeza mbele yake kichwa kitupu, mikono mitupu. Alitegemea nirudi na elimu. Alitegemea nirudi na mali. Kamwe asingefurahi kuona nikirudi mnyonge, kama kinda la ndege, linalotegemea mama akutafutie, akutafunie, umeze.
Lakini kuna sababu nyingine, kubwa zaidi, iliyonifanya nisijisikie kumtazama babu machoni. Hirizi yake. Hirizi hiyo ya familia, ambayo kwa mujibu wa maelekezo yake ilivaliwa na babu yake, baba yake na kisha yeye mwenyewe. Hirizi ambayo ilimpeleka Ughaibuni na kumrejeshha salama. Naam, hirizi ambayo aliivua na kunivisha mimi, badala ya baba, ili nipate kile ambacho aliamini kingeinua ukoo na familia yetu.
Hirizi ambayo niliipoteza kwa uzembe!
Haikuwa kweli kuwa chanzo cha migogoro yangu hii mipya, ikiwa pamoja na kukataliwa nafasi ya kusoma, kwa namna moja au nyingine ilihusiana na kupotea kwa hirizi ile? Mara kwa mara niliwaza.

* * *



Gari moshi liendalo mpanda hulazimika kueleka magharibi kwa kilometa kadhaa kabla ya kuchepuka kuelekea kusini. Kwangu mimi ilikuwa sawa na kuelekea nyumbani, Kigoma. Tuliiacha stesheni ya Tabora, tukatafuna reli hadi Usoke. Toka hapo tuliingia Urambo. Tuliacha Urambo na kufika Kaliua ambako tulianza safari ya kusini.
Kama ilivyokuwa safari ya kutoka Mwanza safari hii pia ilikuwa sawa na kusafiri katikati ya bustani ya Eden. Kila upande tulizungukwa na ama misitu minene iliyoashiria kila aina ya hazina, ama mapori ya kutisha yaliyoonya juu ya wingi wa mbolea katika ardhi yake.
Mara kwa mara tulipishana na wanyama ainaaina waliokuwa kando wakitushangaa, pamoja na ndege ainaaina walioruka hapa na pale juu ya miti, wakifaidi asali ya maua na wadudu wadogowadogo. Baadhi ya maeneo kulikuwa na mabwawa makubwa yaliyoshawishi kilimo cha mpunga au mito ambayo ilinikumbusha samaki wa ziwa Nyanza.
Toka Kaliua tuliingia Mfulu, baadaye Ugalla na hatimaye tukawasili Mpanda. Huo ulikuwa mwisho wa reli hii, lakini haikuwa mwisho wa safari yangu.
Pamoja na shahuku yangu kubwa ya kuondoka Tabora, ndoto yangu ya kuja Mpanda ilikuwa na malengo yake. Zilikuwepo fununu za hapa na pale kuwa maeneo mbalimbali ya huku yalikuwa dhahabu. Uchimbaji wa dhahabu hiyo sikuona kama kwa namna yoyote ile ungenishinda. Kuchimba udongo hadi ufikie mchanga maalumu kuchekecha mchanga huo hadi uone chembechembe za dhabahu na kuiokoteza, vipi kungenishinda?
Hilo lilikuwa wazo la kwanza. Wazo la pili, ambalo nilikuwa na hakika nalo zaidi ni uvuvi. Toka Mpanda hadi



Ikola au Kerema ambayo ni miji ya kandokando mwa ziwa Tanganyika haikuwa safari ndefu. Ningeweza kufika huko hata kwa miguu. Nilipanga, kama kazi ya kuchimba dhahabu ingeshindikana ningeelekea huko na kujiunga na uvuvi. Ndiyo, nasikia ziwa Tanganyika lina kina kirefu kuliko maziwa yote duniani. Kama kuna ukweli kwa hilo bila shaka samaki wake pia ni wengi zaidi na watamu zaidi. Ningekuwa mmoja kati ya walaji wake. Wala nisingeishia kula tu; samaki hao wangenipatia fedha za mtaji ili nirudipo kwetu nirudi kishujaa. Hivyo ndiyo ilikuwa ndoto yangu. Kwa bahati, nzuri au mbaya, haikwenda kama nilivyotarajia. Hali hiyo ilitokana na kukutana kwangu ana kwa ana na mtu ambaye sikutarajia kamwe kumwona tena katika maisha yangu, mtu ambaye sikupata hata kulifahamu jina lake. Alikuwa mmoja kati ya wale Wamanyema wawili waliofuatana na Mwarabu katika safari yetu ya miguu toka Buha hadi kwa Wahaya, miaka zaidi
ya mitano iliyopita.
Ni yeye aliyeniona kwanza, “We mtoto wewe! Kama nakufahamu vile?”
Nikageuka kumtazama. Mara moja nilimkumbuka, “Mmanyema! Unafanya nini huku?” niliuliza kwa mshangao.
“Wewe je? Umefikaje huku?” Sikujua nimweleze nini. “Babu yako hajambo?”
Sikuwa na jibu. Nikainamisha uso kwa aibu.
Nadhani Mmanyema alisoma kitu fulani katika uso wangu, kwani alinitazama kwa muda kabla hajanikaribisha chai kwa mihogo ambayo alikuwa akiila. Nikapokea kikombe cha chai ya maziwa na kipande cha muhogo. Njaa iliyoanza kuninyemelea ikakimbia mara moja.

ITAENDELEA
Tuko pamoja arif
 
Back
Top Bottom