SEHEMU YA 89
niliyodokezwa kuwa inaitwa Kigamboni kwa eneo la takriban meta mia mbili. Eneo ambalo lilikaliwa na wavuvi wengi. Nikiwa nimesimama hapo, nilipoambiwa kuwa panaitwa Magogoni, niliweza kuona mitumbwi ya wavuvi ama ikijishughulisha na uvuvi au kuvusha watu toka upande mmoja hadi mwingine.
Niliamua kupoza kiu yangu kwa kunywa maji ya dafu baada ya kumwona muuzaji akipita karibu yangu na tenga la madafu juu ya baiskeli yake.
“Unataka gumu au laini?” Aliniuliza. “Kwani kuna tofauti gani?”
“Gumu ni lenye nyama na maji matamu zaidi. Laini halina nyama, maji yake kidogo yana chumvi.”
Niliomba laini. Nikanywa maji na kufaidi ujiuji wake badala ya gumu ambalo nyama zake mara nyingine hufanana na nazi.
Wakati nikirejea, juu kidogo ya Pwani hiyo ya Magogoni nilionyeshwa jengo ambalo nilidokezwa kuwa ni makazi na ofisi ya Gavana. Sikuweza kuvumilia, nikachungulia. Macho yangu yalivutwa na bustani kubwa ya miti mbalimbali iliyooteshwa, mingi ikiwa ya asili. Niliweza kuiona miti kadhaa, ambayo babu alipata kunitajia majina yake wakati tukisafiri kwa miguu miaka ile iliyopita.
Kitu kingine kilichonivutia katika Ikulu hiyo ni ndege. Ilionekana kama shamba la wanyama kutokana na ndege aina mbalimbali waliokuwa wakiruka, kuimba na kucheza toka mti huu hadi ule, tawi hili hadi lile. Ndege walionivutia zaidi ni tausi. Walikuwa wengi, waliimba na kutembea kwa maringo kana kwamba wao ndio walikuwa wafalme na malkia wa bustani hiyo. Tausi mmoja, mwenye mkia mrefu na rangi ya kuvutia, alinizawadia kwa kunifunulia mkia wake na kuufanya
ugeuke kuwa mfano wa ……. mzuri wenye mchanganyiko wa rangi ya dhababu, almasi na lulu.
Ningeendelea kuduwaa hapo kama askari mmoja asingetokea na kunifukuza. Nikaondoka na kuifuata barabara inayotokea hapo Ikulu, ambayo nayo ni burudani tosha kwa miti asilia tele, iliyooteshwa kila upande na kuipa barabara kivuli na hewa murua tofauti kabisa na maeneo mengine ya mjini ambayo hayakutofautiana sana na jangwa.
Sikuwa na haraka. Nilitembea taratibu nikitazama hapa na pale. Nilipita katika bustani ya Mnazi mmoja, yenye maua na miti ya vivuli. Nikaiacha na kufika maeneo ambayo hayakuwa na watu hadi nilipofikia hoteli yangu. Ilikaribia saa mbili za usiku.
Wakati tayari nimeoga na kupiga mswaki nikijiandaa kulala mtaa wa pili zilisikika kelele za muziki. Sikuwa mpenzi sana wa muziki. Lakini ile midundo na tungo zao mara nyingi zilinisisimua. Hivyo, sikuhitaji kuambiwa kuwa muziki huo ulikuwa wa mwanamuziki mahiri, Hamisi Machapti aliyekuwa akiongoza
Dar es Salaam jazz, bendi kongwe iliyozaliwa mwaka 1933.
Nilimsikiliza kwa muda kabla ya usingizi kunichukua.
Kiguu n1a Njia
SURA YA KUMI TATU
Ya Kingalu wa Morogoro
“Petro!”
Nilishtuka kidogo lakini sikugeuka. Nani
ananifahamu mimi katika mji huu wa Dar es
Salaam? Zaidi, nani ananifahamu kwa jina hilo la Petro ambalo sina tabia ya kulitumia mara kwa mara? Nikaendelea na hatua zangu, moja baada ya nyingine; nikiwafuata kina Leakey ambao walikuwa wamesimama nje ya gari lao, tayari kwa safari yetu ndefu.
“Petro!” Sasa mwitaji alikuwa nyuma yangu. Pumzi yake, wakati akiniita, ikikifikia kichogo changu. Nikahisi mkono wake ukinigusa bega. Kwa sauti ya kujiamini zaidi nilimsikia akisema, “Wewe ni Petro Kionambali. Sidhani kama nitakuwa nimekosea.”
Nikageuka kumtazama. Aliyesimama pale alikuwa mtu ambaye kamwe nisingeweza kumsahau, mtu ambaye alisababisha safari yangu ya kielimu ivunjike mwanzo tu wa safari. Mtu huyo ndiye chanzo cha mikasa na masaibu yote yanayonipata. Nikamkodolea macho ya mshangao.
“Usiniambie kuwa hunikumbuki?” alisema akitabasamu. “Wewe si yule Petro wa hirizi”
“Ndiye” nikamjibu “Na wewe nakukumbuka vizuri sana.
Unaitwa Byabato. Tulikuwa wote kule Kagera.”
“Naam halafu ukapoteza hirizi yako,” akakumbushia. “Naam, na wewe ukaiokota.”
“Kabisa. Nikaipeleka kwa faza Backhove akaamua kuichoma moto hadharani…”
“Mie nikaikwapua na kukimbia nayo.”
Tulipofika hapo Byabato akaangua kicheko kisha akasema huku akiendelea kucheka, “Ikakuponyoka tena. Nikaiokota tena. Nikamrudishia faza. Akiwa amekasirika sana faza aliichukua na kuitumbukiza ndani ya moto kwa mkono wake mwenyewe.”
Taarifa yake ya mwisho ilikuwa habari mpya kwangu. Kumbe hirizi yangu ilipatikana na ikatiwa moto? Nikamtazama kwa macho yenye maswali mengi ambayo aliyasoma na kuyajibu baadhi.
“Hirizi haikuungua,” alisema. “Haikuungua? Ilikuwaje?” “Ilikataa kuungua!”
“Ilikataa kuungua! Kwa vipi?” nilizidi kushangaa. “Ilikataa tu. Ilikuwa hirizi ya ajabu sana na imeacha
historia kubwa. Kila ilipotupwa katika moto ilidunda na kuchupa kama chura hadi nje ya moto huo. Tukio hilo lilirudiwa zaidi ya mara tano, lakini hirizi haikukubali kuungua. Kila mtu alishangaa. Padri akaamua ikatupwe ziwani, mbali kabisa ya nchi kavu. Nadhani walifanya hivyo, ingawa baadhi ya wanafunzi wanadai padri aliihifadhi ili ipelekwe kwao ikafanyiwe uchunguzi wa kina.
Hirizi yangu ilikuwa na maajabu hayo! Niliwaza kwa mshangao. Nikamkazia macho Byabato kuona kama alikuwa akisema ukweli au uongo. Siku zote shuleni pale alijulikana