Mtafiti77
JF-Expert Member
- Oct 31, 2011
- 1,877
- 2,314
TAFAKURI TUNDUIZI TIBA YA MAENDELEO
UTANGULIZI
Umewahi kujiuliza kwanini watu hugombana katika mijadala? Kwanini kuna migogoro kati ya nchi na chi, mtu na mtu ama jamii na jamii? Kwanini baadhi ya miradi ya kitaifa haikamiliki ama hukamilika kwa mashaka?
Masuala yote hapo juu ni matokeo ya kukosa uwezo wa kufikiri kwa makini, yani, tafakuri tunduizi. Katika kitabu chao The Miniature Guide to Critical Thinking Concepts and Tools, Paul Richard na Linda Elder wanatukumbusha kuwa kila mwanadamu amepewa uwezo wa kufikiri kwakuwa hiki ni kitendo cha asili. Lakini, wanaonya kuwa ili kuwa na fikra makini, ni lazima tujifunze kwakuwa uwezo wetu wa kufikiri una mipaka. Ni vema watoto wakafunzwa tafakuri tunduizi ili kupunguza ubinafsi. Ukosefu wa fikra makini hupelekea mijadala dhaifu, migogoro isiyo na tija na maamuzi dhaifu au hatarishi.
TAFAKURI TUNDUIZI NI NINI?
Katika mjadala wetu, tutatumia fasili ya Elder na Paul (wametajwa hapo juu). Wao wanaona tafakuri tunduizi ni sanaa ya kuchambua na kutathmini wazo au fikra kwa mtazamo wa kuboresha fikra hizo. Msomi mkubwa anaweza kukosa maarifa haya kama tunavyoshuhudia kwenye jamii zetu. Aidha, hakuna utimilifu katika tafakuri tunduizi bali huwa tunapimwa kwa viwango. Utimilifu wa elimu hii ni pale utakapokuwa na uwezo wa kukiri kuwa kufikiri kwako kuna mipaka.
FAIDA ZA KUJIFUNZA TAFAKURI TUNDUIZI
Mtu mwenye maarifa ya tafakuri tunduizi:
MAMBO YANAYOATHIRI TAFAKURI TUNDUIZI
Tafakuri tunduizi huathiriwa sana na mazingira tunayokulia ama kuishi. Mengi yanafunikwa katika utamaduni, dini na elimu (isiyo sahihi). Tutazame hili kwa mifano ya kitafiti. Wanazuoni Geert Hofstede na Edward T. Hall wamependekeza vigezo vya kuzitambua tamaduni mbalimbali hapa duniani. Vigezo hivi ni MAMLAKA (Hofstede) na MUKTADHA (Hall). Walitumia vigezo hivi kuonesha namna jamii zinaathiriwa na vigezo hivi katika maisha na mitazamo yao ya kila siku.
MAMLAKA: Kwa mujibu wa Hofstede , tamaduni zinaweza kugawanywa katika makundi mawili: Zile ambazo mamlaka hutawala mahusiano na mawasiliano kwa kiasi kikubwa, na zile ambazo zinazoathiriwa na mamlaka kwa kiwango cha chini. Kwa zile zinazoathiriwa na mamlaka zaidi, suala la “nani kasema ama katenda” ni muhimu sana. Mtu mwenye mamlaka katika muktadha husika ndiye anaesikilizwa bila ya kujali alichozungumza ni sahihi ama la. Katika jamii hizi, ni vigumu kumkosoa mwenye mamlaka. Jamii za Kiafrika zinaingia katika kundi hili. Tanzania, kwa mfano, wazazi ama viongozi hawakosolewi. Hata kondakta wa daladala pale garini ndiye mwenye mamlaka—anaweza kukukoromea atakavyo. Ni hivi karibuni Rais Samia Suluhu alisikika akisema rais hakosei. Hapa alidhihirisha utamaduni wetu, mzazi ama mkubwa hakosei. Nchi za magharibi kama Marekani ni tofauti kidogo, wao wapo kundi la pili, mamlaka yanakuwa chini katika mahusiano na mawasiliano.
MUKTADHA: Katika kigezo hiki, Hall anadai kuwa kuna tamaduni ambazo muktadha huathiri zaidi mawasiliano na mahusiano kuliko lugha na zile ambazo huathiriwa kwa kiwango cha chini. Kwa maneno mengine, jamii zinazoathiriwa na muktadha zaidi, watu wake hawapo wazi. Maneno pekee hayajitoshelezi kumuelewa mzungumzaji, unahitaji kumuelewa mzungumzaji zaidi ya kile anachokisema. Kwa mara nyingine, Waafrika wanaangukia kwenye kundi hili. Mtanzania akikuomba sukari kijiko kimoja, mpe vijiko zaidi kimoja. Ukimpa kijiko kimoja utatafsiriwa kama mchoyo. Hata bei kwa baadhi ya bidhaa hazipo wazi. Inabidi mteja aoneshe atakacho kisha atajiwe bei. Tabia ya kutokuwa wazi huathiri maamuzi kwa mtu mmojammoja, kikundi, jamiii ama taifa. Hali hii ni tofauti kidogo na nchi za magharibi, wao wapo wazi. Mara nyingi kinachotamkwa humaanishwa. Wao wapo kundi la pili, matumizi ya chini ya muktadha.
Kwa kuhitimisha kipengele hiki, tunasema hivi. Tofauti zinazotajwa hapa si kama vile nyeupe na nyeusi. Yani kama si nyeusi basi ni nyeupe, la hasha, tunatazama ni tabia ipi inatawala zaidi. Jamii zote zinatumia mamlaka, zote zinatumia muktadha, lakini, jamii moja huzidiana na nyingine kulingana na wingi wa sifa tajwa.
Aidha, kama tulivyodokeza hapo awali kwenye kipengele hiki, utamaduni, dini na elimu (isiyo sahihi) huathiri kwa kiasi kikubwa tafakuri tunduizi. Watu tunaoegemea mamlaka na muktadha zaidi tuna hatari kubwa ya kuwa na maarifa duni katika tafakuri tunduizi na hivyo kuathiri maamuzi na maisha yetu ya kila siku. Kuanzia tunapokuwa majumbani hatujifunzi kukosoa, maana baba, mama, dada, shangazi, mjomba n.k., ndiyo wasemaji wa mwisho. Tukiwa mashuleni halikadhalika, mwalimu hahojiwi. Hata kitaifa, wakuu wa serikali ni kila kitu. Ni vigumu watu kuonesha uwezo ama vipaji vyao katika sehemu zao za kazi ama kwenye jamii. Huu ni mfano wa kifo cha tafakuri tunduizi.
VIGEZO VITUMIKAVYO KUPIMA TAFAKURI TUNDUIZI
Elder na Paul pia wamebainisha vigezo kadhaa tunavyoweza kuvitumia kutathmini hoja makini pamoja na maswali ya kufikia vigezo hivyo:
Ufasaha/uhadhiri wa hoja: Iwapo hoja haipo wazi ama dhahiri, unaweza kumuuliza mtoa hoja maswali haya: Unaweza kuboresha zaidi hoja yako. Unaweza kuileza kwa namna nyingine? Unaweza kutoa mifano?
Usahihi: Hoja inaweza kuwa dhahiri lakini ikakosa usahihi. Kwa mfano, “Uchumi wa nchi umekua”. Kauli hii ipo dhahiri lakini inakosa usahihi. Je, ni kweli? Tunathibitishaje?
Utoshelevu: Hoja inaweza kuwa dhahiri na sahihi lakini isijitosheleze. Kwa mfano, “Nchi ya Tanzania ni kubwa” Unaweza kueleza kiundani? Unaweza kuwa bayana zaidi?
Ushikamani: Je, kisemwacho kina uhusiano na hoja inayojadiliwa? Kwanini unalileta suala hili katika mjadala huu?
Kina: Je, ni kweli mchangiaji ameidadavua hoja kwa kina? Ni kweli amezingatia mahitaji ya mjadala ama hoja husika kwa kina?
Mawanda: Ukiacha kina, kuna suala la mawanda. Ni kwa kiasi gani mzungumzaji amezingatia mitazamo mbalimbali katika ujenzi wa hoja? Suala hili litatazamwa vipi ikiwa litatazamwa hivi ama vile? Unapozungumzia masuala tata kama ya mitazamo ya kidini, siasa, rangi n.k, ni vema kuzingatia mitazamo mbalimbali. Kumbuka, kile unachofahamu ni kile ulichojifunza kwenye familia, jamii ama darasani kwako pekee, dunia ni pana na tata.
Mantiki: Je, muunganiko na mfuatano wa hoja upo sawa? Kilichosema awali na sasa vinaendana ama kuna kuyumba kwa hoja? Mfano mzuri ni kauli za wanasiasa. Alichosema ama kutenda mwaka jana ndicho anachokisimamia leo? Kama amegeuka, kwanini? Kama anasimama mlemle wakati anapaswa kubadilika , kwanini?
Uungwana/utu: Je, mzungumzaji anaitendea haki mitazamo yote kwa pamoja? Kama anakataa ama kukubali hoja za upande X, anafanya hivyo kwa vigezo stahiki ama kwa kujali nafsi yake pekee? Je, si kwamba anapotosha baadhi ya taarifa fulani mradi tu akamilishe matakwa yake? Je, anajali masilahi ya wengi ama ni mbinafsi?
ATHARI ZITOKANAZO NA KUKOSA MAARIFA YA TAFAKURI TUNDUIZI
Mambo yafuatayo ni chanzo kikubwa cha matatizo katika jamii zetu.
Msisitizo
Suala la watu kutofautiana kifikra ni muhimu sana katika tafakuri tunduizi. Bw. Abraham Lincoln aliyewahi kuwa rais wa Marekani aliwahi kusema:
“Mchungaji alimfurusha mbwa mwitu kutoka kwenye koromeo la kondoo, ambapo kondoo alimshukuru mchungaji kama mwokozi, wakati mbwa mwitu alimshutumu mchungaji kama mwenye kuunajisi uhuru. Ni dhahiri, kondoo na mbwa mwitu hawana fasili ya pamoja kuhusu uhuru.”
Ni wajibu wetu kujenga jamii yenye kujali haki
Mtafiti77
UTANGULIZI
Umewahi kujiuliza kwanini watu hugombana katika mijadala? Kwanini kuna migogoro kati ya nchi na chi, mtu na mtu ama jamii na jamii? Kwanini baadhi ya miradi ya kitaifa haikamiliki ama hukamilika kwa mashaka?
Masuala yote hapo juu ni matokeo ya kukosa uwezo wa kufikiri kwa makini, yani, tafakuri tunduizi. Katika kitabu chao The Miniature Guide to Critical Thinking Concepts and Tools, Paul Richard na Linda Elder wanatukumbusha kuwa kila mwanadamu amepewa uwezo wa kufikiri kwakuwa hiki ni kitendo cha asili. Lakini, wanaonya kuwa ili kuwa na fikra makini, ni lazima tujifunze kwakuwa uwezo wetu wa kufikiri una mipaka. Ni vema watoto wakafunzwa tafakuri tunduizi ili kupunguza ubinafsi. Ukosefu wa fikra makini hupelekea mijadala dhaifu, migogoro isiyo na tija na maamuzi dhaifu au hatarishi.
TAFAKURI TUNDUIZI NI NINI?
Katika mjadala wetu, tutatumia fasili ya Elder na Paul (wametajwa hapo juu). Wao wanaona tafakuri tunduizi ni sanaa ya kuchambua na kutathmini wazo au fikra kwa mtazamo wa kuboresha fikra hizo. Msomi mkubwa anaweza kukosa maarifa haya kama tunavyoshuhudia kwenye jamii zetu. Aidha, hakuna utimilifu katika tafakuri tunduizi bali huwa tunapimwa kwa viwango. Utimilifu wa elimu hii ni pale utakapokuwa na uwezo wa kukiri kuwa kufikiri kwako kuna mipaka.
FAIDA ZA KUJIFUNZA TAFAKURI TUNDUIZI
Mtu mwenye maarifa ya tafakuri tunduizi:
- Huweza kukusanya, kuchunguza na kutafsiri taarifa kwa ufanisi.
- Huhitimisha na kutoa masuluhisho vema huku akiyapima kwa vigezo stahiki.
- Hufikiri kwa mapana akitumia mikabala/mitazamo tofauti huku akizingatia ubora na udhaifu wa kila mtazamo.
- Huwasiliana kwa ufanisi na hushiriki vema katika kutatua na kutoa masuluhisho ya matatizo mbalimbali (Elder & Paul, 2008).
MAMBO YANAYOATHIRI TAFAKURI TUNDUIZI
Tafakuri tunduizi huathiriwa sana na mazingira tunayokulia ama kuishi. Mengi yanafunikwa katika utamaduni, dini na elimu (isiyo sahihi). Tutazame hili kwa mifano ya kitafiti. Wanazuoni Geert Hofstede na Edward T. Hall wamependekeza vigezo vya kuzitambua tamaduni mbalimbali hapa duniani. Vigezo hivi ni MAMLAKA (Hofstede) na MUKTADHA (Hall). Walitumia vigezo hivi kuonesha namna jamii zinaathiriwa na vigezo hivi katika maisha na mitazamo yao ya kila siku.
MAMLAKA: Kwa mujibu wa Hofstede , tamaduni zinaweza kugawanywa katika makundi mawili: Zile ambazo mamlaka hutawala mahusiano na mawasiliano kwa kiasi kikubwa, na zile ambazo zinazoathiriwa na mamlaka kwa kiwango cha chini. Kwa zile zinazoathiriwa na mamlaka zaidi, suala la “nani kasema ama katenda” ni muhimu sana. Mtu mwenye mamlaka katika muktadha husika ndiye anaesikilizwa bila ya kujali alichozungumza ni sahihi ama la. Katika jamii hizi, ni vigumu kumkosoa mwenye mamlaka. Jamii za Kiafrika zinaingia katika kundi hili. Tanzania, kwa mfano, wazazi ama viongozi hawakosolewi. Hata kondakta wa daladala pale garini ndiye mwenye mamlaka—anaweza kukukoromea atakavyo. Ni hivi karibuni Rais Samia Suluhu alisikika akisema rais hakosei. Hapa alidhihirisha utamaduni wetu, mzazi ama mkubwa hakosei. Nchi za magharibi kama Marekani ni tofauti kidogo, wao wapo kundi la pili, mamlaka yanakuwa chini katika mahusiano na mawasiliano.
MUKTADHA: Katika kigezo hiki, Hall anadai kuwa kuna tamaduni ambazo muktadha huathiri zaidi mawasiliano na mahusiano kuliko lugha na zile ambazo huathiriwa kwa kiwango cha chini. Kwa maneno mengine, jamii zinazoathiriwa na muktadha zaidi, watu wake hawapo wazi. Maneno pekee hayajitoshelezi kumuelewa mzungumzaji, unahitaji kumuelewa mzungumzaji zaidi ya kile anachokisema. Kwa mara nyingine, Waafrika wanaangukia kwenye kundi hili. Mtanzania akikuomba sukari kijiko kimoja, mpe vijiko zaidi kimoja. Ukimpa kijiko kimoja utatafsiriwa kama mchoyo. Hata bei kwa baadhi ya bidhaa hazipo wazi. Inabidi mteja aoneshe atakacho kisha atajiwe bei. Tabia ya kutokuwa wazi huathiri maamuzi kwa mtu mmojammoja, kikundi, jamiii ama taifa. Hali hii ni tofauti kidogo na nchi za magharibi, wao wapo wazi. Mara nyingi kinachotamkwa humaanishwa. Wao wapo kundi la pili, matumizi ya chini ya muktadha.
Kwa kuhitimisha kipengele hiki, tunasema hivi. Tofauti zinazotajwa hapa si kama vile nyeupe na nyeusi. Yani kama si nyeusi basi ni nyeupe, la hasha, tunatazama ni tabia ipi inatawala zaidi. Jamii zote zinatumia mamlaka, zote zinatumia muktadha, lakini, jamii moja huzidiana na nyingine kulingana na wingi wa sifa tajwa.
Aidha, kama tulivyodokeza hapo awali kwenye kipengele hiki, utamaduni, dini na elimu (isiyo sahihi) huathiri kwa kiasi kikubwa tafakuri tunduizi. Watu tunaoegemea mamlaka na muktadha zaidi tuna hatari kubwa ya kuwa na maarifa duni katika tafakuri tunduizi na hivyo kuathiri maamuzi na maisha yetu ya kila siku. Kuanzia tunapokuwa majumbani hatujifunzi kukosoa, maana baba, mama, dada, shangazi, mjomba n.k., ndiyo wasemaji wa mwisho. Tukiwa mashuleni halikadhalika, mwalimu hahojiwi. Hata kitaifa, wakuu wa serikali ni kila kitu. Ni vigumu watu kuonesha uwezo ama vipaji vyao katika sehemu zao za kazi ama kwenye jamii. Huu ni mfano wa kifo cha tafakuri tunduizi.
VIGEZO VITUMIKAVYO KUPIMA TAFAKURI TUNDUIZI
Elder na Paul pia wamebainisha vigezo kadhaa tunavyoweza kuvitumia kutathmini hoja makini pamoja na maswali ya kufikia vigezo hivyo:
Ufasaha/uhadhiri wa hoja: Iwapo hoja haipo wazi ama dhahiri, unaweza kumuuliza mtoa hoja maswali haya: Unaweza kuboresha zaidi hoja yako. Unaweza kuileza kwa namna nyingine? Unaweza kutoa mifano?
Usahihi: Hoja inaweza kuwa dhahiri lakini ikakosa usahihi. Kwa mfano, “Uchumi wa nchi umekua”. Kauli hii ipo dhahiri lakini inakosa usahihi. Je, ni kweli? Tunathibitishaje?
Utoshelevu: Hoja inaweza kuwa dhahiri na sahihi lakini isijitosheleze. Kwa mfano, “Nchi ya Tanzania ni kubwa” Unaweza kueleza kiundani? Unaweza kuwa bayana zaidi?
Ushikamani: Je, kisemwacho kina uhusiano na hoja inayojadiliwa? Kwanini unalileta suala hili katika mjadala huu?
Kina: Je, ni kweli mchangiaji ameidadavua hoja kwa kina? Ni kweli amezingatia mahitaji ya mjadala ama hoja husika kwa kina?
Mawanda: Ukiacha kina, kuna suala la mawanda. Ni kwa kiasi gani mzungumzaji amezingatia mitazamo mbalimbali katika ujenzi wa hoja? Suala hili litatazamwa vipi ikiwa litatazamwa hivi ama vile? Unapozungumzia masuala tata kama ya mitazamo ya kidini, siasa, rangi n.k, ni vema kuzingatia mitazamo mbalimbali. Kumbuka, kile unachofahamu ni kile ulichojifunza kwenye familia, jamii ama darasani kwako pekee, dunia ni pana na tata.
Mantiki: Je, muunganiko na mfuatano wa hoja upo sawa? Kilichosema awali na sasa vinaendana ama kuna kuyumba kwa hoja? Mfano mzuri ni kauli za wanasiasa. Alichosema ama kutenda mwaka jana ndicho anachokisimamia leo? Kama amegeuka, kwanini? Kama anasimama mlemle wakati anapaswa kubadilika , kwanini?
Uungwana/utu: Je, mzungumzaji anaitendea haki mitazamo yote kwa pamoja? Kama anakataa ama kukubali hoja za upande X, anafanya hivyo kwa vigezo stahiki ama kwa kujali nafsi yake pekee? Je, si kwamba anapotosha baadhi ya taarifa fulani mradi tu akamilishe matakwa yake? Je, anajali masilahi ya wengi ama ni mbinafsi?
ATHARI ZITOKANAZO NA KUKOSA MAARIFA YA TAFAKURI TUNDUIZI
Mambo yafuatayo ni chanzo kikubwa cha matatizo katika jamii zetu.
- Jambo X ni kweli kwa sababu tu ninaamini hivyo. Unakomaa na jambo kwa kuwa tu unaamini hata kama hujahoji ukweli wa suala hilo.
- Jambo X ni kweli kwakuwa tu tunaamini hivyo. Eti kwakuwa kikundi ama jamii yenu inaamini, nawe unakomaa hata kama hujawahi kuthibitisha.
- Jambo X ni kweli kwa kuwa ninataka kuliamini. Unakomalia jambo hata kama hujathibitisha ukweli wake kwakuwa tu unataka kuliamini.
- Ninaamini kwakuwa siku zote nimekuwa nikiamini. Unakomalia jambo kwakuwa umekuwa siku zote ukiliamini hata kama hujawahi kuthibitisha.
- Ni kweli kwakuwa nina maslahi nalo binafsi. Kwakuwa jambo X litakunufaisha, basi unalikomalia mradi tu likufikishe ama likupatie utakacho.
- Kuamini jamii , jinsi, rangi yako ni bora kuliko wengine (ubaguzi).
- Kutoweza kuchuja taarifa ama hoja mbalimbali ikiwemo zile za vyombo vya habari , matangazo ya biashara kama vipodozi na yale ya wanasiasa. (Paul na Elder)
Msisitizo
Suala la watu kutofautiana kifikra ni muhimu sana katika tafakuri tunduizi. Bw. Abraham Lincoln aliyewahi kuwa rais wa Marekani aliwahi kusema:
“Mchungaji alimfurusha mbwa mwitu kutoka kwenye koromeo la kondoo, ambapo kondoo alimshukuru mchungaji kama mwokozi, wakati mbwa mwitu alimshutumu mchungaji kama mwenye kuunajisi uhuru. Ni dhahiri, kondoo na mbwa mwitu hawana fasili ya pamoja kuhusu uhuru.”
Ni wajibu wetu kujenga jamii yenye kujali haki
Mtafiti77
Upvote
8