Ng'wanamalundi
JF-Expert Member
- Feb 4, 2008
- 1,203
- 1,422
Niliona mada ikihoji Mwinyi kutaka kugombea uongozi wakati ni mweupe kiasi kwamba mtoa mada anastaajabu ilikuwaje akaaminiwa kufanywa Waziri wa Jeshi. Kichwa cha habari kiliashiria kwamba mtajwa hana asili ya Kiafrika na kwamba hastahili kupewa uongozi huo. Napenda kuchukulia kwamba hoja ya mchangiaji haikuwa juu ya asili ya mtu. Pamoja na hayo, ninapenda kuonya tutofautishe asili ya mtu na uzalendo wake kwa nchi.
Kuna mfano wa Jerry Rawlings wa Ghana ambaye, si kwa jina tu bali hata kwa muonekano, alikuwa dhihiri siyo Mghana au Mwafrika asilia. Alikuwa na nasaba ya Uingereza na bado alipewa kuiongoza Ghana kwa vipindi viwili visivyofuatana, akaiboresha Ghana kufuatia kipindi kirefu cha uongozi wa kijeshi. Yupo pia Barack Oboma mweusi aliyeweza kuwa Rais wa Marekani pamoja na kwamba wapiga kura walijua fika asili yake ni Kenya.
Hapa Tanzania kuna Salim Ahmed Salim, chotara ambaye alidiriki a kushika wadhifa wa Waziri Mkuu, mbali na kuteuliwa Balozi tangu akiwa na umri mdogo wa miaka 29 tu. Kwenye majeshi kulikuwa na machotara wengi, kwa mfano Hans Pope ambaye alikuwa wa kwanza kuuliwa na majeshi ya Amin mwanzoni mwa vita vya Kagera. Amin akatangaza kwamba Tanzania inasaidiwa na askari wa Kichina kutokana na muonekano wa Hans Pope. Tukiachana na machotara hao, ninapenda kutoa mifano minne ya watu ambao hawakuwa na hata chembe ya uweusi lakini walikuwa viongozi wa juu nchini Tanzania.
Wa kwanza ni Mhindi Amir Jamal ambaye alikuwa waziri kwa muda mrefu. Yeye alikuwa Waziri wa Fedha kwa kipindi kirefu kuzidi waziri mwingine yo yote wa Wizara hiyo katika historia ya Tanzania. Alikuwa Mbunge kutoka Morogoro na katika jimbo lake ilikuwa ukithubutu kugombea naye utashindwa vibaya sana.
Alikuwa mchapa kazi na mzalendo halisi anayeipenda Tanzania. Wakati akiwa Waziri wa viwanda na Biashara, Morogoro kulianzishwa viwanda vingi kwa mfano kiwanda cha mafuta ya kula, MOPROCO, kiwanda cha ngozi (tanneries) pamoja na kwamba ng'ombe waliokuwa wakizalisha ngozi hizo walikuwa wanatoka Usukumani; na karakana ya vichwa vya treni ambayo mtu angedhania kama si kuiweka Dar basi iwe Tabora ambapo ni njiapanda ya Kigoma, Mwanza na Dar. Alipostaafu, mwalimu alimfanya Balozi UN huko Geneva.
Kufuatia Azimio la Arusha la mwaka 1967, kulitolewa Mwongozo kwa viongozi nchini, kama vile kiongozi asiwe na nyumba ya kupangisha na tafsiri ya kiongozi ni mtu na mke ili usije ukamwandikisha mkeo kwenye biashara kukwepa kubanwa na masharti ya uongozi. Kuna habari kwamba Amir Jamal alikubaliana kabisa na sera hiyo lakini alimwombi Rais awe waziri bila kulipwa mshahara abakie na ghorofa lake la IPS.
Hivyo akawa anapewa stahili yake ya marupurupu tu ya uwaziri lakini anafanya kazi bila ya mshahara, akipokea kodi ya pango la jumba lake. Hivyo ndivyo alivyokuwa mzalendo na Mwalimu alimpenda sana kwa hilo. Walizaliwa mwaka mmoja, 1922, na yeye alifia Canada mwaka 1995, miaka minne kabla ya Mwalimu. Alipofariki, Mwalimu aliomba mwili wake urudishwe kuzikwa Tanzania lakini Canada ikakataa.
Wa pili ni Mwingereza Derek Brycesson ambaye alikuwa Waziri wa Kilimo kwa muda mrefu na baadaye akawa Mkurugenzi wa Mbuga za Hifadhi ya Wanyama. Alikuwa Mbunge wa Kinondoni. Alikuwa hajui Kiswahili vizuri lakini wananchi walimjua kuwa ni mchapa kazi hodari.
Katika mkutano mmoja wa kujinadi wagombea ubunge huko Manzese ambako ilikuwa sehemu ya Jimbo la Kinondoni, alikuwa akigombea na mama mmoja mfanyakazi wa Radio Tanzania aliyekuwa akijulikana kwa jina la 'Çhips'. Mama akaanza kujieleza mpaka dakika walizopangiwa kuzungumza zikaisha akanyamazishwa na Mwenyekiti. Baada ya maswali ikaja zamu ya Brycesson. Yeye kwa kuwa hata Kiswahili hakifahamu vizuri akazungumza sentensi mbili-tatu tu na hakumaliza hata hizo dakika alizopangiwa.
La muhimu alilowaeleza wapiga kura ni kwamba kama wanataka maendeleo wachague Brycesson; lakini kama wana njaa wanataka kula wachague Chips. Brycesson aliibuka na zaidi ya theluthi mbili za kura kwa kuwa tu wapiga kura wanamjua ni mchapa kazi na hawakumpendelea Mwafrika mwenzao. Yeye alizaliwa mwaka 1923 na akafariki mwaka 1985.
Wa tatu ni Mhindi Al Noor Kassum aliyezaliwa mwaka 1924 na bado anaishi. Huyu naye alikuwa mchapa kazi na Mwalimu alimpa uwaziri kwa kipindi kirefu. Wizara aliyoiongoza kwa muda mrefu ni Wizara ya Nishati na Maji. Bajeti ya Wizara yake zilikuwa zikiwasilishwa Bungeni na Naibu Waziri kwa kuwa Kassum alikuwa hajui Kiswahili vizuri. Siku moja, wakati Bunge likijadili bajeti ya Wizara yake, Waziri Mdogo alielemewa sana na maswali ya Wabunge. Kassum, ambaye alikuwemo Bungeni, akamwomba Spika ruhusa aongee kwa Kiingereza kujibu hoja za Wabunge. Hapo ndipo akaweza kuwapoza Wabunge.
Mtu wa nne ni Mama Joan Wicken aliyekuwa msaidizi wa Mwalimu tangu kabla ya Uhuru. Yeye alizaliwa Uingereza mwaka 1925 na alikuja Tanzania kama mfanyakazi wa Commonwealth. Alikuwa akikubaliana sana na sera za Mwalimu ambaye alimfanya kuwa msaidizi wake tangu enzi za kupigania uhuru, hadi Mwalimu akawa Rais na baadaye akaongoza South-South Commission. Wicken hakuwa waziri. Namjumlisha hapa kwa kuwa alikuwa na cheo nyeti cha kujua yafanywayo na Rais wa nchi.
Nimewataja hao wanne ambao hawakuwa na asili ya Mwafrika mweusi lakini walikuwa na uzalendo wakuaminika. Wicken yeye alizaliwa nje ya Tanzania na alipata uraia wa kujiandikisha tu. Hoja yangu ni kwamba tutazame uzalendo wa mtu bila kujali asili yake.
Kuna mfano wa Jerry Rawlings wa Ghana ambaye, si kwa jina tu bali hata kwa muonekano, alikuwa dhihiri siyo Mghana au Mwafrika asilia. Alikuwa na nasaba ya Uingereza na bado alipewa kuiongoza Ghana kwa vipindi viwili visivyofuatana, akaiboresha Ghana kufuatia kipindi kirefu cha uongozi wa kijeshi. Yupo pia Barack Oboma mweusi aliyeweza kuwa Rais wa Marekani pamoja na kwamba wapiga kura walijua fika asili yake ni Kenya.
Hapa Tanzania kuna Salim Ahmed Salim, chotara ambaye alidiriki a kushika wadhifa wa Waziri Mkuu, mbali na kuteuliwa Balozi tangu akiwa na umri mdogo wa miaka 29 tu. Kwenye majeshi kulikuwa na machotara wengi, kwa mfano Hans Pope ambaye alikuwa wa kwanza kuuliwa na majeshi ya Amin mwanzoni mwa vita vya Kagera. Amin akatangaza kwamba Tanzania inasaidiwa na askari wa Kichina kutokana na muonekano wa Hans Pope. Tukiachana na machotara hao, ninapenda kutoa mifano minne ya watu ambao hawakuwa na hata chembe ya uweusi lakini walikuwa viongozi wa juu nchini Tanzania.
Wa kwanza ni Mhindi Amir Jamal ambaye alikuwa waziri kwa muda mrefu. Yeye alikuwa Waziri wa Fedha kwa kipindi kirefu kuzidi waziri mwingine yo yote wa Wizara hiyo katika historia ya Tanzania. Alikuwa Mbunge kutoka Morogoro na katika jimbo lake ilikuwa ukithubutu kugombea naye utashindwa vibaya sana.
Alikuwa mchapa kazi na mzalendo halisi anayeipenda Tanzania. Wakati akiwa Waziri wa viwanda na Biashara, Morogoro kulianzishwa viwanda vingi kwa mfano kiwanda cha mafuta ya kula, MOPROCO, kiwanda cha ngozi (tanneries) pamoja na kwamba ng'ombe waliokuwa wakizalisha ngozi hizo walikuwa wanatoka Usukumani; na karakana ya vichwa vya treni ambayo mtu angedhania kama si kuiweka Dar basi iwe Tabora ambapo ni njiapanda ya Kigoma, Mwanza na Dar. Alipostaafu, mwalimu alimfanya Balozi UN huko Geneva.
Kufuatia Azimio la Arusha la mwaka 1967, kulitolewa Mwongozo kwa viongozi nchini, kama vile kiongozi asiwe na nyumba ya kupangisha na tafsiri ya kiongozi ni mtu na mke ili usije ukamwandikisha mkeo kwenye biashara kukwepa kubanwa na masharti ya uongozi. Kuna habari kwamba Amir Jamal alikubaliana kabisa na sera hiyo lakini alimwombi Rais awe waziri bila kulipwa mshahara abakie na ghorofa lake la IPS.
Hivyo akawa anapewa stahili yake ya marupurupu tu ya uwaziri lakini anafanya kazi bila ya mshahara, akipokea kodi ya pango la jumba lake. Hivyo ndivyo alivyokuwa mzalendo na Mwalimu alimpenda sana kwa hilo. Walizaliwa mwaka mmoja, 1922, na yeye alifia Canada mwaka 1995, miaka minne kabla ya Mwalimu. Alipofariki, Mwalimu aliomba mwili wake urudishwe kuzikwa Tanzania lakini Canada ikakataa.
Wa pili ni Mwingereza Derek Brycesson ambaye alikuwa Waziri wa Kilimo kwa muda mrefu na baadaye akawa Mkurugenzi wa Mbuga za Hifadhi ya Wanyama. Alikuwa Mbunge wa Kinondoni. Alikuwa hajui Kiswahili vizuri lakini wananchi walimjua kuwa ni mchapa kazi hodari.
Katika mkutano mmoja wa kujinadi wagombea ubunge huko Manzese ambako ilikuwa sehemu ya Jimbo la Kinondoni, alikuwa akigombea na mama mmoja mfanyakazi wa Radio Tanzania aliyekuwa akijulikana kwa jina la 'Çhips'. Mama akaanza kujieleza mpaka dakika walizopangiwa kuzungumza zikaisha akanyamazishwa na Mwenyekiti. Baada ya maswali ikaja zamu ya Brycesson. Yeye kwa kuwa hata Kiswahili hakifahamu vizuri akazungumza sentensi mbili-tatu tu na hakumaliza hata hizo dakika alizopangiwa.
La muhimu alilowaeleza wapiga kura ni kwamba kama wanataka maendeleo wachague Brycesson; lakini kama wana njaa wanataka kula wachague Chips. Brycesson aliibuka na zaidi ya theluthi mbili za kura kwa kuwa tu wapiga kura wanamjua ni mchapa kazi na hawakumpendelea Mwafrika mwenzao. Yeye alizaliwa mwaka 1923 na akafariki mwaka 1985.
Wa tatu ni Mhindi Al Noor Kassum aliyezaliwa mwaka 1924 na bado anaishi. Huyu naye alikuwa mchapa kazi na Mwalimu alimpa uwaziri kwa kipindi kirefu. Wizara aliyoiongoza kwa muda mrefu ni Wizara ya Nishati na Maji. Bajeti ya Wizara yake zilikuwa zikiwasilishwa Bungeni na Naibu Waziri kwa kuwa Kassum alikuwa hajui Kiswahili vizuri. Siku moja, wakati Bunge likijadili bajeti ya Wizara yake, Waziri Mdogo alielemewa sana na maswali ya Wabunge. Kassum, ambaye alikuwemo Bungeni, akamwomba Spika ruhusa aongee kwa Kiingereza kujibu hoja za Wabunge. Hapo ndipo akaweza kuwapoza Wabunge.
Mtu wa nne ni Mama Joan Wicken aliyekuwa msaidizi wa Mwalimu tangu kabla ya Uhuru. Yeye alizaliwa Uingereza mwaka 1925 na alikuja Tanzania kama mfanyakazi wa Commonwealth. Alikuwa akikubaliana sana na sera za Mwalimu ambaye alimfanya kuwa msaidizi wake tangu enzi za kupigania uhuru, hadi Mwalimu akawa Rais na baadaye akaongoza South-South Commission. Wicken hakuwa waziri. Namjumlisha hapa kwa kuwa alikuwa na cheo nyeti cha kujua yafanywayo na Rais wa nchi.
Nimewataja hao wanne ambao hawakuwa na asili ya Mwafrika mweusi lakini walikuwa na uzalendo wakuaminika. Wicken yeye alizaliwa nje ya Tanzania na alipata uraia wa kujiandikisha tu. Hoja yangu ni kwamba tutazame uzalendo wa mtu bila kujali asili yake.