Stephano Mgendanyi
JF-Expert Member
- May 16, 2020
- 2,833
- 1,301
VIKWAZO 10 VYA KIBIASHARA KUONDOLEWA JUMUIYA YA AFRIKA MASHARIKI
Nchi Wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) zimekubaliana kuondoa vikwazo kumi vya kibiashara visivyo vya kiforodha (NTBs), huku vikwazo nane vikiendelea kushughulikiwa, na vikwazo vingine vipya vinne vimewasilishwa ili kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara baina ya nchi hizo.
Makubaliano hayo yamefikiwa katika Mkutano wa 42 wa Baraza la Kisekta la Mawaziri wa Biashara, Viwanda, Fedha na Uwekezaji la Jumuiya ya Afrika Mashariki (SCTIFI) uliofanyika tarehe 03 Juni, 2023 katika Makao Makuu ya Jumuiya hiyo, Jijini Arusha.
Wakizungumza baada ya Mkutano huo, Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji na Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, wamesema kuwa Baraza hilo la Mawaziri wa Kisekta, limekubaliana kutoza dola 10 za kimarekani kwa kilomita 100 kwa ajili ya matumizi ya barabara kwa malori ya mizigo yanayofanya safari katika nchi wanachama badala ya kila nchi kutoza gharama zake, pamoja na kuimarisha utoaji huduma za forodha katika mpaka wa Kenya na Tanzania, ambako kutapunguza msongamano wa malori na kuchochea ukuaji wa biashara.
Aidha, Baraza hilo la Mawaziri la Kisekta, limekubaliana kuondoa gharama ya viza kwa watu wanaotaka kusafiri kutoka nchi moja kwenda nyingine kwa shughuli mbalimbali zikiwemo za kibiashara, ili kukuza mahusiano miongoni mwa wakazi wa Jumuiya hiyo pamoja na kuchochea ukuaji wa biashara na uchumi wa nchi husika.
Kuhusu uondoshaji wa mizigo, Mawaziri hao walifahamishwa kuwa mizigo ya Tanzania inayosafirishwa kwenda Kenya itaendelea kuondoshwa kupitia Mfumo wa Himaya Moja ya Forodha unaotumika
Mkutano huo unaojumuisha nchi wanachama wa EAC ambao ni Tanzania, Kenya, Uganda, Burundi, Rwanda, Sudani Kusini na DR – Congo, hufanyika kwa mujibu wa Kalenda ya Mikutano ya EAC ambapo kwa awamu hii Mkutano huo, uliongozwa na Mwenyekiti ambaye ni Waziri wa Biashara, Uchukuzi, Viwanda na Utalii wa Burundi, Mhe Marie Chantal Nijimbere.