Hivi ni kweli kuwa vinywaji vya kutia mwili nishati (energy drinks) hupelekea upungufu wa nguvu za kiume?
- Tunachokijua
- Energy drinks (Vinywaji vya kuongeza nishati) huwekewa kiasi kikubwa cha viambato vya caffeine, sukari pamoja na kemikali zinazo amsha mwili kama vile guarana, taurine na L-carnitine.
Vinjwaji hivi husisimua mwili pamoja na kuongeza nishati, shinikizo la damu, mapigo ya moyo na kasi ya upumuaji.
Kwa mujibu wa Kituo Cha Udhibiti na Kinga ya Magonjwa (CDC), matumizi makubwa ya vinywaji hivi yanaweza kusababisha athari kubwa kwenye mfumo wa kati wa fahamu.
Athari zingine za vinjwaji hivi ni:
- Kuufanya mwili upoteze kiasi kikubwa cha maji
- Magonjwa ya mfumo wa damu na moyo
- Wasiwasi uliopitiliza
- Kukosa usingizi
Miaka ya hivi karibuni, matumizi yake yameongezeka sana kwenye jamii zetu hasa kwa vijana, hali inayohusishwa na tatizo kupungua kwa nguvu za kiume miongoni mwao.
Kwa mujibu wa Taasisi ya UPMC, hakuna ushahidi wowote hadi sasa unaothibitishwa kwa tafiti kuwa vinywaji vya kuongeza nguvu (Energy drinks) husababisha kupungua kwa nguvu za kiume.
Hata hivyo, UPMC wanaonya kuwa kuchanganya vinywaji hivi na pombe huwa hatari zaidi kuliko kawaida, nafasi ya mhusika kupatwa na magonjwa ya moyo ndani ya muda mfupi huwa ni kubwa.
Pia, JamiiForums imezungumza na wataalam wa afya ya Binadamu waliothibitisha kuwa hadi sasa hakuna ushahidi wowote wa kitafiti unaothibitisha madai haya.
Hivyo, kwa hatua ya sasa, JamiiForums imebaini kuwa madai haya hayana ukweli unaothibitishwa kwa maelezo sahihi ya kitaalamu.