chimpanzeee
Member
- Feb 28, 2018
- 19
- 10
Muda mfupi baada ya Kamati ya Maadili ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kumfungia kifungo cha maisha Makamu wa Rais wa Shirikisho hilo, Michael Wambura ameibuka na kudai kuwa uamuzi huo ni batili huku akitaja madudu yanayotafuna uongozi wa shirikisho hilo tangu ulipoingia madarakani Agosti mwaka jana.
Wambura alitangazwa kufungiwa kifungo cha maisha na Kamati ya Maadili ya TFF baada ya kumkuta na hatia ya makosa matatu ambayo ni Kupokea/Kuchukuwa fedha za TFF za malipo ambayo hayakuwa halali ikiwa ni kinyume na kifungu cha 73(1) cha kanuni za Maadili za TFF Toleo la 2013 na kughushi barua ya kueleza alipwe malipo ya Kampuni ya Jecks System Limited huku akijua malipo hayo sio halali ikiwa ni kinyume na kifungu cha 73(7) cha Kanuni za Maadili za TFF Toleo la 2013
Kosa lingine ambalo limemtia hatiani Wambura ni kufanya vitendo vinavyoshusha hadhi ya Shirikisho ikiwa ni kinyume na Ibara ya 50(1) ya Katiba ya TFF.
Akizungumza jijini Wambura akiwa sambamba na Wakili wake Emmanuel Muga alisema Kamati ya Maadili imeendesha shauri juu ya tuhuma zake kinyume na taratibu hivyo aina yoyote ya uamuzi ambao umetolewa, ni batili kinyume na Katiba ya Shirikisho hilo.
“Ukilitazama suala hili, ni la kimkakati zaidi na sio la kisheria. Jambo hili lina miaka zaidi ya 14 ambayo mimi Wambura nilikuwa raia wa kawaida tu. Unaposema nimefoji nyaraka, watu wa kwanza wanaotakiwa kuthibitisha hilo ni Jeshi la Polisi lakini katika hali ya kushangaza, kamati ikajipa jukumu hilo.
Jambo la pili, kampuni inayodaiwa kwamba mimi nililipwa fedha na sikuzipeleka, ina wakurugenzi ambao walipaswa kuitwa na kamati ili watoe ushahidi wao juu ya uhalali wa hayo madai lakini hawakuitwa je, utasema vipi hiyo nyaraka imefojiwa wakati wahusika hawajaitwa na kuthibitisha wala Jeshi la Polisi halijahusishwa kwenye uchunguzi?,” alihoji Wambura.
Wambura alisema Kamati ya Maadili iliamua shauri hilo pasipo kufuata taratibu za kimahakama ambazo kikatiba ndizo zinapaswa kutumika na kamati zote za kisheria za TFF.
“Barua ya wito ililetwa nyumbani kwangu Jumanne, saa 4 usiku na walipoleta walimkuta mke wangu ambaye aliwakatalia. Kama kikao kinatakiwa kiendeshwe kwa mfumo wa kimahakama, maana yake panatakiwa kuwepo na mlalamikaji na mlalamikiwa ambao kila upande unatakiwa upeleke vielelzo vyake.
Sasa wao wameamua pasipo kuwepo na mlalamikaji wala mlalamikiwa. Kile ni chombo huru ambacho kilipaswa kisikilize kila upande na sio kujigeuza wao washtaki. Lile suala lilishakwenda kwenye Kamati ya Utendaji hivyo hakukuwa na haja ya kupelekwa tena kwenye Kamati ya Maadili ambayo kwa mujibu wa katiba, Makamu wa Rais hapaswi kuwajibika kwenye kamati ndogo kama hiyo,” alidai Wambura.
Makamu huyo wa Rais aliyefungiwa alisema suala hilo pia linachunguzwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) hivyo kitendo cha Kamati ya Maadili kulishughulikia kwa sasa ni kuingilia Mamlaka ya Takukuru jambo ambalo ni kosa.
Awali Mwanasheria wa Wambura, Emmanuel Muga alitolea ufafanuzi makosa ya kisheria ambayo Kamati ya Maadili imeyafanya katika mchakato mzima uliotumika kumfungia Wambura.
“Kisherai mtu anatakiwa apelekewe barua ya wito ofisini kwake na sio nyumbani na baada ya hapo Kanuni namba 48 ya maadili ya TFF, inataja kwamba muhusika atakuwa na siku tatu za kuitikia wito. Kingine ni kwamba kanuni ya maadili inatamka kwamba shauri likishatajwa, pande zote zinapewa nafasi ya kusikilizwa na kasha kuwasilisha vielelezo.
Nilipojaribu kuhoji kuhusu hayo na kuomba muongozo wa mwenyekiti, Wakili Hamidu Mbwezeleni, aliniambia nisiipotezee muda kamati na ninapaswa nikiri tu kwamba mteja wangu amefanya kosa au hajafanya. Baada ya mimi kuomba taratibu za kisheria zifuatwe, mwenyekiti aliamrisha nitoke nje na kabla ya kutoka nilimuambia kuwa baada ya kumalizika kikao, anapaswa aweke kwamba uamuzi ni wake binafsi au wa kisheria.
Kimsingi kesi ya msingi haijasikilizwa kwani kikatiba, ili kamati ya maadili imjadili Mjumbe wa Kamati ya Utendaji, ni lazima kuwepo na muhtasari kutoka ka kamati ya utendaji. Nilipoomba nionyeshwe muhtasari huo kwamba kamati ya utendaji imeridhia Wambura afikishwe kwenye Kamati ya Maadili, sikupewa na haukuwepo,” alifafanua Wakili Muga.
Katika hatua nyingine, Wambura amedai kwamba kinachofanyika ni mkakati uliopo kumg’oa kwenye nafasi hiyo kutokana nay eye kuonekana kikwazo cha kukwamisha mipango mingi ovu ndani ya shirikisho hilo.
“Tatizo ni nafasi ya Umakamu wa Rais, ajira za TFF pamoja na suala la fedha ambalo mimi kwa nafasi yangu ni Mwenyekiti wa Kamati ya Fedha na Mipango ya Shirikisho. Kwenye ajira za TFF kuna shida sana na mimi nilimuandikia barua Rais kumueleza achukue hatua kuhusu hilo.
Moja ya mambo ninayoonekana kikwazo ni nafasi ya Ukatibu Mkuu ambayo nimekuwa nikisimamia msimamo wangu kwamba ni lazima utaratibu ufuatwe katika kumsaka mtu wa kukaa kwenye nafasi hiyo badala ya kupeleka jina la mtu kwenye kamati ya utendaji pasipo kufuata taratibu husiaka ambazo ni kutangaza kwa umma ili watu watume maombi, kasha waombaji wafanyiwe usaili na baada ya hapo ndipo atakayeshinda apelekwe kwa kamati ya utendaji ili kuthibitihswa.
Lakini kingine naonekana kikwazo kwa watu kutumia fedha kwa namna wanayotaka wao. Ndugu zangu kuna matatizo makubwa katika masuala ya fedha ndani ya TFF, kwa sababu tangu tumeingia madarakani hadi sasa, zaidi ya Shilingi 3 Bilioni imetumika pasipo kufanyiwa jambo la maana.
Pamoja na hayo yapo pia matatizo kama vile ya kutolipwa fedha za Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) pamoja na matumizi mabaya ya fedha za wadhamini na ndio maana mnaona ligi ya vijana na ile ya wanawake vimekuwa vikisuasua,” alimaliza Wambura.
Wambura alisema baada ya kupokea uamuzi wa kamati ya maadili, ataitisha mkutano wa waandishi wa habari ili kuujuza umma wa Watanzania nini ambacho ameamua kukifanya baada ya adhabu hiyo.