Umesema vyema ingawa naona kama kuna watu ama hawakukuelewa ama wanataka kutetea wasichoelewa. Kwa mwanahabari wa Kitanzania kujua kiswahili fasaha na kiingereza cha uhakika ni sharti; si sifa za ziada. Kiswahili ndiyo lugha yetu rasmi ya mawasiliano na lazima tuimiliki kikamilifu. Kiingereza ndiyo lugha tuliyoachiwa na mkoloni wetu na ndio mlango wetu mkuu wa mawasiliano na wenzetu duniani. Ukitaka kuhabarika na matukio na midahalo inayoendelea ulimwenguni bila kukimanya kiingereza ipasavyo utaishiwa kupokea simulizi (za pili) hata zisizo na uhalisia. Kwa mwanahabari unayetutafutia habari za ulimwengu ni shurti uwe na uwezo wa kuzipata katika vyanzo vya awali.
Watanzania tunayo bahati kwamba kiingereza ndiyo lugha inayoongoza kwa mawasiliano duniani; hatuhitaji sana kujua nyingine kama wenzetu wasiokuwa na misingi ya kiingereza kwenye nchi zao. Katika mashirika ya kimataifa, watu waliotawaliwa na Wafaransa, Wareno, Wahispania, Waarabu, n.k. pamoja na kujua lugha zao za nyumbani na za wakoloni wao inabidi wajifunze kiingereza kwa taabu ukubwani ili wakubalike, wakati kwa Watanzania, kiingereza tu chatosha. Ukiongeza lugha nyingine inaitwa "added advantage".
Kinachonitibua sana kwetu sisi Watanzania ni hulka ninayoiona ya wengi kukipenda sana kiingereza huku tukipiga chenga juhudi za kukimanya vizuri kwa visingizio vilivyopitwa na wakati kwamba "sio lugha yetu". Halafu unakuta watu wanaosema hivyo ukianza kuongea nao kiswahili kazi ni kuingiza maneno ya kiingereza na lafudhi za Kiingereza/Kimarekani bila mpangilio kiasi cha hata kuharibu kabisa mawasiliano yenu ya kiswahili. Ukiwabana muongee basi hicho kiingereza ndio taabu kabisa hamuelewani. Ni aina fulani ya "ushamba".
Ndio maana majirani zetu Kenya sasa wanatambulika rasmi kama mabalozi wa kiswahili huko nje kuliko sisi. Tuache mikanganyiko isiyo ya lazima; tuimarishe kiswahili na tujitahidi kukijua kiingereza ili tuweze hata kuwafundisha wengine kiswahili fasaha badala ya kuwaacha Wakenya waendelee kueneza kiswahili chao duni (cha kikabila) ulimwenguni.