Kuanzia Kimara Mwisho, Sinza hadi Mikocheni, kila unapopita leo utakuwa huna bahati nzuri kama usipokutana na vibao vinavyotangaza huduma za kuchua (
massage). Matangazo mengi ni ya kujinadi kwa huduma bora na bei nafuu. Utakuta bei ni 35,000 hadi maeneo mengine kuna za 70,000, 80,000 na kuendelea.
Ukiingia huko Insta ndo balaa. Kwa namna fulani unaweza kushawishika kwenda ‘kunyoosha mgongo’ angalau kwa dakika chache. Utakuta kwenye matangazo umewekewa aina za
massage zinazopatikana katika maeneo hayo. Kuna sijui
four hands massage; hii wanadai unahudumiwa na watu wawili. Kuna sijui
romantic massage ambayo sielewi inakuwaje pia. Kuna
full-body massage,
deep tissue massage na nyingine wanatumia vimawe fulani hivi vyenye
soft surface. Zipo aina lukuki kutegemea na mahitaji ya mtaka huduma.
Kwakweli huduma hizi ni nzuri kwa wenye uhitaji. Wenye matatizo ya maumivu ya viungo na misuli, wenye
Post Traumatic Stress Disorder (PTSD), n.k watakuwa ni mashahidi wa hili. Na kama wanapata nafuu za masaibu yao, wewe usiye na uhitaji ni nani mpaka upinge? Andiko moja lililochapishwa na Chuo Kikuu cha Harvard linaeleza umuhimu wa huduma hii kuwa haifanyi tu misuli kujisikia vizuri,
bali pia inasaidia kupona haraka na kuwa imara zaidi.
Lakini pia, vijana wanaomiliki hizi biashara na wanaofanya kazi katika maeneo hayo pia wanajipatia vipato na maisha yanasogea. Sote tumekuja mjini kujitafuta.
Hata hivyo, pamoja na kwamba nami sina pingamizi dhidi ya huduma hizi, nina mambo kadhaa ambayo ningependa kujua – yaani mchakato mzima wa kupata idhini ya kufungua vituo hivi lakini pia na utaalamu wa wale wanaotoa huduma.
Kwa mfano, kwenye
baadhi ya nchi duniani ni lazima mtu apitie mafunzo maalum ya kufanya huduma ya
massage kisha aidhinishwe na mamlaka kwa kupatiwa leseni ya uhudumu baada ya kufaulu mtihani. Na kwa kawaida programu hizo zinajumuisha mafunzo ya vitendo, mafundisho darasani, na uzoefu ambao ataupata katika kliniki za
massage akiwa mtarajali, yaani
intern.
Moja kati ya vitu muhimu kwa mtoa huduma ya
massage ni kuwa na uelewa wa kina kuhusu anatomia na fiziolojia (
anatomy and physiology) - yaani kuelewa misuli, mifupa, mishipa ya damu, na mfumo wa neva ili kufanya massage kwa usahihi bila kuleta madhara kwa mteja (awe mgonjwa au anayehitaji huduma kwa
relaxation tu).
Kwa mujibu wa
American Institute of Alternative Medicine, wale wanaotoa huduma za massage katika kila jimbo nchini humo wanahitajika kupata idadi fulani ya masaa ya uzoefu wa vitendo ili kuhakikisha kuwa wana ujuzi muhimu wa kutoa huduma bora kwa wateja. Uzoefu huu husaidia wanafunzi kuelewa mahusiano na wateja, mbinu sahihi za kutoa huduma, na itifaki za usafi, masuala ya kimaadili, usiri (
confidentiality) n.k
Kwahiyo, baada ya mtu kupata nyaraka zake za ithibati, basi anaweza kufanya kazi katika kliniki za tiba ya mwili, hospitali, saluni za urembo, katika timu za michezo au wanamichezo binafsi n.k.
Well, nimeeleza tu hayo ili tupanue uelewa kuwa wataalamu hawa wa kuchua wanaweza kufanya kazi maeneo gani.
Nikirudi Bongo, swali langu ni je, hapa kwetu kuna miongozo gani ya kuendesha shughuli hizi?
Nimeuliza hivi kwakuwa katika pitapita zangu, nimejionea baadhi ya hizi bishara za
massage hapa mjini zikitoa matangazo ya kutafuta wasichana wa kufanya
massage, na wakati mwingine husema wanataka wasichana “warembo” tu. Sawa, hata kama urembo ndiyo kigezo pekee bila msingi fulani wa elimu na ufahamu, je waajiri wao wanawapatia mafunzo? Je, mafunzo hayo yanatolewa na nani na huyu “
massage therapist” anathibitishwaje kuwa amewiva na kukidhi vigezo vya kutoa huduma hiyo kwa watu?
Hili ni swali tu kwakuwa vyanzo vinaeleza kuwa
massage zinaweza kuwa na madhara fulani, ingawa inaelezwa kuwa faida ni nyingi zaidi. Mfano, inaelezwa kuwa kuna wakati
massage inaweza kuzidisha majeraha/maumivu yaliyopo na kusababisha matatizo ya maumivu ya muda mrefu zaidi au kuathiri mfumo wa neva. Hii yote inategemea na aina ya tatizo ambalo mtu analo na namna atakavyopatiwa
massage.
Inaelezwa pia kuwa
deep tissue massage, kwa mfano, inaweza kusababisha tatizo la
rhabdomyolysis, hali ambapo tishu za misuli zinavunjika kwa kiasi kikubwa na huenda likasababisha matatizo mengine ya kiafya kama vile
kufeli kwa figo au kifo.
Lakini pia, kuna
kisa ambapo mtu alipata hematoma, yaani mkusanyiko wa damu chini ya ngozi unaosababishwa na kupasuka kwa mishipa ya damu. Hii ilikuwa ni baada ya kukandamizwa kwa nguvu kwenye misuli kwa lengo la kupunguza maumivu ya mgongo. Jambo hili lilisababisha mgonjwa kulazwa hospitalini na kufanyiwa upasuaji ili kupunguza uvimbe mkubwa na ganzi kwenye mguu.
Katika vituo vinavyofanya kazi
professionally,
massage therapists huomba mteja kujaza fomu kabla ya kufanyiwa
massage. Katika fomu hiyo kunakuwa na maswali kuhusu ‘
pressure’ anayopendelea mteja na matatizo yoyote ya kiafya aliyo nayo ili kujua ni aina gani ya
massage akipatiwa haitaleta madhara. Hii ni kwasababu kuna kitu kinaitwa
massage contraindication, yaani hali ambayo mtu akifanyiwa
massage inaweza kuleta balaa kutokana na matatizo aliyo nayo. Katika hali hii madaktari wanaweza kuhitajika kushauri kuona namna na aina ambayo mtu huyo anaweza kupatiwa
massage ambayo ni
customized ili kuepuka madhara.
Kwahivyo, hitimisho langu ni kuwa hii kazi kwa namna fulani inahitaji ujuzi na weledi kwani linahusisha afya za watu. Lakini bado nabaki na swali kuwa: Kibongobongo tupo salama kiasi gani tunapopata huduma hizi? Je, na wateja wanaenda kupata huduma hizi wakijua zinaweza kuathiri afya zikifanyika bila utaalamu wowote?
Mimi yangu ni maswali tu Iila nikipata uelewa kutoka
Wizara ya Afya Tanzania nitapendezwa sana.
Yangu ni hayo. Ahsante.