Mamlaka ya Mji Mkongwe Zanzibar imepiga marufuku upigaji wa makachu katika eneo la bustani ya Forodhani baada ya kudaiwa kufanyika kwa matendo ambayo ni ukiukwaji wa maadili ya Zanzibar na kufanyika kwa baadhi ya uharibu katika eneo hilo
Taarifa iliyotolewa na Mamlaka hiyo imesema uamuzi huo umefikiwa baada ya kuona kuna ukiukwaji wa sheria, kanuni na miongozo yaliyojitokeza kwa vijana wa makachu katika eneo hilo ambapo inahusisha pia upigaji makachu kwa kutumia mavazi yanayokwenda kinyume na Utamaduni, Uharibifu wa mifereji na miundombinu mengine ikiwa ni pamoja na kutumia madebe taka kufanyia vichekesho (comedy).
Aidha mamlaka hiyo imesema imesimamisha shughuli hizo hadi kukamilika na kuandaa utaratibu wa kuimarisha utendaji kazi hizo kwani Serikali inatambua mchango mkubwa unaofanywa na vijana hao katika kuutangaza Utalii wa Zanzibar Kimataifa.
Vilevile Mamlaka hiyo inaendelea kufanya uchunguzi wa matukio hayo na kuwachukulia hatua wale wote waliobainika kutenda makosa hayo ikiwemo uharibifu wa miundombinu.
Hivi karibuni ilisambaa video ikionesha baadhi ya Raia ambao ni wa Kigeni kupiga makachu katika eneo hilo wakiwa na nguo ambazo haziendani na maadili ya Zanzibar.