Pre GE2025CCM Iringa yakanusha kauli iliyotolewa na Mwenyekiti wilaya ya Iringa juu ya kupewa kipaumbele wabunge na madiwani walipo madarakani kuelekea uchaguzi
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Iringa kupitia kikao chake cha dharura cha Kamati ya Siasa ya mkoani humo imekanusha vikali taarifa iliyotolewa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya ya Iringa, Steven Mhapa inayodai majina ya madiwani na wabunge waliopo madarakani sasa yatakuwa miongoni mwa majina matatu yatakayorudishwa na chama hicho kwenye mchakato wa mchujo wa kusaka majina ya watakaoiwakilisha CCM kwenye Uchaguzi Mkuu mwezi Oktoba mwaka huu.
Kauli hiyo ambayo ilichapishwa na kutangazwa na baadhi ya vyombo vya habari hususani mitandao ya kijamii na kusambaa kwa kiasi kikubwa imesababisha mkanganyiko na taharuki miongoni mwa wana CCM na wananchi kwa ujumla ambao wamekuwa wakifuatilia kwa karibu siasa mkoani Iringa.
Akitangaza msimamo wa CCM mkoa wa Iringa kuhusiana na kadhia hiyo, Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Iringa, Daudi Yassin amesema Kamati ya Siasa ya CCM mkoa wa Iringa imepokea taarifa hiyo kwa masikitiko makubwa na kuongeza kuwa kauli hiyo sio msimamo wa CCM mkoa wa Iringa na ni kauli yake mwenyewe binafsi.