Excellent ! nasubiri umalizie!
Kwa mujibu wa Mtandao wa Vyombo vya Usalama vya Marekani,Mei 6, 2002 Utawala wa Rais George Bush wa Marekani ulimtaarifu rasmi Katibu Mkuu wa umoja wa mataaifa juu ya Uamuzi wa Taifa la Marekani kujitoa katika mkataba huo. Kulingana na matamshi ya aliyekuwa Waziri wa Ulinzi wa Marekani wakati huo Donald Rumsfeld alisema kulikua na uwezekano wa baadhi ya maofisa wa Marekani wakiwemo maofisa wa jeshi la nchi hiyo kushtakiwa na mahakama hiyo na pia Marekani haikubaliani na baadhi ya vipengele vinavyoinyima Marekani kutekeleza wajibu wake hasa katika kipindi ambacho taifa hilo lilikuwa linakabiliana na vita dhidi ya ugaidi.
Marekani walidhamiria kulinda maslahi yao na mwanya wa kuendelea kupelea majeshi yao popote duniani pale wanapoona maslahi yao yapo hatarini. Hapa viongozi wa Afrika hawakushtuka na pia tangu muda huo walibweteka na hawakufikiria namna bora na mbadala wa kujiandaa kitaasisi ili kuwa na chombo chao cha kimahakama chenye hadhi, imani na uwezo wa kushughulikia masuala kama ICC ili kuepuka matatizo kama haya wanayoyajadili leo hii. Kwao waliona busara na ufahari kuwaomba CHINA kuwajengea jengo la kifahari la makao makuu ya Umoja huo badala ya kufikiria ujenzi wa mahakama na taasisi zenye hadhi na uwezo wa kushughulikia matatizo yetu
Kuna kila dalili kuwa Mabeberu wanaitumia ICC kwa maslahi yao. Lakini pia kupitia udhaifu wa viongozi wa Afrika kutoheshimu mifumo ya kutoa haki kama mfumo wa kimahakama, mataifa haya ya kibeberu yanapata mwanya wa kujenga hoja kuwa Afrika haina mfumo thabiti wa kushughulikia kesi bila kulindana(Impunity).
Kwa mfano,Viongozi wa Kenya walitoa taswira hii pale walipoamua kupeleka kesi ya Uhuru na Ruto wenyewe huko ICC. Kipindi hicho Uhuru na Ruto hawakuwa Marais. Viongozi wa Umoja wa Afrika walikaa kimya kwasababu hawa hawakuwa marais wenzao. Nilikerwa sana lakini wao hawakukerwa. Fedheha ya Afrika. Leo wanasema mahakama ya Afrika inalenga Viongozi wa Afrika? Hoja hii itaonekana nyepesi kwa kuzingatia mazingira niliyoyaainisha.
Inatambulika kuwa Haki za Binadamu ni kanuni ya msingi kwenye Mkataba wa umoja wa Africa (AU Chatter) na imepewa uzito katika mkataba huo maarufu kama ‘Banjul Charter . Kwa hiyo jitihada zozote za kutaka kujiondoa au hata hili la kujadili kama Marais wa Afrika waliopo madarakani wasishtakiwe mbele ya mahakama ya kimataifa ya ICC kupitia Umoja wa Afrika (AU) itatuma ujumbe mzito na mbaya juu ya dhamira ya dhati ya viongozi na umoja huo katika kulinda haki za binadamu na kukataa utamaduni wa kulindana (culture of impunity) ambazo ni tunu na nguzo kuu katika madhumuni ya Uanzishwaji na uwepo wa Umoja huu.
Hii ni ajenda iliyojaa hila na ubinafsi kwa viongozi dhidi ya raia wa bara hili. Naungana na msimamo wa mshindi wa tuzo ya amani ya Nobel, Askofu Desmund Tutu wa Afrika Kusini kuwa Nigeria na Afrika Kusini zikiwa kama mataifa yenye nguvu na ushawishi ndani ya umoja huu ziongoze katika mjadala kuzuia azimio hilo lenye sura mbaya na aibu kwa bara hili. Wito ambao pia umetolewa naye Katibu Mkuu wa zamani wa Umoja wa Mataifa, Dk. Koffi Annan.
Kama viongozi wa Afrika wanaona uchungu kweli basi waimarishe taasisi zetu na hasa mfumo wa Mahakama ambazo mara nyingi viongozi wa Afrika wamekuwa wakizitumia kuwaadhibu wapinzani wao. Mahakama hizi haziheshimiwi na hazipo huru kiasi cha kubeba matumaini na imani kwamba zitatenda haki. Hii ndiyo sababu kuu kwamba hata baada ya uchaguzi na inapotokea utata wa udanganyifu wa kura wapinzani wanaamua kuingia barabarani kudai haki kuliko kwenda mbele ya mahakama hizi ambazo zinaoneka kutumika kama mkono mwingine wa watawala kunyonga haki
Waafrika ni lazima tusimame imara na kujenga misingi ya kitaasisi. Hakuna wa kulitetea bara la Afrika zaidi ya Waafrika wenyewe na ili tupate mafanikio ni lazima tuachane na kasumba chafu ya kutegemea suluhisho la matatizo yetu kutoka nje ya bara la Afrika. Hatuwezi kuingiza suluhisho la matatizo yetu kutoka nje kama tunavyoagiza bidhaa kutoka nje kwa ajili ya kutatua matatizo tuliyojitengenezea wenyewe. Tuache kutegemea Mataifa makubwa ya kibeberu maana maumivu ya Afrika ni nafuu ya mataifa hayo ya Kibeberu.
ICC ina changamoto kama lilivyo Baraza la Usalama la umoja wa Mataifa .Baraza hili la kudumu nalo lina changamoto ambazo tumekua tukizipigia kelele hasa juu ya upanuzi wa wigo wa kidemokrasia na utendaji wake unaozingatia maslahi ya wachache na hivyo kubeba ajenda za mataifa yenye nguvu kuaamua juu ya masuala mazito ya dunia. Amani ya dunia imewekwa rehani kwa mataifa haya matano tu.
Kwa hiyo ICC inatakiwa pia iangalie uhalifu uliofanyika Iraq, Afghanistan, Palestina na Lebanon. Ukweli ni kuwa ‘Silaha za Maangamizi' za Iraq ya Saddam Hussein hadi leo hii hazijawahi kuonekana kama ilivyonenwa na Wavamizi wa Nchi hiyo, lakini Bush na Blair walioendesha vita yenye uharibifu mkubwa kwa madai ya kumnyang'anya Saddam Hussein silaha za maangamizi wapo huru mtaani tu.
Ukweli ni kuwa tunaishi katika mazingira yaliyojaa laana ya uhalifu dhidi ya binadamu uliofanyika pia sehemu nyingine duniani kama vile Iraq, Lebanon, Libya na Palestina uliofanywa na unaondelea kufanywa na Israel, Marekani, Uingereza, Ufaransa na Washirika wao wa Umoja wa kujihami wa nchi za Magharibi na Marekani (NATO) ambao haukuvuta hisia na dhamira ya kiutendaji ya ICC pamoja na kuwa uhalifu huo pengine ni mkubwa na wa kutisha zaidi kuliko kesi zilizofanyiwa na zinazoendelea kufanyiwa uchunguzi za Afrika Kwa hiyo Viongozi wa Afrika kutumia sababu hii ya madai ya kuachwa kwa uhalifu mwengine duniani iwe ni kwa lengo la kutaka ‘hatua zichukuliwe kwa kila upande' na si kwa lengo la kupinga hatua kuchukuliwa kwao kwa udhalimu wao kwa raia wao kama alivyokuwa akidai Waziri Mkuu wa Ethiopia, Hailemariam Desalegn wakati wa Kikao cha juzi. Hailemariam amekwenda mbali zaidi kwa kuongeza sababu nyingine ya ubaguzi wa rangi (Racism) kuwa ni miongoni mwa vigezo ambavyo ICC inatumia ili kuwashughulikia zaidi Viongozi wa Kiafrika huku wakisahau kuwa Mwendesha mashtaka Mkuu wa Mahakama hiyo, Fatou Bensouda ni Mwafrika Mwenzao kutoka Gambia ikiwa pamoja na uwepo wa baadhi ya Majaji wa Mahakama hiyo ambao ni Waafrika.
Kama nilivyosema hapo awali ni jambo la kawaida kwa Viongozi wa Afrika kutumia mfumo wa mahakama zetu dhaifu kuendekeza utawala dhalimu, jambo linalopelekea kuoza zaidi kwa mfumo mzima wa mahakama. Kwa vyovyote vile hadi ninapoandika makala hii, wanaharakati na hata vyama vya upinzani haviwezi kupeleka visa vya uchaguzi au madai yao ya msingi kwenye mahakama hizi zinazolinda watawala na badala yake siku zote mahakama kuu kwao ni zile "Mahakama za Umma" ambazo ni tishio kwa watawala.
Kwa hiyo linapotokea jambo kama hili la "Mahakama za Umma" mara moja watawala hawasiti kutumia majeshi na hata silaha za kivita kuzima maandamano na mikutano itakayotishia utawala wao dhalimu na hivyo kupelekea mauaji ya kutisha kwa raia wasiokuwa na hatia wanaodai haki zao za msingi. Hapa ndipo mahakama ya Kimataifa ya ICC inapowakamata viongozi dhalimu wa Kiafrika na kuwashikisha adabu bila kujali kama Bush na Tony Blair wamewajibishwa kwa makosa yao ama la.
*
Mwandishi ni Mhitimu wa Shahada ya Uzamili katika Sayansi ya Siasa na Mahusiano ya Kimataifa,na pia shahada ya Uzamili katika Uchumi. unaweza kuwasiliana naye kupitia barua pepe; saananeben@gmail.com au +255768078523
NB:Makala hii imechapishwa Katika Gazeti la SURA YA MTANZANIA,Pia Baadhi ya Vyombo vya Habari vya Kenya Vimeomba kuichapisha Makala hii