Hekaya za Abuuwasi na hadithi zingine

Hekaya za Abuuwasi na hadithi zingine

Ok nilijua ni Whatsapp group kumbe kuungwa kwenye App.
Ni app.

Screenshot_20230412-165554.png
 
JOGOO NA SUNGURA​



Hapo kale paliondokea sungura akafanya urafiki mkubwa mno na jogoo, ikawa jogoo hali kitu asipomuona sungura kwanza. Wala Sungura hali asipomuona Jogoo kwanza. Wakakaa katika hali hii kwa muda wa siku nyingi sana, pasipo hitilafu iwayo yoyote.
Hata siku moja Jogoo akawaza moyoni mwake, "Ah! Hivi huyu rafiki yangu anapokuja kwangu na tukizungumza maneno yetu ya siri huyachukua na kwenda kumwambia mkewe nini? Ela safari hii nitamjaribu kumpa neno moja la upuzi tu, nione mwisho wake."
Desturi moja waliyoafikiana wao kwa wao tangu awali ya urafiki wao, ndiyo, mtu akija kwa mwenziwe kutembea, hana ruhusa kulala ndani ya nyumba ya mwenziwe, ila ni kulala upenuni tu, hata ikiwa ni siku ngapi, bora malazi mazuri ya upenuni wala si ndani ya nyumba. Hayo ndio maafikiano yao walioyokuwa nao. Walidumu daima. Wala hapana mmoja aliyenung’unika, maana kwa kila mmoja alitengeneza kipenu kizuri akatia kitanda na matandiko mazuri. Ikawa kwa kila mmoja aendapo kwa mwenziwe huja kulala mahali pake, upenuni.
Hata siku hiyo, mzee Sungura alipokuja kwa Jogoo kwa matembezi na malazi pia, Jogoo katika yale mazungumzo yao, akamwambia Sungura, "Je! rafiki yangu hizi siku unazokuja hapa na ukalala, je! usiku hunisikia nikisema nini au huweweseka na kubwetabweta kwa namna gani?"
Sungura akamjibu, "La, hata siku moja sijakusikia ukisema wala ukibwetabweta neno, ila karibu na asubuhi tu, pale unapotuamsha sisi sote. Nakusikia ukisema, 'Kucha kucheree. Mamiye Mwali Kamie ndege reeee.' Hivi tunakusikia ukihimiza. Watu waende kazini kwao."
Lakini zaidi sifahamu. Ndipo Jogoo akamwambia Sungura, "rafiki yangu, basi tangu leo nakupa siri ya mimi na wewe tu, na siri hii shika moyoni mwako tu wala usimwarnbie mtu, hata akiwa ni mkeo wa nyumbani haifai kumwambia. Wasikia rafiki yangu? Halahala shika hayo yangu wala usidanganyike na neno liwalo lote."
Sungura akajibu, "Vema, rafiki yangu, mimi sithubutu kutoa neno lako nje."Wakakaa
Hata siku moja Jogoo akamwita mkewe ampendaye akamwambia. "Mke wangu, siku moja rafiki yangu Sungura atakuja kula na kulala hapa. Basi mtandikie pale pale upenuni pake pa siku zote, na tena, sikia sana mke wangu mimi usiku. Nitakuamsha nitakuambia, mke wangu. Huachi wee. Mtu wajua kazi yako ya siku zote, ya kukata kichwa changu ndipo nipate usingizi, leo umeniacha kulala na kichwa changu. Nitapataje usingizi?"
Ndipo wewe unijibu, 'Ah! Mume wangu, nisamehe sana usingizi ulinishika upesi nikalala pasipo kukata kichwa chako, haya basi lete kisu nikukate niweke kule, ili upate usingizi.'
Ukisha, useme tena, 'Haya lala sasa nimekwisha kata kichwa chako usinisumbue tena.' Na vile vile kadhalika, asubuhi mimi nitaamka nitatikisa mbawa zangu. Nitakuita, Mke wangu, lete kichwa changu nataka kutoka nje sasa, wewe nawe ujipurukushe.
'Ah! Bwana wee saa, udhia gani huu, watu wote hulala na vichwa vyao wewe ni kunisumbua tu kukata na kukiunga siku zote, mambo gani haya?'''
Maarifa haya yote jogoo akamwelekeza mkewe tangu siku ya kwanza hata siku alipokuja rafiki yake Sungura.
Siku zikipita Sungura akaja kwa Jogoo, wakaamkiana kwa namna zote, wakakaa, wakazungumza sana. Hata katika mazungumzo yao, Jogoo akamwambia Sungura, "je! juzi nilikuambiaje rafiki yangu?"
Sungura akajibu, "Uliniambia ya kuwa siri yangu usimwambie mtu au sivyo?" Jogoo akamjibu, "Ndivyo, ila leo nakupa neno moja tena, ndiyo, La upenuni na halisimuliwi nje; Wakasikia rafiki yangu?"
Sungura akajibu, "nasikia sana." Wakazungumza sana, hata wakati wa kulala, jogoo akaingia ndani na mkewe na sungura akaenda upenuni pake kwenda kulala. Hata kupita muda kidogo tu sungura ndo kwanza usingizi ukaanza kumshika, mara jogoo akaanza kuita.
"Mke wangu! Huachi wee, mtu Wajua Kazi yako ya siku zote kazi yako ya kukata kichwa changu ndipo nipate usingizi leo umeniacha kulala na kichwa changu, nitaupataje usingizi?"
Mara hiyo hiyo mke wa jogoo akajibu, "Ah! Mume wangu, nisamehe bwana, usingizi ulinishika upesi, halala pasipo° kukata kwanza kichwa chako, haya basi, lete kisu nikikate, nikiweke kule upate kulala."
Mke wa Jogoo akaenda kwa Jogoo akakitwaa kichwa cha mumewe akakitia ndani ya bawa, akasema. "Haya lala, nimekwisha fanya kazi yangu."
Wakati huu Sungura amekwisha amka asikiliza tu maneno ya Jogoo na mkewe jinsi wapeanavyo mashauri. Wakalala hata karibu na asubuhi Jogoo akaita tena, "Mke wangu! Mke wangu! Ah! Mambo gani hayo?
Huku atikisa mbawa zake, Ela nipe kichwa changu nipate amsha watu watoke nje."
Mara mkewe yule Jogoo akafanya kama alivyoambiwa na mumewe, akaenda huko na huko, mara huyu, "haya bwana, lete shingo niweke kichwa chako, udhia gani huu, watu wote hulala na vichwa vyao, wewe ni kunisumbua tu."
Mara Jogoo akaanza kuwika.
"Kucha kuchereee. Mamiye Mwali Kaimie ndege-reee." Mara mbili tatu, hata asubuhi kweupee. Watu watoka na kwenda kazini kwao. Yote haya Sungura asikiliza tu na kuona kwa macho jinsi watu watokavyo na kwenda kazini kwao.
Asubuhi kulipokucha, Sungura na Jogoo wakanawa, wakala chakula chao wakaisha. Wakakaa vile vile hata usiku, mambo ya Jogoo yakawa vile vile kama juzi na jana na Sungura ni kusikiliza tu pale upenuni alipolala.
Hata siku za kukaa Sungura kwa rafiki yake Jogoo zikaisha. Sungura akaaga kurudi kwake Jogoo akamuaga vizuri na kumpa zawadi nyingi, zake na za bibi yake pia, akaenda zake.
Sungura njia nzima ni kuwaza tu mambo na maneno yaliyotendeka kwa jogoo mara akawaza moyoni mwake, "Ah! Jogoo ana maarifa gani ya kunishinda? Mimi sungura nina maarifa mangapi yote kwa ajili ya ujanja wangu."
Sungura kufika kwake akamwita mkewe kuzungumza yote aliyoyasikia na kuyaona nyumbani kwa jogoo, hata akamwambia, "kesho kutwa rafiki yangu jogoo anakuja basi nawe nitendee kama hayo ambayo jogoo anatendewa na mke wake.
Lakini mke wa sungura akamjibu, "vema bwana lakini sijawahi kuona mtu akakatwa kichwa akaishi."
Sungura akamjibu mkewe, "mbona rafiki yangu jogoo yupo hata leo! Na kesho kutwa yuaja utamwona akija mzima na kichwa chake."
Wakakaa hata siku ya tatu Jogoo huyu akawasili, Sungura akashughulika sana kumkaribisha rafiki yake. Wakakaa wakamkiana kwa njema zote na kuulizana habari zote.Wakati wa chakula wakafurahi sana hata jionii Jogoo akatandikiwa vile vile upenuni na Sungura na mkewe wakaingia ndani kulala. Jogoo halali, asikiliza tu kuona kama Sungura hakumwambia mkewe siri yao.
Mara akasikia, "Mke wangu! Mke wangu! Mbona hivi? Mtu kazi yako uijuayo sikuzote, leo waniacha kulala na kichwa changu, ela usingizi nitaupataje? Haya upesi, fanya kazi yako kama sikuzote, lete kisu upesi unikate kichwa changu ukiweke. Jogoo aliposikia maneno yale akashtuka, lakini asiseme neno akakaa kimya tu akisikiliza mwisho wa maneno yao.
Mara mke wa Sungura akaenda akatwaa kisu kikubwa na Kikali nakumkata mumewe shingo yote akaiondoa. Sungura akaruka huko na huko anapapatika mkewe akashangaa tu, hajui la kufanya, aona ni ajabu tu hii ya mtu kukatwa kichwa akaishi.
Mzee sungura alipoisha kupapatika akafa kabisa foo pale pale, mke wa Sungura akaenda akalala. Hata asubuhi mke wa sungura akaamka, akaenda kukichukua kile kichwa cha mume wake akaenda kukiumanisha penye shingo, akaanza kumtikisa mume wangu, "mume wangu amka ati, kumekucha rafiki yako anakungoja," kimya hapana sauti wala kuamka, aona nzi tu wanaanza kukusanyika. Akamshukuru Mungu, "Lillahi hamdu. Mume wangu amekwisha kufa hapana zaidi tena."
Akatwaa nguo akamfunika. Muda ule uIe mke wa sungura akafungua mlango amkuta shemeji yake jogoo kaisha amka zamani anamngoja yeye tu.
Jogoo akamwuliza mke wa sungura. "Je! bwana yuko wapi? mbona hata sasa hajaamka anaumwa nini? au kaenda wapi?"
Mke wa sungura akamjibu Jogoo, "Bwana kaisha kufa, ela njoo uone huyu hapa, sijui kama kalala, lakini mimi naona kama amekufa." Jogoo akaenda kufunua nguo na kumwangalia mzee Sungura. Amekwisha kufa.
Jogoo akamwuliza mke wa Sungura, "Umemfanyaje mumeo?"
Mke wa Sungura akamwambia Jogoo, akasema. "Tangu siku alipokuja kwako na kurudi hapa, akanieleza yakuwa rafiki yangu Jogoo halali na kichwa, mkewe humkata kichwa usiku na hata asubuhi hukiunga mahali pake, na jogoo, (wewe ati), huwa mzima vile vile! Basi tangu arejee kutoka kwako, bwana wangu akanifundisha sana maneno na matendo aliyoyaona na kuyasikia kwako, ukitendwa na mwenzangu. Na sasa nami nimemtenda vile vile kama alivyoniamuru, na kumbe mume wangu kafa. Jogoo akamjibu mke wa Sungura, akamwambia. "Nasikitika sana sana kwa kuwa rafiki yangu hakutambua maana ya maneno yangu."
"Maana, mimi nalimwambia
Wakati nilalapo huimwambia mke wangu, Haya upesi nikate kichwa nilale. Maana yake ni kusema, Je! mke wangu, hapana hata ukoko unipakulie nipate kulala? ndipo mke wangu huvumbulia kidogo ukoko aliouficha na kunipa. Na kadhalika kwa asubuhi, humwambia, Mke wangu nipe kichwa changu maana yake, haya fanya upesi chakula, Kidogo angalau nipate nguvu za kutoka nje ndipo mke wangu hufanya chakula kwa upesi na kunipa nikala, ndipo hutoka nje na kuwaamsha watu."
Lakini sasa rafiki yangu kajidhulumu nafsi yake, ndipo jogoo akawaita watu kwao kina Sungura wakamzika. Tangu siku hiyo urafiki wa jogoo na sungura ukakatika kwa kutokusikilizana.
 
KISA CHA PAKA KUPENDA MEKONI​

Zamani za wahenga, paliondokea paka akapeleleza sana jinsi viumbe walivyoumbwa na nguvu na kuwa kila mmoja humpita mwenziwe kwa nguvu. Basi katika kupeleleza kwake akaona na akadhani ya kuwa hapana kiumbe mwenye nguvu kupita simba.
Akashika njia akaenda kwa simba akafanya urafiki mkubwa, ukasitawi kwa siku nyingi, Wakapatana sana. Hata siku moja simba akatoka kwenda kutembea mahali pa mbali, yeye na rafiki yake paka, kule matembezini wakakutana na tembo. Tembo waliipomwona simba wakamfukuza sana, hata wakamkamata, wakamtwaa na kumpachika kwenye panda ya mtini sawia.
Paka alipoona vile akashangaa sana, akasema moyoni mwake, "Ah! Mimi huwaza ya kuwa simba ni bora kumbe kuna aliyemzidi!" Akatoka kwenda kumtafuta tembo, akamwona, akamwambia nataka urafiki, Tembo asikatae, kamwambia vema. Wakakaa, siku zikapita nyingi katika hali ya kupendana na kusikilizana.
Lakini ikatukia siku walipokuwa wakitembea tembea msituni mwao, mara wakamwona mtu mwinda nyama, mara yule mwindaji akaelekeza bunduki yake kwa tembo, akampiga tembo risasi moja tu akaanguka chini akafa. Paka akazidi kushangaa, "Ah! Huyu ndiye mwenye nguvu kupita wote, yaani kaniulia rafiki yangu mpenzi! Paka akafanya majonzi sana sana. Hata mwinda alipoondoka kwenda zake nyumbani, paka akamkimbilia akamwambia, "Ee bwana nataka kukufuata uendako."
Mwinda akiona ni Paka tu, akamjibu, "Vema, haya, twende zetu kwangu. Walipofika nyumbani, mara paka akaona mke wa mwindaji akija mbio akipokea silaha zote za mwindaji, tangu bunduki hata risasi na baruti pia. Paka kwa ujinga wake akazidi kushangaa, akawaza katika moyo wake. "Hakika, huyu ndiye mwenye nguvu kuliko wote, maana kaweza kunyang’anya silaha zote kutoka mkononi mwa mwindaji. Na mwindaji hakutoa neno lolote ila ni kukaa kitako na kupumzika tu. Huyu ndiye wa kumfuata mimi."
Basi papo hapo Paka akamfuata mwanamke ndani, hata jikoni, akakaa karibu na mwanamke jikoni wakati akiandaa chakula cha mumewe. Paka akawa mzoefu sana kukaa jikoni, hata ikambidi yule mwanamke kumtuma Paka kukamata panya na kumlindia vyombo vyake visiharibiwe na Panya. Tangu siku hiyo ndiyo maana ukaona Paka hatoki jikoni hata leo.
 
KISA CHA KUKU NA MWEWE​



Hapo zamani za kale Mwewe alikuwa na mtoto mmoja tu wa pekee, na jina la mtoto huyo alikuwa akiitwa Rahisi. Basi ikatukia yule mtoto wa pekee wa Mwewe akawa mgonjwa sana, hata ikajulikana ya kuwa Rahisi bin Mwewe yu katika hatari ya kufa. Baba wa Rahisi akawaita watu kadha wa kadha awajuao kuwa hawa ni waganga na wenye akiliili kuja kwake kumtibu na wamponye mwanawe. Katika wale walioitwa pasitokee hata mtu mmoja aliyeweza kuuponya ugonjwa wa Rahisi bin Mwewe. Mama Mwewe na Baba Mwewe wakaona majonzi makuu mno hata hawajui la kutenda wameduwaa tu.
Hata siku kupita, akaja mmoja. Akamwambia Mwewe kuwa yeye ana mganga mmoja, ajuaye sana dawa na awezaye kuuponya ugonjwa wa Rahisi maana mganga huyo hutibu magonjwa yaliyo makubwa kupita huo wa mtoto wa Mwewe. Lakini kabla ya kwenda kumwita huyo mganga, sharti nipe fungu kwanza ndipo niweze kwenda kumwita.
Mwewe akamjibu yule mtu, "Vema mimi tayari kutoa fungu lako kukupa, lakini mtoto wangu asipopona? ni vipi?"
Yule mtu akamwambia Mwewe, "ikiwa huyo mganga kaja, na kakupa dawa yake, na mtoto wako Rahisi bin Mwewe kainywa, naye asipone fahamu, ya kuwa nitakurudishia mali yako yote uliyotoa kunipa, huu wahadi nakupa."
Mwewe akaona furaha sana kusikia maneno hayo, akamjibu, "vyema haya, fungu lako kiasi gani wataka?"
"Reale hamsini, bwana." Akajibu yule mtu.
Mwewe akamwamuru mkewe kutoa reale hamsini za Sham. Akampa yule mtu, akamwambia, "Haya tafadhali nenda upesi sana sana maana mtoto wangu yu katika hatari ya kifo."
Yule mtu akatoka mbio, akaenda hata kwa Buibui, akabisha, "Hodi! hodi!"
Akajibiwa, "Karibu! karibu."
Yule mtu akamwambia Buibui, "Ee bwana, nimejua kuwa wewe ni mganga sana, na huko nje mtoto wa bwana Mwewe ni mgonjwa sana sana, basi tafadhali fanya shime, uende upesi ukamponye, maana utapata fungu kubwa sana la mali, kwa kuwa waganga wengi wameshindwa kuuponya ugonjwa wa Rahisi bin Mwewe."
Buibui akamjibu yule mtu, "Vema, mimi ni tayari kwenda, lakini itakulazimu wewe unichukue mimi, kwa maana, wajua sana ya kuwa mzee kuku akiniona tu njiani, atanidonoa hata nife."
Yule mtu akamuuliza Buibui, "Wewe na kuku mna ugomvi gani hata akuue bure bila kisa?"
Buibui akamjibu binadamu, "Hukusikia jana mbiu ya mgambo aliyotangaza mzee Kuku, ya kuwa Kuku akiona mdudu awaye yote machoni pake, na awe chakula kufa afe tu pasipo huruma, basi je! Mimi mdudu mdogo tu machoni pa kuku?"
Lakini yule mtu hakumsadiki, buibui akadhani labda ni uvivu Wake tu, akazidi kumshurutisha ili aende peke yake na mikoba yake tu buibui akaona imembidi kwenda, hana la kutenda.
Akashika njia safarini na mkoba wake wa dawa kwapani. Hata kufika nusu ya njia wala si mbali tena kufika kwa Mwewe, akafika kwa kuku akajiepusha upande wa nyasini ili kujificha lakini kuku akiangalia chini aona nyayo za buibui zaendelea nyasini, akazifuuata huko huko. Akagundua kajificha na mkoba wake nyasini, mara akamkamata na kumpiga mdomo mmoja tu na kumwua sawia.
Akawaita watoto wake akawatupia, watoto walipoona ni nyama wakafurahi na kunyang'anyana kila mmoja ili apate kidogo kidogo hata wakamwisha pasi hata unyayo wake kuonekana. Wakautwaa mkoba wa dawa wakauchanachana. Wakazivunja chupa na kuzimwaga dawa huko na huko wakaenda zao.
Mwewe alikuwa katika hali ya kungoja siku ile waliyoagana na binadamu akakaa hata adhuhuri, aona saa zapita na mtoto wake tena yu katika kutapia roho.
Mwewe akaona binadarnu amemdhihaki na mara akachukua gongo lake akashika njia nakumfuatia binadamu, kumwuliza habari. Alipofika njiani, wala si mbali na kwake mara aona vigae chekwaa vya chupa za dawa zilizovunjika na vitambaa vimepasuliwa na kutupwa huko na huko. Akizidi kuangalia sana akaona barua, akaiokota, akaipasua, akaisoma, akaona imeandikwa hivi;
"Binadamu kaja niita, asema, Rahisi bin Mwewe mgonjwa sana, upesi ukamwahi. Basi nia yangu na lazima yangu, ilikuwa kwenda nyumbani kwa Mwewe."
Yule Mwewe alipokwisha soma ile barua, na kutazama mgaragazo uliotokea pale njiani hakuwa na neno ila kurejea nyumbani kwake kumwuguza mtoto wake. Hazikupata siku mbli tena mtoto wa Mwewe akafa, akapumzika.
Waiipoisha ondoa matanga Mwewe akawaza sasa ndio wakati wa kulipiza kisasi cha mtoto wangu Rahisi bin Mwewe kati ya mimi na Kuku. Akapiga mbiu ya mgambo kwa binadamu na kwa wote wenye miguu minne, ya kuwa, Kwa kila amwonaye Kuku, au mtoto wa Kuku, awe chakula kwake, amwue tu, asiwe na huruma. Na yeye Mwewe akajiapia kiapo kusema, nitamlilia mwana wangu Rahisi mpaka kufa.
Basi tangu siku hiyo ukawa uhasama mkubwa mno kati ya Kuku na Mwewe, na ndiyo manaa ukaona hata leo kuku hana msamaha kwa mwanadamu wala kwa Mwewe, na ndiyo ukamsikia Mwewe alia huko juu "Rahisi, Rahisii." Yaani awakumbusha sababu ya ugomvi wao, ya kuwa kwa kumzuia Buibui kuja mponya Rahisi bin Mwewe ndiyo maana vita hiyo ikawapo wala haitakwisha.
Na tena ndiyo rnaana ukamsikia Kuku akishikwa na mwanadamu alia, "Siye, siye Si mimi, Si mimi." Yaani ajaribu kukataa kuwa yeye hakuwapo katika vita hiyo. Lakini Mwewe amekataa kupambanua, hukamata na kuwala tu hata leo.
 
KISA CHA MAJUHA WATATU(MAANA YA MAJUHA NI WATU UWAPUMBAVU)​



Hapo zamani paliondokea mtu, akaenda kutembea. Akafika njiani akawakuta watu watatu wamekaa kitako, yule mtu akawaamkia, "Salaam aleikum! Majuha." Wakaitikia, "Aleikum salaam." Yule mtu akapita akaenda zake.
Wale Majuha huku nyuma wakabishana wao kwa wao, mmoja akasema, Salamu hizi ni zangu mimi, wa pili akasema juha ni mimi, wa tatu akasema vile vile. Basi wakawa katika hali ya kubishana mmoja akasema, "sisi hatuna haja ya kubishana kutwa maana yule mtu bado kufika mbali, twende tukamwulize, katika sisi watatu juha ni nani?"
Wakakubali wakaenda wote watatu huku wanapiga kelele za kumwita yule mtu, "Ee Bwana weee, simama! Ee Bwana, simama!" Yule mtu akawaza, "Nimefanya nini huko nyuma nilipowapita wale watu?" Akasimama.
Hata walipomfikia karibu mmoja wao akasema, "Ati bwana, ile salamu uliyotoa Si yangu mimi? Juha si mimi?"
Wa pili akamwuliza vile vile, "Je! ile salaam si yangu! Juha si mimi?" Watatu naye akauliza, "Juha si mimi, Bwana?" Yule mtu akawaza rohoni mwake ya kuwa nitawauliza watu hawa. Akamwuliza yule mmoja, "Lete habari za Ujuha kweli!"
Akasema, "Bwana mimi ni juha kweli. Jana nalikwenda sokoni, nikaenda nikanunua nyama, nikampelekea mke wangu akapika, kabla nyama haijaisha kuiva bado, yule mke wangu akatoka, akaenda kuomba chumvi. Huku nyuma nikatwaa vipande viwili vya nyama nikatia mdomoni nikatafuna, kabla sijameza, mke wangu akaja nami kutafuna nikaona haya, ile nyama nikaitia katika shavu moja likajaa fututuu, mke wangu aliporejea akaniona ni hali ile, akasema, 'Alhamdu Lillahi Rabbi-l-alamina, Mwenyezi Mungu ni mkubwa. Mara hii natoka kwenda omba chumvi, naja ndani mume wangu amevimba shavu! Bahati! lete uma na moto.' Akaleta ule uma, ukawashwa moto nikachomwa katika shavu, nikaona shavu hili linaungua, nikageuza nyama katika shavu la pili, nalo likachomwa, nikaona sina mahali pa kugeuzia tena nikaitema ile nyama, nikaiangusha pale chini pu! Mke wangu akaniambia, 'Ah! Mume wangu, mke ni mkeo, nyama ni nyama yako, umefanya upumbavu kama huu, hata nimekutia vidonda katika mashavu?' Je! Bwana, wasemaje mimi si juha?"
Akasema, Kweli juha ni wewe. Naam, yule wa pili akasema, "juha ni mimi, jana nilikwenda sokoni nikanunua nyama, na mchele, na nazi, na bizari na kunipia nikaja nikampa mke wangu akapika akaisha. Na mji huu una amri ikifika saa nne milango hufungwa, lakini ikifika sa nne kama hukufunga mlango hukamatwa ukalazwa korokoroni, asubuhi huzungushwa mji mzima kisha hupelekwa kuchinjwa.
Basi nyumbani petu tumekaa hata ikapita saa nne bado hatujafunga mlango, wala chakula hakijapakuliwa.
Nikamwambia mke wangu, Pakua chakula! Akapakua akaisha akaweka juu ya meza, tukitaka kula nikamwambia mke wangu Tusile, nchi hii ina amri na wewe unaijua, basi kafunge mlango kwanza ndiyo tuje tule; mke wangu akaniambia, 'Kafunge wewe,' nikamwambia, Kafunge wewe, akaniambia, 'Kafunge wewe.'
Nikamwambia mke wangu, Hatuna haja ya kubishana, basi na tukae hivi hivi tu, na chakula tusile, atakayekula, na akafunge mlango, na atakaye sema, na akafunge miango.
Basi tukakaa mimi na mke wangu kimya tukatazamana tu. Tukakaa hata akaja punda mle nyumbani, akala mtama hata ukaisha, punda akatoka, hapana asemaye, atakayesema na akafunge mlango. Akaja mbwa akaingia nyumbani, akaramba vyombo vyote akaja pale mezani akala ule wali wote, sahani akazivunja akaenda zake, hapana asemaye kama Mbwa amekula wali wote,
Atakayesema na akafunge mlango. Tukakaa hata saa saba. akaja askari, akatuuliza, 'sababu gani hamkufunga mlango?'
Tusiseme, tukanyamaza askari akatuchua akatupeleka korokoroni hata asubuhi tukapelekwa kwa Sultani. Sultani akasema, 'Wazungusheni mji mzima kisha mkawachinje.' Mimi na mke wangu tukazungushwa mji mzima hatusemi, hata tulipofika karibu na nyumba yetu, mke wangu akasema, 'Mume wangu, si ile nyumba yetu mbona twaipita?' Mimi nikamzomea mke wangu, Woooo! Mke wangu amesema, Eeeeee Woooo! Mke wangu amesema!'
Yule askari akasema, 'Ah! Watu hawa wana ninii? Sultani ameniambia niwazungushe, nikifika pwani niwachinje, sasa wanasema hivi! watu hawa nitawarudisha kwa Sultani.' Askari akaturudisha, akamweleza Sultani, Sultani akatuuliza, nasi tukamjibu, akatupa ruhusa tukarudi kwetu nyumbani.
Je! Waonaje? Wali wangu, mke wangu, nyumba yangu ikitaka kuniua, Je! Bwana mimi si Juha?'''
Akamwambia, "wewe ni Juha zaidi ya yule wa kwanza."
Watatu akasema, "Bwana, Juha ni mimi, mimi jino langu liliniuma, nikauliza. Humu mjini hamna mganga wa jino? Nikaambiwa, 'yupo hapa anaitwa Ali.' Nikaenda kwa Ali, nikamwambia, jino langu laniuma, unajua kutoa jino?
Akasema, anajua. Nikamwuliza, Unatoa kwa pesa ngapi Akaniambia, Nusu rupia tu. Nami nina nusu rupia yangu ya dhahabu, sawa na reale tano. Nikampa akanitoa jino moja.
Nikarudi nyumbani kwangu, mke wangu akaniuliza, 'umekwishatolewa jino?' Nikamwambia, Nimekwisha kutolewa."
"Akaniuliza, 'umempa fungule?'
Nikamwambia, ile rupia yangu ya reale tano. Akaniambia, 'Ah! Mume wangu, wenzio watolewa jino moja kwa robo ya reale, pesa 32, wewe umetolewa jino moja, umetoa reale 5!'''
"Nikarudi kwa Ali, nikamwambia, Kumbe! Wenzangu unawatoa jino moja kwa pesa 32 mimi umenitoa jino moja kwa reale zangu 5! Basi afadhali unitoe yote! Ali akanitoa yote nikarudi nyumbani. Mke wangu akaniuliza umepata rupia zako? Nikamwambja, Ohooooho: na miye nimemkopa, akaniuliza, 'Kwanini?' Nikamwambia
Amenitoa meno yote kwa robo moja ya dhahabu, je waonaje mke wangu, sikumkopa Ali?
Mke wangu akaniambia, 'ndiyo wewe juha.'''
Yule mtu akamwabia, "Ah! Wewe juha sana, hata salamu zile ni zako wewe."
Wakarudi wakiambiana huyu ameshinda wenzake kwa ujuha
 
SIMBA NA SUNGURA​



Zamani za kale aliondokea simba akaenda mwituni kuwinda wanyama ili apate chakula. Hata siku moja alipokuwa akitembea alisikia mashindo, akitazama aona kundi la nyati, akashangaa kwanza, lakini akawaza kuwa, Miye sikuzote hutafuta wanyama na wanyama ni hawa, nitabahatisha. Akajibanza mahali kimya. Mara walipokaribia akamchagua mmoja akamrukia .Vikaanguka vishindo, patashika. Mzee nyati akaangushwa chini. Huku na huku, akapigwa ukucha wa shingo akafa.
Lakini kwa jinsi vita ilivyokuwa kubwa hata mzee simba naye akajeruhiwa mkono. Lakini maadam amepata chakula basi, akamkokota hata chini ya mti mkubwa penye kivuli kizuri, akakaa akitweta. Mara akatokea Sungura, naye alikuwa anapita tu katika matembezi yake hakujua kama mzee simba yupo pale.
Hata alipomwona akamtambua kuwa ni Bwana mkubwa, akamwambja, "Sabalheri mjomba, mbona upo hapa, tena una nini? Mbona nakuona hali hiyo?" Kumbe Sungura kaisha ng’amu kama mzee simba ana nyama pale. Basi simba akamwita akamwambia, "Njoo mwanangu, hali yangu mgonjwa kidogo."
Sungura akaenda, simba akamwambia, "sungura unaiona nyama hiyo?"
Sungura kanena, "Naam naiona, nini shauri lako bwana?"
Simba akamwambia, "Nataka uichune uzuri, uitumbue uzuri, uoshe uzuri, ukiisha uniletee moyo, maini na figo, nipate kufungua kinywa, maana tangu asubuhi sijala kitu."
Sungura akaenda upesi upesi, akatengeneza ile nyama kama alivyoambiwa. Lakini mahali pa kupeleka vitu vile alivyoagizwa na simba, (ndiyo moyo, maini na figo) akavichoma vizuri akala yeye mwenyewe. Akatwaa nyama ya mafuta akachoma akamchukulia mzee simba.
Simba akiangalia aona hivi sivyo vitu alivyotaka.
Akamwambia Sungura, "hivi sivyo vitu nilivyotaka."
Sungura akasema, "Bwana mkubwa vitu ulivyotaka vimeungua moto vyote." Simba akanyamaza kimya kwa kuwa mkono unamuuma, akatwaa ile nyama ya mafuta akala, akanywa maji akashukuru. Akisha kula akamwambia sungura, "Sasa huna ruhusa kuondoka, kazi yako ni kunipikia maji ya moto, na chakula, mpaka nijaliwe kupona mkono wangu."
Sungura akasema, "Ee walah, bwana wangu, mimi mtumishi wako tokeapo nitathubutu wapi kukutupa katika hali hiyo ya ugonjwa?"
Wakakaa siku nyingi. Hata siku moja akapita mzee fisi pale, naye kafanya kupotea njia tu. Sungura akamkaribisha fisi. Fisi alipoangaza macho akaona mifupa imetupwa ovyo hayana mlaji, akayamezea mate. Sungura alipozidi kumwuliza habari, akasema kuwa amepata habari kama mzee simba hajiwezi, basi kapita hapa ili kumtazama.
Basi Sungura akanena, "Ningoje kidogo nikampashe habari mzee simba."
Akaenda kumpasha habari kama Fisi kaja kumtazama. Simba akamwambia Sungura, "Vema, nakuja sasa hivi." Akatoka nje, akaamkiana na fisi wakakaa. Simba akamwambia Sungura, "Mtafutie chakula mgeni." Sungura akaenda akamkusanyia fisi mifupa yote, nyama akampa kidogo. Maana anamjua fisi ulaji wake ni mifupa. Basi mzee fisi akala hata akashiba, akapewa maji akanywa.
Alipokwisha shiba fisi akaaga akasema, "Bwana mkubwa leo nina haraka sina budi kwenda zangu, lakini sitakawia nitarudi kukutazama. Akaenda zake lakini moyoni mwake asema, "Ah! najua huyu Sungura anafaidi, nifanye hila gani hata na mimi nikae Pale nile mifupa pale?"
Hata baada ya siku mbili tatu, Mzee Fisi huyu akaja tena, "Hodi Hodi!"
Sungura akaitikia, "Karibu,nani Wewe?"
Akajibu, "Ah! ni mimi Fisi nimekuja tena kumtazama mgonjwa."
Akaambiwa, "Karibu."
"Je, Bwana u hali gani mkono Wako?"
"Ah! Sijambo kidogo." Wakakaa kitako. Sungura akaenda akapika chakula, akawapakulia kila mtu mbalimbali. Kwa mzee Fisi akatia mifupa mingi. Fisi akafurah sana.
Walipokuwa wakila Sungura akatwaa mtungi akaenda kuteka maji. Huku nyuma simba akamwuliza Fisi, "Je, mzee Fisi hujui dawa?"
Fisi akamwambia, "Hivi bwana Sungura hajakupa dawa?"
Simba akanena, "La, hata sina habari kuwa ajua dawa!"
Fisi akamwambia, "Sungura ni mganga mkubwa bwana, kama hajakupa dawa fahamu kuwa anafanya kusudi."
Simba akaudhika sana, akasema, "wajua huyu Sungura si kitu. Yupo hapa sikuzote naye hanifanyizii dawa!"
Mara sungura akaja na mtungi wake, akamimina maji, akaenda tena kisimani Na huku nyuma maongezi ya Simba na Fisi yameshika juu ya Sungura. Hata Sungura alipokuja tena na mtungi wake Simba hakuweza kustahimili. Akamwita" Sungura!"
Sungura, Akaitika, "Lebeka bwana."
Akamwambia, "Ati wewe wajua dawa ya vidonda? Mzee fisi ameniambia kuwa wewe unajua dawa. Na wewe upo hapa siku zote hizi hata hunifanyizii nikapona mkono wangu?"
Sungura akanyamaza kwanza akiwaza maana alifahamu kuwa hii ni fitina ya fisi, anamhusudu kwa ile mifupa.
Simba akamuuliza, "Je sungura, mbona kimya?"
Sungura akasem, "nawaza bwana, maana dawa yenyewe ina udhia, ndiyo maana nisikuambie tangu zamani."
Simba akamwambia, "udhia gani? Sema tu, mimi natak kupona."
Sungura akasem, "Ee bwana wanfu,mimi nakumbuka wazee wangu waliniambia dawa ya kidonda kam hiki chako, hapana dawa ila ipatikane ngozi ya mgongoni mwa fisi, ufunhiwe jeraha, utapona."
Simba aliposikia vile hakusaili tena, akamrukia fisi. Akampanda mgongoni na kumrarua ngozi yote ya mgongoni. Fisi akakimbia akaenda zake, simba akapata ngozi kisha akampa sungura, akamwambia, "haya fanya uganga wako."
Sungura akaitwaa, akaikata sawa na jeraha na kuifunga hodari. Hata muda wa siku mbili tatu, mzee simba akajiona yu hai kabisa. Akajua kweli sungura mganga. Sungura akapata kibali kwa simba. Lakini fisi akapata hasara, ndiyo maana hata sasa ukimtazam fisi utaona manyoya yake mgongoni marefu, maana yaneota katika kovu.
 
FIKIRINI NA HEMEDI​


Hapo kale katika nchi ya Pate palikuwa fundi mmoja mshona cherehani. Alikuwa na kiwanda chake, na wanafunzi hawapungui ishirini. Na katika wanafunzi hawa alikuwako mmoja anaitwa Fikirini. Huyu alikuwa mtu mmoja mzuri sana, tena hodari Wa kazi. Lakini alikuwa na hitilafu moja, alikuwa majinuni kidogo. Kuna wakati hufanyiza kazi sana na kuna wakati hushikwa na bumbuazi, akanyamaza kimya wala hafanyi kazi. Ikawa hali yake namna hii, hata bwana wake akamjua kuwa ndiyo hali yake. Na Huyu Fikirini alikuwa mtu mzima sana kwa sura, tena alikuwa mtu mmoja nadhifu sana. Na akapenda kujiweka katika daraja kubwa kubwa, hata pengine hujishugulisha na mtoto wa Sultani kwa makuu yake.
Hata akitembea njiani huvaa nguo vizuri na kilemba, na watu wakimwamkia huitikia kisultani kwa kichwa na mikono. Hata watu wote wakajua kuwa Fikirini apenda sana fahari ya Usultani. Akawa na mawazo yale hata yakamjaa moyoni. Mwisho akaona dhiki kukaa pale mjini kwa kuwa watu hawampi heshima ya mwana wa Sultani. Basi akaazimu kutoka katika nchi ile kwenda nchi nyingine watu watakakomdhani kuwa ni mwana wa Sultani. Lakini kabla hajaondoka, siku moja Sultani wa nchi ile nguo zake anazovaa siku ya rasmi, na siku ya baraza, ziliharibika kidogo, zikahitaji kutengenezwa kwa kushonwa kidogo. Basi zikapelekwa kwa, fundi mshoni. Kwa bahati zikapelekwa katika kiwanda kile kilekile cha fundi wake Fikirini.
Na yule fundi akatwaa zile nguo akampa Fikirini kushona. Hata usiku walipokuwa watu wote wameondoka kiwandani, Fikirini akazitwaa zile nguo akazitazama, akafurahi akacheka moyoni mwake akasema, "Hii ndiyo bahati yangu, nguo hizi nikivaa mimi nitakuwa mwana wa mfalme kwelikweli."
Basi yalipomjia mawazo haya akaondoka akasafiri kwenda nchi ya Mbali. Na alipofika katika nchi ya ugeni akavaa nguo zile. Na watu walipomuona wakadhani kuwa ni mwana wa mfalme bila shaka. Naye Fikirini mwenyewe hakujitupa, akiwa karibu na mji hupeleka habari kama mtoto wa Sultani anakuja na watu huenda kumlaki kwa sherehe. Lakini watu wakistaajabu kwa kumuona anakwenda kwa miguu.
Basi wengine wakamuuliza kuwa, "kwa nini kwenda kwa miguu naye ni mwana wa mfalme?"
Naye akajibu kuwa anapenda tu. Hata usiku alipolala akawaza akaona kweli amepngua neno maadam hana farasi. Basi asubuhi kulipokucha akafanya shauri kununua farasi. Alikuwa na akiba yake reale miteen, akatoa reale mia akanunua farasi mzee asiyeweza kumwangusha. Akawa anasafiri kwenda mji mwingine, njiani akakutana na mwana wa Sultani kwelikweli, jina lake Hemedi.
Na huyu Hemedi naye hakuwa na mtu alikuwa yeye peke yake na Fikirini naye peke yake. Fikirini akaanza kumuuliza Hemedi, "habari zako, anakwenda wapi?"
Hemedi akajibu, "Ah! bwana wangu, sijui ninakokwenda, napotea na dunia tu."
Kisha Hemedi akamwuliza, Fikirini, "je, wewe unakwenda wapi?"
Akamwambia, "Na mimi vivy hivyo bwana wangu, sijui niendako."
Basi wakatoa vyakula vyao wakala, na farasi wao wamewafunga. Kisha wakawa wanazungumza. Fikirini akamwuliza Hemedi, "Je! rafiki yangu ulikuwa unakusudia kwenda wapi?"
Akamwmbia, "Mimi natoka Guba kwa Sultani Umeya bin Azuwan, na huyu Sultani Umeya amekufa Na wakati alipokuwa akifa akaniita akaniusia. Akaniambia, 'Hemedi.' Nikamwambia, Naam!
Akaniambia, 'Njoo karibu yangu.' Nikaenda karibu yake nikakaa. Akaniambia, 'Tazama Hemedi!
Wewe si mtoto wangu. Wala Si mjukuu wangu, wewe ni mtoto wa Sultani mkubwa sana Wa nchi ya Baghdad, Na asili ya kuja huku kwangu ni hii. Siku uliyozaliwa wewe baba yako alikwenda Kwa watu wenye elimu kutazamia Akaambiwa, Mtoto wako mtoe katika nchi yao maana wamo maadui waliomkalia mtoto kwa jicho la uhasidi. Mwondoe katika nchi yako mpeleke katika nchi ya Sultani mwingine, Huko kwa Sultani mwingine aende akakae kwa muda wa miaka ishirini na moja. Na siku ya ishirini na mbili ya mwezi wa Ramadhani iwe ndiyo siku ya kufika kwa wazee wako, Na ninakufa, na ile siku iliyoagizwa na baba yako sasa sasa iko karibu. Na baba yako alinipa jambia hili akasema, Siku utakayomleta mwanangu, mlete katika mnara mkubwa katikati ya mbuga chini ya mlima wa Baghdad. Toka hapo mpaka Baghdad ni mwendo wa siku nne.'''
'''Akanipa na jambia hili nikupe ushike mkononi liwe ndiyo alama yako. Basi sasa shika jambia hili ukae nalo hata ukiona zimebaki siku tano ondoka uandame njia, na ukifika mahali ukiona watu wamejaa tele mahali penye mnara toa jambia hili ndani ya ala, mpe mkubwa wa hao watu useme, Mimi ndiye Hemedi bin Sultani. Na watu watakujibu, Alhamdulilah, Mwenyezi Mungu amekulinda hata sasa umefika mkononi mwetu.'Haya ndiyo tuliyoomba.'''
Wakalala. Na yule Hemedi hakuwa na wasiwasi akajua kama rafiki yake kamuuliza habari kamweleza, basi. Kumbe! Fikirini hakupata usingizi siku ile.
Akawaza mengi. Hata mwishowe akaona hapana njia ila ajifanye yeye kuwa ndiye Hemedi awe mwana wa Sultan kabisa. Basi akafanya hila akamnyang’anya Hemedi jambia lake, wakati huo Hemedi kalala. Akamchukua na farasi wa Hemedi akapanda akaenda zake usiku huo huo.
Hata asubuhi Hemedi alipoamka akaona farasi wake hayupo, na jambia limechukuliwa, na Fikirini hayupo. Hemedi akajua kuwa hii ndiyo kazi ya Fikirini. Fikirini akaenda zake siku ya kwanza, ya pili, ya tatu, akalala karibu na ule mnara wa Baghdad. Asubuhi alipoamka akaona watu wengi sana, wengine wamepanda ngamia, wengine farasi, wamevaa nguo nzuri nzuri. Fikirini naye akavaa zile nguo zake za ufalme, akavaa na lile jambia la Hemedi, amepanda na farasi wa Hemedi. Alipowaona watu akamtoa kasi farasi wake.
Akafika pale walipo watu, akapiga, Salaam aleikum! Watu wakaitikia, aleikum salaam. Mara akalitoa jambia akampa mzee aliyesimama sawasawa na lango la mnara Na huyu mzee alikuwa ndiye baba yake Hemedi. Baba mtu alipoona jambia akasema, "Alhamdulilahi."
Mara zikaamrishwa ngoma nyingi zikapigwa. Na Sultani akamtwaa Fikirini akampakata
Na watu wakashika kusema, "Bwana Hemedi amekuja, amekuja!"
Walipokuwa katika sherehe hii, mara wakamwona mtu amepanda farasi anakuja kasi. Na Fikirini alipomuona akajua kuwa ni Hemedi. Basi akaanza kuwaambia watu ya kuwa yule anayekuja ni mwongo, wala msimsadiki lolote atakalosema, na bado akili zake si barabara, ana wazimu kidogo.
Mara Hemedi akatokea.
Akaja moja kwa moja mpaka mbele ya Sultani akamwangukia, akalia. Akamwanibia, "Mimi ndiye mwanao baba, huyu siye." Mara Sultani akatoa amri aondolewe mbele yake, akasema, "Mwondoeni, ana wazimu."
Hata alasiri saa tisa wakafunga safari kurudi mjini Baghdad. Fikirini akapandishwa farasi mwingine mzuri sana mwenye matandiko ya dhahabu. akatangulia mbele pamoja na Sultani. Na Hemedi maskini amefungwa yuko nyuma amepandishwa juu ya ngamia. Safari ikashikana. Njiani kila mji waliopita watu wakampa Fikirini zawadi kama desturi ya masultani.
Walipokuwa karibu na Baghdad, Sultani akatuma watu waende nyumbani kwa Bibi wakampe habari kama mtoto atawasili kesho. Basi mji ukapambwa na nyumba ya Sultani ikapambwa sana. Asubuhi watu wakaingia mjini.
Sultani akatangulia akaenda akakaa katika chumba cha baraza, na mkewe naye akaja akakaa ili amuone mwanawe. Basi wageni wakaingia katika mji kwa sherehe na ngoma. Walipoingia ndani, Sultani akamwambia Fikirini, Nenda ndani kamwamkie mama yako. Akaenda. Mke wa Sultani akamtazama sana Fikirini akasema, "Mimi mtoto wangu namjua sana, ijapokuwa amepata miaka ishirini na moja hawezi kunipotea." Alipompa mkono, mke waSultani akaupokea, lakini akasema, "A-a-a, huyu si mtoto wangu kabisa." Watu wote wakanyamaza kimya. Na Fikirini naye hana la kusema, uso umeanguka chini. Mara Hemedi akatoka mahali alipokuwa akawasukuma watu akaingia mpaka ndani alikokuwa mama yake. Akaanguka chini akalia sana kwa kupiga kelele, "Ee jamani msisikilize huyu, mnyang’anyi huyu!"
Na mke wa Sultani naye akishika vile vile, "Huyu ndiye mtoto wangu Hemedi." Lakini Sultani hakukubali maneno haya, akaamrisha Hemedi aondolewe, akamchukua mtoto wake Fikirini akapanda juu orofani.
Mke wa Sultani akakasirika sana, akasema, "mimi na mume wangu hatujagombana tangu kuoana, na sasa na yeye pia amekasirika kwa neno hili, lakini haidhuru mimi najua desturi yake, nitamwendea kwa wakati mzuri nikampe shauri langu."
Mke wa Sultani alikuwa mtu mzima, naye ana akili sana basi akawaita wanawake anaokaa nao nyumbani mwake akawauliza je nini shauri lenu katika habari hii? Akatokea mwanamke anaitwa Tamasha akasema, "Tazama, bibi, katika maneno ya Hemedi alipokuwa akisema nawe, kasema kuwa yule mwenzake ni fundi mshona cherehani, Basi kama ni kweli mtake Sultani apate kuwajaribu vijana hawa maana atajulikana aliyekuwa fundi."
Mke wa Sultani akaona ni shauri jema. Akaenda kwa mumewe akamwambia, "mume wangu nisamehe kwa maneno niliyosema jana."
Mumewe akamwambia "nimekusamehe mke wangu." kisha akamwambia, "bwana naomba kila nitakalokuambia, maadam mimi na wewe tunashindana kwa habari ya hawa vijana napenda kuwajaribu, jana tumesikia yakuwa huyu unayemshika wewe kuwa bin Sultani kazi yake ni kushona cherehani. Basi wape kazi ya kushona niwatazame." Sultani akakubali. Zikaletwa cherehani mbili na zana za ushonaji zote, zikatiwa katika vyumba mbalimbali Sultani akawaambia wale vijana, "tazameni wanangu, nasikia ya kuwa ninyi mwaelewa kazi ya kushona. Basi napenda mnishonee joho kila mtu kwa ufundi wake."
Fikirini akawaza moyoni ya kuwa kushona ni kitu gani! Ni mchezo tu kwangu. Nitashona joho hata watu wastaajabu. Lakini yule Hemedi ameshangaa, maana hajui. Wakapewa vitambaa.
Fikirini akashona joho lake vizuri kwelikweli. Hata Sultani na mkewe walipoliona wakashangaa. Walipokwenda kutazama kazi ya Hemedi wakakuta vitambaa vizima havikukatwa Alipoulizwa, akasema, "Sijui mimi, maana kushona cherehani Si kazi ya mtoto wa mfalme."
Mkewe akamwambia, "Je! Bwana sikukuambia miye, mtoto ni huyu asiyejua kushona." Lakini Sultani hakukiri bado. Wakakaa, hata baada ya siku chache Sultani akajaribu vingine.
Katika mji wao kuna mahali watu walipokuwa wakiomba, napo ni makaburini, kwa wazee wao. Basi Sultani akaenda hapa, akasema na babu yake aliyekufa, akamtaka amsaidie katika neno hili ampe mwangaza kidogo.
Akakaa kidogo mara akaona mbele yake visanduku viwili vya lulu, na visanduku hivyo vyote sawasawa. Vyote vimeandikwa
juu. Kisanduku cha kwanza kimeandikwa Mali na bahati, na cha pili kimeandikwa. Heshima na dola. Ikatoka sauti ikamwambia. "Chukua visanduku hivi hata nyumbani, ukakusanye watu wengi, uwaite na hao vijana kila mtu achague chake, baada ya hayo utamjua yupi mwanao."
Siku ya pili Sultani akakusanya watu wakajaa baraza tele, vikaletwa vile visanduku vikawekwa juu ya meza.
Kisha wakaitwa wale vijana mmoja mmoja. Akaitwa Fikirini kwanza, akaambiwa, "Baba nimetaka kukupa zawadi ya kisanduku. Basi chagua kimoja katika visanduku hivi."
Fikirini akasoma kwanza juu na akuchagua kile kilichoandikwa Mali na bahati. Sultani akasema, Marahaba, na kikae hapa kwanza. Kisha akaitwa Hemedi, naye akaambiwa maneno yale yale aliyoambiwa Fikirini. Hemedi naye akasoma kwanza, akachagua kile kilichoandikwa Heshima na dola, maana yeye mtoto wa Sultani mali na bahati hana haja navyo. Halafu akaitwa Fikirini akapewa kisanduku chake, na Hemedi naye akachukua chake. Lakini kabla hawajaondoka vile visanduku vikafunguka vyenyewe. Ndani ya kisanduku cha Fikirini mna zana za ushonaji, na ndani ya kisanduku cha Hemedi mna taji. Sultani akaitwaa ile taji akamvika Hemedi. Na yule haini akazomewa na kupigwa, mwisho akafukuzwa katika nchi ile.
Akatoka na kile kisanduku chake na farasi wake mzee akarudi kwao kwa aibu. Mwizi wa ajabu huyu, watu huiba vitu, yeye akataka kuiba ufalme! Alipofika katika nchi yake, akarudia tena ufundi wake wa kushona. Wenzake walipomuona wakamcheka sana. Lakini bwana mwenye kiwanda hakupenda kumweka tena kiwandani pake, akamfukuza. Akaenda zake akauza kile kisanduku chake akapata fedha akanunua nyumba mali yake, akanunua na cherehani yake. Akakaa kitako akifanya kazi yake ya kushona.
 
KISA CHA MAJUHA WAWILI WANAWAKE​

Hapo zamani za kale palikuwa na maskini katika mji mmoja. Maskini huyo alioa mke na akazaa naye mtoto mmoja wa kike. Alikuwa na ng’ombe mmoja jike na ndiyo ilikuwa rasilimali yake pekee. Na kazi yake ilikuwa ni kulima makonde uko nje ya mji.
Kila siku wakati wa kuingia mjini huchukua majani ya ukoka kama chakula cha ng’ombe wake. Bibi na mtoto hubaki nyumbani. Hata siku moja alipokuwa yule mtoto ametimia miaka saba umri wake, aliota ndoto usiku.
Na ndoto yake ilikuwa ameota kaolewa tena amezaa mtoto mwanamke mzuri sana. Asubuhi baba yake akaamka akaenda kondeni kwake. Yule mtoto alipoamka akaangua kilio akalia, "mama wee! Mama wee mtoto wangu yuko wapi?"
Hata mama mtu akasikia kilio akaenda chumbani akamwuliza, "je mwanangu walilia nini asubuhi yote hii?"
Mtoto akamjibu mama yake kuwa, "nimeota ndoto usiku mmenioza mume, kisha nikazaa mtoto mwanamke mzuri, sasa naamka simwoni, ndiyo maana nalia, umemchukua wewe mama." Akasema hivi na huku analia.
Mama mtoto aliposikia habari ya mtoto aliyezaliwa usiku na kumwona mwanaye analia, naye akaangua kilio akalia. Ikawa kelele moja kwa moja, hata majirani mtaani wakasikia vilio wakaja nao kusikiliza kuna nini? Mama mtu akawaelezea watu mambo yote ya ndoto, majirani wakacheka sana wakanena, "Haya mambo! Hatujapata kuona sisi watu kulia kwa sababu ya ndoto." Lakini wale wenyewe wamekazana kulia,
Jirani mmoja mzee alipoona hawa ni wapumbavu, na kelele zikazidi akataka kuwanyamazisha akaenda kumwambia yule mama, "bibi hapana maana kukaa kitako ukilia, kama mtoto aliyezaliwa usiku amekufa, iliyobaki ni kuweka matanga nakuondoa.
Lakini aliyekufa kwa kuwa ni mtoto mdogo fanyeni chakula tu mpate kuondoa msiba."
Yule mke wa maskini akasema, "hayo ni mashauri mazuri lakini nitafanyaje mume wangu hayupo, naye ndiye mwenye mashauri ya mapesa."
Yule jirani akamwambia, "huna hata kikuku ukachinja?"
Akajibu, "nyumbani hamna kitu ila ngombe wa bwana naye anampenda sana. Akaambiwa, "utafanyaje basi, nawe una sharti ya kuondoa msiba huu, usipoondoa itakua uchimvi utakufa wewe au mume wako."
Yule mwanamke aliposikia vile akafanyiza hofu, akaona afadhali amchinje huyu ng’ombe maana sina kitu kingine.Akaita watu akagiza wamchinje ng’ombe.
Watu wakachekelea sana wakajua leo ndio kufaidi. Wakamchukua ng’ombe wakamchinja, wakamchuna upesi upesi. Wakatwaa mguu wakaenda wakabadili kwa mchele, wakatwaa nyama nyingne wakabadili na vitakataka vingine vya kupikia, Mara upishi ukasimama ukapikwa wali hata ikipata saa saba chakula tayari
Akaitwa mwalimu kuja kusoma hitima. Watu wengi wakaja kula chakula ikawa tena kila aliiyesikia akaja na wote waliokuwa wakija wakapata chakula. Hata habari ikaenea mji mzima kwa maskini kuna hitima, na wakisifu chakula kwa wingi wakati huu wote mume yupo shamba analima hana habari za hitima nyumbani kwake, Kasikia kwa watu waliokuwa wakitoka mjini kwenda shamba lakini hakutia moyoni maana hali ya nyumbani kwake anaijua mwenyewe. Akakaa hata saa zake za desturi akang’oa ukoka wake, akashika safari taratiibu kwenda zake mjini.
Wakati huu kule nyumbani wale watu wamekwisha ondoka, maskini akafika nyumbani kwake mkewe akamlaki juu kwa juu, karibu bwana karibu. Yule maskini kimya akaongoza njia moja kwa moja mpaka zizini, akatua mzigo wake aingie ndani ya zizi ng’ombe hayumo!
Akashangaa, "ng’ombe wangu yuko wapi? Mara mkewe akaja akamwambia, "Mume wangu twende ndani nikakupe habari za mkasa ulionipata, na nikuelezee ng’ombe wako yupo wapi."
Yule maskini akasema, "siendi popote mpaka nimwone ng’ombe wangu kwanza, Mkewe akamwambia, Bwana twende ndani nikakueleze."
Lakini yule madjini akasisitiza, "nieleze hapa hapa." Yule mkewe tena akaona hana budi kumweleza mambo yaliyopita akamweleza yote. Maskini aliposikia kuwa ng’ombe wake amechinjwa kwa ajili ya ndoto, akaduwaa, asijue la kutenda, akaingia ndani akakaa kimya, mkewe akamletea chakula asiweze kula.
Hata usiku Yule maskini akamwambia mkewe, "tangu kuzaliwa sijapata kuona juha kama wewe. Ilikwendaje wewe kusikiliza maneno ya ndoto? Basi sasa nifanyizie mikate nataka nisafiri nataka niende mbali nitafute mtu mwingine aliye juha kama wewe. Nikimwona utakuwa mke wangu hivi hivi. La sikumwona nitakuacha."
Asubuhi mkewe akamtengenezea mikate akafunga akachukua na karatasi na bahasha na wino. Akaondoka akaenda zake msitu na nyika hata zikatimia siku saba akafika katika mji mmoja mkubwa. Na yeye kwa kuwa alikuwa na mashauri yake moyoni hakuingia mjini, akafika katika kibanda cha kizee mmoja mwanamke. Yule mwanamke hakukasirika akamkaribisha, akamfanyizia na chakula.
Yule mgeni akauliza sana habari za mjini, na habari za wakubwa wa mji, kizee mwanamke akamwambia, "mwanangu, je, una haja nao hata ukawauliza hivyo?"
Akanena, "naam, shughuli kubwa." Hata ilipofika usiku kizee akamwuliza, "je utakwenda mjini leo au utalala hapa leo?" Akanena, "Ningependa nilale hapa, asubuhi niingie mjini."
Yule kizee akamwambia, "karibu mwanangu, ipo nafasi tele hapa." Akapewa chumba cha pili katika kibanda chake. Yule mgeni akafurahi sana alipoingia chumbani kwake akafunga mlango wake akatoa karatasi zake, akakaa kitako akaandika barua zake, moja kwa Sultani, moja kwa binti Sultani moja kwa waziri, moja kwa mke wa waziri.
Akazifunga katika bahasha kila barua bahasha ya peke yake.
Asubuhi akamwuliza Yule kizee nyumba za watu hawa aliowaandikia barua ziko wapi?
Yule kizee akajibu, "Nyumba za watu hawa wote zipo pwani forodhani, ila nyumba ya Binti Sultani iko nje ya mji si mbali kwa kutoka hapa." Akauliza namna ilivyokaa, na alama zake akaambiwa zote, basi alipokwisha pata habari zote alizozitaka akaaga akasema, "kwa hapa mama sina budi kwenda mapema nikamuwahi kila mtu nyumbani kwake niwape barua zao."
Akaondoka akaenda akishika njia akaingia mjini akafika panapo ile nyumba ya binti Sultani. Akatazama huku na huko akaona tanuru ya chokaa na ile tanuru inaelekea penye dirisha la binti Sultani. Akachimba chini ya ile chokaa. Akangoja mpaka alipoona sasa ni sa tatu akajifukiza pale penye chokaa kwa kichwa chake, na huku anapiga kelele, "Eeh! Jamani nifaeni mwenzenu natoka, mbali mimi, shime jamaa." Mara akachungulia mtumishi dirishani akaona chokaa inatutumuka na kichwa cha mtu kinatokeza, akaenda akamwita bibi yake akamwambia tazama chini, "Kitu gani kile?"
Akachungulia chini akaona mtu anaotokeza penye chokaa na huku akipiga kelele. Mara binti sultani akamwita mtumishi mwana mume akamwambia, "Uledi nenda upesi ukamtazame mtu yule ana nini?"
Mara Uledi akaenda akamwuliza, "wewe ni shetani au binadamu?"
Yule mgeni akasema, "mimi ni mtu lakini natoka ahera nimetumwa kuja kuleta barua za watu hapa mjini. Je sasa mimi nipo wapi hapa?"
Uledi akamwambia, "hii nyumba inayokukabili ni nyumba ya binti Sultani." Yule mgeni akasema, "ooh! vema sana ninayo barua yake hapa."
Uledi akamshika mkono akatoka katika ile chokaa, akampeleka uani, akapewa maji akaoga, akapewa na chakula, na wakati wa kula akistaajabu. "Hivi ndiyo chakula cha ulimwenguni wa siku hizi?" Anafanya kasahau maana yake katoka ahera. Alipokiwsha wakampeleka kwa bibi, kufika tu yule mtu akamwamkia bibi, akatoa barua akampa, akamwambia, "barua yako hii yatoka ahera kwa mjomba wako, naye anakusalimu pamoja na bwana."
Binti sultani akafungua barua akasoma nayo imeandikwa hivi:
"Saalam mjomba, mimi huku ahera sijambo, na jamaa wote waliopo wazima ila mimi nina dhiki ya deni, nilikopa fedha za watu nami sina cha kuwalipa, basi tafadhali mpe huyu niliyemtuma rupia elfeeni aniletee nilipe deni za watu. Salaam Wakatabahu Mjomba wako."
Yule binti Sultani aliposoma ile barua alisikitika sana akaenda zake moja kwa moja mpaka chumbani akafungua bweta akatoa rupia elfeeni ndani ya mifuko miwili akaenda. Kwenye sanduku la nguo akatoa kanzu ya hudhurungi safi na kanzu melimeli iliyo safi, na kanzu ya doria iliyo safi. Akatoa na buraa Muskati moja, na kitambi cha debwani iliyo njema, na kofia nyeupe ya kazi nzuri.
Akatwaa na vitu vingine vidogo vidogo kama miski, na halundi akatafuta kileso kikubwa cha Hariri akafunga pamoja na vitu hivi vyote. Kisha akaandika barua kwa mjomba wake ahera akaandika hivi:
Salaam mjomba, waama baada ya salam barua yako imewasili. Nami nimefurahi kuniletea huyu mtu wa kunipasha habari ya kuwa wewe mzima, na vitu ulivyoagiza nimempa huyu mtu, nimempa rupia elfeeni, na nguo maana nasikia nguo adimu sana huko.
Salaam, mimi Binti Sultani.
Akampa bahasha Yule mtu wa ahera na barua hii. Akamwambia, "mchukulie mjomba mwambie bwana hukumkuta, ungepewa zaidi ya hivi." Binti Sultani akaendelea kusema, "je nikupe mtu akuchukulie mizigo?"
Yule maskini akanena, "itanilazimu kuchukua mwenyewe maana ahera haendi mtu ila aliyekufa. Basi kwa heri, bibi sina budi kwenda upesi maana jua linapanda na sisi watu wa ahera jua linaatuathiri."
Yule mgeni wa ahera alipotoka nje akaona haina haja ya kupeleka zile barua nyingine.
Akatazama huko na huko akaona mahali njia inapita kwenda vichakani akachagua njia hii, akashika njia kwenda zake. Njiani akapita akasema kimoyo moyo, "Ah! Kumbe majuha wapo wengi nikadhani ni mke wangu tu Kumbe hata katika watu wakubwa wamo majuha!"
Akashika njia akaendda zake upesi upesi, akaviisha vile vichaka akatokea katika mashamba. Alikua anakwenda hivi upesi kwa kuwa alishuku kuwa atafuatwa. Alipofika mle shambani akamkuta mzee mmoja analima, akamwambia, "eeh baba umepta habari za mjini leo?"
Yule baba akasema, "la! Sina habari, kumetokea nini?"
Yule mtu wa ahera akajibu, "imetoka amri kwa Sultani watafutwe vizee vya shamba wote wauawe iwe kafara ya nyumba moja ya Sultani inayojengwa, basi mimi kwa hisani yangu napenda uvae hii kanzu yangu, na mimi unipe nguo zako za kulimia unipe na jembe lako nilimie, na wewe panda juu ya mnazi huu utazame juu njia ya mjini utaona mtu anakuja."
Sasa turudi kwa binti Sultani baada ya kuondoka huyu mtu wa ahera mara bwana mume wa binti sultani akarudi nyumbani, akamkuta mkewe ana majonzi akamwuliza, "je bibi una nini?"
Yule bibi asiseme neno akatwaa ile barua akampa mumewe akaisoma. Alipokwisha soma akamwuliza mkewe jinsi yalivyokwenda mambo haya, mkewe akaleza yote jinsi alivyokuja mtu wa ahera akaleta barua hii, na yakuwa amempa mjomba wake wa ahera haja aliyotaka na zawadi nyingine.
Yule mume akakasirika sana akamwuliza mkewe, "wewe una wazimu! Sasa niambie huyu mtu kaenda njia gani?" Akaambiwa kapita ile njia ya vichakani, mara akaagizwa atandikwe farasi akavaa nguo zake, joho, kilemba na upanga mkononi. Akapanda farasi ili kumfuata huyu mwizi mkubwa lakini akamwambia mkewe, "fahamu mimi namfuata huyu mtu maneno yake yakinielea vema utakuwa mke wangu lakini ukiwa ni upuuzi wako na wazimu nitakuacha."
Akatoka akaenda zake kwa kasi. Basi alipokuwa anakuja mbio, Yule mjumbe wa ahera akasema, "je sikukwambia miye?" Mara yule mpanda farasi akafika pale akamkuta Yule hasimu wake analima. Akadhani huyu ni baba shamba tu, akamuuliza, "hukumwona mtu anapita hapa na bahasha?"
Akamjibu, "sikumwona bwana lakini tazama huko juu mnazini, kuna mtu: huyo ndiye aliyekuja kutoka huko mjini, alipofika hapa akapanda juu ya mnazi, nilipomwuliza akasema anaogopa basi sijui kama ndiye unayemtafuta."
Yule bwana akamwuliza yule mtu kama anajua kupanda mnazi, yule akasema, "la bwana sijui." Yule mwarabu akawa ameshikwa na uchungu, akawa anataka kumwua yule aliyekuwa juu ya mnazi, basi akavua nguo zake kanzu na joho na kilemba na jambia akampa yule mgeni wa ahera amshikie pamoja na farasi. Yeye akapanda juu ya mnazi. Alipokuwa akipanda akawa anasema, "utanitambua leo mwizi mkubwa wewe, leo kutoka yangu au yako."
Na yule aliyekuwa juu akaona kuwa maneno ya yule mgeni wa ahera kuwa ya kweli. Akadhani huyu anakuja kuniua kwa habari ya amri iliyotoka. Basi naye akamwambia, "haya njoo nami nikuoneshe kazi kama sikukupiga na mundu wangu, yule mwarabu akawa anapanda tu, wala hatazami chini.
Yule mjumbe wa ahera kule chini akaenda akatwaa bahasha yake akafunga juu ya farasi. Akatwaa na zile nguo za mwarabu akazifunga juu ya farasi akampanda, Huyooo! Akaenda zake. Yule mkulima aliye juu ya mnazi akamwambia mwarabu, "Ela! Ebu tazama chini yuko wapi farasi wako?"
Akatehemu, kwenda juu hawezi, kushuka chini hawezi. Kisha akaona hana hila ila kushuka apate hakika ya maneno yale. Akamwambia yule mzee, "shuka chini tupate kuulizana vema. Yule mzee akakataa kushuka mpaka mwarabu alipomwapia kuwa hatamuua. Basi wakadhuka wote. Walipofika chini mwarabu akamwambia, "nipe habari ya yule habithi." Mkulima akampa habari yote tangu mwanzo, alivyokuja na aliyosema, na kumtisha kwa amri ya mfalme iliyoko mjini. Hata ikajiri kubadilishana nguo na yeye kupanda juu ya mnazi, hata kutokea yeye mwarabu.
Yule mwarabu aliposikia kisa hiki, badala ya kukasirika akacheka sana. Na yule mkulima naye akanwambia mwaarabu, "Ela na mimi nieleze ilivyokwenda huko mjini." Mwarabu akamweleza habari zote za barua ya ahera, na vitu alivyopewa. Wote wawili wakakauka kwa vicheko.
Yule mkulima akamuuliza mwarabu, "sasa ukienda nyumbani, Utakwenda kusemaje?"
Yule mwarabu akasema, "Sina la kusema ila nitakwenda kumwambia bibi kuwa nimemkuta yule mtu, nami niliposika habari za ahera moyo wangu ukaingia huzuni sana, hata sikuweza kustahimili nikampa farasi wangu na nguo zangu zote awachukulie watu wa ahera. Je! waonaje kizee?"
Kizee akasema, "Kwell maneno yako. Mana ukisema kuwa umenyang'anywa utachekwa sana. Mwarabu akarudi mjini na kikoi chake na Jambia lake mkononi. Kisha akafika kwa mkewe.
Mkewe akamuuliza, "jinsi gani bwana nguo zako na farasi viko wapi?"
Akamwambia, "kweli maneno yako bibi. Habari za ahera nilizosikia kwa yule mjumbe wa ahera zimenitia huzuni sana, hata nimempa farasi na vitu vyangu vyote kuongezea vile uilivyompa wewe."
"Bai sasa Bibi na tukae. Lakini pamoja na hayo akija mtu mwingine kutoka ahera usimpe kitu mpaka unishauri." Sasa tumrejee yule mjumbe wa ahera. Baada ya kupata farasi akamwendesha kasi, akaenda mwendo Wa siku chache kuliko alivyokuja maana sasa kapanda farasi. Akafika hata kwa mkewe, amechoka kwa kwenda mbio. Akamfungua farasi mzigo wake akaimweka katika lile zizi la ng’ombe wake. Na mzigo akauweka ndani.
Alipokwisha pumzika na kula chakula akamweleza mkewe mambo yote ya safari yake. Akamwonyesha na fedha. Akanena Sasa na tukae kitako mke wangu nimekwisha muona aliye juha kuliko wewe. Lakini Pamoja na hayo ukitokea tena Upuzi wa ndoto wajibu uningoje unieleze tufanye shauri pamoja. Wakakaa raha mustarehe.
 
KISA CHA WADIGO​


Hapo zamani palikuwa na wadigo waliokuwa wakija Mvita kutembea, au kuja kuuza vitakataka vyao. Hata siku moja wakapita mahali wakaona wamekusanyika watu wengi. Kumbe ni msikiti, na wale watu wakisali, maana ilikuwa Sikukuu.
Basi wale Wadigo wakasimama kutazama, wakiona ni faraja kubwa vile, watu wakiinama na kuinuilka. Hata ikajiri kuulizana, "pana nini hapa?Amekufa mtu?" Mdigo mmoja akawaambia wenziwe, "Mambo haya si leo tu, lakini kila siku watu hawa hukusanyika hivi wakifanya vivi hivi."
Karibu yao alikuwako mtu aliyetaalamu akawaambia, "Watu hawa wanasali, wanamwomba Mungu."
Wale Wadigo wakajibu, "Eee! Ndiyo kuomba Mungu huku?"
Wakatoka wakaenda zao. Wale wengine wakafanya kusahau habari ile, ila mmoja katika yao ikamkaa sana moyoni. Hata jioni akawa anazungumza na wenziwe, asema, "Hawa Wajomba (Waswahili) nikiwaona kila siku wamekusanyika. Pamoja wanainama na kuinuka, mnajua wanachofanya?"
Wenzake wakanena, "Hatujui."
Asiwaambie neno. Hata siku ya pili wakafunga mizigo yao tena wakaenda mjini kuuza. Majira ya kurudi wenziwe wakarudi, yeye asirudi. Hata jioni akafanya taratibu, akasogea mpaka panapo dirisha, la msikiti akajibanza. Akawaona watu wanaingia, wanatawadha, wanasimama, na kufunga sala na kwenda rakaa. Kisha akamsikia yule Imam aliye mbele kuliko wote anasali. Na watu wanaitikia, Amin. Lakini maneno yanayosemwa hayajui. Hata watu walipokuwa wakitoka, naye akaondoka akaenda kwa nduguye mwanamke aliyekuwa akikaa mle mjini. Akamuuliza akamwambia, "Ndugu yangu, niambie kweli, watu wale wanaokusanyika mle nyumbani hufanyiza nini?"
Akamwambia, "Wanamwabudu Mungu."
Akalala, asubuhi akaenda zake. Alipofika kwake hakuwahi hata kula chakula kwa wasiwasi mwingi. Akaagiza mtu kumwita mjomba wake. Alipokuja akamwambia, "Mjomba, sisi tunakaa ujingani.
Akamwambia, "Kuna nini baba?"
Akamwambia, "Wewe unapokwenda mjini huwaoni watu wanaokusanyika ndani ya nyumba kila siku?"
Akanena, "Nawaona." Akamwambia, "Basi watu wale humwomba Mungu, nao wanapata vitu vyote vizuri, vyakula, nguo, ndiyo maana unawaona watu wa mjini hawana kazi. Basi kesho nataka uwahimize watu wote waende mwituni wakakate miti tupate kujenga nyumba ya Mungu."
Nao wasikasiri, wakaenda kwa umoja wao wakakata miti wakaleta.
Hata alasiri waanza kuchimba mashimo. Siku ya pill na ya tatu kazi ikashikana mkono kwa mikono, hata siku ya nne kazi imekwisha. Wakangoja ifanye kukauka kwanza. Basi katika siku hizi za kungoja msikiti ukauke yule mwenyewe Hamisi Mchinondo haishi kwenda Mvita kutazama watu wanavyofanya.
Tena akamwuliza yule nduguye mwanamke kama watu hawa wanaosali hupata nini hasa. Nduguye akamwambia, "Hupata thawabu na pepo. Na wewe sasa hapo ulipo ii Islamu, yafaa usilimu, ndipo mambo yako yatakwenda vema."
Basi akakubali kusilimu, akaitwa mtu akamtia maji ya tohara, akamsilimisha akamwita jina lake Salehe bin Oman.
Nduguye akamnunulia kanzu, na kisibao cha kwapa, na kofia, na fimbo ya mtobwe, na viatu. Alipokwisha vaa vitu hivi Salehe bin Oman akarudi. Alipofika kwao akawaita watu akawaambia, yeye si Hamisi Mchinondo sasa ila Salehe bin Omari, maana kasilimu. Akafanyiza karamu akachinja ng’ombe akawakirimu watu.
Kisha akawaambia, "Ndugu, mimi nimeona tunapotea bure, ni heri na sisi tuabudu Mungu. Maana mnawaona wale wenzetu wajomba, wanaabudu Mungu tu, kisha wanapata yote wanayotaka, basi na sisi ni afadhali tufanye kama vile. Na mimi nitakuwa mbele nitakalosema lolote itikieni, Amin."
Siku ya kwanza akaja Bwana Saleh bin Omari na kanzu yake. Akasimama panapo kibla akaanza kusalisha, na maneno aliyosema ni haya. Nchisali nasalia tumwa, chinuka chibiru china nluma. Maana yake; nikisali nasalia utumwa, nikiinuka kiuno chaniuma. Na watu huitika amin. Ikawa kuinama na kuinuka maneno hayohayo. Msikiti ukasitawi, watu wakazidi kujaa. Wakasali hivi kwa miaka.
Hata mwaka mmoja mvua ikanya kwawingi sana. Hata upande wa kibla wa msikiti ukabomoka kwa ile mvua kukawa wazi. Hata wakati wa kusali sala za Isha Imam akaenda zake panapo kibla akaanza kusalisha kwa maneno yake yale yale. Nchisali nasalia tumwa, chinuka chibiru china nluma. Watu wakaitikia, Amin, kama desturi. Mara ya kwanza wakaenda rakaa moja, hata wakaenda rakaa ya pili. Mara chui akaingilia pale palipobomoka, akaja akamkamata yule Imam. Na penye kibla ni ndani kidogo napo pana giza, nayo imekuwa magharibi, watu wameshughulika na sala hawakumwona chui.
Basi Imam akaanza kupiga kelele, "Alumee!" Watu wakadhani ni maneno ya sala, wakaitikia, amini.
Alumee! Wao wanaitika, "amin."
Alumee nenda! Amin.
Alumee nenda na tsui(chui)! Amin!
Alumee msihende(msidhani) mzaha! Amin.
Alumee nafa! Amin.
Alumee ndzoni(njoni)! amin ya sala wakaitikia, Amin Alumee, wao Amin. Alumee nenda! Amin! Alume nenda na tsui (chui)! Amin! Alume msihende (msidhani) mzaha! Amin! Alume nafa! Amin! Alume ndzoni (njoni) Amin!
Ikawa hivyo, na Imam Saleh bin Oman achukuliwa na chui. Hata watu wakitazama panapo kibla hawaoni mtu, Imam hayupo. Wakaenda kuangalia waona damu tu, wakafuata alimopita, lakini kwa kuwa ni usiku hawakuweza kwenda mbali. Wakalala hata asubuhi. Asubuhi wakafuata wee wakatafuta maiti imebaki kichwa tu, wakakichukua kichwa wakaja nacho mjini, wakakizika.
 
KISA CHA MTU NA WANAWE​


Palikuwa na mtu mmoja akaoa mke, akazaa watoto watatu wanaume. Na yule mtu hakuwa na kitu, rasilimali yake ilikuwa reale thelatha mia nazo kaziweka chini ya maliwato. Akakaa hata akapatwa na ugonjwa wake akafikiri kuwa mimi nina watoto watatu na mke hawa ndio warithi wangu na fedha hii haiwatoshi hawa. Afadhali niwarithishe kwa akili, kila, mtu asijue kuwa nimemrithisha mwenzake. Akamwita mke akamwambia, "Bibi, mimi siwezi, uhai wangu haba kuliko mauti na akiba yangu ni reale thelatha mia, na warithi ni wewe na wanao. Lakini nataka watoto wasirithi, sharti kwanza wakamrithi Sultani wa Mrisi (Mauritius), wakirudi huko ndipo warithi fedha."
Akakaa, hata hatimaye akamwita mwanawe mkubwa, akamwambia, "Mwanangu, mimi siwezi, naona uhai ni haba, na mauti mengi, lakini nikifa, mimi rasilimali yangu ni reale thelatha mia tu, nazo ziko chini ya maliwato, huo ndio urithi wako, wala usiwaambie nduguzo. Lakini nakutafadhalisha neno moja, usirithi kwanza mpaka uende ukarithi mali ya Sultani wa Mrisi."
Akakaa, akamwita mwanawe wa pili, akamwambia maneno kama yale aliyomwambia mwanawe mkubwa. Kisha akamwita mwanawe wa tatu, akamwambia maneno kama yale aliyowaambia wengine kwa siri.
Basi tena akawaacha kila mmoja anajishuku kuwa mimi napendwa kuliko wengine. Hatimaye baba yao akafa, wakamzika, wakakaa matanga wakaisha. Walipokwisha, yule mkubwa akaondoka usiku akaenda hata chini ya maliwato akafukua akaziona kama aliyosema baba yake, akazichukua. Na yule wa pili akaenda kufukua asizione, akaudhika sana, akasema, Kumbe baba kanihadaa Akarejea nyumbani. Na yule wa tatu vile vile akaenda akafukua asione kitu, akaudhika sana, akasema, Kumbe mze kanihadaa ila kwa hakika fedha ilikuwapo sijui aliyekwiba. Akarejea nyumbani akalala.
Hata asubuhi akawaambia wenziwe, "hamna habari? Baba aliniambia ya kuwa penye maliwato pana fedha reale thelatha mia. Nami nimekwenda tazama, sikuona kitu."
Na yule wa pili akasema vile vile, na mkubwa naye akasema vivyo hivyo. Yule mdogo akanena, "Lakini baba alisema tena fedha hii isirithiwe mpaka tukamrithi Sultani wa Mrisi. Basi aliyechukua yote ni batali, maana hakushika usia."
Basi wakapatana wote kutoka kwenda kumrithi Sultani wa Mrisi.Wakatengeneza mikate yao, na bisi, na vibuyu vya maji, walipokuwa tayari wakaondoka, mkubwa mbele, wa pili kati, mdogo nyuma.
Na vijana hawa walikuwa wamesoma vema sana wote watatu. Basi walipokuwa katika kwenda yule mkubwa akaona unyayo wa mnyama. Akasema, "Unyayo wa mnyama huu, na mnyama mwenyewe ngamia."
Wapili akasema, "Na ngamia huyu katwikwa pau za chuma." Wa tatu akasema, "Na ngamia mwenyewe amepita zamani yapata saa nzima."
Wakaenda hata mbele wakakutana na mtu, akawauliza,
"Je! wakina bwana, hamkunionea mnyama wangu?" Mkubwa akajibu, "mnyama gani?Ngamia, nini?"
Mtu akajibu, "Naam, ngamia."
Wa Pill akasema, "Na ngamia mwenyewe ametwikwa pau za chuma?"
Akaambiwa, "Ndiye hasa."
Wa tatu akasema, "Na ngamia huyo kapita zamani, yapata saa nzima?"
Yule mtu Akajbu, "Naam, ndiye."
Wakasema, Tumemwona hukoo.
Wakashika njia wakaenda zao.
Hata mbele chini ya mti wakaona alama. Mkubwa akasema, "Kitako hiki, nacho cha mtu."
Wa Pili akanena, "Na mtu huyu mwanamke."
Wa tatu akanena, "Naye ana mtoto mgongoni."
Walipofika mbele wakakutana na mtu.
Akawauliza, "Je, wakina bwana, huko mnakotoka hamkunionea mtu wangu?"
Mkubwa’ akajibu, "Mtu mke, nini?"
Akaambiwa, "Naam.
Wa pili akasema, "Ana kekee ya dhahabu?"
Akaambiwa, Eh! bwana mdogo."
Wa tatu akanena, "Ana mtoto mgongoni?"
Akajibu, "Hasa."
Wakanena, Huyoo! tumemwacha huko.Wakaenda zao.
Hata mbele wakamkuta mtu amechinjwa, hana kichwa, kimebaki kiwiliwili tu.
Mkubwa akasema, "Mtu huyu kachinjwa, naye mwanamume."
Wa pili akasema, "Naye ana sharafa ya ndevu."
Wa tatu akasema, "Mtu mwenyewe kizee, umri wake yapata miaka sabini au themanini."
Wakaenda hata mbele wakakutana na mtu, naye ni mwanawe yule aliyechinjwa. Akawaambia, "Je! Wakina bwana hamkunionea mtu wangu huko mtokako?"
Mkubwa akasema, "Mtu mume, nini?"
Akaambiwa, "Naam."
Wa pili akasema, "Naye ana sharafa njema ya ndevu?" Akajibu, "Naam, ndiye."
Wa tatu akasema, "Naye mzee sana, bwana, apata umri wake miaka sabini, themanini hivi?"
Akanena, "Naam, ndiye hasa."
Wakanena, "Huyoo, anakwenda huko.
Kumbe yule mtu kwenda mbele amkuta mzee wake amechinjwa
Akanena, "kumbe! wale wamemwua mzee wangu."
Na wale vijana watatu wakashika njia mpaka wakafika kwa Sultani wa Mrisi. Sultani akawakaribisha vizuri, akawapokea kwa mikono miwili Akawapa nyumba wakakaa. Hata kwa Siku ya tatu Sultani akataka kuwakirimu wageni wake. Akatuma mtu kwenda shamba kwa msimamizi kuchukua mpunga, na mbuzi aliye nona.
Ukaja mpunga ukatwangwa, na mbuzi akachinjwa. Ukapikwa wali mwema. Wakaenda wakaitwa wageni kwa Sultani. Wakapewa maji wanawe ili wale chakula.
Mkubwa akasema, "Wali huu unawalakini."
Wa Pili akasema, "Hata kitoweo kina Walakini."
Wa tatu akasema, "Hata Sultani mwenyewe naye ana Walakini."
Watwana waliosikia maneno haya wakaudhika, wakaenda wakamwambia bwana wao maneno haya, na ya kuwa hawakula chakula. Sultani akaudhika sana, akaona, vijana hawa hawana adabu. Juu ya kuwakirimu namna hii, bado wananitukana.
Akanena, "Kawaiteni hawa vijana."
Wakaitwa wakaja, akawaambia, "Namna gani hii mliyofanyiza ninyi? Mimi nimewakirimuni na ninyi mwanitukana?"
Wale vijana wakajibu, "Tumekutukanaje, Sultani?" kabla Sultani hajawajibu mara yakaja mashtaka ya yule mtu mwenye ngamia njiani waliyekutana naye njiani. Akashtaki kwa Sultani ya kuwa watu hawa wamekwiba ngamia wangu. Na Sultani akawaambia, "Kwa nini ninyi mmekwiba ngamia wa huyu?"
Wale vijana wakanena, "Tumemwibaje, Sultani?
Ametuona naye?"
Mwenye ngamia akasema, "kwa sababu waliniambia alama zake zote. Basi wamezijuaje hao kama hawakumwona?"
Sultani akasema, "mmesikia basi jibuni sasa, mmezijuaje alama za ngamia, nanyi hamkumwona?" wakajibu hivi:
mkubwa, "Mimi nilimjua huyu ni ngamia kwa nyayo zake ,nyayo za ngamia hupotea?"
Wa pili akasema, "Mimi nalijua kuwa amechukua pau za chuma kwa kuwa nyayo zake zilikwenda chini sana. Nikajua huyu kachukua kitu kizito, na hapana kizito kama pau ya chuma."
Wa tatu akasema, "Mimi nalimjua kuwa alipita zamani, kwa kuwa nyayo zake zilikanyagwa, saa nzima, kwa kuwa nyayo zake zilikanyagwa na watu waliokuja nyuma na watu wenyewe tuliwaona njiani, huko nyuma kabisa lakini ngamia hatukumwona."
Sultani akanena, "Hakika hawa hawakuiba ngamia wako nenda zako."
Akaja yule mwenye mke naye akashtaki, akasema, "Bwana, hawa wamenichukulia mke wangu."
Sultani akanena, "Mnasikia ninyi, kwa nini kuchukua mke wa watu?"
Wale wakanena, "Hasha, bwana, sisi hatukumchukua mke wa mtu."
Mwenye mke akasema, "Mbona basi wameniambia alama zote za mke wangu, ikiwa hawakumwona?"
Mkubwa akasema, "Mimi naliuliza tu mtu mwenyewe mtu mke? Huko ni kuiba, bwana?"
Wa Pili ikasema, "Mimi nalijua kuwa huyu mwanamke, maana naliona kekee ya dhahabu kule alikokaa chini ya mti, lakini sikuigusa."
Wa tatu akasema, "Mimi nalijua kuwa ana mtoto mgongoni, maana asingeondoka hana kekee yake, ila alimpa mtoto wake uichezea, ikamponyoka, mama yake hana habari."
Sultani akanena, "Kweli maneno yao, hawakumwona hawa."
Akaja Kijana aliyechinjiwa baba yake, akanena, "Hawa wamemchinja baba yangu." Sultani akanena, "Jibuni ninyi, mmemuuaje baba yake huyu?"
Wale vijana wakanena, "Hatukumwua, bwana."
Yule kijana akanena, "imekuwaje basi kunipa wasifu wake wote?" Mkubwa akasema, "alikuja huyu bwana kututuliza akina bwana mmenionea mtu wangu? Mimi nikamwambia mtu gani, bwana?Mtu mume? Akanena, naam, huko kuuwa bwana?"
Wa pili akasema, "Mimi nalimjua kuwa ana sharafa ya ndevu kwakuona manyoya mengi kifuani, nikajua kuwa hakosi kuwa n sharafa ya ndevu, maana hii ni maujudi."
Wa tatu akasema, "Mimi nalimjua kuwa ni mzee wa miaka sabini au themanini kwa kuona damu yake. Ilikuwa haina nuru tena, ina maji nikajua kuwa hii ni damu ya mzee."
Sultan akasema, "Kweli maneno yao, hawakumwua hawa, nenda zako."
Sultani akashangaa kwa akili zao wale vijana, lakini bado hawajajitakaSa. Imebaki habari ya Sultani mwenyewe.
Sultani akawaambia, "Ehe! Sasa nawauliza mimi, Kwa nini mkafanya wali wangu kuwa na Walakini, na mnbuzi kuwa na Walakini, na mimi kuwa na Walakini?"
Mkubwa akasema, "Mimi nimejua kuwa wali una walakini, kwa kuwa mchele wake mrefu, mnene. Nikajua mpunga huu ulipandwa makaburini, maana ndipo penye rutuba sana. Basi chakula cha makaburini hakinaWalakini?"
Wapili akasema, "Nalijua kuwa nyama ina Walakini kwa kuwa nyama yake ilinona sana, nikajua kuwa mbuzi huyu malezi yake si ya mbuzi wengine."
Wa tatu akasema, "Mimi nimejua kuwa Sultani una Walakini, kwa sura."
Basi Sultani akakasirika sana. Akamwita nokoa, akamuuliza habari za mpunga. Akanena, "Naam, bwana, mpunga huu ulipandwa makaburini, wala si uongo."
"Na habari ya mbuzi je?"
Akasema, "Naam, mbuzi yule mama yake alikufa alipokuwa mdogo akanyonya maziwa ya punda!"
Sultani akaona kweli, mbuzi huyu kama punda. Kisha akamwita mama yake akamfunga panapo nguzo akampiga akamwambia, "Sharti uniambie kweli. Hawa wanasema mimi nina Walakini, namna gani? Wewe ndiye unayejua."
Mama yake akamwambia Kweli, "mwanangu, wewe ni mtoto wa mume wangu wa kwanza aliyekuwa Baniani, si mtoto wa marehemu Sultani."
Sultani akaona vijana hawa wana akili wala hawana mfano wao. Mahali pa kuwafunga akawapa zawadi nyingi, akawaruhusu kwenda zao. Lakini pamoja na hayo ndani ya moyo wake hakutaka kuwaacha wale watoto warudi kwao wazima kwa vile walivyomfedhehi kumtambua kuwa yeye si mtoto wa marehemu Sultani.
Alitaka kuwaua, ila hakutaka kuwaua kwa dhahiri. Basi wakati wa kuondoka akatwaa majoho mekundu akawavika wote watatu. Kisha akatwaa majoho meusi akawavika wanawe watatu, akawaambia, "Nendeni muwasindikize wageni." Akawaacha kwenda zao. Mara nyuma akatuma askari.
Akawaambia, "Nendeni zenu, wafuateni wale wageni, mkiwakuta, waueni vijana watatu wenye majoho mekundu."
Kumbe! wale vijana walipokwenda mbele wakatambua kuwa pana neno hapa. Wakawaambia watoto wa Sultani wa Mrisi, ya kuwa, "Baba yenu ameharibu. Majoho mekundu ni rangi ya kifalme si majoho ya kuvaa sisi. Majoho meusi ni ishara ya msiba, ndiyo yanayotuelekea sisi tuliofiwa na mzee wetu karibu. Basi yafaa tubadili."
Wakabadilisha yale majoho. Wale watoto Sultani wakavaa majoho mekundu. Na wale askari waliambiwa kuwa mkiwakuta wale vijana waueni wenye majoho mekundu.
Basi askari walipowakuta wakatimiza amri yao wakawauawenye majoho mekundu. Kumbe! ndio watoto wa Sultani. Na wale vijana watatu, wakawarudisha kwa Sultani. Sultani alipowaona wanakuja wamevaa majoho meusi, akajua kuwa werevu wao.
Akawapa tena malinyingi mno.
Wakatimiza maneno ya baba yao.Wakamrithi Sultani wa Mrisi kwanza, kabla hawajarithi mali ya baba yao. Kisha wakarudi kwenda kurithi mali ya baba yao.
 
HADITHI YA MTOTO WA SULTANI NA TAJIRI​


Aliondoka Sultani, akafanya urafiki mkubwa na Tajiri. Sultani alikuwa na mtoto mume, na tajiri alikuwa na binti. Hata siku moja Sultani akamwambia tajiri, "Mimi naona shauri lililo jema ni kuwaoza watoto wetu, wangu na wako."
Tajiri akasema, "Maadam unapenda wewe SuItani mimi nina hiari gani?"
Basi wakazatiti arusi. Sultani akamwambia tajiri, "Nataka tufanyize arusi, hata watu wakae wakikumbuka ya kama hawajaona nyingine."
Basi tajiri akatoka akaalika watu, walio karibu, Waliowahusu, ndugu, na majirani, na walio mbali, kusi na kaskazi, magharibi na mashariki. Watu wakaja hawana idadi. Akaambiwa Sultani kuwa watu wamekwisha kuwako. Basi ikafanyizwa arusi mwanzo siku ya Jumatano.
Karamu ikawa kubwa ajabu, mji ukawa hausikilizani kwa ngoma na furaha ya arusi. Asiye na mwana akaeleka jiwe.
Watu wakawa huria tena wa ndani nje, na wa nje ndani.Watu hawaoni, hawasikiani. Mizinga ikapigwa haina idadi, hata watu wakaziba masikio. Muda wa siku saba hapana apikaye wala apakuaye, wote chakula kwa Sultani naTajiri. Baada ya siku saba binti Tajiri akapelekwa kwa mumewe. Wakakaa pamoja kwa miezi saba. Baada ya miezi saba mtoto Sultani akawaita watwana wake, akawaamrisha kuchimba shimo uani katika nyumba yake.
Akaondoka yule kibwana, akamchukua mkewe ili kwenda kutazama ile kazi ya shimo.Walipofika, mume akamwambia mkewe achungulie ndani atazame kama kumekaa vema, yule mume akazunguka kwa nyuma, akamshika mabega, akamsukuma ndani ya shimo kwa nguvu, kisha akaenda zake.
Hata kwa siku ya pili akaja kumwangalia mkewe mle shimoni Akamwita, "binti tajiri." Binti tajiri akaitika, "Lebeka."
Akamwuliza, "Je, hujafa bado?"
Akamjibu, "Mimi sifi, ila nizae watoto wako watatu."
Yule kibwana akamcheka sana, "akamwambia,
Utazaa wapi watoto wangu, nawe humo shimoni?"
Yule mume akarudi nyumbani.
Akaagiza makanda matatu ya mtama, na moja la mahindi, na kibuyu Cha maji na kumpelekea mle shimoni.
Ikawa kila siku anakwenda asubuhi na jioni,ili kumtazama kama amekufa.
Naye kila akimuuliza, "Je hujafa?"
Naye humjibu majibu yale yale.
Hata zilipotimia siku saba, mtoto wa Sultani akaona ya kuwa hafi huyu, akaaga ruhusa kwa baba yake asafiri. Baba yake akamruhusu. Akafunga safari yake, akachukua watu aliotaka, na vitu alivyotaka, akaondoka. Alipofika nchi ya mbele, akaacha baadhi ya watu wake pale.
Yeye akaazimu kwenda nchi iitwayo Manga Komamanga. Huku nyuma kwa mkewe akaja buku na panya.
Wakamwuliza yule mwanamke, "Unafanya nini humu shimoni?"
Akawajibu ya kuwa
"Haya ni ya uliwengu." wakamwambia, "ebu! Tueleze hayo masaibu yako."
Yule mwanamke akanena, "Mume wangu ni mtoto wa Sultani, naye naliozwa kwa radhi za wazee, Baada ya muda wa miezi saba kupita akanitia humu shimoni ili kutaka kuniua bila sababu."
Wakamuuliza, "Je kwenu, unakujua?
Akanena, "nitakujuaje nami nimo ndani ya shimo?" Wakamwambia, "Je! Atokeapo mtu akakupeleka kwenu utampa vyakula hivi? (Yale magunia ya mtama na maindi)."
Yule mwanamke akasema, "atakayenipeleka kwetu, vyakula hivi vyote na atwae yeye."
Buku na panya wakafanya jitihada ya kuchimba hata uvunguni pa kitanda cha mama yake yule binti tajiri. Walipokwisha wakaja wakamchukua yule mwanamke wakampitisha katika ile njia waliyoichimba mpaka uvunguni pa kitanda cha mama yake.
Hata yule mtoto akamwamsha mama yake. Mama yake akashtuka sana, akamwambia "nani wewe."
Akanena, "mimi binti yako." Akamwambia, "umepita wapi na milango yote imefungwa?"
Akamwambia, "mama, waniuliza hivyo, Kwani wadhani natokea nyumbani kwangu? Kaa kitako nikuelezee habari yangu, leo yapata mwezi tangu nimetoka kwa mume wangu. Yule mume amekuwa si mume ila balaa. Aliagiza shimo lichimbwe, kisha akanitumbukiza ndani. Naye akawa anakuja kunitazama ajue kuwa mimi mzima au nimekufa, alipoona nakawia kufa akanikimbia."
Mama yake akajibu, "ah kumbe Safari ile ni kukukimbia wewe?" Kisha akamwita mumewe akampa habari hii yote.
Wakasikitika sana kwa habari hii, yule mtoto akasema, "sasa nisikilizeni mimi, kitendo nitakachomtenda mimi kitapita hiki alichonitendea mimi. nitafutieni chombo, mnipakilie mali kwa wingi, ila mabaharia nataka wanawake, na mavazi yao meusi, kisha mkipeleke kokoni."
Yule mtoto mwanamke akapiga kipande, akatambua kuwa nikitoka hapa nitampata mahali kadha wa kadha, basi akaingia chomboni na watu wake, akasafiri muda wa siku kumi na mbili. Akapiga kipande tena, akaona ya kuwa muda wa siku sita atamtia mkononi
Hata siku ya tano Yule mtoto mwanamke akafanyizia mazingaombwe yake ikawa chombo cha mtoto waSultani kikapigwa na dhoruba asijue aendako, hata siku ya sita akamtia mkononi, wale mabaharia wa mtoto wa Sultani wakakiona chombo kimewakabili kinakuja kasi.
Wakamwambia bwana wao ya kuwa kuna chombo kinakuja, na yule mtoto wa tajiri kavaa kiume, kajifunga na silaha, kashika na mkuki mkononi, amesimama juu ya staha. Yule mtoto wa Sultani akasema, Loooh masalale! Jitu gani hili mwenda usiku kuamkia mchana! Chombo cha yule mwanamke kikapita kikatatongulia mpaka Manga Komamanga, ndiko alikokuwa akienda Yule mtoto wa sultani.
Yule mtoto mwanamke alipofika Manga Komamanga, chombo chake akakitia kokoni. Akaandika barua kwa sultani wa nchi. Sultani alipoisoma akapeleka watu wakaenda kumchukua Yule mwanamke.
Alipofika kwa sultani akamweleza sultani maneno yake, akamwambia nyuma yangu kunakuja mtu nami nina visa naye. Atakapofika hapa lazima atataka kuposa na mimi nataka unifanye binti yako, akija umwambie ya kuwa huna binti ila huyu, naye kaolewa chuo kimoja. Ukitengenea habari hii nitakupa reale elfu.
Mara mtoto wa sultani akafika katika nchi ya Manga Komamanga, akatia nanga bandarini akapiga mizinga. Hata siku ya tatu akaenda kumwamkia Sultani wa Manga Komamanga. Akakaribishwa vizuri. Muda wa juma nzima kupita akaenda kwa Sultani kumposa binti yake.
Na Sultan hakukasiri, akamwambia, Mimi nina binti mmoja tu, naye kaolewa chuo kimoja.
Yule kibwana akakubali akanena, "niko tayari."
Ikatengenezwa arusi akaoa.
Mume akaingia nyumbani. Akakaa muda wa mwaka, mkewe akazaa mtoto mwanamke. Baba yake mtoto akamfulia vyombo vya dhahabu ili pambo la mtoto. Na mwaka huu wote waliokaa pamoja yule mume hakumtambua mkewe, kuwa ndiye yule aliyemtupa shimoni.
Baada ya mwaka mtoto wa Sultani akaomba ruhusa kwa mkwewe, Sultani wa Manga Komamanga ili asafiri. Sultani akamwuliza, "Unataka kwenda wapi?"
Akamwambia, "Nataka kwenda nchi iitwayo Manga Pera."
Akamkabidhi mkewe na mtoto, akasafiri. Na yule binti Tajiri akamwambia baba yake wa kupanga ya kuwa, "Na mimi nataka kusafiri nifike Manga Pera."
Akamwambia, "Mume wako akirudi upesi akakukuta haupo je, nisemeje?"
Akamwambia, Haya ni juu yangu. Akatoka naye binti Tajiri katika chombo chake akasafiri. Wakakutana huko nje ya bahari. Binti Tajiri akampiga mtoto wa Sultani kwa mazingaombwe; akampita vile vile kama kwanza, akatangulia yeye kufika Manga Pera.
Alipofika akafanya kama yale aliyoyafanya Manga Komamanga. Na mtoto wa Sultani sababu ya kwenda katika nchi hii, ni kuoa binti Sultani. Basi alipofika hakukawia, akasema haja yake ya kuwa anataka kumposa binti Sultani.
Na Suitani akamwambia ya kuwa ana mtoto mmoja tu, naye kaolewa vyuo viwili.
Akaambiwa kama akihiari ataozwa. Akanena, nimekubali, Aakaozwa
Hata muda wa mwaka mkewe akazaa mtoto mume, akamfulia naye vyombo vyake akampa.
Kisha akaaga kwa yule mkwewe kuwa yeye anasafiri, anataka kwenda nchi iitwayo Manga Ndimu. Na binti tajiri aliposikia ya kuwa mumewe anakwenda Manga Ndimu, akamngoja aondoke naye akafunga safari akaenda upande ule ule. Akafika yeye kama kawaida yake. Akafanya yale yale maana alifahamu ya kuwa anafanya inadi hii makusudi aje kumbugudhi binti Tajiri akiwa atamkuta hai. Na yule mwanamume alipofika Manga Ndimu akafanya kama yale yale aliyofanya nchi nyingine.
Akamwoa tena yule yule akazaa naye mtoto mwanamume.
Naye pia akamfulia vyombo vyake. Kisha akafunga safari kurudi kwake. Na mkewe na mtoto wake akawaacha kule kule (alivyodhani yeye). Maana anataka mtoto wake mpaka akue. Kumbe binti Tajiri akatoka naye, wakapishana baharini vile vile.
Na yule mwanamke kila nchi aliyopita akamchukua mwanawe.
Akafika mpaka mjini kwao. Punde si punde mtoto wa Sultarü akaja. Ikawa furaha kubwa katika mji, mtoto wa Sultani amerudi Ikapigwa mizinga sana. Yule mtoto mwanamume akamweleza baba yake habari zote za safari. Na binti Tajiri naye akawaeleza wazee wake yote aliyotenda. Lakini akawaambia, Sina budi kwenda kukaa kule kule shimoni, mume wangu akija anikute.
Mtoto wa Sultani alipokwisha pumzika akaenda kule shimoni kumtazama mkewe. Akamwita,
"Binti Tajiri! Binti Tajiri!" Akaitikia, "Lebeka."
Akamwuliza, "Je! u hai bado?"
Akamjibu, "Ni hai bado, sikukuambia kuwa sifi mpaka nizae Watoto wako watatu?"
Akamwambia, "una wazimu! uzae wapi watoto wangu?Mwenzako huko nitokako nimeoa akina binti Sultani watatu na bado nimezaa nao, wewe utachelewa humohumo shimoni." Akatoka Akaenda zake.
Yule binti Tajiri naye akatoka akaenda kwa wazee wake. Akawaambia wazee wake, Nataka mnifanyie karamu kubwa, niwaalike watu wengi kama muezavyo. Nataka Sultani na mwanawe pia wahudhurie. Wakafanyiza karamu kubwa, wakaalika watu wengi wakaja. Akaja na Sultani na mwanawe.
Wakakaa kila mtu kwa cheo chake. Watu wakala chakula, wakaisha. Walipokwisha kula watu wakauliza, "Maana yake nini karamu hii?"
Yule binti Tajiri akasema, "Ngojeni nitawaeleza."
Akaingia ndani, akawatwaa wale watoto wake watatu, kila mtoto amemvika lebasi ya nchi yake, na pambo alilofuliwa na baba yake, na kila pambo mbalimbali.
Akawaleta mbele ya watu.
Akawapitisha kwa watu wote ili wawaone. Kisha akawaambia, Sasa nendeni kwa baba yenu. Watoto wakajinadi wote: Mimi fulani bin fulani au bin fulani. Wakaenda mpaka alipo baba yao. Binti Tajiri akamwuliza mtoto
Sultani, "Je! watoto wa nani hao?" Mtoto wa Sultani akajibu, akanena, "Kwa dalili zote nawaona kuwa wangu."
Wakaulizwa wale watoto mmoja mmoja walipozaliwa. Wa kwanza akajibu, "Mimi nimezaliwa Manga Komamanga."
Wapili akajibu, "Mimi nimezaliwa Manga Pera."
Watatu akajibu, "Mimi nimezaliwa Manga Ndimu."
Binti Tajiri akawauliza, "Mama yenu nani? Wote wakajibu, Wewe, BintiTajiri."
Akamwambia mumewe, "Je! sikukuambia, Sifi mimi mpaka nizae Watoto wako watatu?"
Mtoto wa Sultanu akanena, "Naam umenishinda, binti Tajiri."
Wakakaa pamoja, mtu na mkewe raha mustarehe.
 
WEZI STADI​


Hapo kale palikuwa na wezi wawili, mwizi wa mchana, na mwizi wa usiku. Huyu mwizi wa mchana akiiba Unguja, na huyu wa usiku akiiba Mrima. Wote wawili walikuwa mafundi wa wizi kupindukia. Siku moja yule mwizi wa Mrima akasema, Nitafanya safari niende zangu Ungujà nikafanye kazi yangu huko, maana ndiko kwenye matajiri wengi.
Basi akanauli chombo akavuka, Akafanya kazi yake ya kuiba, na kila alichokipata akiweka pangoni. Kumbe! pango hili ni pango aliokuwa akikaa, na kuficha vyombo vyake yule wa Unguja. Lakini kwa kuwa mmoja wa usiku, na mwingine wa mchana hawakujuana, maana hawaonani. Wakakaa hali hii kwa muda wa miaka saba.
Hata siku moja yule mwizi wa mchana akasema, Leo nitapumzika siendi kuiba. Hata alasiri akatoka. Akatembeatembea mle pangoni, akamkuta ‘yule mwizi wa usiku amelala.
Yule mwizi wa mchana akasema. Huyu amekuja kunifelisha mambo yangu, nitamuulia mbali. Akang’oa shembea lake ampige nalo dharuba moja. Lakini akasita. Hata mwisho akamshika mkono, akamwuliza, "Nani wewe?"
Yule mwizi wa usiku akaamka akitetemeka, "Mimi hapa bwana ah! nimetubu, siibi tena." Akamwambia, "Mwizi wewe eh?" "Eh, bwana, bali sasa siibi tena, basi, nimetubu."
Akamwuliza, "Tangu lini upo hapa wewe?"
Akanena, "Yapata miaka saba sasa. Akamuuliza, "Vitu ulivyokwiba viko wapi?" Akaenda akamwonyesha anakoweka vitu. Akaviona vitu vingi mno ajabu. Akasadiki kuwa huyu mwizi kweli. Aliposadiki kuwa mwizi kweli, wakashikana mikono, ukawa urafiki mkubwa. Walipokaa kitako kuelezana visa vya uwizi wao, ukaingia ubishi, Nani stadi wa kuiba. Kila mtu akasema, Mimi zaidi.Wakapatana kuonyeshana ustadi wao.
Akaondoka yule mwizi wa mchana akatwaa udongo akauviringa vidonge vidonge, akavipaka rangi ya lulu, akapita akitembeza. Ikawa hii ndiyo kazi yake kwa siku nyingi. Hatima ule udongo akautupa pwani.
Hata siku moja akajipamba sana, akapanda farasi, na kuweka watwana mbele na nyuma. Akaenda hata nyumba ya tajiri mmoja, akapiga hodi, akaitikiwa, Karibu.
Akaingia ndani akakaa kitako.
Akamwuliza yule tajiri, "Unazo lulu nzuri hapa?"
Yule tajiri akajibu, "Ninazo."
Akamwambia lete, "zikaletwa lulu nzuri nyingi apate kuchagua mwenyewe." Yule mwizi ikawa kazi kuzigeuza na kuzitazama zile lulu. Hata mwisho mwenye mali akachoka. Akamwambia, "Kama wewe unataka kununua lulu, nunua; la, hutaki, nipe niweke, maana nina kazi nyingine mimi." Mwizi akamjibu, "Unasemaje?Unasema ukitaka nunua, kwani sasa za nani hizi?"
Wakagombana pale kikomo na kiasi, hatimaye wakachukuana sheriani. Walipofika sheriani, akitazamwa yule mwizi sura yake na lebasi yake, wakaona hakuelekea wizi.
Na zaidi kuliko hayo wakatokea watu walioshuhudia kuwa, Huyu ni mchuuzi wa lulu, siku kadha wa kadha amepita akitembeza lulu. Kadhi akampa haki mwizi, akanena, "Hizi lulu ni zake huyu." Mwizi akaondoka akaenda zake.
Akamwambia yule mwizi wa usiku, "Unaona kazi hiyo?" Mwizi wa usiku akamwambia mwenziwe, "Unajuaje kuiba wewe ? ngoja nikuonyeshe kuiba."
Akatafuta misumari yake saba, na nyundo na kenge, akajifanya maskini, Akaondoka akaenda hata mlangoni kwa Sultani, akawakuta mabawabu wamejaa tele, wakamwuliza, "wataka nini?"
Akawajibu, "Nataka kazi kwa Sultani"
Wakamwabia, "leo hupati kumwona Sultani, labda kesho, maana umekuwa usiku tena Kwa hivi sasa lala hapa barazani mpaka kesho."
Yule mwizi akatikia. "Ee walah." Yule Sultani alikuwa na saa kubwa mno ya ajabu, ikipiga mji wote hutetemeka na watu hawasikiani. Yule mwizi akalala hata saa sita ya usiku akampeleka kenge wake kupeleleza. Watu wote wamelala wakati huu.
Basi akaitwaa misumari yake saba akaishika mkononi, na nyundo, akangoja mpaka ipige saa saba. Hata ilipoanza kupiga saa saba, ikipiga Ngool Naye akaukomelea msumari ukutani wakati ule ule ili watu wasisikie.
Ikipiga Ngoo ya pill, akaukomelea msumari wa pili. Akafanya hivyo mpaka yote saba ikaisha. Kisha akatumia misumari hii kuwa ndiyo ngazi ya kupandia. Akapanda hata juu chumbani kwa Sultani, akamkuta amelala yeye na mkewe. Akamvua Sultani pete yake ya dhahabu, akamvua na Bibi kidani chake cha almasi aliyoivaa shingoni, thamani yake yatosha kununua usultani mzima.
Akatwaa na fedha zilizokuwa ndani ya makasiki azimwagamwaga, kisha akaenda zake. Alipofika kwa mwenzie akamwambia, "Unaona namna ya wizi, wewe unaonea maskini, mimi huiba kwa Sultani, na bado nitatenda zaidi kuliko hivi."
Sultani alipoamka asubuhi, akaona pete yake haimo kidoleni, na kidani cha Bibi hakimo shingoni, na fedha zimemwagwa chekwachekwa. Akajua kuwa kulikuja mwizi mkubwa
Sultani akatoa amri mwizi huyu atafutwe. Tena mtu asitembee usiku, atakayeonekana anatembea ndiye mwizi. Yule mwizi aliposikia amri hii, akatwaa kikombe chake na rupia zake kumi na tano akaenda hata dukani kwa mshihiri akabisha.
Akaulizwa, "Nani wewe unayetembea usiku, hukusikia amri, Watu hawatembei usiku?" akanena, "Ah! Nifanyeje nami nataka mafuta, nimeleta rupia zangu kumi na tano nataka kuweka rehani, kesho nitakuja kukomboa. Mshihiri kusikia rupia kumi na tano roho ikamtoka. Akatoa mikono dirishani iii apokee.
Yule mwizi akaushika mkono akaukata. Akakimbia akaenda zake. Akaenda kwa mwenzie akamwambia, "Unaona? Bado, nitatenda kupita haya." Akaenda kupika mikate mitatu, akatia kila namna ya kileo. Kisha akavaa kike, akachukua ile mikate akatoka.
Askari wakamuuliza, "Nani wewe?"
Akajibu, "Miye, akina Bwana."
"Unakwenda wapi?"
Akanena, "Nimechukua mikate, maana naliweka nadhiri, pindi mume wangu arudipo salama, nitapika mikate nipeleke msikitini. Basi sasa nakwenda kuondoa nadhiri yangu. Lakini nadhiri yangu haina haja ya msikitini, hata mkila ninyi hufaa."
Wale askari wakaitwaa ile mikate wakala, kabla hawajadiriki kwisha wakalewa wote, wakalala usingizi mzito. Yule mwizi akazichukua bunduki zote za askari, na panga zao, akaenda zake. Sultani aliposikia ya kuwa askari wameibiwa bunduki na panga zao zote, akaghadhibika sana. Akanena, "Huyu amekuwa si mwizi tena, ila stadi. Akikamatwa au akijileta mwenyewe nitampa enzi bora." Basi Sultani akazidi kuweka watu waulinde mji, na kuvizia ili wamkamate mwizi huyo. Na amri ya kutembea usiku ikazidi kuwa na nguvu.
Hata siku moja jemadari mmoja alipokuwa anazunguka usiku akakutana na huyo mwizi akamkamata. Akamwambia, "Leo Umefika, hutoki hapa.Wewe ndiye mwizi unayesumbua mji mzima." Akautwaa mkono wake akaufunga pamoja na wake. Wakalala Hata usiku wa manane, watu wamelala akafanya jitihadi akafungua zile pingu. Akatwaa ule mkono wa yule Mshihiri (maana alikuwa nao mfukoni) akaufunga kwa pingu pamoja na ule wa Jemadari, akaondoka akaenda zake.
Asubuhi yule jemadari alipoamka akaona mwizi hayupo, anaona kipande cha mkono amefungiwa.
Akanena sasa na atafutwe mtu aliyekatika mkono, maana ndiye mwenye mkono huu. Akapatikana yule Mshihiri akabanwa vikubwa. Akachukuliwa kwa kubururwa, na kupigwa, na watu wakimzomea
Yule Mshiriki akajaribu kusema, "Eh! jamaa siye mimi." Akaambiwa, "Maneno gani hayo, mkono Wako si huu?"
Akanena, "Kweli, lakini na mimi nimekatwa."
Sultani akamhoji sana, akaona kweli, Huyu siye, "mwacheni," nao wakamwacha.
Sultani, akanena, "Leo nitangoja mji mimi mwenyewe peke yangu." Hata usiku Sultani akatandika farasi wake, akawa anazungukazunguka katika mji.
Yule mwizi anazo habari kama leo Sultani anangoja mji mwenyewe. Basi akaondoka kule pangoni, akavaa magunia akienda zake mpaka kwa Mhindi, akabisha hodi. Yule Mhindi akamwuliza, "Nani wewe?"
Yule mwizi akajibu, akanena, "Mimi hapa maskini, tangu juzi sijui riziki tumboni."
Mhindi akamwambia, "Hukusikia amri kwamba watu hawatembei usiku?"
Mwizi akasema, "Nifanyeje, nami hali yangu dhaifu, hata kama ningemwona Sultani mwenyewe ningemwomba anipe chakula tu. Na wewe kama hutaki kunipa chakula bure, nipe kazi nitende nipate chakula."
Mhindi akamwambia, "Haya, pita ndani. Alipoingia ndani akampa ngano kusaga. Akamwambia, "Saga ngano hii mpaka asubihi, utapata thumuni." Akaingia akapewa ngano kuisaga, akawa anasaga ngano, na mlango akaacha wazi yule Sultani akawa anatembea katika mji.
Hata alipopita pale, akaona mlango wazi, na yule kizee anasaga. Sultani akanena, "Nani wewe? Mbona miango wazi hivi?
Mwizi akasema, Kweli, mjukuu wangu, mbona na wewe unatembea usiku hivi?"
Sultani akasema, "Mimi nakuuliza wewe mbona kuacha mlango wazi?"
Mwizi akasema, "Eh! mjukuu wangu, mimi nakuhofia wewe unayetembea usiku, si uzuri
Baba, hukusikia amri?"
Na Sultani akanena, "Kweli hayo, lakini mbona kuacha mlango wazi na mji umengia wezi siku hizi?"
Mwizi akasema, "Kweli na hivyo, sasa hivi kapita mmoja, kaenda huku." Mara yule Sultani akashika njia kumfuatia yule mwizi. Akamtafuta asimwone,
Akarudi pale pale akamkuta kizee anasaga ngano vile vile.
"Je? Baba umemwona?"
Sultani akanena, "Sikumuona.
Mwizi akasema, "Nadhani umesikia vishindo vya farasi amekwenda upande huu."
Basi Sultani akamfuata tena asimwone. Akarudi tena pale pale Yule mwizi akanena, "Wajua Sultani, mwizi huyu atakuudhi.
Amepita hapa sasa hivi amekwenda huku. Lakini sasa nitakupa shauri. Huyu farasi nipe mimi, na hizi nguo nipe mimi. Twaa haya magunia yangu uvae, hatakawia, atakuja sasa hivi, basi akija, mfunge. We kaa kitako usage hii ngano tu, asikutambue." Sultani akakubali, akampa nguo zake, na farasi wake, yeye akavaa gunia, akakaa kitako akisaga ngano.
Yule mwizi akachukua vile vitu akazunguka nyumba akajifanya kama anaenda kukaa upenuni, huyoo akaenda zake. Sultani akabaki akisaga ngano, akangoja hata asubuhi, asimwone mtu yeyote. Hata asubuhi kulipokucha, Mhindi mwenye nyumba akaja akamkaripia sana, maana hakumjua kuwa ndiye Sultani. Akamwambia, Ngano uliyosaga iko wapi? umekaa hapa usiku kucha bure? Akampiga kofi. Akataka kumuongeza la pili, Sultani akanena, "Wanijua mimi?" mhindi akasema, "Sikujui. Akanena, Mimi Sultani."
Mhindi akamwambia, "Jinsi gani basi, Bwana, kunijia usiku na kutaka kazi kwangu?"
Sultani akanena, "Siye mimi niliyekuja kutaka kazi usiku."
Sultani akamweleza mambo yote yaliyopita usiku, Mhindi akashangaa. Sultani akaenda nyumbani kwake, wala hakujua namna yakumpata mwizi huyu.
Lakini siku moja walikuwa wamelala wote wawili pangoni wakaja askari wakawakamata. Wakawapeleka kwa Sultani. Sultani akafurahi sana, akawaambia, "Ninyi mlidhani mtaweza kufanya kazi yenu ya kuiba siku zote bila kukamatwa? mlikosea sana."
"Siku moja kila mwizi hukamatwa, naye hupata adhabu kali. Na ninyi, kwa sababu mu wezi wakubwa, mtapata adhabu kubwa, ndiyo kufa.
Basi akawaita askari wakawaua wale wezi pale pale mbele ya Sultani.
 
Back
Top Bottom