EMT,
..kuna mabalozi ambao huteuliwa toka nje ya serikali, kama Balozi Masilingi, Balozi Paul Bomani, Balozi Omar Mapuri, ... je hao nao mamlaka yao ya nidhamu ni Chief Secretary, au wanaweza kuchukuliwa hatua za kinidhamu na Chief Secretary?
Labda hii makala iliyoandikwa na Ndg Abbas Mwalimi mwaka 2019 itasaida kuelewa zaidi juu ya uteuzi na aina za mabalozi.
ULIVYO UTARATIBU WA KUTEUA MABALOZI
Katika muktadha wa uteuzi wa mabalozi kuna mabalozi wa aina mbili, mosi mabalozi wanaoteuliwa kutokana na utashi wa kisiasa na pili, wanaoteuliwa kutokana na weledi wao. Mabalozi wanaoteuliwa kutokana na utashi wa kisiasa huwa ni pendekezo la Rais moja kwa moja kutokana na kuwa na sifa za kuteuliwa wakati wale wanaotokana na weledi, ni waliotokea Wizara ya Mambo ya Nje na hupatikana kutokana na kufikia ngazi ya mwisho katika vyeo vya utumishi wa maofisa wa wizara hiyo.
Vyeo hivi huanzia katibu wa tatu (kwa sasa nadhani haipo), hupanda na kuwa katibu wa pili, katibu wa kwanza, mshauri, mshauri mwandamizi na mwisho kuwa afisa mkuu wa juu. Afisa mkuu wa juu (MPP) ni ngazi ya mwisho ya utumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje ambapo baada ya hapo inatarajiwa mtumishi huyo kuweza kuteuliwa kuwa balozi kama hajafika umri wa kustaafu. Mabalozi wanaotokana na weledi, uteuzi wao hutokana zaidi na mapendekezo ya Wizara ya Mambo ya Nje.
Uteuzi hufanyika ifuatavyo; kwanza mawasiliano hufanyika kwa siri baina ya wakuu wa nchi au serikali juu ya nia ya kumteua mtu fulani kuwa balozi. Kama ni balozi aliyetokana na utashi wa kisiasa, jina hupendekezwa kwa siri kutoka Ofisi ya Rais na kama ni kutoka wizara ya mambo ya nje jina hupelekwa kwa rais kwa siri. Kama Balozi mtarajiwa ametokana na kundi la kwanza la wanaotokana na utashi wa kisiasa kwa maana ya Rais kuona huenda mtu huyo atamfaa na baada ya kushauriana na timu yake ya ushauri, jina hupelekwa idara ya usalama wa taifa ili kumfanyia uchunguzi mtajwa huyo. Wakati huo huo jina hilo huwa limefika katika idara za upelelezi za nchi ambayo balozi mtarajiwa hutazamiwa kutumwa huko ili wao pia wamfanyie uchunguzi.
Endapo usalama watajiridhisha kwamba mtu huyo anafaa kuwa balozi, jina litarudishwa kwa Rais tayari kwa hatua zinazofuata. Kwa upande wa nchi ambayo jina hilo limepelekwa, nao watakapokuwa wameridhika na mtajwa huyo baada ya kufanya uchunguzi wao wa kina, wataridhia kwa njia za kidiplomasia. Kitendo hiki huitwa kwa lugha ya kilatini agrema kwa mujibu wa Ibara ya nne ya Mkataba wa Vienna wa Mwaka 1961.
Endapo nchi inayotarajiwa kumpokea balozi mtarajiwa itaona mtajwa huyo haifai, itafanya mawili kati ya yafuatayo: Mosi nchi hiyo itatoa taarifa juu ya kutomkubali mtajwa huyo kuwa balozi katika nchi yao kwa njia ya kidiplomasia. Kwa mfano, iliwahi kutokea katika nchi fulani mteule wa ubalozi alikuwa mwandishi wa makala na aliwahi kuandika makala iliyoielezea vibaya nchi aliyotarajiwa kupelekwa. Ile nchi iliyotarajiwa kumpokea balozi ilituma makala aliyowahi kuandika mteule huyo kuisema nchi hiyo, hapo nchi iliyomteua balozi ilijua kuwa jibu ni kuwa mtu huyo ‘hakubaliki.’
Lakini pili, nchi hiyo itakaa kimya bila ya kutoa taarifa yoyote. Zamani baadhi ya nchi zilikuwa zikitoa taarifa, lakini siku hizi hilo halifanyiki na badala yake nchi huamua kukaa kimya. Kitendo hiki cha kukaa kimya moja kwa moja huifanya nchi ambayo imepanga kumtuma balozi huyo katika nchi hiyo kutambua kuwa mtajwa huyo amekataliwa au persona non grata kwa Kilatini.
Kimsingi nchi inayotarajiwa kumpokea balozi haipaswi kueleza sababu za kumkataa balozi mtarajiwa kama ilivyoelezwa kwenye Ibara ya Nne ya Mkataba wa Vienna. Hilo hubaki kuwa kazi ya nchi iliyopendekeza jina kutafuta sababu za balozi mteule kukataliwa ama kumtafutia nchi nyingine au kumbakiza nchini mwao.
Ifahamike vema kuwa, wakati huo huwa hakuna anayejua zaidi ya Idara ya Usalama wa Taifa, Ofisi ya Rais na Waziri wa Mambo ya Nje. Maana yake ni kuwa hata huyo mtarajiwa anakuwa hajui kuwa yeye amependekezwa kuwa balozi na anafanyiwa uchunguzi. Ingawa hutokea kwa baadhi ya watumishi ambao siyo waaminifu wanapobahatika kujua huanza kumdhihaki aliyetarajiwa kuwa amekataliwa, lakini pia hali huwa mbaya pale muhusika aliyekuwa akijua kuwa alikuwa akichunguzwa ili ateuliwe kuwa balozi anapotajwa kuwa amekataliwa. Ndiyo sababu kazi hizo huwa za siri mno.
NAMNA NCHI INAVYOJUA KAMA MTAJWA AMEKATALIWA
Kuna kipindi ambacho nchi ikiona kimya kimetawala hujua kabisa mtajwa amekataliwa. Ikipita zaidi ya miezi mitatu na nchi inayotarajiwa balozi atumwe kwao haijasema kitu nchi iliyoteua jina hutambua kabisa kuwa mteule amekataliwa, hivyo hujipanga upya. Inapotokea nchi hizo kwa pamoja zimeridhishwa na balozi huyo mtarajiwa hatua nyingine hufuata.
Hapa ndipo jina la mteule huyo hutajwa kwa tangazo toka Ofisi ya Rais kupitia Katibu Mkuu Kiongozi. Kwa wale wanaotokana na weledi, majina hupendekezwa na wizara na baadae kupelekwa kwa Rais kwa ajili ya utaratibu zilizoelezwa awali.
Swali la msingi la kujiuliza ni kwamba, kwa nini baadhi yao wateuliwe kuwa mabalozi na wabaki nchini? Tufahamu kuwa muundo wa wizara za mambo ya nje duniani hufanana isipokuwa huweza kuwa na tofauti ndogo sana kutokana na mfumo wa utawala wa nchi husika.
Hivyo sababu ya kuwateua mabalozi na kuwabakisha wakifanya kazi nchini ni kutokana na kwamba mabalozi mbalimbali waliopo nchini hufanya kazi zao kupitia idara za kikanda zilizopo wizara ya mambo ya nje na pia, kikanuni mabalozi hawafanyi kazi na watu wengine moja kwa moja isipokuwa mabalozi wenzao ama watu wenye hadhi ya ubalozi. Hapo ndipo inapokuja sababu ya kuwateua mabalozi kufanya kazi nchini kwa lengo la kuongoza idara za kikanda kama vile Afrika, Mashariki ya Kati, Ulaya, Amerika, Asia na Australasia zilizopo katika wizara ya mambo ya nje ya Tanzania.
Hivyo Stephen Patrick Mbundi aliyekuwa Mkurugenzi Idara ya Ulinzi, Siasa na Usalama katika Wizara ya Mambo ya Nje na wengine Ali Sakila Bujiku na Musa Lulandala waliokuwa Wasaidizi wa Rais, wameteuliwa kuwa mabalozi na watabaki nchini kama alivyosema Katibu Mkuu Kiongozi ili wafanye kazi na mabalozi wanaowakilisha nchi zao Tanzania. Lakini watu wanaweza kujiuliza kwa nini maelezo yaliyotolewa na katibu mkuu kiongozi yalieleza kuwa waheshimiwa Mbundi, Bujiku na Lulanda wamepandishwa vyeo kuwa mabalozi?
Hii inatokana na utaratibu wa vyeo vya utumishi wa Wizara ya Mambo ya Nje kwamba, hawa watatu walipanda mpaka kufika ngazi ya ofisa wa juu kabisa wa wizara (MPP) na kwa vyeo vya utumishi wa wizara hiyo, MPP ni cheo cha mwisho hivyo baada ya hapo hutarajiwa wahusika kuteuliwa na Rais kuwa mabalozi ndiyo maana taarifa ile ilieleza kuwa wamepandishwa vyeo kuwa mabalozi kwa sababu hawa ni mabalozi wanaotokana na weledi.
Chanzo:
Usiyoyajua kuhusu uteuzi wa mabalozi wa nchi