Mimi ni mmojawapo ambaye baada tu ya kuchaguliwa nilimwambia waziwazi kupitia JF kwamba sivutiwi na uwezo wake na nikampa changamoto ya kunibadilisha mtizamo huo. Na mara kadhaa nimekuwa nikikumbushia hilo. Lakini lazima tukubaliane kwamba kuna kukosoana na kuzodoana, kuambizana na kutukanana. Inaweza kuwa Malinzi amefanya makosa kwenye maamuzi au utendaji wake. Lakini huwezi kukosoa kosa kwa kufanya kosa (la kumtukana); kasoro mbili hazizai sahihi moja. Na kama nia ni kumkosoa na sio kumzodoa, hakuna haja na si uungwana - ni kinyume cha sheria kabisa - kumrushia matusi. Mara nyingi anayetukana anakusudia kuudhi na kudhalilisha. Sasa kumuudhi na kumdhalilisha kuongoza wa Juu wa TFF kutasaidiaje kufanikisha uongozi wa TFF na utendaji wa kiongozi mwenyewe? Kama sio kwa nia ya kuudhi na kudhalilisha, matusi ni ushahidi usiowacha shaka kwamba aliyeyatoa ameishiwa hoja. Matusi ya aina hiyo mara nyingi mhusika huwa hamalizi kuyasoma, na hashawishiki kusoma maoni yajayo ya mtukanaji huyo hata yasipokuwa na matusi. Kwa hivyo nayo hayasaidii.
Licha ya kutoridhishwa naye, lakini lazima tukubali kwamba angalau ni muungwana. Alihusikaje na kuruhusiwa Azam kwenda Zambia kwenye Bonanza wakati yeye si kiongozi wa Bodi ya Ligi? Na bado akakubali makosa. Mtu namna hiyo ndiye wa mwisho anayestahiki kutukanwa, kama matusi yangekubalika. Hoja yangu ya msingi ni kwamba wanaotukana Malinzi kwenye JF wanampa uhalali wa kutojibu hoja zao na - pamoja nao - hata za wasiomtukana. Wanaikosea adabu JF na wanatuzindua kwamba hata wao wenyewe hawana busara za kuongoza. Kwa hivyo wao kumkosoa kiongozi ni sawa na chungu kulikosoa birika kwa weusi wake.