Pascal umeleta mada nzuri. Ni mada ambayo inakwenda na wakati huu tulionao.
Kwanza na mimi niseme wazi kabisa hapa kuwa nina maslahi na mada hii. Nilitia nia nyumbani kwetu na niliambulia kura "0". Kwa mazingira ya pale kwetu sikuona au kusikia tetesi za rushwa japo kwakusema hivyo haina maana ya mimi kudhibitisha kuwepo au kutokuwepo kwa rushwa. Hii ilinisukuma kuandika andiko hili:
Hongera sana CCM kwa mchakato wa kura za maoni
Kama ulivyoeleza, na mimi nilienda kwenye mchakato huu nikiwa na moyo wa dhati kabisa wa kuwatumikia watu wangu kwa nafasi hiyo. Kuhusu uadilifu, uwezo na uzoefu wangu, hilo sio jambo la kutilia shaka na wanaonifahamu wanajua hilo.
Niliandaa kipeperushi changu na kukisambaza kwa watu wangu wa karibu, punde katibu wa NEC - Itikadi na Uenezi ndugu Polepole akatoa onyo juu ya Jambo hilo. Haraka sana nikatii na kuwataka ndugu, jamaa na marafiki waache kusambaza kipeperushi hicho. Na hilo lilifanyika "with immediate effect".
Ndugu Pascal na wasemaji, baada ya hatua hiyo sikufanya tena aina yoyote ya kampeni wala sikutoa rushwa. Siku ya kujieleza kwa wajumbe ikafika, nikajieleza, mwenyekiti anauliza, " Kuna swali lolote kwa mgombea?" Wajumbe wakajibu kwa sauti moja "hakunaaaa". Nikatoka. Kura zikapigwa na zikahesabiwa wazi kwa kila mgombea kupewa kura zake. Kika zikitajwa, sitajwi mpaka mwisho.
Basi msimamizi wa uchaguzi akawa anaita mtia nia mmojammoja kupita mbele na kusema amepata kura ngapi. Akaita " Amani Msumari" nikapita mbele na kusema " ninawashukuru ndugu wajumbe, sijapata kura yoyote, nimepata sufuri".
Baada ya mchakato huo, moyo wangu umefarijika kwani nimefanya kile ninachokiamini. Nilifurahi zaidi baada ya wazee flani watatu kuniita na kuniambia " kijana umeongea vizuri Sana, wewe ni kiongozi mzuri Ila kwasasa umegombea na mtu ambaye sisi tunamuamini Sana na ni muhimu kwa Jimbo letu, Mungu hakutaka iwe kipindi hiki". Kwakweli nilifurahi Sana.
Kama hakuna rushwa, ni vigumu Sana kumrudisha mtu aliyepata kura sifuri kwani wajumbe walikuwa na sababu kwanini wasimpe kura. Cha muhimu ni kuwa tumepata ya kujifunza kwenye mchakato huu.
Pascal, mimi na wewe tunazo shughuli zetu zinazotuingizia vipato halali, tena vizuri tuu. Ushauri wangu ni kuwa tuendelee kuonesha uzalendo kwa kuitumikia nchi yetu na chama chetu kwa nafasi nyingine.
Binafsi nimejivika kuwa balozi wa kuyasema mema ya chama na serikali. Kukosoa kwa staha pale inapobidi na sikosolei humu mitandaoni. Sio lazima tuwe wabunge kwenye jitihada za kuhakikisha nchi yetu inasonga mbele zaidi.
Amani Msumari
Tanga