Ingawa huu usemi umetamalaki kwenye sekta mbalimbali hasa za michezo hapa Tanzania, ila kama ulikuwa hujui basi chukua hii Leo.
Mwaka 1993 klabu ya Simba ilifika fainali ya michuano iliyoitwa Caf cup dhidi ya Stella Abidjan ya nchini Ivory coast.
Mchezo wa kwanza ulipigwa nchini Ivory Coast uliisha kwa suluhu, hivyo mechi ya marudia ilikuwa lazima mshindi apatikane
Simba walijiandaa vizuri na mchezo huu wa marudia na hamasa ilikuwa kubwa ambapo aliyekuwa mfadhili wa Simba wakati huo ndugu Azim Dewji aliwaahidi wachezaji wote kuwanunulia magari aina ya Toyota KIA endapo wangeshinda mchezo huo.
Siku ya mchezo ilifika na Uwanja wa taifa wa wakati huo( Uwanja wa Uhuru) ulijaa pomoni kuisapoti timu ya nyumbani simba
Stella Abidjan walipiga mpira mwingi sana na kuichabanga Simba 2-0 magoli yote yakiwekwa kimiani na Mshambuliaji wao hatari BOLIZOZO
Ndipo baada ya mchezo huo, mgeni rasmi akitoka jukwaa kuu huku akiwa amelowa kwa aibu kubwa baada ya kuona timu ya nyumbani inafungwa mbele yake na kombe linachukuliwa kwenye ardhi ya nyumbani alitoa kauli hii" TANZANIA NI KICHWA CHA MWENDAWAZIMU" maneno haya alikuwa akiwalenga Simba waliokubali kufungwa uwanja wa nyumban Tena mbele ya mashabiki wao.
Kuna striker alikua akiitwa Bolizozo, huyo ndiye alipelekea kilio Msimbazi.
Kwa mara ya kwanza Simba na Yanga waliungana na wote kuishabikia Simba kwa nguvu sana.
Simba walipopigwa goli la kwanza, pale uwanjani hali haikubadilika amsha amsha za kuuhimiza Simba zilikua juu sana zikifanywa na mashabiki wa Simba na Yanga.
Hali ilibadilika pale Bolizozo alipotupia goli la pili, Yanga wakaona hawa jamaa vipi? Mbona badala ya kucheza mpira wanakati viuno na kuruhusu goli ziingie kiurahisi ?
Ghafla Yanga wakabadilika na kuanza kuimba "Uzalendoo, umetushinda" na kuanza kuishangilia Stella Abidjan ya Ivory Coast. Hapo wachezaji wa Simba kusikia hivyo wakabomoka kabisa kisaikolojia na kupoteza matumaini huku wakicheza bora liende mpira uishe.
Baada ya ile mechi ya fainali, Stella Abijan waliondoka na kombe. Ilipokuja kupigwa mechi ya Simba na Yanga, jina la Bolizozo likahamishiwa kwa mchezaji James Tungaraza wa Yanga baada ya kuwatungua Simba.
Michuani hiyo ilikua ikidhaminiwa na Bilionea wa Nigeria Moshood Kashimawo Olawale Abiola (Mashood Abiola).
Kuhusiana na jina la "Kichwa Cha Mwendawazimu", kumbukumbu zangu kama vile zinaniambia liliongelewa wakati wachezaji wa timu ya Tanzania Stars ambao walishinda Kombe la FAT walipokuwa wakikabidhiwa kombe hilo kwa ajili ya kuiwakilisha nchi kwenye moja ya michuano ya CAF.