Red Giant
JF-Expert Member
- Mar 9, 2012
- 15,657
- 20,967
Umewahi kusoma hiki kitabu?
Kimeandikwa na: George Orwell, 1945.
Kimetafsiriwa na: Pictuss
Email: Pictuspublishers@gmail.com.
©Pictuss2021
Haki zote zimehifadhiwa. Hakuna sehemu yoyote ya tafsiri hii inayoweza kunakiliwa, kutolewa kivuli(photocopy), kuhamishwa, kurekodiwa au kutolewa kwa namna yoyote ile bila ya taarifa ya awali ya kimaandishi kutoka kwa mmiliki.
SURA YA KWANZA
Mmiliki wa shamba la Mano, bwana Jones alikuwa amefunga banda la kuku. Lakini sababu ya ulevi, alikuwa amesahau kufunga tundu dogo la kwenye mlango ambalo kuku hupita. Alielekea ndani kwake huku mwanga wa taa ya chemli ukichezacheza na kufanyiza miduara ardhini. Alipofika mlango wa nyuma wa nyumba yake alirusha viatu vyake na kujimiminia glasi ya bia kutoka kwenye debe. Akanywa na kuelekea chumbani ambako mke wake alikuwa tayari anakoroma.
Mara tu taa ya chumbani kwake ilipozima pilikapilika zikaanza kusikika kwenye mabanda ya mifugo. Mchana taarifa zilikuwa zimesambaa kuwa Meja, nguruwe dume mkubwa, alipatwa na ndoto ya ajabu sana usiku uliopita na alitaka kuwashirikisha wanyama wengine. Walikubaliana kuwa wote wakutane kwenye banda kubwa mara tu bwana Jones atakapokuwa ameshalala. Meja aliheshimika sana pale shambani, hivyo wanyama walikuwa tayari kupoteza saa moja la kulala ili wakamsikilize.
Kwenye kona moja ya banda kubwa alikuwa ametulia Meja kwenye kitanda chake cha nyasi, chini ya taa iliyokuwa ikining'inia darini. Kitanda chake kilikuwa sehemu ya juu kama jukwaa hivi. Alikuwa na umri wa miaka kumi na miwili lakini bado alionekana ni mshupavu na nguruwe bora. Mwenye hekima na busara, na mwenye roho nzuri japo meno yake yaliyotoka hayakuwahi kukatwa.
Baada ya muda mfupi wanyama wengine wakaanza kuwasili na kukaa, kila mmoja kulingana na aina yake. Walioanza kuwasili walikuwa ni mbwa watatu, Bluebell, Jessie na Pincher, kisha wakaingia nguruwe ambao walienda kukaa mbele karibu na jukwaa alilokaa Meja.
Kuku walikaa kwenye fremu za madirishani na njiwa waliruka na kukaa kwenye mbao za darini. Ng'ombe na kondoo walikaa nyuma ya nguruwe na kuanza kujitafuna. Farasi wawili wa kukokota mkokoteni, Boxer na Clover waliingia pamoja, walitembea polepole wakikanyaga kwa uangalifu ili kama kuna mnyama mdogo kwenye nyasi wasimdhuru.
Clover alikuwa farasi wa kike wa umri wa kati, lakini toka uzazi wake wa mwisho umbo lake halikuwa sawa. Boxer alikuwa ni farasi mkubwa sana, karibu kimo cha mikono kumi na nane na alikuwa na nguvu za farasi wawili wakubwa. Alikuwa na mstari mweupe katikati ya pua yake. Hilo lilimfanya aonekane kama kituko, na kiukweli hakuwa mnyama mwenye akili. Pamoja na hilo, Boxer aliheshimika sababu ya uwezo wake wa kufanya kazi na tabia yake njema.
Baada ya farasi aliingia mbuzi aliyeitwa Muriel na punda aliyeitwa Benjamini. Benjamini alikuwa ndiye mnyama mwenye umri mkubwa kuliko wote pale shambani. Alikuwa si muongeaji na iwapo akiongea ilikuwa ni kutoa kejeli. Mfano, anaweza kusema kuwa Mungu amempa mkia kwa ajili ya kufukuzia nzi, lakini angependelea vyote, nzi na mkia visingekuwepo.
Benjamini hajawahi cheka hata siku moja. Akiulizwa kwanini, alikuwa akijibu kuwa hajawahi kuona kitu cha kumchekesha. Pamoja na hayo, alikuwa na urafiki wa karibu pamoja na Boxer. Mara nyingi walitumia mapumziko ya jumapili pamoja katika malisho yaliyo nyuma bustani. Urafiki wao ulikuwa wa kushangaza, walikaa huko na kula pamoja bila kuongea chochote.
Farasi walipokaa, kundi la bata likaja. Walikuwa ni bata wa umri wa kati waliofiwa na mama yao waliingia. Walikuwa wakishangaa huku na huko wakitafuta sehemu salama ya kukaa. Walipokaa, Clover alizungusha miguu yake ya mbele kuwazungunka, wakakaa humo na haikuchukuwa muda wakawa wamepitiwa na usingizi.
Kisha akaingia Moli. Farasi mweupe mzuri lakini mpumbavu. Alikuwa anatumika kuvuta mkokoteni wa bwana Jones. Aliingia akitembea kwa madaha huku akimung'unya kipande cha sukari guru. Alienda kukaa karibu na jukwaa, na kuanza kuringishia nywele zake ndefu ili wengine waone tepe alizovaa.
Wa mwisho kabisa kuingia alikuwa ni paka. Kama kawaida yake, akatafuta sehemu yenye joto na akajibanza katikati ya Clover na Boxer. Muda wote wa hotuba ya Meja alikuwa akinguuruma kwa raha. Hakuelewa chochote kilichoongelewa.
Wanyama wote walikuwa wamefika isipokuwa Musa. Yeye alikuwa ni kunguru wa kufungwa na aliishi ndani kwa bwana Jones.
Baada ya Meja kuona kuwa wametulia na wako makini kumsikiliza, alikohoa kidogo na kuanza kusema.
"Ndugu zanguni, natumaini wote mmesikia kuhusu ndoto ya ajabu niliyoota jana usiku. Lakini nitazungumza kuhusu ndoto hiyo baadaye. Kuna jambo ningependa niongee kwanza. Ndugu zangu, sidhani kama nina muda mrefu wa kuwa na nyinyi, kabla sijafa nahisi nina wajibu wa kuwapatia hekima na busara nilizonazo. Nimeishi miaka mingi na nilikuwa na muda mwingi wa kufikiri. Hivyo nafikiri naweza kusema kuwa nina uelewa mkubwa kuhusu maisha. Hili ndilo hasa lililonifanya nitake kuongea nanyi. Sasa ndugu zangu, maisha yetu ni ya namna gani?"
"Tuongee ukweli; maisha yetu ni ya taabu, ya kazi ngumu na mafupi. Tunalishwa chakula kinachotosha kutufanya kuishi tu. Wale wanaoweza kufanya kazi, hufanyishwa kazi hadi nguvu yao ya mwisho. Nguvu zinapoisha huchinjwa kwa ukatili wa ajabu. Hakuna mnyama mwenye umri wa zaidi ya mwaka mmoja anayeijua furaha na starehe maishani."
"Uingereza yote hakuna mnyama aliye huru. Maisha ya mnyama ni machungu na ya kitumwa; huo ndiyo ukweli. Lakini jambo hilo ni mpango wa Mungu? Je mazingira ya nchi yetu ni magumu sana kiasi kwamba hatuwezi kuishi vizuri?"
"Hapana ndugu zangu, hapana kabisa! Ardhi ya Uingereza ni yenye rutuba na hali ya hewa ni nzuri. Inaweza kulisha wanyama wengi kuliko waliopo. Hili shamba tunaloishi linaweza kulisha farasi kumi na mbili, ng'ombe ishirini na mamia ya kondoo. Wote hao wakiishi vizuri na kwa ustaarabu kuliko maisha wanayoishi sasa. Basi ni kwanini tunaendelea na maisha haya ya taabu? Ni kwa sababu chakula chote tunachozalisha kinaporwa na binadamu. Hilo ndilo jibu la tatizo letu ndugu zangu. Kwa neno moja jibu ni - binadamu. Binadamu ndiye adui pekee wa kweli tuliyenaye. Mtoe binadamu na chanzo cha njaa na kazi za kitumwa kitakuwa kimeondoka milele."
"Binadamu ndiye kiumbe pekee ambaye anakula bila kuzalisha. Hatoi maziwa wala hatagi mayai, na hana nguvu za kutosha kukokota jembe la kulimia wala hana mbio za kuweza kukamata sungura, lakini ndiye bwana wa wanyama wote. Anawatumikisha lakini anawapa chakula cha kuwafanya wasife njaa tu, kingine chote anachukua. Nguvu zetu zinalima shamba, kinyesi chetu ni mbolea, lakini kati yetu hakuna anayemiliki zaidi ya ngozi yake mwenyewe. Nyinyi ng'ombe mlio hapa, ni maelfu mangapi ya lita za maziwa mlitoa mwaka jana? Na nini kimetokeo kwa hayo maziwa ambayo yalitakiwa yatumike kukuza ndama wenye afya? Kila tone limepita kwenye koo la adui yetu."
"Nanyi kuku, ni mayai mangapi mmetaga mwaka jana, na ni mangapi yametotolewa kuwa vifaranga? Karibu yote yameuzwa na bwana Jones kajipatia pesa, yeye na wafanya kazi wake. Na wewe Clover, watoto wako wanne uliowazaa wako wapi? Watoto ambao walitakiwa wawe msaada na furaha yako katika uzee wako. Kila mmoja aliuzwa alipofikisha mwaka mmoja tu, hutaweza kuwaona tena. Umelipwa nini zaidi ya kibanda cha kuishi na chakula kidogo?"
"Mbaya zaidi, hata haya maisha ya taabu tunayoishi bado hatuachi tukaishi yote. Mimi binafsi siwezi laumu maana nimekuwa kati ya wenye bahati. Nina miaka kumi na mbili na nimepata watoto zaidi ya mia nne. Nilionao ndiyo umri halisi wa nguruwe, lakini mwisho wetu wote ni kuchinjwa kikatili. Nyinyi nguruwe vijana mliokaa hapa mbele yangu, kabla ya mwaka kuisha kila mmoja wenu atalia kwa uchungu wakati wa kuchinjwa. Hiyo ndiyo njia yetu sote, ng'ombe, nguruwe, kuku, kondoo, kila mmoja wetu. Hata mbwa na farasi hawana afadhali. Boxer, siku misuli yako ikiishiwa nguvu bwana Jones atakuuza kwa wanunuzi wa mizoga. Huyo atakuchinja na kukuchemsha kuwa chakula cha mbwa. Nanyi mbwa mkizeeka na meno yenu kung'oka, bwana Jones atawafunga tofali shingoni na kuwatupa dimbwini."
"Je, haiko wazi kuwa mabaya yote ya maisha yetu chanzo ni ukatili wa binadamu? Tunahitaji kumtoa binadamu na chochote tunachozalisha kitakuwa chetu wenyewe.
Kufumba na kufumbua tutakuwa matajiri na huru. Sasa nini kinahitajika kufanyika? Kwanini tusifanye kazi usiku kucha na kwa uwezo wetu wote ili kupindua utawala wa binadamu? Huu ndiyo ujumbe wangu kwenu: Uasi! Sijui uasi huo utatokea lini, inaweza kuwa baada ya wiki moja au inaweza kuchukua miaka miamoja lakini nina hakika utatokea. Kama nilivyo na hakika kuwa naona nyasi hapa chini yangu ndivyo nilivyo na hakika kuwa uasi na mapinduzi vitatokea na haki itapatikana. Kazieni fikra jambo hilo nduguzanguni. Liwekeni akilini kwenye maisha yenu mafupi yaliyobaki, na waambieni ujumbe huu wataokuja. Hakikisheni kizazi kijacho kinaendeleza mapambano hadi ushindi upatikane."
"Ndugu zangu naomba msije kulegea kwenye lengo hili, na hoja yoyote isiwatoe kwenye lengo hili. Msisikilize wala kukubali wawambiapo kuwa maslahi ya binadamu na wanyama ni mamoja. Kwamba mafanikio ya binadamu ndiyo mafanikio ya wanyama. Huo ni ulaghai mtupu, binadamu ni mbinafsi anayejijali mwenyewe tu. Acha kuwe na undugu kati ya wanyama na undugu katika mapambano. Binadamu wote ni adui lakini wanyama wote ni ndugu."
Baada ya kusema hayo kukatokea shangwe kubwa sana. Meja alipokuwa akihutubia, panya wanne wakubwa walitoka kwenye mashimo yao na walikaa kumsikiliza. Mbwa wakawa wamewaona. Ushapu wao wa kukimbilia mashimoni ndiyo uliowaokoa.
Meja akainua mguu kuashiria wanyama wanyamaze, kisha akasema. "Ndugu zangu, hapa kuna jambo linatakiwa tulitatue. Wanyama wa porini kama sungura na panya ni adui zetu au ni ndugu zetu? Naombeni tupige kura. Swali liwe; Je, panya ni ndugu zetu?"
Kura ilipigwa mara moja na kwa kura nyingi ikakubaliwa kuwa panya ni ndugu. Kulikuwa na kura nne tu zilipinga. Kura za mbwa watatu na ya paka ambaye hata hivyo aligundulika amepiga kura ya ndiyo na hapana.
Meja akaendelea kusema: "sina mengi ya kuongezea ila nitaruria tu. Siku zote kumbuka kuwa una wajibu wa kuwa adui wa binadamu na mambo yake yote. Chochote kinachotembea kwa miguu miwili ni adui. Chochote kinachotembea kwa miguu minne au chenye mabawa ni rafiki. Na kumbukeni kuwa, katika kupambana na binadamu hatutakiwi kuwa kama yeye. Hata tukimshinda hatupaswi kuiga mambo yake. Mnyama yeyote hatakiwi kuishi ndani ya nyumba, kulala kitandani, kuvaa nguo, kunywa pombe, kuvuta sigara, kushika pesa au kujihusisha na biashara. Zaidi ya yote, mnyama yeyote hatakiwi kutawala wengine kwa kwa ukatili."
"Wanyama wote ni ndugu, wenye nguvu na dhaifu, wenye akili na wajinga, sote ni ndugu. Mnyama yeyote hatakiwi kabisa kumuua mnyama mwenzake. Wanyama wote sawa."
"Sasa ndugu zanguni nitawaambia kuhusu ndoto niliyoota jana usiku. Siwezi kuwaelezea vizuri jinsi ilivyokuwa ila ni ndoto inayohusu hali ya dunia binadamu atakapokuwa ametoweka, lakini ilinikumbusha zamani sana nilipokuwa bado nguruwe mdogo.
Miaka mingi iliyopita, nilipokuwa mdogo, mama yangu na nguruwe wengine walipendelea kuimba wimbo mmoja. Wimbo wenyewe waliujua kwa ala na maneno matatu ya mwanzo tu. Nilipokuwa mdogo nilikuwa nimeishika ile ala. Ni muda mrefu umepita hivyo ilikuwa imenitoka. Lakini jana usiku imenijia ndotoni, na cha kushangaza zaidi, hadi maneno ya wimbo yamenijia. Maneno ambayo nina hakika yaliimbwa na wanyama hapo zamani za kale na yamepotea baada ya vizazi vingi kupita. Nitajaribu kuwaimbia wimbo huo ndugu zangu. Ila mimi ni mzee na sauti yangu ni ya kukwaruza, lakini nikiwafundisha ala yake natumaini mtauimba vizuri zaidi. Wimbo wenyewe unaitwa Hayawani wa Uingereza."
Meja alikohoa kidogo kisha akaanza kuimba. Sauti ya meja ilikuwa ya kukwaruza lakini alijitahidi kuimba vizuri. Ulikuwa ni wimbo wa kuchangamsha sana.
Maneno yake yalikuwa kama ifuatavyo:
Hayawani wa nchi na nyanda zote
Sikilizeni ujumbe wangu wa shangwe
Ni kuhusu wakati mzuri ujao
Siku ile inakuja
Siku ya kumpindua binadamu mkatili
Ardhi nzuri ya uingereza, itakanyagwa na hayawani tu
Pete zitatoweka katika pua zetu
Na kamba kutoka migongoni mwetu
Vyuma vya kutuendesha vitaliwa na kutu
Mijeledi ya ukatili haitachapa tena
Utajiri usioelezeka
Ngano, shayiri na nyasi
Maharage, mizizi ya beet na matunda
Vitakuwa vyetu siku hiyo
Mashamba ya Uingereza yatameremeta
Maji yake yatakuwa safi
Pepo zake zitakuwa mwororo
Katika siku tutakayo kuwa huru
Sote tutapambana kwaajili ya siku hiyo
Hata tukifa kabla haijatokea
Ng'ombe na farasi, bata bukini bata mzinga
Wote watapambana kwaajili ya uhuru
Hayawani wa Uingereza, hayawani wa Ireland
Hayawani wa nchi na nyanda zote
Sikilizeni vizuri na enezeni ujumbe wangu
Ujumbe juu ya wakati bora ujao
Wimbo huu uliwapamdisha sana mori wanyama wote, na kabla Meja hajamaliza kuimba nao wakaanza kuuimba. Hata wanyama wajinga kabisa wakawa wameweza kuimba ala ile na maneno machache. Wanyama wenye akili kama mbwa na nguruwe waliweza kuimba wimbo wote ndani ya dakika chache tu.
Baada ya mazoezi kidogo, wanyama wote wakaimba Hayawani wa Uingereza pamoja kwa sauti kubwa. Kila mnyama alitia vionjo vyake. Wimbo ulikuwa umewapandisha mori kiasi kwamba waliimba mara tano mfululizo. Na bila kukatishwa wangeweza imba usiku kucha.
Kelele zao zikimuamsha bwana Jones. Bwana Jones aliamka haraka akifikiri labda mbwa mwitu amevamia shamba. Alichukua bunduki iliyokuwa kwenye kona chumbani mwake kisha akatoka na kupiga risasi hewani. Vipande vya risasi vikaruka na kugonga ukuta wa banda lile kubwa walilokuwepo wanyama. Wanyama wote wakatawanyika kila mmoja kwenye eneo lake la kulala. Shamba likawa kimya kabisa.
Kimeandikwa na: George Orwell, 1945.
Kimetafsiriwa na: Pictuss
Email: Pictuspublishers@gmail.com.
©Pictuss2021
Haki zote zimehifadhiwa. Hakuna sehemu yoyote ya tafsiri hii inayoweza kunakiliwa, kutolewa kivuli(photocopy), kuhamishwa, kurekodiwa au kutolewa kwa namna yoyote ile bila ya taarifa ya awali ya kimaandishi kutoka kwa mmiliki.
SURA YA KWANZA
Mmiliki wa shamba la Mano, bwana Jones alikuwa amefunga banda la kuku. Lakini sababu ya ulevi, alikuwa amesahau kufunga tundu dogo la kwenye mlango ambalo kuku hupita. Alielekea ndani kwake huku mwanga wa taa ya chemli ukichezacheza na kufanyiza miduara ardhini. Alipofika mlango wa nyuma wa nyumba yake alirusha viatu vyake na kujimiminia glasi ya bia kutoka kwenye debe. Akanywa na kuelekea chumbani ambako mke wake alikuwa tayari anakoroma.
Mara tu taa ya chumbani kwake ilipozima pilikapilika zikaanza kusikika kwenye mabanda ya mifugo. Mchana taarifa zilikuwa zimesambaa kuwa Meja, nguruwe dume mkubwa, alipatwa na ndoto ya ajabu sana usiku uliopita na alitaka kuwashirikisha wanyama wengine. Walikubaliana kuwa wote wakutane kwenye banda kubwa mara tu bwana Jones atakapokuwa ameshalala. Meja aliheshimika sana pale shambani, hivyo wanyama walikuwa tayari kupoteza saa moja la kulala ili wakamsikilize.
Kwenye kona moja ya banda kubwa alikuwa ametulia Meja kwenye kitanda chake cha nyasi, chini ya taa iliyokuwa ikining'inia darini. Kitanda chake kilikuwa sehemu ya juu kama jukwaa hivi. Alikuwa na umri wa miaka kumi na miwili lakini bado alionekana ni mshupavu na nguruwe bora. Mwenye hekima na busara, na mwenye roho nzuri japo meno yake yaliyotoka hayakuwahi kukatwa.
Baada ya muda mfupi wanyama wengine wakaanza kuwasili na kukaa, kila mmoja kulingana na aina yake. Walioanza kuwasili walikuwa ni mbwa watatu, Bluebell, Jessie na Pincher, kisha wakaingia nguruwe ambao walienda kukaa mbele karibu na jukwaa alilokaa Meja.
Kuku walikaa kwenye fremu za madirishani na njiwa waliruka na kukaa kwenye mbao za darini. Ng'ombe na kondoo walikaa nyuma ya nguruwe na kuanza kujitafuna. Farasi wawili wa kukokota mkokoteni, Boxer na Clover waliingia pamoja, walitembea polepole wakikanyaga kwa uangalifu ili kama kuna mnyama mdogo kwenye nyasi wasimdhuru.
Clover alikuwa farasi wa kike wa umri wa kati, lakini toka uzazi wake wa mwisho umbo lake halikuwa sawa. Boxer alikuwa ni farasi mkubwa sana, karibu kimo cha mikono kumi na nane na alikuwa na nguvu za farasi wawili wakubwa. Alikuwa na mstari mweupe katikati ya pua yake. Hilo lilimfanya aonekane kama kituko, na kiukweli hakuwa mnyama mwenye akili. Pamoja na hilo, Boxer aliheshimika sababu ya uwezo wake wa kufanya kazi na tabia yake njema.
Baada ya farasi aliingia mbuzi aliyeitwa Muriel na punda aliyeitwa Benjamini. Benjamini alikuwa ndiye mnyama mwenye umri mkubwa kuliko wote pale shambani. Alikuwa si muongeaji na iwapo akiongea ilikuwa ni kutoa kejeli. Mfano, anaweza kusema kuwa Mungu amempa mkia kwa ajili ya kufukuzia nzi, lakini angependelea vyote, nzi na mkia visingekuwepo.
Benjamini hajawahi cheka hata siku moja. Akiulizwa kwanini, alikuwa akijibu kuwa hajawahi kuona kitu cha kumchekesha. Pamoja na hayo, alikuwa na urafiki wa karibu pamoja na Boxer. Mara nyingi walitumia mapumziko ya jumapili pamoja katika malisho yaliyo nyuma bustani. Urafiki wao ulikuwa wa kushangaza, walikaa huko na kula pamoja bila kuongea chochote.
Farasi walipokaa, kundi la bata likaja. Walikuwa ni bata wa umri wa kati waliofiwa na mama yao waliingia. Walikuwa wakishangaa huku na huko wakitafuta sehemu salama ya kukaa. Walipokaa, Clover alizungusha miguu yake ya mbele kuwazungunka, wakakaa humo na haikuchukuwa muda wakawa wamepitiwa na usingizi.
Kisha akaingia Moli. Farasi mweupe mzuri lakini mpumbavu. Alikuwa anatumika kuvuta mkokoteni wa bwana Jones. Aliingia akitembea kwa madaha huku akimung'unya kipande cha sukari guru. Alienda kukaa karibu na jukwaa, na kuanza kuringishia nywele zake ndefu ili wengine waone tepe alizovaa.
Wa mwisho kabisa kuingia alikuwa ni paka. Kama kawaida yake, akatafuta sehemu yenye joto na akajibanza katikati ya Clover na Boxer. Muda wote wa hotuba ya Meja alikuwa akinguuruma kwa raha. Hakuelewa chochote kilichoongelewa.
Wanyama wote walikuwa wamefika isipokuwa Musa. Yeye alikuwa ni kunguru wa kufungwa na aliishi ndani kwa bwana Jones.
Baada ya Meja kuona kuwa wametulia na wako makini kumsikiliza, alikohoa kidogo na kuanza kusema.
"Ndugu zanguni, natumaini wote mmesikia kuhusu ndoto ya ajabu niliyoota jana usiku. Lakini nitazungumza kuhusu ndoto hiyo baadaye. Kuna jambo ningependa niongee kwanza. Ndugu zangu, sidhani kama nina muda mrefu wa kuwa na nyinyi, kabla sijafa nahisi nina wajibu wa kuwapatia hekima na busara nilizonazo. Nimeishi miaka mingi na nilikuwa na muda mwingi wa kufikiri. Hivyo nafikiri naweza kusema kuwa nina uelewa mkubwa kuhusu maisha. Hili ndilo hasa lililonifanya nitake kuongea nanyi. Sasa ndugu zangu, maisha yetu ni ya namna gani?"
"Tuongee ukweli; maisha yetu ni ya taabu, ya kazi ngumu na mafupi. Tunalishwa chakula kinachotosha kutufanya kuishi tu. Wale wanaoweza kufanya kazi, hufanyishwa kazi hadi nguvu yao ya mwisho. Nguvu zinapoisha huchinjwa kwa ukatili wa ajabu. Hakuna mnyama mwenye umri wa zaidi ya mwaka mmoja anayeijua furaha na starehe maishani."
"Uingereza yote hakuna mnyama aliye huru. Maisha ya mnyama ni machungu na ya kitumwa; huo ndiyo ukweli. Lakini jambo hilo ni mpango wa Mungu? Je mazingira ya nchi yetu ni magumu sana kiasi kwamba hatuwezi kuishi vizuri?"
"Hapana ndugu zangu, hapana kabisa! Ardhi ya Uingereza ni yenye rutuba na hali ya hewa ni nzuri. Inaweza kulisha wanyama wengi kuliko waliopo. Hili shamba tunaloishi linaweza kulisha farasi kumi na mbili, ng'ombe ishirini na mamia ya kondoo. Wote hao wakiishi vizuri na kwa ustaarabu kuliko maisha wanayoishi sasa. Basi ni kwanini tunaendelea na maisha haya ya taabu? Ni kwa sababu chakula chote tunachozalisha kinaporwa na binadamu. Hilo ndilo jibu la tatizo letu ndugu zangu. Kwa neno moja jibu ni - binadamu. Binadamu ndiye adui pekee wa kweli tuliyenaye. Mtoe binadamu na chanzo cha njaa na kazi za kitumwa kitakuwa kimeondoka milele."
"Binadamu ndiye kiumbe pekee ambaye anakula bila kuzalisha. Hatoi maziwa wala hatagi mayai, na hana nguvu za kutosha kukokota jembe la kulimia wala hana mbio za kuweza kukamata sungura, lakini ndiye bwana wa wanyama wote. Anawatumikisha lakini anawapa chakula cha kuwafanya wasife njaa tu, kingine chote anachukua. Nguvu zetu zinalima shamba, kinyesi chetu ni mbolea, lakini kati yetu hakuna anayemiliki zaidi ya ngozi yake mwenyewe. Nyinyi ng'ombe mlio hapa, ni maelfu mangapi ya lita za maziwa mlitoa mwaka jana? Na nini kimetokeo kwa hayo maziwa ambayo yalitakiwa yatumike kukuza ndama wenye afya? Kila tone limepita kwenye koo la adui yetu."
"Nanyi kuku, ni mayai mangapi mmetaga mwaka jana, na ni mangapi yametotolewa kuwa vifaranga? Karibu yote yameuzwa na bwana Jones kajipatia pesa, yeye na wafanya kazi wake. Na wewe Clover, watoto wako wanne uliowazaa wako wapi? Watoto ambao walitakiwa wawe msaada na furaha yako katika uzee wako. Kila mmoja aliuzwa alipofikisha mwaka mmoja tu, hutaweza kuwaona tena. Umelipwa nini zaidi ya kibanda cha kuishi na chakula kidogo?"
"Mbaya zaidi, hata haya maisha ya taabu tunayoishi bado hatuachi tukaishi yote. Mimi binafsi siwezi laumu maana nimekuwa kati ya wenye bahati. Nina miaka kumi na mbili na nimepata watoto zaidi ya mia nne. Nilionao ndiyo umri halisi wa nguruwe, lakini mwisho wetu wote ni kuchinjwa kikatili. Nyinyi nguruwe vijana mliokaa hapa mbele yangu, kabla ya mwaka kuisha kila mmoja wenu atalia kwa uchungu wakati wa kuchinjwa. Hiyo ndiyo njia yetu sote, ng'ombe, nguruwe, kuku, kondoo, kila mmoja wetu. Hata mbwa na farasi hawana afadhali. Boxer, siku misuli yako ikiishiwa nguvu bwana Jones atakuuza kwa wanunuzi wa mizoga. Huyo atakuchinja na kukuchemsha kuwa chakula cha mbwa. Nanyi mbwa mkizeeka na meno yenu kung'oka, bwana Jones atawafunga tofali shingoni na kuwatupa dimbwini."
"Je, haiko wazi kuwa mabaya yote ya maisha yetu chanzo ni ukatili wa binadamu? Tunahitaji kumtoa binadamu na chochote tunachozalisha kitakuwa chetu wenyewe.
Kufumba na kufumbua tutakuwa matajiri na huru. Sasa nini kinahitajika kufanyika? Kwanini tusifanye kazi usiku kucha na kwa uwezo wetu wote ili kupindua utawala wa binadamu? Huu ndiyo ujumbe wangu kwenu: Uasi! Sijui uasi huo utatokea lini, inaweza kuwa baada ya wiki moja au inaweza kuchukua miaka miamoja lakini nina hakika utatokea. Kama nilivyo na hakika kuwa naona nyasi hapa chini yangu ndivyo nilivyo na hakika kuwa uasi na mapinduzi vitatokea na haki itapatikana. Kazieni fikra jambo hilo nduguzanguni. Liwekeni akilini kwenye maisha yenu mafupi yaliyobaki, na waambieni ujumbe huu wataokuja. Hakikisheni kizazi kijacho kinaendeleza mapambano hadi ushindi upatikane."
"Ndugu zangu naomba msije kulegea kwenye lengo hili, na hoja yoyote isiwatoe kwenye lengo hili. Msisikilize wala kukubali wawambiapo kuwa maslahi ya binadamu na wanyama ni mamoja. Kwamba mafanikio ya binadamu ndiyo mafanikio ya wanyama. Huo ni ulaghai mtupu, binadamu ni mbinafsi anayejijali mwenyewe tu. Acha kuwe na undugu kati ya wanyama na undugu katika mapambano. Binadamu wote ni adui lakini wanyama wote ni ndugu."
Baada ya kusema hayo kukatokea shangwe kubwa sana. Meja alipokuwa akihutubia, panya wanne wakubwa walitoka kwenye mashimo yao na walikaa kumsikiliza. Mbwa wakawa wamewaona. Ushapu wao wa kukimbilia mashimoni ndiyo uliowaokoa.
Meja akainua mguu kuashiria wanyama wanyamaze, kisha akasema. "Ndugu zangu, hapa kuna jambo linatakiwa tulitatue. Wanyama wa porini kama sungura na panya ni adui zetu au ni ndugu zetu? Naombeni tupige kura. Swali liwe; Je, panya ni ndugu zetu?"
Kura ilipigwa mara moja na kwa kura nyingi ikakubaliwa kuwa panya ni ndugu. Kulikuwa na kura nne tu zilipinga. Kura za mbwa watatu na ya paka ambaye hata hivyo aligundulika amepiga kura ya ndiyo na hapana.
Meja akaendelea kusema: "sina mengi ya kuongezea ila nitaruria tu. Siku zote kumbuka kuwa una wajibu wa kuwa adui wa binadamu na mambo yake yote. Chochote kinachotembea kwa miguu miwili ni adui. Chochote kinachotembea kwa miguu minne au chenye mabawa ni rafiki. Na kumbukeni kuwa, katika kupambana na binadamu hatutakiwi kuwa kama yeye. Hata tukimshinda hatupaswi kuiga mambo yake. Mnyama yeyote hatakiwi kuishi ndani ya nyumba, kulala kitandani, kuvaa nguo, kunywa pombe, kuvuta sigara, kushika pesa au kujihusisha na biashara. Zaidi ya yote, mnyama yeyote hatakiwi kutawala wengine kwa kwa ukatili."
"Wanyama wote ni ndugu, wenye nguvu na dhaifu, wenye akili na wajinga, sote ni ndugu. Mnyama yeyote hatakiwi kabisa kumuua mnyama mwenzake. Wanyama wote sawa."
"Sasa ndugu zanguni nitawaambia kuhusu ndoto niliyoota jana usiku. Siwezi kuwaelezea vizuri jinsi ilivyokuwa ila ni ndoto inayohusu hali ya dunia binadamu atakapokuwa ametoweka, lakini ilinikumbusha zamani sana nilipokuwa bado nguruwe mdogo.
Miaka mingi iliyopita, nilipokuwa mdogo, mama yangu na nguruwe wengine walipendelea kuimba wimbo mmoja. Wimbo wenyewe waliujua kwa ala na maneno matatu ya mwanzo tu. Nilipokuwa mdogo nilikuwa nimeishika ile ala. Ni muda mrefu umepita hivyo ilikuwa imenitoka. Lakini jana usiku imenijia ndotoni, na cha kushangaza zaidi, hadi maneno ya wimbo yamenijia. Maneno ambayo nina hakika yaliimbwa na wanyama hapo zamani za kale na yamepotea baada ya vizazi vingi kupita. Nitajaribu kuwaimbia wimbo huo ndugu zangu. Ila mimi ni mzee na sauti yangu ni ya kukwaruza, lakini nikiwafundisha ala yake natumaini mtauimba vizuri zaidi. Wimbo wenyewe unaitwa Hayawani wa Uingereza."
Meja alikohoa kidogo kisha akaanza kuimba. Sauti ya meja ilikuwa ya kukwaruza lakini alijitahidi kuimba vizuri. Ulikuwa ni wimbo wa kuchangamsha sana.
Maneno yake yalikuwa kama ifuatavyo:
Hayawani wa nchi na nyanda zote
Sikilizeni ujumbe wangu wa shangwe
Ni kuhusu wakati mzuri ujao
Siku ile inakuja
Siku ya kumpindua binadamu mkatili
Ardhi nzuri ya uingereza, itakanyagwa na hayawani tu
Pete zitatoweka katika pua zetu
Na kamba kutoka migongoni mwetu
Vyuma vya kutuendesha vitaliwa na kutu
Mijeledi ya ukatili haitachapa tena
Utajiri usioelezeka
Ngano, shayiri na nyasi
Maharage, mizizi ya beet na matunda
Vitakuwa vyetu siku hiyo
Mashamba ya Uingereza yatameremeta
Maji yake yatakuwa safi
Pepo zake zitakuwa mwororo
Katika siku tutakayo kuwa huru
Sote tutapambana kwaajili ya siku hiyo
Hata tukifa kabla haijatokea
Ng'ombe na farasi, bata bukini bata mzinga
Wote watapambana kwaajili ya uhuru
Hayawani wa Uingereza, hayawani wa Ireland
Hayawani wa nchi na nyanda zote
Sikilizeni vizuri na enezeni ujumbe wangu
Ujumbe juu ya wakati bora ujao
Wimbo huu uliwapamdisha sana mori wanyama wote, na kabla Meja hajamaliza kuimba nao wakaanza kuuimba. Hata wanyama wajinga kabisa wakawa wameweza kuimba ala ile na maneno machache. Wanyama wenye akili kama mbwa na nguruwe waliweza kuimba wimbo wote ndani ya dakika chache tu.
Baada ya mazoezi kidogo, wanyama wote wakaimba Hayawani wa Uingereza pamoja kwa sauti kubwa. Kila mnyama alitia vionjo vyake. Wimbo ulikuwa umewapandisha mori kiasi kwamba waliimba mara tano mfululizo. Na bila kukatishwa wangeweza imba usiku kucha.
Kelele zao zikimuamsha bwana Jones. Bwana Jones aliamka haraka akifikiri labda mbwa mwitu amevamia shamba. Alichukua bunduki iliyokuwa kwenye kona chumbani mwake kisha akatoka na kupiga risasi hewani. Vipande vya risasi vikaruka na kugonga ukuta wa banda lile kubwa walilokuwepo wanyama. Wanyama wote wakatawanyika kila mmoja kwenye eneo lake la kulala. Shamba likawa kimya kabisa.