SURA 36. SURAT YA-SIN<br />
KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU<br />
<b>1. Ya-Sin (Y.S.</b>).<br />
2. Kwa Haki ya Qur'ani yenye hikima!<br />
3. Hakika wewe ni miongoni mwa walio tumwa,<br />
4. Juu ya Njia Iliyo Nyooka.<br />
5. Uteremsho wa Mwenye nguvu, Mwenye kurehemu.<br />
6. Ili uwaonye watu ambao baba zao hawakuonywa , basi wao wamekuwa wenye<br />
kughafilika.<br />
7. Bila ya shaka kauli imekwisha thibiti juu ya wengi katika wao, kwa hivyo<br />
hawaamini.<br />
8. Tumeweka makongwa shingoni mwao, yakawafika videvuni. Kwa hivyo vichwa vyao<br />
viko juu tu.<br />
9. Tumeweka kizuizi mbele yao, na kizuizi nyuma yao, na tumewafunika macho yao;<br />
kwa hivyo hawaoni.<br />
10. Ni sawa sawa kwao ukiwaonya au usiwaonye, hawataamini.<br />
11. Hakika wewe unamwonya mwenye kufuata ukumbusho, na akamcha Arrahman, Mwingi<br />
wa Rehema, kwa ghaibu. Basi mbashirie huyo msamaha na ujira mwema.<br />
12. Hakika Sisi tunawafufua wafu, na tunayaandika wanayo yatanguliza, na wanayo<br />
yaacha nyuma. Na kila kitu tumekihifadhi katika daftari asli lenye kubainisha.<br />
13. Na wapigie mfano wa wakaazi wa mji walipo wafikia walio tumwa.<br />
14. Tulipo watumia wawili, wakawakanusha. Basi tukawazidishia nguvu kwa mwingine<br />
wa tatu. Wakasema: Hakika sisi tumetumwa kwenu.<br />
15. Wakasema: Nyinyi si chochote ila ni watu kama sisi. Na Mwingi wa Rehema<br />
hakuteremsha kitu. Nyinyi mnasema uwongo tu.<br />
16. Wakasema: Mola wetu Mlezi anajua kwamba hakika sisi tumetumwa kwenu.<br />
17. Wala si juu yetu ila kufikisha ujumbe ulio wazi.<br />
18. Wakasema: Sisi tumeagua kuwa nyinyi ni wakorofi. Ikiwa hamtaacha basi kwa<br />
yakini tutakupigeni mawe, na mtapata adhabu chungu kutoka kwetu.<br />
19. Wakasema: Ukorofi wenu mnao wenyewe! Je! Ni kwa kuwa mnakumbushwa? Ama<br />
nyinyi ni watu walio pindukia mipaka.<br />
20. Na akaja mtu mbio kutokea upande wa mbali wa mjini, akasema: Enyi watu<br />
wangu! Wafuateni hawa walio tumwa.<br />
21. Wafuateni ambao hawakutakini ujira, hali ya kuwa wenyewe wameongoka.<br />
22. NA KWA NINI nisimuabudu yule aliye niumba na kwake mtarejeshwa?<br />
23. Je! Niishike miungu mingine badala yake? Arrahmani, Mwingi wa Rehema,<br />
akinitakia madhara uombezi wa hao hautanifaa kitu, wala hawataniokoa.<br />
24. Basi hakika mimi hapo nitakuwa katika upotovu ulio dhaahiri.<br />
25. Hakika mimi nimemuamini Mola wenu Mlezi, basi nisikilizeni!<br />
26. Akaambiwa: Ingia Peponi! Akasema: Laiti kuwa watu wangu wangeli jua<br />
27. Jinsi Mola wangu Mlezi alivyo nisamehe, na akanifanya miongoni mwa walio<br />
hishimiwa.<br />
28. Na hatukuwateremshia kaumu yake baada yake jeshi kutoka mbinguni, wala si<br />
wenye kuteremsha.<br />
29. Hakukuwa ila ukelele mmoja tu; na mara walizimwa!<br />
30. Nawasikitikia waja wangu. Hawajii Mtume ila wao humkejeli.<br />
31. Je! Hawaoni umma ngapi tulizo ziangamiza kabla yao? Hakika hao hawarejei<br />
tena kwao.<br />
32. Na hapana mmoja ila wote watakusanywa waletwe mbele yetu.<br />
33. Na Ishara hiyo kwao - ardhi iliyo kufa, nasi tukaifufua, na tukatoa ndani<br />
yake nafaka, wakawa wanazila!<br />
34. Na tukafanya ndani yake mabustani ya mitende na mizabibu, na tukatimbua<br />
chemchem ndani yake,<br />
35. Ili wale matunda yake, na hayo hayakufanywa na mikono yao! Basi je,<br />
hawashukuru?<br />
36. Subhana, Ametakasika, aliye umba dume na jike vyote katika vinavyo mea<br />
katika ardhi na katika nafsi zao, na katika wasivyo vijua.<br />
37. Na usiku ni Ishara kwao. Tunauvua humo mchana, mara wao wanakuwa gizani.<br />
38. Na jua linakwenda kwa kiwango chake. Hayo ni makadirio ya Mwenye nguvu,<br />
Mwenye kujua.<br />
39. Na mwezi tumeupimia vituo, mpaka unakuwa kama karara kongwe.<br />
40. Haliwi jua kuufikia mwezi, wala usiku kuupita mchana. Na vyote vinaogelea<br />
katika njia zao.<br />
41. Na ni Ishara kwao kwamba Sisi tuliwapakia dhuriya zao katika jahazi ilio<br />
sheheni.<br />
42. Na tukawaumbia kutoka mfano wake wanavyo vipanda.<br />
43. Na tukitaka tunawazamisha, wala hapana wa kuwasaidia, wala hawaokolewi,<br />
44. Isipo kuwa kwa rehema zitokazo kwetu na starehe kwa muda.<br />
45. Na wanapo ambiwa: Jilindeni na yalioko mbele yenu na yalioko nyuma yenu, ili<br />
mpate kurehemewa...<br />
46. Na haiwafikii Ishara yoyote katika Ishara za Mola wao Mlezi ila wao huwa ni<br />
wenye kuipuuza.<br />
47. Na wanapo ambiwa: Toeni katika aliyo kupeni Mwenyezi Mungu, walio kufuru<br />
huwaambia walio amini: Je! Tuwalishe ambao Mwenyezi Mungu angependa angeli<br />
walisha mwenyewe? Nyinyi hammo ila katika upotofu ulio dhaahiri.<br />
48. Na wanasema: Ahadi hii itatokea lini, ikiwa nyinyi ni wakweli?<br />
49. Hawangojei ila ukelele mmoja tu utakao wachukua nao wamo kuzozana.<br />
50. Basi hawataweza kuusia, wala kwa watu wao hawarejei.<br />
51. Na litapulizwa barugumu, mara watatoka makaburini wakikimbilia kwa Mola wao<br />
Mlezi.<br />
52. Watasema: Ole wetu! Nani aliye tufufua kwenye malazi yetu? Haya ndiyo aliyo<br />
yaahidi Mwingi wa Rehema na wakasema kweli Mitume.<br />
53. Haitakuwa ila ukelele mmoja tu, mara wote watahudhuruishwa mbele yetu.<br />
54. Basi leo nafsi yoyote haitadhulumiwa kitu, wala hamtalipwa ila yale mliyo<br />
kuwa mkiyatenda.<br />
55. Hakika watu wa Peponi leo wamo shughulini, wamefurahi.<br />
56. Wao na wake zao wamo katika vivuli wameegemea juu ya viti vya fakhari.<br />
57. Watapata humo kila namna ya matunda na watapata kila watakacho kitaka.<br />
58. "Salama!" Hiyo ndiyo kauli itokayo kwa Mola Mlezi Mwenye kurehemu.<br />
59. Na enyi wakosefu! Jitengeni leo!<br />
60. Je! Sikuagana nanyi, enyi wanaadamu, kuwa msimuabudu Shet'ani? Hakika yeye<br />
ni adui dhaahiri kwenu.<br />
61. Na ya kwamba mniabudu Mimi? Hii ndiyo Njia Iliyo Nyooka.<br />
62. Na bila ya shaka yeye amekwisha lipoteza kundi kubwa miongoni mwenu. Je,<br />
hamkuwa mkifikiri?<br />
63. Hii basi ndiyo Jahannamu mliyo kuwa mkiahidiwa.<br />
64. Ingieni leo kwa vile mlivyo kuwa mkikufuru.<br />
65. Leo tunaviziba vinywa vyao, na iseme nasi mikono yao, na itoe ushahidi miguu<br />
yao kwa waliyo kuwa wakiyachuma.<br />
66. Na tungeli penda tungeli yafutilia mbali macho yao, wakawa wanaiwania njia.<br />
Lakini wange ionaje?<br />
67. Na tungeli taka tunge wageuza SURA hapo hapo<br />
walipo, basi wasinge weza kwenda wala kurudi.<br />
68. Na tunaye mzeesha tunamrudisha nyuma katika umbo. Basi je! hawazingatii?<br />
69. Wala hatukumfundisha (Muhammad) mashairi, wala hayatakikani kwake hayo.<br />
Haukuwa huu ila ni ukumbusho na Qur'ani inayo bainisha.<br />
70. Ili imwonye aliye hai, na neno litimie juu ya makafiri.<br />
71. Je! Hawaoni kwamba tumewaumbia kutokana na iliyo fanya mikono yetu wanyama<br />
wa mifugo, na wao wakawa wenye kuwamiliki.<br />
72. Na Sisi tukawadhalilishia. Basi baadhi yao wako wanao wapanda, na baadhi yao<br />
wanawala.<br />
73. Na wao wanapata kwao manufaa na vinywaji. Basi je, hawashukuru?<br />
74. Na wameishika miungu mingine badala ya Mwenyezi Mungu ili ati wapate<br />
kusaidiwa!<br />
75. Hawataweza kuwasaidia. Bali hao ndio watakuwa askari wao watakao<br />
hudhurishwa.<br />
76. Basi maneno yao yasikuhuzunishe. Hakika Sisi tunayajua wanayo yaweka siri na<br />
wanayo yatangaza.<br />
77. Kwani mwanaadamu haoni ya kwamba Sisi tumemuumba yeye kutokana na tone la<br />
manii? Kisha sasa yeye ndio amekuwa ndiye mgomvi wa dhaahiri!<br />
78. Na akatupigia mfano, na akasahau kuumbwa kwake, akasema: Ni nani huyo<br />
atakaye ihuisha mifupa nayo imekwisha mung'unyika?<br />
79. Sema: Ataihuisha huyo huyo aliye iumba hapo mara ya mwanzo. Na Yeye ni Mjuzi<br />
wa kila kuumba.<br />
80. Aliye kujaalieni kupata moto kutokana na mti wa kijani nanyi mkawa kwa huo<br />
mnawasha.<br />
81. Kwani aliye ziumba mbingu na ardhi hawezi kuwaumba mfano wao? Kwani! Naye<br />
ndiye Muumbaji Mkuu, Mjuzi.<br />
82. Hakika amri yake anapo taka kitu ni kukiambia tu: Kuwa! Na kikawa.<br />
83. Basi Ametakasika yule ambaye mkononi mwake umo Ufalme wa kila kitu; na kwake<br />
Yeye mtarejeshwa.