Hata alipokuwa hai hayati JPM kama bunge lingesema limkatae kwa kutumia ibara ya 46 ya katiba ya JMT na kumuondoa madarakani wananchi wangesimama na hayati JPM. Hili halina ubishi.
Kwa hiyo kama wanachi wangesimama na JPM basi ni wazi kuwa angeshinda. Na bunge lingeonekana kituko. Maana lingepigwa chini na uchaguzi kuitishwa upya.
Vivyo hivyo ndicho kinachoendelea sasa hivi. Kupinga kuwa kuna mradi kama SGR amabao una maufaa kwa taifa na JPM alithubutu kuutekeleaza ni kupingana na umma wa Watanzania. Kupinga mradi wa JNHPP.
Kupinga juhudi za ufisadi alizoonyesha, kupinga kuwa mradi wa bandari ya bagamoyo ulikuwa na mapungufu ni baadhi ya hoja ambazo zitawaponza wanasiasa wa CCM.
Na mshupaze shingo alafu mwaka 2025 mtaona nini maana ya nguvu ya umma.
Usiogope kusoma andiko zito la Bollen Ngetti. Hili hapa.
SUKUMA GANG: MHIMILI WA SHETANI ULIOPAGAWA
UKITALII mitandaoni hutoacha kukutana na maneno "Sukuma Gang". Hata katika mijadala isiyo rasmi vijiweni, daladalani, kwenye mabaa na migahawa utakutana na Sukuma Gang. Mtu makini anaweza kujiuliza au kuwauliza wengine, hiki kinachoitwa Sukuma Gang ni nini? Kina dhamira gani? Nani muasisi wake? Nini visheni na matakwa yake? Maswali ni mengi.
Kutokana na taaluma yangu, niliamua ku-dig up kufanya uchunguzi wa kina ili kuja na majibu ya maswali hayo hapo juu.
Ukweli mchungu uliokodoa macho ni kwamba hili ni genge la watu wachache ambao waliimba nyimbo za sifa na kuabudu (praise & worship team) kwa Mpita Njia ambaye utawala wake tumeipa kisogo. Ni watu wachache waliobahatika kuuzunguka meza ndefu ya kula ndani ya Kasri la Mpita Njia.
Neno "Sukuma" limejitokeza sana kwa kuwa Mpita Njia alitoka Usukumani lakini kwa hakika Mhimili huu wa shetani (devil axis) ulisomba wengi hata wasio na nasaba na Usukuma. Genge hili lililoshangilia utawala wa kifashisti lilijipenyeza Bungeni, Makanisani, Misikitini, Vyama vya Siasa, ndani ya Majeshi yetu, taasisi za Umma, vyombo vya Habari nakadhalika.
Wakati Mpita Njia akifanya sanaa ya kula mahindi barabarani wao walikunywa wine na nyama choma wakiendelea kusifu na kuabudu ushetani uliokuwa ukijitanua.
Genge hili linaongozwa na kijana mmoja alikuwa hapo Hazina na vijana 12 likifadhiliwa na Mawaziri wawili walioko madarakani katika uongozi wa SSH. Ni binadamu lakini ambao hawakuamini kuwa Mpita Njia kama binadamu anaweza kutoweka juu ya uso wa dunia na kusahaulika kama sasa.
Ni Watanzania wenzetu lakini waliokuwa wameloa uhondo wa ufedhuli wakila na kusaza tena bila hata kunawa mikono huku wakisifu na kuabudu, "nani kama Mpita Njia?"
Kwa sasa hii "devil axis" limepagawa lisiamini macho na masikio yao kama kweli Mpita Njia hatunaye! Wanaweweseka, wanawayawaya kama machela, homa ya SSH inawagonga vichwa hawaoni dawa maana watamsifu na kumwabudu nani? Aliyeko madarakani hataki sifa na ibada za kishirikina. Amenyooka kama chuma cha reli. Iron Lady!
Yapo mambo yanayowapagawisha Wana Sukuma Gang ndio maana huko mitandaoni wameanza kupiga ramli za kichawi mara "ooh mama nchi itamshinda, ooh anachukua ushauri wa JK" nakadhalika. Al-mradi tu ushirikina wao upate kuungwa mkono na wajinga wachache! Jambo ambalo wameshindwa hata kabla jua kukomaa!
Genge hili haliamini kweli sasa hakuna kuteka, kutesa, kupoteza au kushambulia watu kwa silaha za kivita hadharani?! Wanaumia. Haliamini miili ya watu kutookotwa mitoni ndani sandarusi, kweli?
Genge hili haliamini kama kweli wafanyabiashara waliokimbia nchi kwa kuporwa fedha zao na Mhimili huu sasa wanarejea nchini kufanya biashara. Wanafunika nyuso zao. Haliamini kama "task force" ya TRA limefurushwa na sasa kodi inakusanywa kwa staha, kwa elimu ya mlipa Kodi na maarifa na si mitulinga! Wanashangaa.
Genge hili haliamini kama kweli Uhuru wa kujieleza kwa mujibu wa Katiba Ibara ya 18(3) umerejea ambapo sasa uhulizi mtu pembeni "huyo nani, usiongee utapotea". Haliamini kama kweli Rais SSH (Iron Lady) atakutana na vyama vya upinzani kujadili mustakabali wa demokrasia na maendeleo ya Taifa. Wanapata shida.
Haliamini kama kweli wizi na usombaji wa fedha za umma walioufanya kupitia sekta ya ujenzi na kampuni ya Mpita Njia sasa zitarejeshwa Hazina! Wanadhani masikhara! Kwamba sasa ni zamu yao kuzitapita zikiwa mbichi.
Sukuma Gang haliamini kama kweli "Iron Lady" ameamua kuwaunganisha Watanzania wote bila kujali tofauti zao za kikabila, Kanda, dini, jinsia, rangi, urefu na ufupi wa pua kama walivyozoea enzi za Mpita Njia. Wanalia na kusaga meno.
Haliamini kama kweli mashirika ya umma yalidanganya umma kwa gawio hewa kumbe hasara tupu. Linashangaa kwa nini "Iron Lady" hatumii kabisa maneno, "utawala wangu, Serikali yangu" na badala yake hutumia, "uongozi wangu, Serikali ninayoiongoza na wenzangu". Hawaamini masikio yao.
Genge hili haliamini fumua-fumua inayoendelea Serikalini kuondoa ufashisti kama ni kweli au maigizo. Linashangaa marejeo ya Bagamoyo Economic Zone ikitaka kujengwa badala ya Kijiji Cha Mpita Njia. Kwamba BEZ itashamirisha uchumi wetu maradufu. Haliamini kama zile ngonjera zao zimefutwa kuzimu.
Haliamini imewezekanaje diplomasia ya Tanzania kurejea mahali pake kwa kipindi kifupi namna hiyo. Mulamula aliyedhalilishwa SA anaipaisha Tanziania tofauti na Bwana Yule wa dawa ya Corona ya Madagascar! Upuuzi mtupu.
Haliamini kama wafanyakazi wameanza kupandishwa madaraja. Wanasumbuka kuona umoja ndani ya CCM unavyoshamiri chini vijana wakiunganisha makundi yote. Hawaamini mengi na wataendelea kushangaa mengi.
Kwa leo nihitimishe kwa kuwapa salamu, "enyi Sukuma Gang, tulieni, ache chokochoko za kudhani Rais SSH atafeli, huyu ni Iron Lady, mtafeli ninyi, njooni tuungane pamoja tuijenge nchi yetu". Amina!
Bollen Ngetti@2021
Maoni: 0683 226539