Wakati mradi wa kufua umeme wa Julius Nyerere (JNHPP), ukifikia asilimia 91, Menejiment ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), imeongeza wafanyakazi wengine 24 katika bwawa hilo, na hivyo kufikishwa wataalam 92, wanaondaliwa kuendesha mradi huo pindi utakapokamilika Juni mwaka 2024.
Kauli hiyo imetolewa leo Ijumaa Agosti 25, 2023 na Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Maharage Chande alipotembelea mradi huo, akiambatana na timu ya menejementi ya Tanesco.
Lengo la ziara hiyo ni kuangalia mwenendo wa ujenzi wa mradi na tathimini ya hali ya mvua za vuli zinazotarajiwa kunyesha kati ya Oktoba hadi Disemba.
Amesema maendeleo ni mazuri hadi Julai tulifikia asilimia 90.19 na tunatarajia mwishoni mwa Agosti tutafikia asilimia 91, akisema tayari wameshaongeza wafanyakazi zaidi ya 20 kwa ajili ya kujiandaa kuendesha mradi utakapokamilika.
Chande amesema ili mradi huo uanze kufanya kazi, wafanyakazi 221 wanahitajika kuuendesha, na kwamba kwa sasa wanapelekwa kwa awamu kulingana na hatua ya mradi unapofikia.
"Watu 221 huwezi kuwaleta kwa wakati mmoja, bali kwa makundi yatakayokuja kwa wakati husika, mfano sasa hivi kundi hili lililokuja linahusika uhandisi wa umeme kwa sababu mitambo ndio inafungwa. Kwa hiyo huko mbeleni kukiwa na uhitaji wa watalaamu wa aina hii basi wapo.
"Kwa sababu mradi upo nje ya mji, kutakuwa na wafanyakazi madaktari, walimu wa shule za awali, wahasibu. Tutaendelea kuongeza wafanyakazi kwa makundi kulingana na hatua ya ujenzi wa mradi utakapofikia," amesema Chande.