Rais wa Shirikisho la Soka Hispania, Luis Rubiales ametangaza kujiuzulu katika nafasi yake baada ya kuandamwa na tuhuma za unyanyasaji wa kijinsia baada ya kumbusu mdomoni mshambuliaji wa timu ya wanawake ya nchi hiyo, Jenni Hermoso.
Hermoso (33) alisema busu alilopigwa na Rais huyo halikuwa la maafikiano wala makubaliano kati yao na tayari alishawasilisha madai ya kisheria.
Rubiales alikumbwa na tuhuma hiyo siku ya fainali ya Kombe la Dunia la Wanawake baada ya ushindi wa Hispania dhidi ya Uingereza.
Kwa upande wake Rubiales alisema amewasilisha kujiuzulu kwake kwa Kaimu Rais wa shirikisho hilo.
"Siwezi kuendelea na kazi yangu," alimwambia mtangazaji Piers Morgan kwenye kipindi chake cha televisheni.
Aidha, Rubiales pia amejiuzulu wadhifa wake kama Makamu wa Rais wa Kamati Kuu ya Uefa.
Siku ya Ijumaa, mwendesha mashtaka aliwasilisha malalamiko katika mahakama kuu ya Hispania - kufuatia ushahidi wa Hermoso siku ya Jumanne - dhidi ya Rubiales kwa unyanyasaji wa kijinsia na kulazimishwa.
Rubiales alidai busu hilo lilikuwa "la kuheshimiana na "ridhaa".
Wachezaji 81 wanawake Hispania, wakiwemo washindi wote 23 wa Kombe la Dunia, walisema hawataichezea tena timu ya Taifa kama bado Rubiales atakuwa kwenye nafasi yake.