Abdallahking
JF-Expert Member
- Mar 19, 2018
- 3,985
- 10,840
Simulizi : MALAIKA WA SHETANI
Mwandishi : BEN R. MTOBWA
Imeletwa kwenu na: BURE SERIES
Sehemu ya 1
LANGO uligongwa tena. Safari hii mgongaji aligonga kwa nguvu zaidi. Kwa mbali, sauti yake ilisikika ikinong’ona, ikiwa na kila dalili ya hofu na wasiwasi, ikisema, “Tafadhali
nifungulie… dakika moja tu ya muda wako…”
Joram aligeuka kumtazama Nuru ambaye alikuwa chali, juu ya kitanda, vazi jepesi la kulalia likiwa pazia pekee lililouweka sirini mwili wake laini; unaolazimisha kutazamwa tena na tena. Hata hivyo, halikuwa pazia maridadi kiasi hicho. Wepesi na ulaini wa vazi hilo haukuwa kipingamizi cha haja dhidi ya macho ya Joram ambayo yaliweza kuona waziwazi hazina ya uzuri usiochuja, iliyokuwemo katika umbo hilo; hazina ambayo Joram alikuwa akijifariji kwa kuitazama na kuipapasa; vidole vyake vikistarehe; roho ikiburudika na nafsi yake kuridhika; muda mfupi tu kabla ya yeyote aliyekuwa hapo mlangoni akibisha hajafika.
Macho ya Nuru, ambayo yalikuwa yameanza kulainika kwa mguso wa vidole vya Joram Kiango, vilivyohitimu kugusa, yalirudiwa na uhai yalipoona maswali katika macho ya Joram. Kama aliyejua Joram anauliza nini alitamka kwa upole, “Mfungulie.”
“Anaweza kuwa nani? Na anataka nini saa hizi?”
“Majibu yenye uhakika utayapata hapo baada ya kumfungulia mlango.”
Joram alisita tena, hakuweza kufikiria nani anaweza kufanya
ziara chumbani kwake usiku huo, saa sita kasorobo! Zaidi hakuhitaji kabisa kupata mgeni yeyote muda huo alikuwa akijiandaa kwa mara nyingine kufanya ile ziara ya kila siku katika bustani isiyokinaisha iliyofichwa katika umbo la Nuru, safari ambayo kamwe haimchoshi na bado kila anaposafiri inakuwa kana kwamba ni mpya zaidi. Kama jana alisafiri kwa kila kitu kama ndege, leo itakua kana kwamba yuko katika jahazi linalosukwasukwa kwa mawimbi mazito, ambayo badala ya kutisha na kuogofya yanafariji na kusisimua. Na kesho ataivinjari bustani hiyo huku akielekea angani. Kesho kutwa…
Hapana. Si hilo lililomfanya asite kufungua mlango. Hasa ni hisia. Zilikwishamfanya aamini kuwa mgeni huyo hakuleta habari njema. Si kwamba Joram alikuwa mwoga wa habari mbaya, bali alikuwa ameamua kujitenga kwa muda na dunia aliyoizoea, dunia ya Joram Kiango.
Utashangaa kuwa chumba hiki walichokuwemo kilikuwa kidogo chenye kitanda kimoja kikiwa hoteli ya daraja la nne, au mwisho, katika kimojawapo cha vijimitaa kisicho na jina, katika vitongoji vya Tandale; kijihoteli ambacho Joram hata hakujishughulisha kufahamu jina lake ambalo lilimtoka mara baada ya kupatiwa ufunguo!
Joram, ambaye maisha yake yote ni katika miji mikuu na mahoteli ya daraja la kwanza! Joram ambaye sura yake ni maarufu katika magazeti na televisheni zote duniani, akiwa na uzito wa aina yake katika masikio ya karibu kila mtu. Naam, Joram yuleyule ambaye sasa yuko katika chumba hiki chenye kuta zilizochakazwa kwa utandu wa buibui, chumba ambacho kingeweza kutoa harufu ya kutatanisha, endapo mafuta yenye harufu nzuri ya Nuru yasingeibabaisha harufu hiyo!